Kesi ya Mbowe na Wenzake Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi yaahirishwa. Kuendelea Jumatatu ya tarehe 27/09/2021

Afadhali hata ufipa ya sumbawanga kuliko hiyo midubwana ilitumwa kama majini ambayo hata muongozo wa taasisi yao hayaijui. Police Tz are Form Four Failures who have been Fighting For Food for Four years - FFFFFFF vilaza wa divisheni 0.
Nenda UN na bango lako, acha kunipigia kelele hapa.
 
Afadhali hata ufipa ya sumbawanga kuliko hiyo midubwana ilitumwa kama majini ambayo hata muongozo wa taasisi yao hayaijui. Police Tz are Form Four Failures who have been Fighting For Food for Four years - FFFFFFF vilaza wa divisheni 0.
Hapo sasa umewaonea, ngoja niwatetee kidogo.
 
Jaji ameingia.. Watu wanasimama, Kesi inatajwa, watu wanaketi..

Jaji: Wakili wa Serikali

Wakili wa Serikali: anatambulisha Mawakili wa Jamhuri..

Adv. Kibatala: anatambulisha Jopo la mawakili wa utetezi..
Peter Kibatala
Jonathan Mndeme
Fredrick Kihwelo
Dickson Matata
John Mallya
Sisty Aloyce
Alex Masaba
Idd Msawanga
Gaston Garubindi
Evaresta Kisanga
Hadija Aron
Faraj Mangula
Maria Mushi
George Masoud
Michael Lugina
Nashon Nkungu

Kibatala: ni hayo tu Mheshimiwa Jaji na wengine wakifika tutaijulisha mahakama..

Jaji: nimeona mawakili wa utetezi wapo upande huu, Je mpo sawa?

Wakili wa Serikali: Tupo sawa

Wakili Peter Kibatala: Tupo sawa

Jaji: Wakili Kidando

Wakili wa serikali: shauri limekuja kwa ajili ya kusikiliza na mpaka sasa tumeshaleta mashahidi 3 kati ya 7, na tunaomba hairisho mpaka Jumatatu.. tunaomba kupata muda wa kupitia ushahidi uliowasilishwa.

Wakili wa serikali: tunaomba kuondoa mashahidi wengine waliobakia kwa dhumuni la kesi ndogo tubakie na hao hao watatu Wakili wa Serikali anakaa chini..

Jaji: kuna lolote upande wa utetezi? Jaji anaendelea kuandika..

Kibatala: Hakuna mheshimiwa Jaji..

Jaji anaendelea kuandika..

Jaji: Shauri hili dogo kwa upande wa Jamhuri limefungwa, Nitamsikiliza wakili John Mallya...

Wakili Mallya: Mshtakiwa wa pili atajitetea mwenyewe na mashahidi wengine watatu pamoja na yeye watakuwa jumla wanne

Jaji: Kuna kingine.?

Mallya: Mheshimiwa ni hayo

Jaji: Mpo tayari kuanza utetezi hata sasa? au Mngehitaji muda wa kujiandaa?

Mallya: tupo tayari

Jaji anaandika. Mahakama kimya, Nje mvua inapiga kidogo

Jaji: Shahidi wa kwanza wa shauri dogo la utetezi aje kwenye kizimba..

Shahidi: anaenda kizimbani anasindikizwa na askari Magereza

Jaji: tutajie majina yako kwa ukamilifu wako unaitwa nani..

Shahidi: Adam Kasekwa

Jaji: Kuna Jina limekuwa likitumika la Adamoo unalitambua??

Shahidi: nalitambua

Jaji: Dini yako Mkristo?

Shahidi: ndiyo

Jaji: Apa

Shahidi: Naapa mbele ya mahakama hii, yote nitakayosema yatakuwa kweli tupu, Eeh! Mwenyezi Mungu nisaidie..

Jaji: unaweza kutoa ushahidi wako ukiwa umesimama au umekaa, Wakili John Mallya unaweza kuendelea..

Mallya: Shahidi umetoka kuapa, unaweza kututambulisha ulipokuja mahakamani umetokea wapi?

Shahidi: nimetokea gereza la Segerea..

Mallya: Siku za nyuma ulikuwa wapi?

Shahidi: Nilikuwa askari wa JWTZ kikosi namba 72 Sangasanga Morogoro

Mallya: ni Kikosi cha namna gani?

Shahidi: zamani kikosi cha Makomandoo siku hizi kinaitwa SPECIAL FORCE

Mallya: umehudumu kwa miaka gani?

Shahidi: Miaka sita kuanzia 2012 mpaka 2018

Mallya: Kipi kilikufanya uache kazi?

Shahidi: sikuacha bali niliachishwa na wakuu wangu

Jaji: sijui mnasikia maana naona kelele za mvua zinaingilia, KILA MTU ANAYO HAKI YA KUSIKILIZA HII KESI

Jaji: Jamani Mnasikia

Wote: tunasikiaaaaaa

Jaji: Kama mkiona hamsikii tunaweza ku' break kidogo, Hasa mawakili na washitakiwa muwe free tafadhali..

Shahidi: Mwaka 2016 mpaka 2017 nilikuwa kwenye misheni KONGO na Kurejea salama nchini kwangu na kuendelea na kazi.. wakuu wangu wakagundua kuwa nina tatizo la BATTLE CONFUSION

Mallya: Unaweza kumueleza, Jaji Battle Confusion inakuwaje?

Shahidi: siwezi kujijua sana lakini ni hali ya Askari anaposikia milio ya mizinga na risasi kwa wingi anakuwa hafanyi vile anavyotakiwa na wakubwa wake

Mallya: Kwenye Afya ana athiri mfumo gani?

Shahidi: mfumo wa akili..

Mallya: sasa umeshafukuzwa kazi baada ya Battle Confusion, Je ulikuwa unafanya shughuli gani?

Shahidi: nilikuwa nafanya biashara ya kununua maharage huko Morogoro sehemu inaitwa Nongwe na kuuza soko la Lubeho, kote Morogoro

Mallya: unamfahamu mshtakiwa namba 4?

Shahidi: simfahamu sana ila nilitakiwa nikafanye naye kazi ya VIP PROTECTION

Mallya: kazi ya VIP PROTECTION ni kazi unayoweza kuifanya?

Shahidi: Ndiyo

Wakili wa Serikali: OBJECTION

Mallya: naondoa swali

Mallya ulifanya nini?

Shahidi: nilikuwa kwenye hatua ya mazungumzo ya kazi

Mallya: yalikuwa yanahusisha nini?

Shahidi: kuhusiana na majukumu ya kazi na malipo yetu

Mallya: ilikuwa lini?

Shahidi: Mwishoni wa mwezi wa 7 mwaka 2020

Mallya: Makubaliano ya kufanya kazi na mshtakiwa wa 4 mlikuwa mnafanya wapi?

Shahidi: mara ya kwanza tulifanya Moshi

Mallya: nakupeleka tarehe 05 Mwezi 08 mwaka 2020 kilitokea nini?

Shahidi: siku hiyo nikiwa na mshtakiwa mwenzangu namba 03 Mohammed Ling'wenya sehemu inaitwa maduka, tukavamiwa na watu kama watano, walinivamia mimi kwanza wakaanza kunipiga, mshtakiwa mwenzangu akaja kuniokoa..

Shahidi: alipofika akawauliza "Mbona mnapiga huyu mtu?".. wakamuuliza wewe unamfahamu huyu, akajibu ndiyo namfahamu.. wakachukua madawa na silaha, nikawasikia wakisema ana madawa.. wakati Mimi wakiendelea kunishambulia.....

