Riwaya :Mpango WA kongo
Sehemu ya nane
Lakini mbali na hivyo alikuwa na mtego wake kwa yule mhudumu mana kama mhudumu akisimama kutoa chenji asimkute, basi lazima atatoka nje kumtafuta na ndio mana alikuwa anaelekea kwenye nyumba za kanisa ili atizame vizuri harakati za kuingia na kutoka ndani ya mgahawa ule wa Tunde.
Haikuwa dakika nyingi alichokitarajia alikiona!!
****
Mhudumu alipigwa na butwaa bada ya kuinuka na kumkosa mteja wake.
Akapagawa!!.
Alipagawa kwa sababu hakudhani, sekunde chache vile mtu ampotee kirahisi tu.
Akajaribu kungojea dakika moja au zaidi, lakini tofauti na matarajio yake hakumuona Honda.
Akaamua kutoka nje lau aone uelekeo aliopitia ili tarifa yake ikamilike kwa wakubwa wake.
Mhudumu yule alitoka hadi nje, akaangaza kushoto na kulia hakuona mtu wala kivuli chake.
Shiiit!!” mhudumu akamaka huku mikono ikiwa imeshika kiuno asijue afuate lipi.
Akiwa hajui lipi afanye mara gari ikasimama karibu na miguu yake na hakujiuliza mara mbili akasogea kwenye kioo cha upande wa dereva,akasikiliza kidogo kisha akarudi akandoka kurudi mgahawani.
Kutokea pale alipokuwa ametulia; Honda aliyaona yote yaliofanywa na mhudumu yule nje ya mlango wa mgahawa wa Tunde.
Hata wakati gari inakuja na kusimama na kisha kuzungumza na walioko ndani ya gari, yote Honda aliyaona na sasa alitaka kuona watu wale waliokuwa ndani ya gari wangelifanya nini, lakini pia hakujua wapo wangapi japo aliamini ni zaidi ya mtu mmoja.
Aliendelea kusubiri hadi aone hatima ya watu wale.
Baada ya dakika kadhaa milango ya nyuma ya ile gari ikafunguliwa na kutoka kila upande wakashuka wanaume wawili waliojazia kimazoezi hasa. Wanaume wale wakaangaza huku na huko kisha wakaingia ndani ya mgahawa ule wa Tunde.
Katika hesabu za Honda aliamini ndani ya gari kutakuwa bado na watu wawili,mmoja dereva na mwingine yupo upande wa pili wa dereva.
Kwa kasi aliambaa na kuta za nyumba kadhaa kisha bila kuonesha tashwititi yoyote akavuka barabara huku hesabu zake zikiwa ni namna ataweza kuifikia ile gari bila kutiliwa shaka.
Alipovuka barabara tu akainamisha uso chini kisha akaanza kutembea kama mlemavu mwenye mguu mmoja mfupi na mwingine mfupi huku mkoba ukiwa unaning’inia mgongoni.
Hila za Honda zikazaa matunda, hadi analifikia lile gari hakuna aliekuwa amemtilia shaka na kwa kasi ya hewa akafungua mlango wa nyuma na bila kujiuliza akakaa kwenye kiti huku akiwa amewaelekezea bastola wale watu wawili waliokuwa wamekaa viti vya mbele wakiwa na mzubao usio semekana huku dhahiri hofu ikiwa juu yao.
“ondoeni gari hapa!” alisema Honda huku akiwa makini ili asifanyiwe fitina.
Hakuna aliemjibu wala kutekeleza amri yake nae akajua jamaa wanapoteza muda ili wale mabaunsa watokee na wakitokea hatari ipo kwake tu.
Hilo kamwe hakutaka litokee.
Bastola yake iliokuwa na kiwambo cha kuzuia sauti ikatema jiwe la moto na kupenya katikati ya uti wa mgogo wa mtu aliekuwa upande wa kushoto wa dereva na wala mtu yule hakuomba hata maji akawa hana mawasiliano huku damu ikimwagika kama bomba bovu.
Dereva hakuwa na namna, akaiondoa gari bila kujua ni wapi anapaswa kuelekea.
“endesha hadi nitakapokupa maelekezo mengine.” Sauti kavu ya Honda ikaunguruma bila chembe ya mzaha.
****
Safari ya Honda ilikuwa imegubikwa na ukimya wa kutisha na baada ya kitambo kidogo Honda akamwelekeza pahali alipopswa kugesha gari.
Mateka aliegesha gari kando kidogo ya nyumba ya marehemu Bulembo na
Baada Yakuhakikisha mateka wake amezima gari, kwa kasi ya radi akampiga kwa kitako cha bastola chini kidogo ya kisogo na mateka wake akapoteza fahamu hivyo ndani ya gari akawa na watu wawili, mmoja hana fahamu na mwingine bila uhai.
Haraka akashuka na kulekea lango la kuingilia ndani ya nyumba ya Bulembo na alitegemea kukuta utepe wa polisi wa kuzuia aisehusika kuingia pale na ndivyo ilikuwa.
Licha ya kuwapo utepe, pia kuliwa kimya sana kuashiria hakuna askari anaelinda pale na kuhakikisha zaidi akaingia hadi ndani ya utepe na kujaribu kuita ila hakuitikiwa zaidi alisikia sauti yake tu ikitengeneza mwangwi kwenye eneo pweke.
Haraka akarudi kwenye gari na kumchukua mateka wake ambae bado alikuwa amepoteza fahamu, akaingia nae moja kwa moja ndani na huko akamfunga vizuri kwenye kiti kisha akarudi ndani ya gari na kuliondoa kurudi walikotokea ambapo kwa kitambo fulani akaingia njia za vichochoro kulitelekeza gari ile na maiti yake. Huku akichukua baadhi ya vitu alivyodhani vinaweza kumsaidia.
Alikodi usafiri binafsi na kurudishwa hadi karibu na nyumba ya Bulembo, akalipa pesa kisha akaelekea kwenye kichochoro fulani lengo likiwa ni kumchanganya dereva endapo akibanwa huko ili atoe taarifa zake.
Huko huko alikopitia akajikuta yupo ndani ya mitaa yenye nyumba anayoihitaji.
Alipokwisha kuingia ndani, moja kwa moja akaanza upekuzi wake huku akiwa amemweka mateka wake kama kiporo.
Licha ya kukuta ukaguzi wa hali ya juu lakini bado aliamini kuna kitu kitakuwa mle ndani chenye kuweza kumsaidia hasa katika mambo matatu makubwa.
La kwanza ni kujua mhusika wa mauaji ya Bulembo na balozi Aly Sapi, lakini kubwa zaidi ni kuhusu tetesi za kuwapo mtu ambae historia hailezi wazi kuhusu kifo chake, na sasa tarifa za mwanzo za marehemu Bulembo zinasema yupo hai na anampango wake mahususi juu ya nchi ya Tanzania.
Mpango gani;?
Ndilo lilihatajika kufumbuliwa na mpelelezi Honda.
Honda alikuwa ametumia zaidi ya dakika kumi na tano bila kupata hata dalili ya maelezo yenye kumsaidia.
Alijishika kiuno huku akitembeza macho kila kona ya chumba kilichotumiwa na Bulembo kulala huku kichwani akifikiria kuacha kufuatilia njia aliotumia Bulembo mana inazidi kumwacha njia panda na muda unazidi kwenda.
Alitamani sasa kuingia kivingine na kwa njia zake ili apate ukweli wa sakata lile.
Wakati akili ikitafakari maamuzi; macho yakanasa kitu ukutani juu kidogo ya mto na mto huo ulionekana ndio ulikuwa unatumiwa na marehemu Bulembo kwa kuwa ulikuwa unaonekana kuwa na mafuta ya nywele yaliotengeneza weusi kidogo kwa kulaliwa mara kwa mara.
Juu kidogo ya tendegu la kitanda aliona mikwaruzo, akasogea kwa hatua za aste aste na alipofikia karibu aliona maandishi ila yalikuwa ni maandishi yale yale alioyaona kwenye kikaratasi alichokitafuna wakati akiwa mikononi mwa Sajini Kebu.
Na yalikuwa yamepangiliwa vile vile kama yalivyokuwa kwenye karatasi alioitafuna.
“142BOULEVARD DU JUIN
B. P. 1612
KINSHASA CONGO (81)”
Aliyatazama tena maandishi yale, bado hakuwa amepata walau wazo la kujua Bulembo alitaka kumaanisha nini japo alijua hii ilikuwa ni anuani ya ubalozi wa Tanzania Lakini kilichomchangaya zaidi ni ile alama ya mabano kisha zikafuatia namba (81) ilimaanisha nini hii namba! Hakujua wala kufikiria mbali zaidi ya kuzidi kuchanganyikiwa na asijue afuate lipi katika anuani ile
***
Angalizo ; Mnaosoma na kupita kimya kimya hamtendi haki kabisa, kama haivutii sema, umependa sema pia huo ndio ujira wangu wala sihitaj pesa yako ili niendelee kuweka hapa mtaji Pekee ni koment yako ambapo itasaidia watu wengi kuisoma.
Au mnataka na kusibiri isitishwe ndo muibuke na kutoa mitusi? Wakati inapopostiwa hatuwaoni?
Karibuni kwa maoni