FRIDAY, FEBRUARY 20, 2015
SERIKALI KUAJIRI WALIMU
35,000 - WAZIRI MKUU
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda
amesema Serikali imepanga kuajiri
walimu zaidi ya 35,000 kwa ajili ya
shule za sekondari ili kukabiliana na
tatizo la uhaba wa walimu nchini.
Ametoa kauli hiyo jana jioni
(Alhamisi, Februari 19, 2015) wakati
akizungumza na mamia ya wakazi wa
kata ya Kiwere, mara baada ya
kukagua ujenzi wa maabara na
kuzindua nyumba nne za walimu
kwenye shule ya sekondari ya Kiwere,
tarafa ya Kalenga, wilayani Iringa.
Waziri Mkuu alisema walimu hao
watagawanywa kwenye shule
kulingana na mahitaji
yaliyokwishawasilishwa na kwamba
watakapopata mgao wao hawana budi
kuziangalia kwanza shule zenye
miundombinu iliyokamilika kama
ilivyo kwa shule hiyo.
Akifafanua kuhusu kasi ya ujenzi wa
maabara Waziri Mkuu alisema: Mkoa
mzima wa Iringa unahitaji kuwa na
maabara 318 na zilizo tayari mpaka sasa
ni 108. Lakini kuna nyingine 141 ambazo
zimekwishaanza kujengwa na zimefikia
hatua nzuri. Nimeambiwa katika muda
mfupi ujao kutakuwa na maabara 249
zilizokamilika, alisema.
RC inabidi uwasukume watu wako ili
hizi 69 ambazo bado hazijaanza
kujengwa zikamilike kabla ya Juni mwaka
huu kama ambavyo Mheshimiwa Rais
Jakaya Kikwete alikuwa ameelekeza.
Alisema hataongeza tena muda wa
ujenzi, aliongeza.
Alisema elimu ni sekta ya msingi ambayo
Serikali imeamua kuipa umuhimu wa
kipekee na kuiweka katika moja ya
maeneo sita muhimu ya kipaumbele chini
ya Mpango wa Matokeo Makubwa ya
Haraka (BRN).
Waziri Mkuu aliwataka wanafunzi wa
shule hiyo wasome kwa bidii na wawe
wasikivu ili waweze kufanya vizuri zaidi
kwenye masomo yao.
Mapema, akitoa taarifa mbele ya Waziri
Mkuu, Afisa Elimu wa Wilaya ya Iringa,
Bw. Leonard Msigwa alisema ujenzi wa
nyumba hizo nne ambazo zina pande
mbili (four duplex houses) umegharimu
sh. milioni 323.2. Alisema nyumba hizo
zenye vyumba vitatu vya kulala, sebule na
jiko, zina uwezo wa kubeba familia nane.
Bw. Msigwa alisema ujenzi wa nyumba
ulifanywa shirika la DESWOS la
Ujerumani kwa kushirikiana na
Halmashauri ya Wilaya ya Iringa pamoja
na wananchi. Pia walisaidiwa kujengewa
tenki la maji na mabweni mawili yenye
uwezo wa kuchukua wanafunzi 112 kila
moja kwa ajili ya wasichana.
Akifafanua kuhusu hali ya ujenzi wa
maabara, Afisa Elimu huyo alisema hadi
sasa wamekamilisha ujenzi wa vyumba
viwili vya Kemia na Baiolojia lakini bado
viko kwenye hatua ya kupaka rangi.
Alisema mfumo wa gesi na maji
umekwishafungwa ndani ya vyumba vya
maabara.
Ujenzi wa maabara hadi sasa
umekwishagharimu sh. milioni 52.8/- na
katika kipindi cha Februari 2015,
tumefanikiwa kutengeneza baadhi ya
samani za maabara yaani meza 24 na
stuli 96 zenye thamani ya sh. 8,940,000/-,
alisema.
FRIDAY, FEBRUARY 20, 2015 ~ COPYRIGHT:
MICHUZI BLOG ~
Pia waweza tafuta Magazeti ya Leo jumamosi
21/2/2015 MTANZANIA HALISI NA HABARI LEO
YAMECHAPISHA HABARI HIII!!