Kyodowe
JF-Expert Member
- Mar 6, 2013
- 1,236
- 1,368
Follow along with the video below to see how to install our site as a web app on your home screen.
Note: This feature may not be available in some browsers.
Wow! Umerudi [emoji1] [emoji1]The Bold again [emoji91][emoji91][emoji91][emoji91]
Karibu chiefthank you very much the bold
Yupo chief... not here though
Wow! Umerudi [emoji1] [emoji1]
Hahahah tulia bhana... kila nikiingia humu nakutafuta na tochi sikuoniYaani Jf siku 2 halafu Ban siku 5.
Hahahah tulia bhana... kila nikiingia humu nakutafuta na tochi sikuoni
Safi mkuu japo ya leo imekuwa kilemutuzKILIO CHA MIFEREJI YA DAMU IENDAYO ETHIOPIA
![]()
SEHEMU YA SITA
Katika sehemu iliyopoita nilieleza namna ambavyo Watusi, Paul Kagame, Fred Rwigyema na wenzake walivyoingia kwenye vikundi vya kijeshi chini ya Museveni na kushiriki vita ya Kagera na baadae kushiriki katika kumuondoa madarakani Rais Milton Obote.
Katika sehemu hii ya sita nataka tuangalie namna ambavyo moto wa mauaji ya Kimbari ulivyowaka na hatimaye tuangalie namna ambavyo Paul Kagame ameibuka kuwa mtu mwenye nguvu zaidi kwenye ukanda huu wa Afrika Mashariki na Ukanda wa maziwa makuu.
Ili kuelewa namna ambavyo mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 yalivyoanza ni vyema kwanza kuelewa namna ambavyo RPF (chama tawala cha sasa nchini Rwanda chini ya Paul Kagame) ilizaliwa na kubadilika kutoka kuwa umoja wa wanaharakati na baadae kuwa kikindi cha kijeshi na sasa chama cha siasa
Turudi nyuma kidogo….
Baada tu ya Milton Obote kushika nchi kupitia uchaguzi ambao ulikuwa na utata mkubwa mwaka 1980 na hatimaye Yoweri Museveni kujitenga naye akishutumu uchaguzi kutokuwa wa haki na kuanzisha kikundi chake cha National Resistance Army, Milton Obote mara moja alianzisha kampeni ya kukipiga vita kikundi hicho kwa nguvu ya jeshi lakini pia kwa propaganda akishutumu kuwa kikundi hicho kiko chini ya "Banyarwanda" (watu wa Rwanda) na si raia wa Uganda.
Hii ilipelekea mwaka 1982 serikali ya Milton Obote kulazimisha Watusi wote waliopo nchini Uganda kuwa wanapaswa kuishi kwenye kambi za wakimbizi pekee na si mitaani kama raia.
Ikumbukwe kwamba Watusi wamekuwa wakiikimbia Rwanda tangu miaka ya 1960s, hivyo wengi wao walikuwa wamelowea Uganda, Congo na hata Tanzania na kufikia hatua ya kuishi maisha ya kawaida uraiani kama raia wengine wa nchi hizo. Kwa hiyo kitendo cha Milton Obote kutangaza kwa hakuna Mtusi anayeruhusiwa kuishi uraiani isipokuwa kwenye kambi za wakimbizi pekee ilizua taharuki kubwa sana.
Watusi wote ambao walikuwa bado wanajificha na kuendelea kuishi uraiani, walikamatwa na kufungwa na wengine kuuwawa.
Hata kwenye kambi za wakimbizi zenyewe nako Obote aliweka mashushushu ambao waliwakamata Watusi ambao walionekana kuwa na misimamo mikali kupinga serikali yake au kumuunga mkono Museveni na kikundi chake cha NRA na kisha kuwatia jela na wengi wakipotezwa kusikojulikana.
Hii ilipelekea kuibuka kwa wimbi la wakimbizi wa Kitusi wapatao 40,000 kukimbia Uganda na kurudi Rwanda. Ubaya zaidi walipofika Rwanda kutokana na wakimbizi hawa kiwa Watusi serikali ya Rais Juvenile Habyarimana ilitangaza kuwatambua watu 4000 pekee kati ya wote 40,000 waliorejea.
