Riwaya: Bondia

Jina la Rachel limenistua kulikuta humu kwenye riwaya
Sawa kabisa ram! ra=rachel
m=? m itakuwa initial ya jina la ubini wako! Naendelea lkuitafuta!
 
Last edited by a moderator:
Casuist ni njema sana kukutana na Bondia asubuhi ya leo. Twende kazi Mkuu.
 
Last edited by a moderator:
duuh...jina la riwaya limenitisha..nikajua kimenuka humu ndani....
 
RIWAYA: BONDIA
MTUNZI: HUSSEIN ISSA TUWA


SEHEMU YA NNE


Yule kocha alimtazama mpiganaji wake kwa namna ya kuridhishwa na makeke yake, kisha akamueleza.
“Utapanda ulingoni na Chumbi wa timu ya Wandava Boxing katika uzito wa Bantam! Chumbi ni moto wa kuotea mbali na sina haja ya kukumbusha juu ya hilo, tatizo lako kubwa ni kujiamini kuliko kawaida Dulla, na usipoangalia, hilo ndilo litakuwa kaburi lako katika ndondi…” Hapo macho ya yule mtu mwenye upara yalimuona Roman akiwa ameketi kwenye benchi kando kabisa ya ukumbi ule na hapo hapo alikatisha maelezo yake. Badala yake uso wake ulijaa mshangao huku akifinya macho kumtazama vizuri yule mtu aliyetoka gerezani asubuhi ile. Wale vijana wote nao wakafuata macho ya kocha wao na kumgeukia Roman.
“Roman…!?” Yule mzee alisema kwa sauti ya chini iliyojaa mshangao na maswali ya kutoamini.
Taratibu yule bwana aliyejengeka kimazoezi aliwasogeza pembeni wale vijana waliokuwa mbele yake na kumuendea Roman kwa mwendo wa taratibu. Roman aliinuka kutoka kwenye lile benchi alilokuwa amekalia na kuanza kumsogelea yule mzee. Walitazamana kwa muda huku wakisogeleana, na hatimaye yule mzee alijihakikishia kuwa ni kweli macho yake yalichokuwa yakimuonesha, kwamba kwa hakika yule aliyekuwa akimuona alikuwa ni mtu aliyemtambua kwa jina la Roman.
“Roman! Roman…! Umetoka…?”
Walikimbiliana na kukumbatiana kwa nguvu na upendo wa hali ya juu kwa muda mrefu. Hatimaye yule mzee alimsukuma nyuma kidogo Roman na kumtazama usoni huku akiwa amemshika mabega.
“Ah! Roman! Umetoka lini? Mbona sikuwa na taarifa…? Unaonekana uko fiti sana!” Aliuliza.
“Leo, Kocha! Nimetoka leo…asubuhi hii hii…” Roman alimjibu yule mzee ambaye kufikia pale hakuweza kuyazuia machozi yasimtiririke.
“Ah, Roman my boy! Miaka miwili sio mingi kumbe afterall eenh?” Alisema huku akiachia machozi yamtiririke bila ya kufanya bidii yoyote ya kuyafuta.
“Yeah, Coach…sio mingi kama ilivyoonekana hapo mwanzo.” Roman alimjibu huku akimpangusa machozi yule mzee aliyemwita ‘Coach’ kwa kiganja cha mkono wake. Wale vijana waliokuwa wakifanya mazoezi pale ukumbini walikuwa wakitazama tukio lile kwa udadisi wa hali ya juu. Yule bwana mwenye upara alimshika mkono Roman na kumuongoza kuelekea kule kwenye mlango aliotokea hapo awali na kuwakuta wale vijana wake wakifanya mazoezi pale ukumbini.
“Come on! Twende tukaongee ofisini kwangu!’ Alimwambia bila kujali mshangao ulioonekana wazi kwenye nyuso za wale wanafunzi wake. Waliingia ndani ya ile ofisi na yule bwana alifunga mlango na kumuelekeza Roman aketi kwenye kiti kilichokuwa mbele ya meza yake mle ofisini naye akaketi juu ya meza, akikiacha kiti chake kilichokuwa nyuma ya ile meza.
Walitazamana kwa muda, kisha Roman aliongea kwa upole. “I am out now Mark (Nimetoka sasa Mark). Umeniwekea vitu vyote nilivyokuagiza?”
Makongoro “Mark Tonto” Tondolo, kocha wa ndondi wa muda mrefu, na bingwa wa zamani wa taifa wa ngumi za ridhaa katika uzito wa juu (Heavy Weight) alimtazama Roman kwa muda bila ya kusema neno. Kisha aliinuka na kuzunguka nyuma ya ile meza aliyokuwa ameikalia na kutoa faili jembamba kutoka kwenye droo ya meza ile na kumkabidhi.
“Kila kitu kimo humo ndani Roman, kama jinsi ulivyoagiza!” Alimwambia.
Roman alilipokea lile faili na kulifungua kidogo kisha akaliweka juu ya mapaja yake, na kumtazama tena yule mtu mzima aliyependa kumwita kwa jina la utani “Mark Tonto”.
Walitazamana.
“Una uhakika na unalotaka kulifanya Roman?” Mark alimuuliza huku akimtazama machoni. Roman hakufanya haraka kumjibu. Na alipomjibu, alikuwa na asilimia mia moja za kujiamini katika jibu lake.
“Kwa mwaka mzima nimekuwa nikijiandaa kwa jambo hili Mark. Sasa ndio wakati wa kuanza kutekeleza azma yangu, na Mwenyezi Mungu ni shahidi juu ya hilo!”
Makongoro Tondolo alimtazama Roman kwa muda mrefu bila ya kusema lolote. Na katika muda huo, Roman naye alikuwa akimtazama yule mzee bila ya kusema neno kwa muda, kisha akamuuliza huku akiendelea kumtazama kwa macho makavu.
“Uko tayari kunisaidia kama tulivyokubaliana mara ya mwisho uliponitembelea gerezani? Au umebadili mawazo?”
Makongoro Tondolo aliendelea kumtazama kwa makini huku akionekana wazi kuwa kichwani mwake alikuwa na mawazo mengi.
