Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

*ANGA LA WASHENZI -- 46*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Asiamini macho yake, aliona nyaraka ile, anayoipambania iwe siri, ikiwa imeshatumwa kwenye historia ya maongezi. Na huyu bwana Chen Zi alikuwa yupo huko Hong Kong, China!

Akahisi kuishiwa nguvu. Akapiga moyo konde na kusoma maongezi ya barua pepe ile mwanzo mpaka mwisho. Alipomaliza, akaiweka simu chini akisaga meno. Alipandwa na hasira mno. Alikunja ngumi yake kubwa akifuma ndita.

Akamtazama Alphonce kwa hasira, na mara akanyanyuka na kuchomoa bunduki yake akamuwekea kwenye paji la uso. Hakusema kitu, macho yake yalikuwa tayari mekundu. Akabinua mdomo na kufyatua kitufe cha bunduki!

Klick! Hakuna kitu. Klick! Klick! Klick! Hamna kitu, risasi zilikuwa zimeisha. Kwa hasira akaitupia bunduki mbali Alphonce akishusha pumzi ndefu ya neema.

Akatoka ndani ya chumba na kwenda kuketi sebuleni akiwa ametingwa na mawazo lukuki. Aliwaza, je kuna haja ya kumshirikisha Sheng kwenye mkasa huu?

Vipi kama Sheng akijua hizi habari, ambazo amejitahidi kuziweka chini ya kapeti akashindwa, atafanya nini na atamfanya nini?

Akajikuta akitetemeka mikono.

ENDELEA

Kama kuna usiku ambao uliwahi kuwa mgumu kwake, basi ni huu. Hakupata usingizi kabisa. Kichwa chake kilikuwa kinatepeta mawazo. Alijazwa na hofu moyoni.

Baada ya kufikiria kwa muda, aliona kuna haja ya kushirikisha wenzake, pengine wanaweza kumpatia mawazo mbadala maana aliona kichwa chake hakifanyi kazi tena.

Akawatafuta kwa kuwapigia simu lakini hakuwapata. Pengine walikuwa wamepumzika vitandani mwao. Akaona afanye kazi hiyo asubuhi na mapema, japo kishingo upande maana aliona kama anapoteza muda.

Akaendelea kugaragara kitandani, akaichukua ile simu na kuitazama tena. Akapitia zile jumbe za barua pepe kati ya Foang na Chen Zi. Akahisi moyo wampasuka.

Alitamani kurudisha hali lakini haikuwa inawezekana. Akawaza sana kuhusu yule Chen Zi. Alikuwa ni nani, na kwanini Foang amtumie ujumbe kama mtu wa kwanza.

Kwakuwa hakuwa na usingizi, akaona si mbaya akautumia muda wake huo kusaka taarifa za Chen Zi ndani ya mtandao.

Akiwa amekodoa akatafuta jina hilo huku akiwa ameliambatanisha na Hong Kong, punde chache Chen Zi ikaja ikiwa na majibu kadha wa kadha, lakini haswa lililotamalaki lilikuwa ni jina la Chen Zi aliyetambulishwa kama msanii maarufu wa miondoko ya pop nchini China, Hong Kong.

Lee akafuatilia taarifa za msanii huyo akiwa ameshavunjika moyo kuwa si mtu anayemhitaji. Na kama haitoshi, alipochekechua taarifa za mtu huyo akaja gundua Chen Zi alikwishafariki, tena mwaka jana kwa kuzidisha dozi ya madawa ya kulevya!

*"CHEN ZI 'THE ROCKER' DOPPED TILL DEATH" (CHEN ZI 'MTUMBUIZAJI' AMEZIDISHA DAWA MPAKA KIFO)*

Mojawapo ya kichwa cha habari kilisema vivyo. Akatazama na majibu mengine ya Chen Zi akapata kuona watu wa mitandaoni haswa Facebook. Akasonya na kutoka mtandaoni.

Kitu alichotokea kuamini ni kuwa Chen Zi atakuwa si mtu maarufu mitandaoni. Akawaza sana asilale mpaka asubuhi. Akadhamiria kuwasiliana na Bigo ampe ushauri.

