Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,771
- 41,027
Hiki kisa kinakuja, Ukae chini tulia,
Ni cha Sungura mmoja, hapa nawasimulia,
Ilikuwa siku moja, njaa imemshikia,
Njaa imemshikia, Sungura nawaambia!
Ni Sungura yule yule, aliyezizira ndizi!
Ni yule wa mwaka ule, aliyeleta mapozi,
Tuliyemsoma shule, miaka ile ya enzi,
Miaka ile ya enzi, Sungura nawaambia!
Karudi kakasirika, huku tumbo languruma,
Tumbo lake kalishika, huku meno kayauma,
Jasho linamdondoka, huku anahema hema,
Huku anahema hema, Sungura nawaambia!
Sungura akaondoka, kusaka matunda yale,
Akaondoka na shoka, na mkuki na mishale,
Akawaomba mahoka, na akachanjwa na chale,
Na akachanjwa na chale, Sungura nawaambia
Sungura alitafuta, na kutafuta mitini,
Akatafutafuta, msituni mashambani,
Na mwisho akayapata, matunda alotamani,
Matunda alotamani, Sungura nawaambia.
Akayaona mtini, hakuuliza ya nani,
Yameiva kama nini, kajiambia moyoni,
Tunda hili tunda gani, hakuuliza kichwani,
Hakuuliza kichwani, Sungura Nawaambia!
Karuka tena karuka, mwishowe kayafikia,
Ishirini kayashika, Sungura kashangilia,
Tabasamu likatoka, kacheka hata mkia!
Kacheka hata mkia, Sungura nawaambia!
Katafuna kwa haraka, na kumeza pole pole,
Akayala akicheka, akilamba na vidole,
Na njaa ikamtoka, tumbo limejaa tele,
Tumbo limejaa tele, Sungura nawaambia!
Mwishowe akasinzia, na ndoto ikamjia,
Mbali akakumbukia, ndizi alizoachia,
Bahati kajipatia, matunda amejilia,
Matunda amejilia Sungura nawaambia!
Mara kaanza kulia, na ndoto ikapotea,
Tumbo ameshikilia, hakuna cha kuchekea,
Maumivu asikia, huku anachechemea,
Huku anachechemea, Sungura nawaambia!
Kakimbia kijijini, huku analia lia,
Kagaragara na chini, jamani anaumia,
Kaulizwa shida nini, kisa kawasimulia,
Kisa kawasimulia, Sungura nawaambia!
Kaulizwa tunda gani, alilokula jamani,
Akasema mti gani, mapovu yako kinywani,
Kumbe ya sumu watani, yamtokea puani,
Yamtokea puani, Sungura nawaambia!
Akasema nimekoma, nisaidieni jamani,
Nimekoma vya kukoma, mengine sitotamani,
Sasa nimepata homa, hainitoki mwilini,
Hainitoki mwilini, Sungura nawaambia!
Akapoteza fahamu, mauti yako njiani,
Kumbe kali ile sumu, hakuna dawa porini,
Masikini marehemu, yamemkuta jamani,
Yamemkuta jamani, Sungura nawaambia!
Kaditamati natama, beti zangu zimegoma,
Ya Sungura nimesema, ya tamaa isokoma,
Tamaa ina gharama, yaweza toa uzima,
Yaweza toa uzima, Sungura nawaambia!
Na. M. M. Mwanakiiji (Sauti ya Kijiji)
Ni cha Sungura mmoja, hapa nawasimulia,
Ilikuwa siku moja, njaa imemshikia,
Njaa imemshikia, Sungura nawaambia!
Ni Sungura yule yule, aliyezizira ndizi!
Ni yule wa mwaka ule, aliyeleta mapozi,
Tuliyemsoma shule, miaka ile ya enzi,
Miaka ile ya enzi, Sungura nawaambia!
Karudi kakasirika, huku tumbo languruma,
Tumbo lake kalishika, huku meno kayauma,
Jasho linamdondoka, huku anahema hema,
Huku anahema hema, Sungura nawaambia!
Sungura akaondoka, kusaka matunda yale,
Akaondoka na shoka, na mkuki na mishale,
Akawaomba mahoka, na akachanjwa na chale,
Na akachanjwa na chale, Sungura nawaambia
Sungura alitafuta, na kutafuta mitini,
Akatafutafuta, msituni mashambani,
Na mwisho akayapata, matunda alotamani,
Matunda alotamani, Sungura nawaambia.
Akayaona mtini, hakuuliza ya nani,
Yameiva kama nini, kajiambia moyoni,
Tunda hili tunda gani, hakuuliza kichwani,
Hakuuliza kichwani, Sungura Nawaambia!
Karuka tena karuka, mwishowe kayafikia,
Ishirini kayashika, Sungura kashangilia,
Tabasamu likatoka, kacheka hata mkia!
Kacheka hata mkia, Sungura nawaambia!
Katafuna kwa haraka, na kumeza pole pole,
Akayala akicheka, akilamba na vidole,
Na njaa ikamtoka, tumbo limejaa tele,
Tumbo limejaa tele, Sungura nawaambia!
Mwishowe akasinzia, na ndoto ikamjia,
Mbali akakumbukia, ndizi alizoachia,
Bahati kajipatia, matunda amejilia,
Matunda amejilia Sungura nawaambia!
Mara kaanza kulia, na ndoto ikapotea,
Tumbo ameshikilia, hakuna cha kuchekea,
Maumivu asikia, huku anachechemea,
Huku anachechemea, Sungura nawaambia!
Kakimbia kijijini, huku analia lia,
Kagaragara na chini, jamani anaumia,
Kaulizwa shida nini, kisa kawasimulia,
Kisa kawasimulia, Sungura nawaambia!
Kaulizwa tunda gani, alilokula jamani,
Akasema mti gani, mapovu yako kinywani,
Kumbe ya sumu watani, yamtokea puani,
Yamtokea puani, Sungura nawaambia!
Akasema nimekoma, nisaidieni jamani,
Nimekoma vya kukoma, mengine sitotamani,
Sasa nimepata homa, hainitoki mwilini,
Hainitoki mwilini, Sungura nawaambia!
Akapoteza fahamu, mauti yako njiani,
Kumbe kali ile sumu, hakuna dawa porini,
Masikini marehemu, yamemkuta jamani,
Yamemkuta jamani, Sungura nawaambia!
Kaditamati natama, beti zangu zimegoma,
Ya Sungura nimesema, ya tamaa isokoma,
Tamaa ina gharama, yaweza toa uzima,
Yaweza toa uzima, Sungura nawaambia!
Na. M. M. Mwanakiiji (Sauti ya Kijiji)