Hapa hapazungumziwi usomi wala u-Yanga. Panazungumziwa namna ya kuvumilia na kustahamili machache ya mpito ili kupata hatma yenye neema zaidi. Mandela hakuzaliwa na ANC, lakini angeweza kutolewa mapema gerezani akawa mtu huru kama tu angekana madai ya ANC ya uhuru wa walio wengi. Alivumilia na kustahamili miaka 27 gerezani na akatoka akiwa mtu bora zaidi na nchi yake ikawa huru. Buffon hakuzaliwa na (timu ya ) Juventus, lakini akakubali kubaki nayo iliposhushwa Daraja na nakisi (deficit) tangulizi ya alama kadhaa za kuanzia Serie B. Matokeo yake akaipandisha tena na kuishia na heshima iliyoambatana na mapato mengi zaidi kuliko aliyoyakosa kwa kucheza Serie B msimu mzima. Fuatilia wafanikiwa wengi, kama siyo wote : Lukaku, Mwalim Nyerere, Diamond, Pele, Mzee Kenyatta, ...... na utabaini wamefikia mafanikio yao kwa kustahamili kwa makusudi adha ambazo kama wangependa wangeweza kuziepuka.
Aidha, hata kiuchezaji ndani ya dakika za mchezo, kunahitajika ustahamilivu wa makusudi ili uwe mchezaji bora zaidi. Huo haupatikani kwa mazoezi ya dawati la ufundi wala kwa kipaji cha mchezo wenyewe, bali hupatikana kwa kuizowesha nafsi kustahamili adha na karaha. Wanaoshindwa, hata wawe timamu kiasi gani kimwili, hata wawe na kipaji kiasi gani, wanashindwa kufikia kilele chao cha mafanikio na kukosesha timu au wapenzi wao na mataifa yao ladha ya uwezo wao. Mwangalie Tyson aliyeshindwa kustahamili adha za mchezoni hadi akaamua kumn’gata sikio Holyfield, ikawaje na amekuwaje? Hakuwa amechezewa rafu za makusudi kweli? Mwangalie Serena Williams aliyeshindwa kuvumilia uonevu wa mwamuzi na kumtolea maneno mabaya kwenye fainali ya US Open ya Tennis, ikawaje? Hakuwa timamu? Hakuwa ameonewa kweli?Mwangalie Zidane alivyoikosesha Ufaransa Kombe la Dunia kwa kushindwa kuhimili udhia. Unadhani hakuwa na timamu kimwili? Au hakuwa na kipaji? Hakuwa ameudhiwa kweli?
Mazoezi ya stahamala na uvumilvu kama huo hayapatikani uwanjani, wala hayanolewi na kauli za ‘nani hakuzaliwa wapi’. Yanapatikana kwa kujifunza kutoka kwa walioweza na walioshindwa, na kwa kuwasaidia vijana wetu pale tunapowaona wanaelekea kwenye kukosa mengi kwa sababu ya machache. Lau Samatta ambaye ‘hakuzaliwa Simba’ asingepewa gari aliyoahidiwa pale alipoamua kurudi timu yake ya mchangani, tungekuwa tunaimba wimbo wake hii leo?
Naomba ujifunze kutoka maisha ya Mahatma Gandhi, Mwasisi wa mataifa ya India, Pakistan na Bangladesh na uirithishe kwa Kakolanya na wenye mtizamo kama wake. Gandhi ametanabahisha kwamba kulipiza jicho kwa jicho kutaishia na dunia ya vipofu watupu (an eye for an eye will make the whole world blind). Wakatabahu.