CHUAKACHARA
JF-Expert Member
- Jun 3, 2011
- 12,357
- 6,424
Dar es Salaam. Msiba wa Mbunge wa Mbinga
Magharibi, Kapteni John Komba jana uligeuka
uwanja wa siasa, baada ya makada wa CCM
wanaotajwa kugombea urais pamoja na wapambe
wao kupigana vikumbo na kurushiana vijembe,
ikiwa na maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba.
Ilikuwa kama walijipanga kwani kila mgombea
aliyekuwa anafika katika msiba huo alionekana
kuwa na wapambe waliompokea, kumpeleka kutoa
pole kwa wafiwa na kumuonyesha eneo la kukaa.
Ukiacha kauli mbalimbali walizotoa kumwelezea
marehemu Komba (61), wapambe wa wagombea
hao walionekana mara kwa mara kuwa karibu nao
wakizungumza, hali iliyoonyesha kuwa kila kundi
lilitaka mgombea wao kuonyesha uwepo wake.
Waliohudhuria
Wanaotajwa kuutaka urais ambao walihudhuria
msiba wa mbunge huyo uliotokea juzi jioni ni
Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Waziri wa
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard
Membe, Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja,
Mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi,
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, wote
kutoka CCM, pamoja na Katibu Mkuu wa Chadema,
Dk Willibroad Slaa.
Wapiga picha na Membe
Membe ndiyo alikuwa wa kwanza kufika nyumbani
kwa marehemu eneo la Mbezi Tangi Bovu na baada
ya muda aliwasili Rais Jakaya Kikwete na kukaa
naye.
Mara baada ya Rais Kikwete kuondoka, Membe
alilakiwa na kundi kubwa la makada wa CCM ambao
mbali na kumsalimia walimvuta pembeni na kuomba
kupiga naye picha huku wakisika wakisema kuwa
"Tunataka kupiga picha na mheshimiwa rais".
Watu hao ambao walikuwa wakiongozwa na
Mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Aden Rage ambaye
hata hivyo hakupiga picha na waziri huyo, walisema
kuwa kama mambo yakienda vyema, Membe
anaweza kuwa rais na hata alipokuwa akiondoka
walimsindikiza hadi kwenye gari lake.
Vijana na Nchimbi, Ngeleja
Ukiacha Dk Nchimbi ambaye alikuwa akizongwa
zaidi na vijana wa CCM, kivutio kingine kilikuwa
kwa Ngeleja ambaye mara kwa mara alikuwa
akizungukwa na vijana waliokuwa wakimuuliza
maswali mbalimbali, hasa kuhusu sakata la Akaunti
ya Tegeta Escrow.
Ngeleja pamoja na aliyekuwa Waziri wa Ardhi,
Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna
Tibaijuka walipata mgawo wa fedha kutoka katika
akaunti hiyo na tayari wamehojiwa na Kamati Ndogo
ya Maadili ya CCM, huku Ngeleja akisubiri kesho
kuhojiwa na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa
Umma ambayo tayari imeshamuhoji Profesa
Tibaijuka.
"Kwa sasa siwezi kusema chochote. Chama kilitupa
adhabu (ya kuanza kampeni za urais mapema),
ninaiheshimu adhabu hiyo na ninasubiri tamko la
chama na hapo ndiyo nitakuwa na mengi ya
kusema," aliwajibu Ngeleja.
Mwigulu na wanahabari
Kiongozi mwingine aliyekuwa kivutio ni Mwigulu
Nchemba kwani kila baada ya muda aliitwa na
makada wa chama hicho katika makundi na
kuonekana wakizungumza mambo mbalimbali.
Nchemba ambaye hivi karibuni ziara zake za
mikoani zilisitishwa na Katibu Mkuu wa CCM,
Abdulrahman Kinana kwa maelezo kuwa hazikuwa
na baraka za chama hicho na zililenga kujitangaza,
ndiye kiongozi aliyeongoza kwa kuzungumza na
vyombo vya habari katika msiba huo.
Katika muda wa saa tano aliokaa katika eneo hilo
alizungumza na vyombo vya habari zaidi ya mara
tano, ikiwa ni mara nyingi kuliko kiongozi yeyote
aliyefika katika msiba huo.
Lowassa azima muziki
Kati ya viongozi waliokuwa kivutio zaidi ukiacha Dk
Slaa, ni Lowassa ambaye alifika katika msiba huo
saa 7:30 mchana ikiwa ni nusu saa baada ya
walinzi wake kufika.
Mara baada ya kufika aliwapa pole wafiwa na
kwenda kukaa eneo lililotengwa kwa ajili ya
viongozi wa Serikali karibu na Mbunge wa Kigoma
Mjini, Peter Serukamba na Ngeleja, na mara kadhaa
alifuatwa na makada wa chama hicho na viongozi
mbalimbali na kuzungumza naye.
Wakati akizungumza na vyombo vya habari, muziki
uliokuwa ukipigwa iliamuliwa uzimwe na mmoja wa
waongozaji wa msiba huo kwa maelezo kuwa waziri
huyo wa zamani na mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi
na Usalama alikuwa akizungumza.
Dk Slaa na walinzi
Mara baada ya Lowassa kuondoka eneo hilo, muda
mfupi baadaye aliwasili Dk Slaa akiwa na walinzi
watano wenye miraba minne wakiwa wamevaa suti
nyeusi na miwani nyeusi.
Kuwasili kwa kiongozi huyo wa Chadema kuliibua
minong'ono ya hapa na pale kutokana na walinzi
waliokuwa wamemzunguka ambao hawakumpa mtu
yeyote nafasi ya kumsogelea.
Msafara wa magari manne ya Dk Slaa ambaye
anatajwa kuwa miongoni mwa wanaotajwa kuwania
urais ndani ya Ukawa, yalikuwa yamepambwa na
bendera za Chadema tofauti na viongozi wa CCM
waliofika eneo hilo. source gazetii la mwananchi
Tumewaona! Lililobaki ni kumpa ubunge mwanae Komba kama ilivyokuwa kwa waziri wa fedha-. Just wait and see CCM!