Habari kupitia blogu ya Francis Godwin inasema kuwa, Aliyewahi kuwa Waziri wa Elimu Tanzania, bw. Joseph Mungai pamoja na na wapambe wake wawili, Moses na Fidelis ambaye ni katibu wa UVCCM kata ya Mafinga, leo wamesomewa mashtaka 15 yanayohusiana na tuhuma za rushwa kufuatia uchaguzi ulioisha hivi karibuni wa kuwapata wagombea wa Chama Cha Mapinduzi katika ngazi mbalimbali za uongozi nchini Tanzania.
Bwana Mungai na wenzake walitakiwa kudhaminiwa kwa dhamana ya shilingi milioni 5 kila mmoja na wadhamini wawili ambapo mmoja anapaswa kuwa mkazi wa Manispaa ya Iringa, lakini kutokana na kushindwa kutimiza masharti hayo, iliwabidi kuwekwa chumba cha mahabusu, kama inavyoonekana pichani.
Awali, iliripotiwa leo asubuhi kuwa Donatian Kessy wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, TAKUKURU, alisema taasisihiyo itawafikisha mahakamani Bwana Joseph Mungai na Frederick Mwakalebela kwa tuhuma za kujihusisha na vitendo vya rushwa katika uchaguzi huo.
Mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Iringa, Mary Senapee, Mwendesha Mashitaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Prisca Mpeka alisema Mungai pamoja na Moses Masasi na Fidel Cholela ambao wameunganishwa katika mashitaka hayo, wanashitakiwa mahakamani hapo kwa kukiuka Sheria ya Rushwa namba 11 ya mwaka 2007 kifungu cha 15 kipengele cha 1b pamoja kifungu namba 21 sehemu ya kwanza A na kifungu namba 24 sehemu ya nane vya Sheria ya Gharama za Uchaguzi Namba 6 ya mwaka 2010.
Alisema katika tukio lililotokea Julai 8, 2010 katika kata ya Ihalimba, Mungai na watuhumiwa hao wanadaiwa kutoa Sh 10,000 kwa Obadia Mtokoma ambaye ni Mwenyekiti wa CCM wa tawi la kijiji cha Vikula kama kishawishi ili apigiwe kura za maoni.
Wengine kwa mujibu wa Mpeka na kiasi cha fedha walichopewa kwenye mabano kwa lengo la kumpigia kura Mungai siku ya kura za maoni za CCM ni pamoja na Katibu Uchumi na Fedha wa tawi la CCM la kijiji cha Vikula, Konjeta Kiyeyeu (Sh 10,000), Katibu wa CCM wa Kata ya Ihalimba Aldo Lugusi (Sh 10,000), Mwenyekiti wa CCM wa Kata ya Ihalimba Ezekiel Mhewa (Sh 10,000), Katibu wa Fedha na Uchumi wa CCM Kata ya Ihalimba Tulaigwa Kisinda (Sh 10,000), Jiston Mhagama (Sh10,000), Maria Kihongozi (Sh20,000), Lurent Mdaligwa (Sh 5,000), Victory Kalinga (Sh 20,000), Francis Chonya (Sh 2,000) na Alfred Kisinga (Sh 2,000), Issac Tewele (Sh 2,000), Sosten Kigahe (Sh10,000), Raphael Lutomo (Sh 10,000) na Andrew Mkiwa (Sh 20,000).
Mpeka alisema Mungai na watuhumiwa hao wawili Masasi ambaye ni Mhasibu na Cholela ambaye ni Katibu wa Umoja wa UVCCM Mafinga walitoa rushwa hizo kwa wanaCCM hao wakati wakifanya kikao chao cha Kamati ya Utendaji kilichofanyika katika ofisi ya CCM ya kata ya Ihalimba Julai 8, mwaka huu ili wampigie kura za maoni Mungai na hivyo kufanya jumla ya mashitaka ya rushwa dhidi yao kuwa 15.
Hata hivyo katika kura hizo za maoni, Mungai alishika nafasi ya pili kwa kuambulia kura 3,430 dhidi ya kura 6,386 zilizompa ushindi Mahamud Mgimwa katika kinyang'anyiro hicho kilichokuwa na wagombea sita.
Mpeka alisema Fredrick Mwakalebela ambaye naye anatuhumiwa kujihusisha na rushwa wakati wa kampeni hizo katika jimbo la Iringa Mjini, atafikishwa mahakamani hapo Agosti 17 baada ya kushindwa kutokea leo kwa kile kilichoelezwa kwamba ana udhuru.
Chanzo: wavuti.com