Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Ahaaaa bro yaani me nikifungua device yangu kwanza internet connection, jamii forum, intertaiment, ANGA LA WENYWEWE Full stop unless otherwise mpk nimalize story ndo mengine yanafuata halafu kama kawaida yangu siti ya mbeleeeee namsubiria Jona akate vichwa watu basiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiii
 
So fa so gud...kazi nzuri steve,upo vzur natuko pamoja mpaka mwisho wa safar yetu hii
 
Nashukuru sana mkuu wangu.
 
*ANGA LA WASHENZI --- 51*

*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Mili akamtaka mwanaye amletee viazi vilivyopo kwenye bakuli kabatini, akamlisha Miriam akimsindikizia na maji ya kunywa. Angalau Miriam akapata nguvu.
Kwa taabu, akipambana na hisia za maumivu, na kwa ufupi akamweleza Mili wapi alipotokea na yeye ni nani kisha akawasisitizia Mili na mwanaye wasije wakamwambia yeyote juu yake.
"Hapa ni mbali sana toka huko!" Akasema Mili. "Siku ya kwanza walikuja wanaume wawili hapa wakatuulizia kumhusu mwanamke mwenye sifa zako, lakini tulihofia, tukakanusha kukuona."
Miriam akamuuliza kwanini alifanya hivyo. Mili akamjibu ni kwakuwa waliwaona wanaume hao wakiwa wameficha bunduki ndani ya nguo zao, wakafahamu si watu wema.
"Hata jana mwanangu alipata kumwona mmoja wa wanaume wale akirandaranda na kuangaza huku na huko!" Akamalizia Mili, kisha akamtaka Miriam apumzike wataongea zaidi baadae.
ENDELEA

Alikitazama kioo akatabasamu mwenyewe. Sasa alijiona amependeza na anaweza kutoka. Akajiangalia tena mwili mzima, akajikubali na kujipa ruhusa. Akabeba mkoba wake na kisha akatoka ndani.

Yalikuwa ni majira ya saa kumi na moja jioni. Jua lilikuwa limepoteza nguvu yake likionekana jekundu linaloadhimia kwenda zake na kuuacha ulimwengu kizani.

Ndani ya jioni hii, Glady alikuwa ana mipango kadhaa ya kutekeleza na sehemu kadhaa za kwenda.

Mwendo wake wa madaha na nguo yake ya nusu uchi, zilimfanya awe gumzo barabarani, lakini nani anajali? Sio Glady huyu! Hakuwa anaogopa macho ya watu hata kidogo. Alikuwa anafanya yale yanayopendezesha nafsi yake tu, mengine mtabaki nayo nyie.

Kwa watu waliokuwa wanamfahamu kuwa anajiuza, hawakustaajabishwa naye, pengine walivutiwa. Glady alikata mitaa kwa hatua zake za maringo mpaka alipowasili mbele ya fremu iliyoandikwa;
MSUGULI PHONE ACESSORIES

Alipokutana na fundi, mwanaume mfupi mweusi mwenye nywele pilipili. Akamsalimu na kumuulizia kazi aliyompatia. Mwanaume huyo akatabasamu, kisha akauzamisha mkono wake kwenye kabati la kioo alipotoa simu kubwa nyeusi aliyomkabidhi Glady aipekue.

"Yani nilimaliza kitambo sana, nikajua umeisusa!" akasema fundi.

"Ili uiuze sio?" Glady akauliza akiifungua simu aliyokabidhiwa. Akazama kwenye menyu, ikakubali! Huko akakuta kila kitu. Basi akajikuta akitabasamu.

"Safi sana! Aisee! ... yani nilikuwa siamini kabisa kama ungeweza!" Glady akalipuka kwa furaha.

"Nilikuambia ni kitu kidogo sana hiko," fundi akajigamba. "Yani kufungua maloki ya simu ndo kazi yangu, chap tu mbona unafurahi mwenyewe na roho yako."

Glady akatoa pesa kwenye mkoba wake, shilingi alfu kumi akamkabidhi fundi. Wakazoza kidogo kwani fundi alikuwa anataka zaidi kwa kazi alofanya. Glady akaishia kumwongezea alfu tano alafu akaenda zake.

