Mazungumzo ya alfu lela ulela-Kitabu cha kwanza.

Mazungumzo ya alfu lela ulela-Kitabu cha kwanza.

Lycaon pictus

JF-Expert Member
Joined
Jan 31, 2021
Posts
9,189
Reaction score
16,128
Baada ya kuona kitabu cha pili na cha nne, sasa tuone cha kwanza. hadithi hizi zote unaweza kuzisoma bure ndani ya maktaba app, ipo playstore.

Toleo la kwanza.jpg
 
KIAPO CHA SULTANI.

Hapo zamani sana katika nchi za Uajemi , china na hindi kulitokea sultani aliyefahamika kwa kuwa na upendo kwa watu wake na nguvu pia ya kijeshi na kiutawala. Watu wake walimpenda sana na yeye aliwapenda. Sultani huyu alikuwa na watoto wawili ambao ni Shahriyar ambaye ndiye mkubwa na mwingine ni Shahzanam ambaye ndiye mdogo.

Watoto hawa pia walitambulika kwa ushujaa walio nao na uhodari katika mambo mbalimbali, hususani katika fani ya kupanda farasi. Sultani huyu alipofariki utawala wake akamwachia mwanaye mkubwa ashike madaraka yake. Na mwanae mdogo akabakia anatawala maeneo mengine katika utawala wa baba yake. Huyu mdogo akaelekea maeneo ya Samarkand na huyu mkubwa akabaki palepale.

Sultan Shahriyar alikuwa na mke wake aliyempenda sana kwa muda mrefu. Hakuwahi kuamini kama itaweza kutokea siku moja akamsaliti. Ilitokea siku moja akamkuta mke wake anazini na mtumwa wake. Kitendo hiki kilimuuma sana na akamuuwa mkewe na yule mtumwa. Kutokea hapo akaapa kutokumwamini mwanamke yeyote duniani. Na kitendo hiki kilimfanya ajiwekee utaratibu mpya wa maisha nao ni kuoa kila siku mke mpya na kisha humuua ifikapo asubuhi.

Hivyo mambo yakawa kama hivi kila siku jioni bibi harusi mpya mwanamwali huolewa na na ikifika asubuhi huuliwa. Kitendo hiki kiliendelea kwa muda mpaka watu wakawa wanaogopa. Ikiwa nyumba moja watu wanalia kwa kufiwa na binti yao nyumba nyingine hufanyika arusi. Sultani alikuwa na waziri wake maalum ambaye alikuwa amepewa kazi hii ya kumletea mfalme wanawali na kutekeleza amri ya kuwauwa kila ifikapo asubuhi.

Waziri huyu aliyepewa kazi hii alikuwa na watoto wawili aliyewapenda sana, mmoja aliitwa Schehrazade ambaye ndiye mkubwa na Dinarzade ambaye ndiye mdogo. Schehra-zade alipata upendo mkubwa kutoka kwa baba yake. Alipewa taaluma mbalimbali za matibabu, sanaa, kuandika, masimulizi , kazi za mikono na nyingine nyingi. Ukiacha mbali na taaluma hizi pia alijulikana kwa uzuri wake ulioaminika kuwashinda wanawake wote katika nchi hiyo. Mabinti wawili hawa walipendana zaidi kila mmoja.

Ilitokea siku moja katika mazungumzo waziri mkuu akiwa na mabinti zake wanaongea Schehra-zade alitowa ombi kutoka kwa baba yake ambalo lilionekana kumshangaza sana. “Baba ninaombi ila niahidi kwanza kuwa utanitekelezea,” alizungumza Schehra-zade kumwambia baba yake. “ Naahidi nitalitekeleza kama lipo chini ya uwezo wangu,” alisikika waziri mkuu akimjibu binti yake.

“Ninataka kukomesha tabia ya kikatili ya sultani kuua mabinti.” “Mmmhhh mwanangu kipenzi, vipi utaweza kumaliza tabia hii ya sultani wetu?” Ni maneno yaliyokuwa yakizungumzwa kati ya waziri na mwanawe. “Baba ninataka unipeleke mimi kwa sultani niwe mkewe.” Alizungumza Schehra-zade. “Mwanangu unafahamu fika kuwa ukiolewa punde tu ifikapo asubuhi nitaamriwa nikuue,” alizungumza waziri kwa masikitiko makubwa.

