Mashahidi dhidi ya bosi wa Richmond wakwama

Mashahidi dhidi ya bosi wa Richmond wakwama

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Joined
Sep 24, 2010
Posts
219,468
Reaction score
911,184
Mashahidi dhidi ya bosi wa Richmond wakwama

Thursday, 24 March 2011 20:04 newsroom



NA FURAHA OMARY
MASHAHIDI wa upande wa mashitaka katika kesi inayomkabili bosi wa kampuni iliyopewa zabuni ya kuzalisha umeme ya Richmond Development Company LLC, Naeem Gire wamekwama kutoa ushahidi. Kukwama kwa mashahidi watatu waliofika jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kutoa ushahidi kunatokana na Wakili Alex Mgongolwa anayemtetea Gire kutokuwepo. Gire anayekabiliwa na mashitaka matano ya kughushi, kutoa hati za kughushi na taarifa za uongo kwa taasisi mbalimbali za serikali, alipanda kizimbani mahakamani hapo, mbele ya Hakimu Mkuu Mkazi Warialwande Lema. Upande wa Mashitaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu Fredrick Manyanda akisaidiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi Arafa Msafiri, ulidai shauri linakuja kwa kuanza kusikilizwa kwa mashahidi wa upande wao. Manyanda alidai kwa upande wao wapo tayari na kwamba wana mashahidi watatu.
Kwa upande wa utetezi, Wakili Alex Msumbushi aliyemwakilisha Wakili Mgongolwa kwa niaba ya Gire, alidai kuwa wakili huyo yupo Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Biashara anakosikiliza shauri lingine, hivyo kuomba kesi hiyo iahirishwe na kupangiwa tarehe nyingine.
Wakili Manyanda alidai mshitakiwa ana haki ya kuwa na wakili wake wakati wa usikilizwaji, lakini mashahidi wametoka mbali, kwani yupo aliyetoka mkoani Arusha, hivyo iangalie ipange hata leo.
Hakimu Warialwande aliahirisha shauri hilo ambapo sasa litasikilizwa mfululizo kuanzia Aprili 11 hadi 13, mwaka huu na kuwaonya mashahidi kuhakikisha wanafika mahakamani.
Gire, anadaiwa kwa nia ya kutenda kosa Machi 13, 2006 mjini Dar es Salaam, alighushi hati kuonyesha ameidhinishwa kisheria na Mohammed Gire, Mwenyekiti wa Kampuni ya Richmond Development Company LLC ya Texas, Marekani kufanya kazi za kampuni hiyo nchini.
Pia, anadaiwa Machi 20, 2006, eneo la Ubungo, Dar es Salaam kwa kufahamu kuwa anatenda kosa alitoa hati hiyo kuonyesha Mohammed ametoa idhini kwa Kampuni ya Richmond Development Company LLC kufanya kazi Tanzania.
Gire, anadaiwa siku hiyo hiyo katika eneo la Ubungo alitoa taarifa za uongo kwa Bodi ya Zabuni ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na watumishi wa umma kwamba kampuni ya Richmond ya Marekani, ina uwezo wa kuzalisha megawati 100 za umeme nchini ili kuwezesha kupatiwa zabuni.
Anadaiwa kuwa Juni, 2006 mjini Dar es Salaam, alitoa taarifa za uongo kwa wajumbe wa timu ya majadilino ya serikali kwamba, kampuni hiyo ina uwezo wa kuzalisha megawati hizo ili kuwezesha kupendekezwa kuzalisha umeme.
Shitaka lingine, Gire anadaiwa Juni 2006, akitambua kuwa anatenda kosa, alitoa hati ya kughushi kuonyesha Mohammed alitia saini kumwidhinisha kufanya kazi nchini kupitia kampuni ya Richmond Development Company LLC.
 
Back
Top Bottom