***

Macho ya Jona yalikuja kufunguka akiwa kitandani. Amechoka na mwili ukiwa mzito. Akakohoa na kukunja shingo kutazama kando.

Hakuelewa nani aliyemuweka hapo kitandani, alipatwa na hofu lakini mwili wake haukumruhusu kunyanyuka.

Hakumwona mtu kwa muda wa dakika kama mbili. Hatimaye akamwona mwanaume akiingia, akakaza macho kumtazama akagundua ni Panky. Angalau akawa na amani.

"Unaendeleaje?" Panky akamuuliza akitabasamu kwa mbali. "Ni kama bahati kuja hapa, nilikukuta chini ukiwa hujitambui."

Jona akamshukuru kwa msaada wake. Akajitahidi sana kuketi wakati Panky akimuuliza nini kilijiri akawa kwenye hali ile. Kabla Jona hajamjibu, akamuuliza kwanza kama kuna habari yoyote kumhusu mheshimiwa Eliakimu.

Panky akahamaki. Akatikisa kichwa chake na kuanza kueleza juu ya habari ya kuvamiwa na kuuawa kwa mheshimiwa huyo. Habari yake imesambaa jiji zima na kuzua taharuki.

"Ninavyokuambia mpaka sasa, hakuna mtu aliyekamatwa."

Jona akatulia kwanza. Alikuwa anawaza juu ya hayo aliyoambiwa akichambua kwanini mheshimiwa aliuawa. Na tena ndani ya muda mfupi tangu aondolewe pale.

Kichwani akayapata majibu kuwa ahusikaye hapo si mwingine bali wale waliomteka Nade. Kutoonekana kwa mke wa mheshimiwa, kulithibitisha mawazo yake hayo.

Baada ya muda mfupi wa kuwaza, kwa akili yake timamu, Jona akamwambia Panky kuwa anahitaji kurejea jeshini. Panky akashangazwa na maamuzi hayo, lakini Jona akajitetea kuwa hiyo ndiyo njia sahihi ya kukamilisha anachokitaka.

"Panky, nahitaji covering. Nahitaji authority kwenye mikono yangu. Nahisi kuna haja ya kurejea kukamilisha mambo kadhaa."

Aliposema hayo akaendelea kuwaza. Panky akamhitaji apumzike kwani amechoka sana. Lakini kabla ya kupumzika, Jona akamuuliza kuhusu ile picha. Ni wapi amefikia.

Panky akatabasamu kwanza kabla hajajibu. Akamshika Jona bega na kumweleza kuwa hicho ndicho kilimleta hapo. Na anashukuru kwa maana kama asingelikuja basi angelimpoteza.

"Nimeshapata zile code. Huwezi amini! Na mpaka sasa nashawishika kuamini kuwa ile picha ni siri kubwa ya Sheng! Si bure alikuwa anaitafuta."

Panky alisema kwamba Marwa ndiye aliyemsaidia kung'amua code za picha hiyo baada ya kumshawishi sana na kumuahidi usalama wake kwa gharama yoyote ile. Akampatia "x-ray pictures" ambazo alimtaka azihifadhi sana, akiwa ameziiba toka kwenye tarakilishi ya 'administator' wa kitengo chao.

"Ni kwanini Marwa amekuamini kiasi hicho?" Jona akataka kujua.

"Marwa, ni zaidi yangu. Ni mjuzi wa mambo makubwa sana na ni mtaalamu sana wa mambo haya, lakini hafanyi kazi ile kwa kupenda bali kulazimishwa. Kila mwisho wa mwezi, mbali na kulipwa pesa, hupewa 'antidote' kwa ajili ya kuwapatia wazazi wake ambao walidungwa sindano na Sheng.

Kama Sheng asipompatia antidote hiyo wazazi wake hawatachukua hata dakika tano, watafariki dunia!"

Jona akasisimkwa na hiyo simulizi. Akatamani hata kuonana na Marwa, lakini Panky akamwambia watalifanya hilo taratibu mbeleni kwani hakumwambia Marwa juu yake.

