Roving Journalist
JF Roving Journalist
- Apr 18, 2017
- 3,984
- 13,760
Mratibu wa Mafunzo Kituo cha Shule ya Sekondari Bagamoyo, Winchslaus Balige akizungumza katika mafunzo hayo.
Hatua hiyo imebainishwa na Ofisa Elimu wa Mkoa wa Pwani, Jimmy Nkwamu, wakati akifungua mafunzo ya siku tano kwa walimu wa shule za sekondari wanaofundisha masomo hayo kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, na Morogoro yanayofanyika shule ya Sekondari Bagamoyo.
Nkwamu amesema mafunzo hayo yanalenga kuboresha mbinu za ufundishaji na kuongeza ari kwa wanafunzi kupenda masomo ya Sayansi na Hisabati.
“Tunatarajia kuona ongezeko la wataalamu wa sayansi nchini, kwani walimu watafundisha kwa vitendo zaidi na kutumia zana zinazopatikana kulingana na mazingira yao. Hii itawasaidia wanafunzi kuondoa hofu ya masomo haya na kuongeza ufaulu wao,” amesema Nkwamu.
Mwenyekiti wa Wawezeshaji ambaye pia ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma( UDOM), Dk. Emmanuel Sulungu akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo.
Ofisa Elimu Mkoa wa Pwani, Jimmy Nkwamu akizungumza na walimu wa masomo ya Sayansi na Hisabati, wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa walimu hao yanayofanyika wilayani Bagamoyo katika Shule ya Sekondari Bagamoyo.
Mratibu wa mafunzo hayo, katika kituo cha Shule ya Sekondari Bagamoyo, Winchslaus Balige, amesema program hiyo inatekelezwa kupitia Mradi wa Kuboresha Elimu ya Shule za Sekondari nchini (SEQUIP), ambapo walimu 1,071 kutoka mikoa ya Pwani, Dar es Salaam, na Morogoro wanashiriki.
Ameeleza kuwa mafunzo hayo yanawahamasisha walimu kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) kama nyenzo muhimu ya kufundishia, kubuni na kutumia zana mbalimbali kulingana na mazingira yanayowazunguka.
“Lengo la serikali ni kuhakikisha walimu wa Sayansi na Hisabati wanaboresha mbinu za ufundishaji kwa mujibu wa Sera Mpya ya Elimu ya mwaka 2014, toleo la 2023, inayohimiza matumizi ya mbinu za kisasa kwenye kufundishia ili kuendana na mahitaji ya karne ya 21,” amesema Balige.
Mwenyekiti wa wawezeshaji wa mafunzo hayo, Dk. Emmanuel Sulungu, ambaye pia ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), amesema matarajio ni kuongeza ufaulu wa masomo ya Sayansi na Hisabati kwa wanafunzi.
“Tunawahimiza walimu kutumia mbinu mpya wanazojifunza ili kuongeza idadi ya wanafunzi wanaopenda na kufaulu masomo haya, ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakiogopwa,” amesema Dk. Sulungu.
Esther Mianga, kutoka Shule ya Sekondari Makumbusho, Dar es Salaam, amesema anatarajia kujifunza mbinu mpya za ufundishaji zitakazomsaidia kuboresha taaluma yake.
Mwalimu Mdalahela Raina, anayefundisha Hisabati katika Shule ya Sekondari Mbasa, Ifakara, Morogoro, amesema kupitia mafunzo hayo, atajifunza matumizi ya zana za kufundishia na Tehama ili kuongeza ufanisi wa ufundishaji wake.