Ukweli wa kuwepo, kutokuwepo mitalaa nchini

Dingswayo

JF-Expert Member
Joined
May 26, 2009
Posts
4,019
Reaction score
2,925
Nimeona niiweke hii kwa kuwa kulikuwa na maswali yaliulizwa hapa kuhusu nini hasa maana ya mtaala na madhumuni yake.

Na Profesa Hermes Mosha

Ukweli wa kuwepo, kutokuwepo mitalaa nchini - Makala - mwananchi.co.tz

Katika kikao cha Bunge kilichopita, kulizuka mjadala kama sekta ya elimu nchini ina mtalaa au la.

Kwa vile moshi kuhusu mjadala huu bado unaendelea kufuka, nimeona ni vyema nitoe ufafanuzi wa kitaalamu ili kuwaridhisha wote wenye dukuduku kuhusu ukweli wa jambo hilo.

Ili kuweza kuelewa vizuri mtalaa ni nini, ni lazima tuelewe tofauti zilizopo kati ya dira na falsafa ya taifa, sera ya elimu, mitalaa, mihtasari ya masomo, mpango wa kazi, na andalizi la somo, kwani dhana hizi zote zinarandana.

Dira ya Taifa hujumuisha matamshi ya kina kuhusu matarajio ya maono ya taifa, kuwa tunataka taifa la aina gani, tuseme ifikapo mwaka 2015. Pia inatamka bayana falsafa ya Taifa ni nini.

Mtu akichunguza kwa karibu Dira ya Taifa hadi kufikia mwaka 2025, ataona inatamka bayana kuwa falsafa ya Tanzania ni kuwa taifa ambalo wananchi wake wote wana maisha bora, kuna amani, utulivu, umoja, utawala bora, watu walioelimika na wanaoendelea kujielimisha, uchumi shindani unaoweza kuchochea ukuaji wa haraka na wa kudumu kwa manufaa ya wote.

Tanzania pia ina kusudio la kuwa taifa la watu wabunifu na lenye kutoa elimu bora kwa idadi kubwa ya watu wake, ili waweze kuwa na uwezo wa kuyatatua matatizo yanayoikabili nchi yao, kuwaletea maendeleo ya haraka na kuwa na uwezo wa ushindani barani Afrika na duniani.

Sambamba na Dira ya Taifa, sera ya elimu ya mwaka 1995, inatoa mwongozo wa jinsi elimu inavyoweza kuwa kichocheo cha kutekeleza dira hiyo, kwa kuoanisha na kubainisha mfumo wa elimu, mipango na utekelezaji wake kwa kuhakikisha kuna ongezekao la udahili, usawa, uwiano na ubora wa elimu inayotolewa kwa kila ngazi ya elimu.

Mtalaa ni nini?

Mara nyingi mitalaa hutokana na sera ya elimu. Neno mtalaa, linatokana na neno la Kilatini ‘Currere’ au kukimbia. Katika taaluma ya elimu, neno hilo linamaanisha mpango wa mafunzo ambayo mwanafunzi anapaswa kupata ili awe mkamilifu katika ngazi fulani.

Hata kabla ya elimu hii ya shuleni, elimu yetu ya jadi ilikuwa na mtalaa wake katika ngazi mbalimbali kuhusu maarifa, stadi, maadili, maono na ujuzi ambayo anayepita mtalaa huo anapaswa awe amepata amalizapo mafunzo yale, ili aweze kuwa mtu anayejiamini, anayejituma na anayetoa mchango mkubwa katika sehemu ya kazi ama anapoishi.

Kwa ufupi, mtalaa unajumuisha yale yote ambayo mwanafunzi anapaswa kujifunza na kuyafahamu katika ngazi mbalimbali za elimu. Wataalamu wa elimu wameweza kubainisha aina tano muhimu za mitalaa.

Moja, mtalaa rasmi. Huu ni ule mtalaa unaoandaliwa na Wizara au vyuo vikuu kuhusu aina ya mafunzo yanayopaswa kutolewa katika ngazi husika. Viongozi, walimu wa shule, vyuo na taasisi wanapaswa, wayazingatie na wanafunzi wajifunze.
Mbili, mtalaa unaotundisha. Huu ni ule ambao mwalimu mmoja mmoja anaufundisha, ukizingatia changamoto za mazingira, ubora wa elimu yake, mtazamo juu ya wanafunzi na uhusiano wa kila siku.

Tatu, mtalaa anaojifunza mwanafunzi. Huu unatokana na jinsi wanafunzi wanavyoandaliwa na walimu ili waweze kujenga ari ya kuwa wasikivu, kuuliza au kutokuuliza maswali, kujifunza kuheshimiana au kutokuheshimiana. Hivyo mtaala anaojifunza mwanafunzi ni mpana zaidi wa yale anayofunzwa.

