Jinsi ya kupata marafiki na kushawishi watu (Tafsiri ya kitabu How to win friends and influence people cha Dale Carnegie)

Jinsi ya kupata marafiki na kushawishi watu (Tafsiri ya kitabu How to win friends and influence people cha Dale Carnegie)

“Anayefanya hili, dunia yote ni yake. Yule asiyefanya anatembea katika njia ya upweke.”

Mara nyingi katika majira ya joto huwa naenda kuvua samaki huko Maine. Binafsi ni mpenzi wa maforosadi na aisikrimu, lakini kwa sababu nisizozielewa niligundua kuwa samaki wanapendelea minyoo. Kwa hiyo basi, ninapokwenda kuvua sifikirii juu ya ninachopendelea, nafikiria juu ya kile wanachopenda. “Siweki aisikrimu na maforosadi kwenye ndoano, badala yake naning’iniza minyoo au panzi mbele ya samaki na kusema, “Ungependa kumla?” kwanini usitumie akili hiyohiyo unapovua watu?

Hicho ndicho alichofanya Lloyd George, waziri mkuu wa Uingereza wakati wa vita ya pili ya dunia. Mtu mmoja alipomuuliza amewezaje kubaki madarakani wakati viongozi wengine waliokuwepo wakati wa vita—Wilson, Orlando na Clemenceau—walishasahaulika. Alijibu kuwa kama kubaki kwake madarakani kunasababishwa na kitu kimoja, basi kitakuwa ni yeye kujifunza kuwa ni muhimu kuweka chambo kinachopendelewa na samaki.

Kwa nini kuongelea juu ya tunayotaka? Huo ni utoto na ujinga. Ni kweli kuwa unapenda kuongelea unachotaka. Unakipenda sana. Lakini hakuna mwingine anayekipenda pia. Wengine wote tuko kama wewe; tunapendezwa na yale tunayotaka.

Hivyo basi, njia pekee ya kuwashawishi watu ni kuongelea juu ya wanayotaka, na kuwaonyesha jinsi ya kuyapata.

Kumbuka jambo hilo kesho utakapokuwa unajaribu kumfanya mtu afanye jambo fulani. Kwa mfano, kama hutaki watoto wako wavute sigara, usiwahubirie na usiongee juu ya unachotaka; badala yake waonyeshe kuwa sigara zitawafanya wasiweze kuingia kwenye timu ya mpira wa kikapu, au kushindwa kushinda mbio za mita mia moja.

Jambo hili ni muhimu sana kulikumbuka, haijalishi unashughulika na watoto wako, ndama wa ng’ombe au sokwe. Kwa mfano: Siku moja bwana Ralph Waldo Emerson na mwanawe walijaribu kumuingiza ndama bandani. Lakini walifanya kosa ambalo wengi wetu hufanya, walifikiria tu kile wanachotaka: Emerson alimsukuma na kijana wake alimvuta. Lakini ndama naye alikuwa anafanya kama wao tu. Akifikiria juu ya kile anachotaka: kwa hiyo, alikaza miguu na kugoma kuondoka machungani. Yaya aliona taabu na kuhangaika kwao. Hakuwa msomi lakini katika hili alikuwa na akili kuliko emerson na kijana wake.

Alifikiri juu ya kile ambacho ndama anataka; hivyo aliweka kidole chake kwenye mdomo wa ndama, na kumuacha anyonye, kwa urahisi alimuongoza ndama bandani.

Jambo lolote ulilotenda toka siku unazaliwa, ulitenda sababu ya kutaka kitu fulani. Lakini vipi ulipotoa mchango kwa shirika la msalaba mwekundu? Ndiyo, hata wakati huo ulifanya kwa sababu ya kutaka kitu fulani. Uliwapa msalaba mwekundu mchango sababu ulitaka kutoa msaada; ulitaka kufanya kitu kizuri, kufanya jambo lisilo na ubinafsi, jambo la kimungu nk. Kama ungependa pesa zako zaidi ya kujihisi vizuri, usingetoa mchango huo. Inawezekana umetoa mchango huo kwa kuogopa aibu ya kukataa, au kwa sababu umeombwa kufanya hivyo. Lakini kitu kimoja kinabaki kuwa kweli. Ulitoa mchango kwa sababu ulitaka kitu fulani.

Katika kitabu chake Influencing human behavior, bwana Harry A. Overstreet alisema; “Matendo hutokea kwenye matamanio yetu—na ushauri mzuri unaoweza kupewa kwa anayetaka kushawishi mtu, haijalishi ni katika biashara, nyumbani , shuleni au katika siasa ni huu: Kitu cha kwanza ni wachochee watu watake kitu fulani. Yule anayeweza kufanya hivi dunia nzima ni yake. Yule asiyeweza anatembea katika njia ya upweke.

Mskotishi maskini, Andrew Carnegie, mtu ambaye alianza kufanya kazi kwa malipo ya senti mbili kwa saa, na mwishowe kuweza kuwapa watu utajiri wake wa dola milioni 350, alijifunza angali mdogo kabisa kuwa njia pekee ya kushawishi watu ni kuongea kuhusu yale wanayotaka. Alienda shule kwa miaka minne tu, lakini alijua jinsi ya kushughulika na watu.

