Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Alhamis hiyoooo na Anga la wakata upepo a.k.a Washeeenzi
 
*ANGA LA WASHENZI (MSIMU WA PILI) -- 16*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Na pia vilevile antidote!!

"Hamna shida, naweza kukuwahisha," Miranda akamkarimu. Wakanyanyuka toka sebuleni na kwenda nje walipodumbukia ndani ya Range Rover sport nyeupe na kutimka.

ENDELEA

Kwa kasi waliyoitumia hawakuchukua muda kuwasili, Marwa akashuka garini na kwendaze kituoni baada ya kuagana na Miranda aliyesema anaenda kushughulikia na kuweka mambo sawa.

Marwa akaingia mapokezi na kukutana na afande Devi aliyempokea kwa ukarimu na kumjulia hali.

"Nimekuja kumletea chakula jamaa 'angu," alisema Marwa kisha akafungua chakula na kukionyesha.

"Najua umekuja sababu hiyo," alisema afande Devi pasipo kutazama chakula hicho. Ni kheri akuwapo koplo Massawe, basi akamruhusu akamwone mtu wake upesi huko rumande.

Chap Marwa akafika huko na kumkuta Jona akiwa amejilaza hoi. Akamuita mara tatu akisaidiwa na mahabusu wengine. Jona akaamka na akiwa hajiwezi kwa lolote, wenziwe wakamburuta kusogea langoni.

Kwa namna ambavyo Marwa alimwona Jona, akashindwa kuzuia machozi machoni mwake. Jona alikuwa amepungua. Ni mdhaifu. Hana afya wala havutii kumtazama.

Si Jona yule umjuaye.

"Jona," Marwa akaita. "Kula angalau." Akambembelezea chakula. Jona akatamani sana kumjibu lakini hakuwa anaweza.

Alimtazama Marwa akamwona kwa mbali. Alitabasamu kumpa matumaini lakini Marwa akaishia kulia.

"Nitashinda," Jona alisema kwa sauti ya chini. "Usijali, Marwa."

Akala tonge mbili tatu, akashindwa kuendelea. Alilalama anasikia kichefuchefu, na kadiri anavyotafuna anasikia kichwa kinamuuma maradufu!!

Japo ni kweli alitamani kula, tumbo lilikuwa tupu, hakuweza abadani!

"Nimekulete antidote!" Marwa alimwambia kwa macho ya furaha. Alikuwa amemshikilia na mkono wake kumzuia aketi.

Kabla Jona hajasema kitu, Marwa akatazama kushoto na kulia alafu akachonoa kichupa kidogo mfukoni, akamtaka Jona afungue mdomo.

Akamminia chote kisha akamruhusu ajilaze chini.

"Utakuwa sawa," Marwa aliamini.

Jona akalala asiseme kitu. Muda si mrefu akakata fahamu kabisa!! Hakuwa anasikia, kuona wala kuhisi chochote.

Maumivu yalizidi mwilini mpaka fahamu ikashindwa kustahimili. Marwa asiwe anajua hilo, akamtazama Jona kwa sekunde kadhaa. Na hata alipoona kimya akatambua mwanaume huyo atakuwa katika hatua za kuwa sawa. Hivyo hana haja ya kuhofu.

Akamuaga Jona na kisha kwenda zake.

**

"Afandeee!" Sauti ikavuma ndani ya rumande. Si kwamba kulikuwa kimya, bali sauti hii ilikuwa kubwa kupita kiasi.

"Afandee, kuna mtu anakufa huku!" Alipaza sauti jamaa mmoja aliye ndani ya chumba kimoja na Jona.

Jona alikuwa anatoa damu masikioni, puani, mdomoni na machoni kama machozi!! Hakuwa anatikisika hata kidogo. Hakuonyesha dalili zozote za uhai.

Hata mwili wake ulikuwa wa baridi kana kwamba ametoka kwenye jokofu!!

Haraka afande Devi aliwasilia akamtazama Jona. Mahali alipokuwa amelaza kichwa chake palikuwa pametapakaa damu.

Hata afande huyu akashtushwa sana na hili. Upesi akamweleza na kumsisitiza Massawe akamwambia mkuu wa kituo kuwa wanatakiwa kuchukua hatua upesi la sivyo mtu atawafia rumande iwe tabu!

Taarifa zikafika kwa OCD, ila ikawa bure. Jona hakuruhusiwa kutoka kituoni kwa namna yoyote ile labda awe mfu tu!!

