RIWAYA: Mifupa 206

KIKAO KILICHOFANYIKA MAPEMA SANA alfajiri juu ya jengo moja
la ghorofa lililokuwa kando ya jiji la Dar es Salaam kikiwashirikisha watu
wachache waliopigiwa simu usiku wa manane kilikuwa kimehitimika kwa
kufanyika maazimio kadhaa makubwa na muhimu katika namna ya kukabiliana na
mauaji ya maafisa wa vitengo nyeti vya usalama yaliyokuwa yakiendelea kutokea jijini
Dar es Salaam.
“Hatuwezi kusema nchi yetu ni kisiwa cha amani wakati mauaji ya viongozi
wa vitengo nyeti vya usalama vya nchi hii yanaendelea kutokea“ M.D.Kunzugala
mwanaume mrefu na mweusi mwenye mwili imara uliyojengeka vizuri kwa shibe isiyo
ya wasiwasi na mazoezi ya kutosha akaongea kwa hasira huku akiyatembeza macho
yake taratibu kuzitazama kwa makini sura za wajumbe waliofika kwenye mkutano ule.
Tangu pale alipogiwa simu kujulishwa juu ya taarifa za kifo cha Pierre Kwizera
usiku wa manane M.D.Kunzugala alikuwa hajatulia hata kidogo. Usingizi alioanza
kuutongoa kitandani ukawa umeyeyuka na baada ya hapo akawa akipokea na kupiga
simu kwa viongozi mbalimbali wakiwemo wakuu wa nchi. Maswali yalipokuwa mengi
M.D.Kunzugala akatoka nje ya nyumba na kuwasha gari lake akielekea eneo la tukio.
Kwa mara ya kwanza akajikuta akianza kuichukia kazi yake na kuzitamani kazi
nyingine tofauti zisizokuwa na majukumu kama yake. Kwa muda wa miaka sita tangu
alipoteuliwa kushika kitengo hiki alikuwa hajakutana na misukosuko na changamoto
ambazo kwa sasa alianza kuzihisi kuwa zilikuwa mbioni kukitilia mchanga kitumbua
chake.
“Mauaji yameanza kwa Guzbert Kojo yakahamia kwa P.J.Toddo na sasa ni kwa
Pierre Kwizera. Hivi bado mnataka niamini kuwa mauaji haya yanatekelezwa na
wahalifu wa kawaida kama panya road?. Hilo mimi siliamini na sitaki katu kuliamini.
Binafsi nahisi kuna kitu fulani kinachoendelea na kilichojificha nyuma ya mauaji
haya. Hata hivyo sitaki tuamini sana katika hisia zangu ndiyo maana nikawaita hapa
ili tujadiliane nini cha kufanya kuikomesha hali hii” M.D.Kunzugala akaweka kituo
akikohoa kidogo kusafisha koo lake huku akionekana kufikiria jambo. Wakati akifanya
vile macho yake yakawa yakiendelea kufanya ziara kuzitazama sura za wajumbe
waliohudhuria mkutano ule mfupi wa dharura.
“Mimi naungana na wewe mkuu kwani tangu mauaji haya yameanza kutokea
mimi nimekuwa karibu sana na vyombo vya habari katika kutaka kujua vyombo vya
habari vinaongeleaje matukio haya.
Nataka nikwambie kuwa mtazamo uliopo kwa jamii kubwa ni kuwa serikali hii
ni dhaifu na imeshindwa kusimamia vizuri suala la usalama wa watu wake. Hivyo
nionavyo mimi ili kupambana na matukio haya ni lazima kufanyike mabadiliko
makubwa ya mfumo wa utendaji katika idara husika” Ghalib Chakwe,mwanaume
mfupi mnene mwenye macho makali na pia mkuu wa kurugenzi ya usalama ikulu
alimaliza kuongea huku akijiegemeza vizuri kwenye kiti na hivyo kuufanya mgongo
wake ustarehe lakini macho yake yakitulia kutazama juu ya meza kama anayefikiri
jambo.
“Yeyote anayefanya hivi ana malengo ya kuitia dosari serikali,kufanya hujuma
kama siyo njama za kudhoofisha utendaji wa serikali na hatimaye kuipindua. Mifano ya
namna hiyo tumeiona Bamako nchini Mali wakati Kepteni Amadou Sanogo alipoipindua
serikali ya rais Amadou Touman Touré tarehe 22 mwezi Machi mwaka 2012. Hujuma
za namna hiyo pia zimefanyika mjini Bangui kwenye nchi ya jamhuri ya Afrika ya
kati wakati waasi walipoipindua serikali ya rais Francois Bozize tarehe 24 mwezi Machi
mwaka 2013. Hivyo suala hili ni lazima lipewe uzito wa aina yake mkuu” Tiblus
Lapogo,mwanaume mrefu na mwanausalama mahiri kutoka kitengo maalum cha
upelelezi cha ofisi ya mashtaka ya DPP akaongea kwa msisitizo huku hoja yake ikielea
hewani.
“Mimi nafikiri hili suala ni muhimu tukavishirikisha na vyombo vingine vya
usalama likiwemo jeshi la polisi. Upelelezi wa kina ufanyike wahusika wakamatwe
na kuhojiwa ili tujue mauaji haya yanafanywa na nani na kwa sababu gani” Siraju
Chenga,afisa usalama na mwanakamati ya kudumu ya ulinzi na usalama wa jiji la Dar
es salaam alimaliza kuongea huku akiwatazama wenzake.
“Mimi naona tutoe matangazo kwenye vyombo vya habari kuwatahadharisha
wananchi juu ya matukio haya” Manyama Sululu akatumbukiza hoja yake baada ya
kuhisi kuwa huwenda wazo lake pia lingekuwa na msaada.
“Nionavyo mimi tusitoe matangazo hayo mapema kwani tutasababisha hofu
kwa wananchi na vilevile tutaonekana tumeshindwa kazi. Matangazo pia yatawafanya
wanaofanya mauaji haya wapate nafasi nzuri ya kujificha huko waliko. Katika mazingira
kama haya biashara ya kimyakimya ndiyo inayolipa. Tuvishirikisheni vyombo vyetu
vya usalama ambavyo vina weledi wa hali ya juu na uzoefu wa kutosha” Luteni Kanali
Davis Mwamba mkuu wa kamati ya dharura ya usalama wa nchi na itifaki za jeshi la
wananchi akapendekeza huku akiyatembeza macho yake kuzitazama sura za wajumbe
waliokuwa mle ndani.
“Mimi naona kabla ya kwenda mbele zaidi upelelezi ungefanyika kwanza katika
kuzifahamu nyendo za maafisa wote waliouwawa. Kuanzia hapo huwenda tukapata
sababu za vifo vyao na hiyo itatusaidia kwa hatua inayofuata” James Risasi akaongea
kwa utulivu huku akiupima uzito wa hoja yake.
Baada ya pale kikafuatiwa na wachangiaji wengine kutoka idara tofauti za usalama
wa taifa huku M.D.Kunzugala mkurugenzi mkuu wa usalama wa taifa akiwa ndiye
msemaji mkuu wa mkutano ule.
Hatimaye mkutano ule ukafika tamati huku maazimio yakiwa ni kuongeza ufanisi
katika utendaji na kumvua madaraka Abdulkadir Badru. Mkuu wa intelijensia ya
usalama wa taifa kwa kile kinachosemekana kuwa eti ofisi yake ilikuwa imeshindwa
kutoa taarifa za kueleweka juu ya matukio ya mauaji ya wanausalama yaliyokuwa
yakiendelea jijini Dar es Salaam.
Nafasi ya Abdulkadir Badru akawa amepewa Sulle Kiganja. Mtu mkorofi na mtata
katika kushughulika na wahalifu. Ile nafasi ya marehemu P.J.Toddo akawa amepewa
ndugu Miraji Kasena na zile nafasi zilizoachwa wazi za Guzbert Kojo na Pierre
Kwizera zikaazimiwa kuwa zingetolewa hoja na rais na ndiye ambaye angeamua nani
wa kumteua kwani tofauti na hapo ilikuwa ni sawa na kuingilia madaraka ya rais.
Hatimaye mkutano ule ukafika tamati na wajumbe wakaagana na kuondoka huku kila
mmoja akiwa amechiwa majukumu yake ya kufanya.
Kitendo cha Abdulkadir Badru ama Badru kama wengi walivyozoea kumuita
kuvuliwa madaraka pasipo kupewa ofisi nyingine kilikuwa kimemuacha njia panda
huku akijihisi kuwa ni kama waziri asiyekuwa na wizara maalum.
Mara baada ya wajumbe wale kuondoka Badru akabaki mle ukumbini huku
aliendelea kuwaza namna maisha yatakavyomwia vugumu baada ya kuvuliwa wadhifa
wake. Ikulu alikuwa akiingia na kutoka kama nyumbani kwake mara kwa mara kuonana
na viongozi wakubwa wa serikali. Safari zake nje ya nchi zilikuwa zikigharimiwa na
serikali huku akiendeshwa kwenye gari la kifahari na kupewa ulinzi wa kutosha.
Badru akaendelea kukumbuka hoteli za kifahari alizokuwa akifikia mara apatapo
safari za kikazi nje ya nchi huku akisindikizwa na posho za kila namna. Mawazo ya
kupoteza vitu hivyo vyote kwa wakati mmoja yakampelekea ajihisi mnyonge sana.
Siyo kweli kwamba Badru alikuwa hajafanya kitu chochote tangu mauaji ya
Guzbert Kojo yalipotokea. La hasha! hali haikuwa hivyo kwani tangu mauaji yale
yalipotokea Badru alikuwa hajalala usiku na mchana akiipanga vizuri safu yake
ya kiutendaji katika kuhakikisha kuwa muuaji anakamatwa. Safu yake ikiundwa na
Fulgency Kassy,Pweza,Kombe na watu wengine kutoka katika idara tofauti.
Hata hivyo kwa upande mwingine Badru alikuwa akiufahamu ukweli wa mambo
ingawa alikuwa ameshindwa kuushughulikia kikamilifu kutokana na hofu ya kugusa
maslahi ya wakubwa.
“Potelea mbali watajua wenyewe!” hatimaye Badru akajiambia huku akisogeza kiti
chake nyuma na kusimama baada ya wajumbe wote kutoka mle ukumbini. Mawazo
ya hisia za unyonge yakiendelea kumkabili Badru akapiga hatua zake hafifu akielekea
kwenye dirisha moja kubwa la kioo la mle ukumbini ili kujifariji na mandhari ya nje
ya lile jengo la ghorofa. Mara wakati Badru akilikaribia lile dirisha akasikia mkono
ukimshika begani na alipogeuka nyuma akajikuta akitazamana na Sulle Kiganja,mtu
aliyekabidhiwa kitengo chake.
“Pole sana Badru ila tambua kuwa cheo ni dhamana” Sulle Kiganja akaongea huku
akilazimisha tabasamu ingawa ile haikuwa hulka yake. Kwa muda mrefu Abdulkadir
Badru na Sulle Kiganja walikuwa kama Paka na Panya huku wakitiliana fitina za hapa
na pale kila nafasi ya kufanya hivyo ilipokuwa ikipatikana.
“Nishapoa!” Badru akaongea kinyonge huku akigeuka na kutazama dirishani.
“Hupaswi kumlaumu M.D.Kunzugala kwani hata yeye amepewa shinikizo kutoka
juu” Sulle Kiganja akaendelea kuongea huku akitabasamu.
“Simlaumu mtu yoyote kwani nadhani mchango wa kazi yangu haujaonekana
hivyo ofisi ipo huru kufanya vile inavyoona kuwa ni sawa” Badru akaongea bila
kumtazama Sulle Kiganja huku mikono yake akiwa ameiegemeza dirishani na macho
yake yakitazama nje kupitia kwenye kile kioo.
“M.D.Kunzugala anasema eti inawezekana kuwa mauaji haya yapo nyuma ya
mpango fulani hatari. Vipi wewe ulimuelewa wakati alivyosema vile?” Sulle Kiganja
akauliza baada ya kusimama pembeni ya Badru huku akitazama nje kupitia kile kioo
cha dirishani.
“Mimi sitafahamu kitu chochote ndiyo maana nimeondolewa kitengoni. Kwanini
hukumuuliza mwenyewe wakati alipoongea?” Badru akajibu kwa hasira huku
akimuona Sulle Kiganja kama aliyekuwa akichokonoa vitu ambavyo havikuwa na
maana tena kwake.
“Hapaswi kukasirika Badru kwani bado mchango wako unahitajika. Haya yote
yanafanyika ili kuimarisha usalama wa nchi. Hata rais hulazimika kubadili baraza lake
la mawaziri kila anapohisi kuwa ipo haja ya kufanya hivyo” Sulle Kiganja akaongea
huku akiendelea kutabasamu
“Naomba uniache kwanza kwani nahitaji faragha!” Badru akaongea kwa utulivu.
“Utakuwa na muda mrefu wa faragha baada ya kunikabidhi ofisi”
“Nitakukabidhi ofisi kesho asubuhi!”
“Kwanini isiwe leo Badru?. Huoni kuwa muuaji anaendelea kutabaruku?”
Maelezo ya Sulle Kiganja yakampelekea Badru ageuke kumtazama huku donge la
hasira limemkaba kooni.