Kwa kuonyesha mfano: shemeji yake alikuwa na wasiwasi sana juu ya wana wake wawili waliokuwa wakisoma chuo kikuu cha Yale. Walikuwa wanajishughulisha sana na mambo yao kiasi kwamba walipuuza kuandika barua nyumbani, na wala hawakujali kujibu barua za mama yao.

Hapo Carnegie alipinga kiasi cha dola 100, akisema kuwa anaweza kufanya ajibiwe barua. Mtu mmoja akakubali kamari hiyo; basi akaandika barua ya kirafiki sana kwa wapwa wake na mwishoni akisema kuwa atawatumia kila mmoja dola tano.

Lakini hakuweka pesa hizo ndani ya barua.

Majibu yalirudi wakimshukuru , “Mpendwa mjomba Andrew.” Kwa barua yake ya upendo—unaweza kumalizia.

Mfano mwingine kuhusu ushawishi unatoka kwake Stan Novak wa Cleveland Ohio, mshiriki wa mafunzo tunayotoa. Jioni moja Stan alirudi nyumbani na kumkuta mwanawe mdogo, Tim, akipiga kelele na kupiga vitu sebuleni, ilitakiwa aanze chekechea kesho yake, na alikuwa akipinga hataki kwenda. Pengine kikawaida Stan angemwambia kijana wake aende chumbani kwake na ajiandae kwenda shule kesho atake asitake. Lakini kwa kufahamu kuwa hilo halitakuwa na msaada kwa Tim kuanza shule akiwa sawa kiakili, Stan alikaa chini na kufikiri kwa kina. “Kama ningekuwa Tim, nini kingefanya nifurahie kuanza chekechea?” Baada ya kufikiri sana, yeye na mke wake wakaandika orodha ya vitu vya kufurahisha ambavyo Tim anaweza kufanya shuleni. Kuna kuchora, kuimba na kupata marafiki wapya. “Tukaanza mara moja, mimi, mke wangu Lil na mwana wetu mkubwa tukaanza kuchora jikoni. Haikuchukua muda Tim akaanza kuchungulia. Kisha akaanza kuomba na yeye ajumuike. Hapana, unatakiwa kwenda kwanza chekechea kujifunza kuchora,” nilimwambia. “Kisha kwa furaha kadri nilivyoweza, na kwa namna atakayoelewa kirahisi nikaanza kumuelezea vitu atakavyofurahia akienda chekechea. Asubuhi iliyofuata, nikidhani mimi ndiye wa kwanza kuamka—nilikwenda sebuleni na kumkuta Tim ameketi kitini, akionekana mwenye usingizi. “Unafanya nini huku?” Nilimuuliza. ‘Nasubiri kwenda chekechea. Sitaki kuchelewa,’ Tulikuwa tumeweza kuamsha kitu ndani ya Tim ambacho majadiliano na vitisho visingeweza.”

Kesho unaweza taka kumshawishi mtu kufanya kitu fulani. Kabla hujaongea, simama na jiulize. “Ninawezaje kumfanya mtu huyu atake kukifanya?”

Swali hili litatuzuia kufanya mambo kwa pupa, tukizungumza juu ya matakwa yetu tu bila kupata mafanikio yoyote.

Nyakati fulani nilikuwa nikikodi ukumbi mzuri sana wa hoteli moja nzuri huko New York. Niliukodi kwa siku ishirini kwa msimu ili kutoa mihadhara

Mwanzo wa msimu mmoja nilijulishwa kuwa natakiwa kulipa mara tatu ya bei niliyozoea kulipa. Taarifa hizi zilinifikia baada ya kuwa tiketi za viingilio zimekwisha chapishwa na matangazo yamekwishatolewa.

Kiasili, kama binadamu sikutaka kulipa ongezeko hilo. Lakini ingesaidia nini kuongea na hoteli juu ya ninachotaka. Wao walijali tu kile wanachotaka. Hivyo basi, baada ya siku chache nikaenda kuonana na meneja.

“Nilishtuka sana nilipopata barua yako,” nilimwambia. “Lakini sikulaumu. Kama ningekuwa kwenye nafasi yako pengine ningeandika barua kama hiyo. Jukumu lako kama meneja wa hoteli ni kuhakikisha unatengeneza faida kadri iwezekanavyo. Usipofanya hivyo utafukuzwa kazi, na utakuwa umestahili kufukuzwa. Sasa hebu tuchukue karatasi na tuandike faida na hasara ambazo utapata iwapo utang’ang’ana na ongezeko hili la kodi.”

Nilichukua karatasi na nikachora mstari katikati. Upande mmoja nikaandika “Faida” na upande wa pili nikaandika “Hasara.”

Chini ya “Faida” nikaandika maneno haya. “Ukumbi utakuwa wazi kukodishwa,” kisha nikamwambia meneja. “Utakuwa na ukumbi wazi kwa ajili ya kukodisha kwa dansi na makongamano. Hiyo ni faida kubwa. Mambo hayo yatakupa pesa nyingi kuliko mihadhara. Kama nikizuia ukumbi wako kwa siku ishirini utakosa wateja wenye faida kubwa zaidi.”

