Tukio lililonihuzunisha sana nilipokuwa mdogo miaka ya 90

Tukio lililonihuzunisha sana nilipokuwa mdogo miaka ya 90

gstar

JF-Expert Member
Joined
Jun 19, 2011
Posts
790
Reaction score
1,373
Hadithi hii nikiikumbuka natokwa na machozi, hadithi ya kweli ilitokea huko mkoani Tanga.

Wakati nikiwa mdogo mwanzoni mwa miaka ya tisini, nilikuwa nikiishi kwa wazazi wangu waliokuwa wafanyakazi wa serikalini nilikuwa na dada zangu na wadogo zangu kadhaa, huko mkoa wa Tanga vijijini. Maisha yalikuwa ya kawaida lakini tulikuwa tukiishi kwa ukaribu na majirani zetu kwakuwa tulikuwa tukiishi kwenye nyumba za serikali ilikuwa ni nyumba za quarters, nakadiria zilikuwa kama familia 10 tuliokuwa tukiishi kwa ukaribu na upamoja. Hatukuacha kucheza pamoja inapofika usiku kabla ya kwenda kulala michezo kama kombolela, kuhadithiana hadithi, mchezo wa rede hata mpira wa sodo, mchezo wa rede haukuchagua wakiume wala wakike, hata sisi wakiume tulicheza rede! Maisha hayo yalitufanya tuishi kama ndugu na kupendana kwa upendo wa hali ya juu.

Wazazi wetu waliokuwa wakifanya kazi pamoja pia walikuwa na umoja wao, niliona mara kwa mara walipokuwa wakisaidiana kwenye shida na raha hata inapotokea ugonjwa ama misiba ilikuwa wakishirikiana kwa hali ya juu sana. Nakumbuka kuna muda nilikuwa nikitumwa usiku kwenda kwa jirani kuomba kibaba cha unga kukazia ugali endapo kwetu utakuwa umeisha basi ningepewa na kujaziwa kibakuli cha unga na sisi tukisha kusaga unga tungewarudishia kwa kiasi hicho ama zaidi.

Kuhusu kuomba chumvi ilikuwa nijambo la kawaida mfano ukienda kuomba chumvi usiku ulipaswa kusema naomba dawa ya mboga na sio kutaja chumvi moja kwa moja. Hayo ndio yalikuwa maisha yetu yaliyotawaliwa na upendo na amani pamoja na umasikini uliokuwepo kwa kipindi hicho. Kuna siku tulikuwa tukisafiri usiku kwenda kijijini kwa bibi hivyo usafiri wa uhakika ulikuwa ni wa gari moshi, basi mtaa mzima walitusindikiza kwa kutubeba watoto na kutusaidia mizigo yetu na mabegi mpaka kituo cha treni maarufu garimoshi enzi hizo, nakumbuka hayo na siwezi kusahau ingawa nakadiria nilikuwa na miaka mitano tu ama sita.

Kwenye moja ya jirani yetu aliyekuwa tumeivana kiasi yeye akiwa Mpare na sisi Wachaga, tulizoea kuitana watani, basi alikuja dada mmoja kutoka mjini alikuwa msomi sana na mrembo kumtazma, ingawa mimi nilikuwa mdogo sana lakini uzuri wake naukumbuka hata kumuelezea, dada huyu alikuwa akiitwa Hamisa, tulikuwa tukimwita mamdogo Hamisa. kwa kipindi hicho nikimkadiria alikuwa aweza kupata miaka 17 hivi. Muda wote alikuwa msafi mtanashati, akipenda kuvaa mavazi ya vitenge na mitindo mbalimbali na vilemba ama wakati mwingine nywele zake alikuwa akizichoma kwa kitana cha moto zikiwa zinanyooka na kung'aa, wakati mwingine pia husuka mtindo kama kilimanjaro ama kuzichana na kufunga kitambaa kwa juu.

Hamisa alikuwa ni rangi ya maji ya kunde hakuwa mrefu sana alikuwa wa saizi ya kazi na alikuwa na umbo pana kidogo na alikuwa akitembea taratibu kwa uvivu tu lakini mcheshi kuongea kwa watoto na vijana wa pale quarters alikuwa akitupenda watoto, kila siku akienda mjini mara kadhaa hutuletea zawadi ya peremende ama big G za bublish. watoto tulimpenda Hamisa. Vijana wa kati walikuwa wakimsema kwamba anaringa ama anajisikia lakini kwa wakati huo Hamisa hadhi yake ilikuwa juu naweza kusema hivyo alikuwa mzuri ukifananisha na wasichana waliokuwa wakiishi pale kijijini.