“Tafadhali! naomba uniache nahitaji faragha” Badru akaongea kwa hasira.
“Okay! na vipi kuhusu wale vijana wako?” Sulle Kiganja akauliza kwa tahadhari
“Vijana gani?” Badru akauliza huku akigeuka na kumkata jicho la hasira Sulle
Kiganja pembeni yake.
“Fugnecy Kassy,Pweza na Kombe!”
“Wamefanya nini?”
“Kesho utakaponikabidhi ofisi utawaambia waripoti kwangu kwani nahitaji
kufahamu wamefikia wapi kabla sijaanza kazi yangu” Sulle Kiganja akaongea huku
akitabasamu hata hivyo Badru hakumjibu kitu badala yake akageuka na kutazama nje
ya lile jengo kupitia kwenye kile kioo cha dirishani huku mawazo yake yakiwa mbali
na eneo lile.
 
Japo sifaham hilo jina mm namfahamu kama Kevin mponda BUT I think mbali na kipaji alichonacho cha kusimulia na kutunga atakua kapitia Mafunzo ya votu hivi au anatumikia jeshi..!
Nahisi huyu mtunzi ni CDO ( commando) Octavian Gowele wa 92 kj ngerengere
 
SAA YA GARI LANGU KWENYE DASHIBODI ilionesha kuwa ilikwisha
timia saa tatu na robo asubuhi wakati nilipoegesha gari langu kando ya kituo cha
kujazia mafuta eneo la Mwenge jijini Dar es Salaam. Asubuhi hii mvua ilikuwa
imeacha kunyesha na anga lote la jiji la Dar es Salaam lilikuwa tulivu.
Fikra zangu bado zilikuwa zimetawaliwa na lile tukio la jana la kule Tabata relini.
Kifo cha Momba kilikuwa kimeniweka katika wakati mgumu sana na sikutaka
kujilaumu kuwa mimi ndiye niliyesababisha kifo kile kwani nilikuwa na hakika kuwa
kifo chake kilikuwa kimetokana na kitendo cha kutumika kwa gari lake na yule
mdunguaji hatari.Hivyo hisia zangu zikanieleza kuwa watu wale waliomuua Momba
huwenda walimpata kwa urahisi baada ya kupeleleza gari lake katika vijiwe vya teksi
vya jijini Dar es Salaam.
Nikiwa naendelea kufikiri mara hoja nyingine ikachipuka taratibu kichwani
mwangu pale nilipowaza kuwa kitendo cha mdunguaji kutafutwa na wale watu kwa
maana nyingine ni kuwa watu wale hawakuwa na unasaba wowote na yule mdunguaji.
Hivyo baada ya mimi mdunguaji alikuwa ni adui namba mbili. Swali likabaki kuwa
yule mdunguaji alikuwa nani na kwanini alimdungua yule mwanaume nje ya Vampire
Casino usiku ule?. Majibu sikuyapata hivyo asubuhi hii nilikuwa nimeamua kurudi tena
kwenye kituo kile cha teksi ambacho Momba alikuwa akiegesha teksi yake ili nidadisi
kama ningeweza kupata chochote cha kunisaidia katika upelelezi wangu.
Nilisubiri magari yasimame kwenye foleni kisha nikatumia mwanya ule kuvuka
barabara nikikatisha kwenye uwazi mdogo uliofanywa baina ya gari moja na lingine.
Muda mfupi baadaye nikawa nimetokezea upande wa pili wa ile barabara.
Kituo cha teksi cha eneo la Mwenge hakikuwa mbali na pale hivyo nikakatisha
katikati ya vibanda vya wamachinga na ndani ya muda mfupi nikawa nimefika kwenye
kituo kile.
Wakati nikifika nikaanza kuyatembeza macho yangu nikiwatazama madereva
wa teski waliokuwa eneo lile huku moyoni nikiomba nimkute tena yule mzee wa
kingoni niliyeonana naye siku ya jana. Hata hivyo madereva wale hawakuonesha
kunichangamkia kama ilivyokuwa siku ya jana na sikutaka kukata tamaa.
Kijana mmoja dereva wa teksi mwenye umri unaolekeana na wangu alinikaribisha
kwa bashasha zote akidhani kuwa nilikuwa mteja na nilipomchunguza haraka
nikatambua kuwa hakuwepo jana wakati nilipofika.
“Karibu bosi wangu usafiri wa kuaminika huu hapa” kijana yule akanikaribisha
huku akitaka kufungua mlango wa teksi yake lakini nikamuwahi kwa kumshika begani
huku nikimpa ishara kuwa nilikuwa sihitaji huduma ya usafiri. Yule kijana kuona vile
akasimama na kunikodolea macho ya mshangao.
“Unashida gani?”
“Namuulizia dereva mmoja wa teksi mzee wa kingoni” nilimwambia yule kijana
na hapo akageuka na kunitazama kwa udadisi kisha akaniuliza kwa sauti tulivu ya
kukata tamaa.
“Mzee Ngonyani?”
“Ndiyo!” nilimjibu huku nikijiuliza kama mzee yule niliyeonana naye jana alikuwa
akiitwa Ngonyani au lah!
“Yuko upande ule pembeni ya fundi viatu” yule kijana akanielekeza upande
mwingine wa kile kituo cha teksi.
“Ahsante!” nikamshukuru yule kijana kisha nikaanza kukatisha katikati ya teksi
zilizokuwa eneo lile nikielekea kule nilipoelekezwa.
Mzee Ngonyani alikuwa amefungua mlango wa mbele wa teksi huku akiwa
amelala kwenye kiti cha dereva kifua wazi baada ya kufungua vifungo vya shati lake.
Mguu wake mmoja ulikuwa chini huku ule mwingine akiwa ameutundika mlangoni.
Bila shaka hakutarajia kuniona pale kwani niliubaini haraka mshtuko wake wakati
alipogeuka kunitazama. Hakunichangamkia kama jana na badala yake taratibu
akauondoa mguu wake pale juu ya mlango kisha akakaa vizuri akinitazama pasipo
kusema neno huku uso wake ukionekana kulemewa na lindi la mawazo.
“Shikamoo mzee!”
“Marahaba” yule mzee akanijibu kwa mkato huku akinitazama kwa utulivu.
“Unanikumbuka?” nikamuuliza yule mzee na huwenda swali langu lilimtatiza
kidogo kwani alikawia kunijibu huku akinitazama.
“Nakukumbuka vizuri. Wewe si yule kijana aliyefika hapa siku ya jana kumuulizia
Momba?”
“Ndiyo mimi” nikamwambia yule mzee na hapo akageuka na kunitazama kwa
utulivu bila kusema neno lolote.
“Nimekuja kukupa taarifa mbaya” nikavunja ukimya
“Nafahamu!” yule mzee akaniambia kwa mkato.
“Unafahamu kuwa Momba ameuwawa!”
“Ndiyo”
“Nani aliyekwambia?” nikamuuliza yule mzee kwa udadisi huku nikimtazama
usoni.
“Kila mtu anafahamu hivyo na habari za kifo chake zipo magazetini” mzee yule
akaniambia kwa huzuni na hapo nikakumbuka kuwa nilikuwa sijapitia vichwa vya
magazeti asubuhi ya leo.
“Hicho ndiyo kilichonileta hapa. Nilitaka nikupashe habari kwani hata mimi
nimeshtushwa sana na habari za kifo chake” niliongea kwa utulivu lakini mzee yule
hakuchangia mada na badala yake aliendelea kunitazama.
“Taarifa zinasema kifo chake kimetokana na nini?” nilimuuliza yule mzee kwa
utulivu.
“Amenyongwa na mwili wake umeokotwa nyuma ya jengo la BML eneo la Tabata
relini”
“Kuna mtu yeyote anayetuhumiwa kuhusika na kifo chake?”
“Hapana! hakuna mtu yeyote aliyekamatwa na polisi bado wanaendelea
na uchunguzi” yule mzee akanijibu huku akipunguza sauti ya redio ya gari na
nilipomtazama nikatambua kuwa bado alikuwa kwenye simanzi kubwa ya kifo cha
Momba. Kitambo kifupi cha ukimya kikapita huku nikifikiria juu ya hali ile kisha
nikavunja ukimya.
“Nani aliyekueleza kuwa polisi wanaendelea na uchunguzi wa kifo chake?”
nikamuuliza yule mzee na swali langu bila shaka lilimshangaza sana kwani nilimuona
akigeuka na kunitazama vizuri usoni.
“Uhalifu wowote unapotokea ni lazima polisi wafanye uchunguzi kutaka kujua
nani aliyehusika ili sheria ichukue mkondo wake”
“Yaani ninachotaka kufahamu ni kuwa taarifa hizo za polisi kuendelea na
uchunguzi wa kifo cha Momba ni za kutoka magazetini au unauthibitisho nazo!”
nilimuuliza yule mzee huku nikitaka ufafanuzi wa maelezo yake.
“Ndiyo!” yule mzee akasisitiza.
“Unathibitishaje?” nilimuuliza yule mzee kwa upole na nilichokiona usoni mwake
ni kuwa maswali yangu yalikuwa mbioni kumchosha. Hata hivyo sikuwa na namna
ya kufanya.
“Hivi ninavyokueleza madereva wote wa teksi wa kijiwe hiki muda mfupi
uliyopita tumetoka mochwari ya hospitali ya Amana kuutambua mwili wa Momba”
yule mzee akanieleza na kabla hajamaliza kunieleza nikamuona kijana mmoja akija
pale tulipokuwa kisha akapenyeza noti ya shilingi elfu tano dirishani ambapo yule
mzee aliipokea.
“Niandike jina langu kabisa mzee Ngonyani” yule kijana akaongea huku akiondoka
na hapo nikajua kuwa alikua ameleta rambirambi na mzee Ngonyani ndiye aliyekuwa
mkusanyaji wa rambirambi kwa ajili ya msiba wa Momba kutoka kwa madereva
wenzake wa teksi wa kituo kile.
“Usijali Mashaka nakuandika sasa hivi kijana wangu” mzee Ngonyani akaongea
huku akifunua daftari lililokuwa kando yake na kuanza kuandika jina la Mashaka na
kiasi cha pesa alichotoa. Alipomaliza akaichomeka ile noti ya shilingi elfu tano katikati
ya lile daftari na kugeuka akinitazama.
“Mimi ni mwenyekiti wa madereva wa teksi wa kituo hiki hivyo nakusanya
mchango wa rambirambi kwa ajili ya marehemu Momba” mzee Ngonyani akaongea
katika namna ya kutaka nikitambue vizuri cheo chake. Nilimtazama mzee yule kwa
makini kisha nikatia hisani kwa kutumbukiza mkono wangu mfukoni na kutoa noti ya
shilingi elfu kumi ambapo nilimpa.
“Ongezea na hii” nilimwambia yule mzee na wakati akiipokea ile pesa uso wake
ukaonesha matumaini.
“Ahsante! sana kijana. Waswahili wanasema shida haina mwenyewe” mzee
Ngonyani akaongea wakati akifunua lile daftari la mchango wa rambirambi.
“Jina lako nani?” akaniuliza huku akigeuka na kunitazama
“Oh! haina haja ya kuniandika jina” nikamwambia na kwa kutaka kuondoa ubishi
nikamtumbukizia swali jingine.
“Mazishi ya Momba yatafanyikia wapi?”
“Tutamsafirisha baada ya uchunguzi wa polisi kukamilika kwenda huko kijijini
kwao Tanangozi mkoani Iringa”
“Loh! ni safari ndefu sana hiyo” niliongea huku nikifikiri kisha nikayarudisha
maongezi yetu kwenye mstari.
“Kuna askari yeyote aliyefika hapa kuwahoji?” nilimuuliza mzee Ngonyani huku
nikimtazama usoni.
“Hapana! ila kule hospitali tulipofika tulikutana na polisi watatu waliovaa kiraia
na ndiyo wao waliotueleza kuwa tusiwe na wasiwasi kwani wao walikuwa wameanza
kufanya uchunguzi juu ya kifo cha Momba”
Maelezo ya mzee Ngonyani yakaupelekea moyo wangu upige kite kwa nguvu na
hapo nikaanza kuhisi baridi nyepesi ikisafiri mgongoni mwangu. Fikra zangu zikawa
zimewakumbuka wale watu watatu walionishambulia kutoka juu ya ghorofa kule
Tabata relini.
“Wapoje hao askari?” hatimaye nikamuuliza mzee Ngonyani kwa utulivu.
Mzee Ngonyani akaanza kunipa maelezo juu ya mwonekano wa hao askari kanzu
aliyeonananao hospitali ya Amana wakati walipoenda kuutambua mwili wa Momba.
Mzee Ngonyani alipomaliza kunielezea nikawa nimepata picha kamili juu ya nini
kilichokuwa kikiendelea. Maelezo yake juu ya mwonekano wa hao askari yalikuwa
yamefanana kwa asilimia kubwa na wale watu walionishambulia kule Tabata relini
ingawa sikuwa nimewaona kwa ukaribu siku ile ambao sasa nilifahamu kuwa ndiyo
waliyomuua Momba.
