Kitabu: Unyonge wa Mwafrika.

Kitabu: Unyonge wa Mwafrika.

Lycaon pictus

JF-Expert Member
Joined
Jan 31, 2021
Posts
9,189
Reaction score
16,128
Leo ni siku ya kiswahili duniani. Maktaba app ingependa tuanze kusomea moja ya kitabu kipatikanacho ndani ya Maktaba app. whatsapp 0715278384.

UTANGULIZI 12 Nokora mpumbavu
Hali ya Mtumwa
Kawambwa na makapu ya karanga
Tony mwana wa D. C.
Kijibwa cha mzungu
Togolo na mavazi ya Kijarumani
Kanga hatagi ujani 199 Mtu kwao
Subeti na watu wadogo
Chai ya Kandambili
Urembo wa ndonya
Chambo cha pesa
AZIMIO LA ARUSHA LASEMA
 
UTANGULIZI

Katika Azimio la Arusha tumesema kwamba tunapigana vita, vita vya kuleta heshima na usawa wa Watanzania. Tumeonewa kiasi cha kutosha, tumenyonywa kiasi cha kutosha na tumepuuzwa kiasi cha kutosha. Sasa tunataka mapinduzi; mapinduzi ya kuondoa unyonge tusionewe tena, tusinyonywe tena wala tusipuuzwe tena. Hii ndio kazi iliyoko mbele yetu; ndio mche tunaotakiwa kuulinda na kuupalilia. Rushwa ni adui wa Azimio. Na rushwa inajificha katika hali nyingi. Kama wana-TANU tunapaswa kujikumbusha daima ahadi yetu: "Rushwa ni adui wa haki; sitapokea wala kutoa rushwa."

Kimetolewa na East African Publishing House, SLP 3209,
Dar es Salaam na kupigwa chapa na Printpak Tanzania Ltd.

TANGANYIKA AFRICAN NATION UNION

DARUBINI 1

AZIMIO LA ARUSHA LASEMA

Tumeonewa kiasi cha kutosha;
Tumenyonywa kiasi cha kutosha;
Tumepuuzwa kiasi cha kutosha.
Unyonge wetu ndiyo uliotufanya tunyonywe, tuonewe, na kupuuzwa.
Sasa tunataka mapinduzi. Mapinduzi ya kuondoa unyonge ili tusionewe tena, tusinyonywe tena na wala tusipuuzwe tena.
 
Nokora mpumbavu

Iko hadithi ya nokora mpumbavu. Nokora ni mnyapara wa watumwa; lakini yeye mwenyewe pia ni mtumwa, ila kavikwa kilemba cha ukoka kupewa cheo cha kuwaangalia wenzake. Basi alikuwako Mwarabu mmoja tajiri sana jina lake El-Mahdi. Alikuwa na shamba kubwa na minazi na mikarafuu, akafuga na ng'ombe; pia alikuwa na watumwa wengi. Akamteua mtumwa mmoja jina lake Mondo, na kumfanya nokora wake.

Basi Mondo kupewa unokora kajiona mtu mkubwa sana; akawakataza wenzake wasimwite jina la Mondo tena, maana hilo ni la kitumwa, akajipachika jina la Maftaha. Mondo akawa mkali kwa wenzake kuliko hata El-Mahdi mwenyewe; asubuhi-subuhi huwaamsha wenzake na kuwatia shambani kwa viboko. Kwa kikiri za Mondo, na mvua kunyesha vizuri, mavuno yakaja mazuri sana mwaka ule, na El-Mahdi akazidi kutajirika. Basi El-Mahdi akamsifu sana Mondo, lakini kwa maneno matupu, kwa kazi nzuri ya mwaka ule, bali faida yote ya mwaka ule akaimeza mwenyewe. Maana ingawa Mondo alivimba kichwa kwa sifa za El- Mahdi, na ingawa amewakataza watumwa wasimwite jina lake la zamani, wamwite Maftaha, lakini El-Mahdi alimwona yule Mondo, ni mtumwa tu.

Wale watumwa wengine wakachoka na vitimbi vya Mondo, wakafanya shauri watege, lakini wamweke doria, ili akitokea tu waanze kufanya kazi, tena kwa vishindo na kelele nyingi, na halafu wamtolee shida yao.

