Samahani
JF-Expert Member
- Oct 29, 2018
- 221
- 335
Utangulizi
Zoezi la sensa ya watu na makazi linaloendea nchini limenikutanisha tena na swali ambalo kwa miaka mingi limekuwa likizitamausha fikara zangu. “Unajishughulisha na nini?” ni ‘swali la kawaida’ tunapohitajika kutoa taarifa zinazotuhusu.
Katika kulijibu swali hili, wanawake wengi, pasi na kujali kuwa wameolewa au la, hujitambulisha kuwa “mama wa nyumbani”. Tafsiri yao ya moja kwa moja ni kuwa, hawana kazi rasmi, “wameajiriwa” kama “mama wa nyumbani”.
Jibu hili linaweza kuonekana la kawaida.
Limezoeleka kwa wengi. Lakini ukawaida wa jibu hili hauleti utulivu tunapotazama idadi ya hawa “mama wa nyumbani”. Idadi yao inamlazimisha mtu mwenye utulivu wa fikra kutathmini upya nini hasa ambacho “utitiri huu wa mama wa nyumbani” wanakifanya, na kipekee, nguvukazi hii “inayomwagikia chini”.
Hapa najipa jibu moja tu. Hiki ni “kiwanda kilichojificha”.
Wanawake hawa ambao kila siku wanajiitambulisha kama “mama wa nyumbani” wanafanya kazi kubwa ya kujipatia kipato kwa ‘utengenezaji kwa mikono’ wa bidhaa aushi kwa ajili ya matumizi ya kila siku pamoja na malighafi kwa viwanda vikubwa.
Tunatumia bidhaa nyingi zilizozalishwa na “akina mama wa nyumbani”; vitafunwa, sharubati, sabuni, marashi, mafuta ya kula, mapambo na mavazi, pombe za kienyeji, vyakula vilivyosindikwa, chumvi, asali, pamba na mkonge vilivyochakatwa, mafuta ya nazi, korosho, kutaja vichache.
Viwanda vya mikono vinafanya kazi usiku na mchana!!
Mapinduzi ya kweli ya kiviwanda yalianza baada ya kustawi na kukua kwa “viwanda vya mikono” (cottage industries), ambako zilitengenezwa nyumbani. Baadhi ya bidhaa hizi zilikuwa tayari moja kwa moja kwa matumizi na nyingine zilikuwa malighafi katika viwanda na mashine za kisasa. (Roger LeRoy & Lois Fares, 1992).
Hapa Tanzania, mathalani, mkoani Singida, wanawake huchukua mabaki ya kwanza wakati wa ukamuaji wa mafuta ya alizeti katika viwanda vya ukamuaji.
Huyachemsha mabaki hayo ambayo huitwa “ugido” kuzalisha mafuta safi ya alizeti yanayouzwa kwa bei nafuu. Wengine huchukua maji chumvi kutoka bwawa la Singidani, kisha hutengeneza aina ya “kisahani” cha tope juu ya jiwe lenye uso mpana. Baada ya maji haya kupigwa na jua na kukauka, kinachobaki huwa ni chumvi safi nyeupe ambayo nayo pia huuzwa kwa gharama nafuu.
Mikoa iliyopo pwani, mafuta ya nazi safi na halisi hutengenezwa majumbani kwa kuchemsha makapi ya nazi. Kule Kigoma, tunao utajiri wa mafuta ya mawese pamoja na sabuni ambazo hutengenezwa kwa mikono majumbani. Kadhalika, mikoa ya Manyara, Arusha, Dodoma na Singida, kumekuwepo na wanawake wengi ambao wamejikita katika sanaa ya ushonaji wa vikapu, mikeka, vitanga, mapambo ya miili na nyumba na uchongaji wa vifaa vya matumizi ya nyumbani; machanuo, vinu, vigoda na miiko.
Hapa nimejaribu kuigusa mikoa michache. Kila jamii, kulingana na eneo, wanazo bidhaa ambazo hutengenezwa kwa mikono majumbani. Wengi wanaofanya kazi hizi ni wanawake, hawa ambao wanaamini kuwa “hawana kazi”.
Kutokuvitambua na kuvirasimisha ‘viwanda vya mikono’ kumepelekea uduni wa bidhaa zake na zingine kutokutambulika. Tuna changamoto kubwa katika utayarishaji, uhifadhi na usindikaji wa bidhaa hizi unaozishusha thamani (Wizara ya Kilimo na chakula, 2003). Hii, inakoleza mapigo katika ngoma tunayoicheza kila siku; umaskini na ukatili wa kijinsia.
