Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,809
- 15,421
Leo ningependa kuzungumzia watu wa haiba ya kutoa. Hawa ni watu ambao nguvu yao iko kwenye kukidhi haja na utashi wa mahitaji ya watu wengine. kumbuka hapa sizungumzii kuhusu kuwajali watu wengine au kuwasaidia kwa upendo. Hapa nazungumzia mtu ambaye anajali kuhusu mahitaji ya wengine, ili apendwe au kuwa karibu na watu hao.
Bila shaka umeshawahi kuona mtu ambaye yeye kazi yake ni kuwatimizia wengine mahitaji yao tu, huku akitegemea kwamba, watu hao watamtambua, watamsaidia na yeye kwa maana ya kulipa fadhila.
Kwenye uhusiano wa kimapenzi au ndoa, hali hii hujitokeza pia.
Watu hawa hutoa sana kuliko wanavyopokea, jambo ambalo baadae huwafanya wahisi kuumia na kuonewa. Wanapoingia kwenye hali hiyo huwa na hasira na machozi mengi. Watu wanaotoa sana kwa wapenzi ili wapendwe, bila wao kupendwa, hutokea kuwa na hasira na kisirani. Kwa kuwa ninazungumzia uhusiano, ina maana kwamba, hawa watu ambao hupenda hadi wanajisahau kwamba, wangetakiwa kujipenda wao kwanza.
Wanapenda ili nao wapendwe, jambo ambalo unakuta haliwezekani na hivyo kuwaingiza kwenye maumivu makali. Kama mtu akiwa na mpenzi wa aina hii ni lazima ataumia naye pia.Yeye hatajua ni kipi mwenzake anataka kufanyiwa, kwa sababu watu wenye haiba hii huwa hawasemi mahitaji au wanachotaka kutoka kwa wenzao, bali wao hutoa tu, wakiamini wapenzi wao watajua wanachotaka wao.
Mtoaji anaweka nguvu nyingi sana kwenye kujiweka karibu na mpenzi kwa kutoa. Tunapotoa sana na kujisahau wenzetu huingia kwenye mashaka. Huyu anayepewa huanza kumwona anayetoa kama msumbufu, kama mtu ambaye hawezi kusimama mwenyewe – mtegemezi. Mara nyingi kwenye uhusiano huwa kunatokea kasoro, ambapo mmoja anataka kuwa karibu na mwenzake huku mwenzake akitaka nafasi.
Kwa mtu mwenye haiba ya kutoa, huwa anaumia sana kwa sababu kwa kadiri anavyotoa ili apokelewe ndivyo anavyohisi kukataliwa.Mara nyingi mtu mwenye haiba ya kutoa ni lazima atalazimika kwamba, mwenzake hajui kupendwa, kwa sababu yeye anampenda, lakini yeye haoni wala kujali. Ukweli ni kwamba mwenzake anajali na kupenda, lakini siyo kwa kiwango cha tatizo kama alichonacho mtoaji. Ni kwa kuwa ametoa sana, amefanya mengi sana kwa mwenzake hata yale ambayo haikuwa lazima kuyafanya, ili apendwe, kwa maana mpenzi wake naye afanye kama yeye, ndiyo maana anahisi mwenzake hajui kupenda.
Hebu chunguza utagundua kwamba, mtu ambaye anatoa tu, yaani anayejiumiza ili aonekane wa maana kwenye uhusiano mara nyingi hujikuta akidharauliwa na mpenzi wake. Ndipo pale wanaposema, "ukimpenda sana mtu, anakuringia." Suala hapa sio kumpenda sana mtu, bali ni kujipendekeza sana kwa mtu. Mtu ambaye ni mtoaji, anapaswa kujua kwamba, anapaswa kupenda bila kujali atalipwa nini. Hapaswi kufanya ili apendwe, hapana.
Anapaswa kufanya kwa sababu anapenda. Kupenda haina maana ya mtu kujibadili ili kukidhi mahitaji ya mpenzi. Inabidi mwenye haiba hii aanze kujifunza kuwa na muda mwingine wa kuwa peke yake li kupunguza uwezekano wa kutoa na kutoa.Nikisema, "kutoa na kutoa," maana yake ni kwamba, kwa kuwa na mpenzi muda mwingi, mwenye haiba hii atalazimika kuingia kwenye kujipendekeza. Kuwa peke yake kunampa uhuru wa kujifunza kudhibiti maisha yake. Mtoaji anatakiwa kujifunza kusema mahitaji yake moja kwa moja kwa mpenzi wake. Mara nyingi watoaji huwa hawasemi mahitaji yao kwa wapenzi wao. Ni kama vile wanasubiri hao wapenzi wao watoe mahitaji yao.