Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,872
- 34,363
Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimrod Mkono
Hali ya kisiasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ni tete kutokana na kubainika kuwepo kwa mchezo mchafu wa kusambaza kadi feki, wakati Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ikiwahoji makada kadhaa kwa tuhuma za kupokea simu kwa njia ya rushwa.
Simu hizo ambazo Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimrod Mkono, amethibitisha kumwaga kwenye jimbo lake kwa kile alichosema ni kutekeleza ahadi zake kwa wapigakura, zimewatia matatani viongozi wa Jumuiya ya Wanawake wa CCM (UWT) wa Wilaya ya Musoma Vijijini mkoani Mara, wanahojiwa na Takukuru.
Mkono mwenyewe amethibitisha kutoa simu hizo huku akisema si 80 kama inavyodaiwa ila ni zaidi ya 800 akidai ni kutekeleza ahadi yake aliyoitoa kwa wapiga kura wake na kwamba zitasaidia zoezi la kukichangia chama chake, linaloendeshwa kwa njia ya simu.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Takukuru mkoani Mara, Elias Nyororo, tayari viongozi wanne wamekwisha kuhojiwa, wawili kati yao wamekiri kupokea simu hizo na kusema walipewa na mbunge huyo huku wenzao wakikataa.
Kamanda huyo alisema waliohojiwa ni viongozi wa ngazi ya kata na wilaya kutoka Wilaya ya Musoma Vijijini na kwamba zoezi la kuwahoji wengine zaidi linaendelea hadi ukweli wa sakata hilo upatikane.
Ni kweli taarifa zipo mezani kwangu na tumeshahoji viongozi wanne, taarifa tulizonazo ni kwamba simu hizo zimetolewa na mheshimiwa Mkono, nasi tunawahoji kutokana na tuhuma zilizopo, alisema Nyororo.
Alisema waliohojiwa ni wawakilishi wa UWT toka kata na wilaya ya Musoma Vijijini na kwamba Takukuru itakapojiridhisha kutokana na uchunguzi wake kwamba simu hizo si bure, ndipo hatua za kisheria zitachukuliwa.
Hatuwezi kuwanyang'anya simu hizo kwa sasa na wala hatuwezi kuamua hatua za kuchukua hadi kwanza tuwahoji watuhumiwa wote akiwemo mheshimiwa mbunge ili tupate ukweli wake, alisema.
Nyororo hakutaja majina ya watuhumiwa ambao wameshahojiwa ingawa Nipashe imepata mmoja wao aliyekiri kuwekwa kitimoto.
Ingawa hakuweka wazi zaidi, kuna taarifa kuwa kiongozi huyo aliyekuwa Katibu wa UWT tayari amehamishia Wilaya ya Magu mkoani Mwanza.
Inadaiwa kwamba kosa alilofanya Katibu hiyo ni hatua yake ya kukiri kwamba simu hizo ni za Mkono alipohojiwa Takukuru.
Inasemekana kwamba simu nyingi zilimwagwa kwa wajumbe walioshiriki hivi karibuni kwenye kikao cha Baraza la UWT la Wilaya ya Musoma Vijijini kilichofanyika katika ofisi za CCM za wilaya hiyo.
Walifafanua kuwa wilaya hiyo ina kata 27 ambapo kila kata iliwakilishwa na mwenyekiti, katibu na mjumbe, ambapo kila mmoja alipata simu.
Akizungumza na Nipashe kwa njia ya simu jana, Mkono alisema simu alizotoa ni ahadi yake ya muda mrefu kwa wapiga kura wake na kwamba angewanunulia simu ili ziwasaidie katika mawasiliano.
Alisema kuwa amemwaga simu hizo (zaidi 800), hususan kwa wajumbe wa nyumba kumi kwa kufuata utaratibu uliowekwa na viongozi wa CCM kwa kuzikabidhi kwenye chama.
Hiyo ni ofa kwa wapiga kura wangu na sasa zinaweza kusaidia pia katika kutuma ujumbe wa kuchangia chama chao. Hata wakitoa ki-thumni kinafika sehemu husika, alisema Mkono.
Alisema kuwa ni haki yake kukichangia chama na kwamba alichofanya ni mchango wake kwa CCM na wala sio rushwa kama ambavyo baadhi ya watu wanadai.
Huo ndio utaratibu tulioambiwa sisi wabunge na viongozi wa CCM kwamba vitu vinatolewa kwa utaratibu unaoeleweka kwa kukabidhi ndani ya chama na kisha chenyewe ndicho kinagawa. Hivyo ndivyo nilifanya na si kumpa mtu mmoja mmoja, alifafanua.