"Nenda kaendelee na kazi yako. Kama kufa mwache afie humo. Alivyomuua RPC alidhani atastarehe??" Alisema OCD akiwa anachokonoa meno yake kwa toothpick.

**

"Ewaah ... naona ameshapatiwa ile antidote!" Alisema Kamanda mkuu akitabasamu na simu.

"Yes ... he is in critical situation ... hawezi akafa? ... ooh sawa. Hamna shida nitafanya hivyo."

Kamanda akakata simu kisha akacheka. Alipewa maagizo ya kuyatimiza.

**

"Naomba uningoje hapa," alisema Sarah kwa sauti ya kuamuru. Macho yake yalimtazama Kinoo kabla hajabanduka toka kwenye kiti cha gari na kwendaze ndani ya jengo maeneo ya Msasani.

Kinoo akamtazama mwanamke huyo akizamia humo aliposema anaenda kukutana na dada yake, Sasha, kama walivyopeana maelekezo.

Akawaza kidogo akijiuliza maswali kadhaa. Sasha alikuwa anafanya nini katika hilo jengo maeneo ya Msasani na kwanini Sarah hakutaka kuongozana naye kwenda humo.

Kwani Sasha si shemeji yake??

Hakuwaza wala kujihangaisha sana kwani alidhani pengine Sarah anataka tu kulipiza kisasi kwa vile anavyomfanyia akiwa anaongea na Miranda akimtaka atoke nje.

Akajikuta anatabasamu na kupuuza. Kosa ambalo hakutakiwa kulifanya hata kidogo.

Kwenye ulimwengu wa kijasusi, hakuna kitu kidogo hata siku moja. Kila tendo laweza kugeuka na kuwa sumu kali ys kumshusha tembo ndani ya sekunde kadhaa tu!!

Kusogezea muda wake wa kungoja, akawasha redio na kulaza kiti, akajilaza.

**

"Kwanini haukunambia siku zote hizo Sasha?" Sarah aliuliza akimtazama dada yake kwa macho ya ndita.

"Niliogopa," Sasha akajibu. "Ningeanzia wapi na wewe tayari umebeba mimba yao??"

Sarah akabaki njia panda. Hakuwa na neno la kusema. Sasha akamshika bega na kumuuliza:

"Utanisaidia?"

"Hapana!!" Sarah akajibu akisimama. "Nitawezaje kufanikisha hilo?? Mwanangu atatolea wapi baba mwingine kama ikatokea Kinoo akafa??"

"Ssshhhhh!" Sasha akaweka kidole mdomoni. "Punguza sauti yako, tutasikika!"

Akatazama dirishani kisha akarudisha macho yake kwa Sarah.

"Sijasema tumuue yeyote yule, Sarah!"

"Sasa unadhani hizo taarifa utakazokuwa unapeleka huko zitaishia kwenye nini?" Sarah akamkatiza.

Hakutaka kumwelewa dada yake hata kidogo. Alitoka zake ndani ya nyumba pasipo kuaga akamwacha Sasha akiwa ameduwaa.

Akang'ata meno na kukunja ngumi kwanguvu. Mpango wake ulikuwa umefeli!!

Sasa atafanyaje?? Kichwa chake kilikuwa moto. Hakuna mtu yeyote anayetakiwa kujua siri hiyo ila tayari ashamweleza dada yake.

Hapa akapata shaka kubwa. Hakuamini kama Sarah atautunza mdomo wake asiseme kitu. Kama tu akiufungua mdomo wake basi kazi itakuwa imekwisha!!

"Damu nzito kuliko maji," alijipa moyo. Ila kama mambo yasipoenda kama inavyotakiwa, basi hamna budi.

Hamna budi.

Itabidi amtoe sadaka dada yake!!

Aliwaza.

**

Usiku mzito, ndani ya chumba chenye giza ...

Waaaaa!! Jona alimwagiwa maji ya baridi na kuamriwa aamke upesi. Hakujua hapo alipo amefikaje. Alijaribu kufungua macho yake kutazama lakini hakuwa anaona kitu.

Si tu kwamba kulikuwa ni giza, hakuwa na uwezo wa kuona kabisa mbali na kutokuwa miwani. Hata masikio yake yalikuwa yamepoteza uwezo wake wa kawaida. Pia ngozi yake yake, ilikuwa hafifu kwenye kuhisi.

Lakini ajabu alipomwagiwa maji hayo ya baridi, alilia kwa maumivu makali ambayo hajawahi kuyapata!!

