ADVERTISEMENT
KAZI imeanza. Kocha Mkuu wa timu ya taifa, Taifa Stars Emmanuel Amunike ameanza kazi yake kwa kuwachomoa nyota sita wa Simba katika kikosi chake kilichoingia kambini tangu juzi, huku Shomari Kapombe akishangaa.
Waliochomolewa kwenye kikosi hicho ni John Bocco, Jonas Mkude, Erasto Nyoni,
Shomari Kapombe, Shiza Kichuya na Hassan Dilunga kwa kosa la kuchelewa kambini.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wilfred Kidau, alisema Kocha Amunike, amefikia uamuzi huo baada ya kushangazwa na jinsi nyota wa Stars wanavyojivuta wanapoitwa timu ya taifa.
"Niliongea na Kocha jana baada ya kuona wachezaji wa Simba walivyoipotezea Stars huku kipa Aishi Manula pekee ndiye aliyefika huku wengine wakikausha, licha ya kambi kuwa hoteli wanayoitumia pia Simba," alisema Kidau.
"Niliongea na baadhi yao walieleza hawakuwa na taarifa mapema licha ya sisi kupeleka barua mapema, tunauunga mkono maamuzi ya Kocha kwa vile timu ya Taifa inahitaji maandalizi na hakuna mtu ambaye yupo juu ya timu ya Taifa."
Hata hivyo akisema kwamba nyota hao walisema walichelewa kupata taarifa, cha ajabu Manula anayecheza nao aliwahi mapema kambini, kitu kilichowaponza.
Kuhusu kambi kuanza mapema na kusimamisha baadhi ya mechi za Ligi, ilihali Stars itaenda kucheza na Uganda, Septemba 9 katika mechi ya kuwania fainali za Afcon 2019, Kidau alisema imetokana na Kocha kuwa mpya, hivyo alihitaji muda wa kutosha kukaa na wachezaji na kuwalisha mbinu zake.
KISIWA MATATANI
Kutokana na ishu ya wachezaji hao kushindwa kuripoti ilihali taarifa ilitolewa mapema, TFF imeamua kuwatia matatani viongozi wa timu ya Simba, Meneja Richard Robert na Kaimu Katibu Mkuu, Hamis Kisiwa kwani walipokea taarifa yao.
"Tumewaita katika Kamati ya Maadili ili kupata majibu, wao nduo waliopokea wito wa wachezaji hao na tuliwasisitizia wafike asubuhi ya leo (jana) Jumatano."
Alisema nafasi za kina Bocco zitazibwa na Salum Kimenya (Prisons), Paul Ngalema (Lipuli), Ally Abdukadir (Lipuli), David Mwantika, Frank Domayo (Azam), Kelvin Sabato na Salum Kihimbwa (Mtibwa).
KAPOMBE ASHANGAA
Mmoja ya nyota hao wa Simba aliyepigwa 'stop' Stars, Kapombe jana saa 7 alipoulizwa juu ya adhabu hiyo, alisema mbona yeye yupo kambini mapema tu.
"Mimi sijui lolote ila nakwambia nipo hapa kambini", alisema kwa kifupi.
Hata hivyo TFF ilisisitiza hakuna mchezaji atakayepokelewa kwani muda uliotangazwa ukishaisha.
Upande wa nyota wa Azam walishawasili kambini mapema, huku wale wa Yanga wakitarajiwa kuingia mara baada ya kurejea kutoka Rwanda na wale wanaocheza nje watajiunga na wenzao Septemba 4 wakimaliza majukumu ya klabu za