Schehra-zade aliendelea kusisitiza ombi lake la kutaka kuolewa na sultani ili akamalize tabia yake ya kuua mabinti. Waziri nae hakuacha kumsihi mwanae asithubutu kujiingiza kwenye matatizo haya makubwa. Waziri akawa anamwambia mwanae, “ Hivi mwanangu unataka nikufanyie kitu gani mpaka uachane na msimamo wako huo? Au unataka yakupate yalompata mke wa mfugaji?” Kwa shauku Schehra-zade akauliza, “Kwani baba ni kitu gani kilimpata mke wa mfugaji.” “Mmmmhh.. Ni habari ndefu lakini nitatakusimulia hadithi yake,” alizungumza waziri na kuanza kusimulia hadithi hii:



KISA CHA MFUGAJI NA MKEWE



Hapo zamani kulikuwa na mfugaji maarufu sana na alikuwa ni tajiri na mfanyabiashara aliyekuwa na mafanikio makubwa. Alikuwa anaelewa lugha za wanyama. Alipata tunu hii kwa sharti kuwa asisimulie kwa yeyote mazungumzo ya wanyama na pindi tu akisimulia alichokisikia atakufa hapohapo. Alikuwa akifurahia sana kuwaona wanyama wake na kujua nini wanazungumza. Alikuwa na banda lake la wanyama ambapo ndani kulikuwa na ng’ombe na punda, ambapo kazi ya kuwasimamia wanyama hawa alimpa mtumwa wake.

Sikumoja alipokuwa amekaa pembeni mwa banda hilo akasikia mazungumzo ya kustaajabisha kati ya punda na ngo’mbe. Ngombe akamwambia punda, “Nakuonea wivu kwa raha unayoipata. Wakati mimi ninashinda juani kulima shamba la bwana wetu wewe mwenzangu unaogeshwa na kupambwa na kazi yako ni kumbeba bwana wetu, wananipiga, wananifunga majembe yao shingoni. Nakuonea wivu, natamani ningekuwa wewe.” Punda akamwambia ng’ombe, “Usijali nitakueleza jambo ukilifanya katu hautalimishwa tena. Kesho akija mfanyakazi mpige mateke na mtishe kwa pembe zako na umfukuze. Kataa kula chakula chao. Ukifanya hivi katu hawatakulimisha tena.”

Siku iliyofuata ng’ombe akafanya kama alivyoshauriwa na punda, akamtisha mfanyakazi na akamkimbiza akataka kumchoma kwa pembe zake. Alikataa kula chakula. Siku iliyofuata mfanyakazi akakuta kile chakula alichokileta jana kipo vilevile hivyo akatoa taarifa kwa bwana wake. Mfugaji akamuamuru mfanyakazi wake amchukue punda kwenda kulima. Hivyo siku ile punda akafungwa jembe la kulimia na kwenda kulimishwa. Jioni ile akarudi bandani akiwa amechoka sana.

Kufika hapa waziri akamwambia mtoto wake Schehra-zade “Binti yangu, hivi unataka kuangamia kama punda alivyomshauri mwenzie vibaya na akaumia mwenyewe?” Schehra-zade akamwambia baba yake, “Baba bado msimamo wangu upo pale pale nipeleke kwa sultani nikakomeshe tabia yake. Lakini baba bado sijajua kilichompata mke wa mfugaji ?” alizungumza Schehra-zade kutaka hadithi iendelee. Waziri akaendelea kumsimulia Schehra-zade hadithi hii:

Siki moja mfugaji akiwa na mkewe wameketi karibu na banda la wanyama hawa ili kujua nini punda atamshauri mwenzie. Akamsikia punda akimwambia ng’ombe, “Rafiki yangu nakupa ushauri unisikilize vizuri. Nimemsikia bwana wetu akimwambia mfanya kazi kuwa kama hali yako utaendelea nayo basi uchinjwe na upelekwe ukauzwe nyama. Hivyo nakushauri kesho utii amri ya mfanya kazi hivyo atadhani kuwa ulikuwa umeumwa na sasa umepona.” Ng’ombe alionekana kutii ushauri huu. Hapo mfugaji akacheka sana. Kicheko hiki kilimstaajabisha hata mkewe. Mkewe akataka kujua kinachomchekesha, akamjibu ni siri na nikikwambia nitakufa ila naweza kusema kuwa ninacheka kwa sababu ya mazungumzo kati ya punda na ng’ombe.

Mke huyu alionekana kuwa na msimamo wa kutaka kujua nini hasa kilisemwa mpaka akacheka. Akaahidi kama asipomwambia atarudi kwao. Ugomvi ukawa mkubwa ikafikia hatua ya kuita ndugu waje kusuluhisha. Mfugaji akabaki na msimamo wake kuwa kama atasema atakufa paohapo na mke akafikia kusema kama asiponiambia na mimi nitajiua. Hali hii iliendelea kwa muda mpaka kufikia kuwa mbaya zaidi. Mfugaji akiwaza nimwambie ili nife kwa kumridhisha mke wangu au nisimwambie. Na nisipomwambia atajiua. Ni mawazo ya mfugaji. Ugomvi uliendelea kwa siku kadhaa bila ya maelewano pale ndani.

Siku moja alikaa nyumbani kwake ghafla akamuona mbwa wake aliyempenda sana anamkimbilia jogoo la kuku. Kisha akamuelezea mambo yote yaliyompata bwana wake yaani mfugaji na mkewe. Hapo jogoo akacheka sana kisha akamwambia, “Bwana wako ni mpumbavu kweli, hivi haunioni mimi nina wake zaidi ya hamsini hapa na ninafanya ninalotaka, lakini yeye ana mke mmoja tuu lakini anampa waka timgumu hivi. Akieleza siri atakufa hapa dawa ni ndogo tu. Achukue fimbo nzuri kisha amtandike kisawasawa, bila shaka atarudisha akili yake.” Baada ya maneno haya jogoo likawika na kuondoka zake kwa mwendo wa madaha.

Mfugaji alifikiri atumie ule ushauri wa jogoo, asubuhi ya siku iliyofuata mke wa mfugaji aliendelea na vurumai lake. Mfugaji akaagiza aletewe bakora nzuri na kutekeleza ushauri wa jogoo. Mambo yakatulia nyumbani na hakuleta vurumai lile tena.

Baada ya kumaliza kusimulia hadithi hii waziri akamwambia Schehra-zade, “Binti yangu, je unataka na mimi nitumie uamuzi wa jogoo?” Schehra-zade akamwambia baba yake, “Hapana baba ila mi nadhani hadithi hii hainitoshelezi kubadili uamuzi wangu.” Basi waziri baada ya mazungumzo marefu akakubaliana na maamuzi ya mwanae na kukubali kumpeleka kuwa bibi harusi kwa sultan kwa usiku uliofuata.



Siku ile waziri akaenda kwa sultani kwa masikitiko na majonzi, akamweleza sultan kile ambacho kilitokea kati ya yeye na binti yake. “Sultani; Schehra-zade anataka kwa heshima yako awe mkeo japo kwa usiku mmoja tu. Nimejaribu kumnasihi na kumkataza kwa hali zote nilizoziweza lakini imeshindikana.” Ni maneno ya waziri alomwambia sultani. “Unajua fika kuwa asubuhi baada ya harusi itabidi uchukuwe amri ya kumuua, na ukishindwa na wewe pia utauliwa na kichwa chako kutundikwa.” Ni maneno ya Sultani akisikika anamwambia waziri. Baaada ya mazungumzo marefu Waziri akarudi nyumbani kwa majonzi na kumueleza binti yake ajiandae kwa harusi jioni inayofuata.