“Kama umebadili mawazo mi’ n’taelewa Mark. Lakini sitorudi nyuma. Nitaendelea na azma yangu, na wewe au bila wewe!” Roman alimwambia kwa msisitizo. Mark Tonto aliinuka kutoka kwenye meza aliyokuwa amekalia na kwenda kusimama hatua chache kutoka pale alipokuwa ameketi Roman, bado uso wake ulionekana kuwa na mawazo mengi. Kisha alirudi tena pale alipokuwako Roman na kusimama mbele yake.
“Mimi niko tayari kukusaidia Roman. Unajua kuwa siwezi kukukatalia. Ila kusema kweli nigefurahi na ningekuwa na amani zaidi kama ungeamua kuachana kabisa na jambo hili Roman…”
“No! God Damn it, No! We’ unajua nimepitia wapi kabla ya kuja hapa kwako Mark?” Roman alifoka huku akipiga kiganja cha mkono wake juu ya ile meza naye akisimama, akiwa amelibana lile faili kwapani kwake. “I come straight from the cemetery Mark (Nimekuja moja kwa moja kutoka makaburini Mark)! Rachel yuko chini ya rundo la udongo kule Mark! Na huko amelala milele, Damn shit! Milele!” Alimalizia kwa hasira huku akinyooshea mkono wake kule alipotokea. Mark alinyanyua juu mikono yake kwa ishara ya kutaka amani na kumsogelea kwa mwendo wa haraka.
“Okay, Okay, Okay, Roman, Okay! Usiwe na jazba…nilikuwa nakupa mawazo yangu tu!”
“Lakini utawezaje kufanya hivyo Mark? Baada ya yote yaliyotokea…baada ya yote unayojua kuwa nimelazimika kukabiliana nayo!”
“Okay Roman, tuyaache hayo! Nilikuwa natoa rai hiyo kutokana na kujali maslahi yako mwenyewe na si kwa sababu ya kutojali yaliyokukuta. I am sorry, Okay?” Mark alimjibu kwa upole. Roman alimtazama yule mzee kwa muda, kisha akaketi taratibu kwenye kile kiti alichokuwa amekalia hapo awali. Kwa muda mrefu walibaki kimya mle ndani.
“Kwa hiyo utanisaidia au vipi?” Hatimaye Roman alimuuliza huku akitazama sakafuni bila ya kumtazama.
“Of Course I will help you Roman, why not?” Mark Tonto alimjibu kwa uhakika wa hali ya juu. Roman alimtazama kwa muda, kisha aliinuka na kumkumbatia kwa mara nyingine yule mzee. “Ahsante sana, Mark! Ahsante sana.”
Mark Tonto alimsukuma nyuma kwa upole na kumtazama usoni kwa upendo sawia kabisa na ule wa baba kwa mwanaye ampendaye kwa dhati akiwa amemshika mabega kwa mikono yake miwili.
“Sasa unahitaji kupata josho la nguvu, utoe kabisa jasho na harufu ya Ukonga, Roman. Halafu ukakate hizo nywele…upumzike, tukatembee mjini ujikumbushe jiji ulilolikosa kwa muda mrefu,au siyo?” Alimwambia.
Roman alitabasamu.
“Ni kweli Mark, nahitaji kutoa hii minywele ya gerezani na kuoga maji yaliyostaarabika. Lakini sina muda wa kupumzika wala kutembea hovyo mjini. Nina lengo la kutimiza, na wewe sasa hivi umetoka kuniahidi kuwa utanisaidia kwalo…” Roman alimjibu huku akipitisha mkono wake kichwani. Mark alimtazama kwa muda.
“Okay, Roman, naona umedhamiria…basi nadhani ungeanza kukata nywele kwanza, halafu ndio ukaoge…” Alimwambia.
Mark alimpeleka Roman kwenye moja ya saluni zilizokuwa nje ya ile klabu ya ndondi ambayo alikuwa akiimiliki. Kisha waliingia kwenye moja ya maduka ya nguo za kileo yaliyokuwa yameizunguka ile klabu ambamo Roman alichagua nguo safi zilizoonekana kumtosha na kumkaa vyema.
Bila ya wao kujua, Dihenga na Kate walikuwa wakifuatilia nyendo zao zote wakiwa ndani ya gari lao waliloliegesha mbele ya yale maduka mengi yaliyoizunguka ile klabu. Waliporudi tena ndani ya ile klabu, Roman aliingia bafuni kuoga kwa mara ya kwanza akiwa mtu huru. Alitumia muda mrefu sana kule bafuni, akijisugua kwa nguvu, kama kwamba kwa kufanya vile angekuwa anafuta kabisa ukweli kuwa alikuwa ametoka gerezani na mambo yote yaliyotokea huko nyuma yangefutika katika maisha yake kama jinsi ambavyo taka na jasho vilivyokuwa vikiutoka mwili wake wakati akioga. Na wakati akioga, kumbukumbu ya marehemu Rachel Koga ilimjia kichwani mwake na aliljikuta akibubujikwa upya na machozi, na kwa mara nyingine tena alijithibitishia kutekeleza azma aliyotoka nayo gerezani. Azma ambayo ilionekana sio tu kumtia shaka yule askari wa kike aitwaye Fatma, bali pia rafiki yake na mwalimu wake Makongoro”Mark Tonto” Tondolo, ingawa alikuwa amekubali kumsaidia.
Baada ya kumaliza kuoga na kuvaa nguo zake mpya, Mark alimtaka aende naye nyumbani kwake, ambako hapakuwa mbali na ile klabu, ili ampatie chumba cha kulala na awe anaishi naye, kwani baada ya kutoka gerezani, Roman hakuwa na mahala pa kuishi.
“Hapana Mark. Mimi ningependa kulala hapa hapa klabuni…humu ofisini kwako kama hutajali. Nitahitaji godoro tu, labda na chandarua kama haitakuwa usumbufu…” Roman alimwambia.
“Nini? Roman unachekesha! Yaani utoke gerezani halafu uje huku uraiani tena ulale chini? Yaani ulale humu wakati mi’ n’na nyumba yenye nafasi ya kutosha? No way bwana! No way! Unakuja kuishi kwangu Roman, na kwa hili hakuna mjadala!” Mark alimjia juu. Lakini Roman alikuwa ameshaamua.
