Hadithi : Nitakapokufa

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,743
Reaction score
25,564

MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 1.

Mlango ulisikika ukigongwa kifujo fujo na mzee Kessi ambaye alikuwa ametoka kunywa pombe za kienyeji katika mtaa wa pili kutoka katika mtaa huo aliokuwa akiishi wa Kilingira uliopo Bagamoyo. Sauti yake kali iliyojaa ulevi ilikuwa ikisikika kwa juu sana huku akimtaka mke wake aufungue mlango huo.
Mzee Kessi hakuwa na uwezo wa kusimama wima na kutulia, muda wote alikuwa akiyumbayumba tu kutokana na kunywa kiasi kikubwa cha pombe za kienyeji. Miguuni, mzee Kessi alikuwa na kiatu kimoja tu, chupa moja ya maji ya uhai ambayo ilikuwa na pombe hiyo ya gongo ilikuwa mkononi mwake. Shati lake lilikuwa limeloa jasho, kwa kifupi, hakuonekana kuwa na utanashati wowote ule.
Bi Fatuma alikuwa chumbani kwake, usingizi kwake ukaonekana kuwa mzito kupatikana. Muda wote alikuwa akijigalagaza tu kitandani lakini bado usingizi haukupatikana. Mawazo yake kwa wakati huo yalikuwa yakimfikiria mume wake, mzee Kessi ambaye alikuwa kilabuni akinywa gongo.
Tayari ilikuwa imetimia saa saba usiku lakini bado mzee Kessi hakuwa amerudi nyumbani kitu ambacho kilionekana kumnyima raha Bi Fatuma. Ilipofika saa nane na robo usiku, akasikia mlango ukigongwa kifujo fujo huku sauti ya mumewe ikisikika ikimtaka kuufungua mlango hata kabla hajauvunja.
Huku akionekana kuwa na uchovu mwingi, Bi Fatuma akainuka na kuanza kuelekea ulipokuwa mlango na kisha kuuufungua. Kwanza akakutana na harufu mbaya na kali ya pombe, akaziba pua yake huku mume wake akiingia ndani. Mzee Kessi alikuwa akitembea huku akiyumbayumba kama kawaida yake.
Breki yake ya kwanza ilikuwa katika makochi yaliyokuwa sebuleni hapo, makochi ambayo yalikuwa yamechakaa kupita kawaida. Akajilaza mahali hapo huku pombe yake iliyokuwa katika chupa ya uhai akiwa ameikumbatia kana kwamba hakutaka mtu yeyote aichukue kutoka katika mkono wake.
“Twende ndani ukalale mume wangu” Bi Fatuma alimwambia mume wake, mzee Kessi ambaye hakuonyesha hata dalili kwamba angekwenda kulala chumbani.
“Niache nilale hapa hapa” Mzee Kessi alisema kwa sauti iliyojaa ulevi.
Kila kitu kilikuwa kikionekana kuwa kama zamani. Mzee Kessi alikuwa akilewa kila siku jambo ambalo lilionekana kumkasirisha sana mke wake, Bi Fatuma. Mara kwa mara mzee Kessi alikuwa akirudi nyumbani hapo usiku mkali huku akiwa amelewa kupita kawaida.
Maisha ya ulevi yakaonekana kuwa sehemu ya maisha yake, hakupenda wanawake hata kidogo, starehe yake kubwa wala haikuwa ngono kama walevi wengine, pombe ndio ilionekana kuwa starehe yake kubwa ambayo alikuwa akiipenda kupita kawaida.
Miaka mingi ya nyuma, mzee Kessi hakuwa mlevi kabisa, alikuwa mtu safi, Muislamu ambaye alikuwa akiswali swala tano kila siku. Kila kitu kikaanza kubadilika pale ambapo alipokuja kuchujwa kazini kutokana na kampuni kuwa na wafanyakazi wengi ambao wengine hawakuonekana kuwa na kazi yoyote kazini.
Tukio lile likaonekana kumhuzunisha sana mzee Kessi, kila siku akawa mtu wa mawazo, japokuwa mke wake alikuwa akimfariji sana lakini faraja ile wala haikuonekana kubadilisha kitu chochote kile. Hapo ndipo alipoamua kuanza kunywa pombe kwa kisingizo cha kupunguza mawazo aliyokuwa nayo.
Kila alipokuwa akilewa, mawazo yalikuwa yakimtoka kichwani mwake lakini pombe zilipokuwa zikiisha kichwani mwake, mawazo yalikuwa yakirudi kama kawaida. Mzee Kessi hakufikiria kuanzisha biashara yoyote ile japokuwa alikuwa amelipwa kiasi kikubwa cha fedha. Fedha ambazo alikuwa ameliwa akaziingiza kwenye ulevi.
Baada ya mwaka mmoja kupita, hali ya umasikini ambayo ilikuwa ikiwanyemelea ikawaingia. Fedha zikakatika, hapo ndipo akili ya mzee Kessi ilipoanza kukaa sawa. Akaanza kufanya kazi mbalimbali kama ujenzi na kazi nyingine ndogondogo.
Hawakuweza kugharamia gharama za chumba kikubwa ambacho walikuwa wakikaa maeneo ya Block P jambo ambalo likawafanya kuhamia Kisutu tena katika nyumba mbovu isiyokuwa na thamani yoyote ile.
“Mtakaa kwa muda kabla ya nyumba hii kubomolewa. Nimeamua kukusaidi kwa sababu sisi ni marafiki wa kitambo sana” Mzee Shomari alimwambia mzee Kessi.
Hapo ndipo maisha yao yalipoanzia. Maisha ya ndoa hayakuwa ya amani hata mara moja, kila siku mzee Kessi alikuwa akimpiga mke wake hasa katika kipindi ambacho alikuwa akilewa na kurudi nyumbani. Bi Fatuma alionekana kuwa mvumilivu kwa kila kitu, japokuwa alikuwa akipigwa lakini alikuwa akimpenda sana mume wake.
Siku zikaendelea kukatika, maisha ya Kisutu yakaonekana kuwazoea. Mara kwa mara mzee Kessi alikuwa akigombana na majirani zake kwa tabia zake za kurudi usiku na kupiga kelele ovyo. Japokuwa alikuwa akigombana sana na majirani zake lakini kamwe mzee Kessi hakutaka kubadilika, ndio kwanza alikuwa akipiga kelele zaidi na zaidi kila siku.
Katika maisha yao ya miaka ishirini na tano ya ndoa ambayo waliishi pamoja kama mume na mke, wawili hao walifanikiwa kupata mtoto mmoja tu wa kiume aliyeitwa Yusufu. Kipindi cha nyuma Yusufu ndiye ambaye alionekana kuwaunganisha wote wawili na kuwapa amani kubwa katika maisha yao ya ndoa, walimthamini sana Yusufu na kumpa kila kitu ambacho alikuwa akikihitaji kama mtoto wao, hasa katika kipindi kile ambacho walikuwa na fedha za kutosha.
Kwa sasa Yusufu hakuwa pamoja nao, alikuwa amekwishaanza maisha yake ndani ya jiji la Dar es Salaam huku muda mwingi akiwa anaelekea Bagamoyo kwa ajili ya kuwaona wazazi wake. Hali ambayo walikuwa nayo wazazi wake ikaonekana kumuumiza sana jambo ambalo likamfanya kutafuta sana fedha ndani ya jiji la Dar es Salaam kwa ajili ya kuwatunza wazazi wake ambao walikuwa wakiishi maisha mabovu ambayo hakuyapenda kabisa.
“Nitapata fedha tu na ninyi mtaishi kwenye nyumba nzuri kama ile ya mtaa wa Block P” Yusufu alikuwa akipenda kuwaambia wazazi wake maneno hayo katika kila kipindi alichokuwa akienda kuwasalimia.
*****
Maisha ndani ya jiji la Dar es Salaam hayakuwa rahisi hata mara moja. Kila siku Yusufu alikuwa akifanya kazi mbalimbali lakini wala hazikuweza kubadilisha maisha yake. Kazi zake zilianzia katika kubeba mizigo katika soko la Tandale, huko, maisha yaliendelea kuwa vile vile jambo ambalo likamfanya kuamua kufanya kazi ya ukonda, kwa mbali maisha yake yakaonekana kupata mwanga.
Japokuwa kila siku Yusufu alikuwa na uhakika wa kupata fedha zaidi ya shilingi elfu kumi lakini gharama mbalimbali za maisha ya Dar es Salaam zikamfanya kutumia kiasi kikubwa cha fedha kila siku ambacho hadi inafika usiku, hakuwa na fedha za kutosha mifukoni mwake.
Maisha yale yalikuwa yakimuumiza sana, hakuyapenda maisha yale ya umasikini ambayo alikuwa akiishi katika kipindi kile, nafsi yake ilikuwa ikitamani kuishi maisha ya kifahari, maisha ya kutanua mitaani na gari, maisha ya kuchukua kila aina ya msichana ambaye alikuwa akimtaka.
Maisha yaliendelea zaidi na zaidi, urafiki wake na Kelvin ukaonekana kuwa mkubwa, wakapanga chumba kimoja na kuishi pamoja. Gharama za kulipia chumba ilikuwa jukumu lao wote. Kila siku asubuhi wote walikuwa wakitoka pamoja na kwenda kutafuta fedha kwa kufanya kazi mbalimbali na usiku kurudi wote.
Maisha hayakuonekana kubadilika, kila walipokuwa wakipata fedha ambazo wala hazikumaliza shida ambazo walikuwa nazo. Fedha ambazo walikuwa wakizipata ziliwatosha katika chakula na kubadilisha mavazi tu.
“Maisha magumu sana” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Yaani ni magumu kiasi ambacho wakati mwingine nafikiri ni bora ningekuwa mwizi tu” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Hivi hali hii tutakuwa nayo milele au kuna siku itakuja kubadilika?” Kelvin aliuliza.
“Mmmh! Nafikiri itakuwa hivi milele. Kama unaona kuna siku itakuja kubadilika, itabadilika vipi? Tutapata vipi fedha za kufanyia mambo mengine ambayo hatujayafanya?” Yusufu aliuliza.
“Kufanya mambo gani zaidi?”
“Kumiliki magari, kuwa na mademu wakali, fedha za kutosha na kufanya mambo mengine pia” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Yaani bado unafikiria wanawake tu?” Kelvin aliuliza huku akitabasamu.
“Wewe unafikiri nitafikiria nini zaidi? Ili ujione umefanikiwa katika kila kitu basi ni lazima utembee na msichana yeyote unayemtaka kwa kipindi hicho. Hivi unafikiri kama ningekuwa na fedha yule Agness angenikataa?” Yusufu alisema na kuuliza.
“Ndio. Angekukataa” Kelvin alijibu.
“Thubutuuuuu. Niwe nimemfungia breki miguuni mwake na Range, nashusha kioo na kisha kuongea naye, unafikiri angenikataa. Acha masihala Kelvin, fedha ndio kila kitu katika maisha haya” Yusufu alimwambia Kelvin.
Siku hiyo ilikuwa kama siku nyingine tu, muda wote walikuwa wakiongea kuhusu fedha, walikuwa wakihitaji fedha kuliko kitu chochote kile katika maisha yao. Maisha ya kifahari ambayo walikuwa wakiishi watu wengine yalikuwa yakiwatamanisha kupita kawaida.
“Hivi inakuwaje kuhusu kipaji chako cha muziki? Hakitaweza kukutoa kwenye maisha haya kweli?” Kelvin alimuuliza Yusufu.
“Mmmh! Nafikiri hakiwezi” Yusufu alijibu.
“Hakuna bwana. Inakupasa kujaribu, huwezi jua, unaweza kuwa kama The King” Kelvin alimwambia Yusufu huku akimtaja msanii wa muziki ambaye alikuwa juu sana katika kipindi hicho nchini Tanzania.
“Kitu cha kwanza ni lazima tukumbuke kwamba kurekodi muziki si chini ya shilingi laki tano. Unaweza ukagharamia muziki kwa kiasi hicho halafu mwisho wa siku Madj wa vituo mbalimbali wakaanza kukubania tena” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Ila ngoja tujaribu” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Poa. Ila fedha tutazipata wapi? Kutunga nyimbo si jambo gumu kwangu, tatizo upatikanaji wa fedha za kurekodia tu” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Hakuna jinsi Yusufu. Kila kitu kinaonekana kuwa kigumu kwetu. Nitafanya kitu kimoja kwa ajili ya kuhakikisha kwamba unapata fedha za kurekodia” Kelvin alimwambia Yususfu.
“Kitu gani?”
“Kuiba”
“Acha masihala Kelvin”
“Hakuna jinsi Yusufu. Acha nijaribu kwa ajili yako ila nakuomba nawe fanya kitu kimoja tu” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Kitu gani?”
“Tunga wimbo mkali, wimbo ambao kila atakayeusikia ataupenda na kuanza kukuita sehemu mbalimbali kwa ajili ya kutumbuiza kwenye matamasha mbalimbali” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Hilo si tatizo. Ila na wewe itakubidi kuwa makini kwenye kufanya huo wizi wako. Si unajua sitaki kukupoteza” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Najua. Usijali, kila kitu kitakuwa sawa” Kelvin alimwambia Yusufu na kisha kulala huku kila mtu kichwa chake kikifikiria fedha tu.
*****
Muda ulikuwa ni saa 2.14 asubuhi, Kelvin alikuwa akilandalanda katika barabara za Posta Mpya huku macho yake yakiangalia katika kila gari ambalo lilikuwa limepakiwa. Kichwa chake kwa wakati huo kilikuwa kikifikiria kitu kimoja tu, kufanya wizi wa kitu chochote kile ambacho atakiuza na mwisho wa siku kupata fedha ambazo zitamfanya Yusufu kuingia studio na kurekodi muziki.
Idadi kubwa ya watu ambao walikuwa wakitembea huku na kule ilimfanya kuhofia sana kufanya kile ambacho alikuwa akitaka kukifanya. Mara nyingi alikuwa akiyaona magari ambayo ndani kulikuwa na laptop pamoja na simu za gharama kubwa lakini kukishusha kioo kwa kutumia waya mgumu aliokuwa nao lilikuwa jambo gumu kufanyika.
Alipoona kwamba kila kitu kimeshindikana, hapo ndipo akaamua kwenda katika ghorofa la Macafee lililokuwa Posta mtaa wa Samora View na kisha kupanda kule ambako magari yalikuwa yakiegeshwa. Kelvin akaanza kutembea huku na kule huku akiyaangalia magari yale ambayo yalikuwa yamepakiwa.
Tayari hali ikaonekana kuwa rahisi kwake, kutokana na kuwa na idadi ndogo ya watu ikaonekana kuwa kama nafasi kubwa kwake ya kuanza kufanya kile ambacho alikuwa amepanga kukifanya. Alichokifanya kwa wakati huo ni kuanza kulifuata gari moja la kifahari, Range ambalo lilikuwa limepakiwa pembezoni kabisa mwa sehemu ile ya kuegesha magari.
Alipolifikia, akaanza kuangalia huku na kule kuona kwamba hakukuwa na mtu yeyote ambaye alikuwa akimwangalia, alipoona kwamba kila kitu kipo salama, akaanza kuchungulia ndani ya gari lile huku akiuandaa waya wake.
Macho yake yakatua kwenye laptop moja aina ya Apple pamoja na simu mbili za aina ya iPhone 5. Kelvin hakutaka kuchelewa, kwa hali jinsi ilivyoonekana, ilionyesha kwamba mwenye gari angerudi muda wowote ule kutokana na vitu vyake vyote kuwa ndani ya gari.
Akauchukua waya wake na kisha kuupitisha kwenye uwazi wa kioo ambao ulikuwa umeachwa kwa ajili ya hewa na kisha kuangaika kuitoa loki kwa kutumia waya ule. Kazi haikuwa ndogo hata kidogo, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka huku akihakikisha kwamba haligusi gari hilo hata kidogo kwa kuona kwamba lingepiga kelele ya kumshtua mmiliki wa gari lile.
Alijitahidi sana huku kijasho kikiendelea kumtoka, kila alipokuwa akiikamata loki ya mlango wa gari ile na kujaribu kuivuta kwa kutumia waya ule, loki ilionekana kuwa ngumu kuvutika. Kelvin hakutaka kukata tamaa, kila alipokuwa akiziangalia mali zilizokuwa ndani ya gari lile aliendelea kuvuta zaidi na zaidi.
Huku akiwa anaendelea na kazi yake, mara sauti za watu zikaanza kusikika kutoka katika upande mwingine jambo lililomfanya kuinama na kuanza kusikilizia kwa makini kama watu wale walikuwa wakija upande aliokuwepo. Akasikia mlango wa gari moja ukifunguliwa, watu wale kuingia na kisha gari kuwashwa na kuondoka mahali hapo.
Kelvin akaendelea kufanya kazi yake kama kawaida. Hakujua alijisahau vipi mpaka kuligusa gari lile, ghafla likaanza kupiga kelele. Kadri sekunde zilivyokuwa zikizidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo kelele zile zilivyozidi kuwa za juu zaidi na zaidi jambo ambalo liliwashtua walinzi ambao walikuwa wamewekwa kuhakikisha ulinzi wa magari yale yaliyokuwa yamepakiwa kwenye ghorofa ile kwa juu.
Vishindo vya watu vilikuwa vikisikika vikija kule ambako alipokuwepo, sehemu ambayo gari ile ilikuwa ikiendelea kupiga kelele. Kelvin alikuwa akiendelea zaidi na zaidi kuhakikisha kwamba mlango unafunguka na kisha kuchukua mali zile ambazo zilikuwa kwa juu kabisa.
Kila alipokuwa akijitahidi kutoa loki ile, loki ilionekana kuwa ngumu kufunguka jambo ambalo lilionekana kumtia wasiwasi zaidi. Kuondoka mahali hapo hakutaka kabisa, hakutaka kuondoka na kuziacha mali zile ambazo kwa haraka haraka zilikuwa na thamani isiyopungua milioni sita.
“Funguka. Loki funguka” Kelvin alisema huku akiendelea kufungua loki ile kwa kutumia waya mgumu huku walinzi wale wakizidi kusogea kule kulipokuwa na gari lile ambalo lilikuwa likizidi kupiga kelele.
*****
Walinzi ambao walikuwa na bunduki walikuwa wakizidi kusogea kule ambako kulikuwa na gari lile lililokuwa likipiga kelele, tayari walikwishajua kwamba kuna mtu ambaye alikuwa ameligusa gari lile na hivyo kuanza kupiga kelele. Tayari wasiwasi kwamba mtu aliyeligusa gari lile alikuwa mwizi ukaanza kuwaingia akilini.
Wakaziandaa silaha zao tayari kwa ajili ya kumfyatulia risasi mtu huyo ambaye alikuwa ameligusa gari lile kwa lengo la kuliiba au kuiba kitu chochote kile ambacho kilikuwa ndani ya gari lile. Wakaongeza kasi zao zaidi na zaidi mpaka kulifikia gari hilo ambali lilikuwa likiendelea kupiga kelele kama kawaida.
Hakukuwa na mtu yeyote ambaye alikuwa akionekana mahali hapo, milango yote ilikuwa imefungwa kama kawaida japokuwa gari lile lilikuwa likiendelea kupiga kelele. Walichokifanya kwa wakati huo ni kuanza kuangalia huku na kule kuona kama wangeweza kumuona mtu yeyote ambaye alikuwa ameligusa gari lile lakini hawakumuona mtu yeyote.
“Mbona patupu?” Mlinzi mmoja alimuuliza mwenzake.
“Inawezekana kuna ndege aliingia na kuligusa” Mlinzi mwingine alimwambia mwenzake.
“Labda inaweza kuwa hivyo”
Mara mmiliki wagari lile ambaye alikuwa mwanamke wa makamo akatokea mahali hapo huku akiwa na ufunguo wa gari lake na kisha kuanza kuwaangalia walinzi wale ambao walikuwa wamesimama pembeni ya gari lake.
“Kuna nini? Alamu imenishtua kwamba kuna kitu kimetokea garini mwangu?” Mwanamke yule aliuliza.
“Hata sisi tulisikia alamu na ndio maana tukafika haraka sana ila hatukuona mtu. Inawezekana kuna ndege alikuja na kutua kwenye gari lako” Mlinzi mmoja alimwambia mwanamke yule.
Alichokifanya mwanamke yule ni kuufuata mlango wa gari lake na kisha kuufungua. Macho yake hayakuamini kile ambacho alikuwa akikiona mahali pale, laptop yake pamoja na simu zake mbili hazikuwa zikionekana. Hapo hapo akawageukia walinzi huku macho yake yakionekana kubadilika.
“Nani kachukua simu zangu na laptop yangu?” Mwanamke yule aliuliza swali ambalo liliwafanya walinzi wote kushangaa.
“Unasemaje?” Mlinzi mmoja aliuliza.
“Nani ameniibia simu zangu na laptop yangu?” Mwanamke yule aliuliza kwa sauti ya juu.
Walinzi wote wakapigwa na mshangao, maneno aliyoongea mwanamke yule yakaonekana kuwashangaza kupita kawaida. Hawakujua kwamba kuna vitu vilikuwa vimeibiwa ndani ya lile gari, wakausogelea mlango ule na kuchungulia ndani.
“Nimeibiwa” Mwanamke yule alisema huku akionekana kukasirika.
“Mbona tulipokuja hapa hatukuona mtu yeyote?”
“Ila nimeibiwa. Nimeibiwa kila kitu nilichokiacha ndani ya gari langu. Hadi pochi yangu imeibwa ambayo ilikuwa na fedha nyingi pamoja na kadi yangu ya ATM” Mwanamke yule alisema maneno yaliyowafanya walinzi wale kuondoka mahali hapo na kuanza kuzunguka huku na kule kwa lengo la kumtafuta mtu aliyeiba simu, laptop na pochi ya yule mwanamke.

Je nini kitaendelea?
Je Kelvin atakamatwa?
Je Yusufu ataweza kutoka kimaisha na Kelvin?

Huu ni mwanzo tu, kuna mengi yanakuja na mengi mtajifunza.
 
Mi story mingiiii bila hata mwendelezo.
Huna kazi wewe wala lakujifunza humu jf zaidi ya kucopy mistoy ya watu isiyo na mwendelezo.
 
Mi story mingiiii bila hata mwendelezo.
Huna kazi wewe wala lakujifunza humu jf zaidi ya kucopy mistoy ya watu isiyo na mwendelezo.
Mtoto wa kiume na wewe hiyo staili ya kuvaa nguo chini ya makalio umecopy wapi?
Angalia usije ukawa jamii wa akina James Delicious shauri yako
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 2.

KWA WASOMAJI WAPYA.

Maisha yanaonekana kuwa magumu kwa Yusufu na Kelvin. Kila siku wameonekana kuwa watu wa kuhitaji fedha tu. Wanapoona kwamba maisha hayabadiliki kabisa, hapo ndipo Yusufu anashauriwa kutumia kipaji chake cha muziki ili kiweze kuwaondoa katika maisha hayo ya shida.
Kutunga wimbo si tatizo, tatizo ni mahali ambapo wangepata fedha na hatimae kuurekodi wimbo hio. Hapo ndipo Kelvin anapoamua kuyaweka maisha yake rehani, anakwenda Posta, analiona gari limeegeshwa sehemu ya maegesho ghorofani, anapoangalia ndani, macho yake yanatua katika laptop aina ya Apple pamoja na simu aina ya iPhone.
Hataki kuziacha, tayari kichwa chake kimekwishapiga hesabu kwamba zile ni zaidi ya milioni tatu, anachoamua ni kuchukua waya mgumu na kuupitisha katika kitundu cha kioo kwa ajili ya kutoa loki. Huku akiendelea na kazi hiyo, hajui aliligusa vipi gari lile, likaanza kupiga alamu ambayo ikawafanya walinzi kuanza kusogea kule lilipokuwa huku wakiwa na silaha.

Je nini kitaendelea?
TWENDE PAMOJA.

