Simulizi: Msegemnege


Naipitia
 
Sehemu ya XII – Barua kutoka Manama.

Ilipoishia


Omari akafanya hima kumaliza kazi ya kuwaadaa samaki wake kisha akarudi hadi kwao uswahilini Ukwamani na kumkabidhi mama yake samaki wale, kisha akasafisha kapu lake kama kawaida na akaingia chumbani kwake na kuifungua ile chupa…

Sasa endelea…

Akiwa amekaa kwenye stuli, akaifungua mfuniko wa chupa huku uso akiwa ameuweka mbali, kama vile kuchukuwa tahadhali ya hewa ya sumu au chochote kitokacho mle kwenye chupa, lakini kwa bahati nzuri hakukuwa na la ajabu lolote zaidi ya harufu nzuri ya manukato ya kawaida. Aliendelea kwa kuitoa ile karatasi nyeupe ambayo sasa ilionekana imehifadhi kitu kingine ndani. Akaivuta kwa nguvu hadi ikatoka, chupa akaiweka pembeni sakafuni, na akaanza kufungua ile karatasi ambayo nayo ilionekana ikiwa imeandikwa kwa wino wa bluu, lakini pia alikuta kiasi cha noti za kigeni, mpya kabisa.

Alipoangalia vizuri aliona zote zimeandikwa 20 kisha maneno ya kiarabu, na upande wa pili zilikuwa zote zimeandikwa Central Bank of Bahrain, Twenty Dinar ingawaje alisoma kwa kuchapia matamshi. Akafurahi sana akazihesabu akaona zipo jumla ya noti kumi na moja, lakini hakuweza kujuwa mara moja ni kiasi gani.

Akili ikamjia na akachukuwa ile karatasi ili ajaribu kuisoma aone imeandikwa nini. Lo! Karatasi ilikuwa imeandikwa kwa lugha ya Kiingereza na mwandiko wa wino wa bluu. Akaamua kutoka kimya kimya baada ya kuihifadhi ile chupa chini ya uvungu wa kitanda chake, akiwa ameichukuwa ile karatasi na noti moja. Moja kwa moja akaenda ‘Stationery’ iliyopo Ukwamani zinapogeuzia daladala.

“Dada za jioni?” alimsalimia mhudumu..

“Shwari tu Ommy, karibu…” alijibiwa kwa kuchangamkiwa.

Omari anafahamika sana maeneo ya hapo Ukwamani kwakuwa alikuwa konda wa daladala pia alipiga debe kiasi hapo.

“Naomba nitolee kopi karatasi hii..” alisema Omari

“Nakala ngapi Ommy…” Yule dada alipokea na kuiweka kwenye mashine ya kutolea nakala bila kuisoma…

“Toa mbili tu” alijibu Omari na yule dada akabofya mashine ya kutoa nakala (photocopier) na zikatoka nakala mbili safi.

Baada ya kukabidhiwa zile nakala mbili na ‘orijino’, Omari alitenga nakala moja na orijino pamoja na nakala moja akazikunja kwa pamoja na kuziweka mfukoni.

“Samahani sista, naomba nitafsirie hii karatasi…” Omari aliomba msaada baada ya kulipa shilingi mia kama gharama ya kutolea ‘fotokopi’.

“Mmh, mwenzangu, kwenye kutafsiri hapo sasa!, nisije nikakuongopea bure!, ngoja nikuelekeze sehemu…” alijitetea yule binti hata bila kutaka kuisoma karatasi yenyewe.

“Nenda pale ‘opposite’ na oilcom kwa Frank, pale anapofundishia tuition atakusaidia…” alisema yule Dada.

Baada ya dakika chache, Omari alifika kwa Frank kwenye tuition centre yake maarufu wakati huo hapo Kawe na kukuta darasa likiendelea…

Baada ya kukaribishwa na kueleza shida yake, Frank alimuambia…

“Nitakuchaji ‘buku’ mbili kwa kukutafsiria, na buku kuyaandika…”

Omari wala hakuwa na pingamizi, akatoa noti ya elfu tano na kumpatia Frank…

“Nije baada ya dakika ngapi kuifuata?” aliuliza Omari wakati akipokea chenji yake…

“Aah, hii fasta tu, subiri hapo kwenye kiti” alijibu Frank huku akiipitia ile karatasi.

Karatasi yenyewe ilisomeka hivi…

Date xx-xx-xxxx

Assalaam alaykum.

My name is Nasreen, I am from Manama Barhain.

Whoever will bring this original writtings to me inperson will be my friend. Use dinar bill attached as transport fee, add yours if fare is not enough and I will refund you. Do NOT forget to bring also one note bill attached.

Eager from seeing you, my ideal lucky friend.

May God Almighty bless you.

Nasreen. (+973xxxxxxxxx)


Frank wala haikumchukua muda kuitafsiri na kuichapa upya ile karatasi kisha aka-print na kumkabidhi Omari. Frank alikuwa ‘bize’ na wanafunzi wake hivyo aliendelea kuwafundisha na Omari akaondoka bila hata ya kuisoma ile tafsiri.

Jua lilikuwa limeanza kuzama, alipofika nyumbani chumbani kwake ndipo akanza kuisoma. Awali alivyotoka nyumbani pia alitaka ajue ile noti moja ina thamani kiasi gani lakini kulingana na mazingira ya siku hiyo hakuweza kupata ufumbuzi.

Alifurahi sana baada ya kuelewa yale maandishi na sasa akawa na shauku ya kutaka kujuwa thamani ya noti moja iliyoandikwa ‘20’.

Kesho yake mapema sana alipanda daladala hadi Shoppers Plaza ambako kuna sehemu ya kubadilishia fedha za kigeni…

“Naomba nibadilishie hii nipate Shilingi…” alisema Omari baada ya kusalimiana na mtoa huduma wa ‘bureau de change’ ile…

“Oh, hapana, hii sisi hatubadilishi hapa, sisi tunabadili dola, paundi, rand …” akataja pale orodha ya fedha wanazobadili na kumrudishia noti yake…

“Kwani kama mngekuwa mnabadili ningepata kiasi gani…?” alimpachika swali ambalo ni muhimu sana kwake Omari.