“Hebu fikiri hali ya nyumbani itakuwaje Mark. Mkeo, wanao…watajisikiaje kuwa wanaishi na mtu aliyetoka gerezani nyumbani mwao?” Alimuuliza kwa upole. Mark alianza kupingana naye, lakini Roman alimkatisha. “Wacha Mark! Msaada ulionipatia mpaka sasa, na ambao uko tayari kunipatia, ni mkubwa sana. Mimi nitakuwa radhi kabisa kulala humu ofisini Mark. Kama nikiwa na godoro dogo sitakuwa na wasiwasi hata kidogo. Gerezani nilikuwa nalala sakafuni kabisa bwana!”
Mark alizidi kupingana naye.
“Lakini hapa sio gerezani Roman. Kwa nini unataka kujitesa bila ya sababu? Nakuhakikishia kuwa familia yangu haitakuwa na tatizo lolote na wewe kuwepo nyumbani kwangu…”
“Sio rahisi Mark, mimi naelewa! Najua una nia nzuri sana na mimi, lakini haitakuwa vyema. Hata mimi mwenyewe sitajisikia vizuri kuwa nyumba moja na watu watakaokuwa wakinong’onezana kila ninapotokea kuwa ‘huyo ndiye jamaa aliyetoka jela…’ Sio freshi kabisa!”
“Aaah. Lakini hiyo si itakuwa kwa muda tu? Hatimaye itazoeleka na kuisha kabisa. Unanitia unyonge sana Roman…”
“Usikonde juu ya hilo kocha wangu. Nadhani hii itakuwa ni njia nzuri na salama zaidi. Hasa ukizingatia juu ya mpango nilionao kichwani mwangu hivi sasa. Haitachukua muda kabla polisi hawajaanza kupiga-piga hodi nyumbani kwako na kuanza kuuliza maswali kwa mkeo na wanao juu yangu kama nikiishi nawe, hujafikiria juu ya hilo?” Roman alimuuliza.
“Khah! Polisi? Kwa nini polisi waje kuwauliza maswali wanangu? What are you talking about Roman (Ni nini unachoongea Roman)?” Mark Tonto alimuuliza kwa mshangao mkubwa. Roman alitikisa kichwa kwa masikitiko, kisha akamuelezea tukio zima lililotokea siku ile mara baada ya yeye kutia mguu nje ya gereza.
Mark alichoka!
“Inspekta Fatma? Ni nini tena anachotaka yule mwanamke lakini? Yaani amediriki kuja kukusubiri nje ya gereza na kuanza kukutishia…(alisonya) Ana wazimu nini?” Mark alikasirika kupita kiasi. Alibaki akihema kwa hasira. Kisha akajijibu mwenyewe. “Ana wazimu sana yule mwanamke!” Akasonya tena.
Roman alimtazama kwa utulivu.
“No Mark. Hana wazimu. Na nadhani wewe mwenyewe unaona ni jinsi gani isivyokuwa salama kwa mimi kuja kuishi nyumbani kwako sasa hivi.” Alimwambia.
Mark hakuwa na jibu. Ni wazi kuwa Roman alikuwa sahihi.
Hatimaye walitoka nje ya ile ofisi na Mark alimtambulisha Roman kwa wale mabondia wengine wa ile klabu yake ya ndondi.
“Tumepata bondia mwingine katika timu yetu, anaitwa Roman. Tutaanza naye mazoezi kesho. Na sasa sote tutaenda kupata soda hapo baa kwa ajili ya kumpokea mpiganaji mpya katika timu yetu, kwani sasa tuna uhakika zaidi wa kuchukua sio tu ubingwa wa wilaya, bali hata wa taifa.” Kocha Makongoro Tondolo aliwaambia wanafunzi wake. Wale vijana walilipuka kwa vifijo, hoi hoi na mbinja nyingi kumshangilia bondia mpya miongoni mwao, hususan ule mwaliko wa kupata soda. Kundi zima lilielekea baa na kila mmoja aliagiza soda aliyoipenda.
Kocha Makongoro Tondolo alikaa na bondia wake mpya, pamoja na mabondia wake wengine na kunywa soda pamoja nao. Ilikuwa ni furaha kubwa kwa wale vijana, kwani waliuona ubingwa wa taifa ukiwa mikononi mwao. Lakini kwa kocha Mark Tonto na Roman, ule kwao ulikuwa ni mwanzo wa kutekeleza mpango mkali na wa hatari sana kwao iwapo utagundulika.
Na kwenye kona moja pembeni kabisa ya baa ile, Dan na Kate walikuwa wakishuhudia mkusanyiko ule kwa udadisi mkubwa, huku wakipata vinywaji taratibu. “Mmnh! Master D, unadhani ni nini kinaendelea pale sasa?” Kate alimuuliza Dihenga huku akimkodolea macho Roman. Dan alipeleka bilauri yake ya bia kinywani na kupiga funda kubwa kabla ya kuishusha ile bilauri mezani na kuachia mbwewe kubwa. Mdomo wake ulifanya tabasamu dogo la upande mmoja na kumjibu huku naye akitazama kule walipokuwapo akina Roman.
“Sijui. Lakini nadhani kinachotokea pale ndicho kile haswa nilichokuwa nikikitaka. Na nadhani kazi yetu haitakuwa ngumu sana…”
Kate alimtazama kwa mshangao, ni wazi kuwa hakuwa amemuelewa. Halafu akatazama tena kule walipokuwa akina Roman, na kumgeukia tena yule mtu aliyependa kumwita Master D.
“Sijaelewa…” Alimwambia. Lakini Master D alitoa pesa ya kulipia vinywaji vyao na kuiweka juu ya meza huku akimwita mhudumu kwa ishara ya mkono wake naye akiinuka.
“Utaelewa kadiri tunavyoendelea mrembo. Twen’zetu.” Alimjibu huku akianza kuondoka eneo lile. Kate alimtazama kwa mshangao huku naye akiinuka na kumfuata.
Saa moja baadaye Roman alikuwa ameketi kwenye kiti cha Mark Tonto lile faili likiwa wazi mbele yake pale mezani. Alilitazama kwa muda lile faili, juu yake kukiwa kumeandikwa kwa kalamu ya rangi yenye ncha nene:


........Deusdelity Macha, a.k.a. “Deus-deadly” Macha.


........WBA Champion, Super Middle.


(Deusdelity Macha, a.k.a. “Deus-wa mauaji” Macha. Bingwa wa dunia katika uzito wa Super Middle ,anayetambuliwa na shirikisho la ndondi duniani, WBA.)
Roman alilitazama lile jina kwa muda mrefu. Kisha alilifungua lile faili na kuanza kulisoma.


**KATE na DAN wanataka kitu gani kwa ROMAN??
**Na huyu Deus ni nani hadi taarifa zake zimehifadhiwa katika faili zikimngoja Roman atoke jela???


BPM Sangomwile Mamamercy jonnie_vincy Khantwe mbalu byb sac mlyn VAN HEIST nrango mangimeza muuza ubuyu Jullie ZIgunga Mojaculbby mugaru
 
RIWAYA: BONDIA
MTUNZI: HUSSEIN ISSA TUWA


SEHEMU YA TANO


Kate alimtazama kwa mshangao, ni wazi kuwa hakuwa amemuelewa. Halafu akatazama tena kule walipokuwa akina Roman, na kumgeukia tena yule mtu aliyependa kumwita Master D.
"Sijaelewa…" Alimwambia. Lakini Master D alitoa pesa ya kulipia vinywaji vyao na kuiweka juu ya meza huku akimwita mhudumu kwa ishara ya mkono wake naye akiinuka.
"Utaelewa kadiri tunavyoendelea mrembo. Twen'zetu." Alimjibu huku akianza kuondoka eneo lile. Kate alimtazama kwa mshangao huku naye akiinuka na kumfuata.
Saa moja baadaye Roman alikuwa ameketi kwenye kiti cha Mark Tonto lile faili likiwa wazi mbele yake pale mezani. Alilitazama kwa muda lile faili, juu yake kukiwa kumeandikwa kwa kalamu ya rangi yenye ncha nene:


Deusdelity Macha, a.k.a. "Deus-deadly" Macha.
WBA Champion, Super Middle.


(Deusdelity Macha, a.k.a. "Deus-wa mauaji" Macha. Bingwa wa dunia katika uzito wa Super Middle ,anayetambuliwa na shirikisho la ndondi duniani, WBA.)
Roman alilitazama lile jina kwa muda mrefu. Kisha alilifugua lile faili na kuanza kulisoma.




Ndani ya lile faili kulikuwa vipande vya magazeti vilivyokatwa vizuri kutoka kwenye kurasa za magazeti mbali mbali ya hapa nchini, ya kiswahili na ya kiingereza, na vilikuwa vimepangwa kutokana na tarehe za matukio yaliyokuwa yakiripotiwa katika magazeti yale.
Vipande vyote vile vya magazeti vilikuwa vikiripoti juu ya habari za bondia Deusdelity Macha, bingwa wa dunia uzito wa Super Middle anayetambuliwa na WBA.


Na kutokana na habari zilizokusanywa kwa uangalifu na umakini wa hali ya juu katika faili lile ndani ya mwaka mmoja na nusu, Roman aliweza kusoma na kuelewa kila kitu juu ya bingwa huyu wa dunia katika uzito wa Super Middle aitwaye Deusdelity Macha. Ambaye mashabiki wa ndondi nchini walimbatiza jina la Deus-deadly, yaani "Deus-wa mauaji".
Aidha, katika faili lile kulikuwa kuna picha mbali mbali za bondia Deusdelity Macha akiwa katika mapambano mbali mbali ya ngumi zilizomuonesha akiwasulubu vibaya wapinzani wake.
Habari zilizokusanywa na Mark Tonto katika faili lile zilieleza kwamba Deusdelity Macha aliingia katika ulimwengu wa ngumi za kulipwa (Professional Boxing) kiasi cha mwaka mmoja na nusu uliopita, akitokea kwenye ngumi za ridhaa (Amateur Boxing) ambako alikuwa akipigana katika timu ya vikosi vya majeshi, yeye akiwa mwanajeshi wa jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Uwezo wake mkubwa wa kuzipiga ulionekana kwa kiasi kidogo sana wakati alipokuwa katika michezo ya majeshi, ambapo vikosi vyote vya majeshi ya ulinzi na usalama nchini huwa vinashiriki katika michezo mbalimbali, ikiwemo ndondi. Huko, Deusdelity, aliingia kwenye ndondi tangu akiwa katika chuo cha maafisa wa jeshi Monduli, ambako yeye pamoja na wenzake wachache walijiunga mara baada ya kumaliza elimu ya juu ya sekondari.
Baada kupigana ngumi za ridhaa kwa muda mrefu akiwa mhasibu wa jeshi la wananchi wa Tanzania, promota maarufu wa ngumi nchini alimuona na kuvutiwa naye. Aliamua kumshawishi ajiunge na ngumi za kulipwa ili ajiendeleze zaidi katika ndondi na wote wanufaike zaidi katika mchezo ule uliokuwa ukijipatia wapenzi wengi nchini. Deusdelity alilikubaliana naye mara moja.
Swala la Deus kujiunga na ngumi za kulipwa halikuwa jepesi kutokana na kazi yake, kwani ngumi za kulipwa zilihitaji awe anakuwa nje ya kituo chake cha kazi katika nyakati ambazo muajiri wake, JWTZ, pia alikuwa akimhitaji. Alitakiwa aandaliwe mapambano mbali mbali ya kimataifa ambapo pamoja na yeye kulazimika kuletewa wapinzani kutoka nje ya nchi, pia alitakiwa asafiri nje ya mipaka ya nchi kwa ajili ya mapambano; jambo ambalo lilikuwa gumu kwake, akiwa kama askari wa jeshi la wananchi wa Tanzania.


