Simulizi : Elizabeth Neville

Simulizi : Elizabeth Neville

Abdallahking

JF-Expert Member
Joined
Mar 19, 2018
Posts
3,985
Reaction score
10,840
28472249_1839271999457499_113645294213660672_n.jpg



Simulizi : ELIZABETH NEVILLE
Mwandishi : HALFANY SUDY
Imeletwa kwenu na: BURE SERIES



SEHEMU YA 1

Ni asubuhi na mapema ndani ya mji wa Mafinga uliopo mkoani Iringa, Tanzania. Baridi likiwa kali sana. Watu walikuwa wanatembea mitaani huku wakiwa wamevaa makoti makubwa kupambana na baridi hiyo.

Katika hoteli moja iliyopo katika mtaa wa Pipeline ndani ya mji huo kulikuwa na kikao cha siri cha watu wawili. Saa tatu sasa walikuwa wanapanga mikakati yao.

"Sasa Martin fanya juu chini umpate Elizabeth Neville, ni yeye pekee ndio anajua kila kitu kuhusu mimi, na nina hakika endapo atathubutu tu kusema basi nimeangamia na ndoto yangu ya kuja kuwa rais wa Tanzania itakuwa imefikia kikomo." Lucas alisema kwa sauti ya upole na kusisitiza.

"Usiwe na hofu yoyote Mheshimiwa Lucas. Mimi ndiye Martin, sijawahi kushindwa kazi yoyote ile.

Ukiwa na tatizo lolote lile jua lifikapo kwa Martin limekwisha. Nipe siku tatu tu nitakuletea Elizabeth Neville mikononi mwako na utaamua mwenyewe nini cha kumfanya. Nakuhakikishia siri yako haitotoka katika mdomo wa Elizabeth Neville kwenda katika sikio lolote lile lingine hapa duniani." Martin alisema kwa kujiamini.

"Nakuamini Martin Hisia. Sasa nakupa hizi milioni kumi za awali, na nitakupa milioni kumi na tano baada ya kukamilisha kazi hii. So milioni ishirini na tano ulizozihitaji zitakuwa zimekamilika" Lucas alisema huku akimkabidhi Martin bahasha yenye milioni kumi. Martin alizipokea, wakaagana

"Huyo Elizabeth Neville atakuwa anaijua siri gani ya waziri?. Maana kumpeleka kwake hiko kiumbe dhaifu tu katoa milioni ishirini na tano. Nitaifanya kazi hii siku mbili tu ili animalizie milioni zangu kumi na tano nilale mbele." Martin aliwaza akiwa ndani ya gari yake.

"Namwamini sana Martin atakamilisha hili kwa ufanisi mkubwa. Jamaa anaonesha yupo makini sana kazini. Huu ndio utakuwa mwisho wa Elizabeth Neville na marecord yake, na safari ya kuelekea ikulu itakuwa nyeupee" Lucas alikuwa anawaza.

Martin alirejea katika nyumba yake iliyokuwa katika mtaa wa Pareto. Alipiga honi na mlinzi wake alifungua geti. Baada ya kushuka garini alimsalimia mlinzi wake na moja kwa moja aliingia ndani. Alienda katika chumba chake anachotunza zana zake za kazi, akachukua bastola yake pekee na kuiweka kiunoni vizuri akiifunikia na shati.

"Sihitaji kubeba zana nyingi, hii ni kazi ndogo ingawa malipo yake ni makubwa sana" Martin aliwaza.

Alitoka nje na kuondoka na gari yake ndogo aina ya Toyota vitz. Naenda kumchukua Elizabeth Neville, akijifanya mjuaji naitoa roho yake mara moja. "

Dakika ishirini baadae ilimkuta Martin mbele ya nyumba akiyoishi Elizabeth Neville. Nyumba kubwa na nzuri iliyokuwa katika mtaa wa Kinyanambo.

"Bila shaka hii ndio nyumba ya Elizabeth Neville" Martin alisema wakati akishuka garini.
 
SEHMU YA 2

Alifika getini na kugonga hodi. Alisikia kishindo cha mtu akielekea getini. Martin alikaa tayari kwa lolote. Mara alisikia kelele za mlango ukifungulia. Geti likafunguliwa. Alikuwa anatazamana na mama wa makamo.

"Bila shaka atakuwa mama yake Elizabeth Neville" Aliwaza.

"Shikamoo mama" Martin alisalimia.

"Marhaba mwanangu sijui nikusaidie nini?"

"Nimekuja kumuulizia Elizabeth Neville. Ni rafiki yangu tulisoma shule moja, ila tumepotezana siku nyingi sana kwakuwa mimi nilienda kusoma nje ya nchi" Martin alidanganya.

"Kwani hujasikia yaliyompata Elizabeth Neville? Labda kwa kuwa ulikuwa nje ya nchi muda mrefu."

"Kimempata kitu gani Elizabeth Neville?" Martin aliuliza akiwa na wasiwasi.

Yule mama alianza kulia. Aliivuta kanga yake na kufutia machozi.

"Mwanangu Elizabeth Neville ametekwa mwezi wa pili sasa?"

"Ametekwa? Ilikuaje? Ametekwa na nani?" Martin aliporomosha maswali mfululizo.

"Ingia ndani mwanangu nikuelezee, si vyema kuongelea haya mambo hapa getini"

Martin na yule mama waliingia ndani. Walikaa katika sofa zilizoruhusu waangaliane.

"Elizabeth Neville alitekwa hapo nje. Ilikuwa mida ya saa moja hivi. Elizabeth alikuwa anaenda katika sherehe ya harusi ya rafiki yake, nilimsindikiza hadi pale getini, wakati tunaagana ghafla zilitokea gari mbili nyeusi na kufunga breki miguuni mwetu, walimvuta kwa nguvu Elizabeth na kumtia ndani ya gari na kuondoka nae. Ni mwezi wa mbili sasa tangu tukio lile baya kutokea" Yule mama alisema huku machozi yakimtoka.

"Daah pole sana mama, kwani ulikuwa na mahusiano gani na Eliza?" Akauliza.

"Eliza ni mwanangu wa mwisho. Katika maisha yangu nimejaaliwa kupata watoto wawili tu, Elizabeth na kaka yake Moses" Mama Elizabeth alijibu.

"Huyo Moses anaishi hapa naye?" Martin akauliza.

"Hapana. Moses anafanya kazi Mbeya. Ameoa na anaishi na familia yake huko."

"Je tukio la kutekwa rafiki yangu mliripoti polisi, na walisemaje? " Martin aliuliza.

"Tuliripoti, na kila siku wanasema bado wanaendelea na uchunguzi. Mwezi wa pili huu sasa"

Daah pole sana mama. Kama nilivyokueleza naitwa Peter. Ni rafiki mkubwa wa Elizabeth Neville. Na nakuahidi nitakusaidia katika msako wa kumsaka hadi apatikane. Naomba sana ushirikiano wako mama" Martin alidanganya.

"Karibu hapa muda wowote ule, nitakusaidia chochote kile kuhakisha Elizabeth anarudi na waliofanya huo mchezo mchafu wanakamatwa na kuozea jela" mama Elizabeth alisema kwa uchungu.

Walibadilishana namba za simu kwa ajili ya mawasiliano. Martin alitoka nje akisindikizwa na mama Elizabeth. Aliingia katika gari yake na kuondoka.

"It can't be serious!!! Elizabeth Neville was kidnapped? Nani aliyetuwahi huyo?"

Martin alitoa simu yake na kumpigia Lucas.

"Haloo Martin, vipi umefanikiwa kumpata Elizabeth Neville?"

"Hapana Mheshimiwa, Elizabeth ametekwa!"

"Whaaaat!!!" Lucas aling'aka simuni.
 
SEHEMU YA 3

"Ndo hivyo Mheshimiwa. Nimeenda nyumbani kwake Kinyanambo na kukutana na mama yake mzazi Elizabeth. Amenambia tukio hilo limetokea miezi miwili iliyopita. Elizabeth ametekwa mbele ya macho yake akimsindikiza kwenda katika harusi ya rafiki yake. Gari mbili nyeusi ndizo zilizombeba Eliza"

"Oooh my God, this is very dangerous to me. Ni nani hao waliomteka Elizabeth Neville? Kwa lengo gani?"