“Kwa hii unaweza kupata laki moja hadi laki na kumi hivi…eee nenda kule mtaa wa Lumumba kuna Hoteli (akaitaja) pale utabadilishiwa kirahisi tena kwa reti nzuri…” alijibu yule mhudumu kisha akaendelea na mambo yake kama vile hataki maswali mengine…

“Mida ya kazi hii, lakini ‘potelea pote’ ngoja niende huko Kariakoo.” Omari alijisemea.
---

Alifuata maelekezo vizuri kisha akafika pale hotelini na kueleza shida yake mapokezi.

“Subiri kidogo nikuitie mhusika…” Yule dada wa mapokezi alimjibu Omari kisha akaanza kuita kwa kupaza sauti…

“Mediiiii, Mediiii, njoo kuna mteja huku…” aliongea kwa sauti ya juu.

Kumbe Omari alipoingia mle hotelini, alimuacha nje huyo anayeitwa Medi. Medi ni kijana halfcast wa kiarabu na mwafrika, ndiye alikuwa akisimamia kitengo cha kubadilisha fedha kwenye hoteli hiyo. Hapakuwa rasmi sana lakini maeneo hayo watu wengi wanapajuwa kwa shughuli hiyo na kwa rate ‘nzuri’.

“Eee unataka chenji ya dola ngapi…” Aliuliza Medi huku akiingia kwenye kijiofisi chake kilicho nyuma ya ngazi hapo hotelini.

“Siyo dola, ni hii hapa…” Omari akatoa ile noti akamkabidhi Medi kupitia kidirisha kidogo ambacho kilikuwa kina kimewekwa ‘tint’. (kioo cha giza maarufu kama tinted).

“Aaa kumbe ni Dinari ya Bahrain, eee kwa hii bosi nitakupa laki na ishirini, si unajua tena hizi haziji mara kwa mara…” alisema Medi.

Omari hakuamini masikio yake alipotajiwa hela ile. Kisha akasema…

“Poa tu, nipatie…”

Medi akamuhesabia noti 12 za elfu kumi kumi, kisha akasema hesabu bosi…

“Wakati anahesabu, Omari akasema, nitakuletea nyingine baadaye kama hizi 9”

“Poa, usiponikuta, namba hiyo hapo kwenye kioo utanicheki…”

Omari wala hakuwa na simu ya mkononi, ‘kitochi chake’ kilishasambaratika kitambo wakati akifanya kazi kwenye daladala.

“Sawa, nitakucheki hiyo baadaye…” alijibu kisha akaelekea Kariakoo kununua simu kwa hela aliyopata.
---

Saa kumi kasoro hivi jioni, Omari alikuwa tena pale hotelini Lumumba, na kwa bahati nzuri alimkuta Medi, wakafanya biashara.

Omari Juma siku hiyo alikuwa na zaidi ya shilingi milioni moja na ushee. Akarudi nyumbani na kumkuta mama yake akiwa nje kwenye kigenge chake.

“Mama, nina habari njema mbili, ukishafunga genge lako nitakuambia…” Yalikuwa maneno ya Omari akimtamkia mama yake kwa furaha.

“Sawa Omari, na leo nitafunga mapema naona biashara tangia jana wala haichangamki…” alijibu mama Omari.

Baba yake Omari naye muda si mrefu alifika akitoka matembezini maana siku hiyo alikuwa ‘ofu’ , akiwa amelewa akaanza kumwambia mke wake…

“Nipatie elfu ishirini hapo…” ilikuwa ni sauti ya kilevi…

“Sina mume wangu, tangia jana biashara wala si nzuri, hapa nina elfu nne tu zingine nimefanyia matumizi ya nyumbani…”

“Lete hizo hizo zingine nitajua huko mbele kwa mbele…” alisema afande yule

Mama Omari akafunua gunia kwenye meza ya genge lake kisha akatoa noti moja ya elfu mbili, moja ya elfu moja na chenji chenji zilizofanya jumla kuwa elfu nne. Akampatia mumewe na muda ule ule mumewe akaondoka kupitia uchochoro uliokuwepo jirani kuelekea bar iliyo jirani.

Ilikuwa ni kawaida ya baba Omari akiishiwa na hela kuzichukuwa ki nguvu pesa za mkewe katika biashara yake.

“Atakuwa anadaiwa huyo huko bar…” alisikika mama Omari akijisemea

Omari kwa kuwa alikuwepo jirani alisikia mazungumzo yote, na haikuwa kawaida yake kuingilia ugomvi wa baba yake na mama yake kwani kuna siku ‘alilapuliwa’ na ‘mkanda’ na kusababishiwa maumivu makubwa ambayo yalimuachia alama mwilini.

Lakini siku hiyo Omari akamuambia mama yake, ngoja nimfuate baba huko huko bar, si anakunywaga ile bar ya pale ‘Jamborii’, akaondoka fasta.

Dakika chache baadaye akafika kwenye ile bar, tayari alikuwa ameshatenga noti mbili za elfu 10 ili ampatie baba yake.

Baba yake wakati huo alikuwa amejiinamia kwa ulevi na mawazo wala hakumuona mwanawe wa pekee Omari alipofika karibu naye.

Omari alichuchumaa na kumnong’oneza baba yake sikioni huku akimshikisha zile hela mkononi. Baba Omari alipohisi kitu kama hela hivi, akainua shingo na kuangalia vizuri. Akamuona mwanae na kupigwa na mshangao...

“Ahsante sana Omari, umeniokoa…” alisema kwa kifupi kisha akainuka kuelekea Kaunta na Omari aliondoka haraka maeneo yale kwa kuchelea aibu za baba yake.

Nyumbani alikuta mama yake ameshafunga genge na anaendelea na kuandaa chakula cha jioni.

“Nimerudi mama, nimemkuta baba pale bar na nimempatia elfu ishirini…” alisema Omari.