Ni katika mazingira kama haya, ndipo Deusdelity Macha alipolazimika kuacha kazi yake ya uanajeshi ili aweze kujiingiza kikamilifu katika ngumi za kulipwa. Mwandishi wa habari ile alikiita kitendo cha Deus kuamua kuacha kazi yake ya kulitumikia taifa, ili aweze kushiriki kikamilifu katika ndondi za kulipwa kuwa ni "uanamichezo halisi" na kuwa ni kitendo kilichostahili sifa kubwa.
(Kufikia hapa Roman aliachia tabasamu dogo la dharau huku akitikisa kichwa kuonesha kutokubaliana kabisa na hoja ile).
Baada ya hapo Deus aliweza kuandaliwa mapambano kadhaa na promota wake tajiri yaliyofanyika humu humu nchini dhidi ya mabondia wengine wa hapa nchini. Kutokana na uzito wake, Deus aliingia katika ndondi kwa uzito wa Super Middle, ambao ulihitaji mpiganaji awe na uzito wa kati ya kilo 51.1 hadi 51.5. Na ni hapa ndipo alipojipatia sifa kem kem katika upiganaji wake na jinsi alivyoweza kuwasulubu wapinzani wake.




Katika kipindi hiki, akiwa na miezi minne tu tangu aingie katika ngumi za kulipwa, Deus alipambanishwa na bingwa wa dunia wa uzito wa Super Middle kwa wakati ule, katika pambano lisilokuwa la kugombea ubingwa wowote. Katika pambano hilo, Deus alifanikiwa kumshinda bingwa huyo wa dunia kwa Knock Out!
Pamoja na kuwa pambano halikuwa la ubingwa au mkanda wowote, ushindi huu ulitosha kabisa kumuweka Deus katika ramani ya ndondi sio tu hapa nchini, bali duniani kwa ujumla. Na baada ya hapo Deus hakuzuilika tena.


Alifanikiwa kuwatwanga vibaya wapinzani wake wa hapa nchini, kiasi promota wake akafikia hatua ya kumnadi kuwa Deus hakuwa na mpinzani yoyote nchini. Hivyo alikuwa anamtafutia wapinzani kutoka nchi za jirani za Afrika ili angalau apambane na mabondia wenye uwezo sawa na wake. Pambano lake la kwanza la kimataifa alipambanishwa na bondia kutoka Uganda, na Deus alimdondosha chini kunako raundi ya kumi na kuondoka mshindi kwa Knock Out. Watanzania wakawa wameanza kumtazama Deus kwa matumaini zaidi. Wakati huo malumbano baina ya kambi yake na ile ya yule bingwa wa dunia aliyempiga kwa Knock Out yakawa yameshamiri. Yule bingwa akidai kurudiwa pambano, wakati Deus na promota wake wakisisitiza kuwa hakukuwa na bondia yoyote wa kushindana naye hapa nchini, akiwemo huyo aliyekuwa "akisemekana" kuwa ni bingwa wa dunia.
Hali hii ilizidisha ushindani baina yao na wakati huo huo mashabiki wakaongezeka. Watanzania wakawa na hamu ya kurudiwa kwa mpambano ule. Deus na promota wake wakawa wameshikilia msimamo wao, na upinzani ukazidi mara dufu.
Bondia wa pili wa kimataifa kupambanishwa na Deus alikuwa kutoka Zambia. Huyu alisulubiwa vibaya zaidi, na mnamo raundi ya nane ya mchezo refa alilazimika kusimamisha pambano baada ya Mzambia kuchanika vibaya juu ya jicho na kuvuja damu nyingi. Pambano liliisha na Deusdelity Macha aliibuka mshindi kwa Technical Knock Out (TKO).
Na ndipo hapo alipopachikwa jina la "Deus-deadly", yaani Deus wa mauaji.


Katika pambano hilo na Mzambia, bingwa wa dunia wa wakati ule katika uzito ule wa Super Middle alikuwamo ukumbini akishuhudia pambano, na baada ya kumsambaratisha mzambia, Deus alisogelea upande ambao mpinzani wake mkubwa alikuwa ameketi na kumnyooshea ngumi huku akimpigia kelele, "Sasa nautaka huo mkanda wako!"
Ukumbi ulilipuka kwa hoi hoi na vifijo vya ushabiki, wakati yule bingwa, akiwa ameghadhibishwa na kauli ya Deus, alipoparamia jukwaa na kutaka kuweka naye mpambano pale pale. Ilikuwa hekaheka si kidogo!
Lakini Hatimaye hali ilidhibitiwa na hakuna lolote lililotokea, zaidi ya uhasama baina yao kuongezeka. (Roman alikunja uso alipokuwa akisoma sehemu hii, dhahiri kuwa hakupendezewa na tabia ile).
Bondia Deus alipambanishwa na bondia mwingine wa kimataifa, safari hii alikuwa ni mzungu kutoka Hungary. Huyu alikuwa na historia ya kuua mtu ulingoni, na watanzania waliofurika ukumbini kushuhudia pambano hilo walikuwa wamekuja kumshuhudia Deus akiaga dunia ulingoni. Mpaka kufikia raundi ya kumi na mbili mabondia wote wawili walikuwa hoi ulingoni, lakini hakuna aliyekubali kwenda chini. Pambano lilitangazwa kuwa suluhu.
Alipoongea na waandishi wa habari baada ya pambano, mzungu alimsifia sana Deus, akisema kuwa hajawahi kupambana na bondia mwenye uwezo mkubwa na mwenye ngumi nzito kama yule tangu aanze ndondi, na kwa upande wake alishukuru sana kwa pambano lao kuisha suluhu, kwani kama kungetokea mshindi katika pambano lile, yeye alijipa nafasi ndogo sana.
Hii ilizidi kumpa chati Deus, ambaye kwa upande wake aliongea na waandishi wa habari na kusema kuwa hakuwa ameridhika na matokeo yale, lakini alikiri kuwa kwa mara ya kwanza tangu aingie kwenye ngumi za kulipwa alikuwa amepata mpinzani wa kweli. Alibainisha kuwa alikuwa tayari kurudiana naye baadaye na aliahidi kuwa pindi yule mzungu atakapofanya kosa la kukubali kurudiana naye tu, basi huo ndio utakuwa mwisho wake.
Huyo ndiye bondia Deusdelity Macha.