Shahidi: Mshitakiwa mwenzangu akawawahi akitoa vitu mfukoni, nikasikia kwa maneno akisema huyu mmeshamuwekea madawa? akiwa anamaanisha mimi... mmemuweka madawa na silaha? Mimi natoa vitu vyangu kabisa msije mkaniweka na mimi, Wakati huo mimi wakiendelea kunishambulia..

Mallya: unaweza Kuwakumbuka watu hao ukiwa hapa Mahakamani.?

Shahidi: Mahakamani nimeshawaona watu 2

Jaji: Subiri kidogo, anaendelea kuandika..

Mallya: ni nani umewaona hapa mahakamani?

Shahidi: Ramadhani Kingai na Mahita ambao nimekuja kuwafahamu majina yao hapa mahakamani

Mallya: hawa watu wawili ambao umewataja walikuwa na majukumu gani?

Shahidi: nilikuwa nawatambua kwa sura na matendo yote ya kunipiga na kuniwekea Madawa na silaha..

Jaji: Ukisema kuwekewa madawa na silaha nini kilichotokea?

Shahidi: Wakati wananipiga na wamenibana, akaingiza mkono wake kwenye suruali akasema ana madawa na mwingine akaingiza kitu nyuma ya mkanda akatoa kitu akasema ana silaha

Mallya: hili eneo ambalo tukio limetokea lilikuwa ni eneo la wazi?

Shahidi: pana maduka ya kubadilisha pesa. M-pesa na tiGoPesa na Grocery pembeni

Mallya: Wewe ulikuwa sehemu gani?

Shahidi: nilikuwa katikati upande kulia maduka na upande wa kushoto Grocery..

Mallya: Ulikuwa umekwenda kufanya nini?

Shahidi: kuagiza chakula, Nilikuwa naandaliwa nyama ya kuchoma lakini hata kulipa bado

Mallya: nini kilifuata,?

Shahidi: baada ya mwenzangu kusema natoa vitu vyangu msije kuniwekea kama mlivyo muwekea huyu, wakatukamata na wakatufunga pingu na kutuingiza kwenye gari yao..

Mallya: baada ya kuingizwa kwenye gari waliwapeleka wapi?

Shahidi: Muda wote tulikuwa tunapigwa, hatukujua tunaelekea wapi, baadae wakatufikisha kituo cha polisi

Mallya: kituo gani?

Shahidi: nilikuaa sikijui, lakini baada ya kuongea mahakamani nimegundua ni Central Moshi

Mallya: Baada ya kupelekwa Central Moshi kitu gani kilifuata?

Shahidi: walinitoa pale ndani kituoni kuna chumba cha pembeni palikuwa na jopo la watu wengi wakanivua nguo zote, nikawa ninaning'inizwa kwenye kichuma fulani mithili ya MSHIKAKI au POPO

Mallya: wakakuning'iza kama Popo, kitu gani kilifuata?

Shahidi: wakianza kunipiga na kunitesa na muda wote wananiuliza swali "HUKU MOSHI UMEFUATA NINI" nikijibu kuwa huku Moshi nimekuja kufanya VIP PROTECTION kwa Mheshimiwa MBOWE,Hilo jibu hawalitaki wala haliingii akilini

Shahidi: nikiwa siwezi kusimama wakanitoa pingu wakanivalisha suruali na shati, wakaanza kunikokota

Jaji: umezungumzia kuvaa!

Shahidi: Ndiyo walinivalisha suruali. wakawa wananikokota kunipeleka mahabusu, baada ya kufika mahabusu wakanifunga pingu za mikono wakaniacha ndani

Mallya: jambo gani lilifuata?

Shahidi: ndani ya mahabusu kuna chumba kidogo cha mlango wa nondo wakawatoa watu mule wakanifungia mimi..

Mallya: ulijua hatima ya yule mtuhumiwa mwingine?

Shahidi: sikujua hatima yake

Mallya: nini kilifuata?

Shahidi: niliendelea kukaa ndani

Mallya: kuna ushahidi umetolewa kuwa mlizunguka maeneo mbalimbali Moshi na Hai

Shahidi: hapana sikutolewa kwenda popote

Shahidi: Ndani ya chumba kuna Askari alikuja kumwaga maji

Mallya: nini kiliendelea

Shahidi: kesho yake nilikuja kugundua ni kesho tayari baada ya kuona Jua

Shahidi: wakanitoa wakinilazimisha nitembee lakini nikawa nikawa siwezi.

Simu inaita kwa VIBRATION (mithili ya Philips)

Jaji: naomba kila Mtu aweke simu yake katika mazingira ambayo hayaathiri kazi yangu au ya shahidi, Msilazimishe niongee Jambo ambalo sitaki kuongea..

Jaji: Endelea baada ya kutolewa

Shahidi: wakaja watu wakanikokota na kunipandisha kwenye gari

Mallya: unaweza kukumbuka hao waliokuwa wanakukokota ni akina nani?

Shahidi: namtambua mmoja anaitwa Goodluck

Mallya: baada ya kukukokota na kukufunga Jacket usoni walikupeleka wapi?

Shahidi: sikujua naenda wapi, nilitambua tu nipo kwenye gari na ikaanza kutembea

Mallya: kitu gani kiliendelea?

Shahidi: nikiwa ndani ya gari kabla haijatoka kwa muda wa nusu saa, mateso yaliendelea kwa kunichoma choma na bisibisi

Shahidi: wakawa wananiambia "Leo ndiyo mwisho wa maisha yako, na kwamba hapa tulipo unamjua nani, nikajibu simjui Mtu, wakasema basi na wewe hakuna anayejua upo na nani".

Mallya: Endelea

Shahidi: nilikuwa nimelazwa kwenye floor ya gari, siyo kwenye siti..

Shahidi: baada ya safari ya muda mrefu sana, tukafika sehemu wakanishusha kwa kunikokota vievile na tulipofika kwenye kachumba wakanitoa Jacket wakaniuliza "Unajua upo wapi hapa?" nikawaambia "hapana sifahamu" wakafunga mlango nikiwa ndani nikiwa na pingu lakini Jacket wamenitoa

Mallya: unamkumbuka aliyekuwa anakuuliza hayo?

Shahidi: namkumbuka ni Goodluck

Mallya: Jambo gani lingine lilitokea kwenye kile chumba?

Shahidi: nikiwa na pingu nikajikokota kusogea mlangoni bahati nzuri nikaona watu wengine wamefungiwa kwenye chumba kingine kidogo mule

Shahidi: nikawauliza ni wapi hapa? Wakanijibu hapa ni TAZARA

Mallya: hao watu waliokwambia hapa upo TAZARA ulipata kuwafahamu au ulikuwa unawafahamu?

Shahidi: hapana nilikuwa siwafahamu

Mallya: nini kilifuata?

Shahidi: nilikaa pale tarehe 7, 8 na 9 na ilipofika tarehe 9 usiku wakaja kunichukua usiku.

Mallya: umesema umekamatwa Moshi tarehe 05 je kati ya tarehe 5 Mpaka tarehe 7 kuna nini kilitokea?

Shahidi: tarehe 05 - 7 nilikamatwa Moshi na kuteswa kisha nikasafirishwa kuja TAZARA

Shahidi: tarehe 09 wakanitoa usiku, siku hiyo angalau nilikuwa na uwezo wa kutembea, Lakini wakaniambia huku tunakoenda yanaenda kukuta yaleyale ya Moshi, sasa UJIANDAE

Mallya: Tarehe 09 nini KILIFUATIA?

Shahidi: Wakinitoa wakanipandisha kwemye gari, safari ikaanza..