“Sasa tuangalie na hasara. Kwanza, badala ya kuongeza kipato kutoka kwangu, utakipunguza. Na ukweli ni kuwa utakikosa kabisa maana sitaweza kulipa bei unayotaka. Nitalazimika kufanya mihadhara hii mahali pengine.”

“Pia kuna hasara nyingine kwako. Mihadhara hii inaleta watu wastaarabu na wenye elimu kwenye hoteli yako. Hilo linaitangaza vizuri hoteli yako sivyo? Ukweli ni kuwa, hata ukitumia dola elfu tano kutangaza hoteli yako magazetini, haitawezekana kuleta watu wengi hotelini kwako kama mihadhara yangu. Hiyo ni faida kubwa sana kwa hoteli sivyo?”

Nilivyokuwa naongea niliandika hasara hizi mbili chini ya “Hasara” Na kumpatia karatasi ile meneja nikisema: “Natumaini utaangalia kwa makini faida na hasara zinazoweza kukupata na kunipa mrejesho.”

Kesho yake nikapata barua ikinitaarifu kuwa kodi yangu imeongezwa kwa asilimia 50 tu badala ya 300.

Angalia kwamba nilipata punguzo bila kusema lolote juu ya ninachotaka. Muda wote niliongelea kile ambacho meneja anataka na jinsi ya kukipata.

Fikiria labda ningefanya kama ilivyo asili ya binadamu. Ningevamia ofisi yake na kusema, “Unamaana gani kuniongezea kodi kwa asilimia mia tatu na ukijua tayari nimeshachapa tiketi na matangazo yametolewa? Asilimia mia tatu! Ajabu kabisa. Upuuzi! Sitalipa!”

Nini kingetokea? Mzozo ungeibuka na kukua. Na kama unavyojua ambavyo mizozo huisha. Hata kama ningeweza kumshawishi kuwa amekosea, ili kuepuka fedheha ingekuwa vigumu kwake kujirudi na kunipa ninachotaka.

Hapa kuna ushauri bora kabisa kuwahi kutolewa juu ya sanaa ya mahusiano ya binadamu. “Kama kuna siri ya mafanikio katika mahusiano ya binadamu,” alisema Henry Ford, “Basi ipo katika uwezo wa mtu kuelewa mtazamo wa mwingine, na kuona vitu kwa mtazamo huo na wa kwake.”

Huo ni ushauri bora sana, ningependa kuurudia: “Kama kuna siri ya mafanikio basi ipo katika uwezo wa kuelewa mtazamo wa mwingine na kuona mambo kwa mtazamo wake na wako.”

Ni ushauri rahisi na wa kawaida, kila mtu anaweza kuona ukweli wake mara moja; hata hivyo asilimia 90 ya watu wanaupuuza kwa asilimia 90.

Unataka mfano? Angalia barua zitakazofika mezani kwako kesho asubuhi, utaona kuwa watu wengi hudharau kanuni hii ya kawaida. Angalia barua hii iliyoandikwa na mkuu wa idara ya redio katika kampuni ya wakala wa matangazo iliyokuwa na ofisi nchini kote. Barua hii ilitumwa kwa wakuu wote wa vituo vya redio nchini kote. (Nimeweka hisia na mtazamo wangu kwenye mabano)

Bwana John Blank

Blankville,

Indiana

Mpendwa bwana Blank:

Kampuni ya—inapenda kubaki kuwa wakala kinara wa matangazo katika matangazo ya redioni.

[Nani anajali ambacho kampuni yako inapenda? Ninajali juu ya matatizo yangu. Benki wananidai, na wanataka kuuza nyumba yangu, wadudu wanaharibu maua yangu, jana soko la hisa limeporomoka, sikualikwa kwenye karamu ya Jones jana usiku, daktari kaniambia nina shinikizo kubwa la damu, ugonjwa wa mishipa ya fahamu na mba kichwani. Kisha nini kimetokea? Asubuhi ya leo nimefika ofisini, nikiwa nimejaa mawazo, nimefungua barua zilizofika nakutana na mjivuni mmoja kutoka New York akibwabwaja kuhusu kampuni yake inapenda. Bah! Kama angejua jinsi ambavyo barua yake imechukuliwa angeacha kabisa kazi ya matangazo na kuanza kutengeneza dawa za kuogeshea kondoo]

Wateja wa kampuni hii walikuwa ndiyo mhimili wa vituo vya redio. Uwezo wetu wa kujaza nafasi za matangazo umetufanya kuendelea kuwa wakala kinara mwaka hata mwaka.

[Kwa hiyo nyie ni wakubwa, matajiri na ni wa kwanza siyo? Kwa hiyo? Inanihusu nini hata kama ni wakubwa kama General Motors, General Electric na Jeshi la Marekani vikiunganishwa? Kama ungekuwa na akili nusu tu ya ndege mjinga ungetambua kuwa ninachojali ni jinsi gani nilivyo mkubwa, siyo nyie mlivyo wakubwa. Ukubwa wangu si wenu. Maongezi haya yote ya jinsi mlivyo wakubwa yanafanya nijione mdogo na asiye na umuhimu.]

