Mshambuliaji wa klabu ya Real Madrid Karim Benzema atafikishwa mahakamani mwezi Oktoba kujibu tuhuma ya kuhusishwa na hujuma ya kanda ya Video ya ngono dhidi ya aliyekuwa mchezaji mwenzake wa timu ya taifa ya soka ya Ufaransa Matthieu Valbuena.
Taarifa hiyo imetangazwa leo na ofisi ya mwendesha mashtaka wa serikali wa mji wa Versaille. Benzema atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma katika kesi hiyo inayomkabili kuanzia Oktoba 20 hadi 22 akitajwa kuhusika katika jaribio la kumsaliti mchezaji mwenzie.
Benzema anatuhumiwa kuwa alihusika kumshinikiza Matthieu Valbuena mwaka 2015 kuwalipa fedha watu kadhaa waliokuwa wakitishia kuachia kanda hiyo ya Video ya tukio la kashfa ya ngono linalomuhusisha Valbuena. Valbuena alilipeleka polisi suala hilo.
Kwa upande wake Benzema amedai kuwa alikuwa akijaribu kumsaidia mchezaji mwenzake ambaye walikuwa wote kwenye timu ya taifa huku akiongeza kuwa anadhani hawakuelewana ”Nadhani ni kutokuelewana, mwanzoni nilitaka Mathieu afahamu swala hilo na kuweza kumsaidia kwa sababu waliwahi kufanya kama hivyo kwangu. Yeye ni mtu ambaye nilicheza naye Ufaransa na ni rafiki”
Tangu kuibuka kwa sakata hilo Benzema hakuitwa tena ndani ya kikosi cha timu ya taifa ya Ufaransa. Ikiwa Benzema atapatikana na hatia, anaweza kukabiliwa na kifungo cha miaka mitano gerezani.