Mara doria kamwona Bwana Maftaha anakuja. Ikaanza kazi, kwa kelele nyingi na majembe kugongana. Bwana Maftaha akaridhika kazi inakwenda barabara, akawaambia wapumzike kidogo. Basi mmoja wa watumwa akamsifu sana Bwana Maftaha kwa upole na upendo wake, akasema kazi ingeongezeka maradufu, kama tu wangepata chakula. Hapo watumwa wote wakaangua kilio, "Njaa, njaal"

Ikawa Bwana Maftaha, kwa sifa alizopata kwa watumwa na kwa El-Mahdi, hakutaka shauri hili limshinde, akatoka mbio hadi kwa El-Mahdi. Kufika tu na yeye akamlilia Bwana Mkubwa, na huku chozi linamtoka, "Watumwa tuna njaa!"

El-Mahdi akamwona Mondo kama juha tu, lakini kwa kuwa alitaka kumridhisha kidogo ili kazi iendelee, basi akampa chakula ili kazi iendelee. Watumwa wakafurahi mno, na kumsifu Bwana Maftaha pamoja na El-Mahdi, eti kwa ajili ya kuwapenda sana.

Siku ya pili watumwa wakatumia hila ile ile, safari hii wakajidai wanaharisha. Wakaangusha kilio, "Tunaharisha, tunaharisha!"

Bwana Maftaha naye akakichukua kilio kile, mbio hadi kwa El-Mahdi, "Wanaharisha, wanaharisha!" na huku machozi yakimtoka. Lakini safari hii El-Mahdi hana dawa, akamwamuru Mondo arudi awaambie wasubiri kidogo, atafute dawa. Alipotamka neno hilo tu watumwa wakaja juu, wakawalaani vikali Bwana Maftaha na El-Mahdi pia.

Haya ndiyo yakawa mazoea yao. Wakitaka cho chote kwa El-Mahdi hulia kwa Maftaha, na Maftaha naye hupeleka chozi lile kwa El-Mahdi.
Hatimaye El-Mahdi akafa, lakini hakuwa na mrithi; basi shamba likawa mikononi mwa watumwa wake, likawa shamba lao. lla, kwa sababu ya mazoea yao ya zamani, mambo yakawa yale yale. Wakiwa na njaa huanza kulia, na Maftaha naye huanza kulia, "Njaa, njaa!" Lakini, kwa sababu sasa El- Mahdi kesha kufa, kilio chao hakikuweza kuwapatia, japo yale makombo ya zamani. Shamba wanalo, lakini dhiki ikazidi sana, mpaka walipozindukana na kutambua kuwa sasa shamba ni lao; na kazi yao ya sasa ni kulilima shamba, na kugawana matunda ya juhudi zao kwa haki: siyo tena kupeleka kilio kwa marehemu El-Mahdi.
Na sisi Watanzania zamani wote tulikuwa watumwa; watumwa wa Mwingereza na Mjarumani pia. Tulikuwa na manokora wetu enzi hizo, waliosaidia kutawala, waliojidhania kuwa wamepata u-Maftaha, kumbe Mondo tu. Kama Maftaha, kazi yao ilikuwa kupeleka mbele kilio cha wananchi: "Wanataka barabara, wanataka shule, wanataka hospitali."
Basi, leo El-Mahdi kafa; mkoloni kaondoka, wala harudi tena. Lakini Maftaha bado wapo, ndiyo sababu Baba wa Taifa anasisitiza wakuu wa Serikali wasiwe tena watu wa kutawala, bali watu wa kuhimiza maendeleo vijijini. Huu si wakati tena wa wanyapara wetu kulialia kama Maftaha; huu ni wakati wa kuwaeleza wananchi watumie ardhi yao waliyopewa na Mwenyezi Mungu. Kama wananchi wanataka maji, basi wafanye kazi ya kuyaleta maji; kama wanataka barabara, basi walime barabara.
Na sisi je, tuliokuwa nyuma ya mwenzetu Maftaha? Sisi tulikuwa na mawazo ya kitumwa siku nyingi. Zamani tulikuwa tunamfanyia kazi El-Mahdi, lakini leo tunafanya kazi kwa manufaa yetu sisi wenyewe, na ya watoto wetu. Tusimweke doria tena kutazama kama Maftaha anakuja, ndipo tufanye kazi; bali tufanye kazi kwa roho moja, tujisaidie wenyewe, kwa kuwa sasa nchi hii ni yetu.
 