“Waliwaonesha vitambulisho vyao?” nikamuuliza mzee Ngonyani
“Ndiyo!” jibu lile likanipelekea nimtazame mzee Ngonyani kwa tafakuri
“Hao polisi waliwahoji kitu chochote baada ya hapo?”
“Ndiyo”
“Waliwahoji nini?”
“Kama ni kweli tulikuwa tukimfahamu Momba,mwenendo wa maisha yake na
marafiki zake”
“Ulizungumza chochote kuhusu mimi?” nikamuuliza yule mzee na hapo
akashikwa na kigugumizi. Hata hivyo sikutaka kuendeleza mjadala ule kwani ukweli
nilishaufahamu na kwa kutaka kuyaweka sawa maongezi yetu nikaingiza mkono
mfukoni na kuchukua kitambulisho changu bandia kisha nikampa mzee Ngonyani.
Mzee Ngonyani akakipokea kile kitambulisho na kuanza kupitia maelezo yake.
“Wewe ni askari?” wakati mzee Ngonyani akiniuliza kwa mshangao mimi
nilikuwa tayari nimeshazunguka upande wa pili na kuingia ndani ya teksi. Mzee
Ngonyani akaendelea kunitazama kwa mshangao kama kipofu aliyeona mwezi. Pasipo
kumtazama mzee Ngonyani nikachukua sigara moja kutoka mfukoni na kuibana kwa
kingo za mdomo wangu kisha kwa msaada wa kiberiti changu cha gesi nikajiwashia
sigara ile na kuvuta mapafu kadhaa.
Nilipoupuliza moshi wa sigara yangu nje nikageuka na kumtazama mzee Ngonyani
pembeni yangu. Mzee Ngonyani hakuzungumza kitu chochote kwani bado alikuwa
kwenye mduwao nami nikaitumia nafasi ile kujieleza kuwa mimi ni nani. Maelezo
yangu yakianzia tangu siku ile ya jana nilipo onana naye.
“Nilikuwa kwenye harakati za kuyaokoa maisha ya Momba lakini sasa nakiri kuwa
nimechelewa” hatimaye nikahitimisha maelezo yangu.
“Ulijuaje kuwa Momba yuko hatarini?” mzee Ngonyani akaniuliza.
“Ni mkasa mrefu nadhani nitakusimulia pale utakapokuwa umekamilika”
“Kwa hiyo unataka kuniambia kuwa wale watu waliojitambulisha kwetu kuwa ni
askari polisi ndiyo waliyomuua Momba?”
“Ukirejea maelezo yangu ya awali utagundua kuwa swali lako limekwishajibiwa”
nilimwamba mzee Ngonyani huku bado akiendelea kunishangaa.
“Duh! kweli nyinyi wapelelezi ni watu wa ajabu sana” mzee Ngonyani
akazungumza na mimi sikumfuatiliza maneno yake badala yake fikra zangu zilikuwa
zimezama katika tafakari nyingine.
“Nahitaji maelezo machache kutoka kwako kabla sijaondoka kwenda kuwatafuta
wauaji wa Momba”
“Maelezo gani?” mzee Ngonyani akashtuka na kuniuliza huku akinitazama.
“Nataka kufahamu Momba alikutana na nani kabla yangu” swali langu
likampelekea mzee Ngonyani azidi kunitazama kwa mshangao kisha akayahamisha
macho yake kutazama mbele. Nilipomchunguza vizuri nikagundua kuwa alikuwa
akijaribu kukusanya kumbukumbu za matukio ya nyuma katika fikra zake.
“Ni watu wengi ambao bila shaka ni abiria wake” hatimaye mzee Ngonyani
akaongea kwa utulivu.
“Siku za mwisho kabla ya kifo chake!” nikafafanua na hapo nikamuona mzee
Ngonyani akiupisha utulivu kichwani kwa kitambo kabla ya kuvunja ukimya
“Kulikuwa na mwanamke aliyekuwa akimzungumzia kuwa angelikodi gari lake
kwa siku kadhaa” maelezo ya mzee Ngonyani yakanipelekea nigeuke vizuri na
kumtazama kwa shauku.
“Mwanamke gani?”
“Hawakuwahi kuniambia kinagaubaga kuwa huyo mwanamke ni nani nami
sikutaka kumdadisi zaidi kwani huwenda hakupenda nifahamu. Si unajua hapa mjini
kila mtu na pilika zake” mzee Ngonyani akaongea kwa utulivu huku akionekana
kufikiri.
“Maelezo yake yalisemaje?” nikauliza kwa udadisi
“Kama nilivyokueleza kuwa kulikuwa na mwanamke fulani aliyedai kuwa
angelikodi gari lake kwa siku kadhaa. Hivyo alikuwa akinitahadharisha kuwa nisiwe na
wasiwasi pale ambapo ningekuwa simuoni hapa kijiweni”
“Hakukueleza kuwa huyo mwanamke ni nani na anaishi wapi?”
“Hapana!,hakuniambia jina lake ila alinigusia tu juu ya hoteli fulani ya hapa jijini
Dar es salaam” mzee Ngonyani aliongea huku akionekana kuzidi kufikiria.
“Alisemaje kuhusu hiyo hoteli?” nilimuuliza mzee Ngonyani huku nikimtazama
kwa makini.
“Aliniambia kuwa kuna mtu fulani alimpigia simu akimtaka aende kwenye hiyo
hoteli asubuhi ile na ninavyodhani huwenda mtu huyo ndiye alikuwa huyo mwanamke
aliyetaka kukodi gari lake”
“Kwanini unadhani hivyo?”
“Momba ni rafiki yangu hivyo namfahamu vizuri pale linapokuja suala la
wanawake” nilimtazama mzee Ngonyani kwa utulivu na hapo nikagundua kuwa
kulikuwa na hikika katika maneno yake.
“Hiyo hoteli inaitwaje?” nilimuuliza mzee Ngonyani hata hivyo hakunijibu kwa
haraka badala yake akaendelea kutazama mbele ya gari kama anayefikiri jambo kisha
akavunja ukimya
“Hotel 92 Dar es Salaam ipo nyuma ya stendi ya mabasi yaendayo kasi eneo la
Ubungo kama sijakosea” mzee Ngonyani akaongea kwa utulivu huku akiendelea
kutazama mbele ya ile teksi yake.
Maelezo yale yakanipeleka nimtazame mzee Ngonyani kwa utulivu moyoni
nikimsifu kwa kuweka kumbukumbu zile vyema kichwani mwake.
“Hotel 92 Dar es Salaam…” mara nikajikuta nikiongea kwa utulivu jina lile la hoteli
huku nikijaribu kuvuta picha kichwani mwangu.
“Baada ya hapo nini kilifuatia?”
“Hakuna kwani asubuhi ile ndiyo ilikuwa mara yangu ya mwisho kuonana na
Momba” mzee Ngonyani akaongea huku akitikisa kichwa chake kwa masikitiko.
Hatimaye nikavuta sigara yangu kwa utulivu huku nikiyahurumia mapafu yangu
kisha nikautoa mkono wangu dirishani na kukung’uta majivu ya sigara.
Mpaka kufikia pale akili yangu ilikuwa imeanza kupata afya njema katika ufikirivu.
Kwa tafsiri yangu ya wali kichwani ni kuwa mwanamke aliyampigia Momba simu
na kutaka waonane Hotel 92 Dar es Salaam alikuwa ndiye yule mdunguaji hatari
niliyemuona juu ya lile jengo la biashara la Rupture & Capture wakati nilipokuwa
nimeegesha gari langu nje ya Vampire Casino.
Nikaendelea kukumbuka namna mdunguaji yule alivyonitoroka kwenye yale
maegesho ya magari ya jengo la biashara la Rupture & Capture na ile teksi ya Momba
usiku ule. Bila shaka Momba alikuwa akifahamiana vizuri na mdunguaji yule hatari.
Nikahitimisha huku nikimalizia kuvuta sigara yangu kisha nikakitupa kipisi cha
sigara ile dirishani huku nikiupuliza moshi wake nje taratibu. Hatimaye nikageuka na
kumtazama mzee Ngonyani huku uso wangu ukiwa na matumaini.
“Nashukuru sana kwa maelezo yako kwani huwenda yakanisaidia katika kuwanasa
wauaji wa Momba” nikamwambia mzee Ngonyani kisha nikampa namba zangu za
simu.
“Naomba unipigie simu pale utakapowaona tena wale watu waliojitambulisha
kwenu kuwa ni askari”
“Bila shaka!” mzee Ngonyani akaongea kwa utulivu.
“Nakutakia kazi njema”
“Kazi njema na wewe pia” mzee Ngonyani akaniaga wakati nilipokuwa nikifungua
mlango wa teksi yake na kutoka nje huku macho yake yakinisindikiza kwa nyuma.
_____
WAKATI NILIPOKUWA NIKIENDESHA gari langu kuelekea Hotel 92
Dar es Salaam fikra zangu zilikuwa zimejikita kwenye mjadala mwingine. Mawazo
yangu yalikuwa yamehamia kwa yule mdunguaji huku nikiisumbua akili yangu katika
kutaka kufahamu mdunguaji yule hatari alikuwa nani na aliingiaje katika mkasa huu.
Halafu nikakumbuka siku ile mdunguaji yule hatari namna alivyompopoa vibaya yule
mwanaume kwenye ile baraza Vampire Casino.
Nikiwa naendelea kuvuta kumbukumbu zangu vizuri taswira ya mdunguaji yule
hatari ikaanza kujengeka vizuri kichwani mwangu huku nikikumbuka siku ile ya
kwanza nilipomuona na kuanza kumfuatilia kutoka kwenye maegesho ya magari ya
Vampire Casino hadi kule mtaa wa Nkurumah. Halafu nikaendelea kukumbuka namna
mdunguaji yule alivyonizidi kete na kunitoroka usiku ule kwenye lile jengo la biashara
la Rupture & Capture.
Nikaendelea kuwaza kuwa mtu yoyote ambaye angeweza kumdungua yule mtu
kwenye ile baraza ya Vampire Casino kutoka kule juu ya lile jengo la biashara la Rupture
& Capture alifaa kuitwa mdunguaji makini wa daraja la kwanza mwenye uzoefu
mkubwa wa kazi yake.
Swali likabaki kuwa ni idara gani ambayo ingeweza kumpata mtu wa taaluma ya
udunguaji makini namna ile kama siyo kwenye jeshi la polisi au jeshi la wananchi?. Na
kama mdunguaji yule alikuwa mwanajeshi sasa alikuwa amejiingiza vipi katika mkasa
huu?. Na kwanini wale watu walionishambulia kule Tabata relini walikuwa wakimtafuta
yule mdunguaji?. Maswali bado yalikuwa mengi na sikupata majibu. Kwa vile akili
yangu ilikuwa ikitaabika sana kutafuta majibu nikajitia utulivu wa fikra zangu kwa
mche mwingine wa sigara
Dondoo za mzee Ngonyani zilikuwa zimenipa wepesi kidogo katika harakati
zangu. Hata hivyo nilishindwa kuelewa kama nilikuwa nimepiga hatua yoyote katika
kile nilichokuwa nikikipeleleza ingawa sikutaka kukata tamaa.
_____
HOTEL 92 DAR ES SALAAM ilikuwa miongoni mwa hoteli nyingi za daraja
la kati zilizopandwa kwa fujo karibu kila kona ya jiji la Dar es Salaam. Hoteli hiyo
yenye ghorofa nane ilikuwa imepandwa nyuma ya stendi ya mabasi yaendeyo kasi
eneo la Ubongo huku ikizungukwa na makazi ya watu na majengo mengine marefu
ya ghorofa ambayo sikuweza kuyatambua kwa haraka kuwa yalikuwa yakitumika kwa
shughuli gani. Hoteli hiyo ilikuwa imezungukwa na ukuta mzuri na miti mirefu ya
miashoki iliyopandwa katika namna ya kuvutia.
Baada ya safari ya kitambo nikawa nimeifikia hoteli ile. Ile Hoteli ilikuwa kwenye
mtaa tulivu usiyokuwa na pilika nyingi za kibinadamu. Nilipofika nikapita getini kisha
nikasumbuka kidogo kutafuta maegesho ya gari langu kwani kulikuwa na magari mengi
yaliyokuwa yameegeshwa kwenye eneo la maegesho la hoteli ile. Hata hivyo nikajikuta
nikikata tamaa kidogo kwa kutoiona ile teksi ya Momba iliyokuwa ikitumiwa na yule
mdunguaji katika maegesho yale.
Niliegesha gari langu kisha nikafungua mlango na kushuka nikitembea taratibu
kuelekea kwenye mlango wa mbele wa hoteli ile na wakati nikifanya vile nikawa
nikiyatembeza macho yangu kutazama huku na kule katika namna ya kuyachunguza
magari mengine yaliyokuwa yameegeshwa eneo lile. Ile teksi ya
Momba bado sikuiona. Nilimaliza kupanda ngazi kisha nikapotelea kwenye
mlango wa mbele wa Hotel 92 Dar es Salaam.