Nashinda kukadiria elimu yake lakini huwenda alikuwa amemaliza shule ya msingi na kisha kupitia mafunzo fulani ya uchapaji kwa kutumia typewriter kwa sababu alipofika hapo kijijini alipata kazi kwenye shirika la posta lililokuwa kwenye kituo cha station ya garimoshi akawa akifanya kazi pale kama messenger wa poster. alikuwa akipokea barua na kuziweka kwenye masanduku ya posta iliyokuwepo hapo kituo cha treni, alikuwa akifanya pia kazi ya uchapaji wa barua kwa kutumia mashine ya typewriter.

Naweza kusema kwamba kazi yake ilimtofautisha na vijana wengi wakike hasa wa pale kijijini, alipotoka asubuhi kwenda kazini alikuwa amevaa vizuri sana nguo zake za kitenge alizoshona kama shati na blauzi na viatu vyake vizuri kama chachacha ama skuna alikuwa amevaa kibegi chake kwapani na kichwani nyewe zake nyeusi alizokuwa amezichoma kwa kitana cha moto na kuzifunga kwa kitambaa ama wakati mwingine akiwa amezisuka. Kwa mwendo wa taratibu alikuwa akitembea kuelekea kituo cha posta kuanzia asubuhi sana hutembea taratibu kwa mwendo wa kivivu mpaka kukatisha katikati ya mji kulipokuwa kumechangamka kiasi na taratibu akitembea mpaka kufika kituochake cha kazi.

Huko njiani vijana wakiume walikuwa wakimshangaa na kumtamani kwa uzuri wake lakini ni wachache waliojaribu hata kumsalimia kwa salamu ya habari ama umeamkaje, wengi walimpita kwa woga hawakumsalimia nadhani hakuna aliyejaribu kumtongoza kama wapo basi itakuwa ni wachache sana. Wazee walimwona kama mtoto mwenye majivuno kwa kushindwa wakati mwingine kuwapa salamu ya 'shikamoo' kutokana na aibu zake tu na uoga wa kutozoeana na watu, kumbuka kipindi hicho sifa za uchawi zilikuwa zimezagaa vijiji vingi vya mkoa wa Tanga.

Huyo Hamisa alikuwa akikaa kwa dada yake aliyekuwa ameolewa hapo ndio walikuwa Wapare na sisi Wachagga basi mara kadhaa mimi nilikuwa hapo tu nikicheza na rafiki yangu aliyekuwa wa rika langu tulikuwa kama na miaka mitano ama sita. Tulicheza stoo na kujificha kwenye magunia ya mpunga na maharage tulicheza kombolela na kukimbizana huku ama kukaa uwanjani na kuanza kuchora picha kwenye mchanga ama kukaa tu bila kazi yoyote tukisubiria kudowea "ubweche" kama wamepika. Mpaka nisikie mama yangu ama dada zangu wakiniita kwa sauti we Fulanii! ndio nitoke kwa mbio kukimbia nyumbani kesi huwa kama sijaoga kwanini nicheze kwa watu ama kwanini ninakula kwa watu ama kwanini sijamsaidia dada kazi fulani, basi naweza kupata bakora ama nisipate inategemea na mazingira.

Lakini hiyo haikuzuia mimi na watoto wengine kwenda kumzunguuka mamdogo Hamisa pindi alipotoka kazini alitoka nje kukiwa na mbalamwezi inang'aa angani na kutandika jamvi kisha kuleta redio yake na kisha kuiwasha ilikuwa redio ninayoikumbuka mpaka leo, aliweka mkanda wa 'Mimi mzabibu' kwaya iliyokuwa maarufu kwa kipindi hicho na kuna mkono wa hiyo redio alikuwa akiuzungusha redio iliimba, "Mwanadamu nilikuumba kwa mfano wangu mimi nika kuweka duniani ili usifanye makosa...!" Watoto tulikaa hapo kuusikiliza huo, mkanda mamdogo Hamisa alikuwa akizungusha ule mkono kwenye hiyo redio, redio hiyo haikutumia betrii ilitumia tu kuzungushwa kwa mkono na pindi unapoacha kuzungusha iliacha kuimba.