Shahidi: haikuchukua muda kama Moshi. Siku hiyo sikuwekwa chini kama walivyonisafirisha kutoka Moshi. wakaniingiza kwenye chumba wakanifungua

Jaji: Subiri kidogo..

Jaji: unasema mlipofika wakakushusha?

Shahidi: walifikisha mpaka kwenye chumba, Kilipofunguliwa wakanitoa Jacket usoni, wakaniamuru niingie ndani

Jaji: Ndiyo

Mallya: rudi nyuma kidogo shahidi baada ya kuambiwa kuwa upo TAZARA, Ulifanya jambo lolote kuthibitisha upo TAZARA?

Shahidi: ilipofika jioni nilikuwa nasikia mlio wa honi ya TRENI,nikagundua nipo MAENEO yanayofanana na TAZARA

Mallya: sasa tayari upo sehemu nyingine umefumguliwa koti machoni

Shahidi: niligundua umeshaingia usiku, kesho yake usiku tena akaja Kingai na Goodluck wakanitoa ndani

Mallya: Taratibu Shahidi Jaji aandike

Shahidi: wakanipeleka Kwenye chumba kilichokuwa kina meza, Goodluck akawa mlangoni na Kingai akakaa mbele yangu tukawa tunatazamana

Jaji: NDIYO

Mallyaunazozungumzia ni zipi

Shahidi: pingu za chuma

Shahidi: Kingai akaniambia "mateso yanapopungua ujue kuna kuna mambo mazuri yamekaribia" m tunataka uwe mstaarabu, hapa kuna nyaraka tunakuja mnazo tunataka usaini..

Mallya: Mkono wa kushoto na pingu, wa kulia na kalamu, nini kilifuata!

Shahidi: akawa ananionyesha sehemu za kuandika kama "NATHIBITISHA" au KUSAINI

Mallya: Ulipata Kujua Kimeandikwa kitu gani ktk kile kingai anachokuoatia Kuthibitisha au Kusaini

Shahidi: Hapana

Mallya: Moshi umetuambia walikupiga, wakakulaza kwenye Floor sehemu yenye Joto kwenye gari, Je unauthibisho wowote unaoweza kuonyesha mahakamani?

Shahidi: naweza Kuthibitisha kwa kuonyesha sehemu nilizoumizwa, Makovu yanayoeleka kupona na mguu nimeumia leo siwezi kutembea vizuri

Jaji: kabla hajatuonyesha atueleze yapo sehemu gani, isije ikawa sehemu ambayo yanaweza kutweza utu wake

Mallya: Shahidi tueleze maeneo ya mwili ambayo umeumia

Shahidi: Mguu wangu wa kushoto na mkono wamgu wa kushoto

Jaji: sina tatizo na maeneo hayo, Wakili unaweza kuendelea

Mallya: unaweza kusimama kuonyesha mahakama?

Jaji: unaweza kusimama na mimi nitasogea kuweza kuona..

Jaji: hiyo ni mguuni (anaonyeshwa)

Jaji: sawasawa anarudi kukaa sehemu yake

Shahidi: anarudi sehemu yake pia Mahakama ipo kimyaaa!

Mallya: kuna wakati ulitaka kumueleza Jaji kuna vingine ulitaka kumueleza nini hivyo?

Shahidi: Takribani Mwaka 1 na mwezi sasa tangu niteswe na kuumizwa, sikuwahi kupelekwa hospitali kwa matibabu na mpaka sasa nahisi maumivu makali

Mallya: Je ulipata kutambua kuwa upo kituo gani cha polisi?

Shahidi: nilikuja kujua nipo kituo cha polisi MBWENI

Mallya: Ulijuaje kuwa upo Mbweni?

Shahidi: kuna askari polisi alikuwa zamu, alisema hamtakiwi kujua mpo wapi, lakini mpo kituo cha Polisi Mbweni

Mallya: Utofauti wa majina yako Mbweni ulijuaje?

Shahidi: siku ya kwanza nafika Mbweni nilifika pale Mlangoni nikakabidhiwa kikaratasi kuwa kuanzia siku hiyo naitwa VICENT JUMA na wakikikuuliza umekamatiwa wapi sema TABORA na useme kesi ya UNYANG'ANYI, ukiseme Majina yako tutajua

Mallya: baada ya kujua upo Mbweni nini kiliendelea?

Shahidi: niliendelea kukaa Mbweni muda wote mpaka siku nafikishwa mahakamani na muda wote sikufunguliwa pingu

Mallya: unakumbuka ilikuwa siku gani? Mahakama gani?

Shahidi: ilikuwa Tarehe 19 Mwezi 08 Mwaka 2020

Shahidi: Nilipofika mahakamani ndipo nilikutana na mshtakiwa mwenzangu ambaye tulikamatwa pamoja Moshi na mshtakiwa namba 1..

Jaji: Kama naelewa tangu mtoke Moshi hamkuwahi kuonana

Shahidi: ndiyo hatukuwahi kuonana kwa macho

Mallya: Je mliwahi kuwasiliana?

Shahidi: tukiwa TAZARA tuliwasiliana kwa sauti akitokea chumba kingine lakini hatuonani

Mallya: tarehe 05 RAU Madukani, Moshi ukisema wamekuwekea vitu, Je wewe Binafsi ulikuwa na nini mfukoni?

Shahidi: nilikuwa na pesa Laki 2 na 60 taslimu, simu ya Itel na line ya Halotel

Mallya: hivyo vitu vipo wapi?

Shahidi: tangu wavichukue sijavipata

Mallya: nani alichukua.+?

Shahidi: alichukua mfukoni Goodluck akampatia Kingai

Jaji: Shahidi bado unayo maji mkononi, Kama utahitaji break utasema maana kuulizwa maswali kunatumia sana akili na kuchosha mwili

Shahidi: Asante Mheshimiwa Jaji

Mallya: ukiondoa Kingai na Goodluck kuna mtu mwingine unamkumbuka alikuja Mbweni?

Shahidi: nilimuona Mahita

Mallya: alikuja kufanyeje?

Shahidi: nilimuona wakati wanakuja kuniona, Lakini hakuhusika kuingia katika kile chumba

Jaji: chumba kipi?

Shahidi: chumba kile ambacho kilikuwa na Meza mbili na Kingai

Jaji: nimekuelewa

Mallya: Umesikia wakitoa ushahidi hapa,kwamba walikuwa wanawapa matunzo mazuri na walikuwa wanatunza utu wenu

Shahidi: si kweli

Mallya: walisema waliharibikiwa gari Himo je unasemaje kuhusu hilo?

Shahidi: kwangu ni ngumu kuhusu kuelezea kwa sababu tulikuwa tunasimama sehemu nyingi lakini nilikuwa nimefungwa usoni nisione kitu

Mallya: je unakumbuka tangu tarehe 05 mpaka Kingai anakuletea maelezo yako usaini zilikuwa zimepita siku ngapi

Shahidi: Siku 06

Mallya: Kwa sasa sina la zaidi Mheshimiwa Jaji

Jaji: Wakili Malya unafikiri Shahidi wako anaweza Kuendelea.?

Mallya: it depends

Jaji: nimekupa wewe kuamua nilikuwa naweza kuendelea bila kukuuliza

Mallya: Anaweza kuendelea Mheshimiwa Anaingia wakili Nashon Nkungu

Nashoni: Je ni kweli baada ya kupata Battle Confusion hukupatiwa matibabu?

Shahidi: hapana nilipatiwa kwa maana nilipelekwa hospitali ya Lugalo

Nashoni: kwenye maelezo watu hawa walikwambia sisi hautufahamu na wewe hutufahamu ni sahihi?