Kati ya hao waliobaki na kukataliwa kurejea Rwanda, serikali ya Uganda chini ya Milton Obote ikatangaza kwamba itawachukua wakimbizi 1000 tu.
Kwa maana hiyo walisalia watu 35,000 katikati ya mpaka wa Rwanda na Uganda wakiwa hawana kwa kwenda. Rwanda nyumbani kwao serikali ilisema haiwatambui, na Uganda ambako waliishi kwa miaka kadhaa nako serikali ilisema haiwataki tena na haiko tayari kuwaruhusu kuingia. Kwa hiyo wakabaki kwenye ombwe la sintofahamu kubwa.
Kama nilivyoeleza huko nyuma kwamba Paul Kagame ni 'born tactician' anajua ku-capitalise katika mazingira yote. Yaani anajua kuona fursa katika kila mazingira na muda mwingine hata kushawishi mazingira yatengeneze fursa.
Wanyarwanda hawa 35,000 ambao walisalia mpakani wakikataliwa na nchi yao ya Rwanda na ugenini Uganda walikaa mpakani kwa kipindi kirefu sana. Ndipo hapa Paul Kagame akaanzisha programu maalumu za propaganda na kushawishi vijana wa Kitusi walioko pale mpakani (kati ya wale 35,000) kujiunga na NRA ya Museveni ambaye yeye na Fred Rwigyema walikuwa ni waanzilishi wake wakishirikiana na Museveni.
![]()
Nieleze pia jambo lingine muhimu…
Wakati haya yote yanaendelea, ikumbukwe kwamba tangu mwaka 1979 baada tu ya Idi Amin kupinduliwa kutoka madarakani, Watusi wote walioko Uganda walianzisha taasisi yao iliyoitwa Rwandese Alliance For National Unity (RANU). Hii ilikuwa ni taasisi ya kwanza ya kisiasa kuwa chini ya 'wakimbizi' Afrika Mashariki. Lengo kuu la Taasisi hii ilikiwa ni kuratibu mipango ya kurejesha watusi wote nchini Rwanda kwa amani.
Turejee tena kwenye kile nilichokuwa naeleza…
Vijana wa Kitusi ambao walikuwa mpakani pamoja na wale wengine 35,000 wakashawishiwa kujiunga na NRA ya akina Museveni, Rwigyema na Kagame.
Nilieleza kwa uzuri kabisa namna ambavyo Milton Obote aliondolewa madarakani na NRA… sasa mpaka mwaka 1986 ambapo Milton Obote alitolewa madarakani, NRA ililuwa na wapiganaji wapatao 16,000 na nusu yao walikuwa ni Watusi.!
NRA ikashika nchi, Museveni akawa Rais, Fred Rwigyema Waziri wa Ulinzi na Naibu Amiri Jeshi Mkuu, na Paul Kagame Mkuu wa Intelijensia ya Jeshi na Watusi wengi kupata nyadhifa za juu na nyeti katika jeshi na serikali ya Uganda.
Paul Kagame na Fred Rwigyema walitumia ushawishi wao na kuifanya serikali ya Museveni kutangaza kuwapokea tena Watusi wote ambao walisalia pale mpakani kutokana na kukataliwa na Rwanda na serikali ya Milton Obote. Lakini pia serikali ya Uganda ilitangaza kwamba Watusi wote ambao wamekaa Uganda kwa miaka 10 au zaidi watapatiwa uraia.
Huu ulikuwa ni moja kati ya wakati wa raha zaidi kwa Watusi. Ilikuwa ni neema kubwa. Shukrani zao japo zilikwenda kwa serikali la Uganda lakini shukrani za dhati na zaidi zilikwenda kwa vijana wao Paul Kagame na Fred Rwigyema kwa kufanikisha kuileta Neema hii.
Fred Rwigyema na Paul Kagame wakageuka kuwa mashujaa katika jamii ya Watusi.
Sasa basi…
Ile RANU ambayo nimeeleza hapo awali huwa ilikuwa inafanya Kongamano kuu kila mwaka kujadili uratibu wa mikakati ya kurejea tena Rwanda.