Kelvin alikuwa akiendelea kujitahidi kuufungua mlango ule, sauti za walinzi ambao walikuwa wakija kwa kasi zilikuwa zikizidi kusikika masikioni mwake. Tayari kijasho chembamba kilichokuwa kikimtoka kilizidi kuongezeka zaidi na zaidi na kuliloanisha shati alilokuwa amelivaa.
Loki ilionekana kuwa ngumu kuvutika kwa juu, alijitahidi zaidi na zaidi, bahati ikaonekana kuwa upande wake, loki ile ikafanikiwa kupanda kwa juu. Hiyo ikaonekana kuwa nafuu kwake, alichokifanya mahali hapo tena kwa haraka sana ni kuufungua mlango.
Hakutaka kuchelewa hata mara moja, kila kitu ambacho alikuwa akikifanya mahali hapo alikuwa akikifanya kwa haraka haraka. Kitu cha kwanza akachukua laptop ile aina ya Apple pamoja na simu zile mbili zilizoonekana kuwa za gharama na kisha kutaka kutoka nje.
Huku akionekana kutokuamini, macho yake yakatua katika pochi kubwa iliyokuwa mule ndani ya gari. Hakutaka kuifungua na kujiuliza kwamba ndani ya pochi ile kulikuwa na nini, alichokifanya mahali hapo ni kuichukua na kutoka nayo.
Akaufunga mlango kama ulivyokuwa na kisha kuondoka mahali hapo kwa mwendo wa kuinamainama. Kasi yake ya kutembea ilikuwa kubwa sana jambo lilimfanya kufika sehemu ya kushukia chini na kisha kuanza kukimbia.
Tayari moyo wake ukaonekana kuwa na furaha, alipofika chini, akajibanza sehemu ambayo ilikuwa na ukuta na kisha kuifungua pochi ile. Fedha ambazo alikutana nazo ndani ya ile pochi zikaonekana kumchanganya kupita kawaida.
“Zaidi ya milioni tatu hizi” Kelvin alijisemea huku akikenua kwa furaha.
“Kuna kadi ya benki pia. Huu sasa utajiri” Kelvin aliendelea kujisemea huku akiwa ameipekua ile pochi kwa haraka sana.
Hakutaka kuendelea kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuondoka kwa mwendo wa kasi na kuanza kuifuata bajaji ambayo ilikuwa imepakiwa karibu na benki ya Kihindi iliyokuwa posta karibu kabisa na Maktaba ya Taifa.
“Nipeleke Tandale” Kelvin alimwambia dereva wa bajaji.
“Elfu kumi”
“Wewe nipeleke tu”
Safari ya kuelekea Tandale ikaanza mahali hapo kwa kupitia njia ya Salander Bridge. Muda wote Kelvin alikuwa akiangalia nyuma huku akionekana kuwa na wasiwasi wa kufuatiliwa. Alipoona kwamba kila kitu kipo salama, akaitoa ile kadi ya benki ya ATM ya CRDB na kisha kuanza kuiangalia.
Namba zote za akaunti ile, jina zilikuwa zikionekana lakini hakuwa akifahamu namba za siri. Kelvin akatulia kwa muda huku kichwa chake kikifikiria kitu. Alikaa katika hali ile na ndipo hapo alipoamua kuchukua simu moja kati ya zile mbili na kuanza kupekua.
Kwanza akaenda katika sehemu ya majina na kuanza kuangalia majina mbalimbali. Tayari kichwa chake kilikuwa na uhakika kwamba namba za siri za kadi ile zingekuwa kwenye simu ile. Aliangalia jina moja hadi jingine mpaka pale alipofikia jina lililosomeka CRDB.
Hakutaka kujiuliza, alichokifanya mahali hapo ni kuangalia namba zile na macho yake kutua kwenye namba zilizosomeka 2389. Kuanzia hapo akawa na uhakika kwamba namba zile ndizo zilikuwa namba za siri za kadi ile ya ATM.
“Unaweza kupitia Magomeni pale kituo cha mafuta?” Kelvin alimuuliza dereva wa bajaji.
“Yeah! Ila itabidi tupitie huku Kinondoni”
“Hakuna noma”
Safari iliendelea zaidi na zaidi. Walipofika Kinondoni Manyanya, wakaonganisha kuelekea Magomeni. Muda wote kichwa cha Kelvin kilikuwa kikiendelea kufikiria kiasi cha fedha ambacho angeweza kukutana nacho katika akauti ya yule mwanamke.
“Hivi leo lini?” Kelvin alimuuliza dereva wa bajaji.
“Jumamosi”
“Safi sana. Saa yako inaonyesha saa ngapi?”
“Saa nane na robo”
“Hapo imetulia zaidi” Kelvin alimwambia dereva.
Tayari kichwa chake kilikuwa kikifikiria mbali zaidi. Kwanza alikuwa akifikiria namna ya kukitoa kiasi kile cha fedha ambacho kilikuwa kwenye akaunti ile. Alijua fika kwamba kiasi cha mwisho kutoa fedha kwenye mashine za ATM za CRDB kilikuwa mwisho shilingi milioni tatu kwa siku.
Alichokuwa akitaka kukifahamu kwa wakati huo ni mara ngapi angeweza kutoa kiasi hicho hata kabla ya mwanamke yule kufunga akaunti yake. Tayari alikwishaona kwamba kama kiasi kingekuwa kikubwa zaidi basi angeweza kutoa kiasi cha shilingi milioni sita, yaani akiwa na maana kwamba shilingi milioni tatu angezitoa siku hiyo na milioni tatu angezitoa siku inayofuatia, siku ambayo mwanamke yule angekuwa hajaifunga akaunti ile kwa kuwa huduma za kibenki zisingekuwa zinatolewa siku hiyo.
“Tumekwishafika” Dereva alimwambia Kelvin huku akiwa amesimamisha gari katika kituo cha mafuta cha Magomeni.
Kwa haraka haraka Kelvin akateremka na kuingia katika chumba cha mashine ya ATM ya CRDB na kisha kuchukua ile kadi na kuichomeka. Alipotakiwa kuingiza namba za siri, akaingiza namba zile ambazo alikuwa ameziona kwenye simu ile. Namba zikakubali na kisha kuangalia salio. Salio la shilingi milioni thelathini na tano lilikuwa likionekana katika akaunti ile.
“Mungu wangu! Huu utajiri sasa” Kelvin alisema na kisha kutoa kiwango cha mwisho kabisa cha shilingi milioni moja na nusu na kisha baada ya saa moja kutoa kiasi kama hicho na kuondoka mahali hapo.
Tayari akayaona maisha yakiwa yamebadilika sana, umasikini ambao alikuwa akiishi pamoja na Yusufu ukaonekana kuanza kupotea taratibu. Bajaji ikaendedelea na safari mpaka Tandale ambako akateremka na kumlipa dereva wa bajaji kiasi kilichohitajika na kuelekea ilipokuwa nyumba ambayo walikuwa wamepanga.
“Vipi tena? Mbona unaonekana kuwa na furaha?” Yusufu alimuuliza Kelvin.
“Umekwishatunga wimbo wenyewe kesho twende studio?” Kelvin alimuuliza Yusufu.
“Ndio naendelea nao, upo katika hatua za mwisho kumalizika” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Poa. Wewe jitahidi, yaani nataka wiki hii hii twende studio” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Sawa. Ila mbona unaonekana kunificha kitu fulani. Kumetokea nini uko ulipokwenda?” Yusufu aliuliza.
Hapo ndipo Kelvin alipoanza kumhadithia Yusufu kila kitu ambacho kilitokea toka katika sehemu ya kuegesha magari iliyokuwa ghorofani na mpaka alipoufungua mlango ule na kuchukua kila kitu alichokiona kufaa kuchukuliwa.
“Una hatari sana Kelvin” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Nimefanya hivi kwa ajili yako tu. Nataka kuwekeza fedha zangu katika kipaji chako cha muziki” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Daah! Shukrani sana. Ninaahidi kujitolea zaidi na zaidi” Yusufu alimwambia Kelvin.
Hapo ndipo maisha ya usanii yalipoanzia. Mpaka akaunti ya mwanamke yule inafungwa, tayari Kelvin alikuwa amekwishachukua kiasi cha shilini milioni tisa katika mashine mbalimbali za ATM zilizokuwa ndani ya jiji la Dar es Salaam huku kiasi kingine cha shilingi milioni tatu akiwa amekitoa asubuhi ya Jumatatu.
Yusufu akaanza kurekodi muziki katika studio ya Metropolian iliyokuwa Kijitonyama jijini Dar es Salaam. Wimbo wake ulikuwa mzuri sana ambao aliamini kwamba ungeweza kumtambulisha katika jamii kwamba alikuwa mmoja wa wanamuziki wanaochipukia.
Japokuwa wimbo ulikuwa mzuri lakini bado fedha zilikuwa zikihitajika kutumika kuwahonga madj mbalimbali wa vituo vya redio kwa ajili ya kuupiga wimbo wake. Kila siku Kelvin alikuwa akionekana kuwa karibu nae zaidi. Japokuwa walikuwa wakitumia kiasi kikubwa cha fedha lakini Kelvin hakuonekana kujali kabisa, bado alikuwa akiendelea kutumia fedha zile.
“Haujaanza kuitwa hata kwenye matamasha mbalimbali?” Kelvin aliuliza huku akionekana kutokuamini.
“Bado”
“Daah! Kwa hiyo tufanye nini sasa?”
“Kwani umebakiwa na kiasi gani hapo?”
“Milioni sita na nusu tu”
“Ngoja nirekodi wimbo wa pili halafu tuangalie upepo” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Sawa”
Hakukuwa na cha kusubiri, kwa sababu nyimbo zilikuwa nyingi, Yusufu akautoa wimbo wa pili. Hali haikubadilika, bado ilionekana kuwa vile vile, watu walikuwa wakiuona kuwa wimbo wa kawaida sana. Jambo hilo likaonekana kumuumiza sana Yusufu, kila siku alikuwa akitumia kiasi kikubwa cha fedha lakini hali haikuonekana kubadilika.
“Kwa hiyo tufanye nini sasa?” Yusufu aliuliza huku akionekana kukata tamaa.
“Tutoe video, inawezekana ikaleta hamasa kwa watu. Si unajua watu siku hizi hawapendi kusikiliza redio kwa sana” Kelvin alimwambia Yusufu.
Uamuzi huo ndio ambao ulikuwa umefikiwa kwa kipindi hicho, wakakubaliana na kampuni ya kurekodi video ya Metro iliyokuwa Sinza na kisha kurekodi video hiyo ambayo iliwagharamu kiasi cha shilingi laki tisa.
Kidogo, wimbo huo ukaonekana kuanza kusikika katika masikio ya watu kiasi ambacho kikamfanya Yusufu kuanza kutambulika kama msanii. Hapo ndipo alipoanza kuitwa kwenye matamasha madogo na kisha kuanza kutumbuiza.
Japokuwa alikuwa msanii mdogo ambaye alikuwa akichipukia lakini alionekana kuwa mkali katika siku za usoni. Matamasha mbalimbali ambayo alikuwa akiitwa kwa ajili ya kutumbuiza ndio ambayo kwa kiasi fulani yakaonekana kuanza kumuingizia fedha huku akizitumia pamoja na Kelvin ambaye alionekana kuwa kama familia yake pia.
Yusufu hakutaka kuwasahau wazazi wake, alichokuwa akikifanya ni kuwatumia fedha hata wazazi wake ambao walionekana kufurahia kipaji cha muziki ambacho alikuwa nacho Kelvin. Kila siku Kelvin alikuwa akijitahidi kutunga nyimbo mbalimbali, kitu ambacho alikuwa akikihitaji kwa wakati huo ni fedha za kutosha pamoja na umaarufu tu kwa kuona kwamba kama angekuwa maarufu basi angeweza kuingiza fedha zaidi.
“Fedha na umaarufu” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Vimefanya nini sasa?” Kelvin aliuliza.
“Ndio ninavyovitaka. Ili uweze kuuza basi ni lazima uwe maarufu” Yususfu alimwambia Kelvin.
“Na ili uwe maarufu basi ni lazima uwe na fedha” Kelvin alimwambia Yusufu.
Kila siku Yusufu alikuwa akitamani kuwa na umaarufu mkubwa pamoja na kupata fedha za kutosha, tayari alikwishaona kwamba alikuwa akikaribia kuupata umaarufu na kupata fedha kama ambavyo alivyotaka. Alitamani kuona nyimbo zake zikisikilizwa na watu wengi, kupata mashabiki wengi kwa kuamini kwamba ndio angeuza kupita kawaida.
“Inabidi utoe wimbo mmoja wa mwisho na tuangalie upepo” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Sawa”
“Ila wimbo huu itakubidi ufanye kitu kimoja” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Kitu gani?”
“Itakubidi umshirikishe The King” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Itawezekana kumlipa fedha atakazozihitaji? Naona kama atahitaji kiasi kikubwa cha fedha” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Nafikiri hilo halitakuwa tatizo. Una kiasi gani kwa sasa?” Kelvin alimuuliza Yusufu.
“Milioni tatu na nusu”
“Inatosha sana. Hapa nina milioni mbili. Cha msingi tunamuita, unarekodi nae wimbo na kisha tunarekodi na video tuone itakuwaje” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Sawa. Haina noma”
*****
Msanii wa muziki wa kizazi kipya, Jumanne Rajabu ndiye alikuwa msanii ambaye alikuwa akisifika na kusikika sana nchini Tanzania kwa wakati huo. Msanii huyo alikuwa na mashabiki wengi nchini Tanzania na hata nje ya nchi ya Tanzania kiasi ambacho alikuwa akiingiza kiasi kikubwa cha fedha katika kila shoo moja ambayo alikuwa akifanya.
Watanzania wakamkubali kupita kawaida, kila alipokuwa akipita Jumanne ambaye alikuwa akijulikana kwa jina la kisanii kama The King, watu walikuwa wakimpiga picha huku wengine wakitaka hata kupiga nae picha.
Jina lake lilikuwa likizidi kuvuma kupita kawaida, kwa kila wimbo ambayo alikuwa akiimba, ulikuwa ukipendwa sana hata kama ilikuwa mbaya kiasi gani. Nyota ya kupendwa ambayo alikuwa nayo ikaonekana kuwa na mvuto mkubwa sana kwa mashabiki mbalimbali wa muziki Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla.
The King hakuwa mtu wa kutulia, mara kwa mara alikuwa akiitwa sana nje ya nchi kwa ajili ya kufanya shoo ambazo zlikuwa zikimuingizia sana fedha, fedha ambazo zilikuwa zimebadilisha maisha yake kwa kiasi kikubwa sana. Katika kila wimbo ambayo The King alikuwa akishirikishwa, watu walikuwa wakiupenda hata kama huyo aliyemshirikisha alikuwa akiimba vibaya.
Nembo ya jina lake ilikuwa ya kibiashara sana, mvuto ambao alikuwa nao ulionekana kuwa mkubwa sana jambo ambalo kila wakati alikuwa akinukia fedha tu. The King akanunua magari ya kifahari pamoja na kumiliki nyumba mbili za kifahari sana. Maisha yake yote alikuwa akitegemea muziki ambao ulikuwa ukimuuingizia kiasi cha shilingi milioni ishirini kwa shoo mbili tu ambazo alikuwa akizifanya kwa mwezi.
The King hakuwa mchoyo, kwa kila msanii ambaye alikuwa akitaka kushirikiana nae, alikuwa akishirikiana nae kama kawaida tena kwa malipo ya chini kwa kugundua kwamba kiasi ambacho angekihitaji chenye hadhi ya jina lake, wasanii wasingeweza kumlipa.
Wasanii wengi walikuwa wakipanga foleni katika kutaka kushirikiana na msanii huyo katika nyimbo zao mbalimbali. Zaidi ya wasanii kumi ambao alikuwa amewahi kushirikiana nao tayari majina yao yalikuwa yakijulikana sana nchini Tanzania.
“Mnataka kunishirikisha kwenye wimbo wenu?” The King alimuuliza Kelvin simuni.
“Ndio” Kelvin alijibu.
“Sawa. Mna kiasi gani?”
“Tunakusikiliza wewe mkuu”
“Mna milioni mbili?” The King aliuliza.
“Hizo nyingi sana kwetu mkuu”
“Sawa. Ninyi mna kiasi gani?”
“Milioni moja tu”
“Ongezeni nusu”
“Sawa. Hakuna tatizo”
“Sawasawa. Ila kutokana na ratiba niliyokuwa nayo pamoja na kiasi mnachotoa, hakuna budi mkasubiri mpaka mwezi wa tisa” The King alimwambia Kelvin ambaye alionekana kushtuka.
“Mwezi wa tisa?” Kelvin aliuliza huku akionekana kushtuka kwani muda huo ndio kwanza ilikuwa mwezi wa pili.
“Ndio. Mkipanda dau zaidi napo miezi inapungua zaidi” The King aliwaambia.
“Sisi tunataka tufanye kazi hata wiki ijayo mkuu”
“Kama wiki ijayo, fanyeni tu milioni mbili” The King aliwaambia.
Hakukuwa na kukataa tena, kwa wakati huo tayari walikwishaona kwamba wanahitaji sana kupata fedha nyingi zaidi na zaidi, hivyo kiasi kile cha fedha ambacho walikuwa wakihitajika kukitoa wala hakikuwa na tatizo lolote lile kwani waliamini kwamba wangeweza kupata kiasi kikubwa cha fedha endapo wangefanya kazi na The King.
*****
Kila siku Yusufu na Kelvin walikuwa wakielekea katika nyumba ya The King kwa ajili ya kuuchukulia mazoezi wimbo ambao tayari walikuwa wamekwishautunga. Mara kwa mara The King hakuwa mtu wa kushinda nyumbani jambo ambalo liliwafanya Yusufu na Kelvin kurudi ndani ya nyumba hiyo bila ya mafanikio yoyote.
Ubize wa The King, kusafiri nchi mbalimbali kwa ajili ya kufanya shoo mbalimbali kulimfanya kuwa na wakati finyu sana wa kukutana na Yusufu na kufanya kazi kama ambavyo alikuwa amemuahidi kabla.
Yusufu hakuonekana kukata tamaa kumfuata The King, kwake, mtu huyo alionekana kuwa muhimu sana ambaye angemfanya kusikika katika masikio ya Watanzania na kumjua kwamba alikuwa nani katika anga nzima ya muziki Tanzania. Kila siku alikuwa mtu wa kwenda nyumbani kwa The King bila kufanikiwa kitu chochote kile.
Simuni hakuwa akipatikana kwa wakati huo jambo ambalo lilikuwa likimtia sana wasiwasi Yusufu kiasi ambacho akaonekana kukata tamaa ya kufanya nae kazi. Hapo ndipo Yusufu alipoona kwamba alitakiwa kufanya kitu kingine zaidi, kumuita msanii mwingine na kufanya nae kazi kama kawaida.
“Gorila vipi?” Kelvin alimuuliza Yusufu.
“Anafaa. Kama vipi tutafute namba yake ya simu” Yusufu alimwambia Kelvin.
Hapo ndipo walipoanza harakati za kutafuta namba ya simu ya Gorila, msanii ambaye kwa kipindi hicho alikuwa akisikika sana japokuwa umaarufu wake haukuwa ukilingana na umaarufu wa The King. Kumpata Gorila wala hakukuwa na kazi kubwa, mara baada ya kumpata, wakaanza kufanya mazoezi na kisha kuurekodi wimbo huo ambao aliupa jina la MACHOZI YANGU.
“Unatumia jina gani la kisanii?” Gorila alimuuliza Yusufu.
“Jina langu halisi la Yusufu” Yusufu alijibu.
“Haitakiwi kuwa hivyo, unachotakiwa ni kutafuta jina jingine ambalo litakuwa tofauti zaidi. Jina ambalo litawafanya hata watu kuvutiwa na kutaka kusikiliza nyimbo zako” Gorila alimwambia Yusufu.
“Sawa. Itabidi nianze kutumia jina jingine” Yusufu alimwambia Gorila.
“The Ruler” Gorila alimwambia Yusufu.
“Ndiye nani huyo?”
“Hilo ndilo jina jipya ambalo unatakiwa kulitumia kwa sasa” Gorila alimwambia Yusufu.
“Maana yake nini sasa. Si unajua sisi wengine kingereza kimetupiga chenga”
“Maana yake ni Mtawala” Gorila alimwambia Yusufu.
“Sasa hilo si litafanana na The king”
“Hapana. Yeye atakuwa ni mfalme tu, ila wewe utakuwa ni mtawala. Au unaliogopa jina hilo?” Gorila alimwambia Yusufu.
“Jina hilo haliwezi kuleta bifu kati yangu na The King?” Yusufu aliuliza huku akionekana kuwa na wasiwasi.
“Litaleta bifu. Ila bifu si ndio zuri?”
“Bifu ndio zuri? Uzuri wake nini hapo?”
“Litakufanya kujulikana, litawafanya watu kutaka kufahamu huyu The Ruler ni nani hasa na anaimba nyimbo gani. Watakapoanza kukutafuta kwa lengo la kukufahamu, utakuwa umekwishakuwa maarufu” Gorila alimwambia Yusufu ambaye kwa kiasi fulani maneno yale yakaonekana kumuingia.
“Nimekubaliana nalo. Unalionaje jina hilo Kelvin?” Yusufu alimuuliza Kelvin.
“Limetulia. Limetulia sana” Kelvin alijibu.

Je nini kitaendelea?
Yusufu ameingizwa kwenye bifu na mwanamuziki mkongwe, The King.
Je bifu hilo litakuwaje?
Je Yusufu atafanikiwa kama alivyohisi?
Je bifu litaishia wapi?
Itaendelea kesho saa nane.
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 3.


