Simba imeialika Rayon kuja kucheza nao mchezo wa kirafiki ikiwa ni utamaduni wao wa kila mwaka kuadhimsha Simba Day.
Tamasha hilo hufanyika kila mwaka Agosti 8 na kwa mwaka huu mashabiki wanalisubiri kwa hamu kubwa kwa lengo la kuwaona wachezaji wapya wa timu hiyo waliosajiliwa.
Mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo, aliliambia Nipashe kuwa klabu hiyo ya Rwanda imekubali mwaliko wa Simba na watakuja nchini siku mbili kabla ya tamasha hilo.
“Rayon wamekubali kuja kushiriki na sisi katika maadhimisho yetu ya Simba Day, labda kama mambo yabadilike huko mbele, uongozi ulishafanya nao mazungumzo na kukubaliana,” alisema kiongozi huyo.
Alisema tamasha hilo pia watalitumia kuwatambulisha wachezaji wao wote waliowasajili katika kipindi hiki cha usajili.Kikosi cha Simba chini ya Kocha Joseph Omog kinaendelea na maandalizi yao Afrika Kusini ambapo wachezaji wengine waliokuwa kwenye kikosi cha timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ walitegemewa kutua nchini humo jana kuungana na wenzao.
Aidha, nyota wao mpya Haruna Niyonzima anategemewa kutua Afrika Kusini wiki ijayo baada ya kumaliza kozi ya ukocha anayosomea nchini kwao, Rwanda.
Chanzo: Nipashe