Hali Halisi
Vipo viashiria vingi kuwa, wanawake wamekuwa ni waathirika wakubwa zaidi wa umaskini hapa Tanzania ilhali wao ndio wachangiaji wakubwa katika pato la taifa (Aggripina Mosha & Miranda Johnson, 2004). Zaidi ya 50% ya wanawake na wasichana wanaohusika katika shughuli za moja kwa moja katika kilimo na kazi zingine za mikono katika ‘sekta isiyo rasmi’ (Aggripina Mosha, 2004 Uk. 54).
Katika ukuaji wa uchumi na uzalishaji, wanawake wameendelea kuhudumu katika sekta zenye mchango mkubwa zaidi kiuchumi. Kwa mujibu wa takwimu za pato la taifa, 2004; mgawanyo kisekta ulikuwa hivi; Kilimo (46%), vyakula na vinywaji (17%) na shughuli nyingine za mikono (14%). Sekta zingine ambazo wanaume wameendelea kuwepo kwa wingi zilichangia kwa kiasi kidogo; Viwanda (9%), mawasiliano na uchukuzi (5%), ujenzi (6%) na uchimbaji wa madini (3%). Sekta ya kilimo ilikuwa imechangia 81% huku sekta “isiyo rasmi” (informal Sector ikiwa imechangia 9% ya pato la taifa (Ophelia Mascarenhas, 2007, Uk. 25 – 27, BoT Annual Report 2004/5).
Hali hii haijabadilika kwa kiasi kikubwa hata baada ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012.
Ushiriki wa moja kwa moja wa wanawake ambao wengi wao bado wanajitambulisha kwa cheo cha “mama wa nyumbani” haupaswi kupuuzwa, bali kutambulika, kuendelezwa na kuthaminiwa (UNICEF, 1990). Ni wazi kuwa, namna mojawapo ya kufikia lengo ni kurasimisha “uchumi wa viwanda vya mikono”, tukijua kuwa nguvukazi kubwa tuliyonayo katika taifa imewekezwa huko.
Njia ya kufikia lengo
1. Viwanda vya mikono (cottage insustries), vitambulike rasmi na kuwekwa chini ya wizara inayojitegemea ili kuviandalia mfumo utakaozisaidia kazi zake kutambulika kirahisi zaidi
2. Elimu ya uendelezaji, usindikaji, uhifadhi, usafirishaji na ufanisi wa kimasoko wa bidhaa kutoka katika viwanda hivi vya mikono itolewe kwa upana zaidi ili kuongeza thamani ya vile vinavyotengenezwa.
3. Uingizaji holela wa bidhaa zinazoleta ushindani usio na tija kwa zile zinazotengenezwa ndani usitishwe. Nguvu kubwa iwekwe katika uendelezaji wa bidhaa za ndani ili ziweze kupata masoko nje ya nchi.
4. “Wataalamu” katika viwanda hivi (ambao wengi ni wanawake), wafundishwe kwa kina dhana ya kuungana katika uzalishaji ili kuongeza tija na ufanisi.
5. Elimu ya hakimiliki itolewe kwa upana katika kila uvumbuzi mpya katika viwanda hivi vya mikono, hasa pale inapotokea kuwa uvumbuzi huu unapaswa kuendelezwa zaidi katika viwanda vikubwa
6. Jamii ihamasishwe juu ya ubora na usalama wa bidhaa zinazozalishwa katika viwanda hivi ili kukuza masoko na mrejesho baada ya matumizi ya bidhaa hizo.
7. Viwanda vya kati na viwanda vikubwa vihamasishwe kutumia malighafi zinazozalishwa kutoka katika viwanda vya mikono ili kuendelea kuvikuza zaidi.
8. Mamlaka zinazosimamia ubora wa bidhaa (TBS) zishushe huduma zake na uwepo wake katika ngazi za wilaya ili kuchakata kirahisi ubora wa bidhaa na kuzithibitisha zile zinazofikia viwango kwa urahisi na uharaka.
Zipo jamii ambazo zilishajitathmini na kufuata aina fulani ya uchumi, zikiangalia hasa asili ya shughuli ambazo zehemu kubwa ya watu wake wanazifanya. Zipo ambazo zinatambulika kwa uchumi wa kilimo, viwanda, mafuta, huduma au teknolojia ya taarifa. (Roger LeRoy & Lois Fares, 1992).
Tanzania tuko katika uchumi wa mseto. Tuvirasimishe ‘viwanda vya mikono’ na kuvitengenezea mfumo wake, ikiwa ni pamoja na kuvitambua kama sekta inayojitegemea. Kwa kufanya hivi, tunaweza kujipa miaka michache ya kujionea namna ambavyo tunaweza kwenda kwenye mapinduzi halisi ya kiuchumi.
