Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,872
- 34,363
Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa (kushoto), akikabadilishana hati na Mkurugenzi wa Benki ya Dunia kwa Tanzania, Uganda na Burundi, Phillipe Dongier, kwenye hafla ya kusaini mkataba wa mkopo wa dola milioni 210 za Marekani jijini Dar es Salaam jana.
Serikali imepokea msaada wa kiasi cha dola za Marekani milioni 210 (sawa na Sh. bilioni 344.6) kutoka Benki ya Dunia (WB), zitakazotumika katika ujenzi na ukarabati wa barabara hapa nchini.
Uwekaji wa sahihi katika msaada huo uliwakilishwa na Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa kwa na Mkurugenzi Mkazi wa WB, Philippe Dongier.
Dk. Mgimwa alisema fedha hizo zitatumika katika ukarabati wa barabara ya Mafinga-Igawa yenye urefu wa kilometa 140 na uboreshwaji wa barabara ya Songwe-Kasumulu kwa kujenga kituo cha kutoa huduma za pamoja katika eneo hilo.
Alisema fedha hizo pia zitasaidia kugharimia ubunifu wa miradi mbalimbali ya barabara hapa nchini na pia kusaidia kupunguza gharama za kijamii zikiwamo athari zitokananzo na barabara.
Matumizi mengine ni pamoja na kupunguza msongamano wa magari barabarani kwa kujenga barabara nyingi zaidi.
Aliongeza kuwa kiasi kingine kitatumika katika kuimarisha taasisi au vyombo vinavyosimamia usafirishaji hapa nchini.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkazi wa WB nchi za Tanzania, Uganda na Burundi, Philippe Dongier, alisema mbali na fedha hizo kutumika katika miundombinu pia zitasaidia upatikanaji wa ajira kwa wananchi.
Alisema malengo ya WB ni kuhakikisha Tanzania inakuwa na miundombinu bora ili wananchi wake waweze kusafiri na kusafirisha bidhaa kwa urahisi.
CHANZO: NIPASHE