Tunataka kuhudumia wateja wetu kwa kutumia taarifa za karibuni zaidi kutoka kwenye vituo vya redio.

[Mnataka! Mnataka! Punda kabisa wewe. Sijali kuhusu kile unachotaka au anachotaka Rais wa Marekani. Ngoja nikwambie kwa mara ya mwisho. Ninajali kile ninachotaka na hujasema chochote kuhusu hilo kwenye hii barua yako ya kipuuzi.]



Kwa hiyo basi, uiweke kampuni yetu kwenye orodha yako ya watu wa kwanza kupata taarifa za kila wiki kutoka redioni kwako. Taarifa zote zinazoweza kuwa muhimu kwa wakala ili apange muda wa kutangaza vizuri.

[“Orodha ya watu wa kwanza.” Unathubutuje! Kwanza umenifanya nijione sina maana na maongezi yako ya kuikweza kampuni yako. Halafu unaniomba nikuweke kwenye “Orodha ya upendeleo” na wala hujasema “Tafadhali”]

Majibu ya haraka ya barua hii, ukitueleza juu ya hali ilivyo sasa itakuwa msaada kwa pande zote mbili

[Ewe mpumbavu! Umenitumia barua ya hovyo na bado una thubutu kuniomba kitu wakati nina wasiwasi juu ya deni la nyumba, wadudu wala maua na shinikizo la damu kuweza kukaa chini kukuandikia majibu. Na unanitaka kujibu haraka. Unamaanisha nini “Haraka”? Unafahamu kuwa nimetingwa kama wewe tu? Na hata hivyo, nani amekupa haki ya kuniamrisha? Umesema itafaidisha pande zote mbili, walau sasa umeanza kuona mambo kwa mtazamo wangu. Lakini hujaeleza vizuri nitafaidika namna gani]

Wako muaminifu,

John Doe,

Meneja wa idara ya redio.

Nyongeza: Labda jarida la Blankville lililoambatanishwa litakupendeza, pengine utataka kulitangaza kituoni kwako

[Mwishowe huku kwenye nyongeza umeandika kitu kitakachonisaidia kutatua moja ya matatizo yangu. Kwa nini usingeanza barua yako kwa—lakini kwa sasa itasaidia nini? Wakala yeyote wa matangazo ambaye anaandika ujinga kama ulionitumia, anatatizo kwenye medulla oblongata. Huhitaji barua juu ya hali yetu ya sasa, unahitaji madini ya iodine kwenye tezi yako ya thyroid.]

Sasa kama watu wanaotumia maisha yao wakishughulika na matangazo, ambao wanajiona ni manguli wa kushawishi watu kununua—kama wanaandika barua kama hiyo, tutegemee nini kutoka kwa muuza nyama, muoka mikate au fundi magari?

Hapa pana barua nyingine kutoka kwa msimamizi wa sehemu ya mizigo kwenye bandari kavu kwa mwanafunzi wa kozi hii aliyeitwa Edward Vermylen. Barua hii ilikuwa na matokeo gani kwa aliyeandikiwa? Isome kisha nitakuambia.

  • A.Zerega’s sons, Inc.
  • 28 front st.
  • Brookyln, N.Y. 11201
  • Kwa: Bwana Edward Vermylen

  • Mabwana:
  • Utendaji kwenye eneo kituo cha treni zinazoondoka unasuasua kwa sababu tunapata mizigo karibu na jioni. Jambo hili linasababisha mrundikano, kufanya kazi kwa masaa ya ziada na kucheleshwa kwa magari ya mizigo, na wakati mwingine kucheleshwa kwa treni. Tarehe 10 mwezi wa kumi na moja, tulipokea kutoka kwenye kampuni yako mizigo 510 ambayo ilitufikia saa kumi na dakika ishirini jioni.
  • Tunaomba ushirikiano wako ili kukabiliana na athari zitokanazo na kupokea mizigo kwa kuchelewa. Tungeomba ufanye hivi, siku ambazo unatuma kiasi kama kilichotajwa hapo juu, ifanyike bidii, iwe ya kuleta magari ya mizigo mapema au kutuma sehemu ya mzigo asubuhi.
  • Faida utakayopata ni kwa magari yako ya mizigo kuondoka mapema na uhakika wa mizigo yako kusafirishwa kwa wakati.
  • Wako muaminifu,
  • J. B,
  • Meneja,
Baaada ya kusoma barua hii, bwana Vermylen, meneja mauzo wa kampuni ya A. Zerega’s sons, Inc., alinitumia ikiwa na maelezo haya:

Barua hii imekuwa na matokeo kinyume na yaliyolengwa. Barua imeanza kwa kuelezea matatizo ya bandari. Kitu ambacho hakituhusu. Wameomba ushirikiano wetu bila kuangalia kama inawezekana, mwishowe, kwenye aya ya mwisho imetajwa kuwa iwapo tutatoa ushirikiano, magari yetu ya mizigo yatatoka mapema na uhakika wa mizigo yetu itatumwa tarehe iliyopokelewa.