December mwaka 1987 likafanyika Kongamano kuu la saba la RANU jijini Kampala. Katika Kongamano hilo Fred Rwigyema akachaguliwa kiongozi wa taasisi hiyo na Paul Kagame akiwa Makamu wake.
Nafasi nyingine zote za uongozi na nafasi za kiutendaji waliwekwa maveterani ambao walipigana katika vita za kumng'oa Idi Amin na kumng'oa Milton Obote.
Kwa hiyo kufumba na kufumbua RANU ilibadilishwa kutoka kuwa taasisi ya kisiasa na kuwa chombo cha kijeshi. Na Rwigyema na Kagame hawakuishi hapo tu bali waliibadilisha jina RANU na kuwa Rwanda Patriotric Front (RPF).
Kwa hiyo ilikuwa rasmi sasa kwamba Paul Kagame na Fred Rwigyema walikuwa na misuli ya kijeshi kufanya kile ambacho walikuwa wanakiota tangu wangali watoto.
Walikuwa na maelfu ya vijana wa kitusi mikononi mwao ambao walikuwa na weledi wa kutosha wa kijeshi kutoka NRA ya Museveni na kwa sasa waliwasajili chini ya kikundi chao kipya cha RPF.
Sasa ulikuwa muda sahihi kabisa wa kwenda kuiweka Rwanda kwenye kiganja cha mikono yao na kuisuka upya vile ambavyo walihisi ni sahihi.
![]()
Fred Gisa Rwigyema
![]()
Yoweri Museveni
Jaribio la Kwanza - Octoba, 1990
Mwanzoni mwa mwezi huu octoba, Rais Juvenile Hibyarimana alikuwa amesafiri kwenda Marekani Kuhudhuiria Kongamano la Kimataifa kuhusu watoto ambalo liliandaliwa na Umoja wa Mataifa.
Rais Yoweri Museveni naye pia alikuwa Marekani kuhudhuria Kongamano hilo hilo.
Pual Kagame naye alikuwa Marekani kwa miezi kadhaa sasa kwa ajili ya kozi maalumu ya kijeshi katika chuo cha kijeshi cha Command and General Staff Collage kilichopo kambi ya Leavenwortg huko Kansas.
Kwa miezi kadhaa Kagame na Rwigyema walikuwa wakiwasiliana kwa simu kupanga mikakati ya kumuondoa madarakani Rais Juvenile Hibyarimana na serikali yake ya Kihutu.
Fursa hii ya Rais Hibyarimana kutowepo ndani ya nchi ilikuwa ni fursa adhimu kwao kutekeleza azma yao.
Kwa hiyo mpango ambao walikuwa wakiupanga kwa miezi kadhaa ulikuwa umefika muda wake wa kuutekeleza.
Kwa hiyo siku ya tarehe 1, october 1990 majira ya saa mbili na nusu usiku.… wanajeshi wa weledi wa juu (Special Forces) wenye asili ya Kitusi wapatao 50 waliondoka kutoka kwenye kambi zao za jeshi la Uganda kuufuata mpaka wa Rwanda na Uganda.
Walieleke moja kwa moja mpaka eneo la mpakani la Kagitumba ambako waliwatandika risasi walinzi wa mpaka mahali hapo na kusonga mbele kuingia Rwanda. Kama muda wa saa moja baadae walifuatiwa na maelfu mengine ya wanajeshi ambao walikuwa wamevalia sare za jeshi la Uganda.
Hawa waliluwa ni wanajeshi Uganda sawia kabisa lakini wenye asili ya Kitusi.
Walikuwa na silaha nzito nzito kama vile mashine guns, autocannons, vifaru, pamoja na rocket lauchers aina ya BM-21, vyote hivi vilitoka kwenye jeshi la Uganda.
Jeshi la serikali ya Rwanda walikuwa na wanajeshi wengi zaidi pamoja na vifaa bora zaidi kama vile magari ya kivita pamoja na helikopta ambazo walikiwa wamezipokea kama msaada kutoka kwa nchi ya Ufaransa miezi michache iliyopita. Lakini walikuwa wamezidiwa kete moja adhimu kwenye medani ya vita… hawakujiandaa!!