Kuanzia siku hiyo jina la kisanii la Yusufu likawa The Ruler. Maswali mfululizo yalikuwa yakimiminika kichwani mwa wafuatiliaji wengi wa muziki ambao walikuwa wakilisikia jina hilo. Tayari matatizo na ugomvi ukaonekana kuanza kunukia kati ya msanii nguri wa muziki wa kizazi kipya, The King pamoja na msanii ambaye alikuwa akichipukia, Yusufu au The Ruler kama alivyoanza kujulikana.
Jina lile na ugomvi ambao ulikuwa ukianza kufurukuta chini kwa chini ndio ambao uliwafanya watu wengi kuvutiwa kutaka kumsikiliza msanii The Ruler kwa kutaka kuona kwamba alikuwa na kitu gani kipya na kama alikuwa na uwezo wa kumfunika The King ambaye alikuwa amekaa katika fani ya muziki kwa muda mrefu sana.
Kadri ambavyo watu walivyozidi kumsikiliza The Ruler na ndivyo ambavyo akaanza kujulikana miongoni mwa watu wengi mpaka kufikia hatua ambayo alizidi kuitwa katika matamasha mbalimbali kwa ajili ya kupiga shoo ambazo zilikuwa zikimuingizia kiasi kikubwa cha fedha ambacho alikuwa akikitumia pamoja Kelvin ambaye kwake tayari alikuwa meneja wake.
“Huu ugomvi hautokwisha, huu ugomvi tutapigana sehemu yoyote ile, kuanzia mitaani mpaka stejini” Yalikuwa maneno ambayo alikuwa akiyaongea The King kila alipokuwa akikaa na watu wake.
Tayari ugomvi wa chini kwa chini ukaonekana kuwa mkubwa sana kiasi ambacho kiliwafanya waandishi wa habari kufanya jitihada nyingi za kuwaita pamoja na kuwapatanisha lakini hakukuwa na mapatano yoyote ambayo yaliafikiwa. Kila siku magazeti mbalimbali yalikuwa yakitangaza juu ya ugomvi huo ambao ulikuwa ukizidi kushika kasi kadri siku zilivyozidi kwenda mbele.
“Dogo haniwezi. Yaani haniwezi hata chembe japokuwa ameliiba jina langu” The King aliwaambia waandishi wa habari.
Ugomvi huo ukahama kabisa. Haukuwa ugomvi wa kutafutana na mapanga mitaani, sasa ukaingia ugomvi mpya ambao ukaonekana kuwavutia wapenzi mbalimbali wa muziki nchini Tanzania. Waandaaji wa matamasha mbalimbali wakafanya ugomvi huo kuwa sehemu ya kuingizia fedha, mara kwa mara walikuwa wakiandaa matamasha huku majina ya wasanii hao yakionekana kuwa kivutio zaidi.
Wapenzi wa muziki walikuwa wakiingia kwa wingi kwenye matamasha kwa sababu tu walikuwa wakitaka kuwaona wawili hao juu ya steji moja wakiimba huku wakijitahidi kufunikana. Kwa uwezo, The Ruler alionekana kuwa mdogo sana mbele ya The King kiasi ambacho wakati mwingine mashabiki walikuwa wakimzomea kila alipokuwa akipanda jukwaani kutumbuiza.
Hali ile ilionekana kumuumiza sana Yusufu kupita kawaida, hakuamini kama mwisho wa kulichagua jina lile lingekuwa namna ile. Japokuwa alikuwa akijulikana kama alivyokuwa akitaka lakini mvuto wote ukaonekana kupotea kabisa jambo ambalo likamfanya kutamani kutoka katika anga ya muziki wa kizazi kipya.
“Lakini fedha si tunapata kama tulivyokusudia!” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Tunapata lakini unafikiri kila siku kuzomewa najisikia furaha! Natamani kila nitakapokuwa jukwaani watu wawe wanashangilia kwa furaha na si kunizomea” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Kwa hiyo unaona kipi kifanyike?” Yusufu aliuliza.
“Nibadili jina” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Hapana. Hilo ni jambo lisilowezekana kabisa. Usibadili jina, acha liwe hili hili” Kelvin alimwambia Yusufu,
Kazi ya muziki bado ilikuwa ikiendelea kama kawaida, Yusufu hakutakiwa kukata tamaa au kurudisha nyuma matumaini yake, alitakiwa kuendelea kupigana mpaka pale ambapo kila kitu kingeeleweka. Bado alikuwa akizidi kuzomewa jukwaani lakini wala hakukata tamaa, bado alikuwa akiendelea kuingiza fedha kama kawaida.
Kamwe hakuwasahau wazazi wake, mara kwa mara alikuwa akiwatumia fedha nyingi ambazo zilikuwa zikibadilisha maisha yao kila siku. Jina la The Ruler likaonekana kuwagawa mashabiki, kuna wengine ambao walikuwa wakimuona The King kuwa mkali zaidi yake lakini kuna wengine walikuwa wakimuona The Ruler kujitahidi kutafuta ugomvi na The King kama namna moja wapo ya kujitangaza.
“Kwa hiyo kipi kifanyike? Ninatamani kuwa juu zaidi ya The King, watu wanipende kila ninapopanda jukwaani. Ikiwezekana niwachukue hata mashabiki wake na umaarufu wangu uwe mkubwa” Yusufu alimuuliza Kelvin.
“Hapa ni kuongeza juhudi tu. Kama ukiongeza juhudi, kila kitu kitakuwa safi” Kelvin alimwambia Yusufu.
Yusufu hakutaka kupuuzia ushauri ule, alichokifanya kwa wakati huo ni kutuliza zaidi kichwa chake na kutunga nyimbo ambazo aliziamini kuwa kali sana zaidi ya nyimbo alizokuwa akiimba The King. Kila alipokuwa akizirekodi nyimbo zile, bado alikuwa pale pale alipokuwa hali ambayo kwa kiasi kikubwa ikamkatisha sana tamaa.
Baada ya siku kadhaa mambo yakaonekana kuwa mabaya kwa Yusufu, kitu cha redio cha Peackok Fm ambacho kilikuwa kinapiga sana miziki ya wasanii wengi na kuwatangaza kikatangaza hadharani kwamba kisingeweza kupiga tena nyimbo za The Ruler ambaye alikuwa kwenye ugomvi mkali na msanii nguri, The King.
Hilo lilionekana kuwa kama pigo kwa Yusufu, hakujua angeendelea vipi katika anga ya muziki kama kituo hicho kilikuwa kimekataa kupiga nyimbo zake. Tayari akajihesabia kushindwa, ndoto za kuwa msanii mkubwa hapo baadae zikaanza kufutika kichwani mwake.
Watanzania wengi walikuwa wakikipenda kituo hicho cha redio cha Peackok Fm kwa sababu kilikuwa kikiwatangaza sana wasanii wa Tanzania kitaifa na Kimataifa. Uamuzi huo ambao ulikuwa umechukuliwa na kituo hicho cha redio kilimaanisha kwamba ule umaarufu mchache ambao alikuwa nao Yusufu ungepungua zaidi na kupotea kabisa. Hiyo ilimaanisha kwamba asingekuwa akialikwa kwenye matamasha mengine mfululizo kama ambavyo ilikuwa hapo kabla.
Hilo lilikuwa pigo kubwa kwa Yusufu, hakuamini kama ugomvi wake na The King ungeweza kufikia hatua mbaya kama ile. Moyoni alitamani sana amtafute The King na kisha kumuomba msamaha ili mladi tu nyimbo zake ziweze kupigwa tena katika kituo hicho cha redio.
“Kwa hiyo tufanye nini sasa ili niwe juu?” Yusufu alimuuliza Kelvin.
“Au tutafute mfadhili”
“Tutampatia wapi na wakati watu fedha zao wanazichungulia?”
“Usihofu. Najua kuna wengi ambao wanatamani sana kukufadhili. Cha msingi twende tukamuone Papaa Pipo” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Itawezekana kweli kunifadhili?”
“Ondoa hofu, itawezekana tu” Kelvin alimwambia Yusufu.
Hakukuwa na cha kusubiri, kwa hatua ambayo walikuwa wameifikia waliona kwamba bila kupata mfadhili basi kumfanya Yusufu kuwa juu lingekuwa jambo gumu sana. Mtu ambaye walimfikiria kwa wakati huo alikuwa Papaa Pipo tu ambaye alikuwa akitisha kwa utajiri mkubwa ambao alikuwa nao.
Papaa Pipo ndiye ambaye alikuwa akimiliki kumbi kubwa za starehe ambazo ziliitwa Veteran Club ambazo zilikuwa Dar es Salaam, Arusha na Mwanza. Papaa Pipo ndiye ambaye alikuwa akiwadhamini wasanii wengi sana akiwepo The King ambaye alikuwa akinunuliwa magari ya kifahari na kutanuliwa nayo mitaani.
Kitu ambacho alikuwa akikihitaji Papaa Pipo ni kutajwa tajwa tu katika nyimbo zote za watu ambao alikuwa akiwafadhili. Alichokuwa akikitaka yeye ni umaarufu tu, alijijua kwamba alikuwa na fedha nyingi ambazo zilikuwa zimebadilisha maisha yake lakini alikuwa akihitaji kitu kingine zaidi, umaarufu.
Kutajwa mara kwa mara na wasanii mbalimbali kukamfanya kujulikana na watu mbalimbali kitu ambacho alikuwa akikihitaji sana kukipata katika maisha yake. Ujio wa Yusufu pamoja na Kelvin tayari ukamfanya kuona kwamba kile ambacho alikuwa akikitaka kilikuwa kinakwenda kukamilika, kwani kwa wakati huo alikuwa na uhitaji mkubwa wa kumfadhili Yusufu pamoja na kuongea nae kitu kingine ambacho kilikuwa nje ya muziki.
“Karibuni” Papaa Pipo aliwakaribisha nyumbani kwake.
Kelvin ndiye ambaye alikuwa akiongea huku Yusufu akiwa kimya kusikiliza. Papaa Pipo alikuwa kimya akimsikiliza Kelvin ambaye alizungumzia hatua nyingi walizozipitia mpaka Yusufu au The Ruler kufikia hatua hiyo.
“Mmejitahidi sana” Pipo aliwaambia huku akipiga makofi ya chini.
“Asante sana” Wote walijibu kwa pamoja.
“Kwa hiyo unataka kuwa maarufu zaidi ya hapo?” Pipo alimuuliza Yusufu huku akimwangalia usoni.
“Ndio bosi”
“Na unataka kuwa tajiri mkubwa kupitia muziki?” Papaa Pipo alimuuliza.
“Ndio bosi”
“Hakuna shida. Nakuahidi utakuwa na umaarufu mkubwa sana hapa Tanzania, au labda tuseme Afrika nzima. Kila mtu atakutambua wewe ni nani, muziki wako utapendwa na kila mtu. Utapata mashabiki wengi na hata wale wengine ambao haukuwa ukiwatarajia” Papaa Pipo alimwambia Yusufu maneno ambayo yalionekana kuwafurahisha kupita kawaida.
“Unasema kweli bosi?” Yusufu aliuliza huku akionekana kutokuamini.
“Niamini. Wewe nitakufadhili zaidi ya ninavyowafadhili wasanii wengine. Umenifurahisha sana kuanzisha uhasama na The King” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Nimekufurahisha! Kivipi tena?”
“Yule mtoto anajidai sana, yaani kupata vijisenti vinamfanya hadi kunisahau kabisa. Anatoa nyimbo nyingine wala jina langu silisikii. Bora umekuja ili tumpindue” Papaa Pipo alimwambia Yusufu ambaye alionekana kufurahia kupita kawaida.
Huo ndio ukawa mwanzo wa urafiki kati ya Yusufu na Papaa Pipo, katika kila wimbo ambao alikuwa akiutoa Yusufu, jina la Papaa Pipo lilikuwa likisikika hali ambayo ilikuwa ikimfurahisha sana bosi huyo. Wala haukupita muda mrefu, Papaa Pipo akamnunulia Yusufu gari aina ya X Trail kwa ajili ya kufanyia mizunguko yake huku akimjazia mafuta kila wiki.
Maisha yakaonekana kubadilika kwa Yusufu, hapo ndipo alipoamua kuhamia Sinza, katika nyumba kubwa na nzuri huku gharama za upangaji wa nyumba ile ukiwa chini ya Papaa Pipo. Jina la Papaa Pipo likazidi kujulikana zaidi na zaidi, Yusufu alijitahidi kwa nguvu zote kulipaisha jina hilo kiasi ambacho hata wale ambao hawakuwa wakimfahamu mtu huyo wakawa na kiu ya kutaka kumfahamu.
“Hivi ndivyo ninavyotaka iwe. Hapo ndipo tunakwenda sawa” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
Siku zikaendelea kwenda mbele zaidi, jina la The King bado lilikuwa likiendelea kuwa juu zaidi ya Yusufu ambaye alikuwa akitumia jina la kisanii la The Ruler. Mashabiki wengi walikuwa wakitamani sana kumsikiliza The King zaidi ya The Ruler ambaye kwao alionekana kuwa kama mtu ambaye alikuwa akitamani sana sifa za kutaka kujulikana zaidi ya msanii nguri, The King.
Kila siku Papaa Pipo alionekana kuwa na kiu ya kumwambia Yusufu afanye kitu kimoja, kitu ambacho aliamini kwamba kingemfanya kuwa juu zaidi ya pale alipokuwa kwa kipindi kile. Papaa Pipo hakuonekana kuwa muwazi kumwambia Yusufu kitu kile japokuwa moyo wake ulitamani sana kumwambia akifanye kitu kile haraka iwezekanavyo.
“Kuna kitu nitataka uje nyumbani tuongee” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Kitu gani Bosi?” Yusufu aliuliza.
“Wewe njoo tu. Tutaongea kuanzia mwanzo hadi mwisho. Tutakapomaliza, nadhani utakuwa umenielewa zaidi” Papaa Pipo alimwambia Yusufu kwa kutumia njia ya simu.
“Sawa. Nitakuja mchana”
“Hapana. Mchana sitokuwepo nyumbani, njoo usiku kama saa mbili hivi” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Sawa. Nitakuja tu”
“Ok! Ila naomba uje peke yako. Hapa ninamaanisha kwamba hata Kelvin asijue kitu chochote kile” Papaa Pipo alimwambia Yusufu maneno ambayo kwa kiasi fulani yalionekana kumshtua.
“Kwa nini tena nisije nae bosi?”
“Hii ni kwa ajili yako tu. Kama nae angekuwa mwanamuziki ningekwambia uje nae” Papaa Pipo alimwambia Yusufu ambaye alionekana kuelewa.

Je nini kitaendelea?
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 4

Saa 2: 20 usiku gari aina ya X Trail alilokuwa akilimiliki Yusufu lilikuwa likiingia katika jumba la kifahari la Papaa Pipo. Gari liliposimama, Yusufu akateremka na kisha kuufunga mlango wa gari lile. Akaanza kupiga hatua kuelekea ndani ya jumba hilo na kisha kukaribishwa na Papaa Pipo ambaye alikuwa akiishi peke yake bila mtu yeyote zaidi ya mfanyakazi wake wa getini.
Ujio ule ukaonekana kumfurahisha sana Papaa Pipo, muda wa wote walikuwa wakiongea kwa furaha kana kwamba walikuwa wameahidiwa kupewa kitu kimoja kikubwa ambacho kingewafanya kuwa matajiri milele. Muda mwingi Papaa Pipo alikuwa akimsifia Yusufu kwa kile ambacho alikuwa amekifanya cha kuwa na ugomvi na The King ambaye alikuwa akijiona kuwa juu zaidi yake.
Walitumia masaa mawili kula na kunywa na ndipo hapo ambapo Papaa Pipo akamtaka Yusufu kumsindikiza sehemu fulani ambako Yusufu wala hakupafahamu. Usafiri ambao ulikuwa ukitumika lilikuwa ni gari la Papaa Pipo ambaye aliushikiria usukani na kuanza kuelekea huko ambako alitaka waelekee kwa wakati huo.
Safari hiyo ilitumia zaidi ya dakika ishirini, wakawa wamekwishafika katika eneo ambalo Yusufu alikuwa akilifahamu sana, lilikuwa eneo la Msasani. Katika kipindi hicho Yusufu alikuwa akishangaa sana. Kwa nyakati za mchana ambazo alikuwa akipita sana mahali hapo, sehemu ile ambayo ilikuwa na nyumba wala hakukuwa na nyumba yoyote ile, ila kwa wakati ule kulikuwa na jumba kubwa na la kifahari jambo ambalo lilioekana kumtia wasiwasi moyoni.
Baada ya kuliegesha gari wote wakateremka na kuanza kuelekea ndani huku Yusufu akionekana kuwa na wasiwasi mwingi. Kitu ambacho alikuwa akikiona mahali hapo hakuwa akikiamini kabisa. Maswali mfululizo yalikuwa yakimiminika kichwani mwake kwamba ni muda gani ulitumika kuijenga nyumba ile na wakati si muda mrefu sana eneo lile lilikuwa na kiwanja tu
“Mbona una wasiwasi?” Papaa Pipo alimuuliza Yusufu.
“Hili jumba. Linaonekana kuwa la kifahari sana, inaelekea linamilikiwa na mtu mwenye fedha nyingi sana” Yusufu alimwambia Papaa Pipo.
“Yeah! Mmiliki wa jumba hili ana fedha sana hata zaidi yangu” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Hivi amelitengeneza jumba hili kwa siku ngapi?” Yusufu aliendelea kuuliza.
“Kwa nini unauliza hivyo?”
“Wiki iliyopita nilipita hapa wakati naelekea kwenye ukumbi wa Bosnia ila mahali hapa hakukuwa na nyumba zaidi ya kiwanja. Nashangaa leo tunakuja tunakuta nyumba. Ujenzi wake unaonekana kwenda haraka haraka sana” Yusufu alimwambia Papaa Pipo ambaye alikuwa kimya tu.
“Utafahamu kila kitu. Subiri kwanza” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
Mara baada ya kuingia ndani ya jumba lile, wakakaa kwenye makochi ya kifahari. Wala hazikupita dakika nyingi, mwanaume mmoja ambaye alikuwa na ndevu nyingi akatokea mahali hapo. Huku akionekana kuwa na furaha. Papaa Pipo akasimama na kuanza kumsalimia mwanaume yule kwa kutumia salamu ambazo wala hazikuwa zikieleweka kabisa machoni mwa Yusufu.
“Naona umekuja na kijana mtumishi mpya. Hongera sana” Mwanaume yule ambaye alitambulishwa kwa jina la Onyango alimwambia Papaa Pipo.
“Ndio. Nadhani huyu atakuwa mwenzetu bila shaka” Papaa Pipo alimwambia mzee Onyango.
Yusufu alikuwa kimya akiwasikiliza huku muda mwingi akimwangalia mzee Onyango ambaye alikuwa akionekana kuwa na uso uliojaa tabasamu pana. Kwa wakati huo, Yusufu akaanza kujiona kuwa katika hali ya tofauti sana, hamu ya kutaka kupata umaarufu pamoja na utajiri ikaanza kumshika kwa nguvu moyoni mwake. Kiu ya kuvitamani vitu vile ikaanza kumkaba zaidi na zaidi jambo ambalo lilionekana kumshangaza hata yeye mwenyewe.
“Mwambie mzee Onyango vitu unavyovitaka nae atakupa” Papaa Pipo alimwambia Yusufu ambaye alionekana kutokuielewa kauli ile.
“Vitu gani?”
“Wewe uliniambia unataka nini?”
“Sikumbuki”
“Nakumbuka uliniambia unataka kuwa maarufu zaidi” Papaa Pipo alimwambia Yusufu maneno yaliyomfanya Yusufu kukumbuka zaidi.
“Ndio”
“Aya sasa mwambie mzee Onyango kila kitu unachokitaka” Papaa Pipo alimwambia Yusufu ambaye akayapeleka macho yake usoni mwa mzee Onyango.
“Nataka kuwa na mvuto wa kupendwa kwa mashabiki wote wa muziki ambao watazisikiliza nyimbo zangu. Ninataka kuwa na utajiri mkubwa katika maisha yangu. Ninataka niwe na hofu kubwa sana kiasi ambacho kwa mtu yeyote ambaye atataka kunifanyia ubaya wowote basi aniogope” Yusufu alimwambia mzee Onyango.
“Ni hayo tu?” Mzee Onyango aliuliza.
“Ndio” Yusufu alijibu.
“Kuna moja umelisahau Yusufu” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Lipi?”
“Vipi kuhusu mambo yetu yale?”
“Ok! Umenikumbusha. Pia ninataka kupendwa na kila msichana ambaye ananifahamu. Yaani nisipate shida sana kwa msichana yeyote. Niwe na mvuto kwa kila msichana” Yusufu alimwambia mzee Onyango.
“Ni hayo tu?”
“Ndio”
Mzee Onyango akasimama na kisha kuelekea chumbani kwake, aliporudi, alirudi na kioo kikubwa mahali hapo na kisha kukiegemeza ukutani. Akaondoka tena sebuleni hapo na kisha kurudi chumbani tena, aliporudi alirudi na nguo kubwa kama shuka tatu zilizokuwa na rangi nyekundu.
Nguo moja akampatia Yusufu, akaivaa na kisha nguo nyingine kupewa Papaa Pipo ambaye nae akaivaa na nyingine kuivaa yeye mwenyewe. Kitu ambacho kilitakiwa kufanyika mahali hapo kilikuwa ni kimoja tu, kuingia katika kile kioo kikubwa na kutokea katika upande mwingine huku taa zikiwa zimezimwa.
“Itawezekana kweli?” Yusufu alijiuliza moyoni.
Papaa Pipo akaanza kupiga hatua na kukisogelea kioo kile, alipokifikia, akaingia. Mianga kama ya radi ikaanza kumulika katika kioo kile, hofu ikamjaa Yusufu, akaanza kutetemeka kupita kawaida.
Mtu wa pili kuingia ilikuwa zamu yake. Akaanza kupiga hatua kukisogelea kioo kile na kisha kuhisi akivutwa na kuingia ndani ya kioo kile. Upande wa pili ambao alitokea ulikuwa upande mwingine kabisa ambao ulionekana kuwa tofauti na ulimwengu wa kawaida. Macho yake yakatua kwa watu wengi na wa aina mbalimbali ambao walikuwa wakionekana kuwa katika maumbo mengi ya ajabu ajabu.
Yusufu alionekana kuhofia, mwili ulikuwa ukimtetemeka kupita kawaida. Mzee Onyango akatokea mahali hapo na kisha wote watatu kuanza kuelekea sehemu fulani ambayo ilikuwa na giza nene na kisha kuingia ndani ya lile giza.
Kitu cha ajabu ambacho kilionekana kumshangaza Yusufu mara baada ya kuingia ndani ya giza lile ni uwepo wa mwanga mkali ambao wala hakuuelewa ulitoka wapi. Mbele yao kulionekana kuwa na nyumba ambayo wakaanza kuisogelea na kisha kuingia. Kama zilivyokuwa nyumba nyingine nyingi ndivyo ilivyokuwa nyumba ile. Kulikuwa na makochi, televisheni pamoja na meza moja kubwa ambayo ilikuwa imezungukwa na viti vingi.
Mzee Onyango na Papaa Pipo wakaanza kuisogelea meza ile, walipoifikia, wakakaa katika viti vile. Wala hazikupita sekunde nyingi mzee mmoja ambaye alikuwa na kwato za ng’ombe pamoja na mapembe akatokea mahali hapo. Yusufu alikuwa akitetemeka kwa hofu, hapo hapo akatakiwa kusogea katika meza ile na kukaa.
Mzee yule ambaye alikuwa na umbo la kutisha akaondoka mahali hapo na kuelekea ndani, aliporudi, alikuwa na karatasi nyeupe mkononi mwake pamoja na kalamu ambayo ilikuwa na mrija ambao wala haukuwa na wino na kisha kuviweka mezani pale. Kila kitu ambacho kilikuwa kiiendelea mahali pale kilikuwa kikimtisha Yusufu kiasi ambacho wakati mwingine alifikiri kwamba alikuwa katika ndoto moja ya mbaya na ya kutisha sana.
Alichokifanya yule mzee wa kutisha ni kutoa sindano na kisha kumtaka Yusufu kuuweka mkono wake juu ya meza na kisha yule mzee kumchoma mkononi kwenye moja ya mshipa wa damu na kisha kutoa damu ambayo akaiweka katika mrija ule wa kalamu ambayo alikuwa ameishika na kisha kumgawia Yusufu.
“Kila ulichoomba utakipata tu endapo utaandika maagano yetu pamoja nawe katika karatasi hiyo” Mzee Onyango alimwambia Yusufu ambaye alikuwa akitetemeka.
“Andika mahitaji yako huku ukiwa umekubali kuutumikia ulimwengu huu” Mzee Onyango alimwambia Yusufu ambaye bila tatizo lolote akaanza kuandika mahitaji yake kwa kutumia kalamu ile iliyokuwa na wino ambayo ilikuwa ni damu yake. Alipomaliza, akamgawia karatasi ile mzee yule wa kutisha.
“Umeiuza nafsi yako katika ulimwengu huu. Na kama umeiuza, kamwe hautoweza kuipata mpaka pale utakapokufa. Sisi tutakuwa pamoja nawe, tutakulinda kila uendapo, ulinzi wetu utakuwa pamoja nawe. Afya ya mwili wako itakuwa bora, hakutokuwa na ugonjwa wowote ambao utakuwa ukikusumbua katika maisha yako yote. Sadaka ya kafara itakapotakiwa, utatakiwa kuitoa muda muafaka, kamwe hakutokuwa na mtu yeyote ambaye atakuyumbisha, utakuwa imara kadri siku zitakavyokuwa zinakwenda mbele na ndivyo ambavyo umaarufu wako utazidi kuongezeka zaidi na zaidi, utakuwa na fedha nyingi katika maisha yako kuliko msanii yeyote yule hapa Afrika” Mzee yule wa kutisha alimwambia Yusufu na kuendelea.
“Kwa sasa tutakupa masharti mawili tu. Utatakiwa kuoa muda wowote ule upendao ila kamwe hautotakiwa kuwa na mtoto. Siku yoyote ambayo msichana wako au mke wako atakuwa katika siku za kupata mtoto, hautotakiwa kufanya nae mapenzi. Sharti la pili, hautakiwi kufanya mapenzi katika siku ya Jumapili na Jumatano. Kama kufanya mapenzi basi utatakiwa kufanya mapenzi katika siku nyingine lakini si ndani ya siku hizo mbili ambazo tumezitenga. Kama itatokea siku kuvunja masharti yetu, tutakuadhibu ila kama hautoikubali adhabu yetu, basi hatutokuwa na kizuizi cha kukuua” Mzee yule alimwambia Yusufu.
“Nimekubaliana nawe” Yusufu alimwambia mzee yule huku ile hofu ambayo alikuwa nayo katika kipindi cha nyuma ikionekana kuanza kupotea.
“Mnaweza kwenda. Siku za ibada zitakapofika, mnatakiwa kuja nae katika nyumba ya ibada mpaka pale atakapozoea” Mzee yule aliwaambia mzee Onyango na Papaa Pipo.
“Sawa” Wote waliitikia na kisha kuondoka mahali hapo huku Yusufu akiwa amejiunga na kundi hilo ambalo lilionekana kuwa na nguvu za kumpatia utajiri pamoja na umaarufu mkubwa ambao alikuwa akiutaka.
****
Usiku ulionekana kuwa mrefu kwa Kelvin, muda wote alikuwa akimsubiria Yusufu lakini hakuweza kurudi nyumbani. Dakika ziliendelea kusogea huku masaa yakizidi kukatika zaidi na zaidi lakini hali bado ilikuwa ile ile, Yusufu hakurudi nyumbani. Kelvin akashindwa kuvumilia, mara kwa mara alikuwa akimpigia simu lakini simu haikuwa ikipokelewa, ilikuwa ikiita mpaka kukata.
Hali ile ilionekana kumshangaza Kelvin, tayari wasiwasi ukaanza kumuingia kwa kuona labda Yusufu alikuwa amepata tatizo huko alipokuwa. Alichokifanya ni kuanza kuwapigia simu marafiki zao wa karibu lakini napo huko Yusufu hakuonekana. Alichokifanya Kelvin baada ya kuona sehemu zote muhimu alikuwa amemkosa Yusufu, hapo ndipo akaamua kumpigia simu Papaa Pipo.
Hakukuwa na utofauti na simu ya Yusufu, simu ya Papaa Pipo ilikuwa ikiita bila kupokelewa. Kelvin hakutaka kujiuliza zaidi, tayari akahisi kwamba Yusufu alikuwa pamoja na Papaa Pipo ambaye alikuwa mfadhili wake. Alichokifanya Kelvin ni kutoka nje na kisha kuelekea barabarani ambako akakodisha bajaji na kuelekea nyumbani kwa Papaa Pipo.
“Unataka nikupeleke wapi?” Dereva wa bajaji alimuuliza Kelvin huku tayari imekwishatimia saa nne usiku.
“Unasemaje?” Kelvin alimuuliza kana kwamba hakusikia swali lile aliloulizwa.
“Unataka nikupeleke wapi bosi wangu?” Dereva yule alimuuliza kwa mara ya pili.
“Naomba unipeleke Kijitonyama” Kelvin alimwambia dereva wa bajaji ambaye akawasha gari na kuanza kuelekea Kijitonyama alipokuwa akiishi Papaa Pipo.
Ndani ya gari, Kelvin hakutaka kukata tamaa, bado alikuwa akiendelea kumtafuta Yusufu simuni lakini bado majibu yalikuwa yale yale. Wasiwasi haukupungua kwa Kelvin, muda wote alikuwa akionekana kuwa na mashaka. Hakujua ni kwa sababu gani Yusufu alikuwa ameondoka nyumbani bila kumtaarifu ni sehemu gani alipokuwa amekwenda.
Hiyo ilikuwa imetokea kwa mara ya kwanza tangu walipoanza kuwa marafiki. Ukaribu wao ulikuwa mkubwa sana na ndio maana mpaka katika kipindi hicho Kelvin alikuwa akiendelea kushangaa. Huku akiwa kwenye lindi la mawazo kwa muda mrefu, dereva wa bajaji akamshtua.
“Tumefika Sayansi broo. Tuelekee wapi hapa?” Dereva wa bajaji alimuuliza.
“Twende kule kulipokuwa mtaa wa Hollwoody” Kelvin alimwambia dereva bajaji.
“Upo wapi huo mtaa?”
“Twende na barabara ile ya kwenda Tandale kwa Mtogole. Ukifika kule kulipokuwa na kanisa la Kilokole, kata kona kulia. Nyumba ya pili upande wa kulia” Kelvin alitoa maelekezo na dereva waa bajaji kufuata.
Kutoka Sayansi hadi katika mtaa wa Hollwoody wala hakukuwa mbali sana, ni ndani ya dakika moja wakawa wamekwishafika katika nyumba ya Papaa Pipo na kisha Kelvin kuteremkana kuanza kugonga geti. Mara baada ya kujitambulisha kwa mlinzi, geti likafunguliwa na Kelvin kuingia ndani huku dereva wa bajaji akiwa nje akimsubiria.
“Nimejua tu kama atakuwa hapa” Kelvin alijisemea mara baada ya kuliona gari la Kelvin sehemu ya maegesho.
“Karibu Kelvin” Mlinzi alimkaribisha.
“Asante sana. Wapo ndani?” Kelvin aliuliza.
“Wametoka”
“Wametoka? Mbona ameacha gari lake hapa?”
“Bado sijajua. Ila wametumia gari ya bosi mwenyewe” Mlinzi alimwambia Kelvin.
“Ameondoka na Papaa mwenyewe au?”
“Ndio. Ila wamesema hawatokawia kurudi. Ingia ndani uwasubirie” Mlinzi alimwambia Kelvin ambaye kabla ya kuingia ndani, akamtoka nje ya eneo la nyumba ile na kisha kumlipa dereva wa bajaji kiasi cha fedha ambacho alikuwa akikihitaji.
Kelvin akaelekea ndani na kutulia sebuleni huku akiangalia televisheni. Muda ulikuwa ukizidi kwenda zaidi na zaidi lakini si Yusufu wala Papaa Pipo ambaye alitokea mahali hapo. Ilipoingia saa sita usiku, mlio wa gari ukasikika nje na honi kupigwa. Kelevin akainuka na kuelekea dirishani na kisha kuchungulia, gari la Papaa Pipo aina ya Prado lilikuwa likiingia ndani ya geti lile na Kelvin kurudi kitini na kutulia.
Haikuchukua muda mrefu, Papaa Pipo na Yusufu wakaingia ndani, macho yao yakagongana na macho ya Kelvin ambaye alikuwa sebuleni pale. Kila mmoja alionekana kushangaa lakini hawakutaka kuonyesha waziwazi mishangao yao, walichokifanya wakaanza kusalimiana na Kelvin. Hawakutaka kukaa sana, kilichofuata ni kuaga na kuondoka huku Yusufu akionekana kuwa mwenye furaha tele.
“Vipi tena Yusufu? Mlikuwa wapi?” Kelvin alimuuliza katika kipindi ambacho walikuwa garini wakirudi nyumbani.
“Si unajua Papaa alivyokuwa mtu wa wanawake. Alinipeleka kwa mademu zake kupata nao kinywaji na kunitambulisha kwa watu wake” Yusufu alimdanganya Kelvin.
“Sasa mbona uliniacha? Au haukutaka nami niende kuwaona hao mademu?” Kelvin aliuliza.
“Aliniambia niende mimi tu na ndio maana alitaka hata gari langu niliache kwake” Yusufu alidanganya.
Hawakutumia muda mrefu wakawa wamekwishafika nyumbani huku ikiwa ni saa saba na na robo usiku. Hawakuwa na kitu kingine zaidi ya kujitupa kitandani tayari kwa kulala. Usiku huo ulionekana kuwa mrefu kwa Yusufu, kichwa kwa wakati huo alikuwa akifikiria fedha tu. Tayari alikuwa na uhakika kwamba hata umaarufu mkubwa ambao alikuwa akiutamani sana ungeweza kuwa kwake.
Akajaribu kuvuta picha kama tu angefanikiwa kuwa kama vile alivyoandika katika karatasi ya mkataba wa damu. Akashindwa kuelewa angepata umaarufu na mvuto wa aina gani. Kiasi fulani alitamani kumwambia Kelvin lakini akaamua kunyamaza kwani aliona kama angemwambia basi lingeweza kuwa kosa kubwa ambalo angeweza kulijutia hata baadae.
Ingawa katika kipindi hicho alikuwa ametumia kiasi kikubwa kupanga nyumba nzima ambayo ilikuwa hapo Sinza ndani ya jiji la Dar es Salaam lakini kwa wakati huo tayari alikuwa amekwishaona kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa wa kununua nyumba tena katika maeneo mazuri ambayo yangemfanya kutuliza akili yake kutokana na maisha ya dhiki ambayo alikuwa amekulia.
Mpaka muda huo tayari alikuwa akijiona kuwa tajiri japokuwa hakukuwa na dalili zozote ambazo zilikuwa zimekwishajionyesha katika maisha yake. Alikuwa akijiona kwamba tayari amekwishakuwa na umaarufu mkubwa ambao ulimfanya kumuingizia fedha nyingi na kupiga shoo kwa kiasi kikubwa cha fedha.
Kwa wakati huo hakuacha kumfikiria The King ambaye alionekana kuwa adui yake namba moja duniani. Alijua fika kwamba katika kipindi hicho msanii huyo ndiye ambaye alikuwa akivuma sana Tanzania na ndiye ambaye alikuwa na mashabiki wengi sana. Kwa wakati huo, tayari Yusufu akajiona kuvaa magwanda kwa ajili ya kuingia vitani kupigana na The King ambaye kila siku alikuwa akitamba kwamba uwezo wake haukuweza kulinganishwa na msanii yeyote Tanzania.
“Ngoja kila kitu kikamilike. Nitahakikisha namuacha mbali kimafanikio” Yusufu aliwaza na muda mfupi baadae akapitiwa na usingizi huku ikiwa imetimia saa tisa usiku.