Kwa maneno mengine, kitu tunachotaka kimetajwa mwishoni na matokeo yake inaamsha ubishani badala ya ushirikiano.

Acha tuone kama tunaweza kuiandika upya barua hii na kuiboresha. Acha tusipoteze kabisa muda kuongelea matatizo yetu. Kama Henry Ford alivyosisitiza, “Tuelewe mtazamo wa mwingine, na kuona vitu kwa mtazamo wake na wetu.”
 
Hii ni namna moja ya kuboresha barua hiyo. Inaweza isiwe njia bora kabisa, lakini si imeboreka?

Bwana Edward Vermylen

KK A. Zerega’s sons, Inc.

28 Front St.

Brookyln, N.Y. 11201

Bwana Vermylen:

Kampuni yako imekuwa mteja wetu mzuri kwa miaka kumi na nne. Tunafurahia sana biashara yako na tunatamani kukupatia huduma ya haraka na kwa ufanisi kama unavyostahili. Lakini nasikitika kusema kuwa hilo haliwezekani kwa sababu magari yako ya mizigo hutuletea mizigo mikubwa kwa kuchelewa, kama ilivyotokea tarehe 10 mwezi wa kumi na moja. Kwa nini? Kwa sababu wateja wengine huchelewa kuleta mizigo pia. Hilo linasababisha msongamano. Hilo linasababisha magari yako yachelewe kutoka na wakati mwingine mzigo unachelewa kutumwa.

Hilo ni tatizo, lakini linaweza tatuliwa. Iwapo utaleta mzigo asubuhi, magari yako yatakuwa huru kuendelea na kazi, mzigo wako utahudumiwa kwa haraka, na wafanyakazi wetu watarudi nyumbani mapema kufurahia mlo mzuri wa tambi na macaroni mnaotengeneza

Haijalishi mzigo wenu umefika muda gani, tutafanya kila tuwezalo kuuhudumia kwa haraka.

Umetingwa hivyo tafadhali usijihangaishe kujibu ujumbe huu.

Wako muaminifu.

J—B

Meneja,

Barbara Anderson aliyefanya kazi katika benki huko New York, alitaka kuhamia Phoenix, Arizona sababu ya afya ya mwana wake. Kwa kutumia kanuni alizojifunza kwenye kozi yetu, aliandika barua kwa benki kumi na mbili za Phoenix.

Mpendwa:

Uzoefu wangu wa miaka kumi wa kazi ya benki unaweza kuwa na manufaa kwa benki inayokuwa kwa kasi kama yako.

Nimefanya kazi kadhaa za benki na Bankers Trust Company ya New York, na sasa ni meneja wa tawi. Nimepata ujuzi juu ya nyanja zote za benki, uhusiano na wateja, mikopo na uongozi.

Mwezi wa tano nitahamia Phoenix, nina hakika ninaweza kuwa na mchango kwenye faida na ukuaji wako. Nitakuwepo Phoenix juma la kuanzia tarehe tatu mwezi wa nne, nitathamini kupata nafasi ya kukuonyesha jinsi ninavyoweza kuisaidia benki yako kutimiza malengo yake.

Wako muaminifu,

Barbara L. Anderson

Unadhani bibi Anderson alipata majibu yoyote ya barua yake? Benki kumi na moja kati ya kumi na mbili zilimuita kwenye usaili, na ilikuwa uchaguzi wake ni benki gani aende. Kwa nini? Bibi Anderson hakuongelea kile anachotaka bali aliandika ni namna gani atakuwa msaada kwao. Alikazia matakwa yao na si yake.

Maelfu ya maafisa mauzo hutembea wakizunguka leo, wakiwa wamechoka na kukatishwa tama na malipo duni. Kwa nini? Kwa sababu mara zote wanafikiria kile wanachotaka. Hawatambui kuwa mimi na wewe hatuhitaji kununua chochote. Kama tungetaka tungeenda wanakouza kununua. Badala yake, sote, siku zote tunatamani kutatua matatizo yetu. Na kama wauzaji hao wangetuonyesha jinsi gani huduma zao au bidhaa zao zitatusaidia kutatua matatizo yetu, wasingehangaika kutushawishi kununua. Tungenunua wenyewe. Na mteja anapenda kuhisi amenunua mwenyewe kwa kutaka na si kwa kushawishiwa.

Hata hivyo, maafisa mauzo wengi hutumia maisha yao yote bila kuangalia mambo kwa mtazamao wa mteja. Kwa mfano, kwa miaka mingi niliishi Forest Hills, mtaa mdogo katikati ya jiji la New York. Siku moja, nilipokuwa nikiwahi kituo cha treni, nilionana na dalali wa makazi, kazi yake kuuza na kununua nyumba na viwanja kwenye eneo hilo. Alikuwa anaijua Forest Hills vilivyo, hivyo nikamfuata na kumuuliza iwapo ukuta wa nje wa nyumba yangu umewekewa wavu wa chuma au imejengwa kwa vigae vyenye uwazi katikati. Alisema hafahamu na kisha akaniambia mambo ambayo tayari niliyafahamu—kwamba niwapigie simu Forest hills Garden Association. Asubuhi iliyofuata nilipokea barua kutoka kwake. Je, alinipatia taarifa niliyohitaji? Angeweza kuipata ndani ya dakika moja tu kwa kupiga simu lakini hakufanya hivyo. Kwa mara nyingine tena akaniambia nitaweza kupata taarifa hizo kwa kupiga simu, kisha akaomba awe wakala wangu wa bima.

