Nyakijooga
JF-Expert Member
- Dec 9, 2018
- 276
- 473
Wananchi walianza kuingiwa na hofu baada ya kusikika kwa tetesi kuwa huo uwanja amepewa Mtu binafsi ajenge Shule, tetesi hizo ziliibua minongono ya chini kwa chini.
Lakini siku chache baadae ikaibuka hali ya sintofahamu ambayo ilileta taharuki zaidi, baada ya Mkandarasi kuanza kuchimba eneo hilo na kuanza ujenzi wa msingi, baada ya wananchi kubaini hali hiyo waliamua kulalamika kwa viongozi wa Serikali za Mitaa lakini nao wakawa kimya huku wengine wakawa wanatoa majibu yasiyo eleweka.
Hofu ya wananchi ilikuwa ni juu ya uamuzi wa mamlaka kujenga Shule eneo hilo bila hata kushirikisha wananchi, majibu ya baadhi ya viongozi Serikali za Mitaa na Kata yakawa yanadai kuwa ujenzi huo unaendeshwa na Manispaa ya Kinondoni.
Wananchi wengi waliendelea kuingiwa na hofu baada ya kuona Mwenyekiti wa Serikali za Mitaa akiwa yeye ndio anasimamia ujenzi huku baadhi ya Askari wenye silaha wakiwa wamezunguka eneo hilo huku ujenzi wa msingi ukiwa unaendelea.
Baada ya kuona hali hiyo, baadhi ya wananchi walianza kuandika mabango kwa ajili ya kupaza sauti huku wakipinga ujenzi huo, wakidai kuwa ulikuwa ukifanyika kwenye eneo la uwanja wa michezo ambao umekuwa ukitumika pia kwa shughuli mbalimbali za kijamii zinazozunguka eneo hilo.
Lakini hofu nyingine ikiwa ni kutokana na mazingira ya kuhofiwa kuwa ujenzi huo haufanywi na Serikali bali unafanywa na Mtu binafsi ambaye anakingiwa kifua na baadhi ya watendaji katika mamlaka mbalimbali hasa ngazi ya Manispaa.
Kufuatia malalamiko hayo Waziri wa Michezo, Dr. Damas Ndumbaro August 12, 2024 alifika eneo hilo na kusikiliza malalamiko ya Wananchi. Ambapo baada ya kusikiliza malalamiko yao aliagiza ujenzi wa Shule usitishwe kufanyika kwenye uwanja huo, huku akitoa maelekezo kwamba uwanja ndani ya siku tatu (saa 72) urejeshwe kwenye hali yake ya kawaida na kwamba kama kuna suala la ujenzi wa Shule lifanyike maeneo mengine baada ya wananchi kushirikishwa.
Sakata linaacha maswali yanayohitaji majawabu uhakika
Binafsi nilipomsikiliza Waziri Ndumbalo nikabaini kuna mchezo mchafu utakuwa unaendelea eneo hilo, jambo ambalo linanipa nguvu ya kuomba TAKUKURU kwa kushirikiana na mamlaka nyingine wachunguze kubaini janja janja ili wahusika wakibainika wawajibike.
Kwa mfano, kama ni Manispaa ya Kinondoni inaratibu ujenzi wa Shule hiyo, ni lini iliwashirikisha wananchi katika vikao rasmi na kukubaliana Shule kujengwa eno hilo.
Eneo linavyooneka ni dogo kujengwa Shule hasa ya Serikali, je, mamlaka zilipitishaje ujenzi huo kwenye eneo hilo, ingali kuna maeneo ya wazi ya karibu ambayo yanamilikiwa na Serikali ambayo yangetumika kujenga Shule.
Je, kama Waziri amesitisha ujenzi na kuelekeza miundombinu ambayo ilikuwa imeshawekwa itolewe na uwanja kurejeshewa kwenye hali ya kawaida, nani anatakiwa kuwajibika kwa gharama hizo? au ni pesa za walipakodi zinachezewa.
Hata hivyo kuna harufu ni kwamba ujenzi huo haufanywi na Serikali bali ni Mtu binafsi, sasa najiuliza vibali vya kufanya ujenzi kwenye eneo la Serikali tena kwenye eneo la uwanja amevipata wapi?
Baada ya kufuatilia ni kwamba baada ya Wananchi kuanza kulalamika na kuandika mabango, wahusika walileta kibao kinachoonesha ujenzi unafanywa na Manispaa ya Kinondoni na inajengwa Shule iliyopewa jina la 'Mama Samia Primary School' kama kibao kinavyosomeka, ikiwa lengo ni kuwazima wananchi wasiendelee kuhoji.
Hata hivyo katika mazungumzo yake, Waziri Ndumbaro alisema kuwa Baraza la michezo limeshawasilisha taarifa kwenye Mamlaka kuwa wataweka nyasi bandia kwenye uwanja huo pamoja na taa za sola, je, mamlaka ngazi ya Wilaya hawana taarifa juu ya mpango huo?
Pia soma
Waziri Ndumbaro Asitisha Ujenzi wa Shule Eneo la Michezo Dar
Takukuru wachunguze tufahamu kilichopo nyuma ya pazia
Naomba nitoe wito kwa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na rushwa (TAKUKURU) wafatilie kwa ukaribu suala hilo ili waliofanya uzembe na wataobainika kupokea rushwa kwa namna yoyote wawajibike na kufikishwa kwenye vyombo vya Sheria , jambo hilo lisihishie tu kwenye kusitisha ujenzi, kwa kuwa hata maelekezo ya Waziri kwamba ndani ya saa 72 uwanja uwe umerejeshwa kwenye hali ya kawaida hayajatekelezwa kufukia August 16, 2024.
Pia soma ~ Waziri Ndumbaro alitoa Saa 72 ujenzi usitishwe na Uwanja urejeshwe ulivyokuwa, leo Siku 90 ya 110 hali bado ni ileile