Nne, mtalaa unaotathminiwa. Hii ni sehemu ndogo tu ya mtalaa rasmi ambapo maswali yanatungwa kufuatana na ujuzi wa kutunga mitihani ya yule anayetahini. Japokuwa walimu na Baraza la Mitihani wanaweza kuhakikisha maswali yanatokana na vipengele mbalimbali na kutumia aina mbalimbali za maswali, mara nyingi ni sehemu ndogo tu ya mtalaa inayotahiniwa katika kuainisha ubora halisi wa mwanafunzi.

Tano,mtalaa usio bayana. Kuna mambo mengi muhimu ambayo mwanafunzi anajifunza shuleni ambayo hayako bayana kwenye mtalaa rasmi. Mwalimu Nyerere kwa mfano alisisitiza mambo ya utii, nidhamu, kujifumza na kujenga moyo wa kushirikiana. Haya ni mambo mema yanayokamilisha maisha ya mwanadamu, hayafundishwi lakini shule nzuri huyawekea mkazo.

Aidha, mtalaa wowote mzuri una sehemu kuu nne. Mosi, malengo ya elimu katika ngazi husika. Malengo haya yanatokana na sera ya elimu na kurudiwa kwenye mitalaa na mihtasari ya masomo.

Pili, idadi ya masomo na yapi yanapaswa kufundishwa katika ngazi mbalimbali. Mara nyingi hii hubainishwa na miongozo mbalimbali inayotoka kwa Kamishna wa Elimu kila kunapotokea uamuzi wa kuongeza au kupunguza masomo.

Suala kubwa hapa ni kwa nini tuwe na masomo kadhaa tangu darasa la kwanza, wakati huko nyuma miaka miwili ya mwanzoni ilitilia sana mkazo kwenye misingi ya K tatu yaani kusoma, kuandika na kuhesabu? Hapa ndipo tatizo la wanafunzi wasiojua kusoma, kuandika na kuhesabu linapotokea.

Tatu ni mbinu za kufundishia ambazo zinaweza zikawa zinamtegemea mwalimu (teacher based) au zile zinazomlenga mwanafunzi (student based). Hizi hutenganisha au kuunganisha nadharia na vitendo.

Nne ni namna ya kutathmini, iwe kwa kutumia mtihani wa mwisho au kufikiria jumuisho la mazoezi, tabia na mitihani ya mwisho. Kila mbinu ina matatizo yake. Vitu vyote hivi vimebainishwa katika sekula mbalimbali na katika ngazi ya chuo kikuu, vipo katika kalenda za vyuo.

Kimsingi, mambo haya ndiyo yanawaongoza watunga mihtasari mbalimbali na watunga mitihani katika kazi zao.

Sambamba na mitalaa kuna mihtasari ya masomo. Hii huandaliwa kwa kila somo litakalofundishwa kama ilivyobainishwa kwenye mtalaa. Hupambanua mada muhimu, kiwango cha uwezo, malengo yanayotarajia kufikiwa, mada kuu na mada ndogo, mbinu zitakazotumika kufundishia, zana kufundishia, mbinu za kutathimini na idadi ya vipindi.

Mpango kazi. Ni mkakati wa kutekeleza mtalaa. Mara nyingi huandaliwa kwa mwaka mmoja, muhula au semista moja. Mpango kazi unapaswa uainishe malengo, mada, kazi na majukumu ya mwalimu na ya wanafunzi, zana za kufundishia na namna ya kupima kiwango cha uelewa. Hata hivyo, ufundishaji wa siku hadi siku unaongozwa na andalizi la somo.

Inaendelea chini
 
Andalizi la somo ni mwongozo wa kufundishia kipindi kimoja darasani. Andalizi la somo linapaswa libainishe jina la somo, tarehe, darasa litakapofundishwa, muda, idadi ya wanafunzi, uwezo ambao mwanafunzi anapaswa kuwa nao baada ya kipindi, mada kuu na mada ndogo, lengo pana, malengo mahsusi, zana na vitabu vya rejea.

Pia hubainisha hatua muhimu kama utangulizi, maarifa mapya, namna ya kukazia maarifa, muda wa kufundisha, kazi za mwalimu na kazi za mwanafunzi na mbinu za kutathmini mafanikio ya kila hatua, upimaji wa mafanikio ya somo, mwanafunzi na mwalimu; hatimaye kuna maoni.

Je, Tanzania ina mitalaa?

Tukirejea kwenye swali la msingi kama mfumo wa elimu nchini una mitalaa rasmi au la?, jibu ni ndiyo ipo. Hakuna nchi yoyote duniani ambayo inatoa elimu bila kuwa na mtalaa.

Hata kabla ya elimu ya mkoloni, elimu ilikuwa na mtalaa wake, yaani yule aliyepitia jando au unyago alipaswa kuyaelewa na kuyatenda baada ya mafunzo yake.

