GAZETI
JF-Expert Member
- Feb 24, 2011
- 5,286
- 6,736
WANASUBIRI HUKUMU.
Nilikuwa nimetulia sebuleni nikiangalia TV. Nilikuwa mpweke kiasi kwani wanangu na wajukuu zangu wote walikuwa Ulaya wakiendelea na masomo. Mjomba'ngu mzee Kajisi yeye nilikuwa nimempeleka London akatibiwe kwani alinieleza kuwa anasumbuliwa na mafua. Hata hivyo nilipanga kumpeleka kwa babu mmoja huko Arusha kwa ndege ya kukodi kama tiba ya kule London ingeshindikana. Mke wangu alikuwa ameteuliwa kwenye viti maalum Vijana ingawa umri wake ulikuwa umemtupa mkono. Nashukuru sana teknolojia ya Mchina kuingia hapa nchini kwani mke wangu alikuwa na umri wa miaka 55 lakini aliweza kupunguza miaka 20 kutoka kwenye umri wake halisi. Nilimuomba Muheshimiwa afanye kila linalowezekana ampe hiyo nafasi, angekataa vipi wakati tumesoma wote shule moja?
Mbele yangu mezani kulikuwa na makabrasha ya kampuni zangu tofauti ambazo zinaonyesha kuwa ni za wamiliki tofauti. Sikuwa peke yangu kwenye kampuni hizi. Nusu ya baraza la mawaziri na Makatibu wakuu wa wizara mbalimbali ilikuwa inahusika. Migao iliyopita ilikuwa minono sana. Mgao mmoja tu unaweza kukufanya uishi nchi yoyote unayotaka duniani katika umri wako wote. Halafu sote tulikuwa na uraia wa nchi mbili. Migao minono ambayo siwezi kuisahau ni mgao wa kampuni ya umeme, huu ulikuwa mnono sana kwani umeniwezesha kununua nyumba tatu huko ulaya. Ila kuna mgao ambao ni kiboko! Madini, ule hauna mfano kabisaaa! Dah, ule mgao unafurahisha sana maana kule Shinyanga tumeacha mashimo tu, Kule Arusha nako mh! Na bado nchi itabaki mashimomashimo sisi twaenda kuishi ulayaaaa! Tuna wasiwasi gani? si tuna uraia wa nchi mbili. Halafu Muheshimiwa namsifu ana akili sana. Tunachukua madini wao tunawaletea chandarua! Tena ili gharama isiwe kubwa zaidi tunawaletea zile ndogondogo, Watajua wenyewe sisi haituhusu maana nasikia wengine wanalalia vitanda vya kamba, Eti wanalalamika mbu wanapenya kule chini, Si waweke mikeka? Watanzania bwana kwa uvivu wa kufikiri
Pia kuna ule mradi wa kuingiza NGAO feki, sio ngao za kivita ni zile za kuua mbu. Mwanzo tulileta ngao nzuri sana, tena ukifulia ukamwaga chooni hata mende wanakufa. Ile ngao ilikuwa inahatarisha Miradi yetu. Ingefikia muda ambao asingeonekana mgonjwa wa Maleria, TUNGEKULA WAPI?. Kwetu MBU Ni kiumbe muhimu sana na tunamuheshimu tofauti na unavyofikiri. Pia hatupendi na wala hatutaki kusikia eti dawa ya ukimwi imepatikana! Hiyo itakuwa mbaya sana maana vyanzo vya mapato vitapungua. Wakati naendelea kuwaza nikashikwa na usingizi.
