SULEIMAN ABEID
JF-Expert Member
- Feb 26, 2013
- 390
- 385
MWENENDO WA BEI ZA MBOLEA NCHINI
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hapo awali sababu za kupanda kwa bei ya mbolea ukiacha sababu za vita ya Urusi na Ukraine na janga la UVIKO – 19, hazikuweza kuelezwa kikamilifu. Kwa kuwa wewe ndiye Waziri wa Fedha mwenye dhamana ya kusimamia sera za fedha na bajeti (Fiscal and Monetary Policies) naomba leo tupate maelezo ya kina kwa nini Serikali imeshindwa kudhibiti upandishaji holela wa bei za mbolea unaoongezeka kila uchao, naomba kufanya uchambuzi katika eneo hili kama ifuatavyo:-
Taarifa zinazotolewa na Serikali kuhusu kuongezeka kwa bei katika soko la dunia zinakinzana mfano Waziri wa Kilimo wakati akiwasilisha Bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2022/2023 alikuja na takwimu za vyanzo viwili vya taarifa Wizara na Kilimo na World Bank alisema katika chanzo cha Wizara ya Kilimo bei ya mbolea ya DAP kwa sasa ni Dola za Marekani 1,012 lakini katika Chanzo cha World Bank ni Dola za Marekani Dola 948 (bei hizi ni tofauti kwa Dola za Marekani 64). Upande wa Mbolea ya UREA alisema bei ya mbolea kwa sasa ni Dola za Marekani 1,214 katika chanzo cha Wizara ya Kilimo wakati katika chanzo cha World Bank alisema bei ya mbolea kwa sasa ni Dola za Marekani 723 (tofauti ya Dola za Marekani 491).
- Mheshimiwa Spika, Kitendo cha Waziri wa Kilimo kuwasilisha taarifa mbili tofauti za mwenendo wa bei za mbolea katika soko la dunia kwenye Bunge lako tukufu alikuwa ana maanisha nini? Ni takwimu zipi zichukuliwe kama taarifa rasmi za Bunge, Kwa nini kila tunapouliza bei za mbolea zinatumika takwimu za soko la dunia pekee badala bei halisi ya makampuni yanayoagiza mbolea kutoka viwandani na nchi husika kama Falme za Kiarabu, Qatar, China, Misri, Norway, Morroco, Ubelgiji nk.
- (ii) Kufutwa kwa mfumo wa ununuzi wa mbolea kwa pamoja (Bulk Procurement System - BPS) mwezi Julai 2021, ambapo Waziri wa Kilimo wa kipindi hicho alieleza kuwa mfumo huo ulikuwa unasababisha bei ya mbolea kuwa juu na mbaya zaidi Zabuni za BPS zilizokuwa kwenye mchakato zilifutwa na hii ni kinyume cha Kanuni ya 7(4) ya Kanuni za Ununuzi wa Mbolea kwa Pamoja za mwaka 2017.
Kutokana na due diligence pamoja na zabuni za BPS, TFRA iliweza kufanikiwa kupata bei ndogo sana za mbolea viwandani ikilinganishwa na bei ambazo wafanyabiashara walikuwa wakizisema. Licha ya hapo, kutokana na kurahisishwa sana kwa taratibu za uagizaji wa mbolea ambao uliwezesha hata wasio na uzoefu kabisa na mifumo ya uagizaji wa mbolea kutoka nje ya nchi vikiwemo vyama vya ushirika kushiriki kuagiza mbolea lakini pia ingewezesha ukawepo hata mpango wa wakulima kupata mbolea kupitia mazao yao katika utaratibu wa mikataba ya utatu (tripartite contracts) kama ulivyoshauriwa katika utafiti wa shirika la chakula na kilimo la umoja wa Mataifa (FAO) mwaka 2017 kwenye tovuti ya FAO Publication card | FAO | Food and Agriculture Organization of the United Nations.