Suala muhimu ni je, mtalaa huo unatosheleza kuwaandaa wanafunzi barabara kwa elimu katika ngazi husika, Je, ni wa kisasa na unatekelezwa vizuri? Au umeandikwa kwenye kitabu chenye namba ya ISBN na kutiwa sahihi na Mkurugenzi au Kamishna?

Ukichunguza vizuri utagundua kuwa Kijitabu cha Katiba ya Jamhuri ya Tanzania ni rasmi, lakini hakina namba ya ISBN. Pia Japokuwa Tanzania ina chapisho la katiba yake, nchi kama Uingereza haina katiba iliyoandikwa.

Ni lazima upitie nyaraka mbalimbali ili kuweza kupata Katiba hiyo. Lakini bado Uingereza ni mojawapo ya nchi zenye demokrasia kubwa duniani.

Hivyo katika shule za awali hadi sekondari, mara nyingi ni vigumu kuweza kupata juzuu moja yenye mitalaa ya elimu katika ngazi zote.

Hata hivyo, mitaala yote ya vyuo vikuu inapatikana katika kijitabu kinachojulikana kama Kalenda ambayo hutolewa mara moja baada ya miaka mitatu au minne. Lakini ni lazima ifahamike kuwa mtaalaa una sehemu kuu nne kama tulivyoona hapo awali.

Pia tunapaswa kujiuliza je, mitaala iliyopo inatekelezwa vizuri? Je, mtaala wa shule za msingi unahusishwa vipi na ule wa sekondari na elimu ya juu; au ule wa ualimu?

Je kuna utaratibu mzuri wa kuwaandaa walimu kazini na wanaotunga mitihani, ili kuhakikisha kuwa mitaala mipya inatekelezwa vyema na kutathminiwa vizuri? Kama hivyo vyote havifanyiki ipasavyo, nini kifanyike kuhakikisha haya yote yanatendeka kwa usahihi?
 
Je, Tanzania ina mitalaa?

Tukirejea kwenye swali la msingi kama mfumo wa elimu nchini una mitalaa rasmi au la?, jibu ni ndiyo ipo. Hakuna nchi yoyote duniani ambayo inatoa elimu bila kuwa na mtalaa.

Naona huyu jamaa amelezea vizuri kwa undani ila kwenye jibu muhimu ameleta siasa...., Tatizo ni kwamba hata kama hiki kitu kipo theoretically lakini hakipatikani kwa wale wanaokihitaji (waalimu, au wengine hawajawahi kuona hata hicho kitabu cha kuwaongoza..) whats the use...
 
Mimi nafikiri suala zima la kuwepo ama kutokuwepo kwa mitaala, ama kuwepo kwa mitaala inayokidhi ama isiyokidhi matakwa ya taifa letu ni matokeo ya kukosekana kwa dira, sera ama itikadi (vision, policy or ideology) kwa Tanzania ya sasa.

Baada ya uhuru serikali ilifahamu ya kuwa tunahitaji wataalamu katika kila nyanja. Ukweli ni kwamba mpaka tunapata uhuru Tanzania tulikuwa hatuna Chuo Kikuu hata kimoja. Watu wote waliopata shahada zao kabla ya Uhuru ikiwa ni pamoja na baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, walizipata shahada zao kutoka nje ya nchi, hususan Makerere Uganda, Uingereza na Marekani. Mwalimu alipata M.A. kutoka Edinburgh Scotland. Daktari wa kwanza mtanzania Dr. Mwaisela alipata shahada yake ya Udaktari kutoka Marekani. Ikumbukwe ya kuwa katika kumuenzi hata hospitali kubwa kwa wakati huo ilipofunguliwa na Princess Margareth wa Uingereza jengo zima la wadi liliitwa Mwaisela, jina ambalo linatumika mpaka leo hii, ingawa hiyo historia haiongelewi tena.

Kwa kutambua mapungufu yetu serikali iliazimia kuweka misingi ya kujitosheleza kwenye elimu ya juu, na kuanzisha Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam, wakati huo kilikuwa Mtaa wa Lumumba. Kwa hiyo tayari dira yetu ilikuwa kuwa na wataalamu wazawa waliosoma hapa nchini, na sera ikawekwa kufikia malengo hayo.