Shambulio hili lilikiwa ni la kushitukiza kwao na hawakuliona likija kwa hiyo vijana wa RPF walikuwa wamejiandaa kiakili na kimkakati kuzidi jeshi la Rwanda. Na zaidi ya yote walikuwa na 'mbabe wa vita' Fred Rwigyema akiwaongoza kwenye oparesheni hiyo ya kushtukiza.
Vijana wa RPF walienda kwa kasi mno na walikuwa wanafanikiwa kwa haraka mno kutimiza lengo. Ndani ya masaa machache walikuwa wameingia zaidi ya kilomita 60 ndani ya Rwanda waliuweka mji wa Gabiro mikononi mwao.
Ndani ya siku moja tu RPF walikuwa wamefanikiwa kwa kiwango kikubwa sana na ilikuwa dhahiri kwamba majeshi ya serikali yalikuwa yamezidiwa nguvu na RPF. Kulikuwa na kila dalili kwamba muda wowote kuanzia siku ya pili ya uvamizi huo wa RPF mji wa Kigali ulikuwa unaelekea kuwekwa chini ya Himaya ya RPF na huo ndio unaweza kuwa ndilo anguko la serikali ya Rais Juvenile Hibyarimana.
Lakini kuna jambo la ajabu kabisa likatokea. Jambo ambalo kwa kufikiria kwa haraka haraka lilikuwa haliwezekani kabisa. Katika siku ya pili vikosi vya RPF vikiwa vimewazidi nguvu majeshi ya serikali na wakielekea kuiweka kigali mikononi mwao… katika mzingira ya kutatanisha sana, mwanajeshi na jasusi mbobezi wa uwanja wa vita kuwahi kutokea ukanda huu wa Afrika Mashariki, Fred Rwigyema aliuwawa kwa kupigwa risasi.
Nasema ilikuwa ni jambo la ajabu kwa kuwa vijana wa RPF walikuwa wamewazidi nguvu majeshi ya serikali na walikuwa wanaelekea kuiweka mikononi mwao mji wa Kigali. Lakini jambo la ajabu zaidi Rwigyema aliuwawa akiwa kwenye base (kambini) sio akiwa 'front line' au kwenye mapambano.
Kila mtu kuanzia wapiganaji wa RPF na mpaka viongozi wa jeshi la Rwanda walibakiwa na bumbuwazi wasielewe ni nini ambacho kilikuwa kimetokea. Inawezakanaje Rwigyema auwawe kirahisi hivi tena akiwa kwenye base sio 'front line'? Kulikuwa na kila harufu ya hila kuhusika kwenye kifo hiki. Na mtu pekee mwenye uwezo wa weledi na uthubutu kumfanyia hila ya namna hii komando na jasusi mbobezi wa kaliba ya Fred Rwigyema ni mtu ambaye naye ni mwenye weledi na ubobezi wa kufanana na Rwigyema au kumzidi na si vinginevyo.
Ndipo hapa ambapo unadhihirika msemo wa kwamba kwenye maisha hakuna rafiki au adui wa kudumu… bali kitu pekee ambacho ni cha kudumu ni maslahi.
Yoweri Museveni ambaye nyuma ya pazia alikuwa anajua kila kitu kuhusu uvamizi huu na huku akisaidia kwa siri waasi wa RPF baada ya kupewa taarifa hii ya kuwawa kwa Rwigyema naye alipatwa na mshtuko mkubwa asielewe nini ambacho kilikuwa kimetokea.
Wote wawili, yeye na Kagame walikuwa nchini Marekani, Kagame akiwa Kansas na yeye Museveni akiwa New York. Moja kwa moja akainua simu kumpigia kagame akiwa na swali moja tu la kuuliza… "qu'est-ce qui s'est passé?" (Nini kimetokea?)
Alihisi kabisa… na pengine alijua kabisa kuwa Paul Kagame anajua cha zaidi kuhusi kifo cha Fred Rwigyema.
