Yanayoendelea huko Kenya kuhusu suala la uraia wa Miguna Miguna yanasikitisha.
Lakini mwisho wa siku naamini Miguna atawabwaga tu mahakamani.
Na yote haya yamemfika kwa sababu tu alianza kumkosoa sana Uhuru Kenyatta.
Nakumbuka kwenye ule uchaguzi wa 2013 alivyokuwa anapendwa na watu wa Jubilee kwa sababu alikuwa akimnanga Odinga.
Alialikwa hadi kwenye hafla ya kusherehekea uapisho wa Kenyata.
Muda wote huu, hata kipindi akiwa mshauri wa Raila Odinga kipindi ni waziri mkuu, suala la uraia wake halikuwa na utata!
Kagombea mpaka ugavana wa Nairobi na uraia wake ulithibitishwa na tume yao ya uchaguzi.
Hata kitambulisho cha uraia wa Kenya anacho. Achilia mbali kuwa kazaliwa Kenya.
Sasa ghafla baada ya kuanza kumkosoa sana Uhuru eti ndo suala la uraia wake limeibuka.
Sasa huyu Miguna huwa namfananisha na Tundu Lisu kwa umachachari wao wa kuweza kuongea bila hofu.
Kwa mtaji huo, naamini kuwa kama Lisu angekuwa ni mzaliwa wa mikoa iliyo mipakani mwa Tanzania na nchi inayopakana nazo, kudhani au kuhisi kuwa uraia wake ungekuwa ushahojiwa si jambo la ajabu.
Baadhi ya kesi alizofunguliwa Lisu zinachekesha mno kiasi cha kuweza kumfanya mtu adhanie kuwa hao waliotoa maagizo ya yeye kukamatwa na kufunguliwa kesi ni wanafanya hivyo ili kumsumbua tu na si kwa nia ya kwamba wanamfungulia kesi ili hatimaye wampate na makosa na wamfunge jela.
Nadhani huwa wanajua kabisa kuwa kesi zao hazina mashiko.
Hata kwa Miguna Miguna nako ni vivyo hivyo tu.
Watawala wengi wa Afrika wanafanana kwa mengi. Hawapendi kukosolewa na hawana uvumilivu mwingi wa watu wanaotofautiana nao kimtazamo.
Na hulka hii haijalishi kama mtu yupo upinzani au la. Ni kwamba, mtu huyo akishapata madaraka na mamlaka makubwa anabadilika na kutaka kuwa mungu mtu!
Tuna safari ndefu sana na sidhani kama hata njia ya kutufikisha huko twaijua.