Ni kama vile maji hayo yalikuwa na visu ama viwembe. Yalimfanya ang'ate meno kwa ukali wa maumivu yaliyopitiliza. Alihisi amechanjwa chanjwa kila sehemu ya mwili wake iliyoonja maji hayo ya baridi.

Alihisi maji hayo yameingia mifupani. Yanamtafuna!!

Japo alikuwa dhaifu, akatapatapa kujinasua. Akahangaika huku na kule lakini hakuweza kufua dafu kwenye kamba ngumu alizokabwa nazo kitini.

Lakini kama haitoshi, ndani ya chumba hicho kulikuwa na ndoo tatu za maji baridi kabisa. Zote zilikuwa zinamgojea yeye.

Zinamngoja akileta ukaidi.

"Mzee, hatuna muda wa kupoteza hapa na wewe. Tunataka kitu kimoja tu. Kiri na sisi tutaenda zetu. Ukileta ujuaji, tutasema na wewe usiku huu mzima."

Jona alisikia sauti hiyo kwa mbali mno. Hakumjua anayemwongelesha ni nani. Alikuwa amekunja shingo yake kana kwamba kaelemewa na kichwa.

"Sisemi kitu," akasema kwa kunong'oneza. Mtesi wake akatabasamu kuonekana meno kizani.

Baada ya hapo Jona akamwagiwa ndoo mbili za maji baridi. Maji haya si kwamba yalimfanya asikie baridi, ila mchanganyiko wake na virusi vilivyomo mwilini mwa Jona, ulizalisha maumivu makali yasiyomithilika!!

Haikupita muda mrefu, Jona akazima.

Simu ikapigwa.

"Hatujafanikiwa, mkuu."

"Sawasawa," sauti ikatoka simuni. Sauti nzito ya Kamanda mkuu ikiashiria kutoka usingizini. Mwanaume huyo alisafisha koo lake kisha akasema:

"Sasa tuhamie kwenye njia ya mwisho. Kesho hakikisha mnamteka yule kijana anayemletea chakula kisha mumpatie machaguzi mawili, aidha tumuue huyo kijana ama afanye tunachokitaka."

**
 
*ANGA LA WASHENZI (MSIMU WA PILI) -- 17*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

"Sasa tuhamie kwenye njia ya mwisho. Kesho hakikisha mnamteka yule kijana anayemletea chakula kisha mumpatie machaguzi mawili, aidha tumuue huyo kijana ama afanye tunachokitaka."

ENDELEA

Kesho yake, asubuhi ya saa mbili ...

"Kila kitu kipo tayari," alisema Miranda akimtazama Kinoo kwa jicho la kazi. Kinoo akabinua mdomo wake na kutengua vidole.

"Basi na kazi itendeke!" Akasema kwa kujiamini akinyanyuka.

"Hakikisha hakuna kosa hata moja linafanyika," Miranda alisisitiza. "Hii ni kazi ya kufa ama kupona. Kama tukiharibu basi tumetia mchanga kwenye wali wa kula mwaka mzima."

"Usikonde, bibie," Kinoo akamtoa shaka. "Kila jambo litaenda kama lilivyopangwa. Lakini usisahau ahadi yangu."

Miranda hakusema kitu, akachomoa simu yake na kupiga. Punde akasema:

"Nikukute hapo hapo." Alafu akakata simu na kusimama.

**

"Bila shaka unakumbuka maelezo?"

"Ndio."


Miranda akamshika Marwa mkono wake wa kuume.

"Hakikisha unafanikiwa," akamsihi. "Hatuna nafasi ya kufanya kosa lolote leo. Aidha kama tunataka kupoteza yote.

Marwa akatikisa kichwa.

"Ntajitahidi kadiri ya uwezo wangu."

Miranda akatabasamu, kisha akanyanyuka na kwendaze.

**

Kwenye majira ya saa kumi jioni ...

Baada ya mlio wa gari huko nje, mara Marwa anafungua geti na kuzama ndani. Mkononi amebebelea hotpot ya chakula. Mwendo wake ni wa ukakamavu na usoni hakuonyesha shaka.

Ni katika kituo hiki cha kati. Watu walikuwa kadhaa wakiwa wamesimama huku na kule aidha wakingojea watu wao watoke nje ama wakingoja kuingia ndani.

Kwa haraka haraka Marwa akatazama mazingira hayo alafu akazama ndani. Hakumkuta afande Devi wala koplo Massawe. Alimkuta hapo afande fulani wanne waki wapo bize na kazi za hapa na pale.

