Tatizo la watanzania ni pale tunapomfanya Nyerere kama kanuni ya imani. Wakatoliki wananielewa vizuri ninaposema hili. Wakati nikianza mafundisho ya ubatizo tulikuwa na mtihani ambao pamoja na sara zingine ulitakiwa kuijua vizuri kanuni ya imani ambayo inasema nasadiki kwa kanisa katoliki la Rumi. Nasadiki kwa Mungu baba mwenyezi. Nasadiki, Nasadiki, Nasadiki.
Mawazo yako ukiyaweka katika kuamini kwamba hii ndiyo imani uliyoingia kamwe hutaruhusu kusikia upinzani dhidi ya kile ulichokiamini. Wakatoliki watupu wakiingia katika mjadala juu ya imani ya matumizi ya rozari kamwe hatutegemei upande wa pili katika rozari hiyo. Wasabato wawili watupu katika mjadala juu ya ibada ya siku ya jumamosi kamwe hatutegemei kuiona kasoro ya uhakika wa siku hiyo, hali kadharika mashehe wawili wenye imani juu ya mtume hawataweza kuja na jipya juu ya kasoro ya mtume kwa sababu tu kwamba wako ndani ya kanuni moja ya imani.
Inahitaji msuli na ubabe wa hali ya juu kusimama katikati ya watu walioiva katika kanuni ya imani ya matumizi ya rozari ukaanza kuikosoa, Tegemea ukweli alioubainisha "Henrick Ibsen" katika kitabu chake "An Enemy of the Peole". Utaitwa adui mkubwa wa watu kwa sababu umetamuka jambo ambalo watu hawataki kulisikia. Wenye msuli wa hivi mara nyingi humaliza vibaya. Huishia kupotea kabisa kwa sababu hata walio karibu nao hawako tayari kuonyesha kuungana nao kwa sababu wanajua kanuni ya imani iliyo katika jamii wanayopambana nayo. Kama ni ukweli bado utabaki kuwa ukweli lakini dhahili itaonekana wakati wewe tayari umeshapotea katika jamii. Umeshabwagwa kama msaliti.
Nyerere alikuwa binadamu hivyo kuna kasoro alizozifanya, lakini kwa vile ni kanuni ya imani kwa wengi hakuna mwenye ujasiri wa kutamuka kasoro zake. Ukiruhusu akili zako zimuone kama binadamu utaona kasoro zake nyingi tu za ubinadamu.
Kwa mfano: Nyerere kama kiongozi na mdau mkubwa wa muungano wa dunia tangu katika wazo walilokuwa pamoja na Nkrumah kuunganisha Afrika nzima, dunia ilimshangaa alipokubaliana na waasi wa Biafra waliotaka kujitenga kutoka Nigeria. Hiyo ni kasoro ambayo kama akili yako haijaruhusu kanuni ya imani utaiona na kusema kweli binadamu mwenzangu alikosea.
Nyerere aliwahi kusema katika moja ya Bith day part yake kwamba watanzania wananiombea niishi miaka mingi wakati sayansi inasema miaka kuanzia 80 ni ya shida. Nami nashukuru na kwa afya niliyonayo naamini nitafikisha na kuiona 2000. Kama akiri yako haiko katika kanuni ya imani utaiona kasoro kubwa ya ubinadamu wa kutokujua kwamba Mungu ndiye anaamua. Matokeo yake Nyerere hakuiona 2000. Kama akiri yako iko katika kanuni ya imani utapata tafsiri nzuri. Waweza kusema alikuwa akiwafariji watanzania, au lolote la kupamba kauli hiyo.
Tatizo langu kwa Lissu ni uchaguzi wa maneno ambayo unaweza ukatoa ukweli lakini bado ukaacha faraja kwa wadau wa kanuni ya imani. Anayoyasema yote ni kweli. Kuna sababu gani ya kutokuonekana Abdul Jumbe katika matukio mengi ya kitaifa wakati yuko hapa Mji mwema?
Nani aisiyejua kwamba wasira aliwahi kumwendea Nyerere akimfahamisha kwamba safari hii warioba hataupata ubunge kwa sababu watu wamechoka na mikono mitupu. Nyerere kwa kauri hiyo alizunguka majimbo yote ya mkoa wa Mara akiwaambia wasira ni mtoa rushwa mkubwa. Anachinja ng'ombe, anagawa kanga, chumvi ili kupata ubunge jimbo la Bunda. Akawaambia wasira hafai. WARIOBA anafaa. Haya niliyasikia mimi mwenyewe uwanja wa sabasaba Bunda. (kumbuka Lissu alisema kuna watu waliingia upinzani mpaka Nyerere amekufa ndio wakarejea CCM).
Kwa vile siasa inakutaka uwe mnafiki, sasa hivi wasira ndiye mpinga rushwa mkubwa. Ndiye wa kumuenzi baba wa taifa. Sijui kama rushwa alishaacha au lah.
Ndio maana mara nyingi nimekuwa nikisema katika ngazi ya uongozi wa kitaifa lazima uwe mnafiki na wakati mwingine hata mbinu chafu za kuhakikisha msimamo unaouamini kwamba ni muafaka unakubalika katika jamii. Haya yote wanayafanya wanasiasa akiwemo Nyerere na hawa tulionao leo. Hata Lissu akiingia madarakani lazima awe mnafiki na mzoefu wa mbinu chafu.
Namaliza kwa kumwambia Lissu umegusa kwenye kanuni ya Imani, tegemea mashambulizi mengi. Usiposimama imara utapotea. Mbowe, Slaa, Zitto, Mnyika hawatakutetea kwa sababu wanaogopa kugusa kanuni ya imani.