Shahidi: ni sahihi.

Nashoni: Ulipata hisia gani kuwa na watu hao?

Shahidi: wasiwasi nikaona roho yangu ipo mkononi

Wakili wa Serikali: MHESHIMIWA JAJI HISIA NI KITU GANI

Jaji: hilo linamuhusu mwenyewe, kuhusu hisia zake, haliwezi kuathiri Jambo lolote

Jaji: rudia hisia ulisikiaje hisia zako

Shahidi: niliogopa kwamba naweza kuteswa sana

Nashon: umeeleza kuwa ulikuwa unachomwa BISIBISI, Je ni maeneo gani sasa?

Shahidi: Maeneo ya MBAVU na MATAKONI

Nashon: Ukisafirishwa kutoka ulipokamatwa Moshi kuja Dar es salaam, TAZARA..

Shahidi: baada ya siku MOJA

Nashon: Uliambiwa kuwa mnaanza safari ya kuja Dar es salaam au popote.?

Shahidi: Hapana sikuambiwa

Nashon: unaweza kujua kwanini hamkuanza safari ya kuja Dar es salaam baada tu ya kukamatwa?

Shahidi: Hapana

Nashon: Unakumbuka kuwa mlifika Arusha baada ya kukamatwa?

Shahidi: Sikumbuki na wala halikwepo jambo hilo

Nashon: unasema ulikuwa na Pesa,260,000/= unakumbuka kuandikiwa risiti ya pesa hizo?

Shahidi: Hapana

Nashon: Mheshimiwa Jaji yangu ni hayo tu

Jaji: Wakili Fred na Matata mtauliza maswali wote 2 au 1 kwa niaba ya mshtakiwa wa 3?

Wakili Fred Kihwelo: Kwa niaba ya mshtakiwa wa tatu hatutokuwa na maswali yoyote

Jaji: Kibatala kwa niaba ya mshtakiwa wa nne

Wakili Kibatala: nataka utuambie kwa vitendo Ulikabwaje pale RAU MADUKANI..

Shahidi: nilikuwa naongea na simu nikiwa nimevaa Jacket naongea na simu, akatokea mtu kwa nyuma akashika mkono wenye simu na Jacket wakati najitetea akatokea kwa mbele mwingine, Mwingine akatokea akanishika mkanda hapa kiunoni..

Kibatala: unaweza kutonyesha?

Shahidi: bahati nzuri suruali niliyovaa siku ile nakamatwa ndiyo niliyovaa leo, haina hata RUSKI

Kibatala: naweza KUONA?

Shahidi: Ndiyo unaweza kusogea

Kibatala: sawa lakini pia mahakama inataka kuona

Kibatala: Wakati wanakukamata hapo ikawaje

Shahidi: akatokea mtu mbele akanipiga ngumi

Kibatala: unamkumbuka?

Shahidi: ndiyo alikuwa dereva wa gari tuliyopanda

Kibatala: Kingai alikwepo eneo la tukio.+?

Shahidi: ndiyo

Kibatala: alikuwa anafanya nini?

Shahidi: yeye ndiyo ALICHUKUA PESA ZANGU BAADA YA kusachiwa

Kibatala: Afande anayeitwa Mahita alikwepo wakati unakamwata.l?

Shahidi: alikwepo na yeye ndiye alikuwa wa kwanza kunikaba wakati naongea na simu

Kibatala: uliwezaje kuona tukio hilo la kukabwa?

Shahidi: niliona kwa sababu ilikuwa mchana na nilikuwa na akili timamu

Kibatala: Wakati wanafika kukukamata waliijitambulisha kwa mujibu wa PGO na sheria.l?

Shahidi: Hapana hawakufanya hilo..

Kibatala: na ni kweli kwamba wakati wanakukamata hawakuwa wameshika Ki' Notebook?

Wakili wa Serikali: MHESHIMIWA OBJECTION anachokifanya Wakili Msomi siyo kinacholekezwa kwa mujibu wa TRIAL WITHIN a TRIAL pamoja kwamba haijasema UKOMO wa maswali.. Matters ambazo ni Mpya zitaipotezea Muda Mahakama

JAJI: Wakili Kibatala..

Kibatala: Kwa heshima na taadhima wakili Msomi mwenzangu HANA HOJA, Shahidi analindwa na Jaji kama ningemuuliza SWALI ambalo lingemdhalilisha ningezuiwa, sijui anamaanisha nini?

Jaji: tuendeleee Shahidi ni wa Utetezi siyo wa mashtaka ,Labda iwe kwa maswali yanayo dhalilisha

Jaji: Tuendeleeeeeeeee

Kibatala: uliwahi kuona mtu ameshika NOTEBOOK wakati wa zoezi kukukaba na kukukamata linaendelea?

Shahidi: Ndiyo

Kibatala: wakati unakamatwa ni eneo la wazi bila shaka watu wengi walishuhudia wakati wa Kukamatwa kwako

Shahidi: ndiyo walikuwa wengi

Kibatala: je uliona wakati wowote Kingai anaita watu washuhudie kukamatwa kwako?

Shahidi: Hapana

Kibatala: uliona hapa mahakamani kitabu chochote ambacho mahakamani kimeletwa kinaeleza ni aina gani ya silaha ulikamatwa nayo Moshi?

Shahidi: hapana

JAJI: wakili naomba tu' break ni takribani masaa mawili sasa, na tutaendelea saa 7 kamili mchana.. natoa Break ya nusu saa kisha tutarejea kuendelea...

Jaji ananyanyuka anatoka

Tunasimama..

-------------------------------------------------------------------------------------------------------------------


Jaji ameingia.. Kesi inatajwa..

Mafaili yanapelekwa kwa jaji

Jaji: Wakili wa Serikali kuna mabadiliko yoyote?

Wakili wa Serikali: Hapana

Jaji: Kuna mabadiliko yoyote upande wa utetezi?

Kibatala: Hapana Mheshimiwa

Jaji: Nakuita sasa shahidi na kukumbusha upo chini ya kiapo

Kibatala: kwa Kumbukumbu zako kuna shahidi yoyote aliwahi kuwasilisha hapa mahakamani kwamba bastola imeingia kama sehemu ya ushahidi?

Shahidi: Hapana sijaona..

Kibatala: umesikia mashahidi wa serikali wamesema walipokuchukua Moshi kwamba waliwachukua kwenda kumtafuta Moses Lijenje kwa sababu ya upelelezi?

Shahidi: Hapana sijaona

Kibatala: kuna nyaraka yoyote imetolewa ushahidi wa upande wa mashitaka kwamba kuna nyaraka inaonyesha gari iliharibika na kutengenezwa

Shahidi: Hapana

Kibatala: ushawahi kuona shahidi kutoka Moshi Central Polisi Station Moshi kuwa uliingia na kutoka mara kadhaa ukiwa kituoni

Shahidi: Hapana sijamuona

Kibatala: Umemuona Shahidi ambaye ni dereva ambaye gari lake liliharibika Himo na ndiye aliyewaendesha kutoka sehemu mbalimbali

Shahidi: Hapana

Kibatala: Umemuona RPC ambaye baada ya gari kuharibika ndiye alitoa gari yake kuwaleta DSM kuthibitisha hilo

Kibatala: Ulimsikia Jumanne ndiyo alikupekua Moshi, uliwahi kumuona Jumanne mahakamani kama shahidi muhimu?

Shahidi: Hapana

Kibatala: ulimsikia shahidi kutoka central Police Station DSM kuwa alikabidhiwa watuhumiwa ikiwemo wewe kutoka kwa Jumanne, je Jumanne umemuona Mahakamani

Shahidi: hapana sijamuona

Kibatala: Ushawahi kumuona mahakamani dereva wa RPC ambaye aliwachukua na gari yake kutoka Himo — Dar.?

