KILIO CHA MIFEREJI YA DAMU IENDAYI ETHIOPIA
SEHEMU YA 12
KUUWAWA KWA RAIS JUVENILE HIBYARIMANA NA KUANZA KWA MAUAJI YA KIMBARI
Moja kati ya visa vyenye utata zaidi kwenye historia ya Africa basi ni tukio la mauaji ya Rais Juvenile Habyarimana.
Na utata huu unakuwa mkubwa zaidi kutokana na hata jumuiya ya Umoja wa Mataifa kuficha ficha mno na kukwepa kulijadili suala hili kwa uwazi.
Lakini utata huu unakuwa mkubwa zaidi kutokana na kuwa na zaidi ya makundi matatu ambayo yote yalikuwa na dhamira ya kuona Rais Habyarimana anaondoka madarakani kwa maslahi yao.
Kundi la kwanza lilikuwa ni 'Hutu Power', wahutu wenye itikadi kali dhidi ya Watusi. Hawa katika kipindi hiki walikuwa wamechukizwa mno na kitendo cha Rais Habyarimana kujiingiza kwa nguvu zote kwenye mazungumzo ya amani na RPF jijini Arusha. Katika kipindi hiki walikuwa wanamuona kama ni kikwazo kwao kutimiza azma yao ya kuwa na Rwanda yenye idadi sifuri ya Watusi. Walikuwa wanamuona Rais Habyarimana kama daraja la ambalo linaleta tishio la 'adui' zao hao kurejea tena kwenye utawala wa nch na kurejesha tena 'Ufalme wa Watusi' na kuwafanya wahutu watumwa. Kwa hiyo moja kwa moja wahutu wenye msimamo mkali walikuwa na 'motive' ya kutaka kuona Rais Habyarimana hayupo.
Kundi la Pili ni RPF na Kagame mwenyewe. Hawa nia yao kuu ilikuwa ni kushika madaraka na pia kukomesha manyanyaso ya Watusi ndani ya Rwanda. Rais Habyarimana licha ya kukubali kurudi kwenye meza ya majadiliano lakini ilikuwa dhahiri kabisa kwamba ndani ya moyo wake hakuwa tayari kuachia madaraka. Lakini pia Kagame alimuona Habyarimana si kama mtu mwenye uwezo wa kuwadhibiti Wahutu wenzake wenye msimamo mkali waache kuendeleza mauaji ya watusi na pia hakumuona kama anatosha kwenye kuijenga upya Rwanda na kuwafanya Wahutu na Watusi wakubali kuishi pamoja. Kwa hiyo RPF na Kagame walikuwa na 'motive' pia ya kuona Rais Habyarimana hayupo.
Kundi la tatu hili huwa halizungumzwi kabisa na hata kwenye maandiko yote yanayoeleza utata wa kisa hiki huwa hawaligusii hili jambo. Lakini ni kundi muhimu sana ambalo nalo walikuwa na kila sababu ya kuona Rais Habyarimana hayupo. Kundi hili ni nchi za nje zenye maslahi ya moja kwa moja na Rwanda, ambazo Marekani, Ubelgiji na Ufaransa.
Hawa walikuwa na mslahi ya kijeshi, kidiplomasia na kihistoria. Na ni wazi licha ya kumsaidia sana Rais Habyarimana lakini ilifika kipindi waliuona ukweli kwamba Rais Habyarimana hakuwa na uwezo wa kuituliza Rwanda na kuiunganisha.
Makundi haya matatu kila moja lilikuwa na motive ya kutaka kuona Habyarimana hayupo. Na hii ndio sababu ya kwa nini kisa hili kimejawa na utata mkubwa sana. Unaweza kutengeneza nadharia ya kulituhumu kundi lolote lile kati ya haya.
Na ndio maana katika sehemu hii nimedhamiria kuandika maoni yangu binafsi kwa 100% namna ambavyo naliona suala hili. Si lazima sana kukubaliana na hiki nitakachoandika kwenye sehemu hii, lakini binafsi hiki ndicho ninachoamini kilitokea na tunaweza kutumia maoni haya kama kichocheo cha kuanzisha mjadala wa hoja kwa wale ambao wanaamini labda wahusika walikuwa ni kundi lingine.
(Unaweza kunitumia maoni yako inbox na nitayaweka hapa kwenye group).
Maoni yangu ni haya hapa;
Tuanzie mwanzo kabisa….