Itaendelea…
The Bold - 0718 096811
To Infinity and Beyond
Pls: Ni Follow, subscribe and nitafute WhatsApp
Huu uhondo usiuachie hapa tafadhali tunahitaji mwendelezo wake. Big upKaribu chief
Mkuu achana na huyu jamaa, anakulipisha elfu tano kila mwezi.Huu uhondo usiuachie hapa tafadhali tunahitaji mwendelezo wake. Big up
we jamaa ni hatari thanks sana kwa muendelezo huu nasubili sehemu ya 7 kwa hamu sanaKaribu chief
Kaka sehemu ya inayofuata ni lini? Maana kama hamu hapa imenipanda nataka kujua kilichojiri aiseee.Historia ya Kweli ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda
![]()
KILIO CHA MIFEREJI YA DAMU IENDAYO ETHIOPIA
SEHEMU YA KWANZA
“..kama unasoma ujumbe huu, muda huu… uko mpweke! Pengine ushahidi pekee uliobakia ni kijipande hiki cha maandishi. Sijui kama kuna yeyote kati yetu aliyesalimika kufika kizazi chenu mwaka huu mtakaosoma andishi langu. Sijui hata kama tumeshinda au tumeshindwa vita tunayopigana sasa hivi. Sijui, lakini naamini mwaka huu mliopo nyinyi sasa mwaweza kuwa na jibu sahihi. Vyovyote vile lakini jambo lililo dhahiri ni kwamba hakuna yeyote wa kizazi chetu mliye naye sasa hivi kwenye miaka yenu muusomapo ujumbe huu. Kwa hiyo wacha niwaeleze sisi tulikuwa akina nani, na kwa namna gani tulipambana mpaka tone la mwisho la damu mwilini mwetu ili kutetea kizazi chetu kisifutwe juu ya uso wa dunia. Wacha niwaeleze namna ambavyo japo tulikamuliwa damu mpaka kutiririka kufanya mifereji lakini lakini tulisimama kutetea kizazi chenu na ninyi watoto wetu. Wacha niwaeleze kisa kilichotikisa ulimwengu. Wacha niwaeleze kuhusu mifereji ya damu kwenda Ethiopia.!”
– Habib Anga alias The Bold
March 21, 1994 maeneo ya Uganda ambayo yanapakana na Rwanda, katika ziwa viktoria serikali ilituma vikosi vya jeshi kudhibiti eneo hilo kwa hali ya dharura. Agizo hili la serikali kutuma jeshi halikuwa kwa ajili ya kidhibiti eneo hilo kutoka kwa adui bali agizo lilikuwa ni kudhibiti eneo hilo dhidi ya maiti, maiti za binadamu. Sio maiti mbili au tatu, si mamia bali maelfu ya maiti za binadamu ambazo zilikuwa zinaingia ziwani Victoria zikiletwa na maji ya mto Kagera.
Maiti hizi zilikuwa nyingi kwa maelfu kiasi kwamba mapaka zilikuwa zinafanya maji yatoe harufu. Serikali ya Uganda ilituma jeshi eneo hili ili kudhibiti eneo hili maji yake yasitumiwe na wananchi kwa matumizi ya nyumbani au shughuli za uvuvi. Lakini jeshi lilikuwa eneo hili ili kuhakikisha kuwa taharuki iliyozuka baada ya maelfu ya miili hii kuonekana haigeuki na kuvuruga amanai katika eneo hili. Lakini pia jeshi lilikuwa hapa ili kubaini miili hii ilikuwa inatoka wapi.
Kadiri ambavyo jeshi la Uganda lilivyokuwa linafuatilia kwa kurudi nyuma kufuata mto Kagera ndivyo ambavyo walizidi kubaini kwamba maiti hizo zinaletwa na maji kutoka tawi la mto Kagera lililopita kusini mwa Rwanda. Na kadiri ambavyo walizidi kufuata chanzo cha maiti hizo zinakotoka ndivyo ambavyo walikuwa wanaikaribia Rwanda na maji ya mto rangi yake kuwa nyekundu zaidi.
Wanajeshi wa Uganda ambao walishiriki kwenye ukaguzi huu wa mto huu wanakiri kwamba licha ya baadhi yao kupigana mstari wa mbele kwenye vita mbali mbali lakini hakuna yeyote kati yao ambaye aliwahi kushuhudia ukatili mkubwa wa kiasi hiki.
Siku hii jeshi la Uganda linakisia kwamba waliokota si chini ya miili elfu kumi ya binadamu na yote ilionekana kuletwa na maji ya mto Kagera kutoka nchini Rwanda.