Roman alishusha pumzi ndefu na kufikicha macho. Aliinuka kutoka kwenye kiti alichokuwa amekalia na kutembea mle ndani huku akijinyoosha na akiendelea kufikicha macho. Uso wake ulionekana kuwa na mawazo mengi. Alitoka nje na kwenda kuketi pale kwenye baa akitafakari yale mambo aliyoyasoma kuhusu bondia Deusdelity Macha. Muda huo Mark Tonto aliingia eneo lile akiongozana na mmoja wa mabondia wake wakiwa wamebeba godoro dogo, na begi dogo lililokuwa na vifaa muhimu kama shuka, taulo, chandarua, dawa ya meno na vitu kama hivyo. Kwa muda wa zaidi ya nusu saa iliyofuata, akili ya Roman alihamia katika kujishughulisha kusaidiana na Mark na yule kijana kuweka mazingira ya malazi yake pale ofisini kuwa mazuri.
Baada ya hapo muda wa chakula cha mchana ulikuwa umewadia na Mark alimkaribisha Roman nyumbani kwake kwa ajili ya mlo wa mchana. Roman alianza kusita, lakini kwa hili Mark hakuwa na majadiliano zaidi.


"Nazungumzia mlo wako wa kwanza wa maana baada ya miaka miwili ya kubugia maharage ya kuchemsha na ugali usioiva Roman! Sio mchezo bwana! Huko kuna pilau la kuku na juisi za kila fani....mke wangu amepika maalum kwa ajili yako! Lazima uje ule Roman, na lazima uje ule sasa hivi!" Mark Tonto alimwambia kwa msisitizo, na pamoja na kusita kwake, Roman aliuhisi mdomo ukimjaa mate. Akilini mwake alivuta picha iliyokuwa ikizungumzwa na Mark na akajihisi matumbo yakiunguruma kwa hamu ya kuingiza vile vyakula vilivyokuwa vikitajwa na Mark.
"Mmmnh! Kwa hapo naona umefanikiwa kunishawishi Mark. Twen'zetu...Fasta!" Alimwambia. Mark alicheka kwa furaha na kumuongoza Roman kuelekea nyumbani kwake ambapo hapakuwa mbali na pale. Huko Roman alipigwa na butwaa baada ya kuona maandalizi yaliyofanywa kwa ajili yake. Walipoingia tu ndani ya sebule ya nyumba ile, alikuta maandishi makubwa yaliyowekwa kwa marembo mazuri kama yale yanayowekwa kwenye sherehe za siku za kuzaliwa au katika sikukuu mbalimbali.
KARIBU NYUMBANI ROMAN.
Ni maneno yaliyokuwa yamebandikwa ukutani kwa nakshi maalum, huku yakiwa yamezungushiwa maua mbalimbali na maputo. Mke wa Mark Tonto alimkimbilia na kumkumbatia kwa nguvu huku akimkaribisha pale nyumbani kwao.
"Oooh Roman shemeji yangu! Pole sana baba'angu! Karibu tena uraiani...karibu nyumbani!" Alisema kwa hisia kubwa huku akibubujikwa na machozi yule mama mwenye moyo mkunjufu kama wa mumewe. Hii ilikuwa ni hali ambayo Roman hakuitarajia kabisa. Alimkumbatia yule mwanamke kwa shukurani ya hali ya juu na machozi yalimbubujika kwa furaha lakini pia kutokana na uchungu aliouhisi moyoni mwake kwa mapokezi yale.
"Oooh, Ahsante sana shemeji...." Alijibu huku akibubujikwa na machozi, akilini mwake akijua kuwa kama si Mark na mkewe kumfanyia mambo haya, hakuna mtu yeyote ambaye angejali wala kukumbuka kumfanyia mambo kama yale. Kwani sasa baada ya kutoka gerezani, Roman hakuwa na ndugu wala jamaa yoyote wa damu hapa duniani...zaidi ya urafiki na ukaribu wake na Mark Tonto. Kwa hiyo mambo yale aliyoyakuta pale nyumbani kwa sahibu yake Makongoro "Mark Tonto" Tondolo yalimfariji kupita kiasi.


***ROMA analizwa na mapokezi murua aliyoyapata nyumbani kwa Mark Tondo.......


***Bondia Deus Macha ni nani??? Na mbona anasumbua kichwa cha Roman???


BPM Sangomwile Mamamercy jonnie_vincy Khantwe mbalu byb sac mlyn VAN HEIST nrango mangimeza muuza ubuyu Jullie ZIgunga Mojaculbby mugaru
 
KARIBU NYUMBANI ROMAN.