Njia nzima akawa anatabasamu mwenyewe. Hakuamini kama amefanikiwa kuifungua simu ile aliyoiiba toka kwa Alphonce. Aliona amefanya kazi kubwa na sasa anaweza akaitumia simu hiyo ambayo ipo juu kiteknolojia ukilinganisha na ya kwake.

Akafika nyumbani na kujimwaga kitandani. Akafungua na kuanza kuipekua simu ya Alphonce, aone kama yaliyomo yamo. Cha kwanza kilikuwa ni kamera, akaridhika nayo, 'akajitwanga' picha kadhaa kabla hajaendelea na upekuzi wake.

Akawasili sasa kwenye gallery ambako huko ndipo alichukua muda mrefu kuliko mahali pengine. Akatazama kila picha alizoziona huko. Ajabu ni kwamba, akakuta mpaka picha za watu anaowajua!

Na picha hizi hazikuwa za kawaida, lah! Bali za uchi. Za wanawake mbalimbali, ikiwamo wengine wenye nyadhfa kubwa serikalini ama kwenye mashirika ya umma na yale ya binafsi!

Kama haitoshi, akakumbana na picha kadhaa za watu waliouawa. Akaona mpaka picha ya Mustapha! Hapa sasa kifua chake kikaanza kukita kwa mapigo kasi ya moyo. Akaweka simu pembeni kwa hofu, akigongwa na mawazo kichwani.

Ametoa wapi picha za watu hawa? Je, ameshiriki kwenye mauaji? Ni yeye ndiye alikuwa akimfuatilia Mustapha na hatimaye kumuua? Akawaza sana.

Akaogopa mno kwanini alijihusisha na huyo mtu. Kama amewaua wote hao, je yeye atasalimika? Akajihisi joto, damu inakimbia kwa kasi.

Lakini baadae akakumbuka kuwa mtu yule ni polisi. Naam! Aliona kitambulisho chake kwa macho yake kabisa. Inawezekana zile picha za wafu ni kwasababu za kipolisi? - yani za kipelelezi? Akawaza. Japokuwa hakupata jibu, lakini wazo hili lilisaidia kumshusha presha aliyokuwa ameitengeneza.

Lakini vipi kuhusu hizi picha wanawake walio uchi? - nazo zafanya nini?

Akaelekea kwenye mitandao ya kijamii, huko akapita kila sekta asiache jambo. Ilimgharimu masaa mawili kutimiza haja yake kisawasawa, akikagua kila maongezi ambayo Alphonce aliyoyafanya.

Mwishowe akaja kugundua kuwa mwanaume yule hakuwa mtu wa kawaida. Alikuwa ni muuaji! Na amekuwa akifanya hivyo kwa malipo makubwa na ustadi mkubwa. Na amekuwa akitumia kofia yake ya upolisi kumaliza mambo 'kirahisi'.

Ana miradi kadhaa, na kwenye akaunti yake kuna pesa ya maana anazozipata kwa mkono mchafu! Hapa pakamkamata Glady na kumbadili mawazo. Pesa! Pesa! Pesa!

Hapa akasahau kwamba anaweza akauawa. Hapa hakuona tena hatari ya kifo, bali akijiona yupo Dubai. Akajiona anaendesha magari makubwa na yenye thamani ya hali ya juu!

Alijikuta anataka kupata mgao wa pesa iliyopo kwenye akaunti ya Alphonce. Abadili mfumo wa maisha yake kabisa.

Hivyo basi akajikuta hana budi kucheza mchezo huu na simba. Mchezo wa aidha nipate nitoke, ama nikose nife. Akadhamiria kumtafuta Alphonce kwa namna yoyote alafu amfahamishe kuwa ana siri zake zote kiganjani. Na kama anataka ziendelee kuwa salama, atume mamilioni!

Tabasamu likachipuka usoni. Mara akashtushwa na hodi mlangoni! Haraka akaficha simu na kuuliza:
"Nanii?"

"Aaaaah nawe! Embu funguaga hukoo!" Sauti ikamjibu kwa shombo. Akamtambua ni shoga wake katika kazi.

"Alah! Kumbe muda umeenda!" Akastaajabu. Akasimama upesi na kwenda kumfungulia huyo shoga 'ake - mwanamke aliyekuwa amevalia kikaptula kifupi cha kijani na blauzi nyeupe inayohakisi ya ndani - sidiria rangi nyeusi.

Wasikae muda, wakatoka kwenda kazini.