Je nini kitaendelea?
Je Yusufu atafanikiwa?
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 5

KWA WASOMAJI WAPYA KABISAAAA.

Kijana Yusufu amekulia katika maisha ya kimasikini pamoja na rafiki yake, Kelvin. maisha hayo ndio ambayo yanamfanya Yusufu kujiingiza katika uimbaji wa muziki wa kizazi kipya. Anapewa jina la The Ruler, jina ambalo linafanana na la msanii mkongwe, The King.
Jina hilo linamletea matatizo, watu wanagawanyika, wengine wanampenda lakini wengine wanamchukia. Hiyo ikaonekana haitoshi, kituo cha redio cha Peackock Fm kinamfungia kwa kutokumpigia nyimbo zake redioni katika kituo hicho, Yusufu anaumia sana.
Baada ya kusota sana kwenye muziki, anampata mfadhili, huyu anaitwa Papaa Pipo, mwanaume mwenye fedha nyingi. Papaa Pipo anampeleka kuzimu, huko Yusufu anasaini mkataba wa damu kwa kumtumikia shetani. Anaambiwa kwamba atapata utajiri mkubwa sana, atapata mvuto mwingi sana. Ameahidiwa mengi na kupewa masharti mawili tu. Asifanye mapenzi siku za Jumapili na Jumatano na hata asipate mtoto. kama akitaka kuoa, aoe tu, ila mtoto hatakiwi kumpata. Yusufu anachukulia kila kitu rahisi.

Je nini kitatokea?
Je Yusufu ataweza kupata kila alichoambiwa kuzimu?
TWENDE PAMOJA SASA.

Simu ilikuwa ikipiga kelele kuashiria kwamba kuna mtu ambaye alikuwa akimpigia kwa wakati huo. Simu ile ilikuwa ikiendelea kuita zaidi na zaidi hali ambayo ilimshtua Yusufu kutoka usingizini na kisha kuupeleka mkono wake pembeni mwa kitanda na kisha kuichukua simu ile. Huku macho yake yakiwa mazito na huku akiwa amefumbua jicho moja, akaanza kuangalia namba ya mpigaji ambaye alikuwa amempigia simu asubuhi hiyo ya saa kumi na mbili.
Namba ilikuwa ngeni machoni mwake, kichwa chake kikaanza kujiuliza maswali mengi kuhusiana na namba ile ambayo ilikuwa ikiingia kwa wakati ule kama alikuwa amekwishawahi kuiona sehemu yoyote ile lakini hakuweza kukumbuka kitu chochote kile. Akabonyeza kitufe cha kijani na kisha kuipeleka simu ile sikioni.
“Halllooow” Yusufu aliita kwa sauti nzito iliyojaa uchovu.
“Mambo vipi The Ruler!” Sauti ya upande wa pili ilisikika.
“Poa. Naongea na nani?” Yusufu aliuliza.
“Unaongea na Dj Mimi hapa wa Peackok Fm” Sauti ya upande wa pili ilijibu.
Yusufu akaonekana kushtuka, hakuamini kile ambacho alikuwa amekisikia. Maswali kibao yakaanza kumiminika kichwani mwake, hakutaka kuamini kama kile ambacho kilikuwa kikiendelea kilikuwa uhalisia au ndoto moja ambayo ilikuwa imemjia kwa lengo la kumletea furaha ya muda mchache.
“Wewe nani na kutoka wapi?” Yusufu aliuliza maswali mawili mfululizo huku akionekana kutokuamini masikio yake.
“Dj Mimi hapa wa Peackok Fm” Sauti ile ilijibu.
“Nikusaidie nini tena? Mbona asubuhi asubuhi sana?” Yusufu aliuliza huku bado macho yake yakiwa mazito kutokana na usingizi ambao bado alikuwa nao.
“Tunataka uje tufanye interview na wewe leo asubuhi ya saa nne” Sauti ya Dj Mimi ilisikika.
“Nije kufanya interview na wewe. Dj wa Peackok Fm?” Kelvin aliuliza huku akionekana kutokuamini.
“Ndio”
“Hicho ni kitu kisichowezekana” Yusufu alisema na kisha kukata simu na kuizima kabisa.
Yusufu akabaki kimya kwa muda, hakuamini kile ambacho kilikuwa kimetokea, tayari mafanikio yakaanza kuonekana. Mkataba wa damu ambao alikuwa ameuandika kuzimu ukaonekana kuanza kufanya kazi yake. Yusufu akatamani kuruka ruka kwa furaha, tayari mafanikio makubwa yakaanza kuonekana kwake.
Hakutaka kupoteza muda wake kujiuliza zaidi juu ya nini kilichokuwa kinaendelea, tayari alikwishaona mkataba wa damu tayari ulikuwa umeanza kufanya kazi yake. Alichokifanya ni kulala tu huku kila wakati uso wake ukionekana kuwa na furaha.
Saa tano na nusu asubuhi Yusufu akaamka kutoka usingizini. Kitu cha kwanza alichokifanya ni kuwasha simu yake. Meseji zaidi ya nane zilikuwa zimetumwa kutoka kwa madj tofauti tofauti wa redio ya Peackok Fmambao walikuwa wakimtaka awasamehe, wakae mezani na kisha kuelewana. Yusufu alibaki akiziangalia meseji zile, akaanza kucheka kwa sauti kitu ambacho kilimfanya Kelvin aliyekuwa sebuleni kumfuata chumbani.
“Kuna nini tena?” Kelvin aliuliza huku akimwangalia Yusufu.
“Hebu soma meseji za hawa wapumbavu” Yusufu alimwambia Kelvin huku akimpa simu.
“Wapumbavu gani?”
“Peackok Fm”
Kelvin akaichukua simu ile na kisha kuanza kuzisoma meseji zile. Kelvin akabaki akishangaa, hakuamini kile ambacho alikuwa anakiona kwa wakati ule. Kituo cha redio kile kile ambacho kilikuwa kimetangaza kutokupiga nyimbo za Yusufu au The Ruler ndicho ambacho leo hii walikuwa wametuma meseji mbalimbali za kumuomba Yusufu msamaha. Kelvin akashindwa kusimama, akaamua kukaa kitandani.
“Hili shavu Yusufu. Kubali yaishe” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Si kirahisi kama unavyolichukulia jambo hili. Kama walitangaza kwamba hawatopiga wimbo wangu wowote basi watangaze wao wenyewe kwamba walinikosea” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Hii ndio nafasi Yusufu. Usiidharau. Hapa ndipo pa kujitangaza” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Usitake nionyeshe udhaifu. Unajua mimi ni msanii mkubwa sana ambaye siwezi kubabaishwa na wao hata mara moja” Yusufu alimwambia Kelvin ambaye alibaki akimshangaa tu.
“Huo usanii ukubwa bado haujafika Yusufu. Nenda kawasikilize bwana”
“Hapana siendi mpaka watangaze kwamba walinikosea”
“Unafikiri wataweza kufanya hivyo?”
“Kwa nini wasiweze? Kama wameweza kuniomba msamaha unafikiri watashindwa kufanya hivyo? Lazima wafanye. Jina langu linakwenda kuwa kubwa sana” Yusufu alimwambia Kelvin.
Yusufu hakutaka kuonyesha udhaifu, tayari alikwishajua kwamba kila kitu kilikuwa kimeanza kukaa sawa. Tayari alikwishaanza kuyaona mambo yake yakianza kukaa sawa. Hapo aliposimamia ndipo alipotaka kusimamia zaidi, asingeweza kufanya kitu chochote mpaka pale kituo kile cha redio cha Peackok kimuombe msamaha kwa kile walichokifanya.
Yusufu hakutaka kukaa kimya, alichokifanya ni kumpigia simu Papaa Pipo na kuanza kumuelezea kile ambacho kilikuwa kimetokea. Papaa Pipo hakuonekana kushangaa kwani tayari alikuwa amekwishaona kwamba kitu kama kile ni lazima kitatokea tu kutokana na ule mkataba ambao alikuwa ameuandika kuzimu.
“Mbona kuna wengi watakuja tu. Huo ni mwanzo tu. Karibu katika ulimwengu huu mpya. Ulimwengu wa umaarufu uliojaa mvuto na utajiri” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Nimekwishakaribia” Yusufu aliitikia huku akionekana kuwa na furaha.
Saa sita na nusu mchana simu yake ilikuwa ikiita. Akaichukua kutoka mfukoni na kisha kuanza kuangalia namba ya mpigaji, namba ilikuwa ngeni. Tayari alikuwa na uhakika kwamba mpigaji wa simu ile alikuwa mmoja wa madj waliokuwa wakifanya kazi katika kituo cha redio cha Peackok Fm. Bila kuchelewa, Yusufu akabonyeza kitufe cha kijani na kisha kuipeleka simu sikioni.
“Mambo vipi Yusufu!” Sauti ya upande wa pili ilimsalimia.
“Poa. Naongea na nani?” Yusufu aliuliza.
“Mkurugenzi wa Peackok Fm hapa, Bwana Stambuli” Sauti ya upande wa pili iliskika.
“Nikusaidie nini?” Yusufu aliuliza.
“Unaweza kuja ofisini mara moja?”
“Hapana. Siwezi. Niko bize sana” Yusufu alimwambia.
“Muda gani ubize wako utakwisha?”
“Labda mwezi ujao” Yusufu alijibu kijeuri.
“Mwezi ujao?”
“Ndio”
“Tunakuomba mara moja. Kuna kitu tunataka tukiweke sawa mara moja” Bwana Stambuli alimwambia Yusufu.
“Kuna fedha nije?” Yusufu aliuliza.
“Kama unahitaji fedha. Tutakupatia. Unahitaji kiasi gani mpaka wewe kufika hapa ofisini?” Bwana Stambuli alimuuliza.
“Milioni moja na nusu”
“Hapana bwana. Ni kiasi kikubwa cha fedha hicho Yusufu”
“Kama hakipo, pangeni foleni. Kuna watu waliotoa fedha zao ambao nahitaji kuonana nao sasa hivi” Yusufu alimwambia Bwana Stambuli huku sauti yake ikisikika kuwa na jeuri.
“Sawa. Tutakulipa, wewe njoo tu” Bwana Stambuli alimwambia Yusufu.
“Sawa. Nitakuja”
“Saa ngapi?”
“Nitakapojisikia” Yusufu alijibu na kukata simu huku akiizima.
****
Mkurugenzi wa Peackok Fm, Bwana Stambuli alionekana kukasirika kupita kawaida kutokana na mambo ambayo yalikuwa yameendelea katika kipindi cha nyuma. Kitendo cha Yusufu au The Ruler kutokupigiwa nyimbo zake katika kituo hicho redio kilionekana kumkasirisha kupita kawaida. Madj walikuwa wakiingia kwa zamu ndani ya ofisi yake na kisha baada ya masaa kadhaa kuhitisha kikao cha dharura cha wafanyakazi wa kituo hicho cha redio.
Bwana Stambuli alionekana kuwa mwenye hasira sana, siku hiyo alionekana kuwa tofauti kabisa na siku nyingine. Alimwangalia kila mtu katika kikao kile, hasira kali ilikuwa imemkaba kooni. Kila mfanyakazi alionekana kutetemeka kwa hofu, haikuwahi kutokea siku ambayo mkurugenzi wao alikuwa na hasira kali kama alivyokuwa siku hiyo.
“Kuna watu nawafukuza kazi leo” Bwana Stambuli aliwaambia na kisha kuinuka kitini.
Akaanza kuzunguka zunguka ndani ya chumba kile kidogo cha mkutano. Tayari alionekana kuwa kama mtu ambaye alikuwa amechanganyikiwa. Kila alipokuwa akiwaangalia wafanyakazi wake ndivyo ambavyo hasira yake ilivyozidi kuongezeka zaidi na zaidi. Alipoona kwamba ameridhika kuzungukazunguka ndani ya chumbani kile cha mkutano, akarudi kitini na kuanza kuwaangalia wafanyakazi kwa zamu.
“Ni nani alitangaza kwamba kituo hiki kisingepiga wimbo wowote wa msanii The Ruler?” Hilo lilikuwa swali la kwanza ambalo liliulizwa na Bwana Stambuli huku akionekana kuwa na hasira kali. Hata kabla jibu halijatolewa, wafanyakazi wote wakaanza kuangaliana kwa zamu.
Kila mmoja alionekana kuwa na wasiwasi katika kipindi hicho, uso wa Bwana Stambuli haukuonyesha masihala hata mara moja, alionekana kukasirika sana. Hakukuwa na mtu ambaye alijibu chochote kile, wote walibaki kimya huku wakiangaliana tu. Bwana Stambuli alibaki kimya huku akiwaangalia katika staili ambayo ilimuonyesha kwamba alikuwa akitaka kusikia jibu.
“Kwa hiyo alijikataza yeye mwenyewe kupigiwa nyimbo zake?” Bwana Stambuli aliuliza mara baada ya kuona ukimya ukiwa umetawala.
“Hapana” Michael alijibu.
“Kumbe nani alifanya hivi?”
“Dj Thumb” Michael alijibu hali iliyomfanya Bwana Stambuli kumgeukia Dj Thumb ambaye alionekana kuwa na wasiwasi.
“Kwa nini uliamua kufanya uamuzi huu? Hii ni kwa sababu wewe ni mmiliki wa kituo hiki cha redio au kwa sababu unajiona kuwa na mamlaka zaidi yangu?” Bwana Stambuli alimuuliza Dj Thumb.
“Naomba unisamehe bosi”
“Ishu iliyokuwepo hapa sio kusameheana tena, yaani ninachotaka ni kusikia mengi kutoka kwako. Kipi kilichokufanya kutokutaka kupiga nyimbo za The Ruler? Chuki binafsi au?” Bwana Stambuli alimuuliza Dj Thumb ambaye alibaki kimya.
Siku hiyo haikuonekana kuwa siku ya amani kabisa, watu hawakutulia hata kidogo, hasira za Bwana Stambuli ziliwafanya wafanyakazi wote kuanza kuoneana aibu. Dj Thumb ndiye ambaye kwa wakati huo alitakiwa kumuita Yusufu au The Ruler kwa ajili ya kumuomba msamaha kwa kila kitu ambacho kilikuwa kimetokea.
Kila alipokuwa akipigiwa simu, Yusufu alikuwa akileta mapozi, tayari alijiona kuanza kuwa na jina kubwa nchini Tanzania, kitendo alichokifanya cha kuiuza nafsi yake kuzimu ilionekana kumpa kiburi kupita kawaida.
*****
Yusufu hakutaka kuwa na haraka kwa kila kitu ambacho alitakiwa kukifanya kwa kipindi hicho, siku hiyo alikuwa amekaa chumbani kwake huku akisikiliza redio tu. Nyimbo zake ndizo ambazo zilikuwa zikipigwa mara nyingi kutoka katika redio tofauti tofauti ndani na nje ya jiji la Dar es Salaam.
Muda wote Yusufu alionekana kuwa na furaha, hakutaka kujuta kwa kitendo chake cha kuiuza nafsi yake kuzimu bali kwa wakati huo alionekana kufurahi huku akiona kitendo alichokifanya kuwa sahihi kwa sababu alikuwa akitafuta sana utajiri pamoja na mvuto kwa mashabiki wa muziki wa kizazi kipya.
Kitu ambacho aliamua kukifanya Yusufu kwa wakati huo ni kuanza kutunga wimbo mwingine, wimbo ambao aliamini kwamba ungempa sana umaarufu na fedha za kutosha. Jambo la kutunga wimbo halikuwa jambo dogo kwa upande wake, ilimchukua zaidi ya wiki nzima na ndipo alipokuja kuukamilisha.
Baada ya kumaliza kila kitu, akaanza kuuchukulia mazoezi na kisha kuurekodi rasmi na kuuachia katika vituo vya redio. Hapo ndipo ambapo Yusufu alipokuja kuona kitu ambacho kilionekana kuwa kama muujiza. Wimbo wake ukaonekana kuwa lulu katika masikio ya watu, kila wakati watu mbalimbali walikuwa wakiuimba wimbo ule ambao ulionekana kuwavutia kupita kawaida.
Kila kona jina lake lilikuwa likisikika kitu ambacho kiliwafanya watu kuuchagua kuwa wimbo bora katika kipindi hicho. Yusufu akaanza kuitwa katika matamasha mbalimbali kufanya shoo jambo ambalo lilimfanya kujulikana zaidi na zaidi. Mashabiki wengi wakaonekana kuwa na mvuto kwa Yusufu, kuitwa kwake katika matamasha mbalimbali kukamuongezea umaarufu kupita kawaida.
Hiyo ikaonekana kuwa njia moja ya mafanikio ambayo alikuwa akiyataka. Vyombo vingi vya habari vikaanza kumtangaza jambo ambalo akaanza kuonekana kuwa msanii mkubwa ambaye hakuwahi kutokea nchini Tanzania. Katika kila shoo ambayo alikuwa akiifanya, watu wengi walikuwa wakihudhuria huku wakitaka kumuona msanii huyo ambaye alikuwa amekuja kwa kasi katika anga ya muziki wa kizazi kipya.
Hapo ndipo maisha ya starehe yalipoanza rasmi, kwa sababu jina lake lilikuwa kubwa, wasichana wengi wakatokea kumpenda, mara kwa mara alikuwa akipigiwa simu na wasichana wengi huku wakimtaka kimapenzi lakini Yusufu hakutaka kuwaelewa. Kwa wakati huo, utulivu wake ulikuwa katika muziki, hakutaka kabisa kuyapa mapenzi nafasi maishani mwake.
Ndani ya miezi miwili tu, Yusufu alikuwa akiingiza kiasi kikubwa cha fedha cha zaidi ya milioni kumi kwa kila shoo ambayo alikuwa akiifanya kwenye matamasha mbalimbali. Mafanikio yae yakaonekana kuwa makubwa kwa msanii kama yeye, kitu alichokifanya kwa wakati huo ni kununua gari la kifahari, Range na kisha kuanza kujenga nyumba maeneo ya Mbezi Beach jijini Dar es Salaam.
Makampuni mengi nchini Tanzania yakaanza kufanya kazi pamoja nae kwa malipo makubwa ya fedha, matangazo ya bia, matangazo ya sigara, simu za mkononi pamoja na makampuni mengi yalikuwa yakifanya matangazo mengi ya kibiashara pamoja nae. Sura yake ikaonekana kuwa biashara kubwa, katika kila tangazo ambalo sura yake ilionekana, bidhaa hizo zilikuwa zikinunulika au kutumika sana.
Yusufu akafanikiwa kuliteka soko la muziki Tanzania, akaonekana kuwa mfano wa kuigwa kwa wasanii wengine. Kwa wakati huo Yusufu hakuwa akilala nyumbani kwake, muda mwingi alikuwa akishinda katika matamasha mbalimbali mikoani jambo ambalo lilimfanya kuwa bize kupita kawaida. Katika kila shoo ambayo alikuwa akienda, Kelvin alikuwa pamoja nae huku akisimama kuwa kama meneja wake.
Tayari maisha yao ambayo walikuwa wamepitia yakawa yamebadilika kabisa ndani ya miezi mitatu tu. Yusufu hakutaka kusubiri zaidi, alichokifanya ni kuwanunulia wazazi wake nyumba kubwa na ya kifahari mjini Bagamoyo pamoja na usafiri ambao wangekuwa wanautumia katika kufanya mizunguko yao ya hapa na pale.
Mafanikio yale yalikuwa yamekuja kwa haraka sana katika hali ambayo ilimfanya hata yeye mwenyewe kushangaa kwani haikuwa kawaida sana hata kwa watu wengine ambao walikuwa wameuza nafsi zao kuzimu.
“Mbona mafanikio yamekuja haraka sana?” Yusufu alimuuliza Papaa Pipo simuni.
“Hata mimi mwenyewe nashangaa. Sikutarajia kama yangeanza kuonekana kwa haraka namna hii” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Mmmh! Unajua mpaka nimeshangaa”
“Yeah! Ia ninachohisi ni kwamba wakubwa wanataka uwatangaze. Unajua hapo bado hawajiaanza kufanya kazi pamoja nawe” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Bado hawajaanza kufanya kazi na mimi! Mbona nimeanza kufanikiwa sasa?” Yusufu aliuliza.
“Mafanikio wanakupa. Kitu ambacho utatakiwa kukifanya ni kuanza kuwatangaza kupitia mambo mbalimbali” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Kivipi?”
“Mambo mengi tu. Kwa sababu ushaanza kuhudhuria ibada, utaambiwa mambo mengi ya kufanya” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Sawa. Ngoja niendelee kula maisha”
“Kula kwa raha zako. Ila usivunje masharti. Si unakumbuka hilo?”
“Nakumbuka sana. Si wameniambia nisiwe na mtoto na nisifanye mapenzi katika siku ya Jumapili na Jumatano, nakumbuka sana”
“Kama unakumbuka, vizuri sana” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo jina la Yusufu kama The Ruler ndivyo lilivyozidi kuvuma zaidi na zaidi. Kila siku alikuwa alikuwa akikusanya fedha kupita kawaida, mafanikio makubwa ambayo alikuwa akiyapata katika kipindi hicho yalionekana kumshangaza kupita kawaida. Hakutaka kujiambia kuhusu madhara ambayo angeyapata baadae, kitu ambacho alikuwa akikifikiria kwa wakati huo ni kuendelea kuingiza fedha na kutumia alivyotaka.