Katika sakata la kadi feki, makada kadhaa wa CCM wilayani Simanjiro wako matatani baada kubainika kusambazwa katika wilaya hiyo.
Habari kutoka wilayani Simanjiro zinasema kuwa idadi kubwa ya kadi feki zimesambazwa katika kata kadhaa na kwamba lengo lake ni kuwanufaisha baadhi ya watu wanaotaka kugombea nafasi za ubunge na udiwani.
Baada ya kubainika kuwa kuna kadi feki zilizosambazwa, kikao cha Halmashauri Kuu ya wilaya ya Simanjiro kiliketi Juni 28, ambapo pamoja na kujadili hali ya kisiasa, pia kilijadili suala la kumwagwa kwa kadi feki za CCM.
Viongozi wa CCM wa wilaya hiyo, wameithibitishia Nipashe kufanyika kwa kikao hicho kujadili suala la kadi feki na hatua zilizochukuliwa.
Katibu wa CCM Wilaya ya Simanjiro, Jamilah Mujungu, alisema kuwa zaidi ya kadi 1,000 zisizo halali zilibainika kuingizwa katika kata sita kati ya kata 15 za wilaya hiyo.
Mujungu alisema baada ya kuzigundua walianza kuchukua hatua kuhakikisha zinasimamishwa na kuzikamata zilizokuwa zimeshasambazwa.
Alisema kuwa hatua nyingine ni kuwasimamisha watendaji waliobainika kuhusika katika njama hizo kwa kuzipokea na kuzisajili katika daftari la orodha ya majina ya wanachama ambao mwaka huu ndio watakaowapigia wagombea udiwani na ubunge kura za maoni.
Aliwataja watendaji waliosimamishwa kuwa ni Katibu wa Kata ya Kitwai, James Lesile, Katibu wa Kata ya Rufulemiti, Daniel Mbalakai na Katibu Mwenezi wa Kata ya Terrat, Isaac Abraham.
Aidha, alisema kuwa chama kimemvua uongozi Katibu wa Tawi la Terrat, Simvu Elija, na kwamba wote wamechukuliwa hatua hiyo kwa tuhuma mbalimbali ya ukiukaji wa maadili katika mchakato wa kuelekea katika uchaguzi mkuu.
Mujungu alidai kuwa Lesile alipokea kadi feki na kuzisaini pamoja na kuzipiga muhuri halali wa chama hivyo kuingilia jukumu la katibu wa tawi.
Alisema tuhuma zinazomkabili ni kupokea kadi feki na kuzihalalisha, kutekeleza majukumu yasiyo yake na kuhujumu daftari la orodha ya wanachama.
Kwa upande wa Mbalakai, Mujungu alidai aligonga muhuri kadi ambazo si halali, eneo lake kuwa na kadi nyingi feki pamoja na kuzigonga mhuri wa kata kinyume cha utaratibu.
Kuhusu Abraham, alidai amekosa maadili kwa kuchonga muhuri wa katibu mwenezi ambao aliufanyia kazi katika vikao vya maamuzi ambayo yameathiri shughuli za chama.
Kuhusu Elija, Mujungu alidai kuwa amefutwa kazi baada ya kubainika kubadilisha majina yaliyokuwa yamepitishwa na vikao vya CCM katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa mwaka jana na kwamba baada ya uchaguzi huo, aliwatumia viongozi aliowaingiza kufanya maamuzi kadhaa ya kukipaka chama matope.
Alisema maamuzi ya kuwasimamisha watendaji watatu yalipendekezwa na Kamati ya Siasa na kuridhiwa na Halmashauri ya Wilaya na kwamba uamuzi wa kumvua uongozi Elija ulifanywa na Halmashauri ya Wilaya.
Pia Halmashauri ya Wilaya imeagiza hatua kali ziendelee kuchukuliwa dhidi ya kiongozi, mtendaji na mwanachama atakayekiuka maadili ya chama, alisema.
Katika hatua nyingine, CCM Kata ya Kivukoni mkoani Dar es Salaam, kimelalamikiwa kwa kuandikisha wanachama wapya kwa hila lengo likiwa ni kukipatia ushindi mnono katika chaguzi mbalimbali zijazo ukiwemo wa madiwani ambao baadaye watamchagua Meya wa Jiji.