SShahidiahidi: Sijamuona

Kibatala: hapa Mahakamani ulishawahi kuona kithibitisho chochote kinacho onyesha gari ya RPC imeruhusiwa kutoka Moshi - DSM?

Shahidi: Hapana sijaona

Kibatala: kwanza kwa uelewa wako wewe ulitekwa au ulikamatwa?

Shahidi: nilitekwa

Kibatala: Je Ulishawahi kusikia hapa Mahakamani Kingai au wenzie wanazungumzia kuhusu pesa zako?

Shahidi: Hapana

Kibatala: umesikia Mashahidi wa serikali wanasema waliwakamata mkiwa mnakula?

Shahidi: Ndiyo

Kibatala: Utakubaliana na mimi kama mlienda kula bila shaka ulikuwa na pesa, Je umesikia hapa mahakamani wamezungumzia kuhusu Pesa ulizokuwa unataka kununulia chakula?

Shahidi: Hapana

Shahidi: Hapana

Kibatala: wakati unatoka RAU Madukani kwenda Central Police station Moshi ulifungwa kitambaa usoni?

Shahidi: Hapana

Kibatala: Kwa hiyo ulifungwa kitambaa machoni wakati wa kutoka Moshi kwenda Dar es salaam na wakati kutoka TAZARA kwenda Mbweni?

Shahidi: Ndiyo

Kibatala: ulisema ulipokuwa kituoni TAZARA ulipafahamu kwa kusikia honi ya treni?

Shahidi: Ndiyo

Kibatala: nini kingine kilikufanya utambue kuwa upo TAZARA

Shahidi: kwa sababu niliuliza MAHABAUSU wenzangu

Kibatala: unawakumbuka hao Mahabusu?

Shahidi: ndiyo nakumbuka mmoja alikuwa anavaa kanzu mrefu kama msomali, na mwingine alikuwa mwanajeshi kutoka kambi ya TWALIPO na wote walikuwa na MASHTAKA ya UGAIDI pia

Kibatala: Je kwa kesi hii hii.+?

Shahidi: Hapana

Kibatala: Umesikia shahidi wa serikali amesema rumande aliwaletea uji ilikuwa shimoni, Je rumande ya TAZARA ipo shimoni

Shahidi: Hapana haipo Shimoni

Kibatala: je mlipokuwa TAZARA walikuja maafisa wawili wa JWTZ je unawafahamu

Shahidi: Siwafahamu kwa majina ila nawakumbuka kwa sura kwa sababu nilifanya nao kazi kikosi cha 92KJ

Kibatala: je unafahamu walikuwa wanahusika na nini pamoja na kina Kingai

Shahidi: sifahamu

Kibatala: wakati unakwenda Mbweni ulijua kuwa unaenda kwenye MATESO?

Shahidi: Ndiyo ni sahihi.

Kibatala: ni kweli au si kweli kwa askari aliyekwambia hapa upo Mbweni ingawa hukutakiwa kujua upo wapi, alionyesha utu na kwamba unaonewa?

Shahidi: Ni sahihi Kabisa

Kibatala: Ni sahihi wakati unahojiwa, Afande kingai anakulazimisha usaini maelezo na kupelekea kesi ndogo katika kesi kubwa, Kule Mbweni, muelezee Mheshimiwa Jaji, Goodluck alipokuwa mlangoni alikuwa ameshika bastola?

Shahidi: Sahihi kabisa

Wakili wa Serikali: OBJECTION. Sheria ya ushahidi kifungu 146(1) na (2) kwamba Cross Examination inafanywa na upande wa pili, kwa madhumuni kama haya tunakubaliana, ila madhumuni yake ni kwamba anayefanya mahojiano (Cross examination) awe kwa ushahidi ambao umesemwa,Lakini Cross examination inatumika kuingiza ushahidi mpya.. tena kwa Leading questions ambapo shahidi kazi yake hapa anasema hapa ni kweli, sijui hapa Mheshimiwa tunaipeleka mahakama wapi, imekuwa ni Practice sana.

Jaji: kufupisha muda, unaelewa nini kuhusiana na ADVERSE PARTY?

Wakili wa Serikali: najua mahakama ndiyo ina haki ya ku' Control Cross examination ila tuliruhusu hili sisi tutakosa nafasi ya Kuhoji, Tulitegemea wenzetu wangeuliza kwa kielelezo ambacho wamekigusa wao

Jaji: Kuna kingine?

Wakili wa Serikali: Mheshimiwa Jaji ni kweli Cross examination haina mipaka, Lakini sheria imeaininisha masuala yapi yataulizwa kwenye Cross examination.. Sheria ya ushahidi kifungu namba 151 (6) a,b,c

Jaji: kwa tafsiri yako je?

Wakili wa Serikali: Maana yake ni kwamba anaweza shahidi akaulizwa maswali, lakini maswali hayo lazima yajikite katika mambo yafuatayo kutikisa ushahidi yaelekezwe katika kuvumbua ni nani na nafasi yake katika maisha ni Ipi, yaende katika kutikisa uadilifu wake na uadilifu wake kwa tabia zake kwa mujibu wa kifungu cha 155 Ya Sheria ya ushahidi Maswali ya ulimuona Goodluck alishika bastola hatufanyi kujua yeye ni nani... tukiruhusu tutakuwa tunakiuka sheria, Mahakama ielekeze katika kuhoji shahidi

Jaji: umesoma 155 na ngapi?

Wakili wa Serikali: 155 yenyewe tu ila ina a,b na c

Wakili wa Serikali: kabla, hujaamua tunaomba turejee kifungu cha sheria ya Ushahidi 146 mahakama inayoamua kipi kiiingie katika Ushahidi, anachokiuliza Kibatala hakitakiwi kuingia kwenye ushahidi

Wakili wa Serikali: Swali alililouliza Kibatala "upo Mbweni lakini hutakiwi kujua kama hapa upo wapi" na kauliza swali linalofuata kuwa "Je alikuonea huruma" Je swala hilo linaweza kuthibitishwa? Kifungu kidogo cha( 3) Mahakama ndipo ushahidi huo unaweza kupokelewa

Jaji: NDIYO

Wakili wa Serikali: inaenda kwa maswali aliyokuwa anam' lead shahidi kuwa Je ushahidi uliletwa au haukuletwa,Je ukiwa haukuletwa wataweza kuleta?

Jaji: Kibatala, unaweza kujibu?

Kibatala: Wenzangu Wamechanganya Dhumuni la Ushahidi. wamechanganya Kujua nafasi yao katika kesi hii

Kibatala: Wamechanganya kujua mimi na Mallya ni akina nani.. Sisi sote ni adverse Party tupo upande mmoja na ndiyo maana tulitengana.. Kwa hiyo sisi interest zetu ni adverse party Niende kwa Kifungu cha 155 Shahidi anapohojiwa maswali ya dodoso anaweza, ukiongezea maswali yoyote

Kibatala: Kifungu 152 maswali ya kumuongoza shahidi yanaruhusiwa wakati wa kufanya Dodoso, hakuna mipaka. kwa sababu wa leading huenda kuna mitego, unapouliza maswali ya dodoso unaruhusiwa kuuliza maswali yanayomtega, kwa hiyo kifungu 155 wenzetu wamekisoma visivyo

Kibatala: Hapa tuna discuss mchakato wa kielelezo siyo kielelezo, shahidi yupo Free na hawa siyo Mawakili wa mshtakiwa kwamba mshtakiwa amelalamika nimemtesa na maswali, na mwisho Mallya mwenyewe mteja wake hajalalamila kuwa namtesa shahidi wake..