Schehra-zade akamueleza mdogo wake Dinar-zade, “Mdogo wangu nina kitu naomba unifanyie, huenda likawa ombi la mwisho kabla sijauliwa au likanusuru maisha yangu na maisha ya mabinti wengine wa nchi hii.” Ni ombi gani hilo dada?” Dinar-zade alimuuliza dada yake. Schehra-zade akaendelea kumweleza “Nitakapokuwa nimeingia kwa mfalme nitamwomba ruhusa ya kuwa na wewe katika chumba kile ili nipate kukuaga kabla sijauliwa. Hivyo nikipewa ruhusa hiyo itakapofika saa kumi na moja alfajiri niamshe kisha uniombe nikusimulie hadithi nzuri iwe kama furaha ya kuagana.” Mdogo wake akakubaliana na wazo hilo la dada yake.

Hali ilikuwa kama hivyo na harusi ikafanyika kati ya sultani na binti wa waziri mkuu. Bibi harusi akaingia kwenye jumba la kifalme huko akakutana na sura ya sultani. Kwa madaha na manjinjo akamuomba ombi lake la kuruhisiwa kuwa na mdogo wake usiki ule katika chumba kimoja ili aweze kumuaga kesho asubuhi kabla ya kuuliwa. Sultani akakubali ombi lile na kuamuru Dinar-zade aletwe na chumba maalumu kikaandaliwa ndani pale.

Mambo yakawa kama hivyo usiku haukuwa mrefu kati ya mabinti wawili hawa. Ilipobaki saa moja kabla ya kupambazuka Dinar-zade akamwambia dada yake, “Dada yangu kipenzi, naomba unifurahishe kwa kunisimulia hadithi nzuri iwe kama furaha ya mwisho ya kuagana kabla ya kuuliwa.” Schehra-zade kabla ya kumjibu mdogo wake akaomba ruhusa kwa sultani ili amruhusu aweze kutimiza matakwa ya mdogo wake kipenzi. “Hakuna shida msimulie tuu ….” Alisema Sultani. Hapo Schehra-zade akaanza kusimulia hadithi kama ifuatavyo.
 
HADITHI YA JINI NA MFANYA BIASHARA.



Hapo zamani kulikuwa na mfanya biashara aliyejulikana kwa utajiri mkubwa sana wa mali na watoto. Alifahamika nchi nzima na aliishi maisha ya upendo na familia yake. Alitoka siku moja katika safari zake za kibiashara. Alikuwa amepanda farasi wake akiwa na mfuko uliojaa tende na maji. Alifanya biashara kwa raha na amani na kuanza kurejea baada ya miezi miwili.

Siku ya nne baada ya kuanza safari ya kurudi alipita katika jangwa lililofahamika kwa jina la uwanja wa ujinini. Jina hili lilitumika miaka mingi iliyopita na huenda sasa limesahaulika. Mfanyabiashara huyu alipopita eneo hili akaona kuna mti wenye kivuli, hivyo akaamua kuketi ili apate kula chakula. Hivyo akawa anakula tende na kutupa punje pembeni. Alifanya hivi mpaka alipo maliza kula. Karibia na mti ule kulikiwa na eneo dogo lenye maji, hivyo alipomaliza kula tende zake akanawa mikono na akaswali swala zake.

Wakati yupo pale ghafla kulitokea upepo mkali sana na kimbunga, vumbi lilitanda eneo lile. Upepo uliambatana na moshi kisha kukatokea jini kubwa sana. “NITAKUUWA KAMA ULIVYOMUUA MWANANGU.” Alisema jini yule kwa sauti ya kutisha akimwambia mfanya biashara. “Nimefanya nini mpaka nistahili kuuawa?” Mfanyabiashara alimwambia jini. Jini likaendelea, “Chagua nikuue namna gani.… Wakati ulipokuwa unakula tende zako ukawa unatupa punje na mwanangu alipita eneo lile ukampiga na punje yako akafa papo hapo. Hivyo lazima nikuue kama ulivyomuua mwanangu.”