***

Saa tatu usiku ...

Televisheni ilikuwa inaongea yenyewe. Juu ya meza ya kioo kulikuwa kuna chupa ya mvinyo mwekundu na glasi yake kwa pembeni.

Hakukuwa na nuru ya taa, mwanga pekee uliokuwepo hapa ulikuwa ni ule utokao kwenye televisheni. Na mbali na sauti ya televisheni hii, hakukuwa na sauti nyingine iliyosikika.

Kwenye kochi alikuwa ameketi bwana Lee akiwa ameinamishia kichwa chake chini. Alikuwa ameelemewa na mawazo. Na chupa hii ya mvinyo juu ya meza, ilikuwa inaelekea kukatika pasipo kumsaidia kabisa.

Kwanini asiwe na mawazo wakati maisha yake yapo hatihati? Alikuwa amekonda, endapo ukimtazama vema, wala havutii tena. Rafiki yake mkubwa alikuwa ni pombe, na anajifungia ndani.

Mara kwa mara sauti ya marafiki zake, Nigaa na Mombo, zilikuwa zinamrejelea masikioni zikimtaka asitishe mpango wake wa kwenda Chinakumtafuta Chen Zi.

Wao hawakuona kama hilo wazo ni jema kwani kuondoka kwake kutamsababisha bwana Sheng kuanza kumshuku. Walipendekeza Lee aachane na mambo ya hiyo Nyaraka. Lolote litakalotokea, akane kuhusika nalo.

Lakini atawezaje kufanya hilo? Akajiuliza. Sheng anajua kuwa yeye ndiyo alikuwa na nyaraka hiyo, tena ya thamani kubwa, endapo akisikia huko kwengine atamfikiria nani zaidi yake?

Akajikuta anakataa kabisa wazo la kutokwenda China. Ni lazima aende huko akamaliza alichokianzisha. Akamtafute Chen Zi aliyetumiwa nyaraka hiyo na bwana Foang - mchina aliyemrubuni Mustapha.

Ila sasa kazi inakuja, atatolea wapi sababu ya kwenda huko China? Akahisi kuchanganyikiwa.

Akanyanyuka na kwenda kujiandaa, mara akatoka ndani na kujiweka kwenye gari, safari mpaka klabu. Bahati, akiwa huko akamwona Glady. Alikuwa amesimama na marafiki zake mikononi wakiwa wameshikilia bia za kopo.

Akamfuata mwanamke huyo na kumtaka awe naye kwa usiku huo. Kwa kumtazama tu, Glady akajua Lee hakuwa sawa. Alikuwa na msongo wa mawazo. Basi pasipo kusita, akaridhia kwa kumpa tabasamu.

Lakini kabla hawajatoka ndani ya klabu, Alphonce akazama ndani akiwa anaangaza. Alikuwa amamtafuta Glady!



****
 
*ANGA LA WASHENZI -- 52*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Ila sasa kazi inakuja, atatolea wapi sababu ya kwenda huko China? Lee Akahisi kuchanganyikiwa.

Akanyanyuka na kwenda kujiandaa, mara akatoka ndani na kujiweka kwenye gari, safari mpaka klabu. Bahati, akiwa huko akamwona Glady. Alikuwa amesimama na marafiki zake mikononi wakiwa wameshikilia bia za kopo.

Akamfuata mwanamke huyo na kumtaka awe naye kwa usiku huo. Kwa kumtazama tu, Glady akajua Lee hakuwa sawa. Alikuwa na msongo wa mawazo. Basi pasipo kusita, akaridhia kwa kumpa tabasamu.

Lakini kabla hawajatoka ndani ya klabu, Alphonce akazama ndani akiwa anaangaza. Alikuwa amamtafuta Glady!

ENDELEA

Mwili wake ulivishwa suti nyeusi, lakini kama kawaida yake, haikuwa imemkaa vema. Nguo ilionekana ni kubwa tofauti na umbo lake. Pengine huwa anajiona ana mwili, ama amenenepa kwa ndani, na hivyo basi matatizo ni kwetu sisi tunaomtazama.

Akaelekea kaunta akaoda wiski moja, aliomba iwe ngeni kinywani mwake. Akiwa anasubiri apatiwe, akawa anaangaza macho yake kutafuta. Lakini shida ni kwamba, mwanga uliokuwemo humo ndani, kumeta-meta kwa rangi nyingi kama pinde za mvua, hazikumruhusu aone watu vema.

