WAPINZANI HAWANA NIA YA DHATI YA KUSHIKA DOLA.
Wamekuwa wakali sana pale ambapo wanachama wengine wanajitokeza kuwania nafasi zao za uongozi. Tumeshuhudia wanachama ambao wanathubutu kutaka kugombea nafasi hizo wakizushiwa tuhuma za ajabu, kupakwa matope na kupewa kila aina ya majina mabaya eti wengine wameitwa wasaliti. Hapa mtu unajiuliza mwanachama huyu amefanya kazi kubwa ya kujenga chama chake kwa miaka kadhaa na kazi yake inaonekana, imekuwaje wakati huu aonekane msaliti? Imekuwaje aonekane hafai? Wenye akili wanangamua na kupata majibu kuwa hapa si kingine bali ni maslahi ya mkubwa yameguswa au yametikiswa ndio maana ya vurugu hizi zote kutokea.
Viongozi hawa wamekosa sifa ya kuwa na nia ya dhati, tena kwa namna ambavyo wameshindwa kumaliza migogoro ndani ya vyama vyao kwa njia ya amani, kitu ambacho kila mhusika kwenye migogoro angepata haki yake. Viongozi hawa wamekuwa vinara wa kusigina demokrasia.
Vyama hivi vingekuwa na viongozi wenye kushika misingi ya demokrasia, na wenye kumaliza migogoro ndani ya vyama vyao kwa amani na kuwa na nia thabiti ya kizalendo basi wangeweza kuwa na nia ya kushika dola. Lakini yote haya yanaonyesha nia hiyo ya dhati hawana.
Vyama hivi,vingekuwa na viongozi imara, vijana na mahiri mithili ya akina Zitto Kabwe, Shabiri Mpaka basi kwao ingekuwa rahisi sana kujipanga vizuri na hivyo kuwa na NIA ya DHATI ya kushika DOLA na kwa kweli uchaguzi wa mwaka huu tungeshuhudia wakishika dola. Lakini kwa sasa tusubiri sana hadi hapo viongozi hawa watakapobadirika na kushika misingi ya demokrasia na kujenga uwezo vijana wenye uzalendo na hivyo kupata sifa ya nia ya dhati katika kushika DOLA.
Shabiri Mpaka