"Tutajua Mheshimiwa. Kwakuwa hii kazi umenipa mimi hakuna litakaloshindana. Elizabeth atarudi mikononi mwako, ingawa sio kwa malipo yake tuliyokubaliana awali"

"Pesa kwangu si tatizo. Nitakupa kiasi chochote kile cha pesa ilimradi tumpate Elizabeth. Yeye ndio kikwazo pekee katika safari yangu ya kuelekea ikulu. Lazima tumpate Elizabeth" Lucas alisema.

"Nitakupigia Mheshimiwa...." Martin alisema huku akikata simu baada ya kuona taa nyekundu katika saa yake aliyoivaa katika mkono wake wa kushoto inawaka. Akanyoosha mkono na kuupeleka sikioni kwake.

Aliisikiliza ile saa.

"....kama nilivyokwambia Felix. Kuna jamaa amekuja hapa leo kumuulizia Elizabeth. Amesema ni rafiki yake walisoma shule moja zamani na baadaye yeye akaenda nje ya nchi..." Kukawa kimya. Baadaye mama Elizabeth akaongea tena.

"He is lying. Elizabeth amesoma shule ya wanawake watupu tangu nursery. Yeye kasoma nae wapi?, na ilihal Elizabeth hajafika chuo"

Kukawa kimya tena. Mama Elizabeth akaongea tena.

"Nimeweza kumpiga picha nitakutumia baada ya muda mfupi" Kisha saa ya Martin ikazima ile taa nyekundu.

"Kuna mchezo nachezewa. Mama Elizabeth anawajua waliomteka mwanae. Hanijui mimi ni nani? Kile kifaa nilichoweka pale kwenye sofa kitanisaidia sana kujua watu atakaongea nao akiwa pale ukumbini. Nitarudi tena usiku katika ile nyumba" Martin alijisemea.

Martin alifika nyumbani kwake Pareto. Alijitupa katika sofa.

"Kazi imeanzaa! Kwa mara nyingine hisia zangu zimefanya kazi, nilijua tu yule mama kuna kitu ananificha. Kumbe anafahamu mahali alipo Elizabeth!!! Tutaonana usiku atatapika kila kitu." Alisema kwa sauti kuu huku akigonga mkono wake mezani.

Dakika tatu baadae mama Elizabeth alimtumia picha Felix kupitia mtandao wa kijamii wa WhatsApp. Harakaharaka Felix aliifungua simu yake na kuiangalia ile picha. Alipoiona sura ilimbadilika. Uso wake uliloa jasho.

"Ni Martin!!! Martin Hisia again!!! Martin anatafuta nini kwa Elizabeth Neville? Itakuwa ametumwa na nani?" Felix alijiuliza mwenyewe, hakupata jibu.

"Leo lazima tumbane Elizabeth ili atueleze kila kitu. Baada ya kutuambia tu lazima tumuue. Ashakuwa ni mtu hatari sana katika harakati za kuipata 001. Lazima afe yeye na mama yake baada ya kutueleza wapi ilipo 001" Felix alisema.
 
SEHEMU YA 4

Felix alitoka pale sebuleni na moja kwa moja alienda katika chumba alichofungiwa Elizabeth Neville. Akiwa amefungwa mikono na miguu Elizabeth alimwangalia mtu aliyeingia mle ndani. Alipoiona tu sura ya Felix alianza kulia.

"Mrembo Elizabeth Neville. Nitakachokufanya leo hakika utajutia milele, kitakuwa ni kitu kibaya sana kuliko cha siku zote ulizokaa hapa. Kama hutaki kitokee nitakachokufanya naomba unambie wapi umeiweka 001. Ukisema hiyo siri ndio usalama, la sivyo your going to die today!!!" Felix alisema kwa hasira.

Elizabeth akiwa amejaa damu mwili mzima alimwangalia tu yule mwanaume kwa macho yasiyo na matumaini ya kuendelea kuishi.

"Sasa nakupa nusu saa, nitakuja tena humu ndani, na hapo ndipo utakijua cha mtema kuni kilichomtoa kanga manyoya" kwa hasira Felix alitoka nje. Akiwa sebuleni akapiga simu moja. Akaongea kwa dakika tano kisha akampigia mama Elizabeth. Naye akaongea nae bila kujua kwamba maongezi yao yanasikiwa na mtu wa tatu, alikuwa anaitwa Martin Hisia!!!.

***

Ni saa nane ya usiku. Baridi ilikuwa imechachamaa katika mji wa Mafinga. Mji umetulia hakuna watu watembeao. Katika njia ya kutoka Pareto kuelekea Kinyanambo kulikuwa na pikipiki itembeayo kwa kasi. Dakika kadhaa ilifika kinyanambo. Martin Hisia alishuka katika pikipiki. Alitumia dakika tatu kuizunguka nyumba ya Elizabeth Neville. Aligundua kwamba kuna walinzi wawili ambao hakuwaona alipoenda pale asubuhi.

"Nilimsikia akiomba msaada wa ulinzi kwa mtu aitwaye Felix. Ulinzi wenyewe ndo huu??. Ngoja nitafute namna ya kuingia ndani." Aliwaza Martin.

Martin aliruka ukuta kwa nyuma na kutua ndani ya uzio mpana. Mlinzi mmoja alikuwa amesimama mlangoni na mwengine alikuwa amesimama getini. Martin alianza kumnyemelea yule wa getini kwa nyuma akiambaa na ukuta. Alimkaribia. Akachomoa kitambaa mfukoni na kumziba nacho puani huku akiwa kamkaba kabali. Sekunde thelathini tu jamaa alilala. Sasa alimsogelea yule wa mlangoni. Martin alipiga mluzi, mlinzi aligeuka na ndio lilikuwa kosa lake. Alikutana na ngumi ya nguvu ya uso iliyomtupa chini. Martin alimfata kwa kasi na kumkandamiza shingoni kwa kutumia goti lake. Jamaa nae akapoteza fahamu. Akaenda mlangoni, akatoa funguo moja, aliutekenya ule mlango ukafunguka. Kabla hajaingia akafunika sura yake kwa kitambaa cheusi. Sasa alionekana macho tu. Aliingia ndani. Alifika kwenye sebule ambayo aliyofika asubuhi ya siku ile. Kulikuwa na giza totoro. Alichunguza kwa haraka. Akaona kitaa kidogo hafifu juu ya dari kikiwaka na kuzima.

"Camera, wameweka camera?" Aliwaza. " Kuna siri gani juu ya Elizabeth Neville kiasi kuweka hali ya ulinzi namna hii?" Martin alijuliza huku akielekea mbele.

"Bila shaka huku ndiko vilipo vyumba, nitatambua tu nini kinachoendelea" Alisema huku bastola yake ikiwa imetangulia mbele. Alikuwa anatembea kwa kunyata hakurusu kabisa miguu yake itoe sauti ya namna yoyote. Alifika katika mlango ambao alihisi ndicho chumba cha mama Elizabeth.
 
SEHEMU YA 5

Alitumia funguo uleule kufungua. Sasa alikuwa chumbani. Kwa tahadhari kubwa alitumia macho yake kukichunguza kile chumba. Hakuona kitu. Alipiga hatua mbele.

"Simama hivyohivyo!!" Alisikia sauti nyuma yake. "Ukipiga hatua moja tu mbele nakipasua kichwa chako!!" Jamaa alipiga mkwara.

Martin aliganda, hakuamini kilichotokea.

"Tupa bastola yako chini kisha nyoosha mikono juu!!" Sauti iliamrisha.

Martin aliidondosha bastola chini. Moyoni akitafuta mbinu ya kujitoa.

"Ipige teke bastola yako mbele kuelekea uvunguni!!" Sauti iliamrisha tena.

"Siwezi fanya kila anachoniamrisha. Ngoja nimuoneshe mimi ni nani?"

Martin alifanya kama anataka kuipiga teke ile bastola. Haikuwa hivyo. Martin aliibetua ile bastola mithili ya mpira ikaruka juu. Kisha kwa kasi ileile alijilaza chini huku akijigeuza. Bastola yake ilitua mikononi mwake na kutoa risasi zilizoichakaza vibaya sana miguu yote miwili ya yule jamaa. Jamaa alitoa ukelele wa maumivu huku akiitupa chini bastola yake.

"Sasa ni zamu yako kuamrishwa. Utajibu maswali yangu yote" Martin alisema kwa mbwembwe huku akisimama wima.