Kwahiyo basi yeye alikuwa anasachi kwa mujibu wa maumbo. Alikuwa amelikariri umbo la Glady ma endapo tu angeliona basi angeling'amua kwa wepesi kabisa, hata kama kizani.

Ila mpaka muda huo, alikuwa ameshachelewa. Kwa muda huo, tayari Glady alikuwa ndani ya gari la Lee wakiondoka zao.

"Hii hapa!" Akasema mhudumu akisogeza glasi. Alphonce akaitikia kwa kichwa alafu akapiga pafu moja kana kwamba anakunywa juisi ya machungwa!

Akasafisha koo lake na kumtazama mhudumu machoni. Kwa sauti yenye stara ndaniye, akamuuliza endapo kama anamjua Glady. Si kwa kumtajia jina, la hasha! Bali kwa kumdadavulia mwanaume huyo mhudumu namna gani Glady aonekanavyo. Kuanzia umbo, mwendo na hata sauti.

"Hapana, simfahamu!' Mhudumu akabinua mdomo. Na akiwa mwenye haraka ya kuhudumia wateja wengine wanaomngoja. Akashika shelvu, akafungua jokofu na kuwapatia watu vinywaji, punde alipomtazama Alphonce akakutana naye macho kwa macho. Na mezani Alphonce alikuwa ameweka kitambulisho chake cha kazi.

Ni askari.

"Pengine unaona haja ya kwenda kujadiliana kituoni?" Akamuuliza mhudumu katika sauti ya kutotaka kuwaogofya wengine.

Mhudumu akatazama kando na kando upesi. Hakuona kama kuna haja hiyo. Ni kweli hakuwa anamjua Glady, lakini kutokana na uzoefu wake wa kazi ndani ya eneo hilo, alishafahamu tokea awali kuwa Glady atakuwa ni mwanamke anayejiuza ndani ya eneo hilo. Na huyo mwanaume, yaani Alphonce, atakuwa anamsaka kishari, aidha walikorofishana kihuduma.

Kwahiyo kuepusha zogo, huwa wanajibu sijui. Lakini kesi ya leo haikuwa iliyozoeleka. Alikabwa na hofu. Na kadiri Alphonce alivyokuwa anakaa pale, hakujihisi mwenye amani.

Akanyooshea kidole upande wake wa magharibi ya mbali kisha akamtazama Alphonce.

"Anaweza akawa pale."

"Na kama hayupo?" Alphonce akauliza akiweka kitambulisho chake ndani ya mfuko wa koti.

"Basi wenzake watakusaidia kumpata ... wale wote ni wenzake!... wote wale!"

Alphonce akagida mafundo yasiyo na mwisho kumalizia wiski yake kisha akanyanyuka. Hata hakulipa, akaendaze alipoelekezwa. Lakini hilo halikumshtua mhudumu, bali namna mwanaume huyo alivyoweza kunywa chupa ile ya kinywaji kikali kana kwamba chai baridi!

Akamtazama akiyoyomea mataani. Akaendelea na kazi yake lakini kila dakika akirusha macho kuangaza usalama kule magharibi. Masikio yake hayakuwa yanasikia tena mziki mkubwa uliokuwa unapigwa mule. Muda wowote yalikuwa yamejitenga kusikia yowe ama makelele ya wale madada poa wakimkimbia 'askari'.

Ila haikuwa hivyo. Baada ya muda kidogo akamwona Alphonce akitoka nje akiongozana na mwanamke ambaye hakumwona vema, japo alifahamu ni miongoni mwa wale wadada wanaojiuza.

Hapo, angalau sasa akashusha fundo la pumzi alilolikabia kifuani kwa muda.

***

Mlango wa Prado nyeusi ulipofungwa, gari haikuwashwa, badala yake Alphonce akatoa bunduki ndogo na kuipuliza kana kwamba ina vumbi. Akaitazama kana kwamba msomaji wa gazeti apekuae kisa alichosimuliwa. Alafu pasipo kufanya nayo jambo, akairudisha alipoitoa. Akatengenezea 'sight mirror' vema kisha akamtazama mwanamke yule 'aliyeloki' naye ndani ya gari.

