Viunganishi (U) na aina zake

Viunganishi (U) na aina zake

Suley2019

JF-Expert Member
Joined
Oct 7, 2019
Posts
2,203
Reaction score
5,610
Salaam Wakuu, tunaendelea na somo letu la aina za maneno. Katika andiko hili tutachimba kiasi katika maana na aina za Viunganishi. Twende pamoja hapo hapa chini:

VIUNGANISHI
Viunganishi ni maneno yanayotumiwa kuunganisha vipashio mbali mbali vya lugha. Kwa kawaida, huunganisha vipashio vifuatavyo:
  • Neno na neno
  • Kirai na kirai
  • Kishazi na kishazi
  • Sentensi na sentensi
AINA ZA VIUNGANISHI

1. Viunganishi vya sababu

Viunganishi hivi huunganisha hali moja na sababu yake. Kwa mfano, aliadhibiwa kwa sababu alichelewa.

2. Viunganishi vya masharti
Viunganishi hivi huunganisha hali na masharti ya hali hiyo. Kwa mfano, iwapo atamaliza mitihani mapema, ataenda kwa shangazi yake.

3. Viunganishi vya tofauti
Viunganishi hivi huonyesha tofauti baina ya kitu/hali moja na nyingine. Kwa mfano, wanafunzi wote wamefaulu mtihani isipokuwa wanafunzi wawili.

4. Viunganishi vya kuteua
Hivi hudhihirisha uchaguzi au uteuzi baina ya vitu viwili au zaidi. Kwa mfano, utaenda Malindi au Lamu?


5. Viunganishi vya ziada
Hivi huonyesha hali au vitu vya ziada, licha ya vile vilivyotajwa mwanzo. Kwa mfano, na, pia, aidha, licha, pamoja na.

Mifano katika sentensi:
  • Alikula chapati, viazi vya nazi na sambusa.
  • Licha ya kuwa mwanauchumi, ni mwandishi.

6. Viunganishi vilinganishi
Hivi hulinganisha vitu viwili au zaidi. Kwa mfano: Sembuse, kuliko, zaidi ya, seuze.

Mifano katika sentensi:
  • Anapenda chapati kuliko wali.
  • Umeshindwa kuamka saa moja asubuhi, seuzi saa kumi alfajiri?
Pia Soma:
 
Back
Top Bottom