RIWAYA: BONDIA
MTUNZI: HUSSEIN ISSA TUWA




SEHEMU YA SITA


Ni maneno yaliyokuwa yamebandikwa ukutani kwa nakshi maalum, huku yakiwa yamezungushiwa maua mbalimbali na maputo. Mke wa Mark Tonto alimkimbilia na kumkumbatia kwa nguvu huku akimkaribisha pale nyumbani kwao.
"Oooh Roman shemeji yangu! Pole sana baba'angu! Karibu tena uraiani...karibu nyumbani!" Alisema kwa hisia kubwa huku akibubujikwa na machozi yule mama mwenye moyo mkunjufu kama wa mumewe. Hii ilikuwa ni hali ambayo Roman hakuitarajia kabisa. Alimkumbatia yule mwanamke kwa shukurani ya hali ya juu na machozi yalimbubujika kwa furaha lakini pia kutokana na uchungu aliouhisi moyoni mwake kwa mapokezi yale.
"Oooh, Ahsante sana shemeji...." Alijibu huku akibubujikwa na machozi, akilini mwake akijua kuwa kama si Mark na mkewe kumfanyia mambo haya, hakuna mtu yeyote ambaye angejali wala kukumbuka kumfanyia mambo kama yale. Kwani sasa baada ya kutoka gerezani, Roman hakuwa na ndugu wala jamaa yoyote wa damu hapa duniani...zaidi ya urafiki na ukaribu wake na Mark Tonto. Kwa hiyo mambo yale aliyoyakuta pale nyumbani kwa sahibu yake Makongoro "Mark Tonto" Tondolo yalimfariji kupita kiasi.


Mark Tonto hakuwa amezidisha chumvi alipoongelea juu ya maandalizi yaliyofanywa na mkewe juu ya ujio wa Roman. Pilau ya kuku ilikuwa imetulia na kupendeza kabisa mezani pamoja na aina zipatazo tatu za juisi, na Roman aliushambulia ule msosi kwa nguvu sana. Alikumbuka vyakula duni alivyokuwa akila wakati akiwa gerezani na akashindwa kuelewa aliwezaje kula vyakula vile kwa miaka miwili mfululizo bila kuathirika kiafya.
Baada ya kupata chakula kile kizuri, Roman alimshukuru mke wa Mark na wote wakaketi sebuleni na kuongelea mambo mbalimbali hususan kuhusiana na maisha ya Roman alipokuwa gerezani.
"Nina masikitiko sana shemeji kuwa hukutaka kuja kuishi nasi hapa nyumbani...kwani najua kuwa sasa huna mahala pa kulala..." Mke wa Mark alimwambia Roman kwa ile lafudhi yake ya ki-Tanga ambayo Roman hupenda sana kumtania kwayo. Roman alimtupia jicho la haraka Mark, kisha akajibalaguza kidogo kwa shemeji yake kabla ya kumjibu.


"Aaah...hapana shemeji. Sio kuwa sikutaka kuishi nanyi hapa nyumbani, ila tu kwa sasa ningependelea niwe peke yangu kwa muda. Unajua mambo yaliyotokea kabla ya kupelekwa kwangu gerezani, na..."


"Aaah. Roman mimi sio mtoto bwana! Muda wa kuwa peke yako ulikua nao wa kutosha sana wakati uko gerezani. Sasa unahitaji kuwa karibu na watu wanaokujali na kukupenda bwana! Unahitaji kuwa na sisi! Na ndivyo nilivyomueleza Mark vilevile, lakini inaonekana tayari nyie mmeshakubaliana nami siwezi kubadili lolote katika hilo." Tandi, mke wa Mark Tonto, alimjibu Roman kwa hamasa, huku akimtupia jicho la shutuma mumewe. Mark na Roman walitazamana, kisha wote wakatazama pembeni huku Mark akibwabwaja utetezi wao.


"Ooh Come On, Tandi! Hebu muache Roman afanye anavyojisikia bwana! Ye' anajua kuwa hapa kwetu ni kwake na yuko huru kuja wakati wowote. Lakini sasa anahitaji kuwa peke yake kwa muda...and so be it (basi na iwe hivyo)!" Mark Tonto alidakia na kumkatisha mkewe.
"Eeeh, kwani ugomvi babu? Mtu n'na hamu na shemeji yangu, na n'najua kuwa siwezi kumpata hapa nyumbani kwangu kama ambavyo ningependa, sasa basi hata mawazo yangu nisiyaweke wazi?" Tandi alimjibu mumewe, na hapo Roman aliamua kuingilia kati.


"Hey, shem...hamna muvi nzuri humu jamani? Sijaangalia muvi kwa miaka miwili! Si unajua jinsi nilivyokuwa mpenzi wa muvi?" Alimwambia Tandi huku akimtupia Mark jicho la pembeni. Wazo hilo lilielekea kumpendeza Mark vilevile, lakini lilimpendeza Tandi zaidi. Baada ya kuchagua mikanda na CD za video kadhaa, hatimaye waliishia kutazama kitu ambacho Roman alikuwa akitaka kukitazama kwa muda mrefu. CD za ndondi, ambazo Mark alikuwa nazo kwa wingi mle ndani mwake.


"Nataka kuona tena jinsi Mike Tyson alivyopigwa!" Roman aliwaambia.
Kwa muda wote uliobakia katika siku ile walibaki wakitazama video za ndondi huku Tandi akimdekeza Roman kwa vinywaji mbalimbali na mapochopocho ya kila aina. Ilikuwa ni siku ya furaha sana, lakini pamoja na yote hayo,Roman alikuwa akingalia ile mikanda kwa umakini wa hali ya juu, na mara kadhaa alikuwa akijadili na Mark ni namna gani bondia mmoja angeweza kumkwepa mwingine, au ni wapi bondia mmoja alipotea stepu kiasi cha kumpa mpinzani wake nafasi ya kumshinda. Na wakati akiangalia ile mikanda, msisimko wa ajabu ulimuingia na akajihisi kama aliyezaliwa upya.