Je nini kitaendelea?
Je nini kitaendelea katika maisha ya Yusufu?
Itaendelea.
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 6

KWA WASOMAJI WAPYA KABISAAAA.

Kijana Yusufu amekulia katika maisha ya kimasikini pamoja na rafiki yake, Kelvin. maisha hayo ndio ambayo yanamfanya Yusufu kujiingiza katika uimbaji wa muziki wa kizazi kipya. Anapewa jina la The Ruler, jina ambalo linafanana na la msanii mkongwe, The King.
Baada ya kusota sana kwenye muziki, anampata mfadhili, huyu anaitwa Papaa Pipo, mwanaume mwenye fedha nyingi. Papaa Pipo anampeleka kuzimu, huko Yusufu anasaini mkataba wa damu kwa kumtumikia shetani. Anaambiwa kwamba atapata utajiri mkubwa sana, atapata mvuto mwingi sana. Ameahidiwa mengi na kupewa masharti mawili tu. Asifanye mapenzi siku za Jumapili na Jumatano na hata asipate mtoto. kama akitaka kuoa, aoe tu, ila mtoto hatakiwi kumpata. Yusufu anachukulia kila kitu rahisi.

Je nini kitatokea?
Je Yusufu ataweza kupata kila alichoambiwa kuzimu?
TWENDE PAMOJA SASA.

Jina la mwanamuziki The King likaonekana kuanza kufutika machoni na masikioni mwa watu jambo liliwapelekea wadau wengi wa muziki kuanza kujiuliza juu ya hali hiyo. Nyimbo zake ambazo zilikuwa zikitamba sana, kwa wakati huo wala hazikusikika tena, yaani zilikuwa zimeshushwa chini sana huku nyimbo za The Ruler zikisikika kila kona.
Kwa kipindi kifupi cha miezi mitatu ya Yusufu kuwa juu tayari The King akaonekana kupoteza mvuto kwa wadau wa muziki jambo ambalo lilionekana kumshangaza kupita kawaida. Kitendo cha Yusufu au The Ruler kuwa juu kikaonekana kumpa hasira sana. Hapo ndipo bifu lilipoanza rasmi. Yusufu alikuwa akifanyiwa fujo sana na vijana ambao walikuwa wakijulikana sana kama walikuwa maswahiba wa The King.
Muziki wa kizazi kipya nchini Tanzania ukaonekana kuanza kuingia doa. Kwa upande fulani tayari kukaanza kuonekana kwamba kuna mambo mengi na matukio ya kutisha yangeweza kutokea hapo baadae kama vyombo vya sheria visipoingilia kati. Hapo ndipo ambapo polisi walipoanza kufanya kazi yao, kila mtu ambaye alikuwa akimletea fujo Yusufu jukwaani alikuwa akikamatwa na kuwekwa ndani kwa muda.
Kadri siku zilivyozidi kwenda na mbele na ndivyo ambavyo Yusufu alivyozidi kujulikana zaidi na zaidi mpaka nchi nyingine za Afrika Mashariki. Jina lake lilizidi kukua zaidi na zaidi, alizidi kuitwa sehemu mbalimbali nje ya Tanzania kwa ajili ya kufanya matamasha ambayo yalikuwa yakimuingizia kiasi kikubwa cha fedha.
Yusufu akawa amepata mafanikio makubwa sana tena ndani ya miezi mitatu tu jambo ambalo wala halikuweza kuaminika mioyoni mwa watu wengi ambao walikuwa wakiyafuatilia mafanikio yake. Baada ya kipindi cha mwezi mmoja zaidi na ndipo hapo ambapo maneno ya chini kwa chini yakaanza kusikika kwamba Yusufu alikuwa akijihusisha na dini ambayo ilimkataa Mungu.
Tetesi zile zilianzia chini kabisa lakini mwisho wa siku zikaanza kuvuma hata zaidi ya upepo jambo ambalo likaonekana kuwa si zuri masikioni mwa watu wengi. Mara kwa mara Yusufu alikuwa akiitwa kwa ajili ya mahojiano kuhusiana na tetesi zile ambazo zilikuwa zikisikika sana lakini alikuwa akipinga vikali.
“Hizi ni tetesi ambazo zimesambazwa na watu wasiopenda maendeleo yangu akiwepo The King. Najua wataongea mengi sana kwa sababu jina langu linazidi kupanda juu zaidi na zaidi” Yusufu alimwambia mwandishi wa habari katika mahojiano maalumu.
“Kwa hiyo tetesi hizi hazina ukweli kabisa?”
“Ndio. Huwa mara nyingi ninashinda ndani nikichukua mazoezi sana kwa kuamini kwamba kama unataka ubaki juu zaidi na zaidi basi yakupasa kufanya sana mazoezi ya muziki. Ila pamoja na hayo yote, ninamtegemea Mungu katika kufanya kila kitu katika maisha yangu. Yeye ndiye ananiongoza, yeye ndiye amenifanya kuwepo mahali hapa” Yusufu alimwambia mwandishi wa habari.
Siku hiyo yalikuwa mahojiano maalumu ambayo yalikuwa yakifanyika katika kituo cha televisheni cha PASUA kilichokuwa na makao makuu jijini Dar es Salaam. Kila swali ambalo alikuwa akiulizwa Yusufu alikuwa akijibu kwa ufasaha sana jambo lililowafanya watu wote kuona kwamba yale yaliyokuwa yakisemwa mitaani zilikuwa ni tetesi tu.
“Kwa kumalizia ungependa kuwaambia nini watu wanaeneza tetesi hizi?” Mtangazaji aliuliza.
“Ningependa kuwaambia kwamba Mungu anapoamua kumuinua mtu fulani katika kazi yake tusitake kuongea maneno mengine. Tunachotakiwa ni kumshukuru Mungu kwa kumuinua mtu fulani. Yakupasa kupigana na kujitoa kwa ajili ya kufanikiwa pia” Yusufu alimalizia.
Mahojiano yale ambayo yalifanyika yakaonekana kubadilisha kila kitu kabisa. Tetesi zile ambazo zilikuwa zikisikika zikaonekana kuzimwa kabisa. Mitaani hakukusikika tetesi zile tena, watu walikuwa wakiendelea na kazi zao huku wakimuona Yusufu kuwa mtu mwenye bahati ambaye Mungu alikuwa amempa nafasi ya upendeleo maishani mwake.
****
“Nataka kumuua. Hili bifu nimechoka kuwa nalo, nataka kumuua tu” The King alikuwa akimwambia mtu fulani simuni.
“Lini?” Sauti ya upande wa pili iliuliza.
“Siku yoyote. Ila nataka kumuua” The King alisema.
“Ok! Nimekusikia, subiri nije ili tupange mipango kabambe” Sauti ya upenda wa pili ilisema.
The King alionekana kukasirika kupita kawaida, tayari akaonekana kupoteza umaarufu wake ambao alikuwa nao kabla. Msanii chipukizi ambaye alikwishawahi kumuomba kumshirikisha nyimbo alikuwa juu hata zaidi yake. The King hakuonekana kukubali, tayari alijiona kufanya jambo moja ambalo lingemfanya Yusufu au The Ruler kunyamaza milele, alitaka kumuua tu.
Mipango tayari alikwishaanza kuisuka, alichokifanya kwa wakati huo ni kuwasiliana na watu ambao aliona kwamba wangeweza kumsaidia sana kwa ajili ya kukamilisha mpango wake ambao alikuwa ameupanga kwa wakati huo. Alipomaliza kuongea na simu, akalifuata kochi na kisha kutulia huku uso wake ukionekana kuwa na hasira sana.
Mawazo yake katika kipindi hicho yalikuwa yakimfikiria Yusufu, tayari mtu huyo alikuwa ameanza kukisumbua kichwa chake zaidi na zaidi. The King alijua fika kwamba thamani yake ilikuwa imeshuka kupita kawaida, alijua fika kwamba umaarufu wake ulikuwa umeshushwa kupita kiasi huku Yusufu akichukua nafasi kubwa katika tasnia ya muziki zaidi yake.
The King hakutaka kujiona akishindwa hivi hivi, tayari alijiona kuwa na uhitaji wa kufanya kitu kimoja tu ambacho kama angekikamilisha basi angeweza kurudi juu tena, kumuua Yusufu. Mpango ambao alikuwa akiupanga kichwani mwake ulikuwa mpango kababe ambao aliamini kwa namna moja au nyingine basi ni lazima angekamilisha kile ambacho alikuwa amekipanga.
Baada ya saa moja, mwanaume mmoja akaingia ndani ya nyumba hiyo huku akiwa ameongozana na vijana watatu ambao alikuwa amekuja nao kwa ajili ya kuutekeleza mpango ambao ulitakiwa kufanyika kwa kumuua Yusufu ambaye alionekana kuwa kama kikwazo katika mafanikio yake ya kimuziki nchini Tanzania.
Waliongea mengi huku wakiwa hawajagusia mpango mzima. Walipoona kwamba wamechukua muda mrefu bila kuliongelea suala hilo hapo ndipo walipoanza kuupanga mpango mzima ambao ulitakiwa kufanyika kwa haraka sana hata kabla mambo hayajawa makubwa.
“Ninachotaka auawe tu” The King alisema.
“Wewe unataka afe kifo gani ili ufurahie?” Sudi alimuuliza.
“Chochote tu ili mladi afe”
“Sawa. Tutakachokifanya sisi ni kumchoma moto garini. Unaonaje hapo?”
“Mmmh! Mna hatari nyie. Ila sawa, kifo hicho kizuri sana” The King alisema na vijana wale kuondoka huku wakiwa wameahidi kwamba siku hiyo ndio ingekuwa siku ya kutekeleza kila kitu ambacho kilitakiwa kufanyika.
****
Mipango tayari ilikuwa imekwishapangwa na Sudi ndiye ambaye alikuwa akisimamia mpango huo ambao ulitakiwa kufanyika kwa haraka sana. Kitu cha kwanza ambacho walikifanya ni kununua dumu la lita ishirini la mafuta ya petroli na kisha kulihifadhi ndani huku wakimsubiri Yusufu ambaye alikuwa mikoani akiendelea kufanya shoo mbalimbali.
Walisubiri kwa kipindi cha wiki moja na ndipo Yusufu akarudi jijini Dar es Salaam tena kwa sababu tu alikuwa akihitajika kusaini mkataba na kampuni ya kutengeneza vyandarua ya Netprotector. Yusufu hakutaka kukaa sana ndani ya jiji la Dar es Salaam, alichokuwa akikitaka kwa wakati huo ni kusaini mkataba na kisha kurudi mikoani kuendelea na shoo kabla ya kwenda Kenya na Uganda ambako alikuwa akihitajika sana.
Mara baada ya kuona kila kitu kimeandaliwa vizuri, Sudi akawachukua vijana wenzake wawili na kisha kuanza kuelekea katika majengo ya kampuni ya Netprotector ambako huko kila kitu kingefanyika kwa haraka sana.
Mara baada ya kufika huko, moja kwa moja wakaanza kumsubiria Yusufu kwa nje huku wakiwa katika gari lao. Wala haukupita muda mrefu sana, Yusufu akatoka katika jengo lile huku akiwa pamoja na meneja wa kampuni ile na baadhi ya waandishi wa habari ambao walikuwa kwa lengo la kupiga picha kila kilichoendelea ndani ya jengo lile.
Walipoongea mambo mbalimbali hapo nje, Yusufu pamoja na rafiki yake, Kelvin wakaingia ndani ya gari ao na kisha kuondoka mahali hapo. Kwa wakati huo walikuwa wakielekea Sinza walipokuwa wakiishi. Njia nzima, wote wawili walionekana kuwa na furaha, walikuwa wakiongea mengi kwa wakati huo.
Maisha yao yalikuwa ya juu, shida mbalimbali ambazo walikuwa wamezipitia katika maisha yao ya nyuma kwa wakati huo zikabaki na kuwa historia tu. Vinywaji mbalimbali vilikuwa ndani ya gari lile, walikuwa wakiendelea kunywa huku stori za hapa na pale zikiendelea.
Walipofika Tandale Kwa Tumbo, wakashtukia gari moja likisimama mbele yao jambo ambalo likamfanya Kelvin kufunga breki ya ghafla. Hata kabla hawajafanya kitu chochote kile, vijana wawili wakatoka ndani ya gari lile huku mikononi wakiwa na bunduki na kisha kuanza kuwafuata. Yusufu na Kelvin walikuwa wakitetemeka, hawakujua ni kitu gani ambacho kilikuwa kikiendelea mahali hapo.
Tayari watu walikuwa wamekwishakusanyika kuona ni kitu gani kilichokuwa kinaendelea. Alichokifanya Sudi ni kupiga risasi hewani, watu wote wakaanza kukimbia ovyo mahali hapo. Walipolifikia gari lile, wakaufungua mlango na kumtoa Yusufu pamoja na kuchukua ufunguo wa gari lile na kisha kumpandisha ndani ya gari lao na kuondoka nae huku Kelvin akibaki mahali pale akiwa hajui ni kitu gani alitakiwa kukifanya.
Gari lilikuwa likiendeshwa kwa mwendo wa kasi, tayari muda ulikuwa ni saa kumi na mbili jioni. Gari lilipofika Sinza Kijiweni, likakata upande wa kushoto na kuanza kuelekea Shekilango ambako baada ya kufika huko, wakakata kona kulia na kuchukua barabara ya Morogoro huku wakianza kuelekea kwenye mataa ya Ubungo.
Foleni haikuwa kubwa jambo ambalo likawafanya kutokuchukua muda mrefu mpaka kuvuka mahali pale. Muda wote Yusufu alikuwa akitetemeka kwa hofu, kila alipokuwa akijitahidi kuuliza maswali, alikuwa akipigwa vibao tu na kumfanya kunyamaza.
Kila mtu alikuwa bize kwa wakati huo huku bunduki zao zikiwa mikononi mwao. Walikuwa na uwezo wa kumuua hata kwa risasi lakini aina ya kifo cha kuchomwa moto ndicho kilichoonekana kufaa zaidi kwa wakati huo. Safari iliendelea zaidi na zaidi mpaka kufika Mbezi kwa Yusufu na kuendelea mbele zaidi.
“Twendeni wapi ambapo kunaonekana kufaa zaidi?” Ahmad aliuliza.
“Msitu wa Pande” Sudi alijibu.
Hakukuwa na mtu yeyote ambaye alionekana kupingana nae, msitu ule ulionekana kufaa zaidi kwa kufaya kile ambacho walikuwa wamekikusudia kukifanya kwa wakati huo. Wakazidi kwenda mbele huku mwendo wao ukiwa wa kasi zaidi na zaidi mpaka kufika karibu na Kibamba na kisha kukata kona kushoto na kuingia katika sehemu ambayo wala haikuwa na njia zaidi ya wao kuilazimisha njia kuonekana.
Walikuwa wamekwishaingia porini ambako walikuwa wakiendelea na safari yao zaidi na zaidi. Wakafika katika sehemu ambayo ilikuwa imezungukwa na miti mingi na kisha kulipaki gari lao mahali pale. Sudi na Ahmadi wakateremka na kumuacha Ramadhani na Yusufu garini.
“Tumshushe tumchome moto au tumuache na kumchoma moto humo humo?” Ahmad aliuliza.
“Tumchomeni moto humo humo” Sudi alijibu na kisha kuufungua mlango.
Kitu walichokuwa wakitaka ni kuona kwamba Yusufu alikuwepo au alikuwa amekimbia katika kipindi ambacho walikuwa wametoka nje kuongea. Yusufu alikuwepo ndani ya gari lile lakini katika kipindi hiki alikuwa tofauti sana. Kwanza, hakuwa akionekana kuwa na wasiwasi kama kipindi kilichopita, alionekana kuwa katika hali ya kawaida huku akionekana kufahamu kila kilichokuwa kikienda kutokea mahali hapo.
“Mmmh! Huyu mtu kweli noma. Hata kuogopa haogopi!”Ahmad aliwaambia wenzake huku akimwangalia Yusufu ambaye alikuwa ametulia garini.
Walichokifanya ni kufungua boneti la gari na kisha kutoa dumu la mafuta ya petroli ambalo lilikuwa limejaa mafuta na kisha kuanza kulimwagia gari lile. Yusufu alikuwa kimya garini, hakuongea kitu chochote kile, alikuwa amejiinamia chini tu.
“Hebu mmulikeni tochi usoni. Analia au?” Sudi alisema na Ahmad kummulika Yusufu tochi usoni.
Yusufu alionekana kutokuwa na wasiwasi hata kidogo, hakuwa akilia wala kulalamika hata kidogo. Kitu ambacho kilikuwa kikitaka kutokea kwa wakati huo kilionekana kuwa kama kitu ambacho wala hakikumshtua hata kidogo. Ramadhani bado alikuwa akiendelea kulimwagia petroli gari lile kuanzia nje mpaka ndani na kummwagia Yusufu mafuta yale mwil mzima.
Baada ya kuona kwamba kila kitu kilikuwa kimekamilika, hapo ndipo Sudi alipotoa namba za gari lile na kisha kuliwasha gari kwa kutumia kiberiti ambacho alikuwa nacho mahali hapo. Gari likaanza kuteketea kwa moto. Moto mkubwa ulikuwa ukiendelea kuwaka huku wakiwa wamelizunguka kwa mbali gari lile. Kwa mbali walikuwa wakimuona Yusufu alikuwa akiteketea kwa moto huku akiwa amekaa vile vile kitini huku hata akiwa haangaiki au kupiga kelele zozote zile.
Walichokifanya hasa mara baada ya kuona kwamba Yusufu tayari alikuwa ameteketea kwa moto ni kuanza kuondoka mahali hapo. Wote walikuwa wakipongezana kama kawaida kwa kumaliza kazi ile ambayo wala haikuwa ngumu sana kwa upande wao. Tayari kiasi kikubwa ambacho walikuwa wameahidiwa kilikuwa kimekwishaandaliwa na ilikuwa bado makabidhiano tu.
Walichukua dakika arobaini mpaka kufika barabarani ambapo wakachukua daladala na kisha kuanza kuelekea Mwenge alipokuwa akiishi The King na kisha kumwambia kila kilichokuwa kimeendelea msituni. The King alionekana kutokuamini, kwa furaha aliyokuwa nayo alionekana kuwa kama mtu aliyechanganyikiwa.
“Mungu wangu! Mmefanikiwa bila matatizo yoyote yale?” The King aliuliza huku akionekana kushangaa kwa furaha.
“Kila kitu tayari. Kazi haikuwa kubwa kama tulivyodhani, yaani ilikuwa rahisi kama kumsukuma mlevi mlimani” Sudi alijibu huku akionekana kuwa na uhakika.
Alichokifanya The King kwa wakati huo ni kuandaa bia pamoja na vyakula mbalimbali na kisha kuanza kunywa kama njia mojawapo ya kusherekea. Kila mmoja alionekana kuwa na furaha kwani kifo cha Yusufu kilionekana kuwafurahisha kupita kawaida.
Ilipofika saa mbili usiku, The King akawasha televisheni yake na kuweka kituo cha televisheni cha ITV ambapo hapo akapata uhakika kwamba Yusufu alikuwa ameuawa hasa mara baada ya kutangazwa kwamba alitekwa na watu wasiojulikana ambao walikuwa na bunduki na kisha baada ya saa moja gari hilo ambalo lilikuwa limetumika kwenye utekaji kukutwa limechomwa moto huku garini kukiwa na mwili wa binadamu ambao ulikuwa umeteketezwa vibaya kupita kiasi na ni mifupa tu ndio ambayo ilikuwa ikionekana kwa mbali.
“Mlikumbuka kutoa namba za gari?” The King aliuliza.
“Hatuwezi kusahau hicho. Tulitoa hata kabla hatujalichoma moto. Tena umenikumbusha, ngoja nikupe namba zako” Sudi alisema na kisha kuelekea kule alipouweka mfuko wake na kisha kutoa vibati viwili ambavyo vilikuwa na namba za gari na kisha kumgawia The King ambaye alionekana kuwa na furaha zaidi kwa kuona kwamba kazi kubwa ambayo alikuwa akiitaka kufanyika ilikuwa imekwishafanyika.
“Hakuna kuchelewa. Ngoja niwalipeni haraka sana” The King alisema na kungia ndani, alipotoka, alikuwa na mfuko wa kaki na kisha kumkabidhi Sudi ambaye aliufungua na kuanza kuangalia ndani.
“Kuna milioni kumi kama tulivyokubaliana” The King aliwaambia.
“Poa. Hapa imetulia sasa. Cha msingi jipange kurudi juu tena, mbaya wako kashakufa” Sudi alimwambia The King.
“Hiyo niachieni mimi. Ila kumukeni kwamba kitu hiki kilichotokea itabidi kiwe siri kubwa sana” The King aliwaambia.
“Usijali. Kitaendelea kuwa siri mpaka tutakapokufa” Sudi alimwambia na wote kukubaliana kwamba kila kilichoendelea kilitakiwa kuwa siri.

Je nini kitaendelea?
Je Yusufu amekufa?
Je nini mwisho wa kila kitu?
Itaendelea kesho.
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 7

KWA WASOMAJI WAPYA KABISAAAA.

Kijana Yusufu amekulia katika maisha ya kimasikini pamoja na rafiki yake, Kelvin. maisha hayo ndio ambayo yanamfanya Yusufu kujiingiza katika uimbaji wa muziki wa kizazi kipya. Anapewa jina la The Ruler, jina ambalo linafanana na la msanii mkongwe, The King.
Baada ya kusota sana kwenye muziki, anampata mfadhili, huyu anaitwa Papaa Pipo, mwanaume mwenye fedha nyingi. Papaa Pipo anampeleka kuzimu, huko Yusufu anasaini mkataba wa damu kwa kumtumikia shetani. Anaambiwa kwamba atapata utajiri mkubwa sana, atapata mvuto mwingi sana. Ameahidiwa mengi na kupewa masharti mawili tu. Asifanye mapenzi siku za Jumapili na Jumatano na hata asipate mtoto. kama akitaka kuoa, aoe tu, ila mtoto hatakiwi kumpata. Yusufu anachukulia kila kitu rahisi.
The Ruler hasikiki tena japokuwa yeye ni mkongwe. Jambo hilo linampa hasira, anamchukia Yusufu, anachokiamua ni kumuua tu. Anawatuma vijana wake ambao wanamkamata Yusufu na kisha kumpeleka katika msitu wa Pande na kisha kumchoma moto garini. Yusufu ahangaiki garini, ametulia tuli huku akitekezwa na moto ule.
Je nini kitaendelea?
Je Yusufu amekufa?
TWENDE PAMOJA.