Ghafla, nikasikia kishindo na mtetemeko mkubwa sana! Vitu vikaanza kuanguka hovyo pale sebuleni. Wakati niko pale sebuleni nilikuwa nimevaa msuli. Nikakurupuka na kukimbilia nje. Msuli ukafunguka, nikabaki na nguo ya ndani tu. Huko nje kila mmoja alikuwa anakimbilia upande wake. Wengine walikuwa kama walivyozaliwa bila shaka ni wale waliokuwa wanaoga au katika harakati za kuongeza familia. Jirani na nyumba yangu kulikuwa na Guest kubwa na inayoheshimika. Kama huna lakini 2 ulikuwa huwezi kupata chumba humo. Nilishangaa kuona baadhi ya viongozi waandamizi wa chama tawala wakitoka humo kama walivyozaliwa. Wanne kati yao walikuwa ni mawaziri kamili kutoka wizara zinazoheshimika sana. Kuna wanawake kadhaa nao walitoka kama walivyozaliwa, wawili walikuwa wakuu wa wilaya. Hakuna aliyekuwa na muda wa kujua kwanini mtu katoka katika hali hiyo kulingana na wadhifa wake. Ukweli ni kwamba kila mtu alikuwa katika hali inayomtosha mwenyewe. Wakati naendelea kukimbia nikashangaa kumuona muheshimiwa sana naye akikimbia, sina uhakika alikuwa ametokea jengo gani pale ingawa alikuwa amevaa nguo ya ndani tu. Sijui kama alikuwa ameshaoga ndo akaanza kuvaa au alikuwa anataka kuvua ili aoge! Lakini kwanini aje kuoga huku wakati ana nyumba yake? Tena si mbali sana kwa gari.
Vishindo vikaongezeka hatimaye nuru ya kawaida ya jua ikapotea. Upepo ukawa mkali sana ukaanza kuvuma, nilipogeuka nikashangaa kuona nyumba yangu ikiwa imebaki kuwa gofu, nyumba nyingi zilikuwa zimebomolewa kwa mtikisiko ule. Huu upepo uliokuja ukaanza kuvunja nyumba zilizobaki. Ulipoanza upepo taharuki ikazidi, hakuna aliyeweza kumtambua mwenzake tena. Nikapata wazo, kuna mtaalamu mmoja wa mambo ya utabiri alikuwa anakaa kule kule nilikokuwa nakimbilia, nikaona bora nimfuate yeye labda atanisaidia. Nilipofika nikashangaa kukuta jengo lake limesambaratishwa. Ina nini hii ardhi leo? nilijiuliza bila shaka na watu wengine walijiuliza.
Ikaanza kunyesha mvua kubwa na ya kutisha. Hatimaye mwanga ukapotea kabisa, kiza kikatawala. Sikukumbuka tena hati zangu za Mikataba feki, nilizoziacha mezani, sikumkumbuka mke wangu aliyeko kule bungeni, sikukumbuka hata wanangu kule ulaya. Kiza, kiza, kiza kizito kikatawala, dunia ikatawaliwa na kiza nyoyo nazo zikatawaliwa na kiza.
Hatimaye nikaanguka. Sikukumbuka kitu baada ya hapo mpaka nilipozinduka. Nikashangaa kugundua kuwa kumbe wote tulikuwa tumeanguka. Hatimaye tukaamka. Tulikuwa kwenye ardhi mpya ambayo haikuwa na jengo wala chochote kilichojengwa na binadamu. Bila shaka Mataifa yote yalikuwa yamekusanyika hapa. Halafu tulikuwa tumegawanywa kulingana na mataifa yetu. Na kila Taifa lilikuwa limegawanywa kulingana na watu wake. Mh! Bila shaka hii ndio siku ya hukumu tuliyokuwa tunaelezwa. Nilishangaa kuwaona Marais wakubwa hapa duniani ambao walikuwa na hadhi na heshima kubwa hapa wakiwa dhalili kabisa. Hapa kulikuwa na watu wa aina mbalimbali. Kama ingekuwa ni siku ya kucheka ningecheka sana lakini haikuwezekana kwani nilivuta kumbukumbu za makosa yangu nikajua sitasalimika.
Sauti kubwa ikasikika "Enyi wanadamu, hii ndio siku ya hukumu ambayo hamkutaka kuiamini. Je, mlidhani tutawaacha milele duniani mfanye mpendavyo. Jueni kwamba leo Ufalme umebaki kwa mfale Mkuu, mfalme wa wafalme. Wako wapi leo wafalme, wako wapi leo MAFISADI, Waliokuwa wanawakandamiza wenzao kwa peni na karatasi. Basi tambueni leo mutakandamizwa kwa marungu na mawe ya motoni. Huku ndiko kwenye haki, hakuna rushwa wala umaarufu. Tutamuhukumu kila mmoja kulingana na matendo yake. Tutaanza nchi moja kisha itafuata nyingine."