Mwanamke huyu alikuwa ni yule 'shoga' aliyempitia Glady kwenda naye 'kazini' masaa kadhaa nyuma tu. Kama ni upatu, Alphonce alikuwa ameula.

"Sina shida ya kukupeleka popote, bali mambo mawili. Na katika hayo utachagua mwenyewe lipi linalokufaa. Unipatie taarifa ninayoihitaji ukaenda zako salama, mkononi una pesa, ama nikutoe ndani ya gari hii ukiwa mfu."

Hata kabla Alphonce hajaendelea, mwanamke huyu alikuwa tayari kusema lolote lile atakaloulizwa. Alishafanya chaguzi. Hakuwa na taarifa ya muhimu kuzidi uhai wake, na wala chungu kutia doa utamu wa pesa.

Alikuwa anatetemeka mno na kama milango ya gari isingekuwa 'imelokiwa' basi ni wazi angeshachumpa nje kukimbia kadiri ya urefu na uwezo wa miguu yake.

Bunduki haikuwa kitu alichozoea kukiona.

Kwa utaratibu kabisa, Alphonce akampembua mwanamke huyo, na akapata alichokuwa anakitaka. Akazamisha mkono mfukoni, akatoa noti kadhaa nyekundu, pasipo kuhesabu, akamtupia yule mwanamke mapajani kisha aka'unlock' milango pasipo kusema kitu.

Mwanamke akashuka upesi. Hapo ndo' akagundua kumbe alikuwa ameshalowana mapajani na nguo yake ya ndani ilikuwa mbichi. Haraka akakimbilia ndani ya klabu usidhani amevalia viatu vya visigino virefu!

Akaingia ndani kwa pupa, na kusababisha tahamaki kwa waliomuona. Haswa yule mhudumu wa kaunta!

***

Saaa nne asubuhi ....

'nitakuwa hapo ndani ya dakika kumi,' Jona alituma ujumbe kisha akaizamisha simu yake mfukoni. Akatazama kando, kando tena, alafu akanyanyuka toka kwenye kituo cha basi na kuanza kutembea kwa ukakamavu.

Alikuwa amevalia shati jeupe, tai nyembamba nyeusi, suruali nyeusi ya kitambaa na moka. Mabegani mwake alikuwa ametundika koti kubwa la mvua lilikomea magotini.

Kwa mtu mwenye macho ya 'chujio' ungemtambua huyu mtu hakuwa raia wa kawaida. Alikuwa mtu mwenye mafunzo. Kisigino chake kilikuwa kinaanza kukanyaga chini kwanza kabla ya nyayo, tena kwa ustadi na sare.

Macho yake yalikuwa hayajatulia, yanakwenda huku na kule kuangaza usalama. Alijua anafuatiliwa. Ilipangwa afuatiliwe. Na anatakiwa afuatiliwe!

Hiyo ndiyo maana anatakiwa kuripoti asubuhi na mapema kwa Kamanda mkuu wa mkoa, badala ya kituoni kama ilivyo utaratibu wa kazi, kabla ya kutimiza majukumu yake.

Kufika huku kwa Kamanda kulikuwa ni kwa lengo moja tu, nalo ni kumpachikia 'mkia', na si lingine. Jona alitakiwa kuwa chini ya 'jicho la tai' kwa muda fulani kuhakikisha mienendo yake si 'hatari kwa afya' kwa walioshika mpini.

Alizidi kutembea na huku nyuma yake, hatua kama kumi na nane akiwa anasindikizwa na mwanaume mpana mweusi aliyevalia kaunda suti ya kijivu.

Hatua za mwanaume huyu zilikuwa za kiutu uzima. Suruali yake pana ilikuwa inarushwa rushwa kwa hatua zake za nguvu. Alimjaza Jona kwenye mboni na hakusumbuliwa na kingine chochote kilichokuwa kinakatiza machoni.

Lakini dakika moja ni kubwa sana! Ndani ya dakika moja, yaani sekunde sitini, jambo kubwa linaweza kupangwa, liketekelezeka na kuacha pengo!

Wakavuka kona ya kwanza ... pili ... tatu ... ndani ya dakika moja tu. Mwanaume yule aliyekuwa anamfuatilia Jona akatambua ameshaachwa solemba!

Mbele yake bado alikuwa analiona lile koti alilojivika Jona, halikuwa limebadilika, ni lilelile! Lakini suruali haikuwa nyeusi tena, bali rangi ya udongo! Haraka akakimbia na kumnyaka bega mwanaume mwenye koti hilo, kugeuka alikuwa ni mwanafunzi!

