Wafahamishe wengine yale mazuri

Wafahamishe wengine yale mazuri

kbm

JF-Expert Member
Joined
Oct 5, 2012
Posts
5,224
Reaction score
1,677
Endelea kujifunza Kiswahili na kama ikiwezekana uwafahamishe wengine yale mazuri unayoyapata unaposoma makala haya. Angalia sentensi zifuatazo:
“Alisema mbali na suala la menejimenti lakini pia kulikuwa na matatizo ya mvua kubwa kunyesha kuliko kiwango kilichotarajiwa.”
Matumizi ya neno ‘lakini’ mara nyingi hutumika visivyo. ‘Lakini’ hutumika kama ni kiunganishi cha mafungu ya maneno katika sentensi. Lilivyotumika sasa ni makosa. Tunaweza kuliondoa neno ‘lakini’ bila kuathiri maana iliyokusudiwa. Kwa mfano:
“Alitaka kujua mpango wa Serikali wa kujenga kwa kiwango cha lami barabara za ndani ‘ring roads’(barabara za pembezoni) katika jiji hilo.”
Hakuna umuhimu wa kutumia maneno ya Kiingereza kama ‘ring roads’ kwani wasomiaji wa magazeti ya Kiswahili wana elimu ya kawaida. Hivyo mwandishi alitakiwa kutumia maneno kama ‘barabara za pembezoni’ na kwa ufafanuzi kutumia ‘ring roads’ ingesaidia kushadidia hoja hiyo.
“ Katika shoo hiyo, itasindikizwa na Ben Pol anayewania tuzo sita kwenye Kil Muzic Awards.”
Siyo kawaida kwa msanii kusindikiza shoo bali ni msanii hushiriki katika shoo. Kwa hiyo isomeke,
“Katika shoo hiyo, itahudhuriwa na au atakuwapo Ben Pol anayewania tuzo sita kwenye Kili Muzic Awards.”
“Mwigizaji anayefanya vizuri kwenye tasnia hiyo kwa sasa Recho Haule au Recho Saganda amesema yeye ni jike la shamba.”
Maana ya ‘tasnia ‘ ni shughuli za biashara zenye kutoa huduma kama vile utalii au usafirishaji. Uigizaji ni tasnia ? Hii ni sanaa yenye malengo mawili. Kwanza ni burudani na pili ni biashara. Kwa kuwa ni sanaa kwa sehemu kubwa ni burudani.
Ingefaa iandikwe,
Mwigizaji anayefanya vizuri kwenye sanaa kwa sasa ni Recho Haule au Recho Saganda amesema yeye ni jike la shamba.”
“ Tofauti na miaka mingine yote ya nyuma, Mtibwa inatumia Viwanja vya Manungu Complex nyumbani ina Jamhuri.”
Bado iko haja ya kufafanua zaidi sentensi hii ili ieleweke vizuri hasa pale alipoandika ‘nyumbani ina Jamhuri’. Angeandika,
“Tofauti na miaka mingine yote ya nyuma, Mtibwa ambayo inatumia Viwanja vya Manungu Complex, kwa upande wa nyumbani inatumia Uwanja wa Jamhuri.”
“Uchumi wa Tanzania unatarajiwa kuimarika kufuatia jitihada zinazofanywa na Serikali kupuguza mfumuko wa bei kufikia digiti (dijitali) moja.”
Kwa muda mrefu nimejitahidi kuwaelekeza waandishi kuwa matumizi ya neno ‘kufuatia’ linavyotumika siyo sahihi. Ni mazoea ya watu wengi kulitumia vibaya na hivyo kushindwa kujirekebisha kutokana na mazoea. Ni sahihi kuandika kuwa uchumi umeimarika kutokana na jitihada za Serikali. Kwa kawaida ‘kufuatia’ kiini chake ni kufuata na maana yake ni andama, enda au kuja nyuma
“uzinduzi wa maonyesho ya siku tatu ya OUT ambayo yanaendelea kwenye mjini hapa.”
Kwanza ni wasomaji wengi hawafahamu maana ya OUT? Ingeandikwa, ‘Chuo Kikuu Huria’ (OUT). Vilevile kuandika ‘kwenye mjini hapa’ ni makosa. ‘Neno kwenye’ limetumika visivyo na lingeondolewa. Tunasema ‘mjini hapa’ na wala siyo kwenye mjini hapa.
“ Alisema mbali na suala la menejimenti, lakini pia kulikuwa na matatizo ya mvua kubwa kunyesha kuliko kiwango kilichotarajiwa katika kipindi cha Desemba 2009 hadi Mei 2010.”
Kama nilivyoeleza hapo awali, neno ‘lakini’ ni kiunganishi na hivyo neno hilo halifai kutumika hapo na kama likiondolewa, maana iliyokusudiwa haitabadilika.
“Wachezaji wake wengi ambao wako kidato cha IV kuamua kujikita zaidi katika masomo yao kwa sababu ya kufanya mtihani wao.”
Maana iliyokusudiwa haijakamilika baada ya kutumia ‘ambao’. Kwa ulitoa neno ‘ambao’ sentensi ingesomeka,
“wachezaji wake wengi wako kidato cha IV na wameamua kujikita zaidi katika masomo yao kwa sababu ya kufanya mtihani wao.”
“Hakuna uamuzi yoyote yatakayopitishwa na Fifa juu ya sharia hizo bila kuishirikisha bodi ya sharia.”
Liko neno ambalo limeleta mtafaruku kwa wanafunzi, pia wanazuoni wa Kiswahili hapa nchini, pia nje ya mipaka yetu kuhusu tahajia sahihii ya neno ‘sharia/sheria. Kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu iliyoandaliwa na Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI) mwaka 2004, neno lililokubalika ni ‘sheria’. Hata hivyo wataalamu wengi wa pwani hawakubaliani na tahajia hiyo na wanatumia sharia. Vyombo vilivyopewa dhima ya kusimamia ukuzaji wa Kiswahili kama Bakita na Bakiza vinatakiwa kwa pamoja na kutoa msuluhisho na kuondoka mkanganyiko huu kwa waandishi na watafiti. Nalo neno ‘maamuzi’ linatakiwa kuandikwa ‘uamuzi’ kwani kiambishi ‘ma’ kiomeongezwa bila kuzingatia misingi ya sarufi hasa ngeli zake.
“Katika hatua nyingine Carlos Teves anategemea kuongeza mkataba wake kwenye klabu hiyo.”
Carlos hategemei kuongeza mkataba wake bali anatarajia/anatazamia/anatumainia kuongeza mkataba wake. Kutegemea ni kushikilia, kuegemea na kuzuilia hivyo mwandishi hakuwa makini katika uteuzi wa neno linalofaa.

Chnzo: MCL
 
Back
Top Bottom