"Nilichomwambia ni kwamba hii inaweza ikawa namna ya sisi kujikomboa. Kama unavyojua, hatukuwa na muda mrefu sana wa kuteta. Tunapokuwa kazini huwa tunatazamwa kila saa."

Baada ya maongezi hayo machache, Panky akamwachia Jona bahasha ya kaki ambayo ilikuwa na taarifa zile alizomweleza. Akamwambia anapaswa kwenda kwani kuna mahali anatakiwa kupitia.


***

Saa kumi na moja jioni, Monduli, Arusha.

"Anapoelekea, atakufa," Roba alisema akiketi chini. Akamtazama Nyokaa aliyekuwa anavuta bangi akitazama zake bustani. Ni ndani ya nyumba ya wastani yenye bati la bluu.

"Amekula?" Nyokaa akauliza.

"Hajala, analia tu anataka unga," Roba akajibu kisha akapokea kipisi cha bangi toka kwa Nyokaa naye akawa anakipiga pafu.

Wakawa wanateta juu ya Miriam - mke wa mheshimiwa. Mwanamke huyo alikuwa hoi chumbani akiwa hataki kula wala kunywa chochote isipokuwa heroine. Amekuwa akitetemeka mwili na kuharisha.

"Unadhani ni muda wa kuachana naye sasa?" Akauliza Roba.

Nyokaa akatikisa kichwa chake akikakataa. Akasema hata kama kazi yake ya kuwachomesha 'ma-broker' wa madini, ambao ni majamaa wa Eliakimu imeshafanyika, bado wanamhitaji mwanamke huyo. Watamtumia hata kujaribishia madawa.

"Akifa tutamtupia huko mtoni!" Akahitimisha Nyokaa kabla ya kumuuliza Roba juu ya kazi yake aliyoifanya kwa mheshimiwa.

"Vipi yule manzi? Bado hujasikia habari yake?"

"Bado, sijasikia. Nadhani atakuwa amekufa tu," Roba akajibu kisha akavuta pafu moja.

"Roba, yule mwanamke haikupasa umuache hai kabisa. Siwezi nikakaa kwa amani chali'angu. Anaweza akatuchoma."

Nyokaa akataka Roba amtafute Nade na kuhakikisha anakufa kwa njia yoyote ile. Mara ya mwisho alisikia amelazwa Aga khan kwa mujibu wa vyanzo vyake vya habari.

Alipomsisitizia hilo, akanyanyuka kwenda kumuona Miriam. Akamkuta akiwa amejikunyata. Nywele zake zilikuwa vurugu mwili wake aliokunyata ukiwa ndani ya dera la njano.






****
 
*ANGA LA WASHENZI -- 47*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Nyokaa akatikisa kichwa chake akikakataa. Akasema hata kama kazi yake ya kuwachomesha 'ma-broker' wa madini, ambao ni majamaa wa Eliakimu imeshafanyika, bado wanamhitaji mwanamke huyo. Watamtumia hata kujaribishia madawa.

"Akifa tutamtupia huko mtoni!" Akahitimisha Nyokaa kabla ya kumuuliza Roba juu ya kazi yake aliyoifanya kwa mheshimiwa.

"Vipi yule manzi? Bado hujasikia habari yake?"

"Bado, sijasikia. Nadhani atakuwa amekufa tu," Roba akajibu kisha akavuta pafu moja.

"Roba, yule mwanamke haikupasa umuache hai kabisa. Siwezi nikakaa kwa amani chali'angu. Anaweza akatuchoma."

Nyokaa akataka Roba amtafute Nade na kuhakikisha anakufa kwa njia yoyote ile. Mara ya mwisho alisikia amelazwa Aga khan kwa mujibu wa vyanzo vyake vya habari.

Alipomsisitizia hilo, akanyanyuka kwenda kumuona Miriam. Akamkuta akiwa amejikunyata. Nywele zake zilikuwa vurugu mwili wake aliokunyata ukiwa ndani ya dera la njano.

ENDELEA

"Miriam, mbona hutaki kula?" Akauliza akichuchumaa. Miriam hakujibu zaidi ya kumtazama kwa jicho la husda.