“Elfu ishirini? Umezipatia wapi…!?” aliuliza kwa mshangao mama Omari.

Wakati Omari akiwa anazunguka na daladala ilikuwa ni kawaida sana kurudi nyumbani hadi na shilingi elfu hamsini, lakini alipoanza kupiga debe pato lilishuka hadi akawa anarudi na elfu tatu, siku nyingine nne, na ikizidi sana elfu sita. Lakini alipoanza shughuli za ufukweni ndio aliweza kufikisha elfu kumi wakati mwingine elfu kumi na tano kwa siku.

“Ndiyo maana nimekuambia leo nina habari mbili njema mama…” Omari alitabasamu huku akimuangalia mama yake kwa bashasha.

“Halafu leo, kapu lako naliona unapoliwekaga, hukwenda ‘pwani leo’? “ alisema mama Omari akimaanisha ufukweni.

“Ndiyo mama, leo sikwenda…”, alisema kisha Omari akakaa kitako kwenye kigoda kilichopo eneo la jikoni pembeni ya mama yake aliyekuwa akiandaa mboga za jioni.

Omari akaanza kumsimulia mama yake kisa kizima cha chupa aliyoiokota baharini na habari zake zote hadi muda huo…

“Hivyo mama hapa nina furaha ya kupata milioni moja na kuna ofa ya kusafiri kusikojulikana na kufaidi ya huko…” alihitimisha kwa kutotaja kiasi halisi cha fedha alichonacho.

Omari akatoa nakala ya ile karatasi aliyokuwa nayo mfukoni na kumpatia mama yake.

“Mmmh, si kizungu hiki, haya mie na kizungu wapi na wapi…” aling’aka mama Omari.

“Ipo hii tafsiri yake…” kisha akampatia ile karatasi aliyoandikiwa na Frank.

Mama yake akaisoma na kuirudia na kuirudia kisha akasema…

“Alhamdulillah, Mungu ametuhifadhi, sasa mwanangu usimwambie baba yako…”

Baada ya mazungumzo marefu pale, mama Omari alihitimisha kuwa mwanawe atumie tu zile hela kujianzishia biashara na wala asifikirie kusafiri kwenda huko ughaibuni isije ikawa mtego wa kuishia kwa maharamia, wakamdhuru mwanawe.

“Usije ukaenda huko ukaishia kuwa mtumwa, ama kunyofolewa figo zako ama kudhuriwa kwa namna yoyote ile, baki hapa hapa, tafuta biashara nyingine nipatie na mie niongezee mtaji wa genge langu maana hali halisi ya nyumbani si unaiona?!”

Omari akajibu…

Sawa mama, nimekusikia, ngoja nitafakari kwanza.


Itaendelea...
 
Tupio la XIII - Nyoka

Ilipoishia..


Baada ya mama Rose na Vai wote kuwa wameoga kukawa na mazungumzo ya pamoja na yule mtoto.
Zawadi aliwaeleza kuwa alidhani wanaenda kule Kanisa la mama Mchungaji ili awaoneshe kitu lakini kwakuwa tayari walishapanga ratiba zao basi aliamua awasubiri ili waende wote huko Roman.

“Eti, mama Rose, au twende tu na huyu binti kule kwa mama Mchungaji!?..” Vai aliuliza… kisha mama Rose akasema…


“Ingawaje tumechelewa lakini bado watakuwa wanaendelea na ibada, si unajuwa wale wanachukuwa muda mrefu hadi kumaliza, basi tujiandae twende…”

Baada ya muda mchache wakawa tayari na watoto wao kisha wakafunga milango ya nyumba na kuanza safari ya kwenda Kanisani kwa mama Mchungaji…


Sasa endelea…

Walifika kanisani ibada ya kawaida ikiwa inaendelea na kwakuwa walikuwa wamechelewa hawakupata nafasi katika viti vya mbele badala yake walipata nafasi kwenye safu ya pili kutoka mwisho ambapo wote watano (wakiwemo Junior na Rose) walikaa kwenye safu moja.

Punde si punde ikafika wakati wa sadaka na waumini walianza kujongea mbele kwa ajili ya kumtolea Mungu sadaka…

“Sasa sikilizeni, mimi nitakuwa katikati yenu, wakati tunaelekea kutoa sadaka…” alisema yule binti kwa kunong’ona akiwaambia mama Rose na Vailet.

“Tukifika pale mbele mama Rose usitoe sadaka hadi nikushike mkono ili tutoe pamoja, kisha na wewe mama Junior nitakushika mkono ili tutoe sadaka pamoja, kisha nitambeba Rose naye atoe ya kwake…” aliendelea kusema huku akiwaangalia kwa makini.

“Huyu Junior anayo macho ya kuona, hivyo sadaka yake atatoa mwenyewe wewe mama yake ukimsaidia kuinama kulifikia kapu la sadaka…” alisisitza jambo lililowafanya mama Rose na Vai wastaajabu kuhusu hayo macho ya kuona…

“Kwa hiyo, lengo langu nilitaka muone ninachokiona mimi kwenye Kanisa hili, bila shaka mtapata majibu kwa nini mtoto siku ile alikuwa analia sana…” alimaliza na wakawa wamesimama no kusogea mbele kwa ajili ya kumtolea Mungu sadaka…

Huku wimbo wa kuhamasisha waumini watoe ukiendelea kuimbwa na waumini wote wakiongozwa na kwaya ya kanisa, akina mama Rose wakafika pale mbele akashikwa mkono wa kushoto (mama Rose) na yule binti ili mama Rose atoe sadaka yake…

“Yo!” Mama Rose alipiga kelele kwa kilugha chao (Kihaya) kwa kushangaa kisha haraka haraka akaondoka kurudi kwenye siti yake kule nyuma bila hata kumsaidia Rose naye atoe sadaka.

“iiiiiiiiiii” Ilikuwa sauti ya Vai akishangaa kwa woga wakati aktitoa sadaka na mtoto wake akaanza kulia na kugeuza shingo, mama Junior aliondoka pia na yule binti akawafuata.