Akaeleza dhumuni lake kumwona Jona na kumpatia chakula. Afande wale wakatazamana kisha mmoja akamwambia haitawezekana.

"Kwanini?" Marwa akauliza. Afande wale hawakumpa sababu, wakamwambia tu haiwezekani. Kwa ufupi.

Basi Marwa akatoka zake hapo kaunta na kuelekea kantini akiwaza ni kwa namna gani atafanya. Kwa muda wote aliokuwa pale kaunta roho ilikuwa inamdunda haswa.

Alikuwa ana kauoga ndani yake. Kama wale polisi wangemtazama vema wangelibaini hilo na huenda wakamtia mashakani.

Alivuta kiti akaketi. Akachojoa simu yake na kumtumia ujumbe Miranda kumweleza hali iliyopo. Punde Miranda akampigia.

"Do it," sauti ya kike ilisihi. "You must do it, Marwa. Alafu utatuhabarisha."

Kabla Marwa hajajieleza sana, mara simu ikakata. Marwa akashusha pumzi ndefu. Moyo ulikuwa unamwenda mbio.

Jasho kwa mbali lilianza kutambaa usoni mwake.

"Samahani, naweza nikakusaidia?" Sauti ya mhudumu ilimgutua mawazoni.

"Naomba maji makubwa," akaagiza na kuendelea kutafakari. Kama bahati akamwona afande Devi. Hapa angalau akajikuta anapata ahueni. Lakini haikutakiwa Devi amwone pale kantini!!

Kama Devi angelimwona pale kantini basi afande huyo angeishia kuchukua hotpot na kumtaka aende, yeye atasimamia zoezi.

Hivyo, haraka akanyanyuka na kujificha. Afande Devi hakuketi hapo kantini akateka soda na kulipa kisha akayeya eneo ambalo Marwa aliamini itakuwa ni kule kaunta.

"Pesa yako hii hapa," alisema Marwa pasipo kumtazama mhudumu. Macho yake yalikuwa yanatazama njia asiwaze hata kama kuna chenji anatakiwa kungoja.

"Chenji!"

"Kaa nayo tu," akasema akiondokaze.

Aliwasili kaunta na kama alivyowaza, afande Devi akawa tayari amejaa pale. Kabla hajamsalimu, mmoja wa wale afande waliomfukuza hapo awali akamtazama na kumfokea:

"Haukuerewa enh? ... nitakutia sero sasa hivi ukamkute mwenzako huko!!"

Marwa hakujibu. Alimtazama afande Devi kwa macho ya mhitaji, afande huyo akaingilia kati.

"Chacha," Devi akaita. "Jamaa 'angu huyu bana."

Basi Marwa akacheza karata dume hapa hapa. Haraka akafunua chakula chake alichokiweka pale kaunta na kuzuga analalama kuwa chakula ki safi. Hamna tatizo lolote na hata akitakiwa kuonja atafanya hivyo.

"Huna haja hiyo, ndugu yangu," Afande Devi akamtoa shaka akimwekea mkono begani. "Its ok. Funha tu chakula chako."

"Hapana!" Akasema Marwa akitikisa kichwa. "Labda ana hofu na hiki chakula. Tazama afande ... nipo hapa kumsaidia tu rafiki yangu."

Marwa akaigiza mpaka pale alipoona muda ni sahihi kwake kufunga hotpot, zoezi lake la kwanza likawa limefanikiwa. Lakini la pili, kwenda kumpelekea Jona chakula. Kidogo ikawa tabu.

"Wewe liache tu hapa. Nitalipeleka," alisema Afande Devi akivuta hotpot.

"Lakini afande, tafadhali naomba ulipeleke saa hii. Najua hajala tangu jana na hata leo nikakawia kuleta chakula. Atakuwa naa njaa sana."

"Ooh! Sawa," Afande akatikisa kichwa. "Nitafanya hivyo."

Marwa akaenda zake. Akatoa simu yake mfukoni na kutua ujumbe kwa Miranda.

'ABC'

Akimaaanisha mambo matatu yamekwishafanyika. Alipoletea ujumbe wa 'delivery report' akaweka simu mfukoni na kwenda kukaa mbali kidogo na kituo lakini eneo alilohakikisha anapata hewa ya kutosha kwani ni kama alianza kuhisi kichwa kimeanza kuwa kizito.


**

Wiu!-Wiu!-Wiu!-Wiu!-Wiu!!

Ilikuwa sauti kali ya king'ora.