Kelele ni jambo la kawaida kwenye mkusanyiko wa aina hii lakini hapa tulikuwa kimya kabisa. Nilipotazama kulia nikashangaa kumuona marehemu mama yangu mzazi, nikaanza kuwaona watu wengi ambao walikufa siku nyingi sana. Nikashangaa kumuona Gamba Kisago mchezaji wa zamani wa yannga ambaye alifia uwanjani. Ikatajwa nchi ya kwanza hapa nimesahau sijui ilikuwa nchi gani vile. Hukumu ikaanza.
Akaanza raisi wa nchi yao. Akaanza kusomewa mashitaka yake."......... Hukujali kilio cha wananchi wako uliwatesa......" Baada ya kumaliza tukashuhudia yule Raisi akifungwa minyororo na kutupwa katika moto. Niliogopa sana. Akafuata waziri wa Afya. "......Ulidhulumu sana hasa kwa kushirikiana na watu wa BIMA , unakumbuka mlivyowakata watu fedha eti ni bima ya Afya kisha wakienda HOSPITALI wanadharauliwa na kunyanyasika..... Unakumbuka kuwa ile fedha mligawana wenyewe?" Naye huyu akatupwa motoni. Ikafuata idara nzima ya Afya. Niliowaona sana walikuwa ni wale wa Taasisi ya Mifupa ya hospitali yao kuu(Si MOI), "Ninyi kwa pamoja mliongoza sana kwa rushwa, hakutibiwa mtu pale mpaka atoe fedha ambayo inaenda katika mfuko binafsi wa daktari. Tunawasamehe kwa kufanya operesheni za kukosea wa kichwa kupasuliwa mguu na wa mguu kupasuliwa kichwa, tunajua ni mapungufu ya kibinadamu lakini hatutawasamehe kwa kuwaumiza na kuwatesa wananchi. Kwanini? Hata mtu akija na bima ya Afya alikuwa hawezi kupata huduma......" Nao wakafungwa na kutupwa motoni.
Baada ya kupita zamu ya viongozi wa serikali ikafuata zamu ya viongozi wa dini. Wakaitwa kwanza wahadhiri wa kikristo na kiislamu kwa pamoja. "..... Enhe mnakumbuka jinsi mulivyokuwa mnakutana kwa siri na kupanga mihadhara? ...Mnakumbuka jinsi mlivyokuwa mnajifanya kubishana tena kwa matusi ambayo yangehatarisha amani kisha baada ya muhadhara kugawana mapato ambayo mlichangisha kwa kisingizio eti ni sadaka?" Nao wakatupwa motoni. Ikafuata zamu ya viongozi mbalimbali wa dini, Wengine walikuwa na makosa ya kuingiza madawa ya kulevya kwa kivuli cha dini, wengine walikuwa na makosa ya kutumia Ushirikina kwenye kazi yao. Ili mradi kila mmoja alikuwa na makosa yake. Wakatupwa motoni.
Nikaangalia pale walipo viongozi wa Tanzania mh! Nao walikuwepo wakisubiri hukumu. Nilikuwa najiuliza watahukumiwa nini kwani wengi ni rafiki zangu. Hofu ikatawala kwenye moyo wangu. Nikasikia sauti kubwa. Sasa ni zamu ya watanzania na viongozi wao. Nikaanza kutetemeka. Ashakum si matusi viongozi wengine wa Tanzania nikawaona wakijikojolea. Huku nikiwa na hofu kubwa nikasogea kule mbele kwenda kuhukumiwa.................... sasa ni wazi ilikuwa zamu ya Watanzania WANASUBIRI HUKUMU.
Ghafla nikashtuka kutoka usingizini. Aaaah! Kumbe ilikuwa ni ndoto. Mh! nikaguna baada ya kuiangalia mikataba iliyoko mezani ambayo ni wazi ilikuwa ni dhulma kubwa kwa Watanzania. Dah! hii ndoto bwana. Sasa najiuliza nifanye vipi Toba? niwarudishe wanangu wanaosoma Ulaya kwa pesa za Watanzania? Je yule mwanamke wa pembeni ambaye nimemjengea nyumba kwa fedha za walipa kodi! Nikainuka pale kwenye sofa baada ya kuona maswali yanakuwa mengi kuliko majibu.