Mfanyabiashra akaendelea kumuomba jini msamaha. “Nisamehe mkuu, sikukusudia kumuua mwanao.” Jini kwa hasira likawa linajibu, “Hakuna msamaha wala huruma hapa nitakuua kama ulivyomuua mwanangu.” Jini likatoa upanga wake kuuweka tayari kwa ajili ya kumuua mfanyabiashara.

Mpaka kufika hapa Schehra-zade aligundua kuwa asubuhi imefika tayari na sultani anatakiwa akaswali na akahudhurie kikao cha baraza. “…. Mmmh ni hadithi nzuri sana dada nimeipenda kweli, hivi mwisho wake utakuweje? Mfanyabiashara atauliwa, au jini litamsamehe?” Dinar-zade alimuuliza dada yake. “Mmh ni nzuri kweli na bado huko mbele ni nzuri zaidi kama Sultani ataniruhusu niishi ili kesho nikusimulie muendelezo wa hadithi hii.” Schehra-zade alikuwa akimjibu mdogo wake. Sultani akamruhusu asiuliwe ali aje kuimalizia hadithi yake nzuri.

Siku ile Sultani alitoka akiwa na tabasamu na hata waziri wake alishangaa kuona Sultani ametoka akiwa na tabasamu bila ya kutoa amri ya kumuua Schehra-zade kama ilivyo kawaida yake. Sultani alifanya kazi zake za kawaida huku akiwa na shauku la kutaka kujua mwendelezo wa kisa cha jini.

Usiku uliingia na ilipokaribia alfajiri, Sultani hakusubiri akamwambia Schehra-zade, “Maliza mwendelezo wa hadithi yako, ninashauku la kutaka kujua mwisho wake.” Basi Schehra-zade akaanza kusimulia kama ifuatavyo;-

Basi yule mfanyabiashara alivyoona jini linakaribia kumkata upanga akapiga magoti na kumwambia jini, “Tafadhali mkuu nina neno naomba unisikilize, nina familia mkuu na nina madeni naomba unipe muda angalau nikaiage familia yangu na kulipa madeni yangu.” “Unataka nikuachie ili ukimbie?” Jini lilisema. “Hapana, na ninaapa kwa Mwenyezi Mungu kuwa nitarejea hapa hapa, naweka ahadi mbele ya Mwenyezi Mungu. Alijibu mfanyabiashara

Baada ya kufikiri jini likamuuliza, “Haya ni muda wa siku ngapi nikupe?” Naomba unipe mwaka mmoja,” akajibu mfanyabiashara. Basi jini lile likakubali kuchukuwa ahadi ile na likamwacha mfanya biashara palepale , likotoweka. Mfanya biashara akaondoka akiwa na mjonzi makubwa. Alipofika kwake akaieleza familia yake yote yaliyompata.

Hakuwa na muda wa kupoteza, akalipa madeni yake na kuweka akiba ya kuweza kutumiwa na familia yake pindi atakapoondoka. Mwaka haukuwa mrefu hatimaye miezi kumi na miwili ikakamilika. Mfanyabiashara kwa majonzi na masikitiko akaaga familia na akaondoka kwenda kutekeleza ahadi yake. Alifika eneo la tukio na kumsubiri jini aje.

Katika hali kama hiyo, akiwa amekaa kumsubiri jini akatokea mzee mmoja akiwa na mbuzi wake. Alistaajabu mzee yule kuona mtu eneo lile hatari. Akamuuliza hasa yaliyomkuta kukaa eneo lile, akampa kisa kizima. Kisha yule mzee akamwambia “Nitakaa hapa hapa na mimi nishuhudie kitakacho tokea.” Punde akatokea mzee mwingine akiwa na mbwa wawili weusi. Naye akataka habari ya kilichowakuta wenzie wale mpaka wakakaa pale. Akasimuliwa kisa kizima, na yeye akabaki pale ili ashuhudie kitakacho endelea. Akaja mzee wa tatu akiwa na mbwa wake mwekundu, naye akapewa habari na akakaa ili aone kitakachotokea.

Punde wakaona moshi uliofuatana na upepo, kisha likatokea jini kubwa lililoshika upanga mkononi mwake. Jini lile halikumsemesha yeyote likamfuata mfanyabiashara na kumwambia “Simama ili nikuue kama ulivyomuua kijana wangu, leo sina huruma.”

