Makapuku Forum

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Ndanga Kata ya Mbuyuni wilayani Songwe hawana mahali pa kuishi baada ya mvua kubwa kunyesha na kusababisha mafuriko yaliyoharibu zaidi ya nyumba 100 na miundombinu ya barabara.

Mvua hizo zilizoanza Januari 30, 2024 zimesababisha adha kwa wakazi hao huku baadhi wakianza kuhamia vijiji jirani ili kuokoa maisha yao.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Songwe, Solomon Itunda amesema mvua hizo zimeharibu nyumba za wakazi wa kijiji hicho na miundombinu ya barabara.

"Baada ya kupata taarifa ya mafuriko kupitia diwani tumeamua kuja kujionea wenyewe. Viongozi tuna jukumu kubwa la kuhakikisha wananchi wanaishi mahali salama lakini tuna jukumu kubwa kuwafariji wanapokutana na changamoto hii ya mafuriko,’’ amesema Itunda ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Songwe.

“Maeneo ambayo yamekumbwa na changamoto hii katika wilaya yetu ni mengi. Maeneo mengine ya miundombinu ya barabara imekumbwa na changamoto ya mafuriko, tumepita na meneja wa Tanroads mkoa ili kuhakikisha barabara zote zinapitika. Kule Mheza juzi basi lilisombwa na maji lakini tunamshukuru Mungu watu wote walikuwa wameshashuka.”

Itunda ambaye alilazimika kupanda bodaboda kilomita zaidi ya tano ili kufika katika eneo hilo baada ya gari kushindwa kupita, amesema: “Naomba niwape pole sana ndugu zangu, nimejionea mwenyewe adha na changamoto mnayokumbana nayo.

Nimewaona mama zangu wamebeba watoto na wengine wamebeba mizigo wanavyopita kwenye eneo hili kama wanaogelea kwa sababu njia zote zimejaa maji.”

Hata hivyo, ameagiza wananchi ambao bado wanaendelea kuishi katika eneo hilo kuhama ili kuepusha athari zinazoweza kujitokeza wakati kamati ya usalama ya wilaya hiyo ikiendelea kufanya tathimini ya athari hiyo.

Mafuriko hayo yamesababishwa na mvua zinazoendea kunyesha katika Wilaya ya Songwe kuanzia Januari 30, 2024 huku maeneo mengi katika kata za Mbuyuni na Magamba yakiwa yamejaa maji.
 
Wakati Arsenal haitokuwa na Thomas Partey, Liverpool itamkosa Mohamed Salah timu hizo zitakapoumana kesho kwenye Uwanja wa Emirates jijini London.

Mchezo huo wenye maana kubwa kwa kila timu katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu England (EPL), utatazamwa na nyota hao wawili kupitia runinga au jukwaani kutokana na majeraha ya misuli yanayowakabili.

Kulikuwa na matumaini ya Partey kurejea uwanjani katika mechi hiyo dhidi ya Liverpool itakayochezwa saa 1:30 usiku kwa saa za Afrika Mashariki lakini Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta amethibitisha kuwa kiungo huyo Mghana ataendelea kuwa nje ya uwanja.

Kwa upande wa Salah, Kocha wa Liverpool, Jurgen Klopp amethibitisha kuwa hatokuwepo dhidi ya Arsenal kwa kuwa hajapona maumivu ya misuli aliyopata wakati akiitumikia Misri kwenye Fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon) huko Ivory Coast.

Ushindi katika mechi ya kesho utaifanya Liverpool izidi kujikita kileleni mwa msimamo wa EPL kwa kuwa itafikisha pointi 54 wakati Arsenal ikishinda itapunguza pengo la pointi kwa sasa ina pointi 46.
 
Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za mauaji ya Mohamed Ameir (35), mkazi wa Magomeni- Mwembechai wilayani Kinondoni.

Taarifa iliyotolewa jana Februari 2, 2024 na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro inaeleza mwili wa Ameir umekutwa katika fukwe za Kigamboni, Februari mosi, 2024.

“Taarifa za awali zilipatikana kwa Jeshi la Polisi kutoka kwa ndugu wa marehemu kuwa Januari 28, 2024 mtu huyu hakuonekana na baadaye ikadaiwa alitekwa na watu waliotaka kupewa fedha Sh3 milioni.

“Jeshi la Polisi linafanya mahojiano ya kina kwa watuhumiwa hao wawili, jitihada zinafanyika ili kuhakikisha wengine nao wanakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kwa hatua zaidi,” amesema Kamanda Muliro bila kuwataja watuhumiwa hao.

Tukio hilo limekuja wakati kukiwa na taarifa za watu kutoweka na kutekwa maeneo mbalimbali nchini.

Miongoni mwa matukio hayo ni la kutekwa kwa aliyekuwa mfanyabiasha na fundi simu eneo la Kariakoo, Dar es Salaam, Innocent Elias Liveti (34) maarufu Macheni.

 
Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa Tumaini Nagu amezitaka nyumba za ibada kusitisha utaratibu wa waumini wake kushikana mikono, ikiwa ni sehemu ya kupambana na magonjwa ya mlipuko ya viral keratoconjunctivitis (red eyes) na kipindupindu.

Profesa Nagu alisema hayo jana, wakati akiongoza kikao cha 10 cha Bodi ya Ushauri wa Hospitali Binafsi.

Pia, alitoa rai ya matumizi ya majisafi tiririka na sabuni maeneo ya mikusanyiko, ofisi za umma na binafsi, nyumbani na sehemu za biashara, huku akiwahimiza wanaotumia vyombo vya usafiri kutumia vitakasa mikono.

Profesa Nagu alisema hayo baada ya kuwapo ongezeko la wagonjwa wa macho unaoambukizwa kwa kushikana mikono, kugusa sehemu aliyogusa mwenye maambukizo ambalo kwa sasa imefikia mikoa 17 na ugonjwa wa kipindupindu umesambaa katika mikoa 14.

Januari 29, Wizara ya Afya ilisema jumla ya mikoa 17 imeathirika na ugonjwa wa macho mekundu.

Akitoa taarifa hiyo, Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Profesa Paschal Rugajjo alisema hadi kufikia Januari 26 mwaka huu, idadi ya waliofika kwenye vituo vya afya walikuwa 5,359 kutoka 1,109, Januari 19.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…