Katika seti tatu za makochi ya sofa yaliyokuwa kwenye ukumbi wa chini wa
hoteli ile seti moja ilikuwa imekaliwa na wanaume wanne huku meza fupi ya vioo
iliyokuwa katikati yao ikiwa imebeba aina tofauti za vinywaji. Seti nyingine ya pili
ilikuwa imekaliwa na mwanamke na mwanaume ambao walionekana kwa kila hali
kuwa ni wapenzi. Seti ya mwisho ya makochi ilikuwa tupu. Runinga mbili kubwa
zilizokuwa zimetundikwa kwenye kuta za ukumbi ule zilikuwa zikionesha muziki hata
hivyo hakuna mtu aliyeonekana kuzitazama.
Kipande mstatili cha sakafu nzuri ya tarazo kikanichukia hadi eneo la mapokezi
la hoteli ile ambapo niliwakuta wasichana wawili wahudumu waliovaa sare za kazi.
Nyuso zao zenye furaha zikanieleza kuwa walikuwa wakiyazingatia vizuri maadili ya
kazi yao. Sikujishughulisha na macho ya watu wachache waliokuwa upande wa kulia
kwenye ukumbi ule wakijipatia mlo.
“Hamjambo warembo?” niliwasalimia wale wasichana wa mapokezi huku
nikiigemeza mikono yangu kwenye ukuta mfupi wa mbao uliyopakana na nondo za
eneo lile.
“Hatujambo!”
“Karibu kaka” msichana mmoja wa pale mapokezi akanikaribisha huku akijisogeza
karibu yangu.
“Ahsante!” nikamuitikia yule msichana huku nikayatembeza macho yangu
kuwatazama watu waliokuwa mle ndani. Sura zote mle ndani zilikuwa za kawaida
hivyo nikayarudisha macho yangu kuwatazama wale wasichana.
“Naomba maji baridi” nikamwambia yule dada aliyesogea karibu yangu huku
nikimroga kwa tabasamu langu maridhawa.
“Maji makubwa au madogo?” yule msichana akaniuliza.
“Makubwa tafadhali! niupoze mtima wangu kabla ya hili joto la jiji la Dar es
Salaam halijanitoa roho” nilimwambia yule mhudumu na maji yale yalipoletwa
nikafungua kizibo na kugida mafunda kadhaa kisha nikaitua ile chupa juu ya kaunta
na kuwatazama wale wasichana huku nikipumbazwa kidogo na uzuri wao.
“Mbona asubuhi yote hii inakunywa maji kaka?” yule msichana akaniuliza huku
akielekea kununua maongezi yangu.
“Afya yangu si mnaiona wenyewe kuwa siyo ya kubabaisha” nikawaambia wale
wasichana wa mapokezi huku nikiangua kicheko hafifu na kicheko hicho kilipokuwa
ukingoni nikavunja ukimya.
“Nimemfuata mgeni wangu ila huwenda msinielewe!” nikaongea kwa utulivu na
nilichokiona kwenye nyuso zao ni mshangao usioleweka.
“Kwanini tusikuelewe?” wote wakaniuliza kwa shauku.
“Jina lake silijui” nikawaambia wale wahudumu huku nikitengeneza tabasamu la
kirafiki usoni mwangu.
“Mh! sasa tutakusaidiaje kaka wakati wewe mwenyewe jina la mgeni wako hulijui”
“Mwanamke au mwanaume?” mwenzake akaniuliza.
“Mwanamke na pengine niseme kuwa ni wifi yenu ila msimuonee wivu”
nikawahadaa wale wasichana na hapo wakaangua kicheko cha kimbea.
“Mh! kaka yangu huo siyo mchepuko kweli?”
“Au umempata mitandaoni maana mapenzi ya siku hizi mh!” mwenzake akadakia
“Si bora ingekuwa mitandaoni jina lake ningelijua. Mimi nimeungwa nami
nikaunganika”
“Mh! wanaume nyinyi kwa michepuko” yule msichana aliyeniletea maji akaongea
huku akianguka kicheko hafifu na hapo mwenzake akaungana naye huku wote
wakionekana kufurahishwa na mkasa wangu na kutunga.
“Mh! mnatuonea tu wanaume kwani sisi tunachepuka na nani kama siyo nyinyi”
niliwaambia wale wasichana huku nikitoa noti ya shilingi elfu moja kuyalipia yale maji.
“Sasa huyo wifi yetu ina maana hata namba yake ya simu huna?”
“Ningekuwa na namba yake na jina lake pia ningelijua. Hilo ndiyo kosa nililofanya
tatizo ni kuwa mawasiliano yetu tumeyafanya kwenye simu ya rafiki yake na huyo
rafiki yake sasa hivi hapatikani kwenye simu ingawa alinihakikishia kuwa nikifika hapa
na kumuulizia nitampata”
Wale wahudumu wa mapokezi wakaniangalia kwa utulivu na nilichoweza
kukisoma katika macho yao ni kuwa walikuwa wamenijumuisha kwenye kundi la
wanaume mabingwa wa michepuka jijini Dar es Salaam.
“Sasa tutakusaidiaje kaka?” hatimaye wakaniuliza na swali lao likanipelekea nianze
kuelezea sifa za nje za mwanamke yule mdunguaji hatari. Nilipomaliza kutoa maelezo
yangu nikawaona wale wahudumu wakitazamana kisha mmoja akachukua kitabu
chenye orodha ya majina ya wageni waliofika pale hotelini na kupewa huduma ya
malazi kwa nyakati tofauti.
Halafu nikamuona yule mhudumu akipekua karatasi za kile kitabu kwa haraka
hadi pale alipokaribia ukurasa fulani na hapo akapunguza kasi na kuanza kupekua
kurasa taratibu. Yule mhudumu alipofika kwenye ukurasa fulani akaweka kituo na
kuanza kusoma maelezo yaliyokuwa kwenye ile kurasa halafu akayahamisha macho
yake kunitazama kisha akauliza.
“Mgeni wako ameingia hapa hotelini ndani ya wiki hii?”
“Ndiyo!” nikamwitikia kwa utulivu.
“Wateja wote walioingia hapa hotelini wiki hii wamelala siku moja na wote
wanaonekana kuwa walikuwa wakitoka mikoani” yule mhudumu akaniambia na
hapo nikamuona akinitazama tena. Tukio lile likanipelekea nitambue kuwa fikra zake
zilikuwa zimesimamishwa na jambo fulani.
“Vipi?” nikamuuliza kwa shauku.
“Wifi yetu bila shaka anaitwa Mona kwani hapa anaonekana kuwa ndiye mteja
wetu pekee aliyekaa kwa muda mrefu. Yupo chumba namba 33” yule mhudumu
akaniambia huku akianguka kicheko cha kimbea hata hivyo mimi nilifurahi tu kwani
nilikuwa nimerejewa na matumaini.
“Chumba namba 33 ghorofa ya ngapi?”
“Kipo ghorofa ya nne na ukimpata wifi yetu tupigie simu kaunta tuwaletee
maji baridi makubwa” yule mhudumu akaniambia huku akiangua kicheko hafifu.
Nikaungana naye nikicheka kidogo na kumkonyeza huku nikitabasamu kisha
nikashika uelekeo wa upande wa kulia na nilipozifikia ngazi nikaanza kuzipanda
nikielekea ghorofa za juu za ile hoteli huku ile taswira ya mdunguaji ikianza kujengeka
upya katika fikra zangu. Sikutaka kupanda juu ya lile jengo kwa kutumia lifti kwani
kwa kufanya hivyo ningejinyima fursa nzuri ya kuweza kuitalii Hotel 92 Dar es Salaam.
Nilipomaliza kuzipanda zile ngazi nikawa nimetokezea kwenye korido ya ghorofa
ya pili. Mwisho wa ngazi zile upande wa kulia kulikuwa na dirisha la kioo. Kupitia
dirisha lile niliweza kuliona jengo la stendi ya mabasi yaendayo kasi Ubongo jijini
Dar es Salaam lakini kwa sehemu tu ambayo ilitawaliwa na mapaa ya mabasi na kituo
cha kujazia mafuta. Pilikapilika za kibinadamu zilikuwa zikiendelea kama kawaida.
Nilisimama kidogo nikiitazama korido ile tulivu iliyokuwa ikitazamana na milango ya
vyumba kwa upande wa kushoto na kulia.
Mwisho wa korido ile kulikuwa na dirisha lingine lililofunikwa na pazia refu jeupe.
Nilitulia nikilitazama pazia lile namna lilivyokuwa likipepea taratibu na kwa mbali
niliweza kusikia sauti kutoka kwenye runinga zilizokuwa kwenye vile vyumba. Utafiti
wangu ukanitanabaisha kuwa muonekano wa korido ile usingetofautiana na korido
nyingine zilizokuwa kwenye jengo lile.
Nilikuwa sahihi kwani nilipofika kwenye ghorofa ya nne ya lile jengo la hoteli
nikatambua kuwa mandhari yale hayakutofautiana na yale mandhari ya ghorofa ya pili.
Kitu pekee nilichogundua kuwa kilikuwa kimeongezeka kwenye korido ya ghorofa
ile ilikuwa ni kengele ya tahadhari kwa ajili ya matukio ya moto na hatari nyinginezo.
Nilisimama kwenye korido ile nikiupisha utulivu kichwani mwangu na mara hii
nilijiona kuwa ni mpelelezi mwenye mafanikio niliyekuwa mbioni kuhitimisha mkasa
huu wenye mzongezonge ya aina yake. Taswira ya mdunguaji ikiwa imetafsirika
vizuri kichwani mwangu nikaanza kuvuta picha namna ambavyo fumanizi langu
litakavyomuacha mdomo wazi kama mnzinzi aliyedondosha pakiti ya kondomu
karibu na kapu la sadaka kanisani.
Tofauti na zile korido za chini za lile jengo la hoteli korido ile ilikuwa tulivu sana
na kama ningekuwa sikuhakikishwa uwepo wa mwenyeji wangu ndani ya chumba
33 kwenye korido ile basi huwenda ningeridhisha kuwa katika vyumba vya korido ile
hapakuwa na watu.
Hatimaye nikaupeleka mkono wangu mafichoni kuikagua bastola yangu na
uwepo wake ukaniongezea imani ya kumkabili adui wangu bila wasiwasi wowote.
Bila kupoteza muda nikaanza kuzitupa hatua zangu kwa utulivu kwenye korido ile
huku macho yangu yakitazama upande wa kushoto na kulia nikiikagua milango ya
mle ndani.
Baada ya hatua kadhaa hatimaye nikauona ule mlango wa chumba namba 33
huku namba zake zikiwa zimechongwa vizuri kwenye vibao vyeupe. Mlango wa kile
chumba namba 33 ulikuwa ni wa tano kutoka mwisho wa ile korido na juu ya mlango
ule kulikuwa na kioo kipana chenye mawimbi ya kumzuia mtu kuona ndani ya kile
chumba. Hata hivyo kupitia kioo kile nikagundua kuwa taa ya ndani ya chumba kile
ilikuwa ikiwaka na tofauti na pale chumba kile kilikuwa tulivu na chenye ukimya wa
aina yake.
Nikausogelea ule mlango huku nikitengeneza picha fulani kichwani ya mdunguaji
yule hatari labda akiwa maliwatoni,ameketi kwenye kochi au amelala kitandani
akiendelea kuuchapa usingizi.
Nikaupeleka mkono wangu kwenye mlango ule kisha nikaanza kugonga kwa
utulivu huku mkono wangu mwingine ukiwa tayari umezama mafichoni kuikamata
bastola yangu. Nikaendelea kugonga ule mlango hata hivyo sikupata mwitikio
wowote wala kufunguliwa mlango. Labda huwenda mdunguaji alikuwa akitafakari
kuwa mngongaji wa mlango ule angekuwa nani kama siyo kujadiliana na fikra zake
zilizompelekea ajihisi kuwa alikuwa ndotoni au pengine kilichokuwa kikifanyika
kilikuwa kweli.
Nilirudia kugonga mlango ule tena kwa kishindo zaidi cha kuweza kumwamsha
mwenyeji wa chumba kile kutoka katika usingizini mzito lakini ule mlango
haukufunguliwa wala sauti ya mtu yeyote kusikika.
Hatimaye nikakisogelea kitasa cha ule mlango na kutega vizuri sikio langu nikisikiliza
utulivu wa chumba kile. Mle ndani ya kile chumba kulikuwa kimya na hakuna sauti
yoyote iliyosikika. Nikageuka tena kutazama kwenye ile korido nikichunguza kama
kungekuwa na kamera za usalama. Sikuziona na huwenda hazikuwekwa kwa makusudi
katika namna ya kutunza siri za wateja waliokuwa wakiingia na kutoka kwenye vile
vyumba. Hali ile ikanifurahisha hivyo nikaichomoa bastalo yangu kutoka mafichoni
na kuikamata vema mkononi.
Kisha nikajipapasa mifukoni kuzichukua funguo zangu malaya hata hivyo
nilisitisha zoezi lile pale nilipokumbuka kuwa nilikuwa sijajaribu kufungua kitasa cha ule
mlango. Hivyo katika hali ya kutaka kutafuta hakika nikakishika kitasa cha ule mlango
na kukizungusha taratibu huku bastola yangu ikiwa mkononi. Kile kitasa kikafunguka
na hapo nikafanya jitihada kidogo za kuusukuma ule mlango. Kitu kilichonishangaza
ni kuwa mlango ule ulikuwa wazi na hapo mshangao ukazichukua fikra zangu huku
maswali mengi yakianza kupita kichwani mwangu. Niliusukuma mlango ule taratibu
huku nikiwa nimejidhatiti kikamilifu kukabiliana na masaibu ya namna yoyote mle
ndani. Muda mfupi uliofuata nikawa nimeingia ndani ya chumba kile.
