Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,809
- 15,421
Nilikuwa naishi katika nyumba hii......................
Nilikutana na dhahma hii miaka kumi iliyopita kabla sijamuoa mama Ngina. Nilikuwa najisikia vibaya sana jioni ile, kuanzia kwenye saa kumi hivi nilikuwa nahisi kuumwa na kichwa. Baadae hali ilikuwa ya mchanganyiko , yaani kichwa na kuvurugika kwa tumbo . mpaka kufika kwenye saa kumi na mbili jioni, nilikuwa nahisi kichefuchefu. Nilivumilia kwa muda chumbani kwangu, huku nikifikiria kwenye hospitalini, au kutafuta dawa, hata panado ili nipunguze maumivu ya kichwa. Hatimaye nilizidiwa na kichefuchefu, nilitoka nje ili kama ni kutapika nitapikie nje .
Nilipotoka nilienda moja kwa moja kando ya choo na bafu ya nyumba nilimokuwa naishi. Choo kilikuwa kimejengwa na tope na kuezekwa kwa bati bovubovu, lakini bafu ilikuwa imejengwa kwa makuti naamini wengi mnafahamu nyumba za uswahilini zilivyo na aina ya vyoo vinavyotumika. Wakati huo nilikuwa naishi Mwanayamala Kwa Ali Manjunju. Nilikaa kando ya kibanda hicho cha bafu. Huko ndani kulikuwa na mpangaji mwenzangu ambaye alikuwa akioga, lakini sikujua kama alikuwa ni nani. Wakati nikiwa nimekaa hapo nikijaribu kuvuta matapishi, nilihisi nikiguswa begani. Nilipoinua macho, niliona watu kibao wakiwa wamenizunguka.
"Hatimaye tumekunasa. Tulikuwa tunajiuliza aliyetoboa kitobo hapa bafuni ni nani……. Kumbe ni wewe mshenzi." Mmoja kati ya wale watu walionizunguka alisema. Nilishikwa na butwaa. Watu wale ambao miongini mwao wapangaji wenzangu walikuwa watano na jirani wengine kadhaa walianza kunitukana na kunitia masingi kisogoni…….. "Mwanaizaya we, umezoea, ndio maana hutaki kuoa. Kazi yako kupiga chabo tu………" alisema mwanamke mmoja mwenye kidomo domo na anayejua kusema mpaka midomo imempinda kwa kubeza watu. Kama mjuavyo mambo ya uswahilini, washabiki walizomea na watu wakaongezeka ili kujua kulikoni.
Kutapika kulinijia na nilianza kutapika. Watu wale walinyamaza kimya kwa muda. Nilitapika sana. Nilipomaliza nilirudi ndani kwa kuchechemea. Baadhi ya watu wale walinyamaza, lakini wengine waliendelea kunizonga wakisema najitapisha ili kuuwa soo. Kumbe wapangaji wenzangu ambao wote walikuwa wameoa, isipokuwa mimi, walibaini kwamba, kulikuwa na tundu limetobolewa ambapo kulikuwa na mtu anawapiga chabo wake zao wakioga. Kwa sababau nilikuwa sijaoa waliamini kwamba mtu huyo angekuwa ni mimi. Siku hiyo waliniwekea mtego.
Hata hivyo wakati nikiwa ndani nikiugulia, mke wa mpangaji mmoja alisema… "Mnamuonea bure tu kijana wa watu, anayepiga chabo yuko miongoni mwenu , mwenyewe nimeshawahi kumuona si chini ya mara mbili…." Watu walipiga kelele wakitaka amtaje. …..
Ni kweli alimtaja lakini wakati huo alishakimbia baada ya kusikia mama yule alidai alishawahi kumuona mara mbili akipiga chabo. Lakini kutajwa kwa huyo jamaa kulizusha zogo kwani mkewe alikuwepo na alisimama kidete kumtetea mumewe, na kila mmoja akawa anasema lake…………………………
Nilitoka na kuelekea hospitalini, na wiki mbili baada ya kupona nilihama katika nyumba ile.