Lycaon pictus
JF-Expert Member
- Jan 31, 2021
- 9,189
- 16,128
SANAA YA VITA
XII: KUSHAMBULIA KWA MOTO
XII: KUSHAMBULIA KWA MOTO
1. Su Tzu alisema: Kuna njia tano za kushambulia kwa kutumia moto. Ya kwanza ni kuunguza jeshi kwenye kambi yao. Njia ya pili ni kuchoma maghala ya adui, njia ya tatu ni kuchoma magari ya mizigo, njia ya nne ni kuchoma maghala ya silaha na ya tano ni kumrushia adui moto.
2. Ili kufanya shambulio la moto lazima tuwe na nyenzo. Zana za kuwashia moto zinatakiwa kuwa karibu muda wote.
3. Kuna msimu sahihi na siku maalumu kwa ajili ya kushambulia kwa moto.
4. Msimu sahihi ni msimu au nyakati za kiangazi na siku sahihi ni siku zenye upepo.
5. Kwa kushambulia kwa moto mtu anatakiwa kuwa tayari kwa matokeo matano.
i. Moto ukilipuka kwenye kambi ya adui fanya haraka kushambulia kutokea nje.
ii. Ikitokea moto umelipuka lakini wanajeshi wa adui wametulia basi vuta subira na usishambulie.
iii. Moto ukiwa mkubwa shambulia kama unaweza, kama huwezi baki mahali ulipo.
iv. Kama inawezekana kushambulia kwa moto basi shambulia, usisubiri moto uibuke kwenye kambi ya adui kwa bahati.
v. Ukishambulia kwa moto hakikisha upo upande upepo unakotokea na siyo upande upepo unakoelekea.
6. Upepo wa mchana huvuma kwa muda mrefu lakini ule wa usiku hutulia baada ya muda mfupi.
7. Kwa kila jeshi hayo mambo matano kuhusiana na moto yanatakiwa kujulikana, kufuatilia siku nzuri za kushambulia kwa moto, mzunguko wa nyota na misimu ni vitu vinavyotakiwa kupimwa kwa umakini.
8. Kwa hiyo, wale wanotumia moto kwenye kushambulia huonyesha akili na wale wanaotumia maji kwenye kushambulia hujiongezea nguvu.
9. Kwa kutumia maji adui anaweza kuzuiwa lakini mali zake haziwezi kupunguzwa.
10. Mwisho mbaya ni kwa yule anayejaribu kushinda pigano bila kuamsha mori wa jeshi lake. Matokeo yake ni kupoteza muda na ugoigoi.
11. Kwa hiyo husemwa, kiongozi mwenye uelewa hupanga mipango yake mapema, na jemedari mzuri hutumia vizuri alichonacho.
12. Usisonge mbele isipokuwa umeona kuwa kufanya hivyo kuna faida. Usitumie jeshi lako isipokuwa tu pale umeona kuna faida, usipigane isipokuwa hali ikilazimu.
13. Kiongozi hatakiwi kupeleka jeshi lake kwenye uwanja wa vita ili tu kujionyesha, na jemedari yeyote hatakiwi kupigana sababu tu ya chuki au hasira.
14. Ikiwa kuna faida kwako basi songa mbele. Kama hakuna faida basi baki ulipo.
15. Baada ya muda hasira inaweza geuka kuwa furaha na chuki kuwa upendo na kuridhika
16. Ufalme ulioanguka hauwezi kusimama tena wala wafu kuishi tena.
17. Hivyo, kiongozi mwenye uelewa hufanya mambo kwa umakini mkubwa na jemedari mzuri huchukua tahadhari zote. Hii ndiyo njia ya kuwa na nchi yenye amani na jeshi imara.