Wakati mama Rose, yule binti na Vai wakiwa pale mbele, mchungaji na wasaidizi wake waliokuwa wamesimama pale mbele walikuwa wakiwakodolea macho kwa kuwashangaa na mchungaji kama vile akitamani kumwita yule binti…

Zoezi lile likaisha na watu wote wakawa wamekaa kwenye siti zao.

“Tuondokeni…” Mama Rose alisema akimwambia yule binti pamoja na mama Junior

“Tusubiri kidogo…” Yule binti alisema huku kama akitarajia kitu fulani hivi kitokee…

Mara mama Mchungaji akapaza sauti…

“Bwana Yesu asifiwe!” alisema na waumini wote wakaitikia “Amen”

“Eeee leo tena tumetembelewa na wageni, kwa heshima nawaomba wamama kule nyuma pamoja na huyo binti mje mbele huku…” alisema yule mchungaji.

Wakati huo bado walikuwa hawajapata muda wa kuambiana wameona nini pale mbele. Yule binti (Zawadi) akasimama na kuwaashiria wenzake nao wasimame waende pale mbele.

Kanisa lote lilikuwa kimya kama limepata bumbuwazi fulani hivi baada ya sasa kumkumbuka yule binti…

Akina mama Junior wakasogea hadi jirani na aliposimama mama mchungaji na walivyotulia yule binti akamchukuwa Rose na kumbeba usawa wa ubavu kisha akafanya uelekeo wa macho ya Rose yaone sehemu sadaka zilipo…

“Nyokaaaaa, nyokaaaaa, nyokaaaa!” alipiga kelele Rose na kupokonyoka kwa yule binti na kukimbilia kwa mama yake…

Waumini wakataharuki, wakidhani ni nyoka tu wa kawaida ameingia kanisani.

Yule binti akamsogelea mama Rose na kumgusa mkono kisha akamwambia angalia kwenye sadaka…

“Chatuuuu, chatuuuu” alipiga kelele baada ya kuona kama alivyoona wakati wa kutoa sadaka…

Mara mama mchungaji akasema…

“Tulieni waumini, hakuna nyoka hapa wala hakuna chatu, watakuwa na mapepo hawa ngoja tuanze kufanya maombi ya kukemea…”

Zawadi akamshika mkono Vailet ili naye ashuhudie kwa mara nyingine…

“iiiiiii chatu ameinua kichwaaaa, chatu jamani chatuuuu!” Vai naye alishindwa kujizuia na wote sasa wakashuka pale juu aliposimama mama mchungaji na kurudi usaswa wa viti vya safu ya kwanza huku wakihema kwa taharuki na woga!

Mchungaji akaanza kukemea pale akipaza sauti na waumini wengine wakaanza kufuatisha kila mtu akisema maneno yake ya kukemea…

Pale mbele hapakuwa na chatu wala nyoka aina yoyote kwa macho ya kawaida, lakini mtoto Onesmo Junior, Zawadi, Vailet, Rose na mama Rose wao waliweza kuona dhahiri kilichokuwa kinaonekana kama kapu la kukusanyia sadaka…

Wakati mchungaji akiendelea kukemea na waumini wakifanya hivyo pia kwa namna mbalimbali, ghafla yule binti aitwaye Zawadi alianzisha wimbo tofauti na makemeo yaliyokuwa yakiendelea kanisani…

“…Yua yawe ehehee yua yawe,

You are Yaweh eheheheee,

You are Alpha na Omega… “

Kwa kuwa ni wimbo uliokuwa unajulikana, waumini wote nao wakaacha kukemea na kufuatisha mirindimo ya uimbaji kwa kufuata mashairi ya wimbo huo huku wakichanganya Kiingereza na Kiswahili.

Kuna kundi dogo wao badala ya kuimba walisikika wakisema…

“…ndiyo yule mtoto wa siku ile, leo mchungaji ataumbuka…”

Mwingine alisema…

“...Si nilikuambieni kuwa huyu si mtoto wa kawaida! Mmeona sasa!...”

Kanisa lilirindima kwa wimbo huo wa kuabudu hadi mchungaji akaanza kupepesuka ingawaje naye alikuwa ameanza kuimba kwa kufuatisha, lakini alizidiwa hadi akaanguka chini kisha akatokea dada mwingine kabisa ambaye si mhudumu katika kanisa hilo ingawaje ni mshirika, akasogea pale madhabahuni alipoanguka mchungaji na akaanza kukemea…

“…Ttoka pepo kwa Jjina la Yesu aliye hai, toka, huna mamlaka juu ya mwili wa mwanadamu, nasema ttoka…”

Waumini wengine nao walipoona hali ile wakaanza kukemea na wengine wakawa wanaongea lugha isiyoeleweka vizuri…

Mtoto Zawadi baada ya kuona vile naye akasogea hadi pale lilipokuwa kapu lililowekwa sadaka na kuanza kusema maneno ambayo hayakusikika vizuri lakini ghafla moto ukazuka na kuanza kuunguza lile kapu lakini ajabu hela hazikuwa zinaungua isipokuwa noti chache sana tena ziliungua kidogo tu kwa pembeni…

Waumini wakawa wanazidi kukemea hadi pale yule Zawadi aliposema…

“Kkwishaaa!.... huku akiwa anatetemeka, mkono mmoja bado akiwa amenyooshea lile kapu liliokuwa linateketea na moto ule ukafifia na kupotea, zikabakia hela zikiwa zimezungukwa na majivu ya kapu lile…

Mama mchungaji bado alikuwa amelala pale chini lakini sasa aliacha kugalagala na kubiringita na kujinyonganyonga badala yake alikuwa amelala chali akiwa amefumba macho lakini mdomoni alikuwa ametokwa na mapofu…

“Mfunikeni na kitenge…” mama mmoja mtu mzima aliamuru huku akimsogelea na kufanya kama anapima mapigo ya moyo ya mama mchungaji kwa kuweka vidole viwili kwenye mishipa ya mama mchungaji iliyopo shingoni kwa pembeni…

“Assante Mungu wa Mbinguni kwa wema wako…”

“Assante Baba kwa kuonesha utukufu wako!...”