Hakuwa na nia ya kunisaidia. Alikuwa anataka kujisaidia mwenyewe tu.

Bwana J. Howard Lucas wa Birmingham, Alabama, anasimulia jinsi maafisa mauzo wawili kutoka kwenye kampuni moja walivyoshughulika na jambo kama hilo, alisema:

“Miaka kadhaa iliyopita nilikuwa katika sehemu ya uongozi wa kampuni moja ndogo. Jirani yetu kulikuwa na makao makuu ya wilaya ya kampuni kubwa ya bima. Mawakala wake walikuwa wamepewa maeneo, na kampuni yetu walipewa mawakala wawili ambao nitawaita Carl na John.

“Asubuhi moja Carl alifika ofisini kwetu na kusema kuwa kampuni yao imeanzisha sera mpya ya bima ya maisha kwa viongozi wa makampuni, na alifikiri labda tungeweza kupendezwa nayo hivyo atatutaarifu akipata taarifa zaidi.

Siku hiyohiyo, tulikutana na john njiani tulipokuwa tukitoka kwenye mapumziko ya kahawa, alisema kwa sauti kubwa: ‘Luke ngoja kidogo, nina habari nzuri kwenu.’ Alitukimbilia na kwa shauku akatuambia kuhusu huduma ya bima kwa viongozi ambayo kampuni yao imeianzisha siku hiyohiyo. (ulikuwa ni mpango uleule ambao Carl alikuwa ameugusia). Alitaka tuwe kwenye watu wa kwanza-kwanza kuingia kwenye mpango huo. Alitueleza kifupi jinsi bima hiyo ilivyo na akamalizia kwa kusema, ‘Huduma hii bado ni mpya kabisa, kesho nitamtuma mtu kutoka ofisini aje awaelezee vizuri. Kwa sasa, tujaze nakala za maombi yenu ili awe na taarifa za kutosha kuanza kufanyia kazi.’ Shauku yake iliamsha ari yetu ya kutaka huduma ile japokuwa hatukujua ipoje hasa, tulipopata taarifa zaidi, yalithibitisha yale yaliyosemwa na John jinsi alivyofikiri huduma itakuwa, na hakutuuzia tu huduma hiyo, bali aliongeza kiasi tulicholipia kwa ajili ya bima.

“Carl angeweza kuwa ndiye aliyetuuzia huduma ile, lakini hakufanya bidii yoyote kuamsha ari yetu ya kutaka huduma ile.”

Dunia imejaa watu wanaotaka vitu wao tu, na wanaofuatilia maslahi binafsi pekee. Kwa hiyo, wale wachache ambao bila ubinafsi wanajaribu kuwahudumia wengine wanakuwa na fursa kubwa sana na ushindani mdogo sana. Owen D. Young, mwanasheria na mmoja ya viongozi wakubwa wa biashara katika Marekani amewahi kusema, “Watu ambayo wanaweza kujiweka mahali pa wengine, na wanaoweza kuelewa jinsi akili zao zinavyofanya kazi, hawana haja ya kujali kuhusu maisha yao yatakuwaje.”

Kama kwa kusoma kitabu hiki umepata kitu kimoja tu—yaani kujijengea tabia ya mara zote kufikiria kupitia mtazamo wa wengine, na kuona vitu kwa mtazamo wao—kama umepata kitu hicho kimoja tu kutoka kwenye kitabu hiki, basi hicho kinaweza kuthibitika kuwa moja ya nguzo za taaluma yako.

Kuangalia mambo kwa mtazamo wa mwingine, na kuamsha ndani yake ari ya kutaka kitu fulani, haitakiwi kueleweka kuwa ni kumlaghai mtu huyo ili afanye kitu ambacho kina faida kwako tu na hasara kwake. Kila mmoja anatakiwa kufaidika kwa makubaliano. Kwenye barua za bwana Vermylen, mtumaji na mpokeaji, wote walifaidika kwa kufanya kile kilichopendekezwa. Wote, benki na bibi Anderson walifaidika kwa barua yake, benki ilipata mfanyakazi muhimu na bibi Anderson kazi nzuri. Na kwenye mfano wa mauzo ya huduma ya bima ya John kwa bwana Lucas, wote walifaidika.

Mfano mwingine ambao kila mtu anafaidika kwa kanuni hii ya kuamsha ari ya kutaka kitu, unatoka kwa Michael E. Whidden wa Warwick huko Rhode Island. Bwana Whidden ni afisa mauzo wa eneo hilo wa kampuni ya mafuta ya Shell. Mike alitaka kuwa afisa mauzo namba moja kwenye wilaya yake, lakini kituo kimoja cha mafuta kilikuwa kinamuangusha. Kilikuwa kinasimamiwa na mwanaume mmoja mzee ambaye haikuwezekana kumshawishi asafishe kituo chake. Kilikuwa katika hali mbaya kiasi kwamba mauzo yalikuwa yanashuka kwa kasi.