Hebu kwanza tuangalie tukio hili katika ujumla wake namna ambavyo lilitokea kabla hatujachambua dalili za wale waliohusika kwenye hili tukio.
Rais Habyarimana alikuwa kwenye ziara yake ya nchi za maziwa makuu ambayo aliianza tarehe 4 April mwaka 1994 (siku mbili kabla ya ndege yake kudunguliwa).
Ziara hii aliinza kwa kumtembelea swahiba wake mkubwa Rais za Zaire Jenerali Mobutu Sese Seko. Alikaa Zaire kwa muda wa siku mbili na kisha siku ya tarehe 6 April aliruka kuja Dar es Salaam, hapa Tanzania kwenye mkutano wa wakuu wa nchi ambao ulikuwa umeitishwa na mwenyeji wao Rais Ali Hassan Mwinyi.
Jioni ya siku hiyo baada ya mkutano huo wa wakuu wa nchi kuisha Rais Juvenile Hibyarimana aliamua kurejea nchini kwake Rwanda.
Rais mpya wa Burundi Mhe. Cyprien Ntaryamira ambaye alikuwa na miezi miwili tu tangu achaguliwe kuwa rais wa Burundi ambaye naye alikuwepo kwenye kikao cha Dar es Salaam aliomba 'lifti' kwenye ndege ya Rais Habyarimana. Rais Cyprien alipendelea apande ndege ya swahiba wake, muhutu mwenzake Habyarimana kutokana na ndege hiyo ya Habyarimana kuwa na kasi kubwa na ya kisasa zaidi.
Rais Habyarimana alikuwa anatumia ndege aina ya Dassault Falcon 50. Kwa kipindi kile cha mwanzoni mwa miaka ya tisini, ndege hizi zilikuwa ni moja ya ndege bora zaidi za daraja la kibiashara na hata matumizi ya kijeshi na ilikuwa inagharimu zaidi ya shilingi bilioni 45 za kitanzania kuinunua.
Ndege za Dassault Falcon 50 zilitengenezwa na kampuni ya Dassault Aviation kwa ajili ya wateja wao ambao walikuwa ni jeshi la anga la Ufaransa, Afrika ya Kusini, Ureno na Italia na zingali zinatumika mpaka leo hii.
Kwa hiyo waweza kupata picha ni kwa jinsi gani ndege hii ya Rais Habyarimana ilikuwa adhimu. Ndege hii Rais Habyarimana alipewa na serikali ya Ufaransa kama 'zawadi' na hata marubani ambao walikuwa wanamuendesha walikuwa ni raia wa Ufaransa.
Kwa hiyo jioni hii ya tarehe 6 April 1994 ndege iliruka kutoka uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere (Kipindi kile ukiitwa Dar es Salaam International Airport) ndani yake ikiwa na watu kumi na mbili.
- Rais Juvenile Habyarimana
- Rais Cyprien Ntaryamira
- Bernard Ciza (Waziri wa Kazi wa Burundi)
- Cyraque Simbizi (Waziri wa Mawasiliano wa Burundi)
- Meja Jenerali Déogratias Nsambimana (Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Rwanda)
- Meja Thaddée Bagaragaza (Mpambe wa Rais Habyarimana)
- Kanali Elie Sagatwa (Kiongozi wa Baraza la kijeshi la Rais wa Rwanda)
- Juvénal Renaho (Mshauri wa Rais wa Rwanda kuhusu masuala ya Kimataifa)
- Dr. Emmanuel Akingeneye (Daktari wa Rais Habyarimana)
- Jacky Héraud (Rubani)
- Jean-Pierre Minaberry (Rubani)
- Jean-Micheo Perrine (Injinia wa ndege)
Hawa ndio watu wote ambao walikuwa ndani ya ndege ya Rais Habyarimana alipokuwa anarejea Kigali Rwanda.
Majira ya kama saa mbili na dakika ishirini hivi usiku ndege ya Rais Habyarimana ilikuwa iko juu ya anga la uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kigali ikizunguka kabla ya kufanya 'final approach'.
Lakini katika muda huu huu pia angani kulikuwa na ndege ya kijeshi aina ya C-130 Hercules ambayo ilikuwa inamilikiwa na jeshi la ubelgiji ikiwa imebeba wanajeshi sehemu ya vikosi vya UNAMIR ambao waliokuwa wanarejea kutoka likizo nchini kwao.
Ndege hii iliamuliwa kubakia angani kwanza wapishe ndege ya rais kutua.
Dassault Falcon 50
Ndege ya rais ilipata ruhusa kutua na ikaanza kufanya final approach. Lakini ikiwa kwenye 'approach slope' (inateremka kutoka angani ili kutua) ghafla ilishuhudiwa kitu kama moto kutoka ardhini ukipanda kwa kasi kubwa kuelekea juu usawa ule ule wa ndege inavyoshuka kutua. Lilikuwa ni bomu, "surface-to-air missile".
Bomu hili la kwanza lilipiga bawa la moja la ndege. Kufumba na kufumbua bomu lingine lilirushwa na kuipata ndege mkiani.
Ndege ilianza kuwaka moto ikiwa bado huku huko juu angani na kupoteza muelekeo.
Makazi ya Rais, Ikulu ya Kanombe yalikuwa karibu kabisa na uwanja wa ndege wa Kigali. Ni kama 'pua na mdomo'… umbali wa kilomita mbili tu kutoka uwanja wa ndege na kufika kwenye Kasri la Rais Juvenaile Habyarimana. Ndege ilipopoteza uelekeo baada ya kuwaka moto angani ilienda kudondokea kwenye bustani ya Ikulu na kulipuka kwa moto.
Watu kadhaa walishuhudia tukio hili likitokea lakini wengi hawakujua hasa ni nini kilikuwa kimetokea na hata wale waliojua kuwa ilikuwa ni ndege imedondoka hakuna ambaye alikuwa na hakika ilikuwa ni ndege ya nani au imembeba nani.
Sintofahamu hii ilizua taharuki kubwa sana. Walinzi wa Rais ambao walikuwa uwanja wa ndege kumpokea Rais waliwaweka watu wote waliopo uwanja wa ndege chini ya ulinzi.
Pia kulikuwa na wanajeshi wa Ubelgiji kama sehemu ya vikosi vya UNAMIR ambao walikuwa wanalinda maeneo ya nje kuzunguka uwanja wa ndege walizungukwa nao pia na Kikosi hiki maalumu cha ulinzi wa Rais na kupokonywa silaha.
Ile ndege ya kijeshi ya Ubelgiji kule angani ilikatazwa kutua na kuamuriwa kwenda kutua jijini Nairobi nchini Kenya.
Kwenye kambi ya jeshi ya pale Kanombe, ilipigwa mbiu ya kijeshi kuashiria kwamba kambi imevamiwa na RPF. Wanajeshi wote walijikusanya na kuchukua silaha za kivita tayari kwa mapambano.
Kwenye viwanja vya parade kikosi maalumu cha makomando nacho tayari kilokuwa kimejikusanya majira ya saa tatu kamili usiku.
Maafisa wa juu wa jeshi wa hapo Kigali walipiga simu mpaka Wizara ya Ulinzi kwa waziri ili kuweza kupata maelezo yoyote yale kama yapo.
Bahati mbaya Waziri wa Ulinzi Augustin Bizimana alikuwa nje ya nchi. Afisa ambaye alipokea simu hiyo ya wanajeshi hakufanikiwa pia kumpata Kanali Théoneste Bagorosa ambaye alikuwa mkurugenzi wa Ofisi ya Waziri wa Ulinzi. Kanali Bagorosa alikuwa kwenye sherehe ya kuwapokea wanajeshi kutpka Bangladesh kama sehemu ya vikosi vya UNAMIR.
Kutokana na sintofahamu ya nini hasa kilikuwa kimetokea, katika mfumo wa mawasiliano ya jeshi kuliripotiwa kwamba ghala la silaha la UNAMIR la kigali lilikuwa limelipuka.
Taarifa hii ilimfikia kamanda wa vikosi vya UNAMIR, Jenerali Dallaire na akamuamuru kamanda wa wanajeshi wa UNAMIR waliopo mji wa kigali aliyeitwa Luc Marchal aende mpaka sehemu iliyotokea mlipuko na ili kuchunguza ni nini hasa kilikuwa kimetokea.
Sasa utata wote kuhusu tukio hili ambao tunao mpaka leo hii… 'mchezo mchafu' ulianza kufanyika hapa.
Wanajeshi wa UNAMIR waliotumwa na Jenerali Dallaire kwenda kuchunguza mlipuko unahusu nini (walikiwa wanajeshi wa ubelgiji) walikutana na kizuizi cha wanajeshi wa Rwanda umbali wa mita kadhaa kukaribia Ikulu ya Rais. Kinyume kabisa na sheria na protokali na maadili ya kijeshi, wanajeshi wa Rwanda waliwaweka chini ya Ulinzi wanajeshi hawa wa UNAMIR na kwenda kuwaweka kwenye uwanja wa ndege pamoja na wenzao wengine wale wa awali.
Ajabu ni kwamba dakika chache baadae wanajeshi wawili wa Ufaransa (wanajeshi wa Ufaransa hawakuwa sehemu ya UNAMIR) walifika eneo hili la Ikulu ndege ilipodondoka na kuchukua "flight data recorder" ambayo ilikiwa imeshapatikana na wanajeshi wa Rwanda wanaolinda hapo Ikulu. (Kifaa hii mpaka leo hii hakijulikani kilipelekwa wapi au kiko wapi).
Kisha jeshi la Ufaransa wakapiga simu kwa Jenerali Dallaire kamanda wa vikosi vyote vya UNAMIR nchini Rwanda kumuomba awaachie wao suala zima la kuchunguza mlipuko huo. Bila kusita sita au kujiuliza mara mbili, Jenerali Dallaire alikataa vikali na mzozo mkali ukatokea.
Dallaire kwa muda ambao alikuwa amekaa ndani ya Rwanda alokuwa ameng'amua dhamira ya majeshi ya Ufaransa nchini humo ilikuwa ni ovu kabisa na hivyo hakuwa na imani nao kabisa kabisa.
Wakiwa kwenye mabishano hayo ghafla Dallaire alipigiwa simu kutoka kwa Agathe Uwilingiyimana ambaye alikuwa ni Waziri Mkuu wa Rwanda kumweleza kwamba Mawaziri wake wote ambao wana msimamo mkali (Hutu Hardliners) hawapati kwenye mawasiliano ya simu na hajui waliko.
Tukumbuke kwamba mpaka muda huu hakuna ambaye alikuwa na hakika kwamba ile iliyodunguliwa ilikuwa ni ndege ya Rais Habyarimana.
Dallaire alimlalamikia pia Agathe Uwilingiyimana kwamba wanajeshi wanaolinda Ikulu wanawazuia kufanya kazi yao na wanahisi kuna kitu cha siri wanakifanya wao kwa kushirikiana na jeshi la Ufaransa.
Kwa kutambua kwamba kwa mujibu utaratibu wa mtiririko wa kimadaraka kama kweli aliyedunguliwa alikuwa ni Rais Habyarimana basi Agathe Uwilingiyimana ndiye anachukua madaraka. Hivyo alikiwa anahitaji ushauri wake wa nini hasa cha kufanya. Agathe alikata simu kwa madai kwamba anahitaji kwanza kupata uhakika wa nini kimetokea ndipo atajua nini kifanyike na atamjulisha kwa simu.
Dallaire alimshirikisha taarifa hii mkuu wa kitengo cha siasa cha UNAMIR aliyeitwa Jacquies-Roger Booh-Booh. Na Jacquise alimshauri wasubiri kwanza taarifa rasmi kutoka kwa waziri mkuh Agathe Uwilingiyimana.
Kanombe Presidential Palace
Alipomaliza tu kuongea na simu na Jacquice Dallaire alipokea simu kutoka kwa Ephrem Rwabalinda ambaye alikuwa ni mwakilishi wa serikali ya Rwanda kwenye vikosi vya UNAMIR na alimueleza kuwa anahitajika kwenye kikao. Alipomuuliza kikao cha nini? Alijibiwa kwamba ni kikao cha Kamati ya dharura ya jeshi.
Dallaire alishangaa maana mwenye mamlaka ya kuitisha kikao hiki kwa nchi ya Rwanda alikuwa ni mnadhimu mkuu wa jeshi ambaye alisafiri na Rais kwenda Tanzania.
Ephrem Rwabalinda alijibu kuwa kikao kimeitishwa na Kanali Théoneste Bagorosa. Ambaye anajulikana kwa msimamo wake mkali dhidi ya watusi.
Dallaire aling'amua haraka kwamba kuna kitu ambacho si cha kawaida kilikuwa kinaendelea na kwa namna suala hilo linavyokwenda, kulikuwa na mkono wa mataifa ya nje na hata RPF nyuma ya pazia.
Nitarudi kueleza...
Habibu B. Anga alias 'The Bod' - 0718 096 811
WhatsApp, subscribe and Follow
To Infinity and Beyond