Pale yule mzee mwenye mbuzi akajitupa miguuni mwa jini kisha kwa hisia kubwa akamwambia, “Ewe mkuu wa majini wa eneo hili, naomba usikilize hadithi yangu na huyu mbuzi niliyekuwa naye hapa. Kama utaiona inastaajabisha kuliko hadithi ya mwanao na mfanya biashara huyu, iwe kama fidia ya kumpunguzia adhabu: Jini likafikiri kwa muda na kisha likasema, “Vizuri sana ebu tusikilize hadithi yako.” Basi mzee yule akaanza kusimulia hadithi yake kama ifuatavyo;-
 
HADITHI YA MZEE WA KWANZA NA MBUZI WAKE.



Mkuu sasa nakwenda kukuhadithia habari yangu na huyu mbuzi niliye naye. Kwanza tambua huyu mbuzi unayemuona hapa ni mke wangu wa ndoa niliyeishi naye kwa muda wa miaka thelathini bila ya kupata mtoto. Pale nyumbani kulikuwa na mtumwa hivyo nikamfanya mwanangu kwa maandishi.

Kumbe mke wangu kitendo kile hakukipenda. Nilitoka kwa ajili ya shughuli za kibiashara, huyu mke wangu alijifundisha uchawi na akambadili mtoto wangu na mama yake kuwa ng’ombe. Kisha akawapeleka kwa mfanya kazi wangu wa shambani ili awalishe na kuwatunza.

Haikupita muda nikarudi kutoka safarini kwangu, nikamuuliza kuhusu mtoto wangu na mama yake lakini akanijibu kuwa mama wa mtoto wangu amefariki inapata miezi miwili sasa. Na kuhusu mtoto wangu ametoweka nyumbani na hafahamiki alipo. Jambo hili lilinishangaza sana lakini sikuwa na la kufanya zaidi ya kumtafuta bila ya mafanikio.

Ulipofika msimu wa sikukuu nilimwambia mfanyakazi wangu aniletee ng’ombe aliyenona ili nimchinje kwa ajili ya kusherehekea sikukuu. Nililetewa ng’ombe mmoja mzuri sana mwenye afya. Jambo lililonishangaza wakati nataka nimchinje ng’ombe huyo alikuwa akitoa machozi na akiniangalia kwa huruma. Kwakweli jambo hili halijawahi kutokea. Nikaagizwa arudishwe na niletewe mwingine.

Mkewangu alikasirika kuona ng’ombe anarudishwa, akanifuata na kunisisitiza nimchinje. Nikamweleza mfanyakazi wangu amchinje yeye mimi siwezi. Basi akamchinja ng’ombe yule. Jambo la ajabu ni kuwa ijapokuwa ng’ombe yule alikuwa amenenepa lakini hakuwa na nyama ila ni mifupa mitupu. Nilishangazwa sana. Nikaagiza niletewe mwingine, na akaletwa ndama mmoja aliyenenepa vizuri. Huyu pia alifanya kama yule wa mwanzo alikuwa akitowa machozi na akajilaza miguuni mwangu kama anaomba aachiwe asiuliwe.

Huruma ilinijaa na nikaamuru aondolewe aletwe mwingine. Mke wangu akanilazimisha nimchinge. Nikamuweka vizuri ili kuanza kumchinja, niliweka kisu kooni na nilipokaribia kumchinja aliniangalia kwa jicho la unyonge na huku akitoa machozi. Kisu kilianguka na nikashindwa kumchinja. Nikaagiza arudishwe. Mke wangu alikasirika sana lakini mara hii sikubadili kauli yangu

Siku ilofuata mfanyakazi wangu alinifuata kwa mazungumzo ya faragha, akanieleza kuwa binti yake ana taaluma ya uchawi hivyo anataka kuzungumza na wewe faragha. Ilibidi nikutane nae, mazungumzo yake yalinistaajabisha sana. “Mkuu ulipoondoka mkeo alijifunza uchawi na akambadili mtoto wako na yule mama yake kuwa ng’ombe. Yule uliyemchinja jana ni mama yake, na yule ng’ombe mdogo uliyemrudisha ndiye mwanao. Nitaweza kumrudisha mwanao kawaida kwa masharti, kwanza uniachie mkeo nimpe adhabu, na pili uniozeshe mwanao.” Haya yalikuwa maneno ya binti wa mfanyakazi wangu. Nilikubaliana na masharti yale.