Ajabu ni kwamba miili yote hii ilikiwa inamfanano fulani. Maiti zote zilikuwa za watu warefu, wembamba, wenye nyuso ndefu na pua za kuchongoka. Haikuhitaji kufikiria sana kufahamu kuwa maiti hizi zilikuwa za watu wa kabila la Tusi (Tutsi).
Miezi kadhaa baadae ndipo ambapo jeshi la Uganda na ulimwengu wote walikuja kuelewa kwa nini maiti zilikuwa zinatupwa mto Kagera. Ni ujumbe gani ambao ulikuwa unajaribu kutumwa.
Kwamba Watusi nchini Rwanda walikuwa waapenda kujisifu kuwa mababu zao wana asili ya nchi ya Ethiopia. Kitendo hiki cha watesi wao kuwatupa mtoni, walikuwa wanawaua na wakiwa wanatupa maiti zao mto wanawaambia kwamba “wanawasafirisha warudi kwao Ethiopia ambako wamekuwa wakijisifu ndio asili yao.”
Sio kwamba jeshi la Uganda hawakuwa na taarifa juu ya hali tete iliyopo Rwanda kwa muda wa karibia wiki nzima iliyopita bali hawakujua kama hali hiyo tete ilikuwa ni ya kinyama kiasi hicho.
Wanajeshi hawa wa Uganda walikuwa wameshikwa na bumbuwazi na vihoro vilivyo wapasua mioyo kwa kuona miili hii elfu kumi ya binadamu isiyo na uhai. Kitu ambacho walikuwa hawakijua na hakuna ambaye alidhahania ni kwamba ndani ya siku mia moja zijazo ulimwengu ulikuwa unaenda kushuhudia moja ya tukio la kikatili zaidi tangu kuubwa kwa ulimwengu. Karibia maiti za binadamu milioni moja zikiwa zimetapakaa mitaani nchini Rwanda iking’ong’wa na nzi na kuliwa na mbwa.
![]()
GENESIS
Rwanda: Kabla ya Ukoloni
Asili rasmi kabisa ya watu wa kwanza kuishi katika eneo ambalo leo tubalitambua kama nchi ya Rwanda ni watu wa kabila la ‘Twa’ (Watwa). Kabila hili la wawindaji si la kibantu bali ni sehemu ya makabila yanayotambulika na wanahistoria kama ‘pygmy’ ambao sifa yao kuu ni ufupi. Mtu mzima anayetoka makabila ya namna hii anakadirwa kuwa na wastani wa urefu chini ya sentimita 150. Watwa waliishi Rwanda enzi za kale sana miaka ya 8000 BC na 3000 BC.
Kuanzia miaka ya 700 BC mpaka 1500 AD makabila ya Kibantu kutoka maeneo ya jirani yalianza kuhamia eneo hili.
Kuna nadharia mbali mbali kuhusu ni namna gani haswa makabila haya ya kibantu yalihamia hapa na baadae kupelekea kutokea Makabila ya sasa ya Wahutu na Watusi.
Nadharia ya kwanza inadai kwamba; Wahutu ndio walikuwa wa kwanza kuhamia eneo hili na kuanzisha shughuli za kilimo. Baadae watu wenye asili ya Ukushi (Watusi wa sasa) nao wakahamia kwenye eneo hili na kulitawala.
Nadharia ya Pili inadai kwamba; kuna uwezekano kwamba Watusi si wakushi bali ni wahamiaji tu kutoka maeneo ya jirani kipindi hicho cha kale ambao walihamia na kujichanganya na jamii waliyoikuta hapo (Wahutu) lakini wao walikuwa wafugaji. Chini ya nadharia hii inadai kwamba kuibuka kwa Wahutu na Watusi hakukutokana na kuwa na utofauti wa kinasaba au asili ya mababu bali ulitokana na utofauti wa kimadaraja/matabaka ya kijamii.
Tabaka la wale walio wa daraja la juu ambao walikuwa wafugaji walijitanabaisha kama Watusi wakati ambapo tabaka la chini ambao walikuwa wakulima walijitanabasha kama Wahutu.
Makabila haya yote matatu, Watwa, Wahutu na Watusi wanazungumza lugha moja na kwa wote kwa pamoja wanajulikana kama ‘Banyarwanda’.
