K
Mjini hakukaliki, Yanga tangu wamepata sare na Simba wameshangilia sana matokeo hayo kama vile ambavyo Simba ingeshangilia kupata sare na Real Madrid. Je ni kweli kuwa kiwango cha Yanga kwa sasa kimeporomoka sana kiasi cha kuona sare na Simba ni miujiza na ushindi mkubwa. Takwimu zinaonyesha Yanga kwa zaidi ya mwaka moja na nusu hawajafanikiwa kuifunga Simba.
Kiuhalisia, wenye haki ya kufurahia sare ile ni Simba kwa sababu wameweza kubakisha pengo la alama baina yao na Yanga ambao ndio wanaoonekana kuwa tishio zaidi la kutetea ubingwa kuliko timu nyengine zilizosalia (iwapo atacheza vyema mechi zake za viporo).
Lakini kisaikolojia, sare ile ni ushindi kwa Yanga kwa sababu: 1. Imewaumiza, kuwasononesha na kuwanyon’gonyesha watani wao kiasi kwamba uongozi usipochukua hatua madhubuti, hali hiyo inaweza kuwaathiri hata kwenye mechi zijazo. Si umeshaona wapenzi wanavyomlaumu Aishi na Manara anavyoilaumu timu nzima? 2. Imewaaminisha Yanga kwamba wana uwezo sawa ama zaidi kuliko Simba, na kwa hivyo kama walikosa kujiamini kwenye mechi za Simba sasa watajiamini si kwa Simba tu, bali timu nyengine za kwenye Ligi. 3. Ushindi wa mabao mengi tangu kuja kwa kocha mpya uliwafanya Simba na wadau wake kuamini kwamba hali ile itafuuliza. Lakini tangu kuanza mechi za Ligi (baada ya Lipuli) ufungaji umekuwa ukipungua. Hilo linaanza kuwapa mashaka wadau, na hivyo imani yao kwa timu kutoongezeka. 4. Tangu kuja kocha mpya Simba wamekuwa wakiondoka na hati safi golini, hali iliyowapelekea kuamini kwamba hata wasipotia goli, hakuna timu ya kuwatia goli. Kufungwa mabao mawili ndani ya dakika tatu kumewaondolea imani hiyo na kunaifanya safu ya ulinzi ipunguze kuaminiwa, kuaminiana na kujiamini. 5. Dhana ya kuwa Yanga ni dhaifu kwa sababu tu haina fedha, na hasa baada ya wachezaji kuvunja mikataba kwa sababu ya ukata, imewajengea imani Wanasimba kwamba Yanga hawawezi kujenga timu ya kushindana nao ndani ya miaka mingi ijayo. Matokeo yale yamewafanya kufadhaika, na itawapa taabu kutafuta wachezaji wa ’kuinyanyasa tena Yanga’ baada ya uwekezaji wote wa ‘tajiri wa Manara’. 6. Hakuna raha kuliko kumnyan’ganya mshindani wako ‘tonge mdomoni’ kwa maana zote mbili: ushindi ulioonekana kuwa ni wa wazi na fedha nyingi walizoahidiwa wachezaj. 7. Kama mtani wako ameondoka kichwa chini kwa sababu yako, utaelewekaje iwapo na wewe utaondoka kichwa chini? 8. Labda Yanga wamelipiza kisasi kwa Simba kufurahia sare. Au Simba waliondoka wamenuna siku waliporejesha mabao matatu? 9. Kanuni ya maumbile ni kuwa anayecheka mwisho ndiye achekaye sana (he who laughs last laughs best). Kwa kutumia Kanuni hiyo, nani alicheka mwisho? Sasa nani acheke sana? 10. Baina ya wadau wa Simba na wa Yanga, nani alitoa tambo zaidi kabla ya mech? Mojawapo ninayoikumbuka ni ya shabiki aliyeahidi kwamba wasiposhinda mechi ile, nyumba yake iuzwe na pesa wapewe Yanga. Unategemea wapenzi wa Yanga wanaomjua wanune baada ya matokeo yale, na yeye afurahi? Na ujue kila kona tambo za Wanasimba zilikuwa za namna hiyo.
Kwa hivyo hakuna sababu ya kubeza furaha ya Yanga kwa kukomboa mabao mawili, maana hakuna kwenye historia ya soka kwa timu inayorejesha mabao zaidi ya moja kuondoka uwanjani imenuna. Na anayekombolewa mabao hayo anapokuwa ni mtani wa jadi, furaha kuzidi ni jambo la kawaida. Anayebisha aulize ilikuwaje Simba walipokomboa mabao matatu ya Yanga kipindi cha pili. Au ndiyo ‘mkuki kwa nguruwe, kwa binadamu mchungu’?