Martin alienda karibu na mlango na kuwasha taa. Alikuwa anatazamana na damu nyingi chini huku jamaa akigalagala katika dimbwi la damu. Alimsogelea yule jamaa na kumsachi. Alimkuta na kitambulisho pekee ambacho alikitia mfukoni. Akaichukua na bastola yake na kuendelea kufanya upekuzi katika kile chumba. Hakuna chochote cha maana alichokipata. Alikuwa amechelewa. Kile chumba kilikuwa kimeshapekuliwa.

"Huyu jamaa ndio atanipa mwongozo wa mahali alipo Elizabeth Neville". Aliwaza.

Akarudi kwa yule jamaa. Alikuwa bado anagugumia pale chini kwa maumivu.

" Hawezi kusema chochote akiwa katika hali hii. Yapasa nimchukue huyu nikamhojie nyumbani"

Alijishauri.

Alitoa kichupa fulani mfukoni kwake na kumwagia katika majeraha miguuni. Damu yote ilikata. Alimzoa yule mtu hadi nje. Akamfunga kama furushi nyuma ya pikipiki yake na kuelekea nae nyumbani kwake Pareto. Hadi anakamilisha misheni ile ndogo ilikuwa ni saa nane usiku. Bado mji wa Mafinga ulikuwa kimya hivyo hakupata shida kufika nae kwake. Alipiga honi getini na mlinzi wake alimfungulia. Mlinzi hakuwa na haja ya kuchunguza Martin amebeba nini maana alimjua Martin ni nani?. Alipofika karibu na mlango alimfungua kule nyuma ya pikipiki na kumuingiza ndani. Akamwingiza ndani na kwenda kumtupia katika chumba kimoja wapo katika nyumba yake. Kisha akarudi sebuleni. Akajisachi mfukoni na kutoa kitambulisho cha yule jamaa na kukisoma. Kilikuwa ni kitambulisho cha mwanamke aitwaye Bertha Fidelis. Sehemu akiyofanyia kazi huyo Bertha ilikuwa ni katika mgodi wa dhahabu Geita. Na picha ya huyo Bertha ilikuwa pembeni upande wa kushoto wa kitambulisho. Akakirudisha mfukoni kile kitambulisho.

"Ngoja niende sasa nikamtapishe kila kitu yule jamaa. Lazima nijue yeye ni nani? Na ametumwa na nani?
 
SEHEMU YA 6

Pia anambie Elizabeth Neville yu wapi? Nina hakika atasema tu, akijifanya mbishi nitamfanya kitu ambacho hajawahi kuwaza kufanywa katika maisha yake. Atamjua Martin Hisia" Martin alikuwa anawaza huku akielekea kule chumbani.

***





Ngoja niende sasa nikamtapishe kila kitu yule jamaa. Lazima nijue yeye ni nani? Na ametumwa na nani? Pia anambie Elizabeth Neville yu wapi? Nina hakika atasema tu, akijifanya mbishi nitamfanya kitu ambacho hajawahi kuwaza kufanywa katika maisha yake. Atamjua Martin Hisia" Martin alikuwa anawaza huku akielekea kule chumbani.

***

Kumekucha. Ni saa kumi na mbili asubuhi ndani ya jiji la Dar es salaam. Pilikapilika ndani ya jiji hilo maarufu zaidi nchini Tanzania zilikuwa zimeshamili kama ilivyo ada ya jiji hilo.

Ndani ya ukumbi wa mikutano katika ikulu ya Dar es salaam kulikuwa na kikao cha dharura. Watu wote waliokuwa ndani ya kikao hiko walitumiwa meseji saa nane usiku. Na wote kasoro mtu mmoja tu ndiye aliyekuwa hajafika ikulu saa kumi na mbili asubuhi.

Kulikuwa na rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dr Joseph Mgaya. Kulikuwa na waziri mkuu wa kwanza wa kike Mheshimiwa Dr Jeska Mlamka. Kulikuwa na mkuu wa majeshi Jenerali Selemani Kazi. Mkuu wa jeshi la Polisi John Rondo na mkuu wa ulinzi na usalama wa Taifa Christopher Mangwina. Kilikuwa kikao cha dharura na muhimu sana. Makamu wa rais pekee ndiye hakuhudhuria katika kikao hiko kwakuwa alikuwa katika mkutano wa umoja wa Afrika nchini Addis Ababa nchini Ethiopia.

"...wajumbe nimewaita kwa haraka sana hapa kwakuwa kuna tatizo kubwa sana limetokea hapa nchini" Mheshimiwa rais Dr Joseph Mgaya alianza kuwaeleza wajumbe wake baada ya salaam. Wote walikuwa kimya kutaka kusikia juu ya wito ule wa ghafla wa rais ya jamhuri wa Muungano wa Tanzania.

"...sijui hata nianzie wapi kuwaelezea juu ya mkasa huu mzito uliotokea nchini kwetu. Ngoja niende moja kwa moja kwenye mada maana hatuna muda mrefu wa kukaa hapa" Rais alichukua chupa ya maji na kupiga funda dogo.

"... umetokea wizi mkubwa sana wa madini katika mgodi wetu wa huko Geita" Rais Dr Joseph alitulia ili sentensi ile itue katika ubongo wa wajumbe wake. Aliendelea " Tani mbili za dhahabu zimeibiwa katika ghala la Serikali kule Geita!!"

Wajumbe wote walistuka. Ulikuwa ni wizi mkubwa tofauti kabisa na walivyofikiria.

"Tani mbili? It can't be serious!! Inawezekana vipi dhahabu kiasi kikubwa hivyo kuporwa? Lini? Na kwanini vyombo vya usalama hatuna taarifa? We umejuaje Mheshimiwa rais?" Mkuu wa jeshi la Polisi IGP John Rondo aliuliza maswali mfululizo.
 
SEHEMU YA 7

"Ndio Bwana Rondo. Ni tani mbili za dhahabu zimeibwa. Habari ya kuibiwa kwa dhahabu hizo nililetewa na msichana mmoja anayeitwa Bertha Fidelis.

Wiki iliyopita walinzi wangu walinambia kuna mgeni toka Geita anataka kuonana na mimi. Nikawaambia wamruhusu. Aliingia msichana wa makamo mwenye mvuto mkubwa. Alijitambulisha kuwa anaitwa Bertha Fidelis kutoka mgodini Geita. Yeye ni katibu mahsusi wetu kule. Kubwa lililomleta alinambia kuna watu wamepanga njama za kuiba dhahabu katika ghala letu. Na watu hao wanamsaka yeye hivi sasa ili wamuue baada ya kugundua kwamba amegundua njama zao. Kikubwa aliomba tuhakikishe tunadhibiti wizi wa dhahabu na kumhakikishia yeye usalama wake. Nilimuahidi kutekeleza yote mawili. Moja kwa moja niliwasiliana na waziri wa ulinzi na kumpa taarifa hizo, akanambia atawasiliana na IGP ili kudhibiti hali hiyo. Cha kushangaza jana usiku nimetumiwa taarifa toka kwa meneja wetu kule Geita kuwa kuna kiasi kikubwa cha dhahabu kimeibiwa katika ghala letu. Nilistuka sana.." Rais Dr Joseph alikaa kimya huku akiwaangalia watu wale wanne. Aliridhika na umakini wao akaendelea kuongea.

"Vipi suala la ulinzi kwa Bertha lilifanyiwa kazi?" Dr Jeska aliuliza.

"Kwa mujibu wa mheshimiwa Lucas, Bertha alipewa ulinzi. Lakini cha kushangaza jana usiku nilipigiwa simu na watu wasiojulikana wakinitaka niachane kabisa na suala la wizi wa dhahabu Geita. Huku salamu zao wakitishia kuanza kumuua Bertha endapo sitotii kwakuwa yupo mikononi kwao"

"This is too much. Sijawahi kuona mahali popote pale duniani, rais kutishiwa na wahalifu walioliibia taifa? Its impossible!!" Mkuu wa majeshi jenerali Selemani Kazi alisema kwa hasira.

"Bila shaka Bertha wanae mikononi mwao. Ili kujua kiini cha tatizo hili ni kumpata Bertha ili tujue yeye habari hiyo ya wizi ameitoa..." Mkuu wa usalama wa Taifa alikuwa anaongea na rais alimkatisha.

"....Bertha alinambia kila kitu..alinambia kuna mwanamke mmoja anayeitwa Elizabeth Neville ndiye aliyemwambia juu ya kutokea wizi huo mkubwa wa dhahabu."