Idadi ya watu ilipoongezeka katika eneo hili walianza kujitambua kupitia makundi madogo madogo yaliyoitwa ‘Ubwoko’ au ‘koo’ kwa kiswahili. Ilipofika katikati ya miaka ya 1700 koo nyingi ziliungana na kuunda ‘Falme’.
Moja ya Falme ambazo zilikuwa imara zaidi ulikuwa ni ‘Kingdom of Rwanda’ ambayo watawala wake wote walitokea katika koo ya Kitusi ya Nyiginya.
Ufalme huu ulifikia kileleni kipindi cha utawala wa Mfalme Kigeli Rwabugiri chini ya falsafa yake ya kujipanua na kuteka falme nyingine na kuzifanya sehemu ya Kingdom of Rwanda.
Chini ya Mfalme Rwabugiri alianzisha mfumi wa kiuchumi wa ‘ubuhake’ na baadae ‘uburetwa’.
Katika mifumo yote hii miwili, iliwanufaisha zaidi Watusi na kuwafanya Wahutu kama vijakazi wao kuwafanyia kazi za uzalishaji na kuwa askari vitani kwa ujira wa kupata fursa ya kumiliki mifugo na kutumia ardhi.
Watusi walipaa juu zaidi na kuwa raia daraja la kwanza ma Wahutu kubakia kuwa tabaka la chini kabisa ndani ya Kingdom of Rwanda.
Rwanda: Wakati wa Ukoloni
Mkutano wa Berlin wa mwaka 1884 ulilitoa eneo hili kuwa koloni la nchi ya Ujerumani. Wajerumani walitawala eneo hili kwa kushirikiana na Mfalme na hivyo kuwapa wepesi wa kutawala koloni bila kuwa na askari wengi wa kijerumani ndani ya ardhi ya Rwanda. Yuhi V Musinga ndiye walikuwa Mfalme wa Rwanda kwa kipindi hiki na anakumbukwa zaidi kwa kuwapokea Wajerumani kwa mikono miwili.
![]()
Ikulu ya Mfalme wa Rwanda maeneo ya Nyanza
Wajerumani ndio walikuwa watu wa kwanza kuanza kuwapandikizia Watusi kasumba ya kuwa wao si Wabantu. Wakoloni wa Ujerumani ndio ambao walieneza propaganda kwa kuwafundisha Watusi kwamba kutokana na tafiti zao za kina wamegundua kwamba wao (Watusi) mababu zao wa kale walihamia eneo hilo kutokea Ethiopia. Hivyo wakawashawishi kuamini kwamba Watusi wana vinasaba vya ‘uzungu’ (Caucasian) na hivyo ni wao pekee ndani ya Rwanda walistahili kupata nafasi za ajira kusaidizana kazi na wazungu chini ya utawala huo wa Wajerumani.
Katika Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia, Ubelgiji iliziteka Rwanda na Burundi kutoka mikononi mwa Ujerumani na mwaka 1919 League Of Nations ilizifanya rasmi nchi hizo kuwa makoloni ya Ubelgiji.
Mwanzoni Wakoloni wa Ubelgiji walianza kuitawala Rwanda kwa mtindo ule ule wa kushirikiana na Ufalme lakini baadae wakajilimbikizia madaraka yote ya kutawala kama ambavyo walifanya kwenye koloni lao la Kongo.
Baadae wakaanza ‘kutaifisha’ mali za Wanyarwanda katika mfumo wa kufanana kabisa na mfumo wa asili wa uburetwa na walioathirika zaidi na kampeni hii ya utaifishaji walikuwa ni Wahutu.
Ardhi yao ilinyang’anywa… Mifugo ilitwaliwa na kuwafanya Wahutu kuwa si tu vijakazi wa Wakoloni bali pia vijakazi wa Watusi.
Mwanzoni mwa miaka ya 1930s Ubelgiji walifanya upanuazi mkubwa wa sekta ya Elimu, afya na ajira za umma. Lakini wanufaika wakuu walikuwa ni Watusi.