Zoezi la sensa ya watu na makazi linaloendea nchini limenikutanisha tena na swali ambalo kwa miaka mingi limekuwa likizitamausha fikara zangu. “Unajishughulisha na nini?” ni ‘swali la kawaida’ tunapohitajika kutoa taarifa zinazotuhusu.
Katika kulijibu swali hili, wanawake wengi, pasi na kujali kuwa wameolewa au la, hujitambulisha kuwa “mama wa nyumbani”. Tafsiri yao ya moja kwa moja ni kuwa, hawana kazi rasmi, “wameajiriwa” kama “mama wa nyumbani”.
Jibu hili linaweza kuonekana la kawaida.
Limezoeleka kwa wengi. Lakini ukawaida wa jibu hili hauleti utulivu tunapotazama idadi ya hawa “mama wa nyumbani”. Idadi yao inamlazimisha mtu mwenye utulivu wa fikra kutathmini upya nini hasa ambacho “utitiri huu wa mama wa nyumbani” wanakifanya, na kipekee, nguvukazi hii “inayomwagikia chini”.
Hapa najipa jibu moja tu. Hiki ni “kiwanda kilichojificha”.
Wanawake hawa ambao kila siku wanajiitambulisha kama “mama wa nyumbani” wanafanya kazi kubwa ya kujipatia kipato kwa ‘utengenezaji kwa mikono’ wa bidhaa aushi kwa ajili ya matumizi ya kila siku pamoja na malighafi kwa viwanda vikubwa.
Tunatumia bidhaa nyingi zilizozalishwa na “akina mama wa nyumbani”; vitafunwa, sharubati, sabuni, marashi, mafuta ya kula, mapambo na mavazi, pombe za kienyeji, vyakula vilivyosindikwa, chumvi, asali, pamba na mkonge vilivyochakatwa, mafuta ya nazi, korosho, kutaja vichache.
Viwanda vya mikono vinafanya kazi usiku na mchana!!
Mapinduzi ya kweli ya kiviwanda yalianza baada ya kustawi na kukua kwa “viwanda vya mikono” (cottage industries), ambako zilitengenezwa nyumbani. Baadhi ya bidhaa hizi zilikuwa tayari moja kwa moja kwa matumizi na nyingine zilikuwa malighafi katika viwanda na mashine za kisasa. (Roger LeRoy & Lois Fares, 1992).
Hapa Tanzania, mathalani, mkoani Singida, wanawake huchukua mabaki ya kwanza wakati wa ukamuaji wa mafuta ya alizeti katika viwanda vya ukamuaji.
Huyachemsha mabaki hayo ambayo huitwa “ugido” kuzalisha mafuta safi ya alizeti yanayouzwa kwa bei nafuu. Wengine huchukua maji chumvi kutoka bwawa la Singidani, kisha hutengeneza aina ya “kisahani” cha tope juu ya jiwe lenye uso mpana. Baada ya maji haya kupigwa na jua na kukauka, kinachobaki huwa ni chumvi safi nyeupe ambayo nayo pia huuzwa kwa gharama nafuu.
Mikoa iliyopo pwani, mafuta ya nazi safi na halisi hutengenezwa majumbani kwa kuchemsha makapi ya nazi. Kule Kigoma, tunao utajiri wa mafuta ya mawese pamoja na sabuni ambazo hutengenezwa kwa mikono majumbani. Kadhalika, mikoa ya Manyara, Arusha, Dodoma na Singida, kumekuwepo na wanawake wengi ambao wamejikita katika sanaa ya ushonaji wa vikapu, mikeka, vitanga, mapambo ya miili na nyumba na uchongaji wa vifaa vya matumizi ya nyumbani; machanuo, vinu, vigoda na miiko.
Hapa nimejaribu kuigusa mikoa michache. Kila jamii, kulingana na eneo, wanazo bidhaa ambazo hutengenezwa kwa mikono majumbani. Wengi wanaofanya kazi hizi ni wanawake, hawa ambao wanaamini kuwa “hawana kazi”.
Kutokuvitambua na kuvirasimisha ‘viwanda vya mikono’ kumepelekea uduni wa bidhaa zake na zingine kutokutambulika. Tuna changamoto kubwa katika utayarishaji, uhifadhi na usindikaji wa bidhaa hizi unaozishusha thamani (Wizara ya Kilimo na chakula, 2003). Hii, inakoleza mapigo katika ngoma tunayoicheza kila siku; umaskini na ukatili wa kijinsia.