Hayo ni machache ninayo kumbuka lakini nakumbuka kwamba kuna kipindi kulikuwa kuna albamu ya Mchungaji Munishi iliyoitwa Malebo, dada zangu walikuwa wakifundishwa kucheza kwa kurusha maua kwenye maharusi kwa nyimbo ya 'Wanamwabudu nani' na walikuwa wakitumia redio ya kaseti aina ya Panasonic. aliyekuwa akiwafundisha alikuwa ni huyo mamdogo Hamisa.

Basi nakumbuka kuna ugeni ulitoka huko Upareni kijiji cha Ndungu. Ilikuwa ni posa ya kumuoa dada Hamisa. Alikuwa ni jamaa mmoja aliyekuwa tajiri kiasi alionekana kuwa mtu mzima kama kadirio la miaka 30 na ushee hivi lakini Hamisa alikuwa kama na miaka 18 ukimkadiria. Basi ilikuwa ni kikao kizito cha kupokea na kuidhinisha posa hiyo. Fununu zilitanda na majadiliano yalifanyika kupokea barua na kutaja kiasi cha mahari inayo hitajika ili kumuoa dada Hamisa. Wazee ndio waliokutana watoto tuliwekwa pembeni, mahari zilitajwa. Walipokuja kuleta mahari ilikuwa ni nusu sherehe ilipigwa mbiu wamama wakakutana kutwanga sembe na kisha kupika makande na ubwabwa kwa wageni waliohudhuria tukio hilo.

Nakumbuka mama alitubebea chakula kingine kwenye bakuli kubwa. Wazee wa upareni waliokuja kutoka Ndungu walimsindikiza bwana harusi mtarajiwa, na wazee wa kijijini kwetu. Baba yangu alikuwa akiheshimika sana pia kwa hivyo alikuwa ni mjumbe na msimamizi wa kusimamia mapokezi ya mahali, zilikuwa pesa na ng'ombe na mbuzi, nasema ukweli ngombe waliletwa na mbuzi waliletwa kuchinjwa ila ng'ombe walifugwa mpaka sasa ilikuwa chanzo cha ile familia kuwa na ng'ombe na mbuzi. Harusi ilisimamiwa na dada yake kwasababu upande wa mama mzazi wa Hamisa ulikuwa wamesha tengana na mzee wake na yule bibi pia alikuwa akiishi hapo hapo kwa mwanaye aliyekuwa ameolewa kwahivyo ilibidi harusi isimamiwe na upande wa dada yake.

Lakini nakumbuka harusi ilikwenda kufungwa huko Upareni, na ilikuwa mwanzo wa kutokumwona tena Hamisa kwani baada ya kuolewa alihamia kwa mumewe aliyekuwa akiishi Same mjini. Inavyo semekana harusi ilikuwa ya kukata na shoka kwa kipindi hicho kwani waliosafiri kumsindikiza bibi harusi kutoka hapo kijijini walikuja kutoa ushuhuda. Harusi ilifana sana maandamano ya matarumbeta, walichinjwa ngombe zaidi ya kumi, walipewa zawadi za kila aina vitenge na vyombo vya ndani walicheza mziki wa kanda Bongoman, walicheza nyimbo za Kipare.

Sisi watoto tulisikia juu juu na umbea wetu angalau tuliambiwa kwamba Hamisa ameolewa na mwanaume tajiri, kwa ufupi. lakini watu na wazee wa kipare walionya juu ya ndoa ya kifahari iliyofungwa huko kwani walisema kwamba watu wenye roho mbaya wanaweza kuwaroga kwa wivu wao. Hata hivyo niweze kusema huyo kijana aliyekuja kumwoa dada Hamisa alikuwa ni tajiri lakini ilikuja kujulikana baadaye kwamba alifiwa na mkewe wa kwanza kabla ya kuja kumwoa Hamisa lakini hilo halikujulikana kabla na pia kwa wakati huo haukuwepo utaratibu wa kupima afya kabla ya ndoa ukumbuke kwamba kwa miaka hiyo ugonjwa wa UKIMWI ndio ulikuwa umeingia sana na watu wengi walikufa kwa kuwa ulikuwa ugonjwa usiokuwa na dawa na hatari sana kwa enzi hizo za mwanzoni mwa miaka ya 90.