‘THE RULER AUAWA KWA KUCHOMWA MOTO GARINI, THE RULER AUAWA KIFO CHA KINYAMA, NI MAUAJI AMBAYO HAYAJAWAHI KUTOKEA, MOTO WAMPELEKA THE RULER KABURINI’ Hivyo vilikuwa baadhi ya vichwa vya habari ambavyo vilikuwa vimeandikwa katika magazeti mbalimbali jijini Dar es Saaam.
Watu walionekana kushtuka, hawakuamini kile ambacho walikuwa wamekiona kwa wakati huo, kila mtu ambaye aliiona habari ile aliamua kulinunua gazeti lile. Japokuwa tukio lile lilitokea usiku wa saa moja lakini waandishi walihakikisha kwamba wanaitoa gazetini habari ile hata kama haikuwa na maelezo mengi.
Watu walionekana kusikitika kupita kawaida huku wengine ambao walikuwa na mapenzi ya dhati kwa Yusufu wakianza kulia. Tukio lile ambalo lilikuwa limetokea lilionekana kuwasikitisha kupita kawaida. Hiyo ndio ilikuwa habari ambayo ilikuwa ikisikika sana katika masikio ya watu wengi ndani ya jiji la Dar es Salaam.
Nyimbo zake zikaanza kupigwa katika vituo mbalimbali vya redio pamoja na televisheni kuwa kama sehemu ya kumuenzi. Katika kila kona ndani ya jiji la Dar es Salaam watu walikuwa wakizungumzia kuhusu tukio lile ambalo katika kipindi hicho lilionekana kuwa kubwa kuliko tukio lolote ambalo lilikuwa limetokea mwaka huo.
Waandishi wengi wa habari walikuwa wakielekea nyumbani kwake, Sinza alipokuwa akiishi, milango ilikuwa imefungwa japokuwa hali ilikuwaikionyesha kwamba kulikuwa na mtu ndani ya nyumba hiyo. Kila walipokuwa wakigonga hakukuwa na mtu aliyekuja kufungua ila walipoendelea zaidi na zaidi, Kelvin akatokea mahali hapo.
“Kuna nini?” Kelvin aliwauliza.
“Tumekuja kufanya mahojiano pamoja nawe Kelvin kwa sababu wewe ndiye mtu wa karibu sana na marehemu Yusufu” Mwandishi mmoja wa habari alimwambia Kelvin.
“Kwa hiyo ninyi mnataka niwaambie nini kuhusu Yusufu?” Kelvin aliwauliza.
“Mambo kadhaa”
“Kama yapi?”
“Turuhusu kwanza tuingie”
“Hapana. Kuna kazi nyingi zinafanyika kwa sasa ndani ya nyumba hii. Njooni kesho” Kelvin aliwaambia.
“Ila umepata taarifa kwamba Yusufu ameuawa garini kwa kuchomwa moto?”
“Yeah! Niliona kwenye magazeti yenu ya leo” Kelvin alijibu.
“Unalizungumziaje tukio hili?”
“La kawaida tu ambalo linaweza kumtokea mtu yeyote. Yaani ni kama mwandishi wa habari Vanessa alivyochomwa moto kule nchini Marekani ndani ya gari lake. Kwa hiyo hakuna cha kushangaa” Kelvin alitoa majibu ambayo yalimshangaza kila mtu.
“Kwa jinsi unav.........” Mwandishi wa habari alisema lakini hata kabla hajamalizia sentensi yake Kelvin akaingilia.
“Nafikiri mmemaliza” Kelvin alisema na kisha kufunga geti.
Kila mwandishi wa habari alionekana kushangaa, hawakuamini kama Kelvin asingewaonyeshea ushirikiano wowote ule juu ya kile ambacho walikuwa wakikitaka kukifahamu zaidi na zaidi. Tayari wasiwasi ukaanza kuwaingia kwamba kulikuwa na uwezekano kwamba Kelvin alikuwa nyuma ya kile ambacho kilikuwa kimetokea.
Bado watu walikuwa wakiendelea kuhuzunika huku taarifa ile ikizidi kuvuma kadri muda ulivyokwenda mbele. Kutokana na kuwa na jina kubwa pamoja na kuwa na mashabiki wengi kuliko msanii yeyote yule nchini Tanzania, baada ya masaa ishirini na nne, Tanzania nzima ilikuwa imefahamu juu ya kile ambacho kilikuwa kimetokea jijini Dar es Salaam.
Kila aliyezipata taarifa zile alikuwa akihuzunika kupita kawaida, nyota ambayo ilikuwa ikiwaka tayari ikaonekana kuzimwa na watu ambao walionekana kutokupendezwa na mafanikio ambayo alikuwa ameyapata. Tetesi nyingi zikaanza kusikika kutoka kwa watu mbalimbali kwamba The King alikuwa amehusika huku wengine wakisema kwamba hata mameneja wa wasanii wengine walikuwa wamehusika katika hilo kwa sababu tu Yusufu alikuwa amepata mafanikio zaidi ya wasanii wote nchini Tanzania.
Tetesi hazikuwa hizo tu bali kadri muda ulivyozidi kuongezeka na ndivyo tetesi zaidi na zaidi zilivyozidi kusikika katika kila kona jijini Dar es Salaam. Watu ambao walikuwa wakipafahamu sehemu alipokuwa akiishi Yusufu, wakaanza kuelekea huko huku wakiamini kwamba wangekuta maturubai ila kitu cha ajabu hakukuwa na maturubai yoyote yale jambo ambalo liliwashangaza sana watu.
“Mbona hali haieleweki sasa?” Jamaa mmoja aliwauliza wenzake.
“Yaani hakuna maturubai wala hakuna kitu chochote kinachoonyesha kwamba kuna msiba umetokea. Au watakuwa wameupeleka msiba Bagamoyo? Hapana bwana, hata kama wameupeleka msiba Bagamoyo, hata hapa inabidi kuwe na maturubai” Jamaa mwingine alisema huku kila mmoja akionekana kushangaa.
Tayari hali ilionekana kuwa tata. Mwili ule wa Yusufu ulikuwa umekwishapelekwa hospitali na kuihifadhiwa mochwari lakini kitu cha ajabu hakukuwa na mtu yeyote ambaye aliufuatilia. Waadishi wa habari ndio ambao walionekana kuwa kwenye wakati mgumu kwa wakati huo, walichokifanya ni kuanza kusafiri kuelekea Bagamoyo nyumbani kwa wazazi wake kwa ajili ya kupata taarifa zote kuhusiana na msiba ule.
“Kuna taarifa kwamba mtoto wako amefariki” Mwandishi wa habari, John alimwambia mzee Kessi ambaye alikuwa pamoja na mke wake, Bi Fatuma.
“Yeah! Tumeziona taarifa hizo magazetini siku ya leo” Mzee Kessi aliwaambia.
“Hizi zimekuwa taarifa za kutuchanganya sana mpaka muda huu. Yaani nyumbani kwa marehemu hakuna hata maturubai, tumekuja hapa napo hakuna maturubai. Hivi msiba huu unaweza kuwa wapi?” John aliuliza.
“Unajua ninachokiamini ni kwamba kila siku waandishi wamekuwa watu wa kuandika hisia zao zaidi ya taarifa inavyoonekana. Mimi kama mimi sidhani kama mtoto wangu ameuawa. Moyo wangu umekuwa mgumu sana kuamini hilo” Mzee Kessi alimwambia John.
“Mmmh! Sasa hapa inakuwaje tena? Tumejaribu kumpigia simu lakini napo haipatikani kabisa. Hivi tuelewe nini tena?” John aliuliza.
“Kwani taarifa zilisemaje?”
“Kwamba Yusufu alitekwa. Baada ya kutekwa, saa moja baadae gari lile likakutwa katika msitu wa pande huku likiwa limechomwa moto na mwili wake kuwa ndani” John alijibu.
“Sasa mnaamini vipi kwamba yule atakuwa ni Yusufu?”
“Vipimo. Mwili ulipimwa urefu, ulikuwa sawasawa na urefu wake ambao uliandikwa kwenye leseni yake ya udereva.
“Mmmh! Sasa mbona Kelvin hakutuambia kama Yusufu ameuawa?”
“Hata sisi hatufahamu kwa nini. Yaani hata tulipokwenda nyumbani kwake anapoishi, hakuna hata turubai” John alijibu.
“Ila na nyie mnaonekana kutuchanganya sana”
“Kwa nini mzee?”
“Mna uhakika kwamba Yusufu ameuawa?”
“Kutokana na mashahidi, vipimo, tuna uhakika huo”
“Kwa hiyo vitu hivyo tu ndivyo ambavyo vinawafanya kuamini hilo?”
“Ndio mzee”
“Gari lilichomwa moto saa ngapi?”
“Saa moja usiku” John alijibu.
“Mmmh! Kwa hiyo aliuawa muda huo?”
“Ndio”
“Sasa mbona jana saa nne usiku alitupigia simu na kutuambia kwamba yupo salama!” Mzee Kessi alimwabia John.
“Unasemaje?”
“Kwani wewe umesikia nimesemaje?”
“Hapana. Alikupigia simu na kukwambia kwamba yupo salama?” John aliuliza huku akionekana kushtuka.
“Ndio” Mzee Kessi alitoa jibu ambalo lilionekana kumchanganya sana John.
****
John alionekana kuchanganyikiwa kupita kawaida, jambo aliloambiwa kwamba Yusufu alikuwa hai lilionekana kumchanganya kupita kawaida. Alichokifanya ni kuanza kurudi jijini Dar es salaam na kuwafikishia taarifa ile waandishi wenzake ambao wote waliamini kwamba Yusufu alikuwa ameuawa kwa kuchomwa moto garini.
Hakutaka kuwapigia simu na kuwaelezea jambo lile, alichokuwa akikitaka ni kuwaambia ana kwa ana. Garini, John alionekana kuchanganyikiwa, mpaka katika kipindi hicho hakujua ni kitu gani ambacho kilikuwa kinaendelea. Maswali kibao yalikuwa yakimiminika kichwani mwake juu ya mwili ule ambao ulikutwa ndani ya gari. Katika kila swali ambalo alikuwa akijiuliza, majibu yake yalikuwa yakimchanganya kupita kawaida.
Alipofika jijini Dar es Salaam, akachukua bajaji ambayo ilimpeleka mpaka ofisini kwao na kisha kuwaambia waandishi wenzake kile ambacho kilikuwa kimesemwa na mzee Kessi. Kila mtu aliyezisikia habari zile alionekana kuchanganyikiwa, wakabaki wakimwangalia John mara mbili mbili.
“Unasemaje?” Mhariri mmoja aliuliza kwa mshtuko.
“Hata mimi niliuliza hivyo hivyo” John alijibu.
“Hapana. Ila si vipimo vyote vimepimwa na kujulikana!”
“Ndio”
“Sasa inakuwaje wanaposema kwamba Yusufu alipiga simu usiku?”
“Hata mimi nashangaa sana”
“Hapa kuna kitu bwana. Tayari taarifa hii imeshaonekana kuwa na utata mkubwa”
“Kwa hiyo tuwaambiaje wananchi?”
“Yaani hata cha kuwaambia sikioni. Tukiwaambia kwamba aliuawa, wazazi wanaonekana kukataa hilo. Na kama tukisema yupo hai, Watanzania watatuona wazinguaji kwa sababu tuliandika kwamba ameuawa. Na kama tukisema hivyo hivyo kwamba yupo hai, watatuuliza kwamba yupo wapi?. Yaani kila taarifa tutakayoitoa itaonekana kusababisha maswali mengi” John alisema huku akionekana kuchanganyikiwa.
****
The King alionekana kuchanganyikiwa hasa mara baada ya taarifa kutolewa kwamba Yusufu alikuwa yupo hai, alionekana kutokuamini kabisa juu ya taarifa zile jambo ambalo liimfanya kumuita Sudi na kumuuliza juu ya zile taarifa ambazo alikuwa amezisikia. Akatulia kwenye kochi huku akionekana kutokuwa na furaha.
Mawazo yake kwa wakati huo yalikuwa yakimfikiria Yusufu, hakuamini kama kweli alikuwa hai na wakati alikuwa amelipa kiasi cha shiingi milioni kumi kwa ajili ya kuona kwamba mtu huyo anauawa kwa kuchomwa moto. Maswali mengi yalizidi kuongezeka kichwani mwake hali ambayo ilimfanya kukosa amani.
Akasimama kutoka pale kochini na kisha kuanza kutembeatembea pale sebuleni. Kila wakati alikuwa akiipiga mikono yake kwa hasira, hakuamini kile ambacho alikuwa akikiangali kwenye gazeti. Kila alipokuwa akiliangalia gazeti ambalo lilikuwa na taarifa juu ya Yusufu kwamba alikuwa mzima wa afya na wala hakuwa ameauwa kama ilivyoandikwa ilimfanya kuchukia.
The King alikaa katika hali hiyo kwa muda wa saa moja na ndipo ambapo Sudi akaingia mahali hapo huku akionekana kuwa na mshangao. Wote wakabaki wakiangaliana tu huku kila mmoja akionekana kuwa na dukuduku moyoni.
“Ndio mmefanya nini kutudanganya?” The King aliuliza huku akimwangalia Sudi kwa macho yaliyojaa hasira.
“Wala hatujakudanganya bosi” Sudi alijitetea.
“Kwa hiyo wenye magazeti waongo?” The King alimuuliza huku akichukua gazeti lile na kumpatia Sudi.
“Huu ni uzushi kabisa” Sudi alisema.
“Hapana. Huu si uzushi. Huu ni ukweli kabisa” The King alimwambia Sudi.
“Ni uzushi. Yusufu tulimuua kwa kumchoma moto ndani ya gari. Hatuwezi kukudanganya katika hili” Sudi alijitetea.
“Kwa hiyo waandishi wa habari waongo?”
“Inawezekana. Kama Yusufu yupo hai mbona picha yake hawajaiweka?” Sudi aliuliza.
Swali lile kidogo likaanza kuonekana kuwa na maana kichwani mwa The King. Alijua kabisa kwamba waandihsi wa habari walikuwa wameandika kwamba Yusufu alikuwa ameuawa katika siku iliyopita. Katika siku hiyo, taarifa ilikuwa kinyume chake kwa kusema kwamba Yusufu alikuwa hai, ili kuifanya taarifa yao kuaminika zaidi na zaidi kwa wasomaji, kulikuwa na ulazima wa kuweka picha ya Yusufu.
“Ila inawezekana”
“Umeonaee. Yaani kama yupo hai kama wanavyoamini basi ni lazima picha yake ingeonekana tu” Sudi alimwambia The King.
Kwa wakati huo tayari walikwishaona kwamba waandishi wa habari walikuwa wamefanya makosa ya kuandika kwamba Yusufu alikuwa hai na wakati alikuwa ameuawa ndani ya gari lile ambalo lilichomwa moto na Sudi pamoja na wenzake. Mara baada ya wasomaji kuiona taarifa ile ambayo iliandikwa kwamba Yusufu alikuwa hai, kuna swali moja ambalo liliwajia vichwani mwao, je yule ambaye alikuwa amechomwa moto ndani ya gari alikuwa nani? Hilo lilikuwa swali ambalo lilikosa jibu vichwani mwa watu ambao walikuwa wakijiuliza.

Je nini kitaendelea?
Je Yusufu amekufa kwa kuteketezwa na moto?
Itaendelea kesho saa nne usiku.
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 8

KWA WASOMAJI WAPYA KABISAAAA.

Kijana Yusufu amekulia katika maisha ya kimasikini pamoja na rafiki yake, Kelvin. maisha hayo ndio ambayo yanamfanya Yusufu kujiingiza katika uimbaji wa muziki wa kizazi kipya. Anapewa jina la The Ruler, jina ambalo linafanana na la msanii mkongwe, The King.
Baada ya kusota sana kwenye muziki, anampata mfadhili, huyu anaitwa Papaa Pipo, mwanaume mwenye fedha nyingi. Papaa Pipo anampeleka kuzimu, huko Yusufu anasaini mkataba wa damu kwa kumtumikia shetani. Anaambiwa kwamba atapata utajiri mkubwa sana, atapata mvuto mwingi sana. Ameahidiwa mengi na kupewa masharti mawili tu. Asifanye mapenzi siku za Jumapili na Jumatano na hata asipate mtoto. kama akitaka kuoa, aoe tu, ila mtoto hatakiwi kumpata. Yusufu anachukulia kila kitu rahisi.
The Ruler hasikiki tena japokuwa yeye ni mkongwe. Jambo hilo linampa hasira, anamchukia Yusufu, anachokiamua ni kumuua tu. Anawatuma vijana wake ambao wanamkamata Yusufu na kisha kumpeleka katika msitu wa Pande na kisha kumchoma moto garini. Yusufu ahangaiki garini, ametulia tuli huku akitekezwa na moto ule.
Je nini kitaendelea?
Je Yusufu amekufa?
TWENDE PAMOJA.


Gari lilikuwa likiendeshwa kwa mwendo wa kasi katika msitu wa Pande ambapo baada ya mwendo fulani likasimamishwa katika eneo ambalo lilikuwa limezungukwa na miti mingi mikubwa na mirefu. Muda wote huo Yusufu alikuwa akiomba aachwe huru huku akiahidi kulipa kiasi kikubwa cha fedha kama vijana wale wangekuwa wanahitaji fedha.
Hakukuwa na mtu ambaye alionekana kujali, kitu ambacho walikuwa wakikitaka kwa wakati huo ni kumuua tu kwa kumchoma moto ndani ya gari lile. Baada ya kulisimamisha gari, Sudi na Ahmad wakateremka na kuanza kuangalia angalia eneo Ramadhani akiwa amebaki na Yusufu garini.
Ghafla katika hali ambayo wala Yusufu hakuitegemea akashangaa mlango wa nyuma katika upande aliokaa ukijitoa loki na kujifungua. Kitu cha kwanza alichokifanya Yusufu ni kumwangalia Ahmadi ambaye alikuwa pembeni yake, Ahmadi alionekana kutokuwa na habari yoyote ile. Yusufu akaanza kutoka nje ya gari lile.
Alipotoka nje, pembeni yake kukaonekana kuwa na gogo ambalo alisikia sauti moyoni ikimwambia kwamba alitakiwa kuliingiza gogo lile ndani ya gari lile tena katika sehemu ambayo alikuwa amekaa. Alichokifanya Yusufu ni kufanya kama ambavyo sauti ile aliyoisikia ilivyomuelekeza.
Jambo ambalo lilionekana kumshangaza Yusufu ni kwamba Ramadhani hakuwa akijua kitu chochote kilichokuwa kikiendelea japokuwa alikuwa kwenye kiti kile kile kule nyuma. Mara baada ya kuliweka gogo lile pembeni ya Ramadhani, hapo hapo akaanza kukimbia kuelekea barabarani. Yusufu hakusimama, alikuwa akiendelea kukimbia mpaka pale ambapo akakutana na barabara na kisha kuingia ndani ya daladala na safari ya kuelekea nyumbani kuanza.
Kutokana na giza kuingia, hakukuwa na mtu yeyote ambaye alijua kwamba mtu ambaye aliingia alikuwa Yusufu au The Ruler kama alivyokuwa akijulikana na wapenzi wa muziki. Safari ile iliendelea zaidi mpaka alipofika Ubungo ambapo akaonganisha na bajaji mpaka kufika nyumbani kwake na kuanza kuugonga lango na Kelvin kuufungua.
“Mungu wangu!” Kelvin alionekana kushangaa.
“Niletee ufunguo wa gari haraka” Yusufu alimwambia Kelvin ambaye akaelekea ndani na kumletea ufunguo wa gari.
“Kuna nini tena? Mbona sikuelewi! Wale watu waliokuchukua ni wakina nani tena?” Kelvin aliuliza maswali mfululizo lakini Yusufu hakujibu kitu.
“Nisikilize Kelvin. Kama kutatangazwa taarifa yoyote ile, kubaliana nao ila usiseme kama umeniona. Umesikia?” Yusufu alimwambia Kelvin.
“Ndio. Ila nini kiliendelea?”
“Usijali. Nikirudi nitakwambia”
“Hapana Yusufu. Mimi ni rafiki yako, niambie kitu gani kimetokea” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Usijali. Akili yangu haijatulia. Ngoja nikirudi nitakuelezea. Ila jua kwamba wale watu walitaka kuniua” Yusufu alimwambia Kelvin ambaye akaonekana kushtuka.
“Walitaka kukuua?”
“Ndio”
“Sasa unaelekea wapi tena?” Kelvin aliuliza.
“Kuna sehemu naelekea. Nitarudi muda si mrefu” Yusufu alijibu.
“Ngoja twende wote basi”
“Hapana. Acha niende peke yangu. Nitarudi muda si mrefu” Yusufu alisema na hapo hapo kuwasha gari lake na kisha kuondoka mahali hapo.
Japokuwa hakuwa amekimbia lakini kijasho chembamba kikimtoka. Muda wote Yusufu alikuwa na wasiwasi, hakujua ni kitu gani ambacho kilikuwa kimeendelea. Muda wote alikuwa akijiuliza kuhusu ile sauti ambayo aliisikia ambayo ilimwambia kwamba alitakiwa kuondoka mahali pale huku akitakiwa kuliweka gogo lile katika sehemu aliyokuwa amekaa.
Katika kila swali ambalo alikuwa akijiuliza mahali pale alikosa jibu. Kwa wakati huo safari yake hiyo ilikuwa ni kuelekea nyumbani kwa Papaa Pipo ambapo huko angemuelezea kila kitu ambacho kilitokea. Hakuchukua muda mrefu kufika Kijitonyama, akalipaki gari lake na kuteremka na kuanza kuugonga mlango.
“Karibu” Mlinzi alimkaribisha na kuingia ndani.
Yusufu hakutaka kumsalimia mlinzi, alichokifanya ni kuelekea moja kwa moja ndani ya nyumba ile ambapo akamkuta Papaa Pipo akiwa amejipumzisha kochini akiangalia filamu ya Kitanzania iliyoigizwa na msanii nguri, Vonso Almeida.
“Mbona umekuja bila taarifa? Kuna tatizo?” Papaa Pipo alimuuliza Yusufu hata kabla ya salamu.
“Nimechanganyikiwa” Yusufu alijibu.
“Umechanganyikiwa? Kuna nini tena?” Papaa Pipo alimuuliza huku akionekana kushtuka.
“Nilitekwa”
“Ulitekwa! Na nani?”
“Kuna watu watatu waliniteka maeneo ya Tandale” Yusufu alimwambia Papaa Pipo.
“Acha utani bwana”
“Kweli tena. Yaani hapa unaponiona ni kwamba nimewatoroka porini ambapo walitaka kuniua” Yusufu alimwambia Papaa pipo ambaye alionekana kupigwa na mshangao.
“Unanitania Yusufu”
“Huo ndio ukweli. Yaani hapa nimechanganyikiwa kabisa” Yusufu alimwambia Papaa Pipo.
“Yaani ilikuwaje mpaka ukatekwa?”
“Sina muda wa kukuelezea Papaa. Cha msingi naomba twende kwa mzee Onyango kwa sababu kuna vitu bado sijavielewa kabisa” Yusufu alimwambia Papaa Pipo.
“Kwa mzee Onyango kufanya nini tena?”
“Ili twende kule tulipokwenda”
“Wapi?”
“Nilipoweka agano la damu” Yusufu alijibu.
“Hiyo si lazima mpaka twende kwa mzee Onyango. Hapa hapa kwangu tunaweza kwenda kule” Papaa Pipo alimwambia Yusufu ambaye alionekana kushtuka.
“Sasa mbona siku ile tulikwenda kule kwa mzee Onyango?”
“Ile ni kwa sababu mtu anapotaka kujiunga na imani yetu ni lazima aende kule. Baada ya hapo utaweza kwenda kule kupitia kwa aliyekupeleka. Au haujamuelewa mkuu siku ile ibadani?” Papaa Pipo alimuuliza.
“Nilimuelewa japo si sana”
“Basi hivyo ndivyo ilivyo. Baada ya muda fulani, nawe utapewa kioo chako” Papaa Pipo alimwambia Yusufu na kisha kumtaka kumfuata chumbani.
Wote wakaanza kuelekea chumbani ambapo wakaingia na kisha Yusufu kukaa kitandani huku akionekana kama mtu ambaye alikuwa na shauku ya kutaka kufahamu vitu fulani. Papaa Pipo akalifuata kabati la nguo na kisha kutoa kioo kikubwa na kukiegemeza ukutani na kumtaka Yusufu kuanza kuvua nguo zake kama ilivyokuwa sheria yao. Kwa haraka haraka Yusufu akaanza kuvua nguo na kisha taa kuzimwa huku wote wakiwa watupu.
Wakakisogelea kioo kile na kisha kuanza kuongea maneno yasiyoeleweka. Kama ilivyo kawaida, miale ya radi ikatokea katika kioo kile na kisha Yusufu kuingia huku Papaa Pipo akifuata. Wakafika katika ulimwengu ule mwingine, ulimwengu ambao ulionekana kuwa kama ulimwengu huu ila tofauti ilikuwa pale ambapo watu wa kule walikuwa watupu bila nguo miilini mwao.
Moja kwa moja wakaanza kuelekea katika nyumba ile ambayo mkataba wa damu ulisainiwa na kisha kukalia viti vile ambavyo vilikuwa vimezunguka meza kubwa mahali pale. Wote wakatakiwa kuinamisha vichwa vyao chini katika kipindi ambacho mhusika mkubwa alipokuwa akiingia mahali pale.
Wala haukuchukua muda mrefu, idadi ya viumbe vya ajabu ambavyo vilikuwa na mwili wa binadamu na wanyama wa porini wakatokea mahali pale huku wakiongozwa na mtu ambaye alionekana kuwa kiongozi mkubwa. Huyu hakuwa yule ambaye alimpa mkataba wa damu kuusaini bali alikuwa mwingine kabisa ambaye alikuwa na kichwa cha ng’ombe, miguu ya binadamu na kifuani akiwa na manyoya mengi na videleni akiwa na kucha ndefu.
Mara baada ya kufika katika eneo lile wote wakakaa katika viti huku Papaa Pipo na Yusufu wakiwa wameendelea kuinamisha vichwa vyao chini. Walipotakiwa kuviinua, Yusufu akaonekana kushtuka japokuwa haukuwa mshtuko kama ule wa siku ya kwanza.
Yule kiongozi akaanza kuongea katika lugha ya ajabu ambayo wala haikuwa ikieleweka huku mmoja kati ya vile viumbe ambavyo alikuja navyo vikianza kutafsiri lugha ile kwa lugha ya Kiswahili. Yusufu alikuwa makini kusikiliza.
“Kama tulivyokuahidi ndivyo tutakavyofanya. Tutakulinda kila siku, hakuna atakayenyoosha mkono wake kukuua” Mkalimani alimwambia Yusufu na kuendelea.
“Tulikuwa tumeona kila kinachoendelea. Tulichoamua ni kuendelea kukulinda. Amini kwamba kupitia wewe tumeweza kupa watu wengi sana, tumeweza kupata damu nyingi sana. Kazi yetu unaifanya kwa mafanikio makubwa sana” Mkalimani yule alimwambia Yusufu.
“Sijakielewa kile ambacho kilikuwa kimeendelea kule porini” Yusufu aliwaambia.
“Tulichokifanya ni kumpiga bumbuwazi yule ambaye ulibaki nae gari, hakuelewa kitu chochote kilichoendelea. Tulichokifanya ni kukuwekea gogo na kisha kukutaka kuliingiza garini huku tukilivisha gogo lile taswira yako. Amini kwamba tulichokisema ndicho hicho tutakachokifanya. Kila siku tutaendelea kukulinda na kuwa pamoja nawe” Mkalimani alisema na kuendelea.
“Kuanzia leo hii, kila kitu ambacho tulikupa kitaongezeka mara mbili zaidi. Umaarufu ulioupata utaongezeka mara mbili, fedha ulizozipata zitaongezeka mara mbili. Kila ulicho nacho kitaongezeka mara mbili” Mkalimani alimwambia Yusufu na kutakiwa kupiga magoti na kisha kuanza kumwagiwa damu kama kuwekewa ulinzi zaidi.
Kipindi hicho kila kitu kilikuwa kimefanyika kama kawaida huku akipelekwa katika vyumba vilivyokuwa ndani ya nyumba ile na kisha kupewa begi lililokuwa na nguo mbalimbali ambazo alitakiwa kuzivaa katika kipindi ambacho atakuwa akienda kurekodi au katika kipindi ambacho atakuwa akifaya shoo.
“Na hizi pete ni za nini?” Yusufu aliuliza.
“Hizi nazo utatakiwa kuzivaa muda wote ule. Zinaonekana kuwa pete za kawaida, lakini amini kwamba hizi pete ndizo zitakuwa ulinzi wako na chachu ya mvuto wako kwa wapenzi wa muziki” Yusufu aliambiwa.
“Sawa bwana wangu” Yusufu aliitikia huku akiinamisha kichwa chake kama ishara ya kumuabudu.
Siku hiyo ndiyo ambayo akakabishiwa kioo ambacho angekikuta chumbani kwake katika kipindi ambacho angerudi nyumbani kwake, kioo kile kitakuwa chumbani kwake. Baada ya kukamilisha kila kitu, akaambiwa kwamba hata lile begi la nguo atalikuta chumbani kwake huku likiwa pamoja na manukato yaliyokuwa na mvuto.