"Elizabeth Neville!!" Waziri mkuu alisema kwa nguvu. Who is she? Kwa mara nyingine tena wiki hii ninalisikia hili jina la huyu mwanamke. Yeye ni nani mpaka kuweza kunusa harufu ya wizi wa dhahabu kabla haujatokea?" Dr Jeska aliporomosha maswali mfululizo.

"Wiki hii umelisikia jina la huyo Elizabeth Neville? Umelisikiaje Dr Jeska?" Rais aliuliza.

"Siku ya jumatatu niliwahi sana kufika kazini. Nilikuwa na kazi nyingi za kufanya zilizoniamuru saa kumi na moja alfajiri niwe katika kiti changu ofisini." Waziri mkuu alianza kuelezea. Ukimya ulitawala ofisini kumsikiliza yeye.

" Robo saa tu baada ya kupitia mafaili kadhaa yaliyokuwepo pale mezani kuna karatasi ilidondoka chini.
 
SEHEMU YA 8

Nikaikota nikijua ni moja ya karatasi iliyochomoka tu katika mafaili nikiyoyashughulikia. Niliitazama na kuisoma ili kufahamu ile karatasi imetoka katika karatasi gani? Karatasi ilikuwa imeandikwa majina mawili tu, Elizabeth Neville. Nilikaa na kutafakari sana. Elizabeth Neville ni nani? Na kwanini jina lake liandikwe katika karatasi na kuwekwa juu ya meza yangu. Niliwaza sana lakini baadae niliamua kuachana na mawazo nayo na kuendelea na kazi. Hadi leo sikujishughulisha tena kuhusu Elizabeth Neville hadi leo nilipokusikia wewe ukisema ndiye aliyemwambia Bertha kuhusu wizi wa dhahabu Geita." Waziri mkuu alimaliza.

"Inashangaza sana. Ni kweli wizi wa dhahabu umetokea Geita" Mkurugenzi wa usalama wa Taifa alianza kueleza. "Ni wizi mkubwa sana mana matrilioni ya pesa yamepotea. Lakini naona tuna njia ya kutufikisha kwa wezi wa madini yetu.

" Ni njia gani hiyo?" Rais Joseph aliuliza.

"Ni Elizabeth Neville!! Lazima tumtafute mtu mwenye jina hilo na yeye ndio atatueleza alizipata wapi taarifa za kutokea wizi wa dhahabu. Suala hili niachieni mimi. Nitatuma vijana wangu na jioni tunaweza kukutana hapa tukiwa tunamfahamu vizuri Elizabeth Neville. Na inawezekana tukawa nae katika kikao kijacho." Christopher Mangwina alisema akijiamini.

Maongezi katika kikao yaliendelea kwa nusu saa huku wakikubaliana kukutana tena saa moja usiku wakiwa na taarifa kuhusu Elizabeth Neville na wizi wa dhahabu Geita.

"Elizabeth Neville mwisho wako umefika. Utairejesha tu 001" Dr Joseph aliwaza peke yake.

***

Kwa mwendo wa taratibu Martin alielekea katika chumba alichomfungia yule jamaa. Moyoni mwake alikuwa amepania hasa kumtesa yule jamaa ili amweleze kila kitu.

"Lazima anieleze yeye ni nani? na ametumwa na nani? Kwanini wamteke Elizabeth Neville?" Martin alikuwa anawaza akiwa katika shoroba ndefu kuelekea katika chumba alichomweka mateka wake.

Alifungua mlango taratibu.

Alipigwa na butwaa!

Mbele yake alikuwa anatazamana na mwili uliolala wa yule jamaa ukiwa hauna uhai. Alimsogelea taratibu na kumwangalia vizuri. Jamaa alikuwa amepigwa risasi ya utosi na kupoteza maisha!!

Harakaharaka Martin alitoa bastola yake kiunoni na kuanza kuikagua nyumba yake. Kumtafuta muuaji. Hakukuwa na lolote la hatari. Utulivu wa nyumba yake Ulikuwa uleule aliouzoea siku zote. Alielekea getini. Katika kichumba kidogo anacholala mlinzi alimshuhudia mlinzi wake naye akiwa amelala katika dimbwi la damu sakafuni!!!

"Nani kafanya unyama huu? Kwa muda gani? Inaonesha alikuja kuuwa tu na kutokomea. Ona sasa nimeshaingia katika operesheni nyingine ya hatari. Mwanzoni nilidhani ni ishu ndogo tu ya kumsaka Elizabeth Neville na kumkabidhi kwa Mheshimiwa Lucas, na kama angegoma maagizo yalikuwa ni kumuua. Sasa mambo yamekuwa tofauti."

Martin alirudi ndani kwake. Moja kwa moja akaenda katika chumba cha mwisho upande wa kushoto. Aliingia na kukaa juu ya kiti huku akitazamana na kompyuta.
 
SEHEMU YA 9

Alibofyabofya kama dakika moja. Akaseti kwamba anataka kuyaona matukio yaliyotokea nusu saa iliyopita. Camera alizozitega zilimuuonesha kila kitu. Alijiona yeye akiingia akiwa na pikipiki akiwa amembeba yule jamaa na kufunguliwa geti na mlinzi. Dakika mbili baadae ilimuonesha mtu akiwa anaruka ukuta kwa nyuma. Alimwangalia kwa umakini. Martin alistaajabu. Hakuwahi kuyaona haya anayoyaona leo hata siku moja katika maisha yake. Yule mwanaume akiyenyata kuelekea getini alikuwa uchi, uchi wa mnyama!!

Jamaa aliingia kwa kustukiza kibandani mithili ya jini na kumchalaza risasi kadhaa mlinzi wake kwa kutumia bastola yenye kiwambo cha kuzuia sauti.

Baada ya kuhakikisha jamaa amekufa alielekea nyuma ya nyumba ile. Alimuona akitoa kitu mguuni, ulikuwa funguo wa bandia uliomsaidia kufungua ule mlango wa uwani. Kimyakimya aliingia ndani na kuelekea katika chumba alichomlaza yule mateka wake. Hakumhoji kitu chochote kile. Alimcharaza risasi kisha kutokomea katika njia ileile aliyojia.

Martin alijifuta jacho. "Huyu jamaa ni professional killer!! Jinsi atembeavyo, jinsi anavyoishika bastola na kuitumia inaonesha si mtu wa kawaida. Ni nani huyu? Halafu anavaa viatu tu bila nguo yoyote. Na amejuaje kama nilimweka katika chumba kile? Maana kaenda moja kwa moja ishara kwamba alikuwa anajua kama nimemweka mle. Hii vita ya kumsaka Elizabeth Neville si ya kitoto kama nilivyoifikiria"

Akarudia tena kuiangalia ile video. Akagandisha picha ya yule jamaa. Akaivuta na kuiangalia vizuri kwa dakika kumi. Akaiprint ile picha na kuitia mfukoni. Akatoka katika kile chumba na kumpigia Mheshimiwa Lucas.

"Hallo Martin.. Nambie kijana wangu" Lucas alisema baada tu ya kupokea simu.

"Uko wapi kwa sasa Mheshimiwa, kuna mambo nayahitaji kuhusu ile kazi uliyonipa" Martin alisema.

"Kwa sasa nipo Dar es salaam. Lakini naweza kukupatia chochote ukitakacho. Nakusikiliza kijana ipi shida yako?" Lucas aliuliza.

"Nahitaji nyumba nyingine ya kuishi kwa muda hapa Mafinga. Kwa sasa nyumba yangu si sehemu salama hata kidogo maana maadui wameshapafahamu. Pia nahitaji pesa kwa ajili ya hii kazi"

"Usihofu. Kuhusu suala nyumba nitakupigia baada ya nusu saa. Pesa nitakuingizia kwenye akaunti yako ya benki. Ilikuwa unahitaji shilingi ngapi?"

"Kwa sasa nihitaji kama milioni ishirini hivi" Martin alisema.

" Ok haina shida kijana. Ukachungulie katika akaunti yako baada ya dakika kumi na tano. Vipi maendeleo ya kazi yetu?"

"Kazi bado ngumu. Jana nilikwambia juu ya ile simu aliyopiga mama Elizabeth kumpigia mtu fulani. Usiku nilienda katika nyumba ya mama Elizabeth kupeleleza. Ilikuwa ni kazi ndogo lakini yenye hatari tofauti kabisa na nikivyofikiria. Nilifanikiwa kumteka jamaa mmoja baada ya kumdhibiti alipotaka kuniua" Martin alisema.