Mara tu nilipoingia ndani ya kile chumba nikayatembeza haraka macho yangu
kukagua mandhari ya mle ndani. Upande wa kushoto wa kile chumba kulikuwa na
kabati la mbao lililojengewa ukutani. Kabati lile sasa lilikuwa wazi bila ya kitu chochote
ndani yake. Pembeni ya lile kabati niliuona mlango lakini mlango ule ulikuwa wazi.
Nikazitupa hatua zangu taratibu nikisogea na kutazama ndani ya ule mlango. Mandhari
ya mle ndani yakanijulisha kuwa kile kilikuwa chumba cha maliwato lakini mle ndani
hapokuwa na kitu chochote hivyo nikarudi kule chumbani.
Kilikuwa chumba kikubwa chenye dirisha pana lililofunikwa kwa pazia refu
jeupe lenye maua mekundu yaliyodariziwa vizuri. Katikati ya chumba kile kulikuwa
kitanda kikubwa kilichokuwa kimefunikwa kwa shuka safi za rangi ya kijivu huku
zikiwa zimeandikwa kwa maandishi makubwa Hotel 92 Dar es Salaam. Tafsiri ya haraka
niliyoipata ni kuwa hakukuwa na mtu mle ndani kwani kiyoyozi na runinga pana
vilivyokuwa ukutani mle chumbani vilikuwa vimezimwa.
Hatimaye nikasimama nikiyatembeza macho yangu mle ndani kwa utulivu na kabla
sijafanya uchunguzi wangu taswira niliyoiona kwenye kochi moja la sofa lililokuwa
kwenye pembe ya chumba kile ikaamsha hisia zangu upya. Kijana mzuri wa kiume
mwenye umri wa kati ya miaka ishirini na nne na ishirini na saba alikuwa ameketi
kwenye kochi lile huku akiwa kifua wazi baada ya shati lake kuraruliwa vifungo.
Ingawa macho ya kijana yule yalikuwa yamesimama yakinitazama lakini haraka
nilipoyachunguza nikagundua kuwa hayakuwa na uhai. Nikapiga hatua zangu taratibu
nikimsogolea pale alipoketi na hapo nikagundua kuwa uso wake ulikuwa umetaabika
kwa kuvumilia mateso makali kabla ya kifo chake. Mdomo wake ulikuwa wazi huku
damu nzito ikiwa imeganda na kuacha michirizi puani mwake. Nikasimama kwa
utulivu nikimtazama kijana yule na kwa kweli nilishikwa na hasira.
Risasi za muuaji zilikuwa zimeacha matundu mawili makubwa kwenye mbavu za
kijana yule na damu iliyotoka kwenye matundu yale ya risasi ilikuwa imetengeneza
michirizi mizito juu ya marumaru nyeupe zilizokuwa chini sakafuni kwenye
chumba kile. Alikuwa kijana mzuri na mtanashati ambaye uwepo wake tu ungeweza
kuwababaisha wasichana warembo wasiokuwa na uvumilivu. Pembeni ya kochi la
sofa aliloketi yule kijana kulikuwa na stuli ndogo yenye miguu mitatu na juu ya stuli ile
kulikuwa na chupa ya pombe kali aina Screw driver yenye kinywaji nusu huku pembeni
yake kukiwa na bilauri ya kioo.
Kwa kweli akili yangu ilikataa kabisa kufanya kazi kwani tangu kuanza kwa mkasa
huu mkusanyiko wa matukio ya namna ile ulikuwa bado haujanifungulia njia ya
kunifikisha kule ninapotaka.
Nilikumbuka kifo cha Zera kisha nikamkumbuka yule mtu aliyedunguliwa nje ya
Vampire Casino usiku ule halafu fikra zangu zikahamia kwa kifo cha Momba kabla ya
kumtazama kijana yule mzuri ambaye mwonekano wake ulitosha kunithibitishia kuwa
starehe zilikuwa kipaumbele namba moja cha maisha yake hapa duniani.
Kwa kweli nilisikitika sana nikijiegemea ukutani huku hisia zangu zikitafunwa na
jinamizi baya la muendelezo wa matukio ya mauaji yasiyokuwa na sababu za msingi.
Nilipokuwa katika hali ile fikra zangu zikahamia tena kwa mdunguaji na kabla sijaanza
kutengeneza hoja mara nikasikia mtu akigonga ule mlango wa kile chumba. Tukio
lile likapelekea moyo wangu upige kite kwa nguvu na hapo kijasho chepesi kikaanza
kupenya mgongoni.
Sikutaka kusubiri nini ambacho kingetokea mle ndani hivyo kufumba na kufumbua
nilikuwa chini ya kitanda cha mle ndani huku uwazi mdogo ulioachwa baina ya shuka
la kitanda kile lililokuwa likining’inia na ile sakafu ya marumaru ukiniwezesha kuiona
miguu ya mtu aliyeingia mle ndani baada ya kuchoka kugonga mlango bila kujibiwa.
Hatimaye mtima wangu ukatulia tuli baada ya kumuona mhudumu wa hoteli ile
akiingia mle ndani ambaye nilimtambua haraka kutokana na sare zake. Mwanamke
yule mnene mwenye umri sawa na wa mama yangu mzazi mkononi alikuwa amebeba
ndoo ndogo maalum kwa ajili ya kupigia deki na beseni lenye mashuka masafi ya
hoteli ile.
Mara baada ya kuingia mle ndani yule mama akasimama kidogo akionekana
kustaajabishwa kwa kuukuta mlango wa chumba kile ukiwa haujafungwa au pengine
kwa kukiona kitanda cha mle ndani kikiwa kimetandikwa vizuri.
Yule mwanamke alipogeuka akaiona maiti ya yule kijana kwenye lile kochi
lililokuwa kwenye kona ya kile chumba. Taharuki aliyomfika mama yule ikampelekea
atupe vifaa vyake vya kazi na kuanza kutimua mbio akitoka nje huku akipiga mayowe
ya hofu.
Nilifahamu kipi ambacho kingefuatia baada ya pale hivyo nikajiviringisha na
kutoka chini ya uvungu wa kile kitanda kisha nikaelekea kwenye ule mlango wa kile
chumba. Muda mfupi uliofuata nilikuwa nje ya kile chumba nikilitoroka eneo lile.
Wakati nikishuka ngazi kuelekea chini ya lile jengo nikakutana na mashuhuda
wengine waliokuwa wakizipanda zile ngazi kwa pupa kuelekea kwenye kile chumba
nilichotoka. Nilichokihitaji ilikuwa ni kuondoka haraka eneo lile kabla polisi
hawajaanza kunusa pua zao kwani hadi wakati ule nilikuwa nikiamini kuwa taarifa
zangu zilikuwa tayari zimewafikia polisi na kwa maana nyingine polisi hao walikuwa
mitaani wakinisaka.
Nilifika sehemu ya mapokezi chini ya ile hoteli na hapo nikagundua taarifa za kifo
cha yule kijana kule chumbani zilikuwa zimesambaa kwenye ile hoteli na kusababisha
taharuki ya aina yake. Hivyo wakati nikikatisha kwenye ukumbi ule kuelekea nje
hakuna mtu yoyote aliyeonekana kunitilia mashaka na hali ile ikanifurahisha.
Bastola yangu nikiwa tayari nimeichimbia mafichoni nikamaliza kushuka ngazi zile
za ukumbini nikiharakisha kuelekea nje ya ile hoteli sehemu nilipokuwa nimeegesha
gari langu. Nilipolifikia gari langu nikafungua mlango na kuingia ndani huku akili
yangu ikiwa hoi kwa kulemewa na mtiririko wa matukio yasiyoeleweka huku hisia
mbaya za kushindwa zikiendelea kuutafuna mtima wangu. Hata hivyo sikutaka kukata
tamaa.
Sikutaka kuendelea kuzubaa eneo lile hivyo nikawasha gari langu na kulitoa kwenye
maegesho yale na wakati nikifanya vile nikagundua kuwa kulikuwa na gari jingine
lililokuwa limeongezeka kwenye maegesho yale. Gari hilo jeusi aina ya Landcruiser
lilikuwa limeegeshwa baada ya kuyapita magari mawili upande ule nilioegesha gari
langu.
Kitendo cha kuliona lile gari kikanipelekea nipunguze mwendo na kugeuka
nikilitazama vizuri gari lile. Hata hivyo tinted nyeusi iliyokuwa kwenye vioo vya lile gari
haikuniwezesha kuona mle ndani ya gari ingawa hisia zangu zilinitanabaisha kuwa mle
ndani ya lile gari kulikuwa na watu waliokuwa wakinitazama.
Hisia hizo zikanishawishi nitake kulirudisha gari langu tena kwenye yale maegesho
ili nipate nafasi nzuri ya kuendelea kulichunguza vizuri lile gari. Lakini baada ya
tafakari fupi nikawa nimesita kufanya vile pale nilipohisi kuwa kitendo cha kulirudisha
gari langu kwenye yale maegesho kingepelekea mtu yeyote ambaye angekuwa ndani ya
lile gari Landcruiser ashikwe na mashaka na hivyo kujijengea hadhari.
Hivyo sikusimama badala yake nikaingiza gia na kukanyaga mafuta na kuendelea
mbele nikielekea kwenye geti la ile hoteli. Hata hivyo macho yangu yalijikuta yakivutwa
na namba za lile gari.
Namba za lile gari zilikuwa ngeni machoni mwangu na zisizofanana kabisa na
namba za magari yaliyosajiliwa nchini Tanzania. Kumbukumbu ya kifo cha yule kijana
niliyemuona kule chumbani muda mfupi uliyopita ikaninyima uhuru wa kuendelea
kufanya utafiti wangu hasa pale nilipohisi kuwa polisi wangekuwa mbioni kufika pale
hotelini.
Hivyo nikakanyaga mafuta na kutoka nje ya geti la hoteli ile na kuingia barabara
inayokatisha mbele ya ile hoteli nikishika uelekeo wa upande wa kulia. Kwa kweli
sikufahamu wapi nilipaswa kuelekea kwa wakati ule hata hivyo nilijitahidi kwa kila hali
kuupisha utulivu akilini mwangu.
Nikaendesha gari langu nikiifuata barabara ile na nilipofika mbele kulikuwa na
barabara nyingine iliyokatisha. Hivyo nilipofika kwenye barabara ile nikakunja kona
na kushika uelekeo wa upande wa kushoto nikitokomea katika vitongoji vya eneo la
Sinza.
Wakati nikiendelea na safari yangu kupitia vioo vya ubavuni vya gari langu mara
nikaliona lile gari jeusi Landcruiser lililokuwa limeegesha nje ya Hotel 92 Dar es Salaam
likiwa nyuma yangu. Tukio lile likanishtua hivyo nikapunguza mwendo kidogo ili
niweze kuliona vizuri lile gari nyuma yangu na mara hii nikapata hakika kuwa gari lile
lililokuwa nyuma yangu lilikuwa ndiyo lile lililokuwa kwenye maegesho ya Hotel 92 Dar
es Salaam muda mfupi uliyopita.
Kwa kweli nilishangazwa sana na tukio lile huku nikijiuliza maswali mengi
kichwani. Niliendelea kulitazama lile gari kupitia vioo vya ubavuni vya gari langu huku
nikiupisha utulivu kichwani mwangu. Kabla ya kufanya maamuzi yoyote nilitaka
kwanza kupata hakika kama nilikuwa nikifuatiliwa au lile gari lilikuwa kwenye ratiba
ya safari zake.
Hivyo nikaongeza mwendo na kwa kuwa nilikuwa fundi mzuri wa vichochoro vya
jiji la Dar es Salaam nikapanga kujizungusha zungusha kwenye mitaa kadhaa ya eneo
lile huku macho yangu yakiendelea kulitazama lile gari nyuma yangu kupitia vioo vya
ubavuni vya gari langu. Kwa kufanya vile ningegundua kuwa nilikuwa nikifuatiliwa na
lile gari au lah! na baada ya hapo ningejua nini cha kufanya.
Niliendelea kuendesha gari langu na nilipofika mbele kwenye makutano mengine
ya barabara nikapunguza mwendo na kuingia upande wa kushoto nikiifuata barabara
nyingine ya lami inayokatisha mitaani. Nikiwa kwenye barabara ile nikaongeza
mwendo kidogo huku macho yangu yakiendelea kutazama kwenye vioo vya ubavuni
vya gari langu. Sikuliona lile gari na hali ile ikanipa matumaini kuwa mambo yalikuwa
shwari na hapo nikaanza kuhisi kuwa nilikuwa nikipoteza muda wangu kwa kufanya
uchunguzi usio na tija.
Hata hivyo muda mfupi baadaye niligundua kuwa sikuwa sahihi kwani sikufika
mbali sana katika safari yangu pale nilipoliona tena lile gari Landcruiser jeusi likiingia
kwenye ile barabara na kunifuata kwa nyuma.