(iii) Kusitishwa kwa bei elekezi na usimamizi dhaifu wa bei elekezi ya mbolea. Hali hii imepelekea kukosekana kwa bei inayozingatia gharama halisi ya kununua kiwandani, kuondosha bandarini na kuisambaza mbolea hadi kwa wakulima ambapo kumewafanya baadhi ya wafanyabiashara kupanga na kupandisha bei kiholela/watakavyo kwa maslahi binafsi na baadaye kusingizia UVIKO -19 na Vita huku tukiwaumiza wakulima wetu nchini.
Waraka wa mwisho wa bei elekezi ulitolewa Novemba, 2020 ambapo ilipofika Julai 2021 Waziri wa Kilimo wa kipindi hicho alifuta bei elekezi na kuruhusu wafanyabiashara waingize na kusambaza mbolea nchini bila kufuata bei elekezi na mfumo wa zabuni wa BPS. . Hata hivyo ilipofika Machi 2022 ulitolewa waraka mwingine na Wizara ya Kilimo ingawa pamoja na kuwepo bei elekezi hizo hazifuatwi na Serikali haisimamii kikamilifu kuzuia hali hiyo. Kitendo cha Serikali kufuta na kushindwa kusimamia bei elekezi ya mbolea ni kuvunja kifungu cha 4(1)(u) cha Sheria ya mbolea ya mwaka 2009 na Kanuni ya 56 ya Kanuni za Mbolea za mwaka 2011 zilizopitiwa upya mwaka 2017.
Hivyo kinachoendelea kwenye soko la mbolea ni ukiukwaji wa bei elekezi za mbolea kwani mara tu baada ya kuacha usimamizi wa bei elekezi, bei zilifumka kama mara mbili ya bei elekezi zilizokuwepo na hazijawahi kushuka tena. Wakati Serikali inaanza kusimamia bei elekezi na mfumo wa BPS bei za mbolea zilizokuwepo zilipungua kutoka wastani wa shilingi 100,000 hadi shilingi 40,000 kwa mfuko wa kilo 50 msimu wa kilimo 2017/2018.
Katika kikao alichofanya na wafanyabiashara wa mbolea mwezi Machi, 2022 Mheshimiwa Waziri wa Kilimo amekiri mwenyewe kwamba wafanyabiashara wamekuwa wakipandisha bei holela kwa sababu Wizara kupitia TFRA iliacha kusimamia bei elekezi za mbolea (Taarifa hii ilichapishwa Machi 15, 2022 kwenye YouTube channel ya Wizara ya Kilimo https://youtu.be/jqhud_PYR-o )
Mheshimiwa Spika, Tumeuliza maswali kwenye Wizara husika ambayo yamekosa majibu, tuambiwe kuna maslahi gani ya umma yaliyotokana na kusitishwa bei elekezi? Kwa lugha nyingine, wakulima wamenufaika nini na kusitisha bei elekezi za mbolea? baada ya kufuta BPS na bei elekezi, bei ya mbolea imeshuka? Kinachodhihirika wazi baada ya kufuta BPS na bei elekezi bei za mbolea zilianza kuongezeka kwa kasi kubwa na hii ilikuwa kabla ya vita vya Urusi na Ukraine havijaanza.
(iv) Nchi jirani na zingine zinatumia bandari yetu ya Dar es Salaam kama Malawi, Zambia, DRC, Burundi na Rwanda lakini bei za mbolea ziko chini ikilinganishwa na sisi wakati tunanunua sehemu moja kwenye soko la dunia.
Maelezo ya kwamba bei katika nchi hizo ni ndogo kwa sababu zina ruzuku yanatiliwa mashaka kwa kuwa kabla ya kufuta BPS na bei elekezi hapa nchini kwetu bei ilionekana kuwa chini kuliko hizo nchi jirani na ndiyo maana kipindi hicho kulikuwa na presha kubwa ya utoroshaji wa mbolea kutoka nchini kwenda nchi jirani. upo ushahidi kutoka kwa wakuu wa Wilaya zinazopakana na nchi hizo kuonesha kwamba mbolea za Tanzania zilikuwa zikikamatwa wakati zikitoroshwa kwenda nchi hizo kwa vile bei ya mbolea za Tanzania ilikuwa ndogo kuliko bei katika nchi hizo mfano ni Taarifa ya TBC saa mbili usiku Januari 25, 2018 zilizochapishwa kwenye YouTube ya Global TV .