Je nini kitaendelea katika maisha ya Yusufu?
Umeipenda?
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 9

Kila kitu kilipomalizika, Yusufu pamoja na Papaa Pipo wakaondoka kule walipokuwa na kutokea ndani ya nyumba ya Papaa Pipo. Yusufu akaonekana kuridhika kwa kila kitu katika kipindi hicho, amani ikarudi moyoni mwake kwa kuona kwamba ulinzi mkali bado ulikuwa ukiendelea kuwekwa katika maisha yake.
“Mbona wamesema kwamba nimewapa sana damu? Hapo walinichanganya sana. Hivi walimaanisha nini pale?” Yusufu alimuuliza Papaa Pipo huku wakielekea nje.
“Unakumbuka kipindi kile ulipokwenda kufanya shoo Mwanza kwenye uwanja wa CCM Kirumba?” Papaa Pipo aliuliza.
“Nakumbuka sana”
“Unakumbuka kwamba kuna watu zaidi ya themanini walipata ajali wakati wanatoka Shinyanga kuja Mwanza kuona shoo yako?” Papaa Pipo alimuuliza.
“Ndio”
“Zile zilikuwa zi zawadi ya damu. Yaani kila kitu ambacho kilitokea siku ile kilikuwa kwenye mipango yetu” Papaa Pipo alimwambia Yusufu ambaye alionekana kushangaa.
“Mmmh! Kweli kila kitu kipo kwenye mipango” Yusufu alisema.
Mara baada ya kuagana, Yusufu akaingia ndani ya gari lake na kisha kuanza safari ya kuelekea nyumbani kwake huku ikiwa imetimia saa nne na robo usiku. Alichokifanya kwa wakati huo ni kuchukua simu yake na kisha kuwapigia wazazi wake na kuwaambia kwamba alikuwa mzima na hivyo hawatakiwi kuamini kitu chochote ambacho wangekisikia juu yake.
Kujiamini kukaonekana kuongezeka zaidi na zaidi moyoni mwa Yusufu.Ulinzi ambao alikuwa akipewa kwa wakati huo ulionekana kuwa mkubwa kupita kawaida. Wala hakuchukua dakika nyingi sana, akawa amekwishafika nyumbani ambako akaanza kuelekea sebuleni na kumkuta Kelvin akiangalia televisheni.
“Vipi tena?” Yusufu alimuuliza Kelvin.
“Wametangaza kwamba umeuawa kwa kuchomwa na moto” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Mungu wangu! Kumbe walikuwa na lengo la kunichoma moto!” Yusufu alisema kwa mshtuko.
“Ndio hivyo. Ila mpaka sasa hivi sijaelewa kipi kilitokea! Kwenye taarifa ya habari wanasema kwamba umeuawa garini na mwili wako kuonekana, hapa inakuwaje kuwaje Yusufu?” Kelvin aliuliza huku akionekana kuwa na maswali mengi kichwani mwake.
“Niliwatoroka porini. Nafikiri wameamua kufanya hivi ili kumzubaisha mtu aliyewatuma” Yusufu alijibu.
“Ila mbona kila nik......” Kelvin alisema lakini hata kabla hajamalizia sentensi yake, Yusufu akaingilia.
“Ngoja nikapumzike kwanza” Yusufu alimwambia Kelvin na kisha kuondoka mahali hapo.
Mpaka katika kipindi hicho Yusufu hakutaka maswali zaidi, hakuona kitu ambacho alitakiwa kukijibu na wakati mpaka anaondoka kule porini, alikuwa haelewi vizuri kile ambacho kilikuwa kimetokea zaidi ya kupewa maelezo na viumbe wale ambao alikutana nao kwenye ulimwengu wa giza.
Yusufu akaufuata mlango wa kuingilia chumbani kwake na kisha kuufungua na kuwasha taa. Kioo kikubwa kilikuwa kikionekana mbele yake huku kikiwa kimeegemeshwa ukutani. Yusufu akaachia tabasamu pana na kisha kuanza kukisogelea. Pembeni mwa kile kioo kulikuwa na begi kubwa la nguo, akainama na kisha kufungua zipu.
Nguo kadhaa zilikuwepo ndani ya begi lile. Yusufu akaanza kuitoa nguo moja baada ya nyingine na kisha kuanza kuziangalia. Kwake, zilionekana kuwa nguo nzuri na zilizokuwa zikivutia sana. Hizo ndizo zilikuwa nguo ambazo alitakiwa kuzivaa kuanzia muda huo. Akaanza kuzitoa na kisha kuanza kuzijaribisha, zilionekana kumtosha sana, zilikuwa zimeendana na mwili wake.
“Nimezipenda” Yusufu alijisemea huku tabasamu pana likionekana kuwa usoni mwake.
****
Hali ilikuwa haieleweki kabisa, waandishi wa habari hawakuwa wakieleweka hata kidogo. Siku mbili ziliyopita walikuwa wameandika kwamba Yusufu alikuwa ameuawa kwa kuchomwa moto ndani ya gari ambalo lilitelekezwa katika msitu wa Pande uliokuwa Mbezi lakini siku hiyo taarifa zilionekana kuwa tofauti kabisa.
Watu wakashindwa kuelewa kabisa kwani kila mtu alionekana kuwashangaa waandishi hao ambao waliandika taarifa magazetini bila kufuatilia habari ile kwa kina. Swali likabaki kuwa vichwani mwa mashabiki juu ya mahali alipokuwa Yusufu, msanii ambaye walikuwa wakimpenda kuliko msanii yeyote yule Afrika Mashariki.
Waandishi wa habari walikuwa wakiendelea kumuulizia Yusufu sehemu mbalimbali ikiwemo nyumbani kwake, Sinza lakini wala hawakupata majibu yaliyoridhisha. Uwepo wa Yusufu machoni mwao ndio ambao ungedhihirisha kwamba msanii huyo alikuwa hai na si kama ilivyokuwa imetangazwa na kuandika katika vyombo mbalimbali vya habari.
“Unajua hawa waandishi wa kibongo wanaweza kuua watu aisee” Jamaa mmoja alimwambia mwenzake.
“Umeonaeee. Yaani wanaandika habari bila kuwa na uhakika kabisa” Jamaa mwingine alijibu.
“Yaani niliposoma habari juzi kwamba The Ruler ameuawa, nilijisikia mwili ukifa ganzi kabisa. Yaani kama ningekuwa na moyo mwepesi, ningeweza hata kufa” Jamaa yule aliendelea kumwambia mwenzake.
“Kuna watu kadhaa walikuwa wamekwishaweka maturubai nyumbani kwao, hasa watu wa mikoani”
Siku hiyo mchana ndio ilikuwa siku ambayo Yusufu akajitokeza machoni mwa waandishi wa habari ambao hawakuwa wamemuona kwa muda wa siku mbili tangu gari lile alilokuwa ameingizwa kuchomwa moto na watu wasiojulikana huku mwili wa mtu aliyefanana nae kwa mambo mengi ukikutwa ndani ya gari lile. Waandishi walionekana kushangaa, maswali kibao yakaanza kumiminika juu ya mtu ambaye alikuwa amechomwa moto ndani ya gari lile.
Lawama zote zikashushwa katika jeshi la polisi kwa kutoa taarifa ambazo hazikuwa na uhakika mkubwa na wakati hata uchunguzi haukuwa umefanyika. Yusufu akaanza kuhojiwa mambo mbalimbali na waandishi wale ambao walionekana kuwa na kiu ya kutaka kufahamu ni kitu gani ambacho kilikuwa kimetokea mpaka kuwa hai katika kipindi hicho huku kila mtu akijua kwamba alikuwa ameuawa.
“Siwezi kufa kwa matakwa ya mwanadamu. Nitakufa kwa matakwa ya Mungu tu” Yusufu aliwaambia waandishi wa habari.
“Ila taarifa zinasema kwamba ulitekwa. Ni za kweli hizo?” Mwandishi mmoja, Rebecca alimuuliza.
“Yeah! Nilitekwa pale Tandale kwa Tumbo” Yusufu alijibu.
“Nini kiliendelea baada ya hapo?” Rebecca alimuuliza.
“Walinipeleka porini huku wakiwa na lengo moja tu, kuniua” Yusufu alimwambia.
“Sasa ikawaje mpaka mpango wao haukufanikiwa?”
“Nilichokifanya ni kuwahonga tu ili waniachie” Yusufu limwambia Rebecca.
“Uliwahonga?”
“Ndio. Niliwapa kiasi cha shilingi milioni kumi na tano na ndipo wakaniachia” Yusufu alimwambia Rebecca.
“Wakakubali kukipokea kiasi hicho cha fedha?”
“Ndio. Kwa muonekano ambao walikuwa nao walionekana dhahiri kuhitaji fedha. Nilipowapa, wakaniachia na kuondoka zangu” Yusufu alimwambia Rebecca.
“Na vipi kuhusu yule mtu ambaye alichomwa moto?”
“Hapo sifahamu kitu chochote kile. Sijui walifanya kitu gani mpaka kumuua mtu mwingine” Yusufu alimwambia Rebecca.
“Mmmh!”
“Ndio hivyo dada yangu. Fedha ndio kila kitu” Yusufu alimwambia Rebecca.
Yusufu akaonekana kuridhika. Kitu ambacho alikijua ni kwamba watekaji wale walikuwa wametumwa na mtu fulani kwa ajili ya kumuua. Kile alichokisema mahali hapo kilikuwa ni kama uchochezi kati ya watekaji wale na mtu ambaye alikuwa amewatuma kwenda kufanya mauaji.
****
The King akaonekana kuchanganyikiwa, maneno ambayo alikuwa ameongea Yusufu yalionekana kumchanganya. Hakuamini kama vijana wale ambao alikuwa amewatuma walikuwa wamemgeuka kiasi kile kwa kuchukua fedha za Yusufu na kisha kumuacha hai. Kwa haraka sana huku akionekana kukasirika akachukua simu yake na kisha kumpigia Sudi huku akimtaka nyumbani kwake haraka iwezekanavyo.
Ni ndani ya dakika ishirini, Sudi akafika mahali hapo. The King hakuongea kitu chochote kile, alibaki akimwangalia Sudi huku uso wake ukiendelea kuwa katika hali iliyojaa hasira kali. Akachukua chupa yake ya bia ambayo ilikuwa mezani na kupiga fundo moja na kisha kuyapeleka macho yake usoni mwa Sudi.
“Huwa unaangalia taarifa ya habari hasa kipindi cha usiku?” Lilikuwa swali la kwanza ambalo The King alimuuliza Sudi.
“Hapana” Sudi alijibu.
“Kwa nini?”
“Kwa sababu nakuwa na mambo mengi ya kufanya kipindi hicho” Sudi alimjibu The King.
“Sawa. Mara yako ya mwisho kuangalia taarifa ya habari usiku ilikuwa lini?” The King alimuuliza Sudi.
“Mwaka jana. Tena dakika mbili tu” Sudi alijibu
“Ok! Kwa hiyo hata taarifa ya habari ya leo haujaiangalia?” The King alimuuliza.
“Ndio”
“Hivi una uhakika kwamba mlimuua Yusufu?” The King aliuliza huku akianza kubadilika.
“Ndio. Tulimuua kwa kumchoma moto garini” Sudi alijibu huku akionekana kuwa na uhakika.
“Kweli?”
“Ndio”
“Sasa mbona hizi tetesi zinanichanganya sana. Nyie mliniambia mmemuua, ila tetesi zinasema kwamba yupo hai” The King alimwambia.
“Hizo ni tetesi tu na wala hautakiwi kukubaliana nazo. Kila siku tetesi zitazungumzwa sana lakini naomba uniamini kwamba Yusufu aliuawa, tena mbele ya macho yangu. Mimi ndiye niliwasha kiberiti na kulichoma moto gari lile” Sudi alijibu.
“Una uhakika?”
“Asilimia mia tatu”
“Usinidanganye Sudi. Naomba usinidanganye kabisa. Niliwalipa kiasi cha shilingi milioni kumi kwa ajili ya kukamilisha kazi yangu. Kitu mlichokifanya, kazi yangu hamkunifanyia” The King alimwambia.
“Hapana. Kazi tuliifanya”
“Hamkuifanya....” The King alimwambia Sudi kwa sauti ya juu iliyokuwa na ukali na kuendelea.
“Taarifa ya habari ya usiku imemuonyesha Yusufu akiwa hai kabisa. Yaani anaongea huku akiwa hana hata wasiwasi. Amehojiwa leo mchana na taarifa ya habari kuonyeshwa saa mbili. Yaani ni mzima kabisa, hana hata jeraha mwilini mwake” The King alimwambia Sudi ambaye akaonekana kushtuka.
“Unasemaje?”
“Ndio hivyo. Amehojiwa leo hii. Tena mbaya zaidi, amekisema kitu ambacho kimeonekana kuniumiza sana. Yaani mmemuacha hai kwa kuwa tu aliwalipa milioni kumi na tano. Huu ni ujinga. Kama mliona kwamba mna uhitaji wa fedha zaidu kwa nini hamkuniambia niwaongezee ili kazi yangu ifanyike?” The King aliuliza.
“Hapana. Sikubaliani na hilo. Yusufu tulimuua kwa kumchoma moto garini” Sudi aling’ang’ania.
“Nisikilize kwa makini. Yusufu hajafa. Nianachokitaka ni kuona anauawa ndani ya masaa arobaini na nane. Hapo namaanisha kwamba kwa siku mbili kila kitu kiwe kimekamilika. Mkijiona hamuwezi, nipeni fedha zangu niwatafute watu wengine ambao wataifanya kazi yangu. Umesikia?” The King alisema kwa hasira na kuuliza.
“Nimekusikia. Ila ninachoamini ni kwamba Yusufu tulimuua garini”
“Ikifika kesho, nunua magazeti halafu soma na kisha unipigie simu na kuniambia umeona nini. Ninachokitaka ni kwamba mtu huyu awe ameuawa ndani ya masaa arobaini na nane” The King alisema kwa hasira na kumruhusu Sudi kuondoka mahali hapo.
****
Kutokana na umaarufu mkubwa ambao alikuwa nao pamoja na kuingiza fedha kila siku, wasichana wakaonekana kuchanganyikiwa na vitu hivyo. Hapo ndipo fujo za kumtafuta Yusufu zilipoanza rasmi. Wasichana wengi walitamani kuwa na Yusufu ambaye alionekana kuwa bize sana na kazi ya muziki.
Wasichana wakaanza kujaribu bahati zao. Akili ya Yusufu ikafunguka, akakumbuka maisha yake ya nyuma ambayo alikuwa akiishi, alikumbuka vilivyo namna ambavyo alivyokuwa akikataliwa na wasichana kutoka na hali ambayo alikuwa nayo. Kwa kipindi hicho, aliona kwamba muda huo ndio ulikuwa muda wenyewe.
Yusufu hakutaka kuwapuuzia wasichana hao, alichokifanya kwa wakati huo ni kuanza kutembea na wasichana hao. Kwa kila msichana mrembo ambaye alikuwa akipita mbele yake, alikuwa akihakikisha anatembea nae. Yusufu akaonekana kuanza rasmi kazi ya kuwachukua wasichana ambao walionekana kuchanganyikiwa na fedha pamoja na umaarufu ambao alikuwa nao.
Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo alizidi kupendwa zaidi na zaidi. Kulala na wasichana ndio ikawa tabia yake. Kwa kila msichana ambaye alikuwa akionekana katika video zake ilikuwa ni lazima kutembea nae. Mvuto wake kwa watu haukupungua, kila siku alikuwa akizidi kunawiri na kuvutia zaidi.
Leo alikuwa akilala na msichana huyu na kesho alikuwa akilala na msichana mwingine. Kila msichana ambaye alifanikiwa kulala kitanda kimoja na Yusufu alikuwa akijisifia. Vyombo vya habari havikuwa mbali, vikaanza kuandika kuhusu tabia ile ya Yusufu ambayo alikuwa ameanza nayo. Yusufu hakuonekana kujali, alichokuwa akikijali kwa wakati huo ni ngono tu.
Mazoea ya kulala na wasichana mbalimbali kukajenga tabia. Tabia ile ikaonekana kuwa kubwa kiasi ambacho kilionekana kuwa kero hata kwa marafiki zake. Kama kuwapanga, katika kipindi hicho Yusufu aliwapanga kupita kawaida. Leo kulikuwa na habari kwamba alilala na Miss Kinondoni ila kesho analala na Miss Ilala.
Mamiss ndio ambao walikuwa wakimvutia kupita kawaida. Yusufu hakutaka wasichana wanene, wasichana wembamba ndio walikuwa na mvuto kwake. Aliwapanga kupita kawaida. Japokuwa alikuwa akitembea na wasichana wengi lakini kila alipofanya ngono, mipira ya Salama kondomu ilikuwa ikitumika kama kujilinda na magonjwa mbalimbali.
“Umezidi sasa” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Nimezidi na nini?” Yusufu aliuliza.
“Nyumba umeigeuza gesti”
“Sasa si wenyewe ndio wanataka. Wanazipenda fedha zangu, umaarufu wangu umewachanganya. Sasa kwa staili hiyo kwa nini nisiwapange?” Yusufu aliuliza huku akicheka.
“Kuwa makini bwana. Si unajua wasichana wenyewe hawaeleweki” Kelvin alimwambia Yusufu.
“Yeah! Nafahamu sana na ndio maana mara kwa mara nanunua maboksi ya mipira humu ndani” Yusufu alijibu.
Tabia ya Yusufu ikaonekana kuwa kero. Wazazi wakaanza kuja juu. Mabinti zao hawakuwa wakitulia kabisa, mara kwa mara walikuwa wakielekea katika matamasha ambayo Yusufu alikuwa akitumbuiza na mwisho wa siku kuanza kumpapatikia Yusufu ambaye kazi yake ilikuwa ile ile, kulala nao tu.
Kwa kila msichana ambaye aliambiwa kwamba alikuwa akiitwa na Yusufu wala hakugoma, alikuwa akienda na kumsikiliza. Jina lake likaonekana kumbeba, umaarufu wake ulionekana kuwachanganya wasichana, kila alipokuwa, Yusufu alionekana kunukia fedha, wasichana hawakumkataa kabisa, alikuwa akiendelea na kazi yake ya kulala nao kama kawaida.
Miezi ikakatika na ndipo kukawa na tamasha la walemavu ambalo lilikuwa likitarajiwa kufanyika katika uwanja mkubwa wa mpira wa Panama uliokuwa Bagamoyo. Kama kawaida, Yusufu akawa ameitwa huko kutumbuiza pamoja na wasanii wengine akiwepo The King ambaye alikuwa ameanza kusahaulika kabisa.
Siku moja kabla ya kwenda Bagamoyo Yusufu akahitajika kuzimu, sehemu ambayo alikuwa ameweka mkataba wa damu. Alipofika kule ndipo alipoambiwa kwamba sadaka ya damu ilikuwa ikihitajika kama kawaida, na damu hiyo ingetokana na watu ambao wangekwenda kuangalia tamasha lile.
Yusufu hakuonekana kuwa na wasiwasi, kitu ambacho alikuwa akikihitaji kwa wakati huo ni kulinda utajiri, mvuto na umaarufu ambao alikuwa nao. Siku hiyo damu nyingi zilikuwa zikihitajika na kwa sababu Yusufu alikuwa juu, wahudhuriaji wa tamasha lile wangekuwa wengi sana kwa sababu lilikuwa tamasha lisilokuwa na kiingilio chochote kile.
“Watu wengi watavutwa kwa ajili ya kuja kuangalia tamasha hilo” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
“Hakuna tatizo”
“Umeonekana kuwa mtu muhimu sana katika ulimwengu ule. Umekuwa kivutio sana kwa wakubwa wetu kiasi ambacho wamekuwa wakikutumia sana na kukuongezea vitu ulivyovihitaji zaidi na zaidi” Papaa Pipo alimwambia Yusufu.
Matangazo ya tamasha lile ambalo lilitarajiwa kufanyika likaanza kutangazwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari. Watu walionekana kama kuchangayikiwa, kitendo cha kutangazwa kwamba kumuona Yusufu akitumbuiza jukwaani ilikuwa bure ilionekana kuwa taarifa nzuri ambayo kila mtu alionekana kuifurahia.
Siku ya tamasha ilipofika, watu zaidi ya elfu kumi kutoka Dar es Salaam walikuwa wakielekea Bagamoyo kwa ajili ya kuhudhuria tamasha hilo. Hali ya hewa ya siku hiyo haikuonekana kuwa nzuri kwani tangu usiku uliopita mvua ya hapa na pale ilikuwa ikinyesha katika ukanda wote wa Pwani, hasa Dar es Salaam na Bagamoyo.
Watu hawakuonekana kujali, mvua ile ikaonekana kuwa si kitu kwao, kitu ambacho walikuwa wakikihitaji ni kumuona Yusufu tu. Magari yalikuwa yamejaza sana siku hiyo huku watu kutoka kwenye camp mbalimbali wakiwa wamekodi magari kwa ajili ya kuwapeleka Bagamoyo kumuona Yusufu ambaye alikuwa akitarajia kusafiri kuelekea nchini Uingereza kwa ajili ya kufanya shoo tatu kali katika jiji la Manchester.
“Hii shoo itakuwa kali sana. Jamaa namkubali hata zaidi ya ninavyomkubali Lil Wayne” Jamaa mmoja alimwambia mwenzake garini.
“Haunishindi mimi. Jamaa anajua sana. Yaani kama nyimbo zake zingekuwa za Kizungu halafu yupo Marekani. Hata uraisi wangempa bila kupenda. Hahahahaha” Jamaa mwingine aliongezea.