"Good job. Vipi kuhusu mama Elizabeth? Na umepata lolote toka kwa huyo jamaa juu ya mahali alipo Elizabeth Neville? Lucas aliuliza.
 
SEHEMU YA 10

" mama Elizabeth sikumkuta. Lakini yule mtu nilimbeba hadi nyumbani. Wakati nikitafakari jinsi ya kufanya kuna mtu aliingia kwa kuruka ukuta na kufanikiwa kumuua yule jamaa. Inavyoonesha yule jamaa alikuwa na siri ambayo hawakutaka aniambie. Sasa washakujua nyumbani kwangu. Ndio maana nataka nihame hapa si sehemu salama tena kwangu" Martin alisema.

"Sawa Martin nimekuelewa. Unafanya kazi nzuri sana. Na hakika kwa juhudi zako tutafahamu mahali alipo Elizabeth Neville."

"Ni kweli Mheshimiwa. Lakini nina swali kidogo. Who is Elizabeth Neville? Na ana siri gani aijuayo juu yako?" Martin aliuliza.

Alimsikia Mheshimiwa Lucas akivuta pumzi ndefu simuni.

"Nambie Mheshimiwa. Itanipa mwanga katika harakati za kumsaka Elizabeth Neville. Wewe na mimi ni kitu kimoja sasa, lazima nijue ukweli juu ya misheni hii ili nijue nijiandae vipi. Maana nimeanza kuona vitu vigeni sana" Martin alisema.

"Elizabeth Neville..." Lucas alisema kwa hisia. "Mwanamke wa ajabu aliyeingia kiajabu katika maisha yangu" Mheshimiwa Lucas alisema.

Mheshimiwa Lucas alianza kumsimulia Martin Hisia habari kuhusu miaka minne nyuma kilichotokea jijini Dar es salaam.

***

Ulikuwa usiku wa saa nne usiku katika baa maarufu ya Hongera iliyokuwa maeneo ya Sinza Bamaga jijini Dar es salaam. Muda huo ndani ya baa kulikuwa na watu wengi sana wakioshuhudia promosheni ya bia ya Kilimanjaro ikiyoendelea. Ndani ya ummati huo alikuwepo Lucas, mgombea ubunge wa jimbo la Ubungo kupitia chama cha LID. Lucas alikuwepo mahali pale kwa lengo moja tu, kumsaka dada mmoja aitwaye Jane Munuo. Ni mwaka sasa alikuwa anamsaka Jane hadi hivi juzi alipopata fununu kwamba Jane alikuwa mhudumu katika baa hiyo ya Hongera. Lucas alikuwa amekaa katika meza mojawapo huku macho yake yakiwa hayatulii yakimsaka Jane.

"Ili nipite kiurahisi lazima nimsake Jane na kumuua!! Ni yeye pekee ndiye aijuayo uhusuka wangu kuhusu 001, na ikisambaa siri hiyo lazima itaondoa taswira yangu nzuri kwa wapiga kura wa jimbo la Ubungo. Nina ndoto kubwa katika siasa na ili ndoto yangu itimie lazima niondoe magugu yote njiani. Njia lazima iwe nyeupe ya mimi kuelekea..." Lucas aliacha kuwaza ghafla. Juu ya jukwaa la promosheni alikuwa amepanda mwanamke aliyekuwa anamsaka, alikuwa Jane Munuo.

"Jane, bado yupo vilevile kama nilivyomwacha miaka miwili nyuma. Habadiliki huyu mwanamke. Leo ni mwisho wake" Lucas alisema huku akisimama. Akajipapasa upande wa kushoto wa kiuno chake, aliigusa bastola yake. "I'm going to kill this lady today!! Nitafukia kila kitu akijuacho kuhusu mimi. Si anajifanya ana ushahidi? Sasa ataupeleka kuzimu huo ushahidi!!"

Alimwona jinsi Jane akicheza kule juu. " its your last dance!!" Alisema huku akipiga hatua kuelekea kule mbele. Alijichanganya kwenye kundi la watu waliokuwa wakishangilia kwa shangwe show ikiyotolewa na Jane. Hakuna aliyekuwa makini na mwenzake, wote walitekwa na viuno vya Jane.
 
SEHEMU YA 11

Taratibu na kwa siri kubwa aliichomoa bastola yake na kuifyatua ikielekea kule mbele. Ilimpata!! Jane alirushwa na kudondoka chini. Bastola ilikuwa imemnasa bara'bara katika paji lake la uso.

Watu walianza kutawanyika kwa fujo huku wakimwacha Jane akipigania maisha yake. Lucas nae alijichanganya kwenye ummati wa watu waliotawanyika hovyo na kupata nafasi ya kuelekea katika gari lake na kutokomea, akiamini hakuna anayejua alichokuwa amekifanya.





Watu walianza kutawanyika kwa fujo huku wakimwacha Jane akipigania maisha yake. Lucas nae alijichanganya kwenye ummati wa watu waliotawanyika hovyo na kupata nafasi ya kuelekea katika gari lake na kutokomea, akiamini hakuna anayejua alichokuwa amekifanya.

***

Zulfa Hussein alikuwa ni mwandishi wa kike katika gazeti la udaku la Ngamizi. Gazeti bora kabisa katika kuandika habari za watu maarufu na kufichua habari zisizojulikana za watu maarufu.

Siku hiyo ya jumapili naye alikuwepo katika baa ya Hongera, akisaka umbeya juu ya watu maarufu. Ndipo macho yake yalipomuona mgombea ubunge mtarajiwa wa jimbo la Ubungo. Camera yake ya siri yenye uwezo wa kurekodi video ikawa kwa Lucas ili kuona kama kuna chochote atakipata cha ajabu toka kwa Mheshimiwa huyo. Zulfa aliushuhudia mstuko katika sura ya Lucas alipomuona dada mmoja akiwa amepanda kule juu. Zulfa akawa makini huku akiweka upande wa video na kurekodi kila kitu. Alijua ile ni habari. Alimshuhudia Lucas akiinuka na kujichanganya katika kundi la watu lililopagawa na burudani. Alimwona jinsi alivyoitoa bastola yake na kumpiga yule dada kule juu. Matukio yote hayo aliyarekodi vizuri sana.

"Nimemmaliza!!! Risasi ya utosi hawezi kupumua tena. Sasa ni muda wa kwenda kule nyumbani kwake na kuitafuta 001, nikiipata nitakuwa salama. Ndoto yangu ya kuwa mbunge na hatimaye rais itakuwa inaenda kukamilika" Aliwaza Lucas akikata kona upande wa kushoto Sinza Kijiweni kuelekea Tandale mahali alipoelekezwa kwamba Jane Munuo alikuwa anaishi.

Zulfa Iddi alichanganyikiwa sana. Hakuamini kabisa kama alikuwa ameshuhudia mauaji yale na kumshuhudia moja kwa moja muuaji usiku ule. Ilikuwa ni mara ya kwanza kwake kushuhudia jambo la kutisha tangu aingie katika tasnia ya habari miaka mitatu iliyopita. Alianza kutetemeka mwili pamoja kwamba jiji la Dar es salaam lilikuwa na joto isivyo kawaida. Moyoni mwake aliamini ni wengi sana walioshuhudia mauaji mbele ya jukwaa, lakini aliamini ni yeye pekee ndiye alimyemshuhudia muuaji na kumrekodi bila kutarajia. Alikuwa na siri, siri kubwa sana katika maisha yake.
 
SEHEMU YA 12

"Lucas ameua!!! Sasa nifanye nini mimi?. Ameua nina rekodi hii yenye kumuonesha akiua!! Kwanini nilimfatilia Lucas? Hii ishu itanidumbukiza katika dimbwi la matatizo. Yule mwanamke akiyocheza pale jukwaani ni nani? Na kwanini amuue? Nina woga mkuu moyoni, lakini lazima nisonge mbele kujua mengi zaidi yaliyojificha juu ya mauaji haya. La kwanza lazima nichunguze na kujua yule mwanamke ni nani?".

Akiwa katikati ya mawazo yenye maswali mfululizo ghafla simu yake ikaita. Akaitoa harakaharaka katika mfuko wa suruali yake ya jeans aliyokuwa ameivaa na huku akisogea pembeni sehemu kusipokuwa na pilikapilika za watu wakiokimbia. Alisimama mbele ya hoteli ya Atrium.