Yule binti akachukua maji na akatamka maneno nisiyoyajua, kisha akammwagia yule ng’ombe, papo hapo akawa katik umbo la binadamu. Nilifurahi sana. Kama masharti tuliyokubaliana, alimfuata mke wangu na kutamka maneno flani na mke wangu akageuka kuwa mbuzi huyu ambaye unamuona.

Ni muda mrefu sasa hatujaonana na mwanangu hivyo nimetoka ili kama nitaweza kupata taarifa zake zozote. Nimeona ubaya kumuacha mke wangu huyu mbuzi chini ya uangalizi wa watu wengine. Nikaona bora nimchukue. Hii ndiyo hadithi yangu ewe mkubwa katika majini.



“Naam nakubaliana na hadithi yako, kweli inasikitisha hivyo nitampunguzia adhabu huyu mtu,” lilisema jini lile. Baada ya huyu mzee wa kwanza kuzungumza, mzee wa pili akapiga magoti kwa lile jini akaliambia, “Ewe mkuu katika majini naomba usikilize na mimi kisa changu na hawa mbwa wawili. Kama utaona inasikitisha zaidi naomba umpunguzie adhabu huyu mtu.”
 
HADITHI YA MZEE WA PILI NA MBWA WAWILI WEUSI.

Mzee wa pili akapewa ruhusa ya kusimulia kisa chake na mbwa wawili weusi. “Kwanza utambue ewe mkuu wa majini kuwa hawa mbwa unaowaona ni ndugu zangu wa baba na mama mmoja, kisa kilikuwa hivi.”

Baba yetu alikuwa ni tajiri mkubwa katika mji tuliokuwa tukiishi. Alipofariki alituachia mali nyingi, na tukaigawa mafungu matatu kulingana na idadi yetu. Tuligawana sawa kwa sawa. Ndugu zangu hawa wakajikita kwenye biashara za nje na ndani ya mji. Wakawa wanasafirisha bidhaa kwenda miji mbali mbali, na hata kwenye visiwa.

Mimi niliamua kufungua duka hapa mjini, na kwa neema za Allah biashara ikawa nzuri. Mali yangu ilifikia mara tatu ya ile niliyopata kutoka kwenye urithi. Safari moja ndugu zangu walitoka kibiashara, walikaa kwa muda wa miezi isiyopungua miwili. Siku moja nikaona kuna watu wawili wamesimama mbele ya duka langu. Sikuwatambua watu hawa kutokana na mavazi yao. Walikuwa wamevaa mavazi yaliyochakaa ama yaliyookotwa jaani. Niliastaajabu kuona wananifahamu, baada ya kuzingatia zaidi nikagundua ni ndugu zangu.

Nikawapa mavazi na chakula kisha wakanihadithia mkasa wao. Walikuwa wamepata ajali na malizao zote zimetokomea majini. Nikachukua ile faida yangu na nikaigawa sawa kwa sawa kati yao. Wakaanza biashara tena na hawakukoma, baada ya muda wakaamua kusafiri tena kibiashara. Hali ilikuwa mbaya zaidi wakati huu. Walipata ajali tena majini na wakatupwa nchi kavu wakuwa hata mavazi hawana.

Walipofika nyumbani sikuwatambua kwa kuwa walikuwa uchi na wakiwa wamechafuka ngozi zao. Wakajitambulisha na niliilia kwa huruma. Machozi yangu hayakufaaa kitu kwa kuwa tayari jambo lilishatokea. Kama mara ya kwanza nikawapa mtaji na wakaanza upya biashara zao. Baada ya muda biashara zao zikakaa vizuri, na wakaamua kutoka tena kibiashara. Ila mara hii walitaka niende pamoja nao. Nilipinga zaidi safari hii lakini walinilazimisha na hata maandalizi pia wakanifanyia.