“Assante…”

Yalikuwa maneno yaliyomtoka yule mama mtu mzima huku akinyoosha mikono yake juu kwa kushukuru…

“Muinueni akae…” sauti ya Zawadi ilisikika

Wasaidizi wa mama mchungaji wakaenda kumuinua na sasa mama mchungaji akawa amekaa na machozi yakaanza kumtoka huku amejiinamia…

“Sasa waeleze ukweli waumini wako na uamue kama utaendelea na huduma ama la!” Zawadi alisema kwa sauti ya ‘kuamuru fulani hivi’…

“Naomba maji ya kunywa…” Yalikuwa maneno ya kwanza kumtoka mama Mchungaji baada ya kuinuliwa…

“Mpeni kiti sasa akae na sisi sote turudi kwenye viti vyetu tukakae tumsikilie..” Aliongeza Zawadi baada ya kuona mama mchungaji ameshakunywa maji lakini pia waumini walijazana eneo la mbele kiasi cha kufanya kuwe na hewa nzito na nafasi finyu.

“Bwana Yesu apewe sifa!...” mama mchungaji alianza kufunguka…


Itaendelea…
 
Tupio la XIV - Kurithi Utajiri

Ilipoishia…


Tulitoka mle ndani tukiwa hatuna hata njaa, sijui kwa sababu ya ile chai nzito ama kwa sababu ya utajiri wa ghafla ili mradi tulikuwa na furaha na tulitembea kuelekea restaurant ya jirani kupata chakula cha mchana.

“Dada mimi sisikii njaa hata!” Nilisema wakati tunaingia cafeteria fulani iliyopo kwenye kituo cha kuuzia mafuta.

“Hata mimi Alex, sisikii njaa japo nilionja tu ile kahawa na sambusa kidogo” tukacheka kiasi na kuketi mle mghahawani.



Sasa endelea…


“Karibuni, je niwahudumueni nini?” alikuja mhudumu aliyeonekena amechoka kwa kazi za hapo maana mgahawa huo huwa bize sana mida ya saa saba hadi saa nane ambapo wateja wengi huja kwa mara moja kuja kupata chochote.

Ni mghahawa ambao wanapika chakula chao vizuri kwa kweli na ni wasafi hata jikoni kwao maana panaonekana kupitia dirisha kubwa lililotengenisha jiko na sehemu ya mtu wa kaunta kwa kioo kinachopitisha mwanga.

“Niletee baghia na juisi ya ndimu…” dada aliagiza kisha akaongeza, usisahau ‘chatne’ ya nazi.

Yule mhudumu akawa ananiangalia mimi sasa…

“Mimi nipatie beef curry ilete na chips…” nilisema
---

“Mmh, kumbe baba alikuwa na utajiri wa kiasi hiki lakini wala hakujionesha katika maisha yake halisi…” niliondoa ukimya baada ya kula viazi kadhaa ya nyama laini iliyowekwa pilipili za kutosha…

“Yani Alex, we acha tu, hapa mimi nina maswali kibao kichwani ambayo bado sijapata majibu yake…” alisema Queen,

“Enhee, we mwenzangu utaanzaje maisha mapya baada ya leo…” Nikamuuliza dada…

“Hata sijui, ngoja kwanza tumalizane na benki, kisha nimalizane na brela halafu ndio nianze kutafakari lakini ili niwe na akili iliyotulia lazima kwanza nipate majibu ya maswali niliyonayo…” alisema dada.

“Enhee nimekumbuka, kwani ile meseji iliyotumwa kwenye simu yako uliifuatilia?...” nilimuuliza

“Hapana sijaifuatlitia, unajuwa iliandikwaje? Ngoja nikusomee…” Alijibu huku akiperuzi kwenye yake…

“Queen Jonathan Ngonyani, Umefaulu hatua ya kwanza katika mradi muhimu, tafadhali upatapo ujumbe huu fika Ubungo eneo fulani (lilitajwa) kisha piga simu kwa namba hiyo uliyotumiwa ujumbe kwenda namba iliyokutumia ujumbe, utapokelewa…”

Dada Queen aliusoma ujumbe kama ulivyoandikwa.

“Mmmh, siyo matapeli hao?! hahaha…” nilicheka na kumtahadharisha kuwa huenda ikawa matapeli ama mtego wa kufanyiwa jambo baya.

“Inaonekana siyo matapeli, maana jana napo nimepata ujumbe mwingine kutoka namba ile ile ikiniarifu kuwa badala ya kwenda Ubungo sasa nipige ile namba na kusema maneno ‘kumi na moja kumi na mbili moja – 11121’ kisha nitapokea maelekezo kwa njia ya simu….”

“Duuuu, sasa itakuwaje?! Umeshawapigia?” Niliuliza kwa shauku na mshangao

“Hapana. Sijawapigia, nilitaka sakata hili kwanza liishe kisha ndio niwapigie nijue kulikoni, na kama wataniambia sijui niende Ubungo au sehemu fulani basi sintoenda kizembe, nitakuwa na timu yangu…” alijibu dada Queen kwa kujiamini.

“Kwani huko kwenye matembezi yenu ya usiku hudaiwi!?, isije kuwa kuna deni unaenda kulilipa!!” Nilimuuliza tena nikiwa na wasiwasi..

“Hapana Alex, nilishamalizana na madeni yangu yote, sana sana sasa hivi mimi ndiye ninaye wadai watu…”

Nikaamua kukatisha habari ile ili tuzungumzie jambo lililo mbele yetu muda huo…

“Dakika arobaini na tano sasa zimepita, kama vipi tusogee maeneo ya benki…” nilisema.

“Ni sahihi, ngoja nikalipe pale kaunta kisha nitakukuta hapo nje…” alisema.