Hali ya Mtumwa


Yasemekana kwamba siku hizi utumwa umekwisha duniani. Lakini hadithi za utumwa bado tunazikumbuka. Mtu aliye utumwani hutambua kuwa hana njia tena ya kuondoka; kwa hiyo hujitafutia raha katika adhiki yake. Mtumwa hutumikishwa sana, lakini hapendi kufanya kazi, maana anajua kwamba jasho lake halimfaidii yeye, ni faida ya Bwana wake tu. Tena akipata nafasi ya kutega, basi hutega sana.
Mtumwa hujipendekeza - pendekeza, apendeke japo kwa nokora, ili yeye aonekane bora kuliko watumwa wengine: wenzake wafanye kazi, yeye apate visingizio. Mtumwa hajui usawa; anaona kuna binadamu wa aina mbili; kuna mabwana, na kuna watwana. Basi madhali yeye ni mtumwa, humtazama sana El-Mahdi, akautamani sana u-Bwana.
Ndiyo sababu Mondo akajigeuza jina kujiita Maftaha, kwa sababu ya kuupata U-Nokora. Hayo ndio mawazo ya kitumwa. Hafikirii lini atapata nafasi ya kujifanyia kazi ya kujitegemea, awe sawa na binadamu wengine; ila anafikiria lini atapata nafasi ya kuwa Bwana, awatawale wengine.
Hata wakati anapoachiwa huru, mawazo yake ni yale yale tu. Japo zamani alikuwa akifanya kazi kucha-kutwa, lakini leo kazi hawezi tena. Kushughulika na kazi ya kitumwa, anatamani sana amwige El- Mahdi, akae ghorofani atoe amri, na wengine wafanye kazi. Huo ndio uhuru.
Mtumwa alikuwa akimtazama sana El-Mahdi alivyokuwa akiishi, akayahusudu sana maisha yale; na yeye sasa madhali kesha kuwa huru, basi uhuru ni kuwa namna ile; na kama hawi vile basi hulaumu. Kwa mtumwa uhuru maana yake ni kuwa Bwana; awe na watu kem-kém chini yake wanafanya kazi, yeye anatoa amri tu na kutafuna tambuu. Hayo ndiyo mawazo ya kitumwa.
Na nchi zetu kadhalika. Nchi zetu zilikuwa zikitawaliwa na wakoloni wa aina mbali mbali; lakini wote wakoloni tu, wametuweka utumwa. Chini yao sote sisi tulikuwa watumwa. Wote tulikuwa tunawafanyia kazi wakoloni, si kwa faida yetu, bali kwa faida yao. Baadhi yetu tuliishi kwa kujipendekeza- pendekeza kwa wazungu. Akija mzungu basi chifu hutengeneza kapu la mayai, ampe mzungu ale anenepe, wakati watoto wetu wanaugua kwa kukosa chakula bora. Hayo hatujasahau bado. Yote ni kujipendekeza tu, ili aonekane bora kuliko wenzake.
Na dada akizaa mtoto chotara hujisifu sana, maana kaambatana na uzungu; na chotara huwa na makeke kuliko hata mzungu mwenyewe. Maana tulipokuwa tunatawaliwa tulikuwa na mawazo ya binadamu namna mbili. Kuna weupe wanaotawala, na sisi weusi tunaotawaliwa; na kwa fikara za kitumwa wengine tulikuwa tunatamani sana tufanane-fanane na wazungu.
Hata tulipojitawala baadhi yetu tukabakia na mawazo yale yale. Tukabaki na fikara za u-Bwana na utwana; na kila mmoja anataka awe Bwana. Kazi za mikono basi tena, maana hizo ni za kitumwa. Anayesoma kidogo kesha kuwa malaika, ameumbika kuwatawala wengine tu. Mtu akihimiza kazi, japo za ofisini, huitwa mkoloni, maana uhuru ni kukaa bure, kama El-Mahdi.
Bwana Mkubwa anayehimiza kazi naye hutamani awe kama mzungu, bora kuliko watu weusi, na mitemba sita-sita. Tukausahaulia mbali usawa tulioukubali katika misingi yetu ya TANU na Afro-Shirazi. Hayo ndio maradhi ya kutawaliwa.
Ndipo serikali ilipolazimika kutafuta dawa ya maradhi hayo. Serikali ikaanzisha Jeshi la Kujenga Taifa, au National Service, ili kujaribu kusawazisha mawazo hayo, yarudi kwenye usawa wa binadamu. Lakini, kama desturi ya kina Maftaha, wengine walipinga, maana dawa yenyewe ni kali.
Mtu ambaye zamani ulikuwa unatoa amri, sasa ujidhili upokee amri sawa na mwenzio; mtu ambaye zamani ulikuwa unaamka saa mbili, ndipo upate maji ya kuoga, sasa unaamshwa saa 11 asubuhi, na hulali tena hadi saa nne za usiku, sawa na wenzako wote. Mnapokimbia mbio au kucheza gwaride, shahada yako haikufai, wala udaktari wako; zinahesabiwa mbio tu. Unafunzwa tena kufanya kazi; unafunzwa tena heshima na usawa wa binadamu.
Wananchi sasa wameanza kukubali usawa wa binadamu. Wale waliopitia katika Jeshi la Kujenga Taifa hawana tena fikara za ubwana na utwana, wana fikara za usawa na umoja. Na Jeshi la Kujenga Taifa limekuwa sasa mahali pa kujipatia moyo mpya wa kuendesha nchi yetu. Kurekebisha mawazo kwa vitendo ni jambo la maana sana. Lakini wako bado watu wachache wenye mawazo ya u-Bwana, na wanaofikiria cheo kuwa kama mali yao. Huo ndio ugonjwa wa kutawaliwa, yawapasa kutibiwa.
Dawa ya jipu ni kulipasua.
 
