Bodi ya Ligi kuu England, inaangalia uwezekano wa kuanza tena michezo ya EPL bila mashabiki, kuanzia wikiendi ya kwanza ya mwezi Mei na kufikia kikomo Jumapili ya Julai 12 mwaka huu.
Pendekezo hilo litajadiliwa na klabu zote 20 Ijumaa hii kwa njia ya Mtandano, huku wadau wengine wakiwa ni serikali, mamlaka za afya na chama cha wachezaji wa kulipwa (PFA).
Lengo la kuirejesha EPL ni kukwepa hasara kubwa ya kifedha kama msimu hautamalizika kwasababu ya mlipuko wa virusi vya #Corona.
Kinachowaumiza kichwa zaidi ni mkataba wa mwaka mmoja wa haki za matangazo wenye thamani ya Pauni bilioni tatu, unaopaswa kumalizika Julai 31.
Kama msimu hautamalizika, Sky Sports, BT Sport na kampuni nyingine za kimataifa zenye haki ya kurusha mubashara EPL, zitatakiwa kufidiwa kwa pamoja, jumla ya pauni Milioni 762.
Tayari wenye haki za matangazo, wameanza kuipa presha Bodi, wakitaka kujua ni lini EPL itarejea kwasababu wanazidi kupoteza wateja wa kulipia.