"Inabidi ule, sawa?" Nyokaa akamshika Miriam. Mara Miriam akaanza kububujikwa na machozi yasiyo na kikomo. Kifuani mwake alikuwa anaumia. Maisha yake yalikuwa yameharibika na hakuwa na namna tena kuyarejesha kama hapo awali.

Leo amekuwa mtu wa kuvuta unga! Pua yake haikuwa kawaida asipotia kitu hicho mwilini. Amekuwa mdhoofu na asiyevutia tena. Zaidi ya yote, mwanaume aliyemuingiza huko akiwa ni yule aliyempenda na kumtumaini.

"Nyokaa," akaita kwa sauti ya chini, kisha akasema:

"Sitakusahau maishani mwangu. Na Mungu wangu aliye juu atakulipia."

Nyokaa hakujali hayo maneno. Kwake hilo lilikuwa ni dua la kuku kwa mwewe. Akatabasamu na kunyanyuka akisema:

"Utakapojisikia kula, utasema sawa? Sina muda wa ngonjera hapa." Kisha akaondoka zake akimwacha Miriam akiendelea kumwaga machozi akimshuhudia mwanaume huyo akiyoyoma.


***


Saa nne asubuhi, ofisini kwa Kamanda wa mkoa.

"Mkuu, una ugeni," alisema mwanaume mkakamavu ndani ya sare ya jeshi la polisi. Kamanda pasipo kumtazama, akamtikisia kichwa kama ishara huku macho yake yakiwa yameganda kwenye gazeti la MAMBOSASA alilolijaza mkononi.

Punde kidogo, Kamanda akasikia sauti ikimsalimu. Sauti hii ikamfanya abandue macho yake gazetini na kumtazama mgeni huyo nje ya miwani yake ya kusomea. Akastaajabu ni yule mwanaume aliyekuwa anamtafuta.

"Ooh Jona! Karibu sana!"

Jona akashukuru na kuketi. Wakasalimiana, Kamanda akijawa na tabasamu. Lakini haikuchukua muda kwa Kamanda kujua kuwa Jona hakuwa sawa kiafya.

"Vipi, upo sawa?" Akauliza. Jona akalazimisha tabasamu akijibu:

"Nipo sawa." Kisha akaeleza haja yake iliyomleta pale pasipo kupoteza muda. Kuwa anataka kurejea kwenye jeshi kama alivyokuwa akisisitiziwa.

Kamanda akastaajabu kwanza kabla ya kulipuka kwa cheko la furaha. Kwake hizi habari zilikuwa za kufurahisha ambazo hakuzitarajia kabisa! Hatimaye mbuyu ulikuwa umeangushwa chini.

Akamkabidhi Jona mkono wa pongezi na kusifia maamuzi yake hayo.

"Hapo sasa, umeamua kiume, Jona!"

Lakini pia akataka kujua sababu iliyomfanya Jona arejee jeshini ingali alipingana na hoja hiyo kwa muda mrefu.

"Nimerudi kumalizia kazi zangu nilizoziacha kiporo," hilo likawa jibu la Jona kabla Kamanda hajampatia tena mkono na kumuahidi ushirikiano kwenye kutimiza adhma yake hiyo.

"We unaweza kwenda sasa, kesho ukarejea hapa majira ya asubuhi. Kuna mambo machache yanipasa kuyakamilisha ili kuweka vitu sawa," alisema Kamanda. Jona akaenda zake.

Kabla ya kurejea gazetini, Kamanda akatambaliwa na mawazo kichwani. Akalaza kichwa chake kwenye kiti akizunguka kwenda kushoto na kulia huku akitafakari jambo lile la Jona.

Ingawa alifurahishwa nalo, lilimpatia walakini kwa kiasi chake. Ni 'kiporo' gani hicho Jona anachotaka kuja kumalizia ndani ya jeshi?

Pengine akawaza Jona atakuwa ameng'amua hila zake za kumtesa ili arejee jeshini na hivyo basi amekuja kumuadhibu? Akawaza. Alitamani sana kufahamu nyuma ya 'kiporo' cha Jona, na basi kujiweka salama kwenye bandari hii, akaona ni vema kumtaarifu Alphonce. Wanatakiwa kuwa makini na nyendo za Jona. Lakini mwanaume huyo hakuwa anapatikana tokea jana yake alivyomuita ofisini!