****
Iteendelea kwenye comment..
 
Inaendelea...

Basi nakumbuka ilipita kama miaka miwili au mitatu, ikasemekana kwamba dada Hamisa anaumwa sana lakini ni baada ya kujifungua mtoto na yule mtoto alikuwa nidhaifu sana na haikuchukua muda yule mtoto akafariki ambapo ilizidisha huzuni sana kwenye ile familia. Hakuna aliyejua kwamba Hamisa alikuwa akiumwa na ugonjwa gani, hata sisi watoto tulisikia watu wakisema kuwa amerogwa kwa sababu ya wivu wa watu walipoona kuwa ameolewa na mwanaume tajiri.

Yule mwanaume alilia sana, sikufuatilia alikuwa na kazi gani lakini itoshe kusema kwamba alikuwa na pesa kwani kwa miaka hiyo ya 90 kuna kipindi aliweza kuja na gari fulani iliyokuwa na mlango wa kuslide na kutubeba watoto wote kwenye gari kisha kutuzungusha mjini na kutununulia soda na bisikuti kisha kuturudisha nyumbani.

Watu waliomwona Hamisa waliona kuwa amepata mume kweli kweli, ulikuwa ni wivu kwa wasichana wa rika lake na wazee waliokuwa wakisifika kwa uchawi. Hamisa alipokuwa akirudi kusalimia kwa dada yake hakuruhusiwa kutembea barabarani kwa sababu ya woga kwamba huwenda angepigwa juju ama kuharibiwa ndoa yake. Lakini mara alipopata ujauzito na kujifungua mtoto ambaye alikuwa dhaifu na baadaye mtoto yule kufariki ndipo ilipozusha hofu na huzuni kwa familia na ukoo mzima hata sisi majirani na watoto tuliokuwa tukimpenda dada Hamisa (mamdogo) tulipoambiwa hivyo tulilia tukasema atakuwa amesha rogwa. Mume wake alilia na kugaragara, nakumbuka nilimwuona akilia alikuwa kijana mrefu mweupe mwenye mwili wa kiasi na mwenye ndevu za mtindo wa o mtanashati akiongea lakini alivyolia kwa kwikwi kwa kumpoteza mwanaye ilileta huzuni sana, wazee walimsihi kunyamaza yule mtoto alizikwa kijijini. walipouleta msiba kutoka wilayani Same.

Lakini hata ile siku ya msiba nilipomtazama dada Hamisa nilishtuka kumwona alikuwa amepooza na kuchoka sana rangi yake ilibadilika ikawa kama ya njano hivi na alikuwa amekonda kiasi, alikuwa amejitanda khanga kuanzia juu mpaka chini alikaa kwa wamama. Mama yangu alikaa naye karibu, alilia ila alionekana hakuwa na nguvu za kulia dada yake alikuwa busy kusimamia msiba ule na hata sisi watoto tulizuiwa kusogelea eneo la makaburi vijana walienda kuchimba makaburi, yule mtoto alikufa akiwa na miaka miwili tu lakini alileta huzuni kwa jamii yote.

Tulikunywa uji na viazi na mchana tukala makande tukamaliza msiba mimi nilisahau kama huumsiba umeishaishaje, ila niliona dada Hamisa akiondoka na mumewe alipokuja kumchukua baada ya siku kadhaa kupita alisindikizwa na wamama kadhaa mpaka huko mbele kijijini na kuwaacha walikuwa na gari binafsi aina ya hiace, ni ile gari yao ambayo sisi watoto tulikuwa tukiipanda na kuzunguka huko mtaani na kisha kutununulia pipi machungwa pamoja na bisikuti.

Zilipita siku na miezi kama sita hivi, ikasikika kwamba Hamisa anaumwa sana dada yake akasema aletwe kijijini ili amauuguze mwenyewe maana wamesema wamehangaika kila hospitali lakini ugonjwa hauonekani. Wakasema aletwe kijijini labda wajaribu mambo ya kienyeji huwenda akawa kweli amerogwa. Kuna watu walienda huko wakamuona Hamisa akiwa amekonda sana na hivyo alibidi atumwe mtu kwenda kumchukua.