Usimamizi dhaifu unathibitishwa pia na hotuba ya Bajeti ya Waziri wa Kilimo kwenye ibara ya 89 ambapo Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) ilipokwenda kufanya ukaguzi iliibua mambo mazito ikiwemo kuuzwa kwa mbolea zisizosajiliwa aina 9, mbolea kuuzwa bila vibali, kuuzwa mbolea zilizofunguliwa na uwepo wa mbolea zenye uzani mdogo ikilighanishwa na vipimo.
(v) Utegemezi wa mbolea kutoka nje ya nchi, hakuna mkazo wa kutumia mbolea za asili kama Samadi na Mboji zitokanazo na vinyesi vya mifugo na mabaki ya mazao mashambani. Mifugo yetu inazalisha matani kwa tani ya samadi kila siku lakini aina hii ya mbolea haitumiki kikamilifu na tuko bize kuagiza mbolea kutoka nje ya nchi. Katika hotuba ya Waziri sijaona mkazo, mkakati wala bajeti katika tasnia hiyo ambapo mifugo yetu ndio kiwanda cha malighafi na uzalishaji unafanyika kila siku, mbolea inapatikana kiurahisi na kwa gharama nafuu.
Mheshimiwa Spika, pamoja na nia njema ya Serikali ya kutenga ruzuku ya mbolea kwa wakulima kiasi cha Shilingi Bilioni 150 lakini kwa vile mfumo wa ruzuku huko nyuma ulisitishwa kutokana na kugubikwa na rushwa, upendeleo na taarifa za kughushi (malipo hewa ya mbolea), Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kuwa changamoto zilizosababisha mfumo wa ruzuku kusitishwa zimeshughulikiwa kabla ya kuanza utaratibu mpya wa utoaji wa ruzuku ili kuhakikisha kuwa ruzuku itakayotolewa na Serikali itumike kulipia ‘bei halisi’ ya mbolea na kuleta unafuu mkubwa wa bei kwa wakulima wetu.
Mheshimiwa Spika, hiyo fedha ya ruzuku iliyotolewa na Serikali kiasi cha Shilingi Bilioni 150 kwa ajili ya kutoa ruzuku ya mbolea kwa bei ya sasa itaweza kuingiza tani 64,000 tu ambayo itatosheleza 25% ya mahitaji ya mbolea aina DAP na UREA ambayo ni tani 250,000 kwa mwaka.
Mheshimiwa Spika, ruzuku pekee haiwezi kupunguza bei za mbolea nchini na pengine inaweza kupanda zaidi na wananchi kukosa unafuu wowote hivyo ni lazima Serikali ipitie upya mfumo wa uagizaji na usambazaji wa mbolea nchini ili kurekebisha kasoro zote zinazosababisha bei ya mbolea kupanda kila uchao. Mfumo wa BPS na bei elekezi ambao umefutwa kinyume cha sheria urejeshwe. Aidha ni muhimu kuweka mikakati thabiti ya kuongeza kasi ya uzalishaji katika viwanda vya mbolea nchini, pia kuweka mkazo katika uzalishaji na usambazaji wa mbolea za asili.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ushauri mwingi umekuwa ukitolewa kuhusu mwenendo wa bei za mbolea nchini lakini Serikali imekuwa na kigugumizi kusimamia na kutekeleza ushauri huo nakuomba uridhie kuundwe kwa Tume huru ya Bunge ili kuchunguza mambo yote kwa kina yanayosababisha kupanda kwa bei za mbolea nchini na Bunge lako Tukufu kutoa maelekezo kwa Serikali hatua za kuchukua.
Naomba kuwasilisha,
Luhaga Joelson Mpina (Mb)
Mbunge wa Jimbo la Kisesa
Luhaga Joelson Mpina (Mb)
Mbunge wa Jimbo la Kisesa