Basi akajikuta hana namna zaidi ya kungoja akiwa amedhamiria kama leo hatomwona Alphonce, inabidi juhudi za makusudi zifanyike kumtafuta.

Akashika gazeti lake, lakini kabla hajaanza kulisoma, akasikia mtu akiingia.

"Samahani sana, mkuu!" Alikuwa ni Alphonce! Alikuwa amevalia suti rangi ya kahawia, koti limemzidi kipimo. Akasimama kwa ukakamavu kutoa salamu kisha akaketi.

Kabla ya kuulizwa, akaanza kujitetea kwa Kamanda ni kwanini alishindwa kutimiza agizo lake la kufika ofisini jana yake.

"Nilipata ajali, mkuu. Sikuwa na uwezo wa kuwasiliana nawe pia kwani simu yangu iliibiwa."

Kamanda hakuwa na muda wa kupeleleza maelezo hayo ya Alphonce, donge lilikuwa limemkaba shingoni kungoja, akamwambia kuhusu habari za Jona kurejea jeshini.

"Nimekutana naye huko nje, nikastaajabu kufika kwake hapa," Alphonce akateta akitabasamu.

"Amekuona?" Kamanda akauliza.

"Yah! Tumesalimiana tu kila mtu akaenda zake."

Kamanda akavuta kwanza pumzi akiweka kituo. Alafu akamwambia Alphonce juu ya hofu yake.

"Unadhani mkono wake utatuacha salama?"

Alphonce akaangua kicheko. Hakuona sababu ya kuhofia. Akamwambia Kamanda wake kama Jona angekuwa anataka kuwamaliza wala hakuwa na sababu ya kurudi jeshini kwani angeweza kutimiza haja yake hiyo hata huko nje.

"Tujipongeze maana hila zetu zimefanikiwa," akasema Alphonce na kuongezea: "ametambua kuwa maisha yake hayawezi kuwa sawa akiwa nje ya jeshi."

Lakini bado Kamanda hakujiona mjinga. Bado aliona kuna haja ya kumtazama Jona kwa darubini ya pekee hivyo akamuagiza Alphonce kutenda hilo.

Alphonce aliyekuwa hana shaka akalipokea hilo jukumu.

... lakini hakujua uzito wake kamili.


---


Akiwa ndani ya daladala kurudi kwenye makazi yake, Jona aliyekuwa ameketi kwenye viti vya nyuma kabisa, alikuwa anawaza juu ya kile alichokiona kule ofisini.

Macho yake yalikuwa nje ya gari lakini ndani ya mawazo. Kichwani kwake taswira ya gari aina ya Prado nyeusi ilikuwa inamjia. Gari lililomwagia risasi nyingi akiwa anaelekea nyumbani kwa Eliakimu ndani ya taksi.

Mbona ameliona gari hilo pale ofisini kwa Kamanda? Akakumbuka pia na taswira ya mwanaume anayemtambua akishuka toka kwenye gari hilo. Alikuwa amevalia suti kubwa ya kahawia - suti inayofanana na ya yule aliyeambiwa na shuhuda kuwa ndiye muuaji wa Jumanne, mshirika wake kwenye biashara ya kuchora na kuuza picha!

Taswira hizo mbili zikamnyima raha. Zikampa ukweli mchungu kuwa Kamanda anahusika na jaribio lake la kumuua, vilevile la kuharibu biashara yake. Haswa kwanini?

Akakumbuka kauli aliyoambiwa na Kamanda kwa mara ya mwisho alipoonana naye ofisini kwake. MAISHA YAKE KAMWE HAYATAKUWA SAWA NJE YA JESHI. Hatomtafuta tena, bali ni yeye atakayemtafuta.

Akashtuliwa na kondakta akidai nauli. Akatoa nauli hiyo na muda si mrefu akashuka toka chomboni, akishkuru kondakta kumshtua kwani hakuwa anafahamu kama alikaribia, kisa mawazo.
.
.
.
****
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…