Alikuja na mumewe ikawa amewekwa ndani, kilitengwa chumba maalumu kwa ajili ya kumuuguza walikuja waganga kutoka vijiji vya jirani wakamganga wa chale na kumpa dawa za asili waganga wote walisema amerogwa lakini kila mganga aliyejaribu kumtibu bado hali yake ilizidi kuwa mbaya. Walisema alikuwa akiharisha na kutapika na pia ngozi yake ilibadilika, lakini cha ajabu mumewake alikuwa yupo mzima wa afya mumewe alikaa kidogo kama wiki moja kisha akarudi Same kuendelea na kazi zake kwani pia zilihitajika fedha za matibabu na za kuwalipa waganga kutoka sehemu mbalimbali, Hamisa alikuwa amerogwa uchawi mkali sana.

Nilisikia wakisema kwamba anakunywa uji mwembamba wa bada tena wenye malimao mengi, na pia walimlaza kwenye kitanda cha supatu, wakaweka ndoo chini alikuwa akiharisha mfululizo. Matibabu ya waganga yaligonga mwamba. Nakumbuka nilikwenda huko ndani kwake na rafiki yangu ambaye ni mtoto wa dada yake tuka mwimbia wimbo wake alioupenda, ni wimbo alioimbiwa siku ya harusi yake. "Hamisa hamisa hamisa dada ...." (sikumbuki maneno mengine yalikuwa ya lugha ya Kipare)

Haikuchukua muda alikuja akafariki akatuachia huzuni nyingi sana. mumewe alikuja kwenye msiba alilia kwa kwiwi na majonzi mazito, alitoa lawama kwa upande wa mkewe kwa kushindwa kumsaidia alipokuwa akimuuguza mkewe hapo mwanzo. Alilalamika na kuongea mambo mengi. wanakijiji walifika nakumpumzisha Hamisha, alikuwa amekonda na kubaki mifupa mitupu, wengi wakiamini kwamba binadamu ndio waliofanya kitendo hicho. "Binadamu wabaya wamemuua hamisa kwa ajili ya wivu juu yake."

Hadithi hii ilinihuzunisha sana kwa kipindi hicho, hata mimi nililia siku ya msiba japo nilikuwa mdogo, nilielewa kila kitu. Bada ya kuwa mtu mzima ndio nilitambua kuwa dada Hamisa alifariki kwa ugonjwa wa UKIMWI, pamoja na uzuri wake na kujitunza kwake lakini alijiingiza kwenye janga lililochukua uhai wake, hakuyafaidi maisha kama alivyotegemea, maisha yake yalikatishwa kwa mteso makali, alifariki kwa UKIMWI kipindi ambacho jamii ilikuwa haija elimishwa vyakutosha juu ya janga hili, kipindi ambacho imani za kishirikina zilishika kasi na kwamba kila ugonjwa ulioonekana usiotibika basi watu waliuhusisha na imani za kishirikina, mumewake aliondoka lakini nilisikia kwamba naye hakuchukua miaka mingi aliumwa na kuaga dunia. Ingawa ni miaka mingi imepita lakini bado siwezi kusahau tukio hili, matukio mengi ya namna hii yaliacha simanzi kwenye jamii nyingi za kiTanzania.

MWISHO
 
Hamisa Mobeto

Bado sijaona tukio

coz ukimwi umeua wengi kuliko hao kina hamisa

Mie mwenyewe sijapima bado
 
ukimwi umeua wengi sana bila kujua. jamii izidi kuelimishwa kuhusu hili gonjwa hatari.
 
UKIMWI wa zamani ulikuwa hatari sana. Nilimuonaga dada mmoja miaka ya 1980 au early 1990's aliletwa nyumbani kwao akiwa ameathirika, inaniumizaga hadi leo.

UKIMWI bado upo ila mzungu kajitahidi kupunguza makali na mateso ya ugonjwa huo. Watu waliteseka sana zamani.
 
Huu ugonjwa hakuna familia haujapiga, nakumbuka marehemu anko tulivyohangaika miaka ya mwishoni 90 waganga wotee madawa yoteeee, mpaka mara ya mwisho anko alipewa nyama ya simba( hii ni baada ua kupigwa stroke ,mganga akasema nyama ya simba ni dawa ya stroke)

Hangaika weee aisee ukimwi ule kama ungekuwepo mpaka sasa nna uhakika kila mtu angepoa ,elimu ya kuenea ilikua ndogo dah sio kuharisha kule,sio kukonda kule😟😟😟
 
Back
Top Bottom