NADHARIA Ni kweli Rais Idi Amin Dada alikuwa mla nyama za watu?

NADHARIA Ni kweli Rais Idi Amin Dada alikuwa mla nyama za watu?

Taarifa hii ni nadharia tu, tumeitolea ufafanuzi kwa kadiri ilivyowezekana
<div class="bbWrapper"></div>
 
Tunachokijua
Idi Amin Dada Oumee au kwa wasifu wa kipekee aliojipatia wa Mheshimiwa, Rais wa Maisha, Field Marshal Al Hadji Dkt. Idi Amin Dada, VC, DSO, MC, CBE, Bwana wa Wanyama wote wa Dunia na Samaki wa Bahari na Mshindi wa Dola ya Uingereza Afrika nzima na Uganda alizaliwa mwaka 1925 huko Koboko, Uganda.

Afisa huyu wa kijeshi na Rais wa Uganda (1971-79) ambaye utawala wake ulijulikana kwa hali mbaya iliyosababishwa na ukatili wake alikuwa na asili ya kabila dogo la Kakwa linalopatikana kaskazini-magharibi mwa Uganda.

Amin alikuwa na elimu ndogo isiyo rasmi sana na alijiunga na Jeshi la kikoloni la Uingereza (King's African Rifles)mwaka 1946 kama mpishi msaidizi.

Ingawa alidai kuwa alipigana huko Burma wakati wa Vita vya Pili vya Dunia (1939–1945), rekodi zake za kijeshi zinaonyesha kwamba utumishi wake ulianza mwaka wa 1946.

Alipanda vyeo haraka, na alihudumu katika vita ya Uingereza dhidi ya Uasi wa Mau Mau nchini Kenya (1952–56). Amin alikuwa mmoja wa wanajeshi wachache wa Uganda walioinuliwa hadi cheo cha afisa kabla ya uhuru wa Uganda mwaka 1962, na alishirikiana kwa karibu na waziri mkuu na Rais wa taifa hilo jipya Milton Obote.

Alifanywa mkuu wa jeshi la anga (1966-70). Mgogoro na Obote ulitokea, hata hivyo, Januari 25, 1971, Amin aliandaa mapinduzi ya kijeshi yenye mafanikio.

Alikua Rais na mkuu wa jeshi mnamo 1971, field marshal mwaka 1975, na Rais wa maisha mnamo mwaka 1976.

Vita dhidi ya Tanzania
Jaribio la Amin la kutwaa sehemu za Mkoa wa Kagera wa Tanzania kwenye mwaka 1978 lilisababisha Vita ya Kagera baina ya Tanzania na Uganda na mwisho wa utawala wake, kitendo kilochomfanya akimbie nchi yake.

Amin, ambaye mara nyingi alikuwa akila hadi machungwa 40 kwa siku akiwa uhamishoni kwa sababu alidai kuwa yaliongeza hamu yake ya kushiriki tendo la ndoa aliwekwa kwenye mashine ya usaidizi wa maisha Julai 18, 2003, na kutangazwa kufariki Agosti 16, 2003 huko Jeddah, Saudi Arabia.

Inadaiwa kuwa aliacha watoto kati ya 46 na 54, wake sita na alitekeleza mauaji ya zaidi ya 500,000.

Hukumbukwa zaidi kwa kauli yake isiyopenda uhuru wa kujieleza inayodai kuwa kila mtu anao uhuru wa kujieleza na kutoa maoni lakini hana hakikisho la usalama/uhuru wake baada ya kutoa maoni yake.

Madai ya kula nyama za watu
Baadhi ya majarida yamewahi kumnukuu akikiri ulaji wake wa nyama ya binadamu. Sehemu ya nukuu hizo inasema;

“Nimekula nyama ya binadamu. Ina chumvi nyingi, hata kuliko nyama ya chui."

Sehemu nyingine ya nukuu hizi inayodaiwa aliitoa wakati akifafanua kama hutumia nyama ya binadamu alikiri kuwahi kutumia, lakini hakuwa tena na nia ya kula nyama hizo kutokana na ladha yake ya chumvi nyingi.

“Sio kwa ajili yangu. Nimewahi kula nyama hii (ya binadamu), ina ladha ya chumvi ngingi sana kwangu” alisema Amin.

Nukuu hizi hazipatikani kutoka vyanzo vingine vya kuminika, pia hakuna uthibitisho wa moja kwa moja unaoonesha Amin akifanya jambo hilo.


Hata hivyo, kuna uwezekano pia kwamba Idi Amin hakula nyama ya binadamu. Huenda huu ni uvumi unaotumiwa kuongeza taswira ya ukatili wake, ingawa hakuna njia ya kuthibitisha hili.

Kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba Amin alitambua tetesi hizo na kuzitumia kwa nguvu za kisiasa.

Rais wa zamani wa Venezuela, Hugo Chavez (1999-2013), aliwahi kunukuliwa akimtetea Amin kuwa hakuwa muuaji na mkatili kama inavyojulikana duniani.

“Tulifikiria kuwa Amin ni muuaji mla nyama za watu” Chavez alisema alipokuwa akimuongelea Idi Amin ambaye anatuhumiwa kuwaua mamia ya wapinzani wake wakati wa utawala wake nchini Uganda kwenye miaka ya 1970.

“Nina shaka kama Idi Amin alikuwa muuaji kama inavyosemekana, badala yake alikuwa mwanaharakati mtetezi wa nchi yake” alisema Chavez.

Kauli hii inaongeza pia mashaka huu ya suala la Amin kula nyama za watu.

Hata hivyo, JamiiForums inatambua uwepo wa video inayosimuliza na kuelezea maisha ya Amin, na mojawapo ya matendo yanayoonekana humo ni tukio la ulaji wa nyama mbichi za watu.

Tukio hilo sio halisi, maana mhusika wake sio Idi Amin mwenyewe, bali ni mtu mwingine anayefahamika kwa jina la Joseph Ogola Olita aliyetumika kuwasilisha matendo yanayodhaniwa kufanywa na Amin.

Pamoja na kuwa mtu katili mwenye mkono wa chuma, hadi sasa, hakuna ushahidi wa moja kwa moja unaoweza kusimama kuthibitisha madai ya Amin kwenye ulaji wa nyama za binadamu.
Back
Top Bottom