"Mhariri wa gazeti la Ngamizi" Alisema kwa sauti ndogo. Aliipokea simu na kuiweka sikioni.

"Haloo Alphonce Mnubi" Aliita Zulfa simuni kwa sauti iliyotulia.

"Kuna tukio limetokea Hongera baa sasa hivi, naomba uende haraka ili nasi tuliripoti katika gazeti letu kesho" Alphonce alisema harakaharaka.

"Nipo njiani Alphonce. Ila nami kuna tukio kubwa nimelipata kuhusu Lucas. Nitakuletea baada ya kutoka Hongera baa" Zulfa hakutaka kumwambia Alphonce kwamba alikuwa amepata kila kitu pale Hongera baa.

"Lucas yupi? Yule mgombea ubunge jimbo la Ubungo?" Alphonce aliuliza kwa shauku.

"Ndio, kwani kuna Lucas mwengine maarufu katika nchi hii zaidi ya Lucas Mohamed mgombea ubunge wa jimbo la Ubungo?. Kuna tukio baya sana amelifanya usiku huu na kwa bahati mbaya limenaswa na camera zangu. Nikitoka hongera baa moja kwa moja nitakuja ofisini. Amini kesho mauzo ya gazeti letu yatakuwa juu sana. Ni mimi pekee ndio mwenye habari hiyo" Zulfa alisema.

"Haina shida, fatilia ya Hongera baa kisha tutakuja kuyajumuisha yote kwa pamoja. Uwe hapa kabla ya saa saba usiku, mana saa saba kamili tunaanza kuchapa gazeti" Alphonce alisema.

"Sawa mkuu, nitakuwa hapo"

"Sijui kama nimefanya sahihi kumueleza Alphonce jambo hili. Aaah nahisi nimekosea. Kwanini sikufanya subra? Ningemchunguza kwa kina yule mwanamke kisha ndo ningeitoa gazeti. Lakini lipi sahihi, kwenda kuliweka katika kurasa ya mbele ya gazeti la Ngamizi ama kulipeleka suala hili katika vyombo vya ulinzi? Nahisi kuchanganyikiwa" Zulfa aliwaza peke yake akiwa kaishikia nguzo ya umeme. Uso wake ulikuwa umeloa jasho.

Kule kwa Alphone Mnubi, ilipokatika tu simu kutoka kwa Zulfa Iddi, mhariri Alphonce alipiga simu nyingine.

"Bila shaka naongea na Mheshimiwa Lucas?" Alphonce alianza kwa kuuliza swali mara tu simu yake ilipopokelewa.

"We ni nani? Nani mwenzangu?" Badala ya kujibu swali Lucas aliuliza swali kwa sauti iliyojaa uwoga.

"Unaongea na Alphonce Mnubi mhariri mkuu wa gazeti la Ngamizi. Bila shaka naongea na Mbunge mtarajiwa wa Ubungo" Alphonce alisema kwa sauti tulivu.
 
SEHEMU YA 13

"Ni kweli lakini mbona umepiga simu usiku sana ndugu mhariri? Ungesubiri asubuhi ndio unipigie kama unataka kujua harakati zangu za kuwania ubunge" Lucas alisema huku bado sauti yake ikiwa imejaa woga.

"Hapana, nimekupigia si kwa ajili ya kutaka kujua harakati zako za ubunge" Alphonce alisema. "Kuna tukio umelifanya leo usiku na limefika katika meza yetu ya uhariri hilo ndilo limenifanya nikupigie" Alipozi.

"Tukio? Tukio gani hilo mhariri? Tukio gani nimelifanya mimi? Kwanza wapi? Lini? Saa ngapi? " Maswali ya kubabaika yalimtoka Lucas.

"Sina haja ya kukwambia umelifanya wapi hilo tukio, ila lini nitakujibu ni leo usiku. Pia jua kwanza kila ulichokifanya kimerikodiwa kamera za gazeti la Ngamizi na ukijifanya mjuaji kitaanikwa katika gazeti la hilo kesho asubuhi na mapema, tena katika ukurasa wa mbele. Ila tunaweza tusiiweke habari hiyo kwa makubaliano maalum" Alphonce alisema kwa sauti yenye majigambo.

"Makubaliano? Makubaliano gani unayoyataka?" Lucas akajiingiza kwenye mkenge.

"Ndani ya dakika kumi na tano zijazo niikute milioni hamsini imeingia toka kwako katika akaunti yangu ambayo nitakutumia baada ya kukata simu hii. Ukifanya hivyo hii habari haitokuwepo katika ukurasa wa mbele wa gazeti la Ngamizi. Sharti la pili, kabla ya jua halijachomoza mwandishi wa habari, Zulfa awe ameuwawa!!!.

Hapo ndipo itakuwa salama yako Lucas. Tutakuwa tumemfunga mdomo Zulfa na tutadestroy all records kuhusu tukio lako" Alphonce alisema kwa kirefu.

"Kwanini sasa mwandishi Zulfa afe? Hilo la pesa halina tatizo kwangu, nitafanya kama ulivyoagiza. Ila nami nina ombi, sitaki uziharibu hizo records, nataka unikabidhi mimi mwenyewe" Lucas alisema.

"Hakuna tatizo kuhusu kukukabidhi hizo records. Hilo lawezekana Lucas. Na kuhusu Zulfa kufa ni muhimu sana, kwakuwa ni yeye ndiye alikurekodi wakati ukifanya tukio. Na endapo asipoiona hii habari ikichapwa katika gazeti la kesho litakuwa tatizo, lazima tumfumbe mdomo!" Alphonce alisema.

"Nimekuelewa ndugu yangu. Nashukuru sana kwa kunifahamisha jambo hili. Acha nitekeleze makubaliano yetu. Lucas alisema na kukata simu.

" Woooow! 50 millions in my account. Hahaha tukio lenyewe silifahamu but naingiza kiasi kikubwa sana cha pesa. Sijui ni tukio gani litakalokuwa Lucas kalifanya?. Kakubali masharti magumu kwa urahisi sana. Napaswa kujua? No only I need money!!! " Alphonce alikuwa anawaza peke yake.

Hakujua! Hakujua! Hakujua!!!!!!!

Nje ya mlango wa ofisi yake kulikuwa na mtu ambaye hakupaswa kusikia yake maongezi ya siri, lakini kwa bahati mbaya kabisa alisikia kila kitu kilichokuwa kinaongelewa mle ndani na Alphonce Mnubi. Mtu huyo alikuwa ni mwanamke mnene wastani, mweusi, nywele zake alikuwa amezikata ndogondogo katika mtindo wa ungaunga. Na kwa majina mwanamke huyo alikuwa anaitwa Elizabeth mtoto wa pili wa mzee Neville.

Naam Elizabeth Neville!!!!

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 14

***

"Nimekwisha!" Lucas alisema kwa nguvu na kuugonga usukani wake kwa mikono yake. "Zulfa kanirekodi saa ngapi? Mbona nilifanya mauaji kwa siri sana. Sasa siri yangu ipo hadharani nimekwisha. Sina jinsi itabidi nifanye kama Alphonce alivyoniagiza.

Milioni hamsini katika akaunti yake na mauaji juu. Nitafanya nini sasa? Kwa mara nyingine tena 001 inanipeleka katika matatizo. Kwanini Jane Munuo uliniibia 001 we mwanamke?. Ona sasa Jane unazidi kunipeleka katika mdomo wa mamba" Lucas alikuwa anawaza peke yake. Alisimama njiani badala ya kuelekea Tandale nyumbani kwa Jane Munuo. Mambo yalikuwa yameingiliana. Aliwaza na kuwazaua. Hakupata jibu.

"Martin!" Lucas aligutuka. "Kiumbe pekee anayeweza kunisaidia katika kisanga hiki ni Martin Hisia. Sijui kwanini sikuliwaza hili mapema, hata yale mauaji ya Jane angeyafanya yeye yasingenipeleka katika matatizo. Martin atanisaidia". Alichukua simu yake na kumpigia Martin.

Muda huo. Disko lilikuwa limenoga katika ukumbi wa starehe wa Ambiance uliopo Sinza. Idadi ya wanawake katika ukumbi huo ilikuwa wengi kuliko wanaume tofauti kabisa na iwavyo. Wengi wa wanawake hao walikuwa ni wale wanaojiuza nje ya ukumbi huo ambapo kulikuwa na baa kubwa maarufu kama Kona baa.