Baada ya Azimio la Arusha na kutangazwa kwa siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, sera nzima ilifanyiwa mabadiliko. Sera ya Elimu ya Kujitegemea ilianzishwa. Nia ikawa siyo tu kupata wataalamu wazawa waliosoma hapa nchini, ila ni kuwaandaa watanzania katika kutekeleza sera zitakazolenga katika kujitegemea. Kujitegemea huku hakukuwa tu kwenye vitabu vya siasa, bali ilikuwepo nia ya dhati ya kuhakikisha ya kwamba baada ya miaka kadhaa Tanzania iondokane kabisa na kuhitaji kuagiza 'wataalamu' kutoka nje kuja kutufundisha ama kutusaidia kutatua matatizo yetu. Elimu ilikuwa imelenga kumfanya mtanzania ajitegemee yeye mwenyewe, na nchi ifike mahali iweze kujitegemea kwa kuwa na wataalamu wakutosha katika fani na nyanja mbalimbali. Hapo ndipo wengi wetu tulipopata nafasi za kusoma kufikia upeo wetu. Tukapata madaktari, wahandisi, wataalamu wa kilimo, wataalamu wa madawa (pharmacists), walimu, manesi, mafundi mchundo, wanasheria, waandishi wa habari, marubani n.k. Ni kweli mganga hajigangi, na kuna nyakati kila mtu atahitaji msaada kutoka kwa mtu mwingine, hata kwa taifa ni sawa, lakini ilifika mahali tukawa na wataalamu wetu katika kila nyanja muhimu.

Tulipofika sasa hivi baada ya Azimio la Arusha kutunguliwa kwa mizinga na wachache kwa maslahi yao, ni kuiacha ile dira ya maendeleo tuliyokuwa nayo na kuacha elimu iendeshwe na vipofu. Nchi haina itikadi, dira wala sera za kusimamia elimu tunayotaka kuitoa kwa watu wetu. Inasikitisha sana kuona mpaka leo hii bado tunapeleka wagonjwa kutibiwa nje ya nchi hususan India, Afrika Kusini n.k, wakati mwaka jana madaktari wanafunzi walifukuzwa kwa kugoma wakidai hali nzuri zaidi za kufanyia kazi... Halafu bila aibu serikali inaunda tume kuchunguza kwa nini watoto wetu wanafeli mitihani. Hakuna sera iliyo wazi katika elimu, tunataka nchi ya watu wa aina gani, tunawaandaa vipi watanzania wa kesho, tunawaandaa vipi walimu wetu ili waweze kutoa elimu iliyo bora kwa ajili ya watanzania wa karne ya ishirini na moja na karne zijazo.

Malumbano ndani na nje ya Bunge hayatamsaidia mtanzania kama yasipokwenda sambamba na mabadiliko katika fikra za watu walioko madarakani na waliokabidhiwa majukumu ya kutunga sera ili watutafutie muarobaini utakaotutoa hapa tulipo sasa. Ni lazima turudi kwenye ubao (drawing board) na kuweka bayana dira yetu, sera yetu na itikadi yetu itakayoweza kutpeleka kule tunakotaka kufika. Lazima tuwe na mipango inayolenga miaka mitano, kumi ama zaidi, tunataka Tanzania ya kesho na kesho kutwa iweje. La sivyo bora tu tutangaze kabisa ya kuwa tuna uhaba wa wataalamu kwa hiyo tutaomba wawekezaji kutoka nje waje kutusaidia hata kutunga sheria ikiwemo na kutuchagulia viongozi. Hofu inanijia kila mara ninapofikiria itakuwaje baada ya miaka kadhaa, wakati wale wanafunzi asilimia zaidi ya 60 waliofeli watakapokuwa wao sasa ndiyo wako kwenye madaraka. Tusishangae itakapofika wakati hata Rais wa Tanzania hajui kusoma wala kuandika... ndivyo tulivyomwandaa! Atajua sana kuimba Bongo fleva, kuita wawekezaji kutoka nje na kutembeza bakuli kuomba huku na huko! Tunasema mababu zetu walikuwa hawakusoma wakauza nchi kwa wakoloni. Hao tunaweza kuwasamehe, hawakujua walilokuwa wanalitenda. Lakini hawa wanaotupeleka huko ilhali wanafahamu fika matokeo ya matendo yao, ninachoweza kusema ni ole wao!

Nguvu ya umma haitawasamehe!
 

mitaala ipo ila ina mapungufu mengi haswa kutotambua vipaji vya wanafunzi na kuwalazimishia vipaji ambavyo siyo vyao.
 
mkuu nimekusoma vizuri sana na nimepata elimu kuhusu mambo hayo. hebu naomba tafsiri ya maneno haya Syllabus na curriculum kwa kiswahili kisha tofauti zake halafu yanahusianaje na mtaala?
 
Tafadhali usiandike kitu kama hujui kinaandikwaje,ona sasa mi nikuwa hata sijui unazungumzia nini! Kumbe unamaanisha MTAALA! Mawazo yako ni mazuri
 
Kuwasaidia jamani neno mtalaa lililotumiwa na mwandishi halina makosa, Kiswahili hicho kinakubalika ila hata ukisema mtaala kama wanavyotumia wengi wetu bado hakuna makosa. Hilo laonyesha utajiri wa Kiswahili. asanteni
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…