Kibatala: halafu kuhusu Goodluck aliongea Mallya wakati wa kuhoji ushahidi wake hawakuhoji, sasa ikipita imeshapita.. Kuhusu Relevance nimemuuliza kitu kilichoingia kwenye ushahidi wa kwanza Kuhusu kumuita huyo Goodluck mimi naweza kumuita kwa kupitia mshtakiwa wa nne

Kibatala: walitakiwa kumzuia Mallya kuhusu kumuongelea Goodluck, ilishapita imepita. Ujumla Mh Jaji yalipo ni maoni binafsi ya mawakili wenzetu siyo maoni ya sheria, Hatuwezi kufunika haki kwa sababu upande fulani unakereketwa, katazo au ruhusa lazima lipimwe katika vigezo hivyo

Jaji: Kama nilivyosema wiki iliyopita, Jambo hili linahusu ushahidi gani upokelewe au ushahidi gani usipokelewe, kwa hiyo najipa tena dakika chache kabla sijaamua.. kwa hiyo nita' break na kuamua..

Jaji ananyanyuka anatoka mahakamani..

-----------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------


Mawakili wa upande wa utetezi wanaingia..

Mawakili wa Serikali pia wamerejea na kuketi swadakta..

Washtakiwa wao mara hii hawakutolewa kwenda mahabusu.. Walibakizwa..

Tunaendelea kumsubiri Mheshimiwa Jaji arejeee..

Jaji amerejea

Kesi inatajwa tena

Mafaili yanapelekwa mezani kwa Jaji

Jaji: anatania anasema askari wake wasikate pumzi ya kelele za 'kooooooooortiii' kabla yeye ajakaa, ili aongeze mazoezi..

Jaji: nimechukua muda mrefu kutafakari hoja zilizoibuliwa na mawakili wasomi, Mawazo yangu kifungu cha 252, 165 na kifungu 161 cha sheria ya ushahidi kinatoa nafasi ya shahidi kuulizwa maswali yoyote isipokuwa yale yanayotweza utu wa mtu

Jaji: yapo maamuzi ya mashauri mbalimbali na mengi ya hayo mashauri yanayosema Contradict, Ku shake au kupunguza thamani ya ushahidi uliokwisha kutolewa.. Kwa maoni yangu mtu anapokuwa ana contradict au kupunguza thamani ya ushahidi wake, si vyema maneno hayo yaanze na neno KWELI.

Jaji: kwa sababu Ukiuliza KWELI au SI KWELI unamnyima Shahidi nafasi ya kuuliza.. Unaweza kuondoa neno si kweli hivi na hivi, lakini sizuii kuuliza swali lolote...

Jaji: Wakili kibatala unaweza kuendelea...

Kibatala: naomba Shahidi arudi kizimbani

Kibatala: Nakuuliza kuhusu Afisa wa polisi Goodluck alikuwa ameshika nini mkononi akiwa mlangoni?

Shahidi: alikuwa na Pistol mkononi

Kibatala: Pistol umeijuaje?

Shahidi: ninaifahamu kwa sababu nimeisoma sana

Kibatala: kwani Goodluck kwa kusimama na bastola mlangoni kulikuwa na shida gani?

Shahidi: Sikuona shida yoyote lakini walisha ni Alert kabla kuwa wakiona siwapi ushirikiano basi hali ya amani itakuwa imeharibika.

Kibatala: ACP kingai anasema alikufuata Central Police Station akakupandisha floor ya kwanza na kwenda kukuchukua maelezo

Shahidi: Siyo kweli

Kibatala: kama ungepewa nafasi wakati wa kutoa Maelezo ungemuita au usingemuita Mwajiri wako Freeman Mbowe?

Shahidi: Ningemuita..

Kibatala: kama Freeman Mbowe asingekuwa na nafasi, mwingine wa kumuita kukusaidia kwenye matatizo?

Shahidi: ningemuita mke wangu

Kibatala: Mke wako yupo wapi?

Shahidi: Chalinze

Kibatala: nakurudisha Moshi, Mahabusu ilimwagiwa maji, tatizo lako lipo wapi, Je kama wanasafisha?

Shahidi: nilijua mateso yanaendelea kwa sababu sikuweza kulala tena

Kibatala: ukawa unafanyeje?

Shahidi: nilikuwa nimekaa usiku kucha

Kibatala: Ulipewa chakula lini na wapi?

Shahidi: TAZARA

Kibatala: Moshi hukupewa chakula?

Shahidi: Sikupewa chakula Moshi..

Kibatala: Ulipewa chakula TAZARA muda gani?

Shahidi: Chakula cha mchana cha mahabusu wote, ugali na mboga za majani

Kibatala: Mwambie Mheshimiwa Jaji kama wakati wote ulipokuwa Moshi ulipewa chakula

Shahidi: Hapana sikupewa chakula

Kibatala: Wanasema mlipokuwa Himo, gari baada ya kuharibika mkala chakula na kuja Dar es salaam, je kwa kumbukumbu zako, uliwahi kula chakula HIMO?

Shahidi: Hapana

Kibatala: Je unakumbuka kama ulibadilisha na kupanda gari nyingine?

Shahidi: Sikumbuki, nakumbuka baada ya kutoka Moshi nilikuja kushuka baada ya kufila DSM

Kibatala: Unasema Moshi ulipigwa na kuteswa kama mishikaki au popo kwenye chuma, ulipigwa kipigo gani?

Shahidi: Nilikuwa napigwa kwenye unyayo, magotoni, nikiwa miguu juu kichwa chini

Kibatala: Zoezi lilichukua muda gani?

Shahidi: lilichukua dakika 45

Kibatala: husianisha kati ya kipigo chako na kwenye nyayo na hilo chuma na kushindwa kutembea mpaka kurudishwa mahabusu, ikabidi wakuburuze..

Shahidi: Kuna uhusiano nilipopigwa miguu ilivimba nikawa nashindwa kukanyaga chini, nikikanyaga chini miguu inakuwa inauma kama nimepigwa shoti

Kibatala: Kupigwa kuna uhusiano gani na kupoteza fahamu kwenda kwenye ubongo?

Shahidi: Kupigwa kwenye unyayo ni TORTURE unayasikia maumivu kutoka kwenye miguu mpaka kichwani

Kibatala: Hapa kuna maelezo, kielelezo nataka kujua kweli ulisaini maelezo yako?

Shahidi: nilishasema mwanzo kuwa nilitaarifiwa tangu mwanzo, endapo nitaenda kinyume, nitakuwa nayatafuta mengine, kwa kuwa nilishakuwa nimeteswa sana ikabidi kukubaliana nao..

Kibatala: unasema suruali uliyovaa leo ndiyo suruali uliyovaa 05 August ambayo haina (Ruksi) Je, dhumuni lako lilikuwa kuja kuonyesha makusudi mahakama?

Shahidi: Hapana kwa sababu leo sikuwa nimejiandaa kuja kutoa ushahidi, wala sikutegemea kuwa leo nitatoa ushahidi

Kibatala: kwani kwa unavyojua upande wa mashtaka watakuwa na mashahidi wangapi?

Shahidi: Mashahidi 7

Kibatala: leo ulitegemea nini?

Shahidi: waendelee kutoa ushahidi..

Kibatala: Mheshimiwa Jaji ni hayo tu..