Sikuwa na jinsi nikajiandaa na mimi kwa safari. Nikachukua mali zangu nikazigawa sehemu mbili, sehemu moja nikachukua na nyingine nikaificha. Safari ilianza vizuri na tulifika miji mbalimbali tukifanya biashara. Nilipata faida kubwa na nikanunua baadhi ya bidhaa ambazo ningeziuza pindi nitakapo rejea.

Muda wa kurudi ulipowadia tukawa tunaanda safari ya kurudi. Nilipokuwa matembezini nikitafuta bidhaa na zawadi za kwenda nazo nyumbani, nilipita ufukweni nikakutana na mwanamke aliyevaa mavazi yaliyochakaa. Nilimsalimia na akarudisha salamu, nikamchukua na kumtafutia mavazi yaliyo mazuri. Kwa mavazi yale uzuri wake ulidhihiri mbele yangu. Kwakuwa sikuwa na mke ilibidi nifuate taratibi za kufunga nae ndoa na akakubali. Maandalizi yote yalipoisha nilimchukuaa mke wangu kurudi nae nyumbani.

Tukiwa kwenye jahazi sikugundua kumbe ndugu zangu walikuwa wananionea wivu. Wakawa wananipangia njama ya kuniua. Ulipofika usiku walinichukuaa na kunitumbukiza majini. Baada ya pale sikujua kilichoendelea nikajikuta nipo nchi kavu. Mke wangu akanieleza khabari za yote yaliyotokea na akanieleza kuwa yeye si mtu wa kawaida. Akaniambia pia hatoweza kuwasamehe ndugu zangu kwa walichonifanyia. Nilimuomba asiwaue ila nipo radhi kwa adhabu yeyote ile.

Alinichukua mpaka nyumbani kwangu, kisha akalizamisha jahazi waliopanda ndugu zangu. Mali zangu zote akaziokoa. Siku iliyofuata nikiwa nyumbani nikaona kuna mbwa wawili weusi wanakuja huku wakionesha majonzi na hali ya kuomba msamaha. Nilistaajabishwa na tukio hili. Haukupita muda mke wangu akatokea na akaniambia hawa ni ndugu zangu amewapa adhabu hii. Watakuwa hivyo kwa muda wa miaka kumi.

Miaka kumi sasa imefika, na kwakuwa alinielekeza sehemu ya kukutana, ndio nimetoka kuelekea hapo sehemu. Nikaona niwachukue ndugu zangu kwa kuhofia kuwaacha kwa mtu asije akawadhuru.

Hiki ndicho kisa changu na mbwa hawa ewe mkuu wa majini. “Hii ya kwako ina makubwa zaidi,” lilisema lile jini. Baada ya hapo mzee wa tatu akajitupa miguuni kwa jini na kutaka ruhusa aruhusiwe kuhadithia kisa chake ili iwe ni kafara ya kuachiwa huru mfanyabiashara. Lile jini likasema “Hapana, nimetosheka na hizi mbili, na nimekubali kumuacha huru mfanya biashara.” Lilipokwisha kusema maneno haya likaondoka.

Mfanyabiashara akawashukuru wazee wale. Basi wakati wazee wale wapokaribu na kuondoka yule mfanya biashara akamuuliza mzee yule wa tatu mwenye mbwa mwekundu kuhusu habari ya mbwa yule. Mzee akamwambia ni stori ndefu ila kwa ufupi huyu ni mke wangu. Akaanza kusimulia hadithi yake kwa ufupi huku akiwa na haraka ya kutaka kuondoka eneo lile.
 
Maktaba nimedownload lakin inafail kudownload kitabu chochote
Inatakiwa unapoinstall uallow app iaccess storage yako maana vitabu vinatumia storage yako. Na hilo linakusaidia kusoma hata ukiwa offline.
 
Back
Top Bottom