Hali hiyo imesababisha baadhi ya wananchi wakiwemo wanachama wa chama hicho kuweka pingamizi kwa baadhi ya wananchi waliojiandikisha wakidai kuwa si wakazi wa eneo hilo hivyo wamekosa sifa za kujiandikisha eneo hilo.
Chama hicho kinashutumiwa kuandikisha wanachama kutoka vyuo vya Usimamizi wa Fedha (IFM), Mwalimu Nyerere na Chuo cha Utumishi wa Umma Magogoni jijini Dar es Salaam.
Wanaotaka kuweka pingamizi walidai kuwa baadhi ya wananchi waliojiandikisha kwenye kata hiyo si wakazi wake hivyo wanataka kujua uhalali wa wao kujiandikisha kwenye eneo hilo.
Katika moja ya nyaraka za CCM ambayo Nipashe inayo, inaonyesha kuwa wanachama wengi wameandikishwa uanachama siku moja jambo ambalo linatia shaka kuhusu uhalali huo wa uanachama.
Waraka huo unaonyesha zaidi ya wanachama 300 wa CCM wa Kata hiyo walijiandikisha kuomba uanachama siku moja ya tarehe 01/01/2010, wengine zaidi ya 50 walijiandikisha tarehe 25/1/2010.
Barua iliyoandikwa na kada mmoja wa CCM Tawi la Kivukoni kwenda kwa Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Yusuf Makamba, inasema anahujumiwa na baadhi ya watendaji.
Alidai kuwa anashangazwa kuhusishwa na kufutwa kwa majina ya wanachama halisi kwenye kadi zao na kuandikwa majina ya watu wengine kwenye kadi hizo kitu ambacho alisema hakimhusu.
Alisema matatizo hayo yameleta mgawanyiko mkubwa miongoni mwa wanachama na viongozi wa ngazi za matawi, kata, wilaya na mkoa kwa ujumla kwani imefikia mahali wanaletwa watu kutoka maeneo mengine kama Gongo la Mboto na kujiandikisha katika daftari la kudumu la waopiga kura.
Tujiulize watu hawa wametoka huko walikotoka wakaacha kujiandikisha huko na kuja kujiandikisha katika Kata ya Kivukoni ni kwa ajili ya maslahi ya nani? Kwani hali hii ndiyo imeleta mgogoro katika matawi yetu kwa kuletewa wanachama mamluki tuwaingize kwenye matawi yetu, alisema.
Alisema hali hiyo inaweza kuvuruga zoezi zima la kura za maoni kuelekea katika kuwapata wagombea wa CCM hasa katika kata nyeti kama Kivukoni ambayo Mwenyekiti wa CCM taifa, Rais Jakaya Kikwete anaishi.
Ofisa Mtendaji Kata ya Kivukoni, Harold Uisso, alisema ni kweli kuna watu walikwenda kuweka pingamizi kwa baadhi ya wananchi waliojiandikisha, lakini walikosa sifa za kuweka pingamizi hilo.
Alisema aliwaelekeza watu hao kuleta vitambulisho vyao vya kupigia kura na waeleze sababu za kuweka pingamizi hilo, lakini hawakufanya hivyo hadi kufikia jana.
Kuna masharti matano ya kutimiza mtu anayetaka kuweka pingamizi moja ikiwa ni kuwa na kitambulisho cha kupigia kura na aelezea alijiandikisha wapi na lini, amtaje mtu anayemwekea pingamizi kisha atoe sababu za kuweka pingamizi wale waliokuja hawakuwa na sifa hizo wakaenda hawajarudi, alisema Uisso.
Aidha, alisema watu wakishaweka pingamizi ofisi yake inakagua kuangalia ukweli wa pingamizi lililowekwa na baada ya hapo ndipo hatua zaidi zinachukuliwa.
Alithibitisha kusikia maneno ya watu kujiandikisha katika kata hiyo wakati si wakazi wa eneo hilo, lakini alisema hajui ukweli wa malalamiko ya wananchi hao hadi uchunguzi utakapofanyika.
Kwa upande wake, Katibu wa UVCCM wa kata hiyo, Bakari Itariel, alisema hawana takwimu sahihi za wanachama wa CCM kwa kata hiyo kwa kuwa uhakiki bado unaendelea.
Alisema takwimu sahihi zitapatikana baada ya kazi ya kuhakiki wanachama litakalomalizika Julai 15, mwaka huu kwa kuwa kuna wanachama wengi wamehama na wengine wapya wamejiunga na chama hicho.
Imeandikwa na Joseph Mwendapole na Sabato Kasika
CHANZO: NIPASHE