Mara gari la wagonjwa lililokuwa katika kasi kubwa liliingia ndani ya eneo la kituo na mara wakashuka watu wawili waliovalia sare za kiuguzi. Wakashusha machela harakaharaka na mmoja wao akazama ndani!

Punde wakatoka na Jona na akiwa amebebwa. Na wasiwe na haraka sana, yule muuguzi aliyebakia nje akaweka sikio lake kifuani. Akachopeka dripu na kumwingiza Jona ndani.

Alafu kukatisha utepe, muuguzi yule awali akarudi tena ndani na kumtoa afande Devi. Hakuonekana kama mtu anayejielewa. Alikuwa anarembua akikokotwa. Mkono wake wa kuume ulikuwa shingoni mwa muuguzi.

Naye wakamzamisha ndani na kisha gari likahepa!!

Hata wale maafande waliokuwepo mlangoni wakiwa wamebaki na butwaa.

**

"Habari zilizotufikia hivi punde!" mwanamke mrembo nyuma ya kioo cha televisheni alinguruma kwa sauti yake ya kuvutia watazamaji na wasikilizaji.

Alikuwa amevalia suti rangi ya damu ya mzee. Na kwa namna alivyokuwa amependeza, ungeliweza kupuuza habari anayoitangaza na badala yake ukamtazama yeye.

Lakini kwa ukubwa wa habari hii, hakuna ambaye angeweza kudiriki kufanya hivyo. Habari hii iliyowafikia hivi punde ilikuwa ni ya moto!!

Ya kustaajabisha na kuvuta watu wasonge karibu na vyombo vyao vya habari.

"Mtuhumiwa nambari moja wa mauaji ya aliyekuwa mkuu wa polisi mkoa, ametoroshwa kituoni na watu wasiojulikana ... watu hao wakiwa wamefika hapo kwa kutumia gari la wagonjwa, walifanikiwa kuondoka na mtuhumiwa huyo pia na polisi mmoja ambapo mpaka sasa haijajulikana wamepelekwa wapi ... tukutane saa mbili usiku kwa habari zaidi."

Taarifa hiyo ikazua gumzo kubwa haswa jijini. Watu wakapigwa na bumbuwazi na kwa namna wahalifu walivyowazidi akili polisi mpaka kufanikiwa kukwapua mtu tena kituo kikuu!

Watu waliosikia habari hiyo wakiwa ndani ya madaladala wakapata mada ya kusogezea muda angalau kuwasahaulisha foleni ya kukera nyakati kama hizi.

Na wale wa mitandaoni wakazisambaza upesi. Si katika namna ya kusikitika bali kushangazwa!!

**

"Kamanda siwezi nikakuelewa hata kidogo!" Alifoka Sheng kana kwamba anaongea na mtoto wake. Na kadiri akiwa na hasira basi lafudhi yake ya ki-mandarin inafanya asieleweke kabisa nini anaongea.

Kila mara Kamanda akawa anamuuliza simuni ni nini anaongea.

"Ametorokajhe??" Sheng alitoa macho akibamiza meza.

"No! No! No! I can't understand!"

Uso wake ulikuwa mwekundu. Jasho jembamba lilikuwa linakatika kwenye paji lake la uso.

Akatoa agizo:

"Namtaka! ... I want him kabla siku ya kesho haijakwisha. La sivyo ..." akakata simu na kuibamizia mezani.

Kutazama mlangoni alikuwa amesimama mdada mchanga wa kichina ndani ya sare, sketi nyeusi na form six nyeupe, akiwa amebebelea trey yenye chupa kubwa ya mvinyo na glasi yake.

Mdada huyo alikuwa amesimama kwa hofu akimtazama Sheng kwa mashaka. Bila shaka alishaona mambo yametibuka.

Sheng, kwa hasira, akavuta droo na kutoa bunduki yake ndogo. Pasipo kujiuliza mara mbili, akamtwanga risasi tatu mwanadada huyo, akafa papo hapo!!

Mwanadada ambaye hakuwa na hatia bali akitimiza tu kazi yake.



**
 
Sasa kumekucha Miranda kazini....
Ahsante Sana mkuu Steve
 
I tellfortunes ,The great "Jona" he is going to end up the race.
Come on Stive, Unajua unachokifanya(Stivemollel(SM) the great boy).
 
Kweli Sterling hafi ila chamoto lazima akione. Steve umetisha boss, sio kwa msoto unaompitisha Jona..duh[emoji119][emoji119]. Thank you for tireless efforts to keep us entertained. God bless.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…