Msimamizi huyu hakusikia chochote alichoambiwa na Mike juu ya kuboresha kituo chake. Baada ya vitisho vingi na kumsihi—njia ambazo hazikuzaa matunda—mike akaamua kumualika msimamizi huyo kutembelea kituo kipya cha Shell kwenye eneo lake.

Msimamizi yule alistaajabia sana ubora wa kituo kile kipya. Mike alipomtembelea safari iliyofuata, kituo chake kilikuwa kimesafishwa na mauzo yameongezeka. Hili lilimuwezesha Mike kuwa afisa mauzo namba moja kwenye wilaya yake. Kuongea kwake na kujadiliana kote hakukusaidia kitu, lakini kwa kuamsha ari ya kutaka ndani ya msimamizi, kwa kumuonyesha kituo cha kisasa, alikuwa amefanikiwa lengo lake, na wote, Mike na msimamizi walifaidika.

Watu wengi hupita chuo kikuu na kujifunza kusoma mashairi ya Virgil na kubobea katika masuala ya hesabu bila hata ya kufahamu ni jinsi gani akili zao wenyewe zinavyofanya kazi. Kwa mfano: wakati fulani niliwafundisha wanafunzi vijana wa chuo waliokuwa karibu kuanza kazi kwenye kampuni ya Carrier, watengenezaji wakubwa viyoyozi juu ya uzungumzaji wenye matokeo. Mmoja wa washiriki alitaka kuwashawishi wenzake wawe wakicheza mpira wa kikapu kwenye muda wao wa ziada, alisema: “Napenda kucheza mpira wa kikapu, lakini mara chache nilizoenda uwanjani hakukuwa na watu wa kutosha kucheza mechi. Jana usiku wawili au watatu kati yetu tukaamua tu kurushiana mpira—na nilidhurika jicho. Ningependa kesho usiku wote mje. Ninataka kucheza mpira wa kikapu.”

Aliongea chochote juu ya unachotaka? Bila shaka hautaki kwenda kwenye kiwanja ambacho hakuna mwingine anaenda sivyo? Haujali kuhusu anachotaka. Hautaki kudhurika jicho.

Je, angeweza kukuonyesha jinsi ya kupata vitu unavyotaka kwa kutumia uwanja? Bila shaka, angeweza kuzungumza juu ya burudani utakayopata ukihudhuria.

Nikirudia maneno ya busara ya Profesa Overstreet: Kwanza, amsha ari ya kutaka ndani mtu. Anayeweza kufanya hivyo dunia yote ni yake. Asiyeweza hilo, anatembea katika njia ya upweke.

Mmoja wa wanafunzi katika kozi ya kujifunza uandishi alikuwa na wasiwasi juu ya mvulana wake mdogo. Mtoto wake alikuwa na uzito chini ya wastani na alikuwa akigoma kula impasavyo. Wazazi wake walitumia njia zilizozoeleka. Walimfokea na kumsema mara zote. “Mama anataka ule hiki na kile.” “Baba anataka ukue uwe mtu mkubwa.”

Je, mvulana huyo alijali maneno hayo? Kama tu ambavyo wewe unajali juu ya punje moja ya mchanga kwenye mchanga wa ufukweni.

Hakuna mtu, hata yule mwenye akili za farasi atategemea mtoto wa miaka mitatu aelewe mtazamo wa baba yake mwenye miaka thelathini. Lakini hichi ndicho baba yule alitarajia. Ilishangaza. Mwishowe aliona hilo. Hivyo akajiambia: “Mtoto wangu anataka nini? Nawezaje kuunganisha matakwa yangu na yake?”

Mara alivyoanza kufikiri kwa namna hiyo mambo yakawa rahisi. Kijana wake alikuwa na baiskeli ya miguu mitatu aliyopenda kuendesha mbele ya nyumba yao huko Brookyln. Nyumba kadhaa mbele, kulikuwa na mvulana mmoja mkubwa na mbabe ambaye alikuwa akimnyaganya kijana wake baiskeli na kuendesha yeye.

Kiasili, kijana yule mdogo angekimbia kwa mama yake akilia, naye angetoka na kumnyang’anya mbabe yule baiskeli na kumpandisha kijana wake tena, hili lilitokea karibu kila siku.

Je mtoto yule alitaka nini? Haikuhitaji Sherlock Holmes kujibu hilo. Heshima yake, hasira yake, tamaa yake ya kujiona wa thamani—hisia zote zenye nguvu ndani yake—zilimsukuma kutaka kisasi, kumpiga yule mbabe ngumi ya pua. Na baba yake alipomueleze kuwa siku moja ataweza kumpiga mbabe yule kama akila vitu ambavyo mama yake anamtaka ale—baba yake alivyomuahidi hilo—hakukuwa na tatizo tena kwenye suala la kula. Kijana yule aliweza kula kila kitu ili awe mkubwa—chochote ili kuwa na ukubwa wa kutosha kumpiga yule mbabe aliyekuwa akimdhalilisha kila mara.