Wakati nipo hapo nje namsubiri dada Queen, nilijiwa na yale maswali tatanishi kichwani, kwamba inawezekanaje baba yetu awe tajiri vile lakini aliishi maisha ya kawaida tu kama wafanyabiashara wengine wa kawaida, mbona alikuwa anamiliki hela nyingi na wala hakutaka kununua magari mazuri ya kutembelea…

Yani ilikuwa ni mfululizo wa maswali ambayo majibu yake sikujapata muda huo, na mara dada akawa ameshatoka naye pale nje tukaanza kujongea kuelekea NMB.
---

Tulifika pale benki, kweli tukakuta mlango umefungwa kuzuia wateja wa kutoka nje kuingia ndani maana muda ulikuwa umeisha ingawaje nadani kulikuwa na huduma kwa wateja waliopo.

Tukaenda mapokezi / maulizo, tukajitambulisha kuwa sisi ni wageni wa DCEO, tukaambiwa tusubiri, baada ya dakika chache tukafuatwa na mhudumu akatuongoza hadi ofisini kwa DCEO.

“Karibuni vijana…” alianza kuongea yule afisa DCEO.

“Lengo la kukuiteni mje hapa ni kutaka tuende wote BoT ili niwakutanishe na Gavana…”

Mimi na dada tukaangaliana kisha dada akajibu, sawa baba.

“Hivyo nisubirini dakika chache namalizia kazi fulani kisha tutatoka wote …” alimaliza kisha akawa bize na kazi zake.

Wakati tupo pale, akaingia mhudumu akiwa na maji ya kunywa pamoja na juisi, akatukaribisha kisha yeye akaondoka.

“Benki hii ni wakarimu sana kwa wateja wao…” nilinong’ona kumwambia dada

Dada akatabasamu kisha akasema kwa kunong’ona “Sisi ni wateja wakubwa…”

Tukawa tunabadilishana maneno pale kwa kunong’ona nyoyo zetu zikiwa zimetulia na kufurahi.

Mimi na dada wote tulikunywa maji, wala hatukugusa ile juisi kwa kuwa tulitoka kula chakula muda si mrefu.

“Eeee sasa wanangu, twendeni, mimi nipo tayari…” Alisema yule DCEO na akawa anayanyuka nasi tukanyanyuka…

“Nifuateni…” alisema.

Tukaanza kumfuata lakini safari hii haikuwa ile njia ya kurudi kule mapokezi bali tulijikuta tumetokea nyuma ya jengo ambako kuna gari kadhaa zilikuwa zimepaki. Akatuongoza hadi kwenye gari yake, akatufungulia mlango , tukaingia ndani ya gari kisha naye akazunguka upande wa dereva akaingia na kuendesha yeye mwenyewe.

Dakika chache tu tukawa tumefika BoT na baada ya kuegesha gari, tulianza kuelekea kwa miguu upande wa mapokezi, tulipita sehemu za ukaguzi wa kawaida kisha DCEO akaenda kwenye moja ya madirisha ya huduma za mapokezi.

Baada ya sekunde chache akatufuata tulipokuwa tumesimama akatuongoza hadi chumba kilichoandikwa Gavana.

Tulisalimiana pale na DCEO alifanya utambulisho kisha akafungua mazungumzo…

“Kama ulivyonielekeza mkuu, nimetekeleza, wale vijana ni hawa hapa…” alisema.

“Sawa, umefanya vizuri, hawa vijana wamepata tabu sana hadi kufikia leo hii hili jambo lao lilipokamilika. Basi wewe unaweza kuendelea na majukumu yako hawa nitawapatia usafiri wa kuwafikisha amjumbani kwao…”

Kikao kile hakikuwa kirefu sana tukiwa na DCEO, lakini baada ya DCEO kuondoka ndipo Gavana akaanza kutuhoji…

“Je mirathi yenu mmeshakalishiwa ipasavyo!?” aliuliza

Kama kawaida, mimi nilitulia ili dada ajibu…

“Ndiyo baba, tumeshahamishiwa hela kwenye account zetu za akiba na corporate, kwenye hisa za makampuni ya uwekezaji imebakia kuweka saini na kwenye Kampuni ya Jonathan Ltd imebakia imebakia kwenda brela kwa ajili ya kukamilisha uhamishaji wa umiliki…. Tunashukuru baba kwa msaada wako, tunashukuru sana kwa msaada wenu…”

Dada Queen alimaliza kwa kupiga magoti kama heshima ya shukrani. Na Mzee Gavana akasema…

“Sasa sikilizeni wanangu, nawasihi mkaendeleze vizuri rasilimali mlizoachiwa, na mkipata tatizo lolote msisite kunitafuta. Baba yenu alikuwa rafiki yangu sana. Nawatakieni kila la heri katika maisha yetu mapya baada ya kupitia kipindi kigumu kiuchumi…”

Alimeza funda la mate kisha akauliza…

“Je mna maswali yoyote mnataka kuuliza?” tukaangaliana na dada, kisha dada akatamka…

“Ndio baba, mimi nina maswali mawili tu kwa leo…”

“Enhee uliza Queen…” Gavana alidakia kwa shauku..

“Swali la kwanza, ni kwanini upelelezi uliishia kwenye busara ya kuacha kama ilivyo badala ya kufuata sheria? Na swali la pili ni kwa nini marehemu baba yetu tumeona alikuwa na ukwasi mkubwa lakini hatukuona akiishi katika hali hiyo ya ukwasi wala kifahari?” Dada Queen alimaliza…

“Enhe, wewe Alex una swali lolote pia!?...” aliuliza Gavana huku akinikodolea macho…

“Hapana mzee, sina, nilichotaka kuuliza dada tayari ameshauliza, lakini kuna ujumbe mfupi wa maandishi alipokea dada kwenye simu yake ukimtaka apige simu namba fulani, je hii nayo imekaaje, ina uhusiano na kifo cha baba ama mirathi hii…?”