Kwa kutaka kujiridhisha zaidi nilipofika mbele kidogo nikaingia barabara nyingine
inayochepuka kuingia upande wa kulia huku nikiendesha gari langu kwa mwendo
wa wastani. Mara tu nilipoingia kwenye barabara ile haukupita muda mrefu mara
nikaliona tena ile gari Landcruiser nyuma yangu likikunja kona na kuanza kunifuata
tena. Tukio lile likanipelekea nishikwe na hasira hivyo nikaichomoa bastola yangu
kutoka mafichoni na kuiweka kando yangu tayari kukabiliana na rabsha za namna
yoyote.
Kilichofuata baada ya pale ikawa ni kuingia barabara ya mtaa mmoja na kutokezea
kwenye barabara ya mtaa mwingine huku macho yangu yakiendelea kutazama kwenye
vioo vya ubavuni vya gari langu. Yeyote ambaye alikuwa akinifuatilia kwenye lile gari
nyuma yangu nilitaka nimfanye ajutie kwa kitendo kile na hatimaye nimtie hasira ili
aweze kuonesha vizuri hisia zake nami niitumie fursa hiyo vizuri kumshikisha adabu.
Baadaya kulichezesha shere za kutosha lile gari nyuma yangu sasa nilikuwa
nimeamua kugeuza gari langu na kuanza kurudi kule nilipotoka huku nikipunguza na
kuongeza mwendo hapo na pale katika nyakati tofuati. Lengo langu likiwa ni kutaka
kuliweka karibu zaidi lile gari nyuma yangu kwani kufikia pale nilikuwa na hakika
kuwa nilikuwa nimefungiwa mkia. Jambo lililonifurahisha ni kuwa lile gari Landcruiser
nyuma yangu halikutaka kuniacha hivyo nikawa nacheza na uwanja mpana nitakavyo.
Nikaendelea kuendesha gari langu kwenye barabara ile na nilipofika mbele
nikaingia kwenye kituo kimoja cha kujazia mafuta huku nikiwa tayari nimeshaiona
orodha ya mafuta yaliyokuwa yakiuzwa katika kituo kile kupitia bango kubwa
lililokuwa barabarani.
Mara tu nilipoingia kwenye kituo kile cha kujazia mafuta nikasimama na kuulizia
mafuta ambayo hayakuwepo kwenye ile orodha iliyokuwa kwenye lile bango la
barabarani. Lengo langu likiwa siyo kutaka kuongeza mafuta bali kuitumia nafasi ile
kuchunguza mtu au watu waliokuwa ndani ya lile gari nyuma yangu.
Nikiwa bado nimesimama kwenye kile kituo cha kujazia mafuta haukupita muda
mrefu mara nikaliona lile gari jeusi Landcruiser nalo likipunguza mwendo na kuingia
kwenye kile kituo cha kujazia mafuta. Nikiwa natarajia tukio lile macho yangu yalikuwa
makini kutazama mbele ya lile gari na hapo nikawaona wanaume wawili yaani dereva
wa lile gari na mtu mwingine aliyekuwa kando kwenye kiti cha abiria. Wale watu
walikuwa makini wakilitazama gari langu.
Nikiwa nimejiandaa vizuri kwa tukio lile mara tu lile gari jeusi Landcruiser
liliposimama mimi nikakanyaga mafuta na kuondoka eneo lile. Kwa kufanya vile mara
nikaliona tena lile gari jeusi Landcruiser nalo likiacha kile kituo cha mafuta na kuanza
kunifuata. Kwa kweli sikutaka kuendelea kufuatiliwa kama mtoto mdogo hivyo
nikaanza kufikiria namna ya kukabiliana na hali ile.
Nilitaka nipate hakika ya mambo machache kuhusiana na wale watu kwenye
lile gari nyuma yangu kabla ya kupiga hatua nyingine zaidi hivyo nikakanyaga vizuri
pedeli ya mafuta ya gari langu na hapo injini ya gari ikaniletea mrejesho maridhawa.
Sauti ya muungurumo wa injini ikabadilika kadiri nilivyokanyaga klachi na kutupia gia
nyingine. Mwishowe gari langu likawa jepesi huku usukani ukiwa laini hivyo nikawa
nauzungusha kwa mkono wangu imara nikishika uelekeo ninaoutaka. Watembea kwa
miguu kando ya barabara ile wakawa wamestaajabishwa sana na mwendo wangu wa
kasi hata hivyo dereva wa ile Landcruiser nyuma yangu alikuwa mwerevu kuishtukia
dhamira yangu hivyo naye akaongeza mwendo akinifuata.
Muda mfupi uliyofuata lile gari jeusi Landcruiser likawa limenifikia na hapo nikasikia
sauti kali ya dafrao nyuma yangu. Lile gari lilikuwa limenigonga kwa nyuma kiasi cha
kufanikiwa kuyumbisha kidogo uelekeo wangu. Nikayumba kidogo kwenye barabara
ile kabla ya kukaa sawa huku watembea kwa miguu kando ya barabara ile wakiogopa
na kurukia kwenye mitaro iliyokuwa kando ya barabara ile.
Gari langu lilipokaa sawa nikakanyaga klachi na kutupia gia nyingine huku
nikikanyaga vizuri pedeli ya mafuta. Injini ya gari ikalalamika kidogo na ilipotulia gari
likawa jepesi na hapo nikaushika vizuri usukani wa gari kwa mkono mmoja huku
mkono mwingine ukiichukua ile bastola yangu pembeni.
Hatimaye nikayapeleka macho yangu kwenye kioo cha ubavu cha gari langu
kulitazama lile gari jeusi Landcruiser lililokuwa nyuma yangu. Hata hivyo sikufanikiwa
kwani kile kioo cha ubavuni cha gari langu kiliondoshwa haraka kwa kuchanguliwa
vibaya na risasi iliyotoka nyuma yangu. Baada ya pale mirindimo ya risasi ikafuatia
huku baadhi ya risasi hizo zikitoboa vibaya bodi la gari langu. Nikiwa nimeanza
kuhisi hatari nikaongeza mwendo huku nikiliyumbisha gari langu upande huu na ule
ili kuzikwepa zile risasi lakini bado zile risasi ziliendelea kuniandama huku zikitoboa
vibaya kioo cha nyuma cha gari langu na kunikosakosa.
Hali ile ya hatari ilipozidi kuongezeka nikaikamata vyema bastola yangu mkononi
kisha nikashusha kioo cha dirishani. Hata hivyo nilipokuwa mbioni kufanya shambulizi
mara ile Landcruiser ikawa tayari imenifikia tena na kunigonga kwa nyuma. Tukio lile
likanipotezea umakini hivyo nikavuta kilimi cha bastola yangu pasipo kutaka na hapo
risasi moja ikachomoka kwa kasi na kuchana anga huku mlio mkali wa risasi ukisikika.
Sikutaka kuendelea kuiruhusu hali ile hivyo nikaukamata vizuri usukani wangu
kisha nikakunja kona ya ghafla mbele yangu nikiufuata uelekeo wa upande wa kulia.
Hata hivyo lile gari Landcruiser halikuniacha kwani muda mfupi uliyofuata likanifikia
na kuanza kunigongagonga ubavuni na kwa kuwa gari langu lilikuwa dogo kwa kweli
lilizidiwa nguvu na kupondekapondeka ubavuni huku likiminywa kwenye ukuta
wa pembeni wa kiwanda cha maji kilichopakana na barabara ile. Zile risasi zikawa
zikiendelea kuniandama na muda mfupi uliyofuata kile kioo cha nyuma cha gari langu
kikachanguka vibaya na kutawanyika. Hali ilikuwa mbaya na endapo ningeendelea
kuiruhusu hali ile wale watu wangeyakatisha maisha yangu kiulaini.
Gari langu lilikuwa limebanwa mno na kwa upande wa kushoto wa barabara ile
kulikuwa na mtaro mkubwa wa majitaka hivyo endapo ningeendelea kuiruhusu hali
ile basi huwenda ningesukumiwa mtaroni na hapo gari langu lingepinduka. Hivyo
nikaanza kufikiria njia mbadala ya kujinasua.
Nikapangua gia zote hadi kufikia gia namba moja kisha nikakaza mguu wangu na
kukanyaga pedeli ya mafuta. Kwa kufanya vile gari langu likapaa hewani na lilipotua
chini magurudumu yake ya upande wa kushoto yakahamia upande wa pili wa ule
mtaro. Hivyo ule mtaro wa majitaka ukawa katikati ya difu.
Lilikuwa tukio la hatari lakini salama. Lile gari Landcruiser kwa kuwa lilikuwa
limezoea kuniegemea hapo awali likapoteza mhimili na kuanza kuserereka likiyumba
ovyo barabarani. Hata hivyo yule dereva alikuwa mtundu wa kucheza na gari hivyo
hatimaye akafanikiwa kulituliza vizuri gari lake barabarani kisha akaanza kunifuata na
safari hii lile gari lilikuja kwa kasi zaidi.
Niliweza kuinusa hatari iliyokuwa mbioni kunikabili na sikutaka kuisubiri hivyo
nikaikamata vizuri bastola yangu na kuvuta kilimi chake nikiiruhusu risasi moja
kusafiri. Risasi ile ikasafiri na kuchana kioo cha mlango wa mbele wa ile Landcruiser
ikitokezea upande wa pili wa dereva. Wale watu ni kama walikuwa wameishtukia
mapema dhamira yangu hivyo wakawahi kulala chini na kuiacha risasi ile ikiparaza juu
ya vichwa vyao na hivyo kupunguza kasi ya lile gari kunifikia. Sikupunguza mwendo
hivyo baada ya muda mfupi nikawa nimeliacha lile gari nyuma yangu. Hatimaye
nikalirudisha tena gari langu barabarani huku kioo cha nyuma kikiwa kimeondoshwa
kwa risasi. Baadhi ya taa za nyuma za gari langu zilikuwa zimepasuka na matundu ya
risasi za wale watu yalikuwa yamelipelekea gari langu kwa baadhi ya maeneo lifanane
na chujio.
Zile risasi ziliendelea kuniandama na kweli nilijitahidi kuzikwepa kwa kila hali
nikiliyumbisha gari langu upande huu na ule barabarani. Watu waliokuwa wakitembea
kando ya barabara ile walipoona vile wakaruka kando huku wakipiga mayowe ya hofu.
Wakati nikifikiria namna ya kujinasua mara nikapata wazo na bila kupoteza muda
nikaubana usukani wa gari langu vizuri kwa mkono mmoja kisha nikakusanya nguvu
za kutosha. Nilipochungulia dirishani kutazama kule nyuma nikajua nini cha kufanya.
Risasi tatu makini nilizozifyatua moja ikachana kioo cha mbele na kutengeneza tundu
dogo lenye nyufa za mipasuko. Sikujua kama risasi ile ilikuwa imempata mtu au lah!
lakini risasi zile mbili zilizosalia angalau zilifanya kazi niliyoitaka. Risasi zile zikaiharibu
na kuitawanya vibaya kabari ya boneti ya ile Landcruiser kwa mbele na kwa kuwa lile
gari lilikuwa kwenye kasi sana hivyo upepo mwingi ukaingia kwenye lile boneti na
hapo lile boneti likafunguka vibaya kama soli ya kiatu iliyotatuka.
Lilikuwa pigo safi la kiufundi lenye matokeo mazuri ya kuridhisha kwani boneti
lile lilifumuka vibaya na kufunika kile kioo cha mbele cha ile Landcruiser. Tukio lile
likampelekea yule dereva wa ile Landcruiser apoteze ueleko kama kipofu. Lile gari
Landcruiser likaanza kuyumba ovyo likipoteza uelekeo. Watu waliokuwa eneo lile
kuona vile wakaanza kupiga mayowe ya hofu.
Dereva wa lile gari akajitahidi kwa kila hali kuuthibiti usukani wake hata hivyo
hakufanikiwa kwani hatimaye lile gari Landcruiser likagonga ukingo wa daraja dogo
la mfereji wa majitaka uliokuwa kando ya barabara ile. Tukio lile likayapelekea
magurudumu ya mbele ya lile gari yapande juu ya ukingo wa daraja lile dogo na hapo
nikaona tukio la kushangaza.
Katika hali ya kushangaza mara nikaliona lile gari Landcruiser likipaa hewani kama
mwanasesere na lilipotua chini likapinduka mara mbili kisha likaserereka na kwenda
kujikita mtaroni kando ya barabara ile na hivyo kulipelekea eneo lile lote ligubikwe na
wingu zito la vumbi na mnuko wa mafuta ya gari yaliyokuwa yakivuja kutoka kwenye
tenki.
Kwa kweli lilikuwa ni tukio la aina yake na muda mfupi uliyofuata mashuhuda
wakaanza kukusanyika eneo lile wakitaka kufahamu vizuri nini kilichokuwa kimetokea.
Niliegesha gari langu kando ya barabara kisha nikafungua mlango na kushuka
nikielekea kule lile gari Landcruiser lilipopinduka huku nikiwa nimeikamata vyema
bastola yangu mkononi pasipo kuitilia maanani halaiki ya watu iliyokuwa ikizidi
kuongezeka eneo lile.