Mwaka 1935 Ubelgiji walifanya kitu ch a ajabu sana ambacho kilipanua zaidi mpasuko wa kijamii na kitabaka uliopo ndani ya Rwanda. Walianzisha mfumo wa raia wote kuwa na vitambulisho. Vitambulisho hivi viliwatambua raia wote katika makundi manne kulingana na makabila yao. Watwa, Wahutu, Watusi na Raia wa kuomba (Naturalised).
Kutokana na Watusi kuwa ndio raia wa daraja la kwanza na tabaka la juu huku Wahutu wakiwa ni watu hafifu wa kudharaulika nchini humo, ilifikia hatua Wahutu wenye mali au ushawishi walikuwa wanahonga fedha ili kupatiwa vitambulisho vya Kuonyesha ni Watusi na watawala hawakuwapa Utusi kamili bali waliwapa ‘utusi wa heshima’ (Honorary Tutsi).
Hadhi ya Wahutu wote iliendelea kushuka kwa kasi wakionekana ni kabila na kizazi cha “Washenzi” huku Watusi wakionekana ndicho kizazi cha “wastaarabu” na kabila lenye darja.
Lakini kuna suala ambalo lilifanyika mwanzoni likionekana kuwa na manufaa makubwa lakini kadiri siku zilivyokwenda lilianza kuwa kama mkuki mgongoni. Kanisa Katoliki.
Kanisa Katoliki lilikuwa limeenea sana nchini Rwanda na raia wake wengi wakiwa ni waumini wa kanisa hilo. Tukumbuke kwamba tangu kipindi hicho Wahutu ndio walikuwa idadi kubwa zaidi ya raia wote ndani ya Rwanda. Hii ilimaanisha pia kwamba waumini wengi wa kanisa Katoliki walikuwa ni Wahutu.
Kwa kiasi fulani ndani ya kanisa Katoliki mapadri na watawa wengine walikuwa wanajisikia hatia kuacha waumini wao kuwekwa kwenye kundi la kizazi cha “washenzi” na kudharaulika ndani ya jamii. Kwa hiyo zikaanza juhudi za makusudi za kanisa katoliki kutoa elimu kwa vijana wenye asili ya Kihutu.
Baada ya miaka kadhaa kukaanza kuwepo walau kidogo uwiano wa wasomi wa Kihutu na Kitusi.
Mwaka 1957, mwezi March kikundi cha wasomi na watu wenye ushawishi wenye asili ya Kihutu walifanya jambo la “kimapinduzi” ambalo lilipanda mbegu mpya kwenye nafsi za watu wa kabila na kizazi cha cha Kihutu. Waliandaa waraka ulioitwa _'Manifeste des Bahutu' (Bahutu Manifesto).
Huu ndio ulikuwa waraka wa kwanza rasmi kubainisha kwamba Wahutu na Watusi ni mbari (race) mbili tofauti.
Katika waraka huu, wasomi hawa na watu hawa wenye ushawishi walijenga hoja kuu kwamba… Watusi wanapaswa kutoka kwenye jukumu lao walilojivesha la kuwa watawala wa Rwanda na badala yake nafasi hiyo ya kutawala Rwanda wapewe Wahutu. Hoja yao hii waliijenga kwenye nadharia ambayo wenyewe waliita “Statistical Law”, kwamba kitakwimu Wahutu ni wengi mno kushinda Watusi. Si sawa wakiendelea kutawaliwa na kufanywa vijakazi na Watusi.
Wanasema kwamba kabla kibanda cha nyasi kuungua kwanza utaanza kukiona kinafuka moshi. Kuna vugu vugu lilianza chini kwa chini ndani ya Rwanda.
Waraka huu… Bahutu Manifesto, ulitoka tarehe 4 March mwaka 1957. Japokuwa ilikuwa ni miaka takribani 37 kabla ya mwaka 1994, lakini ndio siku ambayo mbegu ya mauaji ya kimbari ilipandwa.
Usikose sehemu inayofuata….
Itaendelea…
The Bold
To Infinity and Beyond.
0718 096 811 (Whatsapp Only)
BOFYA HAPA KUSOMA SEHEMU YA PILI
BOFYA HAPA KUSOMA SEHEMU YA TATU
BOFYA HAPA KUSOMA SEHEMU YA NNE
BOFYA HAPA KUSOMA SEHEMU YA TANO
BOFYA HAPA KUSOMA SEHEMU YA SITA