Ndani ya ukumbi huo hakuna hata mtu mmoja akiyejua kilichotokea mita chache tu nje ya ukumbi huo. Ndani kulikuwa na makelele na watu walikuwa wanajirusha isivyo kawaida. Miongoni mwa watu hao alikuwepo kijana mmoja aliyezungukwa na rundo la wasichana. Yeye alikuwa katikati huku akipapaswa na kutekenywa na wasichana hao. Mezani kulikuwa na bia zisizo na idadi. Ghafla simu ya mwanaume huyo iliita.

" Excuse me warembo, ngoja nikapokee simu nje" Martin alisema huku akinyanyuka pale katikati ya rundo la wasichana.

"Lucas Mohamed anataka nini usiku wote huu?" Martin alisema.

Simu iliita hadi ikakata.

Martin alisogea pembeni ya ukumbi ule ambapo kulikuwa na kituo cha mafuta. Sasa alipiga yeye simu.

"Haloo Lucas nambie kaka?" Martin aliongea simuni.

"Upo wapi Martin kuna tatizo!"

"Nipo Ambiance hapa mkuu. Tatizo gani tena usiku huu? Nipo nakula maisha hapa" Martin alisema kwa utani.

"Its serious issue Martin, usilete mas'hara hata kidogo. Kuna watu wamechoka kuliona jua la kesho!!"

"Wakina nani hao? Na wanapatikana wapi? Sababu na malipo utanambia kesho" Martin alisema.

"Ni mhariri wa gazeti la Ngamizi anaitwa Alphonce Mnubi yupo ofisini kwake pale Mwenge hivi sasa. Mwengine ni mwandishi mbeya Zulfa Hussein yupo njiani kuelekea Mwenge ama atakuwa Mwenge. Kabla hujaua wahoji kuna kitu changu wanamiliki. Hakikisha unakipata. Ni muhimu sana Martin. Donge nono lakusubiri kesho asubuhi" Lucas alisema.

"Nitakupigia" Martin alisema na kukata simu.
 
SEHEMU YA 15

"Kazi imekwisha" Lucas alipumua pumzi ndefu. Alijisikia amani, alimwamini sana Martin. Aliamini Martin anaenda kuimaliza kazi. Lucas aliendelea na safari ya kuelekea nyumbani kwa Jane Munuo. Alikuwa na taarifa zote mahali alipokuwa akiishi Jane. Alifika, kwa kutumia funguo bandia na kujitosa katika chumba kidogo akichoishi Jane. Aliyoyakuta ndani ya chumba kile kidogo yalimwacha mdomo wazi! Lucas alikuwa anatazamana na chumba kilichochambuliwa vibaya sana. Chumba kilikuwa kimepakuliwa kila mahali. Godoro lilikuwa chini. Kapeti lilikuwa limefumuliwa huku kabati la nguo likiwa lipo wazi nguo zikiwa zimechambuliwa. Juu dari ilikuwa inamcheka.

"Nani kaniwahi hapa. Kwa mara nyingine 001 itakuwa imechukuliwa hapa. Ooh my God this is very dangerous to me. Nimekwisha, nimekwisha mimi" Lucas alikuwa anawaza akiwa kasimama katikati ya chumba cha Jane Munuo. " Nitafanya nini sasa? 001 ipo mikononi kwa mtu asiyehusika. Ni nani huyo? Na kajuaje kama 001 ilikuwa mikononi mwa Jane Munuo?"

Ghafla simu yake iliita. Jina lililotokea ni Martin. Aliipokea simu kusikia Martin ana habari gani.

"I killed Alphonce Mnubi dakika saba zilizopita but Zulfa Iddi nimemkosa. Sasa naelekea nyumbani kwake kumdhibiti." Martin alisema.

"Uliwahi kumhoji chochote Alphonce?" Lucas aliuliza.

"Yes, na ndiye aliyenielekeza nyumbani kwa Zulfa. Nilimbinya kidogo kabla ya kifo chake, akanambia Zulfa ndiye mwenye records zinazokuhusu wewe, tutaonana baadae Lucas nakaribia katika nyumba ya Zulfa hapa" Martin alikata simu.

"Aisee Martin kiboko!! Kwanini sikumshirikisha tangu awali. Haya mambo yasingetokea na 001sasahivi ingekuwa mikononi kwangu?" Lucas aliwaza huku akitoka nje.

Lucas alitoka nje, alipanda katika gari yake na kuelekea nyumbani kwake. Alikuwa amewahiwa, hakuhangaika hata kupekua mle chumbani. 001 aliikosa kwa mara nyingine tena. Dakika kumi na tisa baadae alikuwa nyumbani kwake. Hakukuwa na foleni hata chembe iliyomfikisha mapema nyumbani kwake Ubungo Riverside. Aliposhuka tu garini simu yake iliita. Jina lilisomeka Martin. Aliipokea harakaharaka.

"Nambie Martin Hisia? Umefanikiwa?" Lucas aliuliza kwa sauti yenye uwoga.

"Hayupo. Zulfa hayupo nyumbani kwake wala kazini. Sijui atakuwa wapi huyu mwanamke. Nina simu ya Alphonce Mnubi hapa. Nimejaribu kuipiga namba ya Zulfa hapatikani!!" Martin alisema kwa sauti yake ya taratibu.

"Daah aisee, tutafanya nini sasa? That records is very important to me. Jitahidi juu chini umpate Zulfa na that records" Lucas alisema kwa kusisitiza.

"Ngoja niingie kazini tena. Nitampata tu huyo mwanamke kabla hakujakucha" Martin alisema na kukata simu.

Alipanda pikipiki yake na kurudi Hongera baa. Alijua kila kitu atakipata huko.
 
SEHEMU YA 16

"Ngoja nirudi Hongera baa. Alphonce alinambia Zulfa alimtuma huko. Nitampata tu"

Mara simu yake iliita. Akaitia mfukoni na kuiangalia. Jina lililotokea ni Lucas. Akaipokea.

" Martin! Zulfa is dead!!!" Lucas alisema simuni.

"What!!!, nani kamuua? We umejuaje? I wapi maiti yake?" Martin ilikuwa zamu yake kuuliza.

"Amepata accident Sinza madukani. Nimeona taarifa katika group moja la waandishi wa habari ambalo mimi pia nipo. Nenda Sinza Martin hakikisha unaipata records!!" Simu ikakatwa.

Martin alielekea Sinza Madukani kuisaka record ikiyoonesha mauaji aliyoyafanya Lucas.





Martin alielekea Sinza Madukani kuisaka record ikiyoonesha mauaji aliyoyafanya Lucas.

***

Saa kumi na moja alfajiri Martin alikuwa Ubungo Riverside nyumbani kwa Lucas. Walikuwa wamekaa sebuleni, wote jasho likiwatoka .

"Nilifika eneo la ajari kama ulivyonitaka" Martin alieleza. "Imetokea bonge la ajari ambayo hata sababu yake haieleweki na nilikuta kuna watu wengi sana. Kwa mbinu zangu nimejaribu kuupekua mwili wa Zulfa ambaye alikuwa amelowa damu kila sehemu ya mwili wake. Mheshimiwa Lucas amini nakwambia Zulfa hana records yoyote ile. Na huu ndio mkoba wake aliokuwa nao. Zaidi ya simu hakuna lolote la maana. Tumempoteza Zulfa. Bila shaka tumeipoteza na records" Martin alisema.

" hii ni mbaya!!! Mbaya, mbaya mbaya sana kwangu. Hiyo records ni muhimu sana kwa mustakabari wa maisha yangu ya kisiasa. Nitafanya nini mimi Martin?" Kwa mara ya kwanza tangu atimize miaka kumi na nane Lucas alikuwa analia. Tena analia mbele ya mwanaume mwenzake.

"Upo na mimi amini hakitoharibika kitu. Tutaipata records. Nitaisaka usiku na mchana. Don't cry my boss. I will make it" Martin alisema.

Tangu siku hiyo hawakuiona records wala tetesi zinazohusu hiyo records. 001 nayo iliyeyuka. Uchaguzi ulipofika Lucas aligombea ubunge na kuupata wakati Mheshimiwa Dr Joseph akichaguliwa kwa awamu ya pili. Na Mheshimiwa Joseph alimchagua kuwa waziri wa ulinzi. Cheo ambacho alikitumia katika harakati zake za kuisaka record na 001. Hakuvipata.