Bastola yangu ikiwa mkononi muda mfupi tu mara nikawa nimelifikia lile gari
Landcruiser pale mtaroni. Lile gari Lilikuwa limepinduka vibaya na magurudumu yake
ambayo sasa yalikuwa yakitazama juu yalikuwa yakiendelea kuzunguka kwa kasi.
Kifuniko cha tenki la mafuta la lile gari kilikuwa kimezibuka na hivyo kupelekea
mafuta mengi kuvuja na kusambaa eneo lile. Kitu pekee kilichonishangaza ni kuwa
pamoja na hali ile lakini injini ya lile gari bado ilikuwa ikiendelea kuunguruma.
Nikasogea karibu na nilipochungulia ndani ya lile gari nikawaona wanaume wanne.
Watatu miongoni mwao walikuwa hawajitambui kutokana na mshtuko mkubwa wa
ajali ile kama siyo majeraha makubwa katika baadhi ya sehemu za miili yao. Mwenzao
mmoja alikuwa na nafuu kidogo kwani aligeuka taratibu kunitazama hata hivyo
hakuweza kufanya chochote kwani mguu wake ulikuwa umeminywa vibaya na kunasa
kwenye chesesi ya lile gari.
Nikafungua mlango wa dereva na kuwatazama wale watu kwa makini huku
nikijaribu kuzinakili vizuri sura zao akilini mwangu. Hata hivyo sura za watu wale
zilikuwa ngeni kabisa machoni mwangu. Nikamtazama yule mtu mwenye fahamu
mara mbilimbili kwa udadisi zaidi na hapo nikamuona namna alivyojawa na hofu.
Hofu iliyomfanya ayakwepeshe macho yake na kutazama pembeni.
“Mna shida gani na mimi?” nikamuuliza yule mtu ambaye ndiye pekee aliyekuwa
na fahamu mle ndani. Yule mtu hakunijibu badala yake aliendelea kunitazama huku
akilalamika maumivu ya mguu wake.
“Nakuuliza wewe mna shida gani na mimi?”
“Hakuna mwenye shida na wewe” yule mtu akanijibu huku akiuma meno yake
na kukunja sura katika namna ya kukabiliana na maumivu makali ya majeraha yake.
“Sasa kwa nini mnanifuatafuata kila mahali ninapokwenda?” nikamuuliza yule
mtu na nilipomuona akiendelea kunitazama bila kuongea chochote nikamzaba
makofi mawili ya nguvu kumuweka sawa. Wenzake bado walikuwa wakining’inia
kwenye mikanda ya viti za gari huku fahamu zao zikiwa zimewatoka.
“Nyinyi ni akina nani?” nikamuuliza yule mtu huku nikianza kuwapekua mifukoni.
Vitambulisho vyao vikanitanabaisha kuwa wale watu walikuwa ni askari wa vitengo
nyeti vya usalama wa taifa ingawa sura zao bado zilikuwa ngeni kabisa machoni
mwangu.
“Askari” yule mtu akaongea kwa taabu hata hivyo sikushtushwa na hali ya afya
yake badala yake nikamchapa tena makofi matatu mazito usoni mwake na hapo
kamasi nyepesi za damu zikaanza kumtoka puani.
“Nani aliyewatuma mnifuatilie?” nikamuuliza yule mtu huku akigugumia
maumivu.
“Hatujatumwa na mtu” yule mtu akaongea huku akilalama.
“Kama nyinyi ni wanausalama kweli kwanini msishughulike na mafisadi
wanaofahamika hadi magazetini kwa kuzitafuna pesa za walipakodi kama mchwa na
badala yake mnatumika kuwaonea wanyonge?” nikamuuliza tena yule mtu na mara
hii nikajihisi kama niliyekuwa nikijiongelesha mwenyewe kwani yule mtu hakunijibu
na nilipomchunguza vizuri nikagundua kuwa alikwisha poteza fahamu huku akiwa
ananing’inia kwenye mkanda wa kiti cha gari. Huwenda hali ile ilitokana na maumivu
makali ya majeraha aliyokuwanayo mwilini mtu yule.
Nikatulia kidogo nikiyatembeza macho yangu kuwatazama wale watu mle ndani
na hapo nikagundua kuwa wote walikuwa na bastola mikononi. Nilitaka kuendelea na
uchunguzi wangu lakini mazingira ya eneo lile hayakuniruhusu kufanya hivyo kwani
mashuhuda walikuwa wengi sana.
Sikutaka kupoteza muda hivyo nikaanza kupitisha msako makini mle ndani.
Kitu cha ajabu ni kuwa wale watu mle ndani ya lile gari hawakuwa na simu kama
nilivyodhani badala yake simu pekee iliyokuwa mle ndani ilikuwa ni simu ya
upepo kama zile zinazotumiwa na askari wa usalama barabarani ambayo ilikuwa
imechomekwa sehemu fulani kwenye dashibodi ya lile gari.
Mwishowe nikapata kadi ndogo ya biashara ama business card yenye anwani fulani.
Nikaichukua kadi ile na kuitia mfukoni na wakati nikijishauri nini cha kufanya mara
nikaliona lile kundi la mashuhuda likisogea kando taratibu na kutengeneza nafasi nzuri
ya kupita na hapo nikajua kuwa polisi wa usalama barabara walikuwa wamefika eneo
lile.
Sikutaka polisi wale wanikute hivyo nikatoka kwenye lile gari haraka na
kujichanganya kwenye kundi la wale mashuhuda huku bastola yangu nikiwa tayari
nimeichimbia mafichoni. Baadhi ya mashuhuda walinishangaa hata hivyo sikuwatilia
maanani.
Askari watembeao kwa pikipiki maarufu kwa jina la Vodafaster tayari walikuwa
wamefika eneo lile na kuanza kuwasogeza watu pembeni ili wapate nafasi nzuri ya
kufanya kazi yao.
Muda mfupi uliofuata nikawa nimelifikia gari langu kule nilipokuwa nimeliegesha
ambapo nilifungua mlango na kuingia ndani. Sikutaka kuendelea kuwepo eneo lile
hivyo nikawasha gari langu nikiliacha eneo lile.
_____
DAMU ILIKUWA IKINICHEMKA vibaya mwilini na mzuka wa kazi ulikuwa
umenipanda kichwani na moyo wangu nao haukupingana katu na hisia zangu. Wakati
nikiendelea na safari mawazo mengi yalikuwa yakipita kichwani mwangu. Nilikuwa
nikimtafuta mdunguaji kwa udi na uvumba lakini hadi wakati huu nilikuwa sijamtia
machoni.
Yule kijana aliyeuwawa kwenye kile chumba cha mdunguaji cha Hotel 92 Dar es
Salaam nao ulikuwa ni mkasa unaojitegemea. Niliwakumbuka wale askari wa usalama
wa taifa waliopata ajali wakinifukuza na hapo maswali mengi yakaibuka kwenye fikra
zangu. Askari wale wenye vitengo nyeti vya usalama wa taifa walikuwa wameingiaje
kwenye mkasa huu?. Nikajiuliza bila kupata majibu hata hivyo hisia zangu zikanieleza
kuwa huwenda kulikuwa na jambo kubwa lililokuwa limefichika katika mkasa huu na
huwenda jambo hilo lilikuwa na mtazamo wa kimaslahi kwa baadhi ya viongozi wa
serikali kama siyo serikali yenyewe.
Nilikuwa na hakika kuwa watu wale ndiyo waliohusika na kifo cha Zera na
Momba kwa nyakati tofauti na hapo nikajiuliza kuwa watu wale walikuwa wakitaka
kuzuia kitu gani hadi nguvu yao igharimu uhai wa watu. Jibu sikulipata hivyo fikra
zangu zikahamia kwa mdunguaji. Kwa namna nyingine sikuona sababu kubwa ya
kumchukia mdunguaji kwani mdunguaji yule alikuwa akisakwa kama mimi na hapo
ule msemo wa “Adui wa adui yako ni rafiki yako” ukajengeka kichwani mwangu.
Sikufahamu mdunguaji yule hatari alikuwa ameingiaje kwenye mkasa huu hata hivyo
moyoni niliomba nikutane naye kwa mara nyingine.
Saa saba kasoro mchana ilipotimia niliegesha gari langu lililopata misukosuko ya
kutosha nje ya jengo moja refu la ghorofa eneo la posta jijini Dar es Salaam. Bila
shaka gari langu lilikuwa kivutio kwa watu waliokuwa eneo lile kutokana na yale
matundu ya risasi,michubuko ya rangi ubavuni,kupasuka kwa taa za nyuma pamoja
na kutokuwepo kwa kioo cha nyuma cha gari langu.
Sikujali kitu badala yake mara tu niliposhuka kwenye gari langu nikaharakisha
nikielekea sehemu ilipokuwa lifti ya ghorofa lile na kwa bahati wakati nikifika eneo lile
na kile chumba cha lifti nacho ndiyo kilikuwa kinafika nchini ya lile jengo.
Mara tu kile chumba cha lifti kilipofika chini na mlango wake kufunguka msichana
mmoja mrembo akatoka na kupishana na mimi wakati nikipotelea ndani ya chumba
kile cha lifti. Nilipoingia kwenye kile chumba cha lifti nikabonyeza kitufe cha ghorofa
namba sita ya lile jengo. Muda mfupi baadaye kile chumba cha lifti kikatia nanga
kwenye ghorofa ya sita ya lile jengo na mlango ulipofunguka nikatoka na kujikuta
kwenye korido pana iliyokuwa ikitazamana na milango upande wa kushoto na kulia.
Kabla ya kuendelea mbele na harakati zangu nikaichukua ile business card
niliyoichukua kutoka kwa mmoja wa wale majeruhi kwenye ile Landcruiser na kuyapitia
maelezo yake. Kwa mujibu wa maelezo yaliyokuwa kwenye ile business card bado
nilikuwa sehemu hii. Hivyo nikaanza kutembea taratibu huku nikiitafuta namba ya
mlango iliyokuwa kwenye ile business card.
Kulikuwa na utulivu mkubwa katika eneo lile la ghorofa na kitu pekee nilichoweza
kukisikia eneo lile ni mashine za viyoyozi zilizokuwa zikiunguruma mle ndani. Sakafu
ya korido ile ilitengenezwa kwa marumaru safi zinazovutia na kulifanya eneo lile
lipendeze sana.
Niliitazama milango iliyokuwa kwenye korido ile huku nikijaribu kutengeneza picha
fulani akilini mwangu juu ya kitu ambacho kingekuwa kikiendelea mle ndani na kwa
kweli sikuwa na hisia ya kitu chochote. Hivyo hatimaye nikaanza kutembea taratibu
kwenye korido ile huku nikiyatembeza macho yangu huku na kule nikiichunguza
milango iliyokuwa ikitazamana na ile korido.
Maelezo yaliyokuwa kwenye ile kadi bado nilikuwa nikiyakumbuka vizuri hivyo
macho yangu yakaendelea kusumbuka huku nikiutafuta mlango niliokuwa nikiuhitaji.
Nikiwa mbioni kukata tamaa hatimaye nikauona ule mlango. Mlango huo ulikuwa
katikati ya milango miwili iliyoachana kwa umbali mrefu upande wa kushoto wa korido
ile. Niliyatembeza macho yangu upande wa kulia na nilipoihesabu milango iliyokuwa
upande ule nikagundua kuwa jumla yake ilikuwa ni milango kumi na mbili. Aina ile
ya ujenzi ilinishangaza sana kwani sikuwahi kuiona katika mejengo yote niliyobahatika
kuyafikia katika jiji la Dar es Salaam.
Kilichonishangaza zaidi ni kuwa milango yote iliyokuwa ikitazamana na ile korido
ilikuwa imetengenezwa kwa fomeka isipokuwa mlango mmoja mweusi uliokuwa
katikati ya ile korido upande wa kushoto ambao hata hivyo ulikuwa mkubwa zaidi ya
ile mingine.
Nikausogelea ule mlango na kusimama mbele yake huku maswali mengi yakipita
kichwani mwangu. Niliutazama ule mlango kwa makini huku nikijiuliza kwanini
mlango ule ulikuwa ukitofautiana na milango mingine ya mle ndani. Juu ya ule mlango
kulikuwa na namba na mara hii nilishtushwa sana na namba iliyokuwa juu ya mlango
ule.
Ilikuwa ni namba 666 iliyochongwa kwa ustadi kwa madini ya shaba. Chini ya
namba ile kulikuwa na maneno mengine yaliyoandikwa kwa hati nzuri ya kupendeza
kwa madini yaleyale ya shaba. Maneno hayo yakisomeka Restricted Members Only na
chini ya maandishi yale kulikuwa na mstari mnyoofu uliyoyakinga yale maneno kwa
chini na kufuatiwa na alama sita za nyota za shaba.
Niliutazama mlango ule kwa makini huku nikiupisha utulivu kichwani mwangu
kisha nikaanza kugonga na wakati nikifanya vile nafsi yangu ikaanza kusumbuka katika
kuwaza juu ya kitu gani ambacho kingetokea mbele ya safari. Baada ya kugonga kwa
muda mrefu hatimaye nikapumzika kidogo na wakati nilipokuwa nikijiandaa kugonga
kwa mara ya pili ghafla nikasita baada ya kuuona ule mlango ukifunguliwa.
