Watu wengi niliosoma nao tokea shule ya msingi mpaka chuo wamekuwa wakiogopa sana kujihusisha na michepuo ya masomo ambayo ina hesabu kwa wingi, au ikitokea somo la hesabu ni lazima katika mchepuo huo, hufanya vibaya sana katika somo hilo.
Rafiki mmoja alitutania kwa kusema yeye amependelea kusoma mambo ya sheria kwa vile huko namba hazina nafasi kabisa kiasi kwamba hata orodha ya vitu hutamkwa kwa kutumia herufi badala ya namba, mfano a, b, c, na kuendelea badala ya 1, 2, 3, na kuendelea.
Nijuavyo mimi kujua hesabu ni moja ya nyanja muhimu ambayo bila hiyo elimu kwa ujumla wake yaweza kuwa duni. Hesabu hupanua sana uwezo wa kufikiri na kujenga hoja za kisayansi na kijamii. Mfano hesabu za "logic", "probability", "statistics", maumbo n.k. zote zina nafasi pana ya matumizi katika kila idara iliyo kwenye mifumo yoyote ile ndani ya jamii, hii ikiwa ni pamoja na mahakama, hospitali, familia, biashara, kilimo, michezo, n.k.
Ikiwa tatizo hili linaendelea kwa vizazi vyetu vya leo tutambue kuwa watoto wetu na vizazi vijavyo vinaweza kugubikwa na taifa lenye watendaji wengi wenye uvivu wa kufikiri na matokeo yake ni kudidimia zaidi kwa maendeleo ya nchi yetu.
Natia shaka kuwa, yawezekana kabisa utendaji mbovu wa uchumi katika nchi yetu unatokana na watendaji wengi katika sekta mbalimbali kuwa na uelewa mdogo sana (ukilaza) wa somo hili la Hesabu na hivyo kushindwa kulitumia ipasavyo. Hebu sema ni jambo gani haliwezi kutumia hesabu ili kusaidia kufanya maamuzi bora?
Natoa mtihani mdogo sana hapa kwa wanaJF kupima 'vilaza' wa hesabu (usikwazike, sijatukana). Kokotoa na kuweka jibu la swali hili dogo, samahani sijaweka 'multiple choice' na kisha changia mada katika kutoa ushauri nini kifanyike kuhamasisha vijana mashuleni na vyuoni kupenda Hesabu.
Swali: Pande mbili za sambamba trapeza zina urefu wa sm 5 na sm 8. Ikiwa umbali kati ya pande hizo ni sm 10, kokotoa eneo la trapeza hiyo.
Tahadhali: ukijibu na kukosa ni kilaza, usipojibu hujui.