Ushairi: Undugu ni kufaana

ramadhani kimweri

Senior Member
Joined
Apr 22, 2016
Posts
181
Reaction score
179
UNDUGU NI KUFAANA.

Undugu ni kufaana, wala sio kufanana,
Na mikono kushikana, mambo kushirikiana,
Mapenzi na kupendana, wala si kuchukiana,

Undugu wa kugombana, kwangu hauna maana,
Hadharani kutukana, na kudharauliana,
Hilo nalipinga sana, kwangu nasema hapana,

Undugu ni raha bwana,kwa watu wakipendana,
Ni furaha kukutana, salamu tukapeana,
Si vema kuchukiana, njiani mkapishana.,

Ndugu wakikoseana, kheri ni kuambiana,
Kisha kusameheana, na kutubu kwa rabana,
Na mema kuombeana, kwa mola subuhanna.

Ndugu kusaidiana, ila sio kuchekana,
Pamoja tukiungana, tutafika mbali sana.
Ni ushamba kutengana, pembeni kusengenyana.

Mimi nachukia sana, ndugu wakibaguana,
Kutokuheshimiana, mabaya kuombeana,
Na ukiwa pesa huna, watakukimbia mbona.

Sitaki kusema sana, muhimu kukubushana,
Nasaha tukapeana, pia kuelimishana,
Pamoja tukaungana, malengo kufikishana..

[emoji2400]IBN KIMWERI(BABA JUMA)
Ramadhanikimweri7@gmail.com
MOSHI – KILIMANJARO.
• TANZANIA.

Mashairi mengine soma Shairi: Hakuna siri tena
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…