Hakugundua tangu kona ya kwanza, Jona alikuwa ameshamwacha akiendelea kumalizana na kona ya tatu.

"mkuu, amenipotea," akavuma kwa fedheha akiongea na simu.

***

'Nipo nje ya mlango' Ujumbe uliingia ndani ya simu ya Marwa. Akanyanyuka toka kochini alipokuwa ameketi akauendea mlango na kuufungua. Akakutana na Jona. Hakuwa na koti.

Wakasalimiana na kumkaribisha kitini.

"Ungependelea kinywaji gani, mkuu?"

"Hapana, nashukuru ... umewasiliana na Panky?" Jona akaenda moja kwa moja kwenye 'biashara'.

"Ndio, amesema anakaribia," Marwa akajibu kwa kujiamini akiketi.

Nyumba ilikuwa kimya. Hakukuwa na dalili yotote ya kuwa na mtu mbali na wao walioketi sebuleni. Na kwa Jona, kwa muda mfupi alioketi hapo, akagundua Marwa amekuwa akiishi maisha ya kipweke. Nyumba haikonekana kama ina 'mguso wa kike' wala shurba za mtoto.

Alipokuwa amekaa aliweza kuona jiko, ukuta wa korido, samani, sakafu na kadhalika. Havikuwa katika namna ambavyo vingekuwa endapo Marwa angekuwa anaishi na mtu mwingine mule ndani.

Hakujali, ila hakukuwa na kingine cha kufanya wakiwa hapo wanamngojea Panky zaidi ya kuperuzi peruzi. Hakutaka kuanza kumpekenyua Marwa kwa kumrushia maswali mapema yote hiyo, kwani hakuonekana kama mtu aliye 'comfortable' mbele ya uwepo wake.

Akaendelea kutazama tazama pasipo kutia neno, mpaka macho yake yalipotua mezani kulipokuwa na tarakilishi nyeusi HP modeli ya kisasa, makaratasi kadhaa, mengine meupe, mengine ya grafu, zaidi kalamu tatu, penseli nne na rula moja.

Kwenye makaratasi hayo kulikuwa kuna michoro michoro mingi, na mengine mahesabu mahesabu yakiwa yametapanywa. Bila shaka Marwa alikuwa anayatumia kufanyia zoezi analoendelea nalo kwenye tarakilishi, akawaza Jona.

Akasafisha koo lake, na kuvunja ukimya.

"Hata leo haupo off?" Akauliza akitabasamu kwa mbali. Marwa akatabasamu zaidi.

"Sijawahi kuwa off. In fact, nafanya kazi overtime mara kwa mara. Nadhani n'shazoea!" Marwa alimalizia kwa kupandisha mabega yake.

"Basi pasi na shaka, mshahara wako ni mnono," Jona akaendelea kuchokoza mada. Macho yake yalikuwa makini kutazama kila kitu toka kwa Marwa.

"Lah! Nafanya kazi si kwa ajili ya pesa, bali maisha."

"Pesa ni maisha."

"Hapana. Pesa si maisha ... pesa haiwezi nunua maisha."

Hapa Jona akaona kuna cha zaidi Marwa alikuwa anataka kusema lakini aidha anakosa namna bora ya kukisema, ama anajitahidi kuzuia kutokukisema.

Lilikuwa ni jukumu lake kukijua hiko kitu.

"Kama pesa kwako si kitu. Unafanyiaje kazi maisha? Wafanya kazi kwa kuwa umezoea?"

Marwa hakujibu upesi. Alitulia kwanza. Jona hakuona haja ya kumshinikiza ajibu kwani uso wa mwanaume huyo ulimwonyesha jibu lipo karibuni. Ni vile anapanga namna ya kulitamka.

Marwa akashusha pumzi ndefu. Pasipo kumtazama Jona, akasema kwa sauti iliyotoka chini ya vungu la moyo wake.

"Output ya kazi yangu, ndiyo pumzi ya wazazi wangu."

Jona hakupata wasaa wa kuendelea kumdadisi, Panky akawasili. Sasa wakaanza kujadili kuhusu ile picha.

_Picha ya siri._

_Picha ya Bite inayotia rehani roho zao wote._

***
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…