Taharuki ya dunia

Taharuki ya dunia

saidi bunduki

Member
Joined
Mar 10, 2018
Posts
24
Reaction score
23
Imeripuka tufana, kuvunja za watu chemba
WUHAN nchini CHINA, kumi natisa DISEMBA
Si nyingine ni Korona, ndo hii imetukumba
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

Tulisema ni wachina, itaishia ilipo
Kwa ile yao namna, ya kula mpaka popo
Leo amani hatuna, nchi zote gonjwa lipo
Dunia ni taharuki, watu tunateketea

Asia na Afrika, gonjwa limekuwa jipu
Yaongoza Amerika, kwake mjomba Trampu
Na Ulaya Kadhalika, ni shida na tabu tupu
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

COVID kumi na tisa, unaweza itamka
kila siku vipya visa, dunia yaweweseka
Ukifungua kurasa, mitandao inanuka
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

Shule, vyuo - madrasa, vimefungwa kisheria
Misikiti makanisa, tahadhari twachukua
Hali ni mbaya kwasasa, kila mtu anajua
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

Hizi ni zake dalili, ukiwa nazo UNAO
Ni kuwa na homa kali, na kuwashwa koromeo
Pia mafua makali, na joto kila uchao
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

Tuchukue tahadhari, bado tupo kwenye kiza
Janga hili ni hatari, tiba bado miujiza
Masikini na tajiri, wote unaangamiza
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

Nawa mikono vizuri, kabla kazi kuanza
tumia maji tiriri, jipake na sanitaiza
Zipo njia za asili, unaweza jifukiza
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

Jingine hili pokea, wasemalo watalamu
Jivalishe barakoa, wala usyone ugumu
Ziba mkono na pua, chafya mbele ya kaumu
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

Epuka mikusanyiko, isiyokuwa lazima
bakia nyumbani kwako, wakuu wameshasema
mlinde pia mwenzako, kwenye safiri za umma
Dunia ni taharuki, watu wanateketea

Wito wangu kwako dada, mama na bibi kizee
Tuzidishenini ibada, Kwa mungu tunyenyekee
Wala sina la ziada, naomba nitokomee
Taharuki ya dunia, Korona kizungu zungu.

LIMEANDIKWA na

mrbunduki.com
 
Back
Top Bottom