"Shemeji una mpango wa kuingia kwenye ndondi nini?" Tandi alimuuliza kwa utani, na Roman alicheka sana, lakini hakutoa jibu lolote.
Ilikuwa ni saa moja ya usiku wakati Roman aliporudi kwenye makazi yake mapya pale kwenye klabu ya ndondi ya Mark.
"Unaona ilivyokuwa hatari mimi kuja-kuja kwako Mark? Tayari Tandi alishaanza kuuliza maswali ya kipolisi! It's very dangerous, Mark! Very dangerous I tell you!(Ni hatari sana nakwambia!)" Roman alimwambia Mark wakati wakisindikizana kurudi kule kwenye klabu yao ya ngumi.
"Kweli Roman. Nadhani tunahitaji kuwa makini sana tunapokuwa na shemeji yako..."
"Nadhani njia ya salama zaidi ni mimi kuwa bidhaa adimu nyumbani kwako Mark." Roman alisema na wakaendelea na safari yao wakiwa kimya hadi walipoagana.


*****


Roman alipitiliza moja kwa moja hadi kwenye ule mlango wa chuma uliotokea kwenye ule ukumbi wa ngumi wa ile klabu ya ngumi ya Mark Tonto. Alikuwa akiingia kwenye mlango ule huku akiingiza mkono wake mfukoni kutoa ufunguo wa mlango wa ofisi ya Mark, wakati ghafla alipopamiana na mtu aliyekuwa akitokea kule kwenye ukumbi wa ngumi kwa mwendo wa haraka. Yule mtu alijigeuza upesi kuficha uso wake na kutaka kutoka nje, lakini Roman alimkamata na kumsukumia ndani kwa nguvu huku akiusukuma ule mlango kwa kisigino cha mguu wake.


"Heeey! We' vipi?" Sauti ya kike ilimkemea kwa ukali, na haraka sana Roman alipeleka mkono wake kando ya ule mlango na kuwasha taa za mle ukumbini, ambapo taa zaidi ya sita za mianzi ziliwaka kwa pamoja na kukawa kweupe kama mchana. Na hapo alijikuta akitazamana uso kwa uso na binti mmoja mrembo sana aliyekuwa amevaa suruali ya jeans iliyombana na kuonesha miinuko muhimu ya sehemu ya chini ya mwili wake, na juu alikuwa amevaa fulana kubwa nyeupe iliyoonesha miinuko midogo ya matiti yake.


"We' vipi kivipi? Unatafuta nini humu wewe saa hizi?" Roman alimchachamalia yule mrembo. Woga ulimtawala Kate na akabaki akimkodolea macho yule mtu ambaye asubuhi tu ya siku ile alikwenda kumvizia nje ya gereza la Ukonga, sasa akiwa naye uso kwa uso. Mate yalimkauka ghafla na akajikuta akijaribu kukohoa ili angalau apate kuongea vizuri, akilini mwake akijilaumu kwa kuruhusu yule jamaa amkute mle ndani muda ule.


"Nakuuliza wewe mwanamke! Unatafuta nini humu?" Roman alimuuliza tena huku akimsogezea uso wake kwa kumshutumu. Kate alirudi nyuma kwa woga.


"Aam...Ni...nilikukwa natafuta choo! Nimepotea tu,samahani...!" Alimjibu kwa kitetemeshi kikubwa. Roman alimtazama yule binti kwa muda, na yule binti alijaribu kumzunguka na kuuendea mlango wa kutokea nje ya ukumbi ule lakini Roman alisogea mbele yake na kumzuia huku bado akiendelea kumtazama.
"We! Unataka kujitia mbakaji sio? N'tapiga kelele sasa hivi nikujazie watu hapa!" Kate alimwambia kwa sauti ya kitetemeshi huku akimnyooshea kidole.


"Hebu acha ujinga weweee! Sasa kama hutaki kubakwa humu ndani umefuata nini,eenh?" Roman alizidi kumchachamalia. Kate alimtazama kwa woga. Moyoni akilaani kiherehere chake cha kutaka kujitia kuja huku peke yake muda ule.


"Nimekwambia kuwa nilikuwa nataka kwenda chooni nikapotea njia! Mi' mgeni katika baa hii..."
"Kwa hiyo na kusoma pia hujui?" Roman alimuuliza.
Kate alimtazama kwa mshangao na kumuuliza alikuwa anamaanisha nini kwa swali lile.


"Yaani unataka kuniambia kuwa hujaona kuwa hapo nje ya huu mlango kumeandikwa "Kawe Boxing Club"? Au ndio hujui kusoma?"
Kate hakuwa na ujanja. Alimtazama na kuinamisha kichwa chake chini, kisha akamtazma tena.


"Okay...Nilikuwa nakutafuta wewe Roman." Alimjibu huku akimtazama usoni, na Roman alibaki mdomo wazi kwa mshangao. Yaani ulikuwa ni mshangao wa mwaka kwake, na alibaki akimkodolea macho yule binti mzuri kama kwamba alikuwa ameona jini.
"U...nini? We' umenijuaje mimi?" Aliropoka kwa jazba huku akiukamata mkono wa yule binti kwa nguvu kama kwamba alijua kuwa muda wowote yule msichana angeanza kutimua mbio. Kate alitoa mguno wa maumivu na kujaribu kuuchomoa mkono wake bila mafanikio.
"Aaah! Sasa...unaniumiza wewe!!" Kate alilalamika kwa uchungu.








****KATE anatafuta nini kwa ROMAN………sasa Roman amemfuma…nini kitajiri…

ram
BPM Sangomwile Mamamercy jonnie_vincy Khantwe mbalu byb sac mlyn VAN HEIST nrango mangimeza muuza ubuyu Jullie ZIgunga Mojaculbby mugaru
 
Last edited by a moderator:
Hahaha eti kama hutaki kubakwa huku ndani umefuata nini?? Na mimi nasema abakwe tu maana hakuna namna nyingine
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…