Ule mlango ulipofunguka mbele yangu nikajikuta nikitazamana na msichana mzuri
sana ambaye kwa kumbukumbu zangu za haraka sikuwahi kumuona msichana mzuri
kiasi kile tangu nizaliwe. Yule msichana alikuwa mrefu zaidi yangu na mwembamba
kiasi. Manukato yake ya gharama yakaziroga pua zangu wakati nilipoyatembeza
macho yangu taratibu kumtazama. Msichana yule mrembo alikuwa amevaa gauni
jepesi la hariri ya rangi nyekundu lakini hata hivyo gauni lile halikuwa na maana
yoyote machoni mwangu kwani wepesi wake ulilichora bila kificho umbo lake refu
la ulimbwende na kuziacha chuchu zake zilizotuna na kusimama wima kuzivuruga
kabisa hisia zangu.
Uso wangu ukiwa tayari umetengeneza tabasamu la kirafiki taratibu nikaanza
kuyatembeza macho yangu nikimtazama mrembo yule kuanzia juu mpaka chini na
mara hii nikagundua kuwa mrembo yule hakuwa amevaa nguo ya ndani. Nikalitazama
gauni lake na hapo nikagundua kuwa lilikuwa limeishia kwenye mapaja yake marefu
yaliyohifadhi misuli laini.
Mikono yake ilikuwa mirefu na inayopendeza yenye kucha ndefu sana zilizopakwa
rangi nzuri inayoendana na vazi lake. Nikayahamisha macho yangu tena kumtazama
kichwani. Nywele zake ndefu,nyeusi na laini zilining’inia hadi mabegani mwake na
kuifanya sura yake nyembamba kiasi ipendeze. Pua yake nyembamba ya kisomali
ilitengeneza kionjo kingine cha uzuri juu ya mdomo wake wa kike wenye kingo pana
na laini zilizokolezwa lipstick nyekundu. Shingoni alining’iniza mkufu mwembama
sana unaometameta wa madini ya almasi nyeupe. Nilipomchunguza masikioni
nikagundua kuwa sikio lake la upande wa kulia halikuwa na kitu lakini lile la kushoto
lilikuwa limetogwa herini nne tofauti ambazo zilikuwa zikimetameta ingawa sikuweza
kufahamu kuwa herini zile nzuri zilitokana na madini gani.
Hata hivyo pamoja na uzuri wa kustaajabisha wa yule msichana lakini bado moyo
wangu ulishtuka sana na kuingiwa na hofu pale nilipoyatazama macho yake. Niseme
kuwa sikuwahi kumuona shetani kwa haya macho yangu ya nyama zaidi ya kuona
matokeo ya kazi zake hapa duniani. Lakini kwa muonekano wa macho ya msichana
yule sikuwa na shaka kusema kuwa huwenda yule alikuwa ndiye shetani mwenyewe
aliyekuwa akizungumziwa na waumini wa dini mbalimbali kama siyo dada yake,wifi
au ndugu yake wa karibu sana. Kwani macho yake yalikuwa yakimetameta sana katika
namna ya kuniogopesha mno. Yale macho yake yaliyokuwa yakimetameta yalifunikwa
kwa kope zake nyeusi na ndefu sana na kumfanya azidi kuonekana msichana wa ajabu.
Nilikuwa mbioni kujishauri kuwa nimtake radhi msichana yule kwa usumbufu
uliojitokeza huku nikidanganya kuwa nilikuwa nimekosea mlango kisha niondoke
eneo lile. Hata hivyo sikufanikiwa kwani yule msichana akawahi kuvunja ukimya huku
akitabasamu.
“Karibu ndani” akaongea kwa sauti ya kubembeleza iliyotuama vyema kwenye
sakafu ya mtima wangu. Moyo wangu ukapiga kite kwa nguvu na kusababisha
usumbufu mdogo wa nafsi na hapo ujasili wangu wote ukatokomea kusikojulikana.
Hivyo nikabaki nikitabasamu tu mbele yake.
“Pita ndani kaka” yule mrembo akanikaribisha na sikutaka kujiuliza mara mbili
badala yake nikapiga hatua zangu taratibu kuingia mle ndani na wakati nikimaliza
kuingia nyuma yangu nikausikia ule mlango ukifungwa. Mara tu nilipoingia mle ndani
haikunichukua muda mrefu kutambua kuwa nilikuwa nimeingia kwenye mazingira
tofauti yenye hisia za hofu.
Harufu ya mle ndani ilikuwa tofauti kabisa na sehemu nyingine zote nilizowahi
kufika hapa duniani. Kwa kweli sikuipenda kabisa harufu ile na hewa ya mle ndani
haikuwa nyepesi wala nzito.
Mara tu tulipoingia mle ndani yule dada akageuka kidogo kunitazama huku
akitabasamu na wakati akifanya hivyo nikaiona tatoo iliyokuwa shingoni mwake.
Ilikuwa ni tatoo ya namba 666 iliyochorwa kwa ustadi sana na ufundi wa hali ya juu
na chini yake kulikuwa na tatoo nyingine ya nyoka aliyeachama mdomo na kutoa nje
pacha ya ulimi wake. Nikaitazama tatoo ile na kweli hofu ikazidi kuniingia hata hivyo
sikusema neno.
Mwanga hafifu wa mle ndani ukaniwezesha kuona mle ndani kwa sehemu
tu. Tulikuwa kwenye chumba kipana lakini kisichokuwa na kitu chochote.
Nilipoyatembeza macho yangu haraka mle ndani mara ukutani nikaiona michoro
mbalimbali ambayo katu haikunivutia kabisa kuitazama ingawa nilihisi kuwa huwenda
ilikuwa imechorwa kwa sanaa ya hali ya juu.
Mchoro mmoja ulionesha kichwa cha mwanamke mzuri lakini mwenye kiwiliwili
cha nyoka. Mchoro mwingine uliwaonesha wanaume wakilawitiana. Mchoro
mwingine uliyofuata ulikuwa na umbo la dunia lililozungukwa na moto mkali. Kisha
kukafuatiwa na michoro mingine kama ya;pete,mnyama fulani asiyeeleweka mwenye
miguu ya binadamu. Mchoro mwingine ulikuwa ni wa mwanamke aliyekuwa uchi wa
mnyama huku amempanda farasi mwenye kichwa cha binadamu. Kwa kweli michoro
ile sikuipenda.
Hatimaye nikayapeleka macho yangu kutazama kwenye sakafu ya kile chumba.
Kwa kufanya vile nikauona mchoro mkubwa wa popo aliyetanua mbwawa zake.
Miguu ya popo yule ilikuwa na misuli imara kama ya simba na mwili wa yule popo
ulikuwa wa binadamu mwanamke mwenye matiti. Nilikuwa nimesimama juu ya
mchoro ule bila kujua na yule msichana akanisukuma kando kwa nguvu za ajabu
zilizonishangaza huku macho yake makali yakinionya kuwa nisilete upinzani wa
namna yoyote.
“Usirudie tena kukanyaga hapa!” yule msichana akanifokea kwa hasira na wakati
nikitafakari yale maneno yake mara nikamuona akitabasamu tena na kwa kweli kitendo
kile kilinichanganya sana na kuniongezea mshaka.
“Wewe ni mwanachama wa humu ndani?” yule msichana mrembo akaniuliza kwa
utulivu huku akiwa amesimama kando yangu.
“Hapana!” nikamjibu huku nikitafakari matokeo ya jibu langu
“Hukusoma maelekezo yaliyokuwa mlangoni kabla kuingia humu ndani?”
“Kuhusu nini?” nikamuuliza kwa shauku
“Aina ya watu wanaotakiwa kuingia humu ndani” yule msichana akaniambia na
hapo nikakumbuka yale maelezo yaliyokuwa juu ya ule mlango wa kuingia mle ndani
yakisomeka Restricted Members Only na hapo jasho jepesi likaanza kunitoka. Hata hivyo
nilipomtazama yule msichana nikamuoana akizidi kutabasamu.
“Basi naomba uniruhusu nitoke nje” nikamwambia yule msichana huku nikianza
kupiga hatua zangu kuuendea ule mlango wa kuingilia mle ndani. Hata hivyo yule
msichana aliwahi kunizuia huku akiniambia
“Usijali kaka,nifuate!” yule msichana akaniambia na hapo tukuanza safari huku
yeye akiwa ametangulia mbele. Sehemu fulani katika ukuta wa kile chumba upande wa
kushoto nikamuona yule msichana akibonyeza tarakimu fulani katika vutufe vyenye
namba vilivyokuwa ukutani katika mlango uliokuwa eneo lile. Kwa kufanya vile mara
nikauona ule mlango ukifunguka. Mlango ule ulipofunguka tukaingia mle ndani kisha
ukajifunga nyuma yetu.
Mara baada ya mlango ule kujifunga tukawa tumetokezea kwenye eneo jembamba
lenye ngazi za kushuka chini. Tukasimama kidogo tukilitazama eneo lile na hapo yule
msichana akageuka na kunitazama huku akitabasamu. Kisha tukaanza kwenda chini
kwa kushuka zile ngazi taratibu na wakati tukishuka yule mrembo akawa akigeuka tena
mara kwa mara kunitazama huku akitabasamu nami nikafanya hisani kwa kutabasamu
kidogo ingawa kwa wakati ule tabasamu halikuwa nafsini mwangu. Hivyo nikapiga
moyo konde na kuendelea na ile safari.
Mwanga hafifu wa taa zilizokuwa ukutani kwenye zile ngazi ukaniwezesha kuona
maandishi yaliyokuwa ukutani eneo lile yakisomeka Vampire Casino-Our place in Dar
es Salaam. Nikayatazama maandishi yale huku nikishtuka sana hata hivyo sikutaka
mshtuko wangu uonekane kwa yule msichana wakati alipogeuka na kunitazama.
“Tunaelekea wapi?” hatimaye nikamuuliza yule msichana.
“Hutaki kuwaona wenzangu?” yule msichana akanijibu huku akitabasamu.
“Ni wazuri na warembo kama wewe?” nikatumbukiza utani kuzipeleleza hisia
zake.
“Nilipokutazama tu nikajua haraka kuwa unapenda wasichana wazuri ndiyo
maana nikakukaribisha humu ndani” yule msichana akaongea huku akiangua kicheko
hafifu. Nilicheka kidogo nikikubaliana naye ingawa ile haikuwa dhamira yangu.
Hatimaye tukawa tumefika kule chini mwisho wa zile ngazi na hapo tukawa
tumetokezea kwenye ukumbi mdogo wenye watu wasiopungua hamsini. Mara hii
nikashtuka sana nilipowatazama wale watu. Ulikuwa mchanganyiko wa wanaume kwa
wanawake vijana kwa wazee. Kitu kilichonishtua zaidi ni kuwa baadhi ya watu wale
nilikuwa nikiwafahamu. Kulikuwa na wanasiasa maarufu,wanamuziki,wanamichezo
na hata viongozi wa dini wakubwa niliokuwa nikiwafahamu.
Watu wale walikuwa wameketi wakimsikiliza kwa makini mtoa mada aliyekuwa
ameketi mbele yao kwenye kiti kama mfalme huku amevaa majoho mekundu. Kitu
kilichonishangaza ni kuwa wakati tukipita eneo lile wale watu hawakujishughulisha
kututazama badala yake waliendelea kumsikiliza mtoa mada mbele yao.
“Wale watu wanafanya nini?” nilimuuliza yule msichana huku nikishangazwa sana
na hali ile.
“Siwezi kukuleza mpaka uwe miongoni mwetu” yule msichana akaniambia huku
tukiendelea na safari.
“Kwani nyinyi ni akina nani?” nikamuuliza yule msichana na wakati huo tulikuwa
tumefika kwenye korido nyingine nyembamba tofauti na ile ya awali. Wakati
tukiendelea na safari nikayatega masikio yangu vizuri mle ndani na kwa mbali niliweza
kuzisikia kelele za vitoto vichanga vikilia kwa sauti kubwa mle ndani. Hali ile ikazidi
kunichanganya kwani mandhari ya mle ndani hayakufaa kufananishwa na wodi ya
wazazi. Kitu kilichonishangaza zaidi ni kuwa kelele zile zilikuwa zimeambatana na
sauti ya vicheko vya wanawake.
Nikiwa nyuma ya yule msichana nikachungulia kwa jicho la pembe ndani ya
vyumba tulivyopishanavyo. Kwa kufanya vile mle ndani nikawaona wanaume kwa
wanawake wakiwa wamevaa makoti marefu kama yale yanayovaliwa na madaktari
na glovu nyeupe mikononi. Wale watu walikuwa wakiweka vitu fulani vyeupe
kwenye mifuko ya nailoni ingawa sikuweza kuona vizuri. Mara hii tena nafsi yangu
ikanitahadharisha kuwa nilikuwa nimejitumbukiza kwenye hatari nisiyoifahamu.
Tulimaliza kuivuka korido ile kisha tukaingia upande wa kulia na hapo nikasikia ile
sauti ya vicheko ikiongezeka. Sikutaka kumuuliza yule msichana kwani niliamini kuwa
majibu ya maswali yangu yalikuwa mbioni kupatikana
 
Viongozi wa nchi na usalama wa taifa ni wajumbe wa shetani ?
 
Kule alipoingia détective. Amekutana na waabudu shetani
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…