Je nini kitaendelea?
Tukutane kesho mahali hapa.
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 10

The King bado alionekana kuwa na hasira kupita kawaida, bado lengo lake kwa wakati huo lilikuwa ni kumuua Yusufu tu. Siku mbili ambazo alikuwa amewapa Sudi na wenzake zikapita lakini hakukuwa na taarifa zozote ambazo aliletewa zaidi ya kumuona Yusufu akizidi kutangazwa tu kwenye vyombo vya habari.
The King hakuonekana kukubali, akaanza kumpigia simu Sudi lakini simu haikuwa ikipatikana kabisa. Tayari Sudi na wenzake wakaonekana kumgeuka kwa wakati huo kwa kutofanya kile ambacho alitaka wakifanye. The King akaonekana kuwa na hasira kupita kawaida. Kitu ambacho akaamua kujiahidi kwa wakati huo ni kumuua Yusufu kwa mikono yake mwenyewe.
Siku zikakatika na hatimae kupigiwa simu kwamba nae alikuwa miongoni mwa wanamuziki ambao walikuwa wamechaguliwa kutumbuiza katika uwanja wa Panama mjini Bagamoyo katika siku ya walemavu duniani. Taarifa hiyo ikaonekana kuwa nzuri kwake, alichoamua siku hiyo ni kumuua Yusufu huko huko Bagamoyo.
Mara baada ya wasanii wote kulipwa nusu ya malipo yao wakatakiwa kujiandaa kuelekea Bagamoyo huku wakitumia usafiri mmoja kitu ambacho The King hakuonekana kukubaliana nacho.
Kwake, alijiona kuisaliti nafsi yake kama angetumia usafiri mmoja na aliokuwa akiutumia Yusufu. Alipotoa taarifa kwamba angetumia usafiri wake mwenyewe, kila mtu akaonekana kumshangaa ila hawakutaka kuyaingilia maamuzi yake.
Siku hiyo The King alikuwa akiendesha gari kwa kasi huku akionekana kuwa na hasira nyingi. Kichwani mwake, kwa wakati huo kulikuwa kukifikirika kitu kimoja tu, kumuua Yusufu mjini Bagamoyo.
Siku hiyo barabara haikuonekana kuwa nzuri hasa kwa magari ambayo yalikuwa kwenye kasi kubwa. Huku akionekana kutokujali, ghafla matairi ya gari lake yakaanza kuteleza na hatimae gari kupoteza muelekeo wake. Gari likaanza kuingia porini. The King alijitahidi kwa nguvu zake zote kulirudisha gari katika muelekeo sahihi lakini ikaonekana kushindikana kabisa.
Gari likaenda likazidi kwenda pembeni ya barabara zaidi na kuugonga mti mkubwa. Uzembe wake wa kutokufunga mkanda wa kiti ukamfanya The King kurushwa nje kupitia katika kioo cha mbele na kwenda kukibamiza kichwa chake katika mti ule. Kichwa chake kikapasuka, damu zikatapakaa pale mtini na mauti kumkuta hapo hapo.
Kama ilivyokuwa imepangwa ndivyo ambavyo ilivyotokea. Kutokana na mvua kunyesha sana, barabara ikaloa sana na idadi kubwa ya daladala zilizowabeba watu waliokuwa wakielekea kwenye tamasha lile kupata ajali. Zaidi ya watu elfu moja mia tano wakajikuta wakipoteza maisha katika ajali hizo idadi ambayo ilionekana kuwa kubwa sana kuwahi kutokea nchini Tanzania.
Damu nyingi ambazo zilikuwa zimemwagika zilionekana kuwa matunda ya mkataba wa damu ambao Yusufu alikuwa ameusaini. Wasanii walipofika mjini Bagamoyo, tamasha likafanyika kama kawaida. Taarifa za ajali ambazo zilikuwa zimetangazwa ndizo ambazo ziliinua vilio vikubwa mahali hapo.
Hilo likaonekana kuwa janga kubwa la Taifa. Idadi ya watu ambao walikufa kwenye ajali hiyo ilikuwa kubwa. Miili yao ilikuwa imeharibika sana kiasi ambacho hata watu wengine hawakuweza kufahamika kwa ndugu zao na hivyo kuzikwa katika kaburi moja. Katika kila kilichotokea, Yusufu alikuwa akikifahamu zaidi. Kifo cha mbaya wake, The King kikaonekana kumfurahisha.
Baada ya ajali hizo ambazo zilisababisha umwagaji mkubwa wa damu ndipo mafanikio ya Yusufu yakazidi kuongezeka zaidi na zaidi. Ingawa alikuwa amealikwa nchini Uingereza kwa ajili ya kufanya tamasha jijini Manchester hasa kwa watanzania ambao walikuwa wakiishi kule, majiji mengine kama Leicester, London, Birmingham na Liverpool wakahitaji kutaka kuzisikiliza nyimbo zake.
Mafanikio yake yakaonekana kutisha kupita kawaida. Wasichana wakazidi kumpenda na kuvutiwa nae. Kitu ambacho alikuwa akikifanya Yusufu ni kulala nao tu na kufanya nao ngono usiku kucha. Maisha yake yakawa ya kifahari sana. Mara baada ya kurudi kutoka nchini Uingereza, akanunua nyumba kubwa Mbezi Beach ambayo ilimgharimu zaidi ya shilingi milioni mia moja na hamsini na kisha kuibomoa na kutengeneza nyumba ambayo aliitaka yeye.
“Mmmh! Huyu jamaa kwa sasa anatisha. Na kuna tetesi zinasema kwamba anataka kununua ndege” Jamaa mmoja alisikika akiwaambia wenzake.
“Daah! Anaweza bwana. Jamaa anapata kiasi kikubwa cha fedha”
Hayo ndio yalikuwa matunda mazuri ambayo alikuwa akiyapata kutokana na mkataba ambao alikuwa ameuweka. Fedha zilizidi kumiminika katika akaunti yake, umaarufu ukawa mkubwa katika maisha yake, mvuto wa kupendwa ukazidi zaidi na zaidi mpaka pale alipoamua kutangaza kwamba alikuwa akitaka kuoa.
Habari ile ikaonekana kuwa njema. Watu wakawa na hamu ya kusikia ni msichana gani alikuwa akitaka kuolewa na Yusufu. Picha ya msichana ilipotolewa, alikuwa msichana mgeni machoni mwa watu wengi, msichana huyu aliitwa Samiah, msichana mzuri ambaye alikuwa na asili ya Kisomali.
“Anastahili” Watu wengi walisema mitaani na baada ya miezi miwili, harusi kufungwa huku Shekhe Omari Koba ndiye aliyefungisha ndoa hiyo katika nyumba yake iliyokuwa Mbezi Beach.
****
Maisha ya ndoa yakaanza pamoja na mke wake ambaye alikuwa akimpenda sana, Samiah. Watu walikuwa wakijiuliza maswali mengi juu ya uamuzi ambao alikuwa ameufanya wa kuoa mapema sana lakini jibu lake lilikuwa moja tu, kutengeneza familia yake katika kipindi hicho ambacho alikuwa katika mafanikio makubwa ya kimuziki nchini Tanzania.
Tabia yake ya kutembea na wasichana mbalimbali akawa amekwishaiacha, aliiheshimu sana ndoa yake pamoja na kumheshimu sana mke wake. Akili yake alikuwa ameituliza katika maisha ya ndoa katika kipindi hicho, kila kitu ambacho alikuwa akikifanya alikuwa akimshirikisha mke wake ambaye alikuwa akimpenda sana.
Hakuacha muziki, bado alikuwa akiendelea kuimba muziki kama kawaida yake, mapenzi ya mashabiki wake hayakupungua, kila siku idadi ya mashabiki ilizidi kuongezeka zaidi na zaidi. Mara kwa mara alikuwa akiitwa nje ya nchi kwa ajili ya kutumbuiza katika matamasha mbalimbali ambayo yalikuwa yakifanyika.
Jina lake likawa kubwa, katika kila kona ya Afrika Mashariki, Yusufu au The Ruler alikuwa akijulikana sana. Nyimbo zake zilikuwa katika chati za juu sana jambo ambalo likamfanya kupata mafanikio zaidi. Siku ziliendelea kukatika zaidi mpaka kufika kipindi kile cha ugawaji wa tuzo za muziki zilizojulikana kama Kisima kutarajiwa kufanyika nchini Kenya ndani ya jiji la Nairobi.
Kama kawaida yake, Yusufu alikuwa katika sehemu tano kama mtunzi bora wa muziki, mwanamuziki bora wa kiume, wimbo bora wa mwaka, wimbo bora wa kushirikiana na video bora ya mwaka. Mpaka siku ya ugawaji tuzo unafika, tayari Yusufu alikuwa amepigiwa kura na kuongoza katika vipengele vyote ambavyo alikuwa amechaguliwa.
Hayo yalionekana kuwa mafanikio makubwa katika kazi yake ya muziki, uamuzi ambao aliuchukua wa kuuza roho yake katika ulimwengu wa giza ndio ambao ulikuwa umempa mafanikio hayo yote. Umaarufu wake, utajiri wake ukawa mara nne zaidi ya vile alivyokuwa kabla.
Yusufu hakutaka kuchelewa sana, hapo ndipo alipoamua kufungua biashara mbalimbali, akaanzisha maduka yake makubwa ya nguo ambayo yalikuwa yakichukua nguo na viatu nchini Malaysia na kuvileta nchini Tanzania. Yusufu hakuishia hapo, bado aliendelea kufungua biashara nyingine nyingi kama supermarket na biashara nyingine.
Yusufu akazidi kutangazwa zaidi na zaidi kiasi ambacho mpaka akajiona kuukaribia umaarufu mkubwa kama waliokuwa nao wanamuziki wa Marekani. Kwa sababu alikuwa akijulikana sana katika kipindi hicho, akajikuta akichaguliwa kuwania tuzo kubwa kuliko zote Afrika, tuzo za Kora.
Kama kawaida alikuwa amechaguliwa katika vipengele vichache na akafanikiwa kuwa msanii bora wa kiume barani Afrika katika kipindi hicho. Yusufu akaona kumaliza kila kitu japokuwa kulikuwa na vitu vingi sana mbele yake. Tanzania ikajivunia, Yusufu akaonekana kuwa lulu zaidi ya wanamuziki wote wa Tanzania.
Hapo ndipo maisha ya majigambo yalipoanza rasmi. Yusufu akaanza kubadilika, tayari alijiona kuwa juu zaidi ya wanamuziki wote wa Kitanzania. Akaanza kuhitaji malipo makubwa katika shoo zake mbalimbali ambazo alikuwa akizifanya. Mapromota wengi walikasirika lakini hawakuwa na jinsi, kwa sababu walikuwa wakitaka fedha, walipaswa kumuita Yusufu katika matamasha yao.
“Tupange familia yetu” Samiah alimwambia Yusufu katika kipindi ambacho alikuwa ametulia nyumbani.
“Familia! Mbona kila kitu kipo sawa. Au ulikuwa unamaanisha nini mke wangu?” Yusufu alimuuliza Samiah.
“Kuwa na watoto wetu. Nyumba imekuwa kubwa sana na ukimya umetawala” Samiah alimwambia Yusufu ambaye kwa mbali akaonekana kushtuka.
Tayari kumbukumbu zake zikarudi nyumba kabisa mpaka katika siku ile ambayo alikuwa amesaini mkataba wa damu wa kuiuza roho yake katika ulimwengu wa giza. Alikumbuka vilivyo sharti ambalo alikuwa amepewa katika kipindi ambacho alihitaji utajiri na mvuto. Hakutakiwa kupata mtoto katika maisha yake yote na kama angekwenda kinyume angeweza kuuawa au kupewa adhabu yoyote ile.
“Unasemaje?” Yusufu aliuliza kana kwamba hakusikia vizuri.
“Nahitaji watoto mume wangu” Samiah alimwambia Yusufu kwa sauti ya chini iliyoja upole.
“Haiwezekani kwa sasa” Yusufu alijibu.
“Kwa nini?”
“Fahamu kwamba haiwezekani mpenzi, kuna vitu navirekebisha kwanza” Yusufu alimwambia mke wake, Samiah.
Siku hiyo kukaonekana kutokuwa na maelewano, kila mtu kwa wakati huo alikuwa akitaka kitu chake. Samiah bado alikuwa aking’ang’ania uamuzi ule ule ambao alikuwa amejiwekea kwamba alikuwa akihitaji kuwa na watoto lakini akaonekana kutokuelewa kabisa.
Kutokana na kuonekana kukasirishwa siku hiyo, Yusufu hakutaka kulala nyumbani hapo, alichokifanya ni kwenda katika hoteli ya Serena na kisha kupumzika huko. Kichwa chake kilikuwa na mawazo mengi, hakujua ni kitu gani ambacho alitakiwa kukifanya kwa wakati huo.
Si kwamba Yusufu hakutaka kuwa na mtoto, alikuwa akitamani sana jambo hilo kutokea lakini masharti ambayo alikuwa amepewa yalionekana kumkosesha raha, kamwe asingeweza kuwa na mtoto kwani kwa kufanya hivyo aliogopa kupewa adhabu kali na hata kupokonywa vile ambavyo alikuwa navyo katika kipindi hicho.
Siku ziliendelea kukatika kama kawaida. Samiah hakuonekana kukubali kabisa, katika kipindi hicho alikuwa akihitaji kitu kimoja tu katika maisha yake, kuwa na mtoto. Hakujua angeweza vipi kumlaghai mume wake ambaye alionekana kuwa mkali katika kila kipindi ambacho alikuwa akizungumzia kuhusiana na wao kupata mtoto.
Samiah hakutaka kuona hali ile ikiendelea zaidi, kitu ambacho alikuwa akikihitaji kwa wakati huo ni kupata mtoto tu. Alichokifanya ni kuziangalia siku zake na kisha kuanza kupiga hesabu kichwani mwake. Akazijua siku zake vilivyo ila kitu ambacho alitaka kumficha mume wake katika kipindi hicho ni tarehe zake za kuingia mwezini.
Jambo hilo likaonekana kufaulu, katika siku ambayo Samiah alijua fika kwamba angeweza kupata mimba kama angefanya mapenzi na ndio siku hiyo ambayo akafanya mapenzi na mume wake. Kitendo kile kilimpa furaha sana Samiah pasipo kujua kwamba kilikuwa ni kitendo kimoja ambacho kilikuwa ni cha hatari sana katika maisha ya mume wake, Yusufu.
Kuanzia hapo kila siku alikuwa akilishika tumbo lake huku akitabasamu. Tayari katika kipindi hicho Samiah akajiona kuwa mshindi zaidi ya washindi, kitendo alichokifanya cha kufanya mapenzi na mume wake, Yusufu katika tarehe ya hatari ya kupata mimba ikaonekana kumfurahisha kupita kawaida.
Yusufu hakujua kitu chochote kile, hakujua kama kipindi hicho mbegu zake zilikuwa zimekwenda katika yai la uzazi la mke wake, Samiah na kuanza kutengeneza kiumbe. Samiah hakutaka tena kuzungumzia suala la kutaka mtoto kwani katika kipindi hicho alijua fika kwamba ilikuwa ni lazima kupata mtoto wake mwenyewe.
Siku zikaendelea kukatika mpaka kufika siku zile ambazo Samiah akaanza kutapika na kusikia kichefu chefu hali iliyoonyesha kwamba mambo yalikuwa yamekaa sawa. Yusufu alipogundua hali ile akaonekana kuogopa kupita kiasi, alikuwa akimwangalia mke wake kwa wasiwasi mkubwa kwamba tayari alikuwa mjauzito.
“Vipi tena? Mbona unatapika hovyo?” Yusufu alimuuliza Samiah huku akionekana kuwa na wasiwasi.
“Nahisi Homa” Samiaha alidanganya.
Yusufu hakupenda kumuona mke wake akiwa katika hali hiyo, alichokifanya ni kumpeleka hospitali na kisha kupatiwa matibabu. Hali haikubadilika, bado ilikuwa ikiendelea vile vile mpaka pale ambapo tumbo la Samiah lilipoanza kuwa kubwa. Muonekano wa tumbo lake ukaonekana kumuogopesha zaidi Yusufu ambaye alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa.
“Mmmmh! Sio mimba hii?” Yusufu alimuuliza Samiah huku wasiwasi ukiongezeka zaidi.
“Ndio yenyewe” Samiah alijibu huku akitabasamu.
“Mimba ya nani?” Yusufu aliuliza.
“Mimba yako” Samiah alitoa jibu lililoonekana kumchanganya sana Yusufu.


Je nini kitaendelea?
Je Yusufu atapewa adhabu au kupokonywa kila alichopewa?
Je Samiah atajifungua mtoto salama?
Itaendelea.
 
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI.
MAHALI: DAR ES SALAAM.
SIMU: 0718 069 269.

NITAKAPOKUFA 11

Malumbano makali yalikuwa yakisikika kutoka ndani ya nyumba ya Yusufu. Muda wote Yusufu alikuwa akimlalamikia mke wake, Samiah kwa kitendo kile cha kuruhusu kupata ujauzito ule. Yusufu alionekana kukasirika sana huku wakati mwingine akitetemeka mwili mzima na kijasho chembamba kumtoka.
Tayari alijua kwamba mwisho wa maisha yake ulikuwa umefika kwa sababu alikuwa njiani kuvunja moja ya masharti ambayo alikuwa amepewa katika ulimwengu ule wa giza. Moyoni akakosa raha, kila alipokuwa akimwangalia mke wake, Samiah alionekana kukasirika zaidi. Unyonge ukaanza kuingia katika maisha yake, kichwa chake kilikuwa kikifikiria zaidi kupokonywa umaarufu, utajiri na kila kitu ambacho alikuwa nacho.
Ndani ya wiki nzima, Yusufu hakutaka kulala nyumbani, alikuwa akishinda hotelini tu akilala. Hakutaka kufanya shoo yoyote ile kwa sababu hakuwa katika hali nzuri hata mara moja. Alijiona kuwa na uhitaji wa kukaa mbali na mke wake, kwa jinsi alivyokuwa na hasira nae katika kipindi hicho, alijiona kama angeweza kumuua muda wowote ule.
“Huyu mwanamke kwa nini ameamua kunifanyia hivi?” Yusufu alijiuliza huku akiuma meno yake yake kwa hasira.
Kulala hotelini akaona kutokusaidia, kitendo cha mke wake kumpigia simu pamoja na kumtumia meseji nyingi mara kwa mara kukaonekana kumuudhi sana kitu ambacho akaamua kuondoka nchini Tanzania na kuelekea Afrika Kusini kwa ajili ya mapumziko ya muda fulani hata kabla hajajua nini kingetokea mbeleni.
Kwa Samiah mambo yalikuwa hivyo hivyo, hakuonekana kuwa na raha hata kidogo, kitendo cha mume wake kuondoka na kuelekea pasipojulikana kulionekana kumuumiza kupita kawaida. Muda mwingi alikuwa akimpigia simu na hata kumwandikia meseji lakini hali haikuonekana kubadilika.
Alikuwa akimpigia sana simu lakini haikuwa ikipokelewa, alipiga kwa zaidi ya mara hamsini kwa siku lakini hali ilionekana kuwa ile ile, simu haikupokelewa kabisa na baada ya siku kadhaa, simu haikuwa ikipatikana. Alichokifanya Samiah ni kuanza kumtumia meseji lakini hali napo ilionekana kuwa pale pale, meseji hazikuwa zikijibiwa kabisa.
Yalikuwa ni maumivu makubwa moyoni mwake, maumivu ambayo wala hayakuelezeka hata kidogo. Kitendo cha mume wake kumfanyia mambo yote yale kilionekana kumuumiza sana. Alichokifanya Samiah ni kuchukua gari lake na kisha kuelekea mpaka Bagammoyo na kisha kuwaeleza wakwe zake juu ya kile ambacho kilikuwa kinaendelea nyumbani kwake.
Mzee Kessi na mkewe, Bi Fatuma hawakuonekana kumuelewa kabisa Samiah kwamba ingewezekana kwa Yusufu kufanya mambo yale kisa kilikuwa ni ujauzito, walichokifanya ni kuanza kumpigia simu. Kama ilivyotokea kwa Samiah ndivyo ambavyo ilitokea kwa wazazi hao pia, simu haikupatikana kabisa.
Kila mmoja alionekana kutokuamini kile ambacho kilikuwa kimetokea, hawakujua mahali ambapo Yusufu alipokuwa kwa kipindi hicho, wasiwasi ukaanza kuwashika, hatua waliyoichukua kwa kipindi hicho ni kumpigia simu rafiki mkubwa wa Yusufu, Kelvin. Majibu yaliyotoka kwa Kwelvin yakawachanganya zaidi.
“Sijamuona kwa siku mbili sasa kitu ambacho si kawaida kabisa” Kelvin aliwaambia.
“Hebu jaribu kuwapigia marafiki zake wa karibu na kuwauliza kuhusu mahali alipokuwa kwa sasa” Mzee Kessi alimwambia Kelvin ambaye alifanya kama alivyoambiwa.
Wote wakakaa kwa dakika kadhaa huku wakiisubiria simu ya Kelvin ambayo ingewaambia ni mahali gani alipokuwa Yusufu katika kipindi hicho. Walibaki wakiisubiria simu ile kwa dakika zaidi ya ishirini, simu ikaanza kuingia, alikuwa Kelvin.
“Yupo wapi?” Mzee Kessi aliuliza.
“Nimejaribu kuwapigia watu wengi lakini wote wanasema hawajui alipo” Kelvin alijibu.
Kila mmoja alionekana kuchanganyikiwa zaidi, hawakuamini kama Yusufu angeweza kufanya jambo kama lile la kuondoka nyumbani na kuelekea katika sehemu isiyojulikana. Samiah alikaa Bagamoyo kwa muda wa siku mbili na ndipo alipoamua kurudi jijini Dar es Salaam na kupanga kuelekea Dodoma kwa wazazi wake.
Katika kipindi hicho hali ikaonekana kuwa vile vile, kila walipokuwa wakijaribu kumpigia simu Yusufu, simu haikuwa ikipatikana kabisa. Hali ilizidi kuwa mbaya kwa Samiah kiasi ambacho muda mwingi alikuwa akijutia uamuzi wake uliompelekea wa kupata ujauzito na wakati mume wake, Yusufu alikuwa amekataa kuhusiana na jambo hilo.
Mawazo juu ya mume wake ndio ambayo yalimpelekea kutokula kabisa, moyo wake ulikuwa ukimkumbuka sana mume wake, Yusufu. Hakujua ni mahali gani ambako alitakiwa kumtafuta kwa kipindi hicho. Mara kwa mara alikuwa akipigiwa simu na marafiki wa karibu wa Yusufu wakimtaka kumtaarifu ni mahali Yusufu alipokuwa lakini hakuwa na cha kuwajibu.
Kuondoka kwa Yusufu nyumbani kukaanza kusikika masikioni mwa watu, watu wakaanza kushangaa jambo ambalo liliwapelekea waandishi wa habari kufika nyumbani hapo na kisha kuanza kuongea na Samiah ambaye muda mwingi alionekana kuwa na majonzi mengi usoni.
“Kwa hiyo hakukuaga?” Mwandishi wa habari, Penina alimuuliza Samiah.
“Hakuniaga”
“Kwa nini?”
“Sijui kwa nini”
“Au mligombana?”
“Hapana”
“Sasa tatizo nini?”
“Hata mimi sifahamu” Samiaha alificha.
Magazeti yakaanza kuandika kuhusiana na Yusufu kwamba alikuwa ameondoka nyumbani kwake na kwenda kusipojulikana. Kwa kila mtu ambaye aliiona taarifa ile ilionekana kumshtua, tayari wakaanza kujua kwamba kuna kitu kilikuwa kimetokea nyuma ya pazia ambacho wala hawakutakiwa kukifahamu.
****
Ulikatika mwezi mmoja na ndipo Yusufu aliporudi nchini Tanzania akitokea nchini Afrika Kusini. Mara baada ya kupata taarifa kwamba Yusufu alikuwa amerudi nyumbani, waandishi wa habari wakaanza kufika nyumbani kwake na kisha kuanza kufanya mahojiano pamoja nae. Kwa kila kitu ambacho alikuwa akiongea Yusufu mahali hapo alionekana dhahiri kuficha kitu fulani moyoni mwake.
Yusufu hakuwa muwazi, kila alipokuwa akiulizwa hili, alijibu lile tena kwa maelezo mengi ambayo yaliwafanya waandishi wa habari kutokumuelewa kabisa. Hakuonekana kama alikuwa radhi kufanyia mahojiano katika kipindi hicho kitu ambacho kiliwafanya waandishi hao kuondoka nyumbani kwake.
Uamuzi ambao alikuwa ameupanga Yusufu mahali hapo ni kumpa talaka Samiah. Hilo lilionekana kuwa tukio kubwa na baya kutokea katika maisha ya Samiah ila hakuwa na jinsi, akaondoka nyumbani hapo na kuelekea nyumbani kwa wazazi wake waliokuwa wakiishi Dodoma.
Taarifa ya kuachwa kwa Samiah ndio ambayo ilionekana kutawala sana katika vyombo vya habari, kila mtu alikuwa akijiuliza sababu lakini hakukuwa na mtu aliyeweza kufahamu kitu chochote kile. Katika kipindi hicho Yusufu akaonekana kuwa mkali kwa kila mwandishi wa habari ambaye alikuwa akitaka kufahamu kile ambacho kilitokea katika maisha yake ya ndoa mpaka kuamua kumpa talaka mke wake, Samiah.
“Ni mambo ya watu wawili kati yangu na Samiah, sidhani kama ninyi mnatakiwa kufahamu” Yusufu aliwaambia waandishi wa habari kwa sauti iliyoonyesha kwamba alikuwa na hasira.
“Lakini sisi kama waandishi naona kuna umuhimu mkubwa wa kufahamu hilo. Watu wengi wanahoji juu ya hilo” Mwandishi Rebecca alimwambia Yusufu.
“Mmekosa cha kuandika au mmekosa wa kumhoji?” Yusufu aliwauliza huku hasira zake zikiongezeka zaidi.
“Punguza hasira Yusufu”
“Nimewaambieni kwamba jambo hili ni la watu wawili tu kati yangu na mke wangu, ninyi mnang’ang’ania nini sasa? Mlitaka niendelee kuwa nae? Acheni upuuzi wenu huko, kwanza tokeni ndani ya nyumba yangu” Yusufu aliwaambia waandishi wale wa habari.
Waandishi hawakutaka kuondoka, kitu ambacho walikuwa wakikitaka mahali hapo ni kufahamu ni kitu gani ambacho kilikuwa kimetokea katika maisha ya Yusufu mpaka kuamua kumpa talaka Samiah ambaye alionekana kuwa mjauzito. Alichokifanya Yusufu mahali hapo ni kuelekea ndani ya nyumba yake na kutulia.
Yusufu alikaa katika hali ya mawazo mengi kupita kawaida, kwa wakati huo alijua fika kwamba alikuwa njiani kupoteza kila kitu ambacho alikuwa nacho katika kipindi hicho. Kama Samiah angejifungua salama basi mvuto wake kwa mashabiki wake ungetoweka kabisa, utajiri wake ungetoka kabisa na hivyo kurudi katika hali yake kama zamani.
Usiku ulipoingia, Yusufu akaamua kumfuata mtu ambaye alikuwa kila sababu zilizomfanya kuingia katika mkataba wa damu na ulimwengu wa giza, Papaa Pipo. Alilipaki gari lake katika uwanja wa nyumba ya Papaa Pipo, akateremka na kuanza kuelekea ndani ya nyumba hiyo na kutulia sebuleni ambapo baada ya muda Papaa Pipo akatokea mahali hapo.
“Kwa nini ulitoweka ghafla? Ulikwenda wapi rafiki yangu?” Papaa Pipo alimuuliza.
“Afrika Kusini” Yusufu alijibu.
“Mbona ghafla sana na wala haukuniaga?”
“Ilikuwa ni safari ya ghafla sana. Si wewe tu, hata mke wangu na wazazi wangu sikuwaaga” Yusufu alimwambia Papaa Pipo.
“Kwa nini sasa uliamua kufanya hivi?”
“Mawazo. Yaani naona kila kitu kitakwenda kuharibika hapo mbeleni” Yusufu alimwambia Papaa Pipo.
“Kwani kuna nini kimetokea?”
“Nimevunja masharti” Yusufu alimwambia Papaa Pipo.
“Unasemaje? Umevunja masharti?”
“Ndio. Mke wangu kapata ujauzito” Yusufu alitoa jibu lililoonekana kumchanganya Papaa Pipo.
Papaa Pipo hakuongea kitu chochote kile, alibaki kimya huku akiangalia juu. Kichwa chake kwa wakati huo kikaonekana kuanza kufikiria mambo mengi, baada ya muda wa sekunde kadhaa akayapeleka macho yake usoni mwa Yusufu ambaye alionekana kuwa mwingi wa mawazo.
“Sasa kwa nini uliamua kuvunja masharti?”
“Tatizo mke wangu. Mke wangu ndiye aliyenichezea mchezo huu” Yusufu alijibu.
“Pole sana ndugu yangu”
“Asante sana. Yaani sijui itakuwaje. Akili yangu imechanganyikiwa kabisa” Yusufu alimwambia Papaa Pipo.


Je nini kitaendelea?
Je Yusufu ataweza kuadhibiwa?
Je nini hatma ya kila kitu?
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…