Gavana akavuta pumzi kisha akajibu…

“Kwakweli hayo ni maswali ambayo hata kwangu mimi pamoja na mheshimiwa Jaji hatujamaliza uchunguzi wetu wa ziada, ukikamilika tu tutawaiteni ili tukupeni mrejesho, aidha kuhusu sulala la hiyo meseji sijui, hebu niione…” akanyoosha mkono akiomba simu ya dada

Dada Queen akafungua kwenye ile meseji ya pili na kumuonesha, akaisoma kisha akasema…

“Kwa kweli hata sijui, huenda ni matapeli hivyo usiitilie maanani, kama ni muhimu sana basi njia nyingine isiyotia mashaka watatumia.”

Baada ya maswali na majibu tukaahirisha kikao kile na tukapatiwa usafiri wa kurudishwa majumbani kwetu.
---

“Tulilala masikini na leo tumeamka matajiri…” Nilijisemea wakati napitia akaunti zangu kupitia njia za simu.

“Lakini hata hivyo, itanibidi ni-maintain hali hii hii niliyo nayo hadi hapo baadaye sana au hadi nikigraduate, nataka watu wasione tofauti kubwa iliyopo kati ya jana na leo…” niliendelea kujisemea na wakati huo nilikuwa naelekea maeneo ya IFM.
---

Queen kwa upande wake aliamua kuwakomesha wote waliokuwa wanamdharau, aliamua kufanya kwanza shopping ya maana ya nguo azitakazo, za kiofisi, za mitoko mbalimbali nk.

“Mbona watanikoma kudadadadeki!...” alikuta akijesemea.

“Nitanunua gari ya maana ya kutembelea, nitapanga apartment nzuri Masaki, nitaenda kuirejesha biashara yangu ya pale namanga kwa kuinunua kwa gharama yoyote, kisha nifurahie maisha na kupanga mipango ya maendeleo…”

Itaendelea…
 
Tupio la XV – Afande akubali matokeo

Ilipoishia...


Baada ya mazungumzo marefu pale, mama Omari alihitimisha kuwa mwanawe atumie tu zile hela kujianzishia biashara na wala asifikirie kusafiri kwenda huko ughaibuni isije ikawa mtego wa kuishia kwa maharamia, wakamdhuru mwanawe.

“Usije ukaenda huko ukaishia kuwa mtumwa, ama kunyofolewa figo zako ama kudhuriwa kwa namna yoyote ile, baki hapa hapa, tafuta biashara nyingine nipatie na mie niongezee mtaji wa genge langu maana hali halisi ya nyumbani si unaiona?!”

Omari akajibu…

Sawa mama, nimekusikia, ngoja nitafakari kwanza.


Sasa endelea…


Siku hiyo Afande Juma, akawahi kurudi nyumbani, wala haikuwa kawaida yake maana huwa anatumia muda mwingi huko kilabuni ama kwenye baa, alikuwa habagui sehemu ya kunywea na hurudi nyumbani kwake mida mibaya siku ikiwa tayari imeshapinduka.

Kabla ya saa tatu usiku alirudi, lakini tayari akiwa amelewa na aka kaa sebuleni na kuomba chakula. Ikabidi mama Omari amsongee ugali harakharaka maana hakuwa na ratiba ya kula nyumbani usiku.

“Leo nimefurahi sana…” kwa sauti ya ulevi baba Omari alisema…

“Mwangangu Omari leo amenivisha nguo…” Alifungua kinywa baada ya kimya fulani hivi kile cha kusubiria chakula.

Kwa muda mrefu tangia aliporudi kutoka Dafur Sudan afande Juma hakuwa na kawaida ya kula chakula cha jioni pamoja na familia yake, hivyo siku hiyo ilikuwa si jambo la kawaida kwa Omari hata kwa mama yake kumuona afende cha pombe huyo muda huo akiwepo pale sebuleni.

Wakati baba Omari anaenda kwenye fatiki huko Dafur, mke wake alimuacha akiwa mja mzito. Ulikuwa ni ujauzito mchanga ambao pia uligubikwa na sintofamau nyingi afande Juma akimtuhumu mkewe kuwa amebeba mimba nje ya ndoa.

Alivyorudi kutoka Sudan ndipo tabia za ulevi zikakithiri kiasi kilichopelekea baba kutokuwa na mapenzi na mtoto wake Omari. Hali hii ilidumu hadi siku hiyo baba Omari alipowahi kurudi nyumbani na kula chakula huku familia yake yaani mkewe na mwanawe Omar wakiwa sebuleni wakifuatilia tamthilia kwenye runinga.

“Mwanangu Omari leo umenivesha nguo…” alirudia tena ile kauli yake kwa sauti ya kilevi huku akiwa na chakula mdomoni.

Pakawa na ukimya tena, na afande Juma akamalizia kula kisha akasema…

“Mwanangu Omari, nisogezee maji ya kunawa…”

Omari kwa unyenyekevu kabisa akamsogezea maji ya kunawa kisha akamwagilizia ili baba yake anawe. Wakati huo mama Omari alikuwa kimya kama akisubiri kitu kwa shauku kutoka kwa mumewe. Mumewe ambaye aliolewa naye kwa ndoa ya kiislamu mama Omari akiwa binti mdogo kabisa wa miaka 18 na Private Juma wakati huo alikuwa ana miaka minne tangia aajiriwe jeshini.

“Leo mwanangu amenivesha nguo!” akarudia tena kusema maneno yale na kuendelea...

“Nilikuwa nadaiwa deni la muda mrefu pale Jambo Lee Bar, nimelipunguza sana lakini zikabakia elfu hamsini tu ambapo mimi leo nilikuwa nina shilingi elfu 20 tu mfukoni. Sasa nilipofika pale nimekuta meneja wa bar amechachamaa akisema nisimpomlipa leo basi suala langu atalifikisha kazini…”

Akatulia kidogo kisha akaendelea…

“Sasa kazini ‘osii’ wangu sipatani naye juzi tu ametoka ‘kunipiga gadi’ wiki kwa sababu zisizo za msingi. Sasa nilikuwa sipendi suala hili lifike kazini ndio maana nilirudi kuja kukuomba mke wangu elfu ishirini ili nikiongeza na zangu ningekuwa na elfu arobaini ningepooza kidogo labda na hiyo elfu kumi ningepata pale pale bar kwa jamaa zangu…”