Hadi hivi juzi alivyopigiwa simu na mtu aliyejiita Elizabeth Neville na kudai kuwa ana records inayomuhusu yeye pamoja na 001 na ajiandae kukutana naye mahakamani. Hapo ndipo alipomtafuta Martin Hisia na kumpa kazi ya kumtafuta huyo aitwaye Elizabeth Neville.

"Hivyo ndivyo ilivyotokea Martin" Lucas aliongea simuni. Ule mkasa wa records wa kipindi kile ndio chanzo cha kazi hii mpya Martin. Elizabeth Neville ni tishio kwangu katika safari yangu ya kuelekea ikulu. Lazima tumsake na kutupa vitu vyetu" Lucas alisema.

"This is very big issue as i think. Lazima nitafute mtu wa kunisaidia. Siwezi fanya peke yangu kazi hii" Martin alisema.
 
SEHEMU YA 17

"Wewe ndio master plan wa hii ishu. Nimekuamini. Nimeakuachia wewe kila kitu. Fanya ufanyavyo tumpate Elizabeth Neville" Lucas alisema.

"Kwakuwa tunamtafuta mwanamke lazima tumpate mwanamke ili atusaidie kumsaka huyo Elizabeth Neville. Lucas, tunamuhitaji Binunu katika hii ishu. Nikiwa na Binunu am sure we will complete this as soon as possible" Martin alisema.

"As I say ni wewe tu. Ongea na Binunu na umjumuishe kazini. Malipo na kila kitu ni juu yangu. Nitawalipa kiasi chochote kile" Lucas alisema.

Simu ikakatwa.

Muda uleule Martin alipiga simu kwa Binunu.

"Hallo comrade, leo maajabu umenikumbuka lete maneno" Binunu alianza kwa mbwembwe simuni.

"Nipo comrade mambo tu yamekuwa mengi, vipi maisha yanasemaje?" Martin alijibu.

"Ni bomba kabisa. Twamshukuru Mungu tunaendelea kupumua" Binunu alijibu.

"Sasa Binunu kuna misheni imetokea" Martin alianza kusema. " ilianza kama misheni ndogo lakini siku zinavyosonga mbele naona yazidi kuwa kubwa. Nahitaji sana msaada wako mtu wangu" Martin alisema.

"Daah kwa sasa Mimi sifanyi hizo mambo. Nimeamua kuachana na maisha hayo. Napenda sana kuwa katika misheni lakini kwa sasa hapana. Nimeamua kuwa mtu wa kawaida tangu ile misheni yetu ya mkanda wa siri." Binunu alisema.

"Come on Binunu. Hayo siyo majibu ya Binunu nimjuaye. Binunu hawezi kujibu hivyo. Binunu apewapo misheni siku zote mwili wake humsisimka na huwa tayari kwa lolote. Binunu my dear kuwa Binunu yule, naomba unikubalie tuwe wote katika misheni hii, kama vipi hii iwe misheni yako ya mwisho kama mimi nilivyojiahidi" Martin alisema.

"Ok, upo wapi Martin tuje tuongee kwa kina" Binunu alisema.

"Kwa sasa nipo Mafinga katika hiyo misheni so kama vipi kesho chukua ndinga uje Mafinga"

"Sawa Martin. Tutakuwa wote kesho jioni.

Simu ikakatwa.

" Yes we're going to make it. Binunu ndani ya nyumba. Yule jamaa mtembea uchi usiku atajuta kuzaliwa" Martin aliwaza.

***

Ni dakika thelathini na tatu sasa Elizabeth Neville alikuwa katika mateso makali. Felix akitumia kila aina ya mateso kuhakikisha Elizabeth anasema kila kitu anachokijua juu ya 001.

"We mwanamke nitakuuwa mimi!! Usugu wako haukusaidii kitu chochote kile. Kukaa kwako kimya kwakufanya uzidi kuchakaa. Answer this simple question... Ipo wapi 001? Mbona swali dogo tu hilo!!" Felix aliuliza kwa ukali.

Elizabeth alikuwa anamwangalia tu. Uso wake ukionesha alikuwa anapitia katika maumivu makali.

"Elizabeth, this is last warning. When i come back nakuua!! Huna thamani tena kwangu. Husemi tunachotaka useme. Bora ufe tutajua how tutapata hiyo siri ya Lucas" Felix alisema huku akiondoka..

Alifika sebuleni. Kulikuwa na watu watatu waliokaa kwenye sofa.

"Vipi amesema chochote?" Mtu mmoja aliuliza Felix alivyotokea tu.
 
SEHEMU YA 18

"Ameendelea kuwa bubu. This woman ni sugu sijawahi kuona. Nimempa kila aina ya mateso. Yupo nyang'anyang'a lakini still amegoma kusema." Felix alisema huku akikaa sofani.

"Sasa tunafanye? Na bosi anakuja leo na anahitaji majibu kuhusu 001?" Jamaa mmoja kati ya wale watatu alisema.

"Yaani nimempiga kila sehemu katika mwili wake. Nimemswaga hasa lakini mwanamke hajasema kitu chochote kile kutoka katika mdomo wake zaidi ya kulia kwa kutoa machozi, hata sauti hatoi. Ni mwanamke wa ajabu, hata wewe nikikufanya nilichomfanya utasema lolote lile nitalikuuliza lakini sio kwa Elizabeth Neville. Mwanamke sugu sijapata kuona hapa duniani" Felix alisema.

"Sasa naona tubadili mbinu" jamaa mwengine mwembamba alisema. " tutumia njia soft siyo ya mateso yaweza kusaidia. Nina imani ni lazima aseme!! Atasema tu...Nimelisoma faili la Elizabeth Neville kwa kina. Nimeona kwamba Elizabeth ana ndugu mmoja wa kiume ambaye wanapendana sana. Sasa naona huyo nduguye ambaye anaitwa Moses Neville tumtumie ili kufanikisha jambo hili" Jamaa mwembamba ambaye alikuwa anaitwa Richard alisema.

"Sijaelewa hiyo itafanyaje kazi? Huyo Moses sidhani kama anayajua mambo haya. Atatupelekaji katika majibu ya maswali yetu?" Felix aliuliza.

"Ni hivi" Richard alifafanua "Tumtume mtu mmoja aende Mbeya ambapo familia ya Moses inaishi kwa mujibu wa maelezo wa hili faili. Akifika huko aiteke familia yote ya Moses. Familia ya Moses na Moses mwenyewe wakiwa mikononi mwetu tuweke makubaliano na Moses kwamba afanye awezavyo kumfanya dada yake Elizabeth amwambie siri aliyonayo juu ya Lucas ndio tuiachie familia yake. Moses anaipenda sana familia yake hasa mtoto wake mdogo aitwaye Anna, kwa kutumia njia hiyo lazima atatafuta namna tu ya kumshawishi dada yake mpaka aseme" Richard alieleza kwa kirefu.

"Fantastic!!! Hilo ni bonge la mbinu. Richard we jamaa una akili sana. Ni kweli sometimes sio lazima kutumia nguvu tu mara zote na akili pia yahitajika sana" Yule jamaa mwengine mrefu alisema.

"Kwa hilo tumekubaliana?" Wote wakaitikia kwa vichwa. Jamaa mfupi mnene akaendelea " Felix utaenda Mbeya kutekeleza hiyo kazi. Utaenda leo ili leo usiku au kesho asubuhi uwe hapa. Kuna tatizo lolote?"

"Hakuna tatizo, ika kuna kitu nilikuwa sijawaeleza" Felix alisema. "Jana asubuhi kuna mtu alienda kumuulizia Elizabeth nyumbani kwake. Si unajua pale tulimweka kibaraka wetu ili ajifanye mama wa Elizabeth ili tujue ni watu gani wanaenda kumuulizia Elizabeth Neville. Basi jana kuna jamaa mmoja alienda pale ambaye dada Beatha alivyomwona tu akamtilia shaka. Alijifanya yeye amesoma na Elizabeth na wamepoteana muda mrefu baada ya kwenda kusoma nje ya nchi. Baada ya huyo jamaa kuondoka Beatha aliwasiliana na mimi moja kwa moja na kunitaarifu.
 
Back
Top Bottom