Nokora mpumbavu

Iko hadithi ya nokora mpumbavu. Nokora ni mnyapara wa watumwa; lakini yeye mwenyewe pia ni mtumwa, ila kavikwa kilemba cha ukoka kupewa cheo cha kuwaangalia wenzake. Basi alikuwako Mwarabu mmoja tajiri sana jina lake El-Mahdi. Alikuwa na shamba kubwa na minazi na mikarafuu, akafuga na ng'ombe; pia alikuwa na watumwa wengi. Akamteua mtumwa mmoja jina lake Mondo, na kumfanya nokora wake.

Basi Mondo kupewa unokora kajiona mtu mkubwa sana; akawakataza wenzake wasimwite jina la Mondo tena, maana hilo ni la kitumwa, akajipachika jina la Maftaha. Mondo akawa mkali kwa wenzake kuliko hata El-Mahdi mwenyewe; asubuhi-subuhi huwaamsha wenzake na kuwatia shambani kwa viboko. Kwa kikiri za Mondo, na mvua kunyesha vizuri, mavuno yakaja mazuri sana mwaka ule, na El-Mahdi akazidi kutajirika. Basi El-Mahdi akamsifu sana Mondo, lakini kwa maneno matupu, kwa kazi nzuri ya mwaka ule, bali faida yote ya mwaka ule akaimeza mwenyewe. Maana ingawa Mondo alivimba kichwa kwa sifa za El- Mahdi, na ingawa amewakataza watumwa wasimwite jina lake la zamani, wamwite Maftaha, lakini El-Mahdi alimwona yule Mondo, ni mtumwa tu.

Wale watumwa wengine wakachoka na vitimbi vya Mondo, wakafanya shauri watege, lakini wamweke doria, ili akitokea tu waanze kufanya kazi, tena kwa vishindo na kelele nyingi, na halafu wamtolee shida yao.