Akakaa vizuri kwenye kochi kisha akaendelea…

“Sasa zile elfu nne ulizonipatia wala zisingefaa kitu, hivyo nilirudi kwa unyonge pale bar huku nikiwa na mawazo tele, kule meneja akinsubiri kwa hamu maana wakati natoka nilimwambia ngoja nikachukue hela nyumbani…”

“Nilifika pale nikiwa na elfu 24 tu mfukoni, nikawa nimejiinamia ingawaje rafiki zangu walikuwa wananipa ofa za bia lakini nilikunywa kidogo tu na nikawa nimeinama nikitafakari…”

“Nilikuwa nawaza miaka zaidi ya 22 niliyotumikia jeshi, kupanda vyeo hadi kufikia sajinitaji lakini kutokana na sababu za kinidhamu nilivuliwa vyeo na kubakishiwa mbavu moja, Koplo usu mimi naenda kudhalilika kwa sababu ya shilingi elfu 50!...”

“Yani mimi niliyefanya fatiki kadhaa katika nchi mbalimbali pamoja na utaalam wangu wa milipuko niliosomea huko ughaibuni ndio elfu hamsini inidhalilishe ofisini!?...”

“Nilikuwa nimejiinamia nawaza mengi sana ikiwemo hii hali iliyosababisha hadi mimi kuwa mlevi wa kupindukia, hii hali ya kutokuwa na uwezo wa kutungisha mimba…”

Mama Omari akashtuka na kutoa macho Omari yeye akiwa anasikiliza tu kwa makini…

“Ndiyo mke wangu, ninajuwa kuwa Omari si mwanangu, hata baba yake mzazi namjua, lakini niliamua kulewa tuu ili nisifanye jambo baya…”

“Lakini, kuanzia leo natamka hapa mbele yako mke wangu na mbele ya Omari na mbele za Mungu kuwa kuanzia leo hii Omari ni mtoto wangu, nitamlea vizuri na kumsaidia katika kuanzisha maisha yake, na wewe mke wangu nakupenda sana ndio maana licha ya kujuwa ukweli huo ambao umeniumiza siku nyingi sijakupa talaka wala kukufukuza sana sana ni maneno ya kilevi tu nikiwa nimelewa sana…”

“Leo sijalewa, nimekunywa bia tano tu tena zote za ofa. Sasa katika hali ile ya mawazo ndipo nikahisi kuguswa begani na kushikishwa kitu kama karatasi mkononi, nikafumbua macho na kuangalia mkononi ndio nikakuta noti mbili za elfu kumi kumi…”

“Nikageuza shingo na kuangalia nani aliyenipa zile hela ndipo nikamwoma mwanangu Omari amechuchumaa…”

Pakawa na ukimya na afande Juma akawa anatoa machozi… kisha akasema…

“Sikutegemea kama Omari anaweza kunifanyia wema wa namna hii… nimekuwa baba mbaya kwake, sikumjali tangia utoto wake licha ya yeye kusaidia sana katika bajeti za humu ndani, usifikiri mimi sijui…”

Akatoa leso akajifuta machozi kisha akaendelea…

“Nilivyorudi kutoka Sudan niliamua kwenda maabara kupima afya yangu ya uzazi, ndipo afande Seba akaniambia kuwa mbegu zangu za uzazi hazina uwezo wa kurutubisha mayai, kwa maana ya kwamba mimi ndiye mwenye tatizo la uzazi kwenye ndoa hii…”

“Licha ya majibu hayo sikuridhika, nikaamua kupekua kepua hapa mtaani na huko kazini lakini wapi, hata wa kusingiziwa sikupata nikaamua kunywa pombe ili nipoteze mawazo, kumbe ni balaa, nikaanza kuona ‘duble duble’…”

“Sasa kuanzia leo, kama nilivyopsema, mimi sijalewa hapa, naongea nikiwa na akili zangu timamu, wewe Omari ni mtoto wangu na nimeamua kuacha pombe rasmi.”

Akaweka kituo, pakawa na ukimya wa sekunde kadhaa kabla mama Omari hajainua kinywa chake na kusema…

“Omari, nenda chumbani kwako kapumzike, tutaongea kesho…” kisha mama Omari akasimama pale alipokaa na kumkabili baba Omari na kupiga magoti mbele yake na kusema…

“Nisamehe mume wangu…” machozi yakaanza kumtoka…

“Mawifi na ndugu upande wenu walianza maneno, eti najaza choo, sasa katika hali ya kutapatapa nikasema ngoja nimkubalie rafiki yako maana amekuwa akinisumbua kwa miezi mingi…”

“Nikavizia siku za hatari nikashiriki naye mara moja tu, miezi mitatu baadaye ndio ukaniambia kuhusu safari yako kwenda Sudani…”

Mama Omari alikuwa anaongea kwa kwikwi na kwa uchungu sana…

“Nakupenda sana mume wangu na ndio maana hujaona nikiwa na mimba nyingine tena baada ya Omari maana nilishajuwa kuwa kumbe tatizo halipo kwangu, nimekutunzia heshima muda wote na wala huyo Saidi hajui kama Omari ni mtoto wake na imekuwa bora alivyohamishiwa Kigoma.”

“Inuka mke wangu kipenzi, nimekusikia. Afande Saidi na wenzake walifariki kwa ajali ya gari huko huko Kigoma, usiwe na wasi wasi wewe ni mke wangu halali…”

Wakakumbatiana pale kisha wakabebana msobemsobe kuelekea chumbani ambako huko waliendelea kuombana msamaha kiutu uzima.
---


Usiku huo, Omari hakupata usingizi mzuri, alijawa na mawazo mengi…

“Bora niende tu huko ughaibuni…” alijisemea baada ya kutafakari kwa muda mrefu.

Akachukuwa ile barua iliyotafsiriwa na kuisoma mara kwa mara…

“Kesho nitaipeleka hii orijino kwa mtu mwingine anitasfirie nione kama Frank alinitafsiria sawa…” hatimaye akapitiwa na usingizi…


Itaendelea...
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…