KINACHOTUSUMBUA BARABARANI NI ULIMBUKENI, YAANI MTAZAMO NA KUKOSA UTAMADUNI WA USALAMA BARABARANI.
Kinachogomba kwetu sisi ni Kukosa utamaduni wa Usalama Barabarani. Huu sio utamaduni wetu. Sio utamaduni wa wamiliki au waajiri wetu;
Sio utamaduni wa Mtanzania mmoja mmoja;
Sio utamaduni wa dereva; wala
Sio utamaduni wa abiria.
Ndio maana kila tunachoambiwa kuhusu usalama barabarani tunaona kama tunalazimishwa tu.
Madereva vyuoni hawafundishwi usalama barabarani, bali wanafundishwa alama na michoro ya barabarani na kujua kuliongoza gari. Usalama barabarani ni zaidi ya alama, michoro na kujua kupeleka gari mbele au nyuma.
Kwetu sisi kujua kuendesha gari au kumiliki gari ni ulimbukeni. Wachache sana tumezaliwa tukakuta magari majumbani kwetu. Wengi tunayakutia ukubwani. Kwa hiyo maisha na matamanio yetu yanakuwa kuendesha gari kuliko usalama wenyewe. Kwa ufupi, sisi ni LIMBUKENI.
Ndio maana utaona mtu akijua kuendesha gari anafurahi halali hata usingizi. Akipewa kuendesha gari kama ajira anafurahi kupitiliza hata mkataba haulizi, anachojali yeye ni chombo. Mtu akifanikiwa kumiliki gari, ndo kabisaa. Matangazo kijiji kizima na ndio maana atataka aendeshe gari lake mwenyewe kutoka Dar hadi Kijijini akawaoneshe wazazi wake.
Tusipoendesha gari kwa kukimbiza sana tunaona kama hatujaendesha vile. Tunaona kama watu wanatudharau hatujui kuendesha. Dereva hataki dereva mwingine akae mbele yake kwani huo ni udhaifuu. Hata kama hawajaagana safari na huyo mwenzake atahakikisha hapitwi.
Tena madereva wa mabasi ni LIMBUKENI zaidi. Wee utajua tu kutokana na stori zao Kijiwe Nongwa au Mti majungu pale au kwenye basi, utasikia dah ile chuma kali kishenzi. Dah! Yaani hii mashine moto wa kuotea mbali, hili jiko hugusi hiliii. Yaani wee tukitoka hapa tuelekee Mwanza, hunipiti hata dakika 1 tu. Kwa ufupi Mwendo ni ufahari, Ovateki ya gari moja au zaidi ni ufahari.
Ndio maana madereva wa mabasi utaongea nao saa hizi hapa. Watakusikiliza, watakuelewa vizurii, ngoja wapande kwenye siti zao washike usukani utaona aisee. Kila mlichozungumza wakiwa chini wamesimama, wamesahau kabisaa. Utadhani sio wale waliokuwa wakiitikia ndio, ndio, ndio. Ndio maana utaona dereva akipigiwa miluzi au kushangiliwa anavyochanganyikiwa. Anapandisha mori, anajiona bonge la shujaa, anataka hata mwanae mdogo au mkewe nyumbani angekuwepo aone jinsi huko njiani alivyotengeneza heshima. Akiona ameendesha hamumsifu, hadi anaweza kwenda kwa mganga kujiuliza kuna nini mbona jamaa hawanishangilii kabisa na kupiga gia kote hukuu?
Hivyo, tuna kazi kubwa sana ya kujenga Utamaduni wa usalama barabarani, utamaduni ambao watu tangu wakiwa wadogo wataona hili ni jukumu letu sote. Wataona magari ni kitu cha kawaida sana. Wataona kujua kuendesha ni kama kupata ujuzi mwingine wowote. Wataondoa mtazamo kwamba kupitwa na gari nyingine ni udhaifu, watafahamu kwamba barabarani magari yanatofautiana spidi, na kila gari dereva wake ana ratiba yake tofauti na ya kwake.
RSAadmin1
RSA Tanzania
Usalama Barabarani ni Jukumu Letu Sote.