Mara doria kamwona Bwana Maftaha anakuja. Ikaanza kazi, kwa kelele nyingi na majembe kugongana. Bwana Maftaha akaridhika kazi inakwenda barabara, akawaambia wapumzike kidogo. Basi mmoja wa watumwa akamsifu sana Bwana Maftaha kwa upole na upendo wake, akasema kazi ingeongezeka maradufu, kama tu wangepata chakula. Hapo watumwa wote wakaangua kilio, "Njaa, njaal"

Ikawa Bwana Maftaha, kwa sifa alizopata kwa watumwa na kwa El-Mahdi, hakutaka shauri hili limshinde, akatoka mbio hadi kwa El-Mahdi. Kufika tu na yeye akamlilia Bwana Mkubwa, na huku chozi linamtoka, "Watumwa tuna njaa!"

El-Mahdi akamwona Mondo kama juha tu, lakini kwa kuwa alitaka kumridhisha kidogo ili kazi iendelee, basi akampa chakula ili kazi iendelee. Watumwa wakafurahi mno, na kumsifu Bwana Maftaha pamoja na El-Mahdi, eti kwa ajili ya kuwapenda sana.

Siku ya pili watumwa wakatumia hila ile ile, safari hii wakajidai wanaharisha. Wakaangusha kilio, "Tunaharisha, tunaharisha!"

Bwana Maftaha naye akakichukua kilio kile, mbio hadi kwa El-Mahdi, "Wanaharisha, wanaharisha!" na huku machozi yakimtoka. Lakini safari hii El-Mahdi hana dawa, akamwamuru Mondo arudi awaambie wasubiri kidogo, atafute dawa. Alipotamka neno hilo tu watumwa wakaja juu, wakawalaani vikali Bwana Maftaha na El-Mahdi pia.

Haya ndiyo yakawa mazoea yao. Wakitaka cho chote kwa El-Mahdi hulia kwa Maftaha, na Maftaha naye hupeleka chozi lile kwa El-Mahdi.
Hatimaye El-Mahdi akafa, lakini hakuwa na mrithi; basi shamba likawa mikononi mwa watumwa wake, likawa shamba lao. lla, kwa sababu ya mazoea yao ya zamani, mambo yakawa yale yale. Wakiwa na njaa huanza kulia, na Maftaha naye huanza kulia, "Njaa, njaa!" Lakini, kwa sababu sasa El- Mahdi kesha kufa, kilio chao hakikuweza kuwapatia, japo yale makombo ya zamani. Shamba wanalo, lakini dhiki ikazidi sana, mpaka walipozindukana na kutambua kuwa sasa shamba ni lao; na kazi yao ya sasa ni kulilima shamba, na kugawana matunda ya juhudi zao kwa haki: siyo tena kupeleka kilio kwa marehemu El-Mahdi.
Na sisi Watanzania zamani wote tulikuwa watumwa; watumwa wa Mwingereza na Mjarumani pia. Tulikuwa na manokora wetu enzi hizo, waliosaidia kutawala, waliojidhania kuwa wamepata u-Maftaha, kumbe Mondo tu. Kama Maftaha, kazi yao ilikuwa kupeleka mbele kilio cha wananchi: "Wanataka barabara, wanataka shule, wanataka hospitali."
Basi, leo El-Mahdi kafa; mkoloni kaondoka, wala harudi tena. Lakini Maftaha bado wapo, ndiyo sababu Baba wa Taifa anasisitiza wakuu wa Serikali wasiwe tena watu wa kutawala, bali watu wa kuhimiza maendeleo vijijini. Huu si wakati tena wa wanyapara wetu kulialia kama Maftaha; huu ni wakati wa kuwaeleza wananchi watumie ardhi yao waliyopewa na Mwenyezi Mungu. Kama wananchi wanataka maji, basi wafanye kazi ya kuyaleta maji; kama wanataka barabara, basi walime barabara.
Na sisi je, tuliokuwa nyuma ya mwenzetu Maftaha? Sisi tulikuwa na mawazo ya kitumwa siku nyingi. Zamani tulikuwa tunamfanyia kazi El-Mahdi, lakini leo tunafanya kazi kwa manufaa yetu sisi wenyewe, na ya watoto wetu. Tusimweke doria tena kutazama kama Maftaha anakuja, ndipo tufanye kazi; bali tufanye kazi kwa roho moja, tujisaidie wenyewe, kwa kuwa sasa nchi hii ni yetu.
Linapokuja swala la wengi tunakuwa wazito kuungana tunaipa nafasi ile roho ya tamaa na ubinafsi kututawala
 
Back
Top Bottom