Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,809
- 15,421
Kwanza anza kujipenda wewe mwenyewe. Kama wewe mwenyewe hujipendi, usitegemee kuwa wengine watakupenda. Ukimudu kujipenda, utamudu kumpenda kila mtu na suala la kuolewa na nani, linakuwa halina maana.
Pili elewa majukumu yako. Ni vizuri kama mwanamke ulielelewa vyema kujua majukumu yako. Kwa kweli awe ni mwanamke au mwanaume, anatakiwa kujua majukumu yake mapema kabla hata ya ndoa ili kupunguza migongano baadaye.
Tatu, wanaume wanapenda wanawake imara. Hawapendi mwanamke ambaye akiudhiwa kidogo tu kakimbilia kwa mtu kwenda kuomba msaada. Lazima uwe imara kukabiliana na masaibu ya maisha. Haina maana usiombe ushauri pale unapozidiwa. Hapana, unapozidiwa huna budi kuomba msaada.
Nne wanaume wanaenda polepole na ni waangalifu linapokuja suala la kumpata mwenza wa maisha. Wanataka kwanza wamjue msichana ipasavyo, kabla hawajaamua kumuoa. Kwanza anaanza kwa kumpa mialiko ya kutoka naye ili kuweza kuichunguza tabia yake vizuri. Utaratibu huu wa wanaume ndio unaowakera wanawake ambao wanataka kuoana kwa harakaharaka. Waache wanaume wafanye utafiti wao kwani ni kwa faida yenu nyote wawili. Unavyozidi kumshinikiza mwanaume akuoe harakaharaka kabla hajakufahamu vizuri ataanza kukushuku. Unatakiwa usubiri mpaka aseme mwenyewe kwamba angependa kukuoa, hata hivyo unaweza kuanzisha mada ya ndoa kama muda wa mwaka mmoja umepita.
Tano, onesha kujiamini. Unatakiwa kuwa ni mtu unayeweza kutatua matatizo yaliyo mbele yako. Wanaume wengi wanapenda wanawake wanaojiamini.
Sita, unapoongea na mwanaume unayempenda, mwangalie machoni kwa mahaba fulani ambayo mwanaume huyo atajua kwamba unamtofautisha na wanaume wengine unaokuwa nao.
Saba, onesha kumkubali na kuukubali uwezo alionao. Na kama analo jambo ambalo ni mtaalamu sana nalo, basi mwambie hivyo na kwamba unafurahia mafanikio yake.
Nane, kuwa mchangamfu, na hata kama uchangamfu wako utaambatana na kuchekesha ni jambo muhimu sana na katika uhusiano. Usiwe mtu mwenye msimamo mkali kiasi cha mtu kuchagua mada za kuongelea akiwa na wewe. Kuwa mtu rahisi kuingilika.
Tisa, wanawake ambao wana furaha muda wao wote wa maisha yao, wana mvuto kwa wanaume wote. Wanawake wa aina hii ni kama vile wanafurahia kuwa hai! Wanaishi kwa tabu wana furaha; wanaishi kwa raha wanafuraha!
Kumi, mapenzi uliyo nayo moyoni kwa mwanaume huyo yaoneshe hivyo hivyo uwapo mbele yake kila unapokutana naye. Hiyo ndiyo gia kali sana ya kumteka mwanaume unayempenda na ambaye unataka awe mwenza wako wa baadaye.
Kumi na moja, jifunze kuwa mnyenyekevu, mtu mnyenyekevu ni yule anayejishusha awapo mbele za watu. Ni mtu ambaye anaona shida zake ni za pili kuliko shida za wenzake.
Kumi na mbili, usimkataliye mwanaume unayempenda kutoka naye, jiamini na jenga heshima ya mwili wako na hakikisha unaujali uhusiano wenu. Kutoka ni kwa ajili ya kujuana kiundani kuhusu maisha ya kila mmoja wenu na siyo zaidi ya hapo. Wapo wanaoamni kuwa kutoka maana yake ni kwenda kuonjana, si hivyo mwanamke, kuonjwa onjwa kunaweza kukusababishia ukampoteza huyo mpenzi wako kirahisi.
Kumi na tatu, baadhi ya wanaume huchukua muda mrefu sana kuamua kukuambia kwamba wangependa kukuoa. Kama unampenda na unaona kwa tabia zake anakufaa kuwa mumeo mtarajiwa, basi endelea kuwa na subira. Kama anaonekana shauku aliyonayo kwako inazidi kupungua na anaanza kuleta visingizio hata baada ya muda mrefu kupita, huna budi kuanza kuangalia mustakabali wa uhusiano wenu. Kumbuka kwambamapenzi ya kweli hayaletwi na kushinikizana.
Kumi na nne, mapenzi yanatakiwa yatoke pande zote mbili. Mwanaume akionesha kwamba anakupenda basi na wewe muoneshe kwamba unampenda, wala usifiche. Kuficha kwamba unampenda hakuwezi kukusaidia zaidi ya kumkimbiza mpenzi wako huyo.
Kumi na tano, onesha mapenzi yasiyo na masharti, urafiki wa kweli ni wakati wa shida na raha. Mwanamke anatakiwa kuwa karibu na mpenzi wake wakati wa matatizo pia, na si kumtelekeza.
Kumi na sita, weka malengo, suala la ndoa linatakiwa kuwekewa malengo kama jambo lolote la kimaisha. Maisha yanasonga mbele; anza sasa kujiandaa kwa ajili ya maisha yako ya baadaye ya kindoa.
Kumi na saba, hakuna mwanaume anayetaka kufunga pingu za maisha na mwanamke mwingi wa mambo na anayejifanya kujulikana sana, hasa na wanaume, ukijifanya kuwachangamkia na kuwa karibu sana na wanaume wengine mbele ya mpenzi wako usitegemee kuvishwa pete ya ndoa, itakula kwako!
Kumi na nane, ni jambo muhimu kujua sifa uzitakazo ambazo ungependa mumeo mtarajiwa awe nazo. Huo utakuwa ndio muongozo wako mkubwa.
Kumi na tisa wanaume wengi wanapenda mwanamke mwenye maumbile na tabia ya kike.
Ishirini, ni muhimu kujali mwili wako, wanaume wanavutiwa na wanawake warembo na wenye mvuto wa kimapenzi. Jipende na hakikisha unajiremba na kujipamba kwa staha na sio kujikandika vipodozi na mikorogo………. Utaharibu. Jitahidi kuwa natural, lakini tumia simple make ups ambazo hazitaubadili muonekano wako kwa kiasi kikubwa.