Hali Halisi
Vipo viashiria vingi kuwa, wanawake wamekuwa ni waathirika wakubwa zaidi wa umaskini hapa Tanzania ilhali wao ndio wachangiaji wakubwa katika pato la taifa (Aggripina Mosha & Miranda Johnson, 2004). Zaidi ya 50% ya wanawake na wasichana wanaohusika katika shughuli za moja kwa moja katika kilimo na kazi zingine za mikono katika ‘sekta isiyo rasmi’ (Aggripina Mosha, 2004 Uk. 54).
Katika ukuaji wa uchumi na uzalishaji, wanawake wameendelea kuhudumu katika sekta zenye mchango mkubwa zaidi kiuchumi. Kwa mujibu wa takwimu za pato la taifa, 2004; mgawanyo kisekta ulikuwa hivi; Kilimo (46%), vyakula na vinywaji (17%) na shughuli nyingine za mikono (14%). Sekta zingine ambazo wanaume wameendelea kuwepo kwa wingi zilichangia kwa kiasi kidogo; Viwanda (9%), mawasiliano na uchukuzi (5%), ujenzi (6%) na uchimbaji wa madini (3%). Sekta ya kilimo ilikuwa imechangia 81% huku sekta “isiyo rasmi” (informal Sector ikiwa imechangia 9% ya pato la taifa (Ophelia Mascarenhas, 2007, Uk. 25 – 27, BoT Annual Report 2004/5).
Hali hii haijabadilika kwa kiasi kikubwa hata baada ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012.
Ushiriki wa moja kwa moja wa wanawake ambao wengi wao bado wanajitambulisha kwa cheo cha “mama wa nyumbani” haupaswi kupuuzwa, bali kutambulika, kuendelezwa na kuthaminiwa (UNICEF, 1990). Ni wazi kuwa, namna mojawapo ya kufikia lengo ni kurasimisha “uchumi wa viwanda vya mikono”, tukijua kuwa nguvukazi kubwa tuliyonayo katika taifa imewekezwa huko.
Njia ya kufikia lengo
1. Viwanda vya mikono (cottage insustries), vitambulike rasmi na kuwekwa chini ya wizara inayojitegemea ili kuviandalia mfumo utakaozisaidia kazi zake kutambulika kirahisi zaidi
2. Elimu ya uendelezaji, usindikaji, uhifadhi, usafirishaji na ufanisi wa kimasoko wa bidhaa kutoka katika viwanda hivi vya mikono itolewe kwa upana zaidi ili kuongeza thamani ya vile vinavyotengenezwa.
3. Uingizaji holela wa bidhaa zinazoleta ushindani usio na tija kwa zile zinazotengenezwa ndani usitishwe. Nguvu kubwa iwekwe katika uendelezaji wa bidhaa za ndani ili ziweze kupata masoko nje ya nchi.
4. “Wataalamu” katika viwanda hivi (ambao wengi ni wanawake), wafundishwe kwa kina dhana ya kuungana katika uzalishaji ili kuongeza tija na ufanisi.
5. Elimu ya hakimiliki itolewe kwa upana katika kila uvumbuzi mpya katika viwanda hivi vya mikono, hasa pale inapotokea kuwa uvumbuzi huu unapaswa kuendelezwa zaidi katika viwanda vikubwa
6. Jamii ihamasishwe juu ya ubora na usalama wa bidhaa zinazozalishwa katika viwanda hivi ili kukuza masoko na mrejesho baada ya matumizi ya bidhaa hizo.
7. Viwanda vya kati na viwanda vikubwa vihamasishwe kutumia malighafi zinazozalishwa kutoka katika viwanda vya mikono ili kuendelea kuvikuza zaidi.
8. Mamlaka zinazosimamia ubora wa bidhaa (TBS) zishushe huduma zake na uwepo wake katika ngazi za wilaya ili kuchakata kirahisi ubora wa bidhaa na kuzithibitisha zile zinazofikia viwango kwa urahisi na uharaka.
Zipo jamii ambazo zilishajitathmini na kufuata aina fulani ya uchumi, zikiangalia hasa asili ya shughuli ambazo zehemu kubwa ya watu wake wanazifanya. Zipo ambazo zinatambulika kwa uchumi wa kilimo, viwanda, mafuta, huduma au teknolojia ya taarifa. (Roger LeRoy & Lois Fares, 1992).
Tanzania tuko katika uchumi wa mseto. Tuvirasimishe ‘viwanda vya mikono’ na kuvitengenezea mfumo wake, ikiwa ni pamoja na kuvitambua kama sekta inayojitegemea. Kwa kufanya hivi, tunaweza kujipa miaka michache ya kujionea namna ambavyo tunaweza kwenda kwenye mapinduzi halisi ya kiuchumi.
Attachments
Upvote
8