--------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------

Taarifa kwa wasomaji wote wanaofuatilia ukurasa huu, Sasa hapa tutakuwa tunatumia (W.S) kama ufupisho wa neno "WAKILI WA SERIKALI"... Ahsanteni..
---------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------

Jaji: Upande wa Mashtaka

W. S:Unaitwa Adam Hassan Kasekwa?

Shahidi: Naitwa Adam Hassan Kasekwa na Pia kama nilivyomwambia Jaji

W. S: Ulikuwa unafanya kazi gani

Shahidi: ni MWANAJESHI, KOMANDOO

W. S: Wewe ni KOMANDOO mahiri sana?

Shahidi: KOMANDOO.. Mahiri gani?

W. S: Umahiri wa ujuzi?

Shahidi: Ndiyo

W. S: umesema ulikuwa VIP PROTECTION?

Shahidi: ndiyo

W. S:Ulikuwa unaajiriwa kwenda vitani?

Shahidi: Hapana Niliajiriwa kwenda kumlinda MBOWE

Wakili Mallya: OBJECTION Mheshimiwa naomba distance kati ya wakili na mteja wangu, kwa sababu za ki Afya akae mbali kidogo, wakili amevua barakoa makusudi

Jaji: Sababu za Ki Afya KAA MBALI KIDOGO

W. S: Kwakuwa wewe ni Komandoo uliyefuzu na miongoni mwa mafunzo uliyofuzu ni kuvumilia hali ya mateso?

Shahidi: NDIYO, NA NDIYO MAANA UNANIONA HAPA

W. S: Makomandoo ni watu siyo legelege ni watu wenye kuhimili shida mazingira watakayo kumbana nayo?

Shahidi: NDIYO

W. S: Kwa kuwa +Makomandoo ni watu wanaohimili shida ni nadra kumkuta Komandoo analalamika

Shahidi: Si Kweli

Jaji: wakili,Hebu rudia swali unaposema hali ngumu, hali ngumu, ni hali ngumu ya Maisha, Fedha au Mateso?

W. S: Kwa kuwa makomandoo ni watu wanaohimili Shida ni nadra kumkuta Komandoo analalamika

Shahidi: nimekwambia NDIYO, kwa Sababu MAKOMANDOO na wao wanadamu..

W. S: Kwa hiyo Unataka kuiambia mahakama kwamba makomandoo si wastahimilivu

Shahidi: Ndiyo

W. S: Katika mafunzo ya ukomandoo ulifuzu kukaa na njaa kwa muda mrefu?

Shahidi: Ndiyo

W. S: Hatutegemei kusikia unalalamika kukaa njaa kwa muda wa siku 2

Shahidi: Si Kweli

W. S: Ni kweli Kwambaaaaaaa

Mallya: Objection kama nimekuelewa Rulling yako ya maswali kuanza, ni kweli ilikuwa inatuhusu wote

W. S: Unakumbukumbu nzuri sana

Shahidi: Ndiyo kabisa

W. S: Ulikuwa unakumbuka mlolongo wa kesi vizuri sana?

Shahidi: Ndiyo sahihi kabisa

W. S: Yaliyojiri kule Moshi na kule Mbweni ulimuuliza wakili wako kabla kesi haijaanza

Shahidi: Si kweli

Jaji: Subiri kidogo, Shahidi ukiona kichwa kinapata moto unaeeza kuomba maji, naona unayo uongezwe maji

Shahidi: Ndiyo niongezewe mheshimiwa

W. S: Kwamba mpaka kesi inaanza ulikuwa hujamwambia wakili wako kuhusu yaliyotokea Moshi mpaka tarehe 09 Mbweni?

Shahidi: Sijamwambia

W. S: ulimweleza wakati gani?

Shahidi: wakati kesi inatolewa Kisutu

W. S: Kuanzia siku Ramadhani Kingai anatoa ushahidi mpaka Leo hii unatoa ushahidi wako wakili wako alikuwa anafahamu mambo yaliyokusibu?

Shahidi: sahihi kabisa

W. S: Ulishawahi kutuhumiwa makosa ya utovu wa nidhamu ukiwa Jeshini?

Shahidi: Hapana

W. S: Ulipokuwa Jeshini wakati wa misheni DRC unazitambua kamati za kinidhamu zilizopo Jeshini?

Shahidi: Ndiyo

W. S: Unapotuhumiwa kwa jambo lolote unatakiwa kupewa Haki ya KUSIKILIZWA?

Shahidi: ni HAKI ndiyo..

W. S: kule Jeshini wakikutuhumu wakakupeleka kwenye kamati, kwanini wewe lazima uwepo?

Shahidi: Unapoitwa kwenye Jambo kama hilo, wanataka kujua kutoka upande wako

W. S: Usipoitwa utakuwa umenyimwa Haki?

Shahidi: NDIYO

W. S: kwa hiyo haifai Kumtuhumu Mtu wakati haupo

Shahidi: ndiyo

W. S: Hata wewe huwezi kukubali tunazungumza maneno dhidi yako, Kasekwa kafanya 1,2,3,4,5 Wakati wewe haupo

Shahidi: Hilo mimi siwezi kulijibia, inategemea hao wenyewe

W. S: Wewe kazi yako kujibu, lazima ujibu.

Jaji: Msijibizane wenyewe kwa wemyewe, Ni vema Wakili kuangalia kama nimemaliza kuandika

W. S: Mimi nataka kujua Jambo DOGO tu, Kitendo kikifanyika dhidi yako halafu watu wakakaa wenyewe bila wewe kuwepo, Je ni Haki?

Shahidi: ni sahihi

W. S: Kama hali ipo hivyo kama Usilopenda kufanyiwa wewe Usimfanyie Mwenzio,Kingai wakati anatoa ushahidi wake wakati wanakukamata wewe tarehe 05, RAU Madukani, walipokukamata walikupekua na wakakuta na KETE 58 za Madawa ya kulevya na wakakukuta pistol

Shahidi: Ndiyo alivyoeleza unayarudia tu yote

W. S: Usilete kujua sana

Mallya: OBJECTION maneno hayo kujua sana yana lengo yakumtoa shahidi wangu nje ya lengo

Jaji: Maneno hayo ya kujua sana nafikiri yasirudiwe tena

W. S:: Wakati wa ushahidi wa Kingai alieleza kuwa alikuandikisha MAELEZO na akaita mashahidi wawili wanawake wakati wa upekuzi

Shahidi: Ndiyo alieleza

W. S: Kingai hakueleza suala lolote la kuhusu kukupiga?

Shahidi: ni sahihi

W. S: Wakili wako hakumweleza Kingai Kuwa Wewe Kingai ulimuwekea Madawa ya kulevya na Pistol

Mallya: OBJECTION wakili anauliza mambo ambayo mimi na mteja tulikuwa tunaongea

Jaji: Upande wa mashtaka jibu

W. S: Nilichomuuliza kuhusu kutoka moshi Mpaka hapa siyo jambo la siri

W. S: nimeuliza kwamba Kingai hakuhojiwa unayoyaleta leo..

Jaji: Sijaona tatizo katika namna ambayo wakili wa serikali amemuuliza shahidi

W. S: Shahidi narejea tena maneno yangu

Adhana inapigwa,Jaji anaomba tusubiri Kidogo

------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------

Jaji tunaweza KUENDELEA.....

W. S: Kingai wakati anatoa ushahidi wake hakuulizwa suala lolote kuhusiana kukutilia wewe madawa ya kulevya na kukuwekea wewe Pistol na siku ile walikupiga eneo lile la RAU Madukani

Shahidi: SIVYO

W. S: Kwa hiyo hali ilikuwaje?

Shahidi: aliulizwa na wakili Kibatala

W. S: Kingai anasema wakati wana kukamata uliwapa ushirikiano, wakafanya walichofanya, si ndivyo walivyosema?

Shahidi: Sijaelewa

Mallya: Maneno ya KWELI au SI KWELI ulishayatolea muongozo

Shahidi: Si kweli nilisikia hapa ingawa mimi siyo Mwanasheria yaliulizwa

W. S: Maneno haya ni sawa na kusema kukamatwa na kupigwa ni Kinyume na sheria na vile vile na kupigwa ni kinyume cha sheria

Shahidi: Sijakuelewa

Jaji Hebu subiri Kidogo, Adamoo upo sawa?

Shahidi: nipo timamu Mheshimiwa Jaji

Jaji: Mallya

Mallya: Shahidi yupo sawa sawa

JAJI: nadhani nimeweka bayana yasitumike Mwanzoni inakuwa kama mangigizo ila mwishoni yanaweza kutumika.

W. S: Leo hii ndiyo mara ya kwanza Mahakama inaelezwa wakati unakamatwa palikuwa na hali ya vurumai, Madawa yakawekwa kiunoni kwako, Pistol Ikawekwa kiunoni kwako pia ulipigwa

W. S: Namwambia mtu kitendo cha kukamata na kumpiga mtu ni kinyume na sheria, na huyo Bwana akasema ni kweli sheria haziruhusu kumpiga mtu wakati unamkamata, Swali linakuja kitendo cha kumwambia kukamatwa na kupigwa ni kinyume na sheria ni vitendo tofauti?

Shahidi: vinaoana

Jaji: Wakili usiweke story ndefu sana, Uliza maswali Direct, Usizunguke sana mtaulizana maswali mpaka asubuhi na bado sitoelewa, Go straight...

W. S: Kitendo cha kukiuka utaratibu na kusema ni Kitendo..

Shahidi: Hakuna Tofauti

W. S: Kingai kasema mlipofika kituoni mkawashusha wakina mama mkarudi mitaani kumtafuta Moses Lijenje

Shahidi: Ndivyo alivyoeleza

W. S: Kingai akasema kuwa baadae wakawarudisha kituoni baada ya kumkosa Moses Lijenje

Shahidi: Ndivyo alivyoeleza

W. S: Ni kweli kuwa Kingai hakuhojiwa kuwa alikuwa anadanganya, isipokuwa mlipofika kituoni mkaenda kuteswa,vHili suala hakuhojiwa wala hukuhojiwa

Shahidi: Sijakuelewa, kuhojiwa na nani

W. S: Wakati mnamuuliza Kingai maswali kama haya ya Dodoso

Jaji: nafikiri kuna tatizo hapa na hali haijabadilika, bado wakili unaweka explanation, ndiyo maana kila wakati anarudi kusema rudia swali sijakuelewa.

Mahakama Kimyaaaaaa

Jaji: Mkishindwa kueleza nitasema tuje Jumatatu

W. S: Kwanini maswali mengi ninayokuuliza hutaki kujibu

Shahidi: Yana, mlolongo, Mreeeeefu swali halijukikani lipo wapi..

Mahakama: Wote kichekooooo

W. S: Wakati Kingai anahojiwa hakuulizwa kuhusu wewe kuteswa

Shahidi: si kweli, alihojiwa

W. S: Umeleeza kuwa walikutesa wakawa wanakuchoma na bisibisi matakoni na tumboni

Shahidi: Kweli

W. S: kwa hiyo baada ya kuchomwa na bisibisi ulitokwa na damu nyingi sana!

Shahidi: Si kweli

W. S: Kwa kuwa hukutokwa na damu nyingi Majeraha yalikuwa madogo sana

Shahidi: sahihi

W. S: Kama majeraha haya yalikuwa Madogo, Uliweza kuyavumilia?

Shahidi: sahihi

W. S: Majereha hayo Madogo ambayo uliyavumilia hayakuwa kitu kikubwa

Shahidi: Yalikuwa kitu kikubwa ndiyo maana nimeiambia mahakama

W. S: Mwanzo ulisema Kitu kilichokufanya Majeraha yalikuwa madogo, sbabu ya kuvumilia ilikuwa sababu hayakutoa damu au Kwa sababu ya mazingira

Mallya: OBJECTION kumuharasi Shahidi kwa Jambo ambalo Shahidi ameshajibu ni kupoteza muda wa mahakama

W. S: Sawasawa Mheshimiwa

W. S: Kwa sababu majeraha yale hayakutia Damu hayakuweka Vidonda kwenye Matako yako

Shahidi: Sahihi

W. S: Ulichomwa sana bisibisi kwenye matako yako, Damu haikotika na majeraha hayakutoka, Je ni kweli au si Kweli

Shahidi: Kwel

Jaji: Ndiyo

W. S: Kwa ruhusa yako naomba tushauriane hapa

Jaji: sawa na ukirudi tumalize juu ya bisibisi za matako

W. S: Nishamliza Mheshimiwa Jaji

Mahakama Kimyaaaaaa Kidogo

W. S: Wale waliokuwa wamekuzingira na kukufanyia uhalifu tarehe 05 hakuna hata mmoja uliweza kumtambua?

Shahidi: Ni kweli kabla ya pale sikuwa namfahamu hata mtu mmoja

W. S: hukuwahi kuwaona kabla ya hapo?

Shahidi: Ni sahihi

W. S: Kabla ya hapo hukuwahi Kugombana, kurushiana maneno kwa namna yoyote ambayo inaweza kuleta chuki?

Shahidi: Sahihi

W. S: Sikuwahi kuwa na kinyongo nao kabla ya wakati ule

Shahidi: Sahihi kabisa

W. S: Watu hawa licha ya kuwa huna kinyongo, Walikuja kukufanyia UBAYA

Shahidi: ndiyo

W. S: Hakika HALI hii ni ya kustaajabisha sana

Mallya: OBJECTION maneno hayo anayotumia wakili anajaribu kumlisha maneno kabla ya Swali

Jaji: nafikiri SHAHIDI Mwenyewe anaweza KUJIBU

Shahidi: ni kweli

W. S: Watu waliokuvamia siku ile, ukiachia Ramadhani Kingai na Mahita wengine wote huwakumbuki wala huwafahamu?

Shahidi: si kweli

W. S: kwa hiyo wote unawakumbuka na kuwafahamu

Shahidi: Siyo wote

W. S: ieleze MAHAKAMA kuanzia siku ile wanakukamata RAU Madukani tarehe 05 mwezi wa 8, Mpaka tarehe 07 Mwezi 08 hukuwa unawafahamu majina yao, Ndiyo maana umekuja kuwafahamu hapa wakina Ramadhani Kingai kwa sababu hakukwambia majina yao

Shahidi: Sahihi Kabisa

kimya kidogo wanashauriana Upande wa Serikali

Jaji: nafikiri inatosha kwa leo Siku ya Jumatatu tunaeweza kuendelea

Jaji: upande wa utetezi mnasemaje?

Kibatala: Tutakuwa na nafasi

W. S: Tutakuwa na nafasi Mheshimiwa

Jaji anaandika kidogo, Mahakama ipo kimya

Jaji: tutakuwa na shahidi mwingine upande l wa Utetezi?

Mallya: Ni Mshitakiwa

Jaji anainama na kuendelea kuandika, Mahakama ipo kimya

Jaji: nahairisha mpaka Jumatatu, kwa sababu ya MUDA umekuwa changamoto, natarajia tutaanza SAA 3

Mpaka Jumatatu, nawashukuru Mawakili wa pande zote pamoja na kuvutana

NAWASHUKURU WOTE WANAOTUMIA MUDA WAO KUFUATILIA SHAURI HILI

Jaji ananyanyuka anatoka..
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…