Baada ya kutatua tatizo hilo, wazazi wake wakahamia kupambana na tatizo lingine. Mtoto alikuwa na tabia ya kukojoa kitandani.

Alikuwa akilala na bibi yake, bibi yake alipoamka asubuhi, alishika mashuka na kusema: “Johnny ona ulichofanya tena jana usiku!”

Mtoto alijibu: “Hapana siyo mimi. Ni wewe.”

Kumfokea, kumchapa, kumuabisha—na kusisitiza kuwa wazazi wake hawataki afanye hivyo—hakuna kati ya hayo yaliyofanya kitanda kiwe kikavu. Hivyo wazazi wake waliuliza: “Tunawezaje kumfanya kijana wetu atake kuacha kukojoa kitandani?”

Matakwa yake yalikuwa ni nini? Kwanza, alitaka kuvaa nguo za kulalia kama baba yake na si gauni la kulalia kama bibi yake. Bibi yake alikuwa amechoshwa na tabia zake za usiku hivyo akajitolea kumnunulia nguo za kulalia iwapo ataacha kukojoa kitandani. Pili, alitaka kitanda chake peke yake. Bibi yake hakupinga.

Mama yake akamchukua hadi kwenye duka la samani huko Brookyln, alimkonyeza msichana wa mauzo na kusema: “Huyu bwana mdogo anataka kufanya manunuzi.”

Urefu ukiwa umemuongezeka kwa inchi kadhaa sababu ya kauli ile, alisema: “Nataka kujinunulia kitanda.”

Alipoonyeshwa kitanda ambacho mama yake alitaka akinunue, mama yake akamkonyeza tena yule muuzaji na mtoto wake akashawishiwa kukinunua.

Kitanda kililetwa siku iliyofuata; na usiku huo, baba yake aliporudi, mvulana alimkimbilia mlangoni akipiga kelele: “Baba! Baba! Njoo ghorofani uone kitanda changu nilichonunua!”

Baba yake, huku akiangalia kitanda, akatii kanuni ya Charles Schwab: “Alikuwa mwenye kuonyesha uthamini kutoka moyoni na mwingi katika kupongeza.”

“Hautakojoa kwenye kitanda hiki, siyo?” alisema baba.

“Hapana, hapana! Sitakojoa kwenye kitanda hiki.” Na mtoto alitunza ahadi yake, maana fahari yake ilihusika. Na hiyo ni kitanda chake. Ni yeye mwenyewe ndiye amekinunua. Na sasa alikuwa akivaa nguo za kulalia kama baba yake. Alitaka kutenda kama baba yake. Na alitenda.

Baba mwingine, K. T. Dutchmann, aliyekuwa ni mhandisi wa simu, ambaye naye alikuwa ni mwanafunzi wa kozi hii, alikuwa ameshindwa kumfanya binti yake wa miaka mitatu ale kifungua kinywa. Njia za kawaida kama kumfokea, kumtisha na kumbembeleza zote hazikufanikiwa. Kwa hiyo wazazi wake wakajiuliza: “Tunawezaje kumfanya binti yetu atake kula?”

Binti yule alipenda kumuiga mama yake, kujihisi mkubwa na mtu mzima; kwa hiyo siku moja walimsimamisha kwenye kiti na kumuacha atengeneze kifungua kinywa. Wakati huo huo, ili kucheza na saikolojia yake, baba yake aliingia jikoni binti alipokuwa akiandaa kifungua kinywa, binti akasema: “Ona baba, naandaa kifungua kinywa leo.”

Siku hiyo alikula mara mbili ya kiasi ch kawaida bila kulazimishwa, sababu alikuwa amependezwa nacho. Alikuwa amefanikiwa kupata hisia za kuthaminiwa; kwa kuandaa kifungua kinywa, alikuwa amepata uwanja wa kujieleza/kujionyesha.

William Winter amewahi kusema, “Kujieleza/kujionyesha ni hitaji muhimu la asili la mwanadamu.” Kwa nini hatutumii saikolojia hii kwenye masuala ya kibiashara? Tunapokuwa na wazo zuri, badala ya kuwafanya wengine wafikiri ni wazo letu, kwa nini tusiwaache wapike na kukoroga wazo hilo wenyewe. Hapo watalichukulia kama wazo lao; watalipenda na pengine watalila zaidi ya kawaida.

Kumbuka: “Kwanza, amsha ari ya kutaka ndani ya mtu. Anayeweza kufanya hili, dunia yote ni yake. Asiyeweza, anatembea katika njia ya upweke.”

KANUNI YA 3

Amsha ndani ya wengine ari ya kutaka
 
Kwa Kifupi

MBINU KUU ZA KUSHUGHULIKA NA WATU

KANUNI YA1


Usishutumu, usilaumu wala usilalamike

KANUNI YA 2

Onyesha kuthamini bila unafiki

KANUNI YA 3